Mkopo:Nahju al-Balaghah
| Taarifa za kitabu | |
|---|---|
| Tarehe ya kuandikwa | 400.H |
| Mada | Kauli na maandish teuzi ya baadhi ya Imamu Ali (a.s). |
| Mtindo | Simulizi |
| Lugha | Kiarabu |
| Kwa juhudi za | Sayyid Radhi |
| Iliyohakikiwa na | Watu Tofauti |
| Idadi ya juzuu | 1 |
Nahju al- Balagha ni kitabu kinachojumuisha hotuba, barua, na semi fupi za Imamu Ali (a.s) ambazo Sayyid Radhi alizikusanya na kuzipanga kupitia juhudi zake binafsi. Wataalamu na watafiti wanakichukulia kitabu hichi kama ensaiklopidia ya utamaduni wa Kiislamu na moja kati ya vyanzo muhimu zaidi kwa ajili ya kuuelewa Uislamu pamoja na maadili ya kidini. Kitabu cha Nahju al- Balagha kina sifa ya kuwa na kiwango kikubwa cha ufasaha na uandishi makini. Jambo hili linasimama kama siri kuu ya mvuto na kudumu kwa maandiko haya katika historia yote.
Ujumuishi wa mada mbalimbali na upana wa maudhui za kitabu hichi vinasimama kama moja ya sifa na fadhila kubwa za Nahju al- Balagha. Maudhui ya kitabu hichi yanafuata mlolongo maalumu katika sehemu tatu kuu ambazo ni hotuba, barua, na semi fupi za hekima. Katika sehemu ya hotuba na semi fupi, unakutana na mada mbalimbali kama uelewa wa kumjua Mwenyezi Mungu, masuala ya kimaadili, kuuelewa ulimwengu, asili ya uumbaji, maumbile ya mwanadamu, pamoja na mifumo ya umma na serikali zilizofanya uadilifu au dhuluma mbalimbali. Kwa upande mwingine, sehemu ya barua za kitabu hichi imejikita zaidi katika uchambuzi wa masuala ya uongozi wa serikali, utawala bora, pamoja na namna ya viongozi na maafisa wa serikali wanavyopaswa kutangamana na kuamiliana na wananchi wao.
Wataalamu wa lugha wamekitafsiri kitabu cha Nahju al- Balagha katika lugha mbalimbali duniani zikiwemo lugha ya Kifarsi, Kiingereza, Kifaransa, Kihindi, Kiitaliano, Kituruki cha Istanbul, Kitajiki, na Kiurdu. Wasomi na wanazuoni wamekiandikia kitabu hichi vitabu kadhaa vya sherehe (tafsiri chambuzi). Miongoni mwazo ni kitabu Sharhu Nahji al- Balagha kilichotungwa na Ibnu Abi al Hadid pamoja na Sharhu Nahji al- Balagha kilichoandikwa na Ibnu Maitham al Bahrani. Vitabu viwili hivi vinasimama kama sherehe muhimu zaidi za lugha ya Kiarabu kuhusiana na kitabu cha Nahju al- Balagha.
Baadhi ya watafiti wamefanya juhudi kubwa za kukusanya semi na maneno mengine ya Imamu Ali (a.s) kutoka katika vitabu vyengine mbalimbali vya kihistoria ambayo Sayyid Radhi hakuyajumuisha katika matini asili ya Nahju al- Balagha. Wasomi hao wamechapisha maneno na semi hizo chini ya anwani ya Mustadraku Nahji al- Balagha. Miongoni mwa jitihada hizo za kitaaluma ni kitabu maarufu kiitwacho Nahju al Saada fi Mustadrak Nahji al- Balagha kilichotungwa na mwanachuoni maarufu aitwaye Muhammad Baqir al-Mahmoudi.
Kabla ya kuvumbuliwa kwa teknolojia ya viwanda vya uchapishaji, waandishi wa zama hizo walifanya juhudi kubwa za kunakili kwa mkono mamia ya nakala za kitabu cha Nahju al- Balagha . Nakala ya kale zaidi ya maandishi ya mkono iliyosalia hadi leo mikononi mwetu, ni ile iliyoandikwa mnamo mwaka wa 469 Hijria. Bado nakala hiyo ya kihistoria inaendelea kubaki salama ikiwa imehifadhiwa ndani ya Maktaba ya Ayatullah Mar'ashi Najafi iliyoko mjini Qum nchini Iran. Baada ya kuingia kwa teknolojia ya viwanda vya uchapishaji, mashirika yalichapisha kitabu hichi mamia ya mara katika nchi mbalimbali ulimwenguni, ikiwemo Iran, Misri, Lebanon, Syria, na Qatar, huku baadhi ya matoleo yake yakiwa kimesindikizwa na sherehe pamoja na tafsiri mbalimbali za lugha tofauti.
Uanzishwaji wa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, kupitia msaada vya vyombo vya habari na sekta ya utamaduni, ulifanya kitabu cha Nahju al- Balagha kupenya na kuzagaa kwa haraka katika jamii. Tukio hili lilisaidia kuanzishwa vyuo vikuu pamoja na taasisi mbalimbali zilizojikita mahususi katika taaluma za kitabu cha Nahju al- Balagha. Miongoni mwa taasisi muhimu zilizoanzishwa wakati huo, ni ile Taasisi Kuu ya Nahju al- Balagha iliyoanzishwa kwa lengo la kueneza na kufanya tafiti maalumu na za kitaalamu za kitabu hicho, ambayo bado inaendelea kufanya kazi hiyo hadi leo. Hali kadhalika, wataalamu wa mifumo ya kidijitali walitengeneza programu maalumu za kompyuta pamoja na simu zinazohusiana na Nahju al- Balagha chini ya anwani za Daneshnameye Alawi na Daneshnameye Jamie Nahju al- Balagha ili kurahisisha kazi za utafiti.
Miongoni mwa vyanzo vikuu alivyovitumia Sayyid Radhi katika kukusanya na kuandaa kitabu cha Nahju al- Balagha, ni vitabu vilivyoandikwa na wanazuoni wa Ahlu Sunna. Baadhi ya vyanzo hivyo ni kitabu cha Al-Bayan wa al-Tabyin kilichoandikwa na Al-Jahidh, kitabu cha Al-Maghazi kilichotungwa na Sa'id bin Yahya al- Umawi, kitabu cha Al-Jamal kilichoandikwa na Al-Waqidi, pamoja na Tarikh al- Tabari. Baadhi ya watafiti wanaamini kuwa hatua ya Sayyid Radhi ya kutosheka na vyanzo vya Ahlu Sunna, pamoja na kutoashiria isnadi za maneno ya Imamu Ali (a.s) ndani ya kitabu cha Nahju al- Balagha, kulileta ukosoaji na mapungufu kadhaa ya kitaalamu. Sababu hiyo ndiyo iliyowafanya wanachuoni na watafiti wengi kuchukua juhudi kubwa za kukusanya isnadi za Hadithi za kitabu hichi kutoka katika vyanzo vya kale vya kihistoria ya kuziweka katika mfumo wa nyaraka za isnadi, ili iwe ni thibitisho la kuthibitisha usahihi na ukweli wa maandiko yake.
Baadhi ya wanazuoni wa Kisunni wanatilia shaka utambulisho wa mkusanyaji wa athari hii, pamoja na kutilia shaka usahihi wa kunasibishwa kwa mapokezi ya kitabu hicho na Imamu Ali (a.s). Watafiti wanaounga mkono usahihi wa mapokezi hayo, wamebainisha wakisema kuwa, shaka hiyo inayohusiana na utambulisho wa mkusanyaji inadhihirisha ukosefu wa mapitio ya matini asili ya kitabu chenyewe, kwa sababu jina la mkusanyaji ambalo ni Sayyid Radhi linaonekana mara nyingi ndani ya matini ya kitabu hicho. Hali kadhalika, Ibnu Abi al-Hadid ambaye ni miongoni mwa wanazuoni wakubwa wa Ahlu Sunna, anaeleza kuwa kutilia shaka juu ya kunasibishwa kwa maudhui za Nahju al- Balagha na Imamu Ali (a.s) ni matokeo ya kufuata matamanio ya nafsi pamoja na ushabiki na taasubi pofu.
Umuhimu wa Nahju al- Balagha
(بئس الزاد إلی المعاد العدوان علی العباد) Tafsiri: Akiba mbaya zaidi kwa ajili ya Akhera ni kuwafanyia dhuluma waja wa Mwenyezi Mungu.
Nahju al Balaghah, uhakiki wa Subhi Salih, 1414 H, Hikma ya 221, uk. 507.
Nahju al- Balagha ni kitabu kinachojumuisha hotuba, barua, na semi fupi zilizotokana na Imamu Ali (a.s) katika zama za ukhalifa wake.[1] Watafiti wanakitambua kitabu hichi kama ensaiklopidia ya utamaduni wa Kiislamu, na wanakitaja kuwa ni chanzo muhimu zaidi kwa ajili ya kuuelewa Uislamu na maadili ya kidini, kinachoshika nafasi ya tatu baada ya Qur'ani Tukufu na Hadithi.[2] Hali kadhalika, wanazuoni wamekieleza kitabu cha Nahju al- Balagha kuwa ni miongoni mwa vitabu vinavyopewa kipaumbele kikubwa cha kukihifadhi baada ya Qur'ani Tukufu, mtazamo ambao unapatikana ndani ya madhehebu ya Kishia bila ya kushirikiana na madhehebu mengine katika fikra hiyo.[3] Reza Ostadi amerekodi majina ya vitabu 370 katika tasnifu yake iitwayo Kitabnameye Nahju al- Balagha, vilivyoandikwa kuhusiana na Nahju al- Balagha hadi kufikia mwaka 1980 M.[4]
Sayyid Muhsin al-Amin katika kitabu cha A'yan al Shiah, amekitambulisha kitabu cha Nahju al- Balagha kama moja ya fahari kubwa zaidi za ulimwengu wa Kiarabu na Kiislamu.[5] Tafiti za kihistoria zinaonesha kuwa kitabu hichi kinashika nafasi ya pili baada ya Qur'ani Tukufu kwa kuwa na idadi kubwa ya nakala za maandishi ya mkono, sherehe, na tafsiri ndani ya utamaduni mzima wa Kiislamu. Fasihi nyingi za lugha ya Kifarsi na Kiarabu, zinaonesha kuwa Nahju al- Balagha inachukuwa nafasi ya pili baada ya Qur'ani Tukufu katika kuziathiri lugha mbili hizo.[6] Hali kadhalika, Muhaddith al- Nuri katika kitabu cha Mustadrak al Wasa'il anasema kuwa, idadi kubwa ya wanazuoni wa zama za kale walikuwa wakikitaja kitabu hichi kwa jina la Akhu al-Qur’an (Kaka wa Qur'ani) pale walipotaka kuwakabidhi wanafunzi wao idhini (ijaza) rasmi ya kupokea na kunakili Nahju al- Balagha.[7]
Mkusanyaji
Makala asili: Sayyid Radhi
Mnamo mwaka wa 400 Hijria (sawa na mwaka 1010 M.), Sayyid Radhi alikusanya na kukipanga kitabu cha Nahju al- Balagha katika mfumo wa kitabu kamili.[8] Mwanazuoni huyu anatokana na ukoo wa Aalu Abi Talib.[9] Naye alikuwa ni mfasiri mzuri wa Qur'ani Tukufu na gwiji wa fasihi ya Kiarabu katika madhehebu ya Kishia, na alikuwa ni mwanatheolojia shupavu katika ulimwengu wa Kiislamu.[10]
Uteuzi wa Jina
Sayyid Radhi amebainisha akisema kuwa, nia kuu ya kukusanya kitabu cha Nahju al- Balagha ilikuwa ni kuitikia wito wa maombi ya marafiki zake waliomwomba akusanye semi zenye ufasaha mkubwa zaidi kutoka kwa Imamu Ali (a.s).[11] Mwandishi huyu alidhibiti na kukusanya sehemu maalumu tu ya semi zilizofikia kiwango cha juu zaidi cha ufasaha na balagha.[12] Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya kukiita kitabu hichi Nahj al-Balagha, jina lenye maana ya Njia ya Balagha[13] ambayo Muhammad Abduh, aliyekuwa miongoni mwa wanazuoni wakubwa wa Ahlu Sunna, alilieleza kama sifa sahihi zaidi kwa ajili kitabu hichi.[14]
Thamani ya Kifasihi
Ufasaha wa balagha ya Nahju al- Balagha unazingatiwa kama sababu kuu zinazokipa kitabu hichi mvuto mkubwa na sifa ya kudumu katika uwanja wa historia.[15] Wanazuoni wameziweka semi za Nahju al- Balagha katika daraja iliyo chini ya maneno ya Muumba, huku ikiwa juu ya maneno ya viumbe.[16] Wataalamu wa lugha ya Kiarabu wanatoa maelezo yanayothibitisha thamani kubwa ya kifasihi ya kitabu hichi. Miongoni mwa maelezo ya waalamu hao ni kama ifuatavyo:[17]
Kwanza, Ibnu Abi al-Hadid, mwanazuoni wa Ahlu Sunna na mshereheshaji wa karne ya saba, yeye anaona mstari mmoja tu wa kitabu hichi kuwa ni bora kuliko mistari 1,000 ya semi za Ibnu Nabatah.[18]
Pili, George Jordac, mwandishi wa Kikristo, yeye anaamini kuwa kitabu cha Nahju al- Balagha kinashika nafasi ya juu kabisa ya ufasaha baada ya Qur'ani Tukufu.[19]
Tatu, Sheikh Nasif al-Yaziji, mwanafasihi na mshairi wa Lebanon, yeye anaamini kuwa uhifadhi wa Qur'ani Tukufu na Nahju al- Balagha ndiyo nguzo kuu za kuwa nguli katika ufasaha na balagha ya lugha ya Kiarabu.[20]
Nne, Muhyi al-Din Abdul Hamid, mtaalamu wa lugha ya Kiarabu, huyu yeye amekitaja kitabu hichi kama chemchemi inayobubujika balagha na ufasaha, huku akiamini kuwa, maneno ya Nahju al- Balagha ndiyo maneno fasaha zaidi baada ya maneno ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w).[21]
Baadhi ya washereheshaji vya kitabu hichi wanamchukulia Imamu Ali (a.s) kuwa ndiye mwasisi wa fani ya utungaji wa tamthiliya yenye mafunzo.[22] Wataalamu hawa wanaamini kuwa Imamu Ali (a.s) ametumia fani hii chini ya hekima namba 289 ya Nahj al-Balagha akielezea wasifu wa mtu mwema ambaye kiuhalisia hayupo, akitengeneza mhusika wa kufikirika (kidhahania) kwa ajili ya kutoa kigezo bora kwa jamii mbalimbali.[23]
Mvuto kwa Wasio Waislamu
Kitabu cha Nahju al- Balagha kina mvuto mkubwa si tu kwa Mashia, bali hata kwa wasio Mashia and wasio Waislamu, hii ni kutokana na kiwango chake kikubwa vya ufasaha wa maneno yake.[24] George Jordac alitunga kitabu maalumu kiitwacho Rawa'iu Nahju al-Balagha, kwa ajili ya kutoa uchambuzi wa kifasihi na kuchunguza hekima zilizomo ndani ya Nahju al- Balagha.[25] Hali kadhalika, kuna idadi kadhaa ya wasio Waislamu waliosilimu baada ya kukisoma kitabu hichi.[26] Mwanafalsafa wa Kimarekani Muhammad Legenhausen alisilimu na kufuata madhehebu ya Kishia mara tu baada ya kusoma na kutafakari matini za kitabu cha Nahju al- Balagha.[27]
Maudhui ya Nahju al- Balagha
Muhammad Abduh, mmoja wa wanazuoni magwiji Ahlu Sunna akitoa wasifu wa kitabu hiki anasema: Unaposoma kurasa la kitabu hiki, nyakati fulani unajikuta ukipaa katika kipeo cha juu cha lulu za maana na misamiati teule aliyoisuka kwa ufasaha wa juu kabisa, huku nyakati nyingine ukijiona katikati ya vumbi na dhoruba za uwanja wa vita. Na mara nyengine unashuhudia akili iliyotukuka inayodhihiri kupitia nuru maneno, ikifanya kila juhudi kukuokoa wewe kutoka kwenye kiza nene ili ikupandishe hadi kileleni mbingu na kukupa maskani salama katika ulimwengu mtakatifu. Aidha wakati mwingine unajiona upo bega kwa bega na viongozi wa dola, ambapo Imamu Ali anawaongoza na kuwatadibisha katika sanaa ya siasa, busara ya uongozi, na njia za hekima.
Abduh, Sharh Nahju al Balaghah, uk. 10.

Nasir Makarim Shirazi anaona kuwa ujumuishi wa mada mbalimbali pamoja na upana wa maudhui za kitabu hichi ni sifa ya kipekee kabisa kuhusiana na Nahju al-Balagha. Mwanazuoni huyu akikisifu kitabu hichi anasema kuwa, kimesheheni hotuba tamu na zenye maana ya kina juu ya mada tofauti, na wakati mwingine zenye sura ya kupingana zenyewe kwa zenyewe.[29] Ibnu Abi al-Hadid anaeleza kuwa, wakati mwingine Imamu Ali (a.s) ndani ya kitabu hichi anazungumza kama mpiganaji shupavu, na wakati mwingine kama mtawa anayetoa mawaidha na nasaha mbalimbali kwa umma wake.[30] Abbas Mahmoud al-Aqqad amekitaja kitabu hichi kama chemchemi inayobubujika hekima za Kiungu.[31]
Wasomi wanaeleza kuwa, uchambuzi na usomaji wa kitabu hichi unamfanya msomaji kuwa na uelewa mpana juu ya mtazamo wa Imamu Ali (a.s) kuhusiana na Mwenyezi Mungu, mwanadamu, ulimwengu, asili ya uumbaji, na Siku ya Kiyama.[32] Kitabu hichi kinabainisha wazi sifa za kimaadili zinazohitajika katika kujenga shakhsia ya mwanadamu aliyekamilika.[33] Pia kinatou maelezo ya kutosha kuhusiana na utume wa manabii, Uimamu, uongozi na utawala wa serikali, haki za mtu binafsi na jamii, asili ya maumbile, tabia za wanafiki na makafiri, pamoja na kutambulisha makundi katika uwanja wa kihistoria kama vile; Nakithina, Mariqina, na Qasitina.[34] Abdullah Jawadi Amuli anaamini kuwa, Sayyid Radhi aliteua maudhui za Nahju al- Balagha kwa ustadi mkubwa ili kuzuia mifarakano kati ya Shia na Sunni, jambo lililosaidia kuandikwa sherehe makini na madhubuti kupitia wanazuoni wa madhehebu ya Ahlu Sunna.[35]
Muundo wa Maudhui
Maudhui za kitabu cha Nahju al- Balagha zimepangwa kwa mlolongo maalumu katika sehemu tatu kuu ambazo ni hotuba, barua, na semi za hekima.
Hotuba
وَ إِنَّمَا يَنْبَغِي لِأَهْلِ الْعِصْمَةِ وَ الْمَصْنُوعِ إِلَيْهِمْ فِي السَّلَامَةِ أَنْ يَرْحَمُوا أَهْلَ الذُّنُوبِ وَ الْمَعْصِيَةِ وَ يَكُونَ الشُّكْرُ هُوَ الْغَالِبَ عَلَيْهِمْ وَ الْحَاجِزَ لَهُمْ عَنْهُم) Tafsiri: Inawapasa wale wasio na dhambi na waliosalimika katika dini yao, kuwahurumia wenye dhambi na waasi, na kushukuru kwa neema hii, na shukrani hizo ziwashughulishe kwa kiwango ambacho zigeuke kuwa ni ngao ya kuwazuia wasitaje aibu za watu.
Nahju al Balaghah, uhakiki wa Subhi Salih, 1414 H, Hotuba ya 140, uk. 197.
Sehemu ya kwanza inajumuisha hotuba teule za Imamu Ali (a.s) yenye jumla ya hotuba 241.[36] Sayyid Ja'afar Shahidi anaichukulia sehemu hii kama ensaiklopidia ya utamaduni wa Kiislamu iliyosheheni mada mbalimbali, kama vile uelewa wa kumjua Mwenyezi Mungu, kuuelewa ulimwengu, asili ya uumbaji, maumbile ya mwanadamu, na mifumo ya serikali.[37] Mwanazuoni huyu anaamini kuwa, lengo la Imamu Ali (a.s) katika kubainisha masuala haya lilikuwa ni kutoa elimu ya kumjua Mwenyezi Mungu.[38] Sayyid Radhi aliteua hotuba nne miongoni mwa hotuba zote na kuzipa majina maalumu, ambayo ni Shiqshiqiyyah, Gharraa, Ash-bahu, na Qasi'ah.[39]
Hotuba ya Shiqshiqiyyah
Hotuba ya Shiqshiqiyyah ni miongoni mwa hotuba zinazoibua udadisi mwingi ndani ya kitabu cha Nahju al- Balagha.[40] Imamu Ali (a.s) amebainisha masuala yote yanayofungamana na ukhalifa na Uimamu ndani ya hotuba hii, huku akikosoa vikali utendaji kazi wa Makhalifa waliomtangulia, huku akiweka wazi makosa ya utawala wao, pamoja na kuonesha uharamu wa utawala wao.[41] Hali kadhalika, anaelezea lile tukio la kufurika kwa watu waliomiminika kwa ajili ya kula kiapo cha utiifu kwake, pamoja na kubainisha sababu zilizomfanya akubali kubeba majukumu ya uongozi wa serikali baada ya Othman bin Affan.[42]
Hotuba ya Gharra
Imamu Ali (a.s) amehimiza mno suala la ucha Mungu ndani ya Hotuba ya Gharra, huku akikumbusha neema za Mwenyezi Mungu, uhalisia wa dunia kama mahali pa mitihani, matukio ya Siku ya Kiyama, pamoja na mauti.[43] Sayyid Radhi anaeleza kuwa hotuba hii ilitetemesha miili ya wasikilizaji wake na kuwafnaya watokwe na machozi mara tu baada ya kuisikia maneno mazito ya hotuba hiyo.[44] Hotuba hii ilipewa jina la Gharra kutokana na kusheheni kwake fani za lugha na miondoko mizito ya kifasihi kama vile jinasi (mfanano wa lafudhi) na saj'i (vibwagizo).[45]
Hotuba ya Muttaqina
Hotuba ya Muttaqina (Wacha Mungu) ni miongoni mwa hotuba za kiroho na kimalezi zenye uzito mkubwa ndani ya kitabu hichi.[46] Imamu Ali (a.s) alitoa hotuba hii kwa ajili ya kuelezea sifa za wacha Mungu, kufuatia maombi ya mmoja wa wafuasi wake aitwaye Hammam.[47] Kiongozi huyu amezichambua kwa kina sifa mia moja za wacha Mungu na wenye kujiepusha na maovu katika hotuba yake.[48] Hammam al zidiwa na hisia za kiroho jambo lililopelekea kufariki dunia kutokana na mguso mzito wa mawaidha ya hotuba hii.[49]
Barua
Imamu Ali (a.s):
وَ إِنَّمَا يَنْبَغِي لِأَهْلِ الْعِصْمَةِ وَ الْمَصْنُوعِ إِلَيْهِمْ فِي السَّلَامَةِ أَنْ يَرْحَمُوا أَهْلَ الذُّنُوبِ وَ الْمَعْصِيَةِ وَ يَكُونَ الشُّكْرُ هُوَ الْغَالِبَ عَلَيْهِمْ وَ الْحَاجِزَ لَهُمْ عَنْهُم) Tafsiri: Na wala usikihatarishe kitu chochote kwa matumaini ya kupata kilicho zaidi ya hicho (yaani usijihatarishe kwa tamaa ya kupata ziada).
Nahju al Balaghah, uhakiki wa Subhi Salih, 1414 H, Barua ya 31, uk. 403.
Sehemu ya barua za Nahju al- Balagha inajumuisha jumla ya vifungu 79 vyenye barua 63, maandiko 12 ya wasia yanayohusiana na maagizo ya kiserikali, na maandiko mengine ya mikataba mbalimbali.[50] Maudhui ya barua hizi, ambazo walengwa wake wakuu walikuwa ni, magavana, makamanda wa kijeshi, na wakusanyaji wa kodi, yamejikita katika uchambuzi wa masuala ya uongozi wa nchi, utawala bora, na namna maafisa wa kiserikali wanavyopaswa kuamiliana na wananchi wao.[51] Imamu Ali (a.s) anaweka wazi sifa za uongozi thabiti wa kisiasa.[52] Sayyid Ja'afar Shahidi anaamini kuwa, ingawa barua hizi zilitoka kwa mtawala mkuu kwenda kwa magavana wake, ila lugha ya mwandishi wake haikuwa ya kimabavu, bali inasomeka kama barua ya baba mwenye upendo anamuandikia mwanawe.[53] Barua ya Imamu Ali (a.s) kwenda kwa Imamu Hassan (a.s), agizo kwa Malik al-Ashtar kwa ajili ya uongozi wa Misri, na barua kwa Othman bin Hunaif na Ash'ath, zinasimama kama barua mashuhuri zaidi kati ya barua mbalimbali za Imamu Ali (a.s).
Semi Fupi
Imamu Ali (a.s):
إِذَا أَرْذَلَ اللَّهُ عَبْداً حَظَرَ عَلَيْهِ الْعِلْم Tafsiri: Mwenyezi Mungu anapomdhalilisha mja Wake, humzuia kupata elimu (humnyima elimu).
Nahju al Balaghah, uhakiki wa Subhi Salih, 1414 H, Hekima ya 288, uk. 526.
Sehemu ya tatu inajumuisha idadi ya semi fupi za busara 480, ambazo ima ni mawaidha, au majibu ya maswali mbalimbali.[54] Sayyid Radhi alitenga fungu maalumu alilolipa anwani ya Faslun fi Ghara'ibi Kalaamihi (Fungu linalohusu semi za kushangaza za Imamu Ali). Fungu ambalo limekusanya semi ngumu maalumu zinazohitaji ufafanuzi wa kina.[55] Fungu hili lina jumla ya Hadithi 9, ambapo Hadithi ya kwanza kabisa inazungumzia dhana ya kudhihiri kwa Imamu wa Zama (Imamu Mahdi).[56]
Pia angalia: Orodha ya maneno mafupi ya Nahju al-Balagha
Vyanzo vya Nahju al- Balagha
Sayyid Radhi alitaja vyanzo kahdaa alivyovitegemea katika kukusanya semi za Imamu Ali (a.s), vikiwemo kitabu cha Al-Bayan wa al-Tabyin cha Al-Jahidh, Al-Muqtadhab cha Al-Mubarrad, Al-Maghazi cha Sa'id bin Yahya al Umawi, Al-Jamal cha Al-Waqidi, Al-Maqamat cha Abu Ja'afar al-Iskafi, pamoja na Tarikh al Tabari.[57] Tafiti zinasema kuwa kuna idadi ya vyanzo kumi na saba vilivyotajwa moja kwa moja ndani ya kitabu hichi.[58] Sayyid Radhi aliweza kufaidika na maktaba mbili kubwa zilizokuwepo Baghdad kwa ajili ya kazi hiyo, moja ikiwa ya kaka yake Sayyid Murtadha yenye vitabu 80,000 na nyingine ikiwa ni Maktaba ya Baitul-Hikma yenye vitabu 10,000.[59]
Ingawa baadhi ya wanazuoni waliisifu kazi kubwa ya Sayyid Radhi, ila pia hawakuacha kuwasilisha ukosoaji wao na kutaja mapungufu kadhaa ya mwandishi huyu shupavu.[60] Muhammad Taqi al-Shushtari katika tasnifu yake Bahju al-Sabbaghah fi Sharhi Nahji al-Balagha amebainisha akisema kuwa, kwa sababu ya kutegemea kwake vitabu vya Ahlu Sunna peke yake, hiyo ilipelekea kupatikana kwa changamoto zifuatazo:
- Kwanza, kunasibishwa kwa baadhi ya semi na Imamu Ali (a.s) huku semi hizo zikiwa zimetengenezwa na maadui zake.
- Pili, kukatwa kwa baadhi ya sentensi kwa namna inayoharibu maana halisi iliyokusudiwa.
- Tanu, kunasibishwa kwa baadhi ya semi ambazo mapokezi ya Shia yanazikanusha.
- Nne, kunasibishwa kwa baadhi ya Hadithi za Maimamu wengine na Imamu Ali (a.s).
- Tano, kunakiliwa kwa semi zilizosikiwa kupitia ndoto tu.
- Sita, kunakiliwa kusiko sahihi kwa matukio ya kihistoria yaliyofungamana na hotuba husika za Imamu Ali (a.s).[61]
Isnadi za Hotuba, Barua na Hekima

Kutoashiria isnadi za semi za Imamu Ali (a.s) ndani ya kitabu hichi kunatajwa kama changamoto kubwa dhidi ya kazi hii maridadi, jambo lililopelekea baadhi ya wanazuoni kuzichukulia Hadithi za kitabu hichi kama mapokezi yaliyokatika isnadi zake, na kutoweza zitumia kama ushahidi thabiti katika masuala ya kifiqhi.[62] Katika ketetela mbinu ya Sayyid Radhi, watafiti wanasema kuwa, vyanzo vya semi hizi vilikuwa ni mashuhuri mno katika zama zake, na hakukuwa na umuhimu wa kuvitaja katika kunukuu kwake.[63] Pamoja na hayo, wanalugha wengi walichukua juhudi kubwa za kukusanya isnadi kutoka katika vyanzo vya kale vya kihistoria na kuziweka katika mfumo wa nyaraka thibitishi za isnadi za Nahju al- Balagha, ili kuthibitisha usahihi wa kunasibishwa kwake na Imamu Ali (a.s).[64] Zifuatazo ni baadhi ya tasnifu za kitaalamu kuhusiana na vyanzo hivyo.
- Nahju al-Sa’adah fi Mustadrak Nahji al- Balagha kilichotungwa na Muhammad Baqir al-Mahmoudi.[65]
- Madaariku Nahji al-Balagha wa Daf’u al-Shubahati Anhu, kilichoandikwa na Hadi Kashif al-Ghita.[66]
- Masaadiru Nahji al-Balagha fi Madaariki Nahji al-Balagha, kilichotungwa na Sayyid Hibatuddin al-Shahristani (tasnifu hii haijachapishwa).[67]
- Masaadiru Nahji al-Balagha kilichoandikwa na Abdullah Ni'imah.[68]
- Asnaad va Madaarike Nahju al-Balagha[69] pamoja na Ruwwaate wa Mohaddithine Nahju al-Balagha, vilivyotungwa na Muhammad Dashti.[70]
- Bahthe Kutah Piramune Madaarike Nahju al-Balagha, kilichoandikwa na Reza Ostadi.[71]
- Masaadiru Nahji al-Balagha wa Asaaniiduhu, kilichotungwa na Sayyid Abdul Zahra al-Husseini al-Khatib.[72]
Tafsiri

Wataalamu wa lugha wamekitafsiri kitabu hichi katika lugha mbalimbali ulimwenguni zikiwemo lugha ya Kifarsi, Kiingereza, Kifaransa, Kihindi, Kiitaliano, Kituruki cha Istanbul, Kiurdu, Kimalayu, Kialbania, Kibosnia, Kigujarati, Kiashuri, Kiarmenia, Kiswahili, Kihausa, Kijapani, Kichina, Kirusi, Kihispania, pamoja na Kitajiki.[73] Tafiti za kibibliografia zinabainisha kuwa kuna zaidi ya aina 100 za matoleo ya tafsiri za kitabu hichi,[74] ambapo kuna karibu aina 40 za tafsiri kwa lugha ya Kifarsi,[75] takriban tafsiri 10 za Kiingereza, na tafsiri 13 za lugha ya Kiurdu.[76]
Ja'far Subhani anaamini kuwa, ididadi kubwa ya tafsiri za Kifarsi si sahihi na wala hazikubaliki kitaalamu, hii ni kwa sababu watafsiri wake hawakutou (au hawakuwa na) uzito unaostahichi katika elimu ya leksikolojia, fasihi, na sarufi ya lugha ya Kiarabu. Mwanazuoni huyu anasisitiza kuwa, tafsiri ya Mohammad Saleh Barghani pamoja na tafsiri ya Sayyid Ja'afar Shahidi, ndizo kazi zinazoaminika na zenye ufasaha mkubwa kuliko nyengine zote.[77] Wasomi wametaja kazi nyengine kadhaa za watafsiri wengine wa lugha ya Kifarsi ikiwemo kazi ya Ali Naqi Faidhu al-Islam,[78] Abdul Mohammad Ayati,[79] Mohammad Taqi Ja'fari,[80] Mohammad Dashti,[81] Mohammad Mehdi Fooladvand,[82] pamoja na Hossein Ansarian.[83]

Moja ya matoleo muhimu ya lugha ya Kipashto ni lile lenye jina la Goftare Mughaddas, lililotolewa mnamo mwaka 1962 M. Toleo hili lilitolewa likiwa na maelezo ya pembizoni yaliyoandikwa na mshairi aitwaye Amir Hamza Khan Shinwari yaliyotokana na tafsiri ya Kiurdu ya Rais Ahmad Ja'afari.[84]
Watafiti wa Kimagharibi wanaitaja tafsiri ya lugha ya Kiingereza iliyoandikwa na mwanamke aitwaye Tahireh Saffarzadeh kama moja ya kazi mahiri na mashuhuri zaidi za lugha ya Kiingereza.[85]
Tafsiri za Kimashairi
Washairi mbalimbali wamekitafsiri kitabu hichi katika muundo na mtindo wa kimashairi.[86] Miongoni mwa wasanii mashuhuri waliofanya kazi hii katika lugha ya Kifarsi ni Mohammad Ali Ansari Qommi, Mehdi Shafi’i, pamoja na Nasir Barikani. Pia kuna kazi kadhaa kama hizi zilizoanikwa kwa lugha mbalimbali, ikiwemo lugha ya Kisindi iliyoandikwa kupitia kalamu ya Hafiz Mir Mohammad Hassan Ali Khan Hydari, na kwa lugha ya Kituruki kupitia Hassan Molayi Alamdari.[87] Hali kadhalika, baadhi ya magwiji wa lugha wa kule Mumbai nchini India, walikitafsiri kitabu hichi na kukipanga katika muundo wa beti za ushairi kupitia lugha ya Kihindi.[88]
Sherehe
Uandishi wa sherehe za Nahju al- Balagha ulianza miaka michache tu baada ya kukamilika kwa utunzi wake, amali ambayo bado inaendelea hadi leo.[89] Katika historia nzima ya Uislamu, hakuna kitabu chochote kile kilichofafanuliwa na kushereheshwa kwa kiwango kikubwa baada ya Qur'ani Tukufu kama ilivyo kuhusu Nahju al- Balagha.[90] Kuwepo kwa idadi kubwa ya sherehe za Nahju al-Balagha, kunaleta ugumu wa kupata idadi kamili na sahihi ya vitabu vyote vinavyohusiana na Nahju al-Balagha. Na hii ndiyo sababu iliyopelekea kuandikwa kwa makala maalumu kwa ajili ya kutafiti orodha kamili ya vitabu hivyo.[91] Baadhi ya vitabu katika orodha ya sherehe hizi ni kama ifuatavyo:
- Sherehe za Kiarabu:
- Sharhu Nahji al- Balagha: kazi ya Ibnu Abi al-Hadid, mshairi wa madhehebu ya Muutazila,[92] ambaye sherehe yake ilileta mapinduzi makubwa katika mifumo ya uandishi wa sherehe za Nahju al- Balagha.[93]
- Sharhu Nahji al- Balagha: Kazi iliyofanywa na Ibnu Maitham al-Bahrani.[94]
- Minhaaju al-Baraa’a fi Sharhi Nahji al-Balagha: kilichoandikwa na Habibullahi al-Khui.[95]
- Minhaaju al-Baraa’a fi Sharhi Nahji al-Balagha: Kazi ya Qutb al-Rawandi.[96]
- Hada'iqu al-Haqa'iqi fi Sharhi Nahji al-Balagha: kilichotungwa na Qutbuddin al-Kaidari mnamo mwaka 576 Hijria.[97]
- Sherehe za Kifarsi:
- Tarjume wa Tafsiri Nahju al- Balagha: kilichoandikwa na mwanazuoni Mohammad Taqi Ja'fari.[98]
- Tarjume wa Sharh Nahji al-Balagha: Kazi ya Sayyid Ali Naqi Faidhu al-Islam.[99]
- Sharh Nahji al-Balagheh: Kazi iliyoandikwa kupitia kalamu ya Mirza Mohammad Baqir Nawab Lahiji.[100]
- Payame Imam Amir al-Mu'minin: Kitabu kilichoandikwa na mwanazuoni Nasir Makarim Shirazi.[101]
Mustadrak za Kitabu
Kuna idadi kubwa ya wanazuoni waliofanya juhudi za kukusanya semi mbalimbali za Imamu Ali kutoka katika vitabu vya kihistoria ambazo hazikujumuishwa katika matini asili ya Nahju al- Balagha. Kazi za wanazuoni hawa zilichapishwa chini ya anwani ya Mustadrak.[102] Hata Sayyid Radhi mwenyewe pia naye aliacha baadhi ya kurasa za kitabu chake cha Nahju al- Balagha zikiwa tupu, wakati wa kukitunga kitabu hichi. Alifanya hivyo kwa lengo la kupata nafasi ya kuongeza semi mpya pindi atakapozipata hapo mbeleni.[103] Baadhi ya vitabu vya wanazuoni hao mbalimbali ni kama ifuatavyo:
- Al-Tadhyilu ala Nahji al-Balagha: Kazi ya Abdullah bin Ismail al-Halabi, iliyoandikwa mnamo karne ya tano ya Hijria.[104]
- Mulhaqu Nahji al-Balagha: Kazi iliyofanywa na Ahmad bin Yahya bin Naqah mnamo mwaka 729 Hijria.[105]
- Mustadraku Nahji al-Balagha: Kitabu kilichoandikwa na Hadi Kashifu al-Ghitaa, kilichochapishwa mnamo mwaka 1354 Hijria.[106]
- Tamamu Nahji al-Balagha: Tasnifu iliyotungwa na Sayyid Sadiq al-Musawi.[107]
- Nahju al-Saadah fi Mustadraki Nahji al-Balagha: Kazi iliyoandikwa kupitia kalamu ya mwanazuoni Muhammad Baqir al-Mahmoudi.[108]
Uhusiano wa Nahju al-Balagha na Mapinduzi ya Iran

Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, kupitia msaada vya vyombo vya habari na sekta ya utamaduni, ilikifanya kitabu hichi kupenya na kuzagaa kwa haraka mno ndani ya jamii,[110] kiasi ya kwamba hivi sasa kinasimama kama moja ya maandiko yanayopatikana sambamba na Qur'ani Tukufu, katika kila nyumba ya Muislamu nchini humo .[111] Murtadha Mutahhari akielezea suala hili alibainisha akisema kuwa, katika zama zake kulionekana kutiliwa mkazo mkubwa zaidi juu ya kujifunza na kueneza maarifa ya Nahju al- Balagha, ilhali kitabu hichi katika karne zilizopita kilikuwa ni kigeni kwa kila mtu, hata miongoni mwa wanafunzi wa vyuo vya kidini (Hawza).[112]
Kuundwa kwa serikali ya Kiislamu kulipelekea kuandaliwa kwa makongamano na mashindano mengi ya kitaifa na kimataifa kuhusiana na Nahju al-Balagha. Miongoni mwa matukio muhimu zaidi ni ule Mkutano wa Milenia wa Nahju al- Balagha ulijiri mnamo tarehe 18 Mei 1981 M. mjini Tehran, ulioandaliwa kwa lengo la kuadhimisha miaka elfu moja tangu kukamilika kwa ukusanyaji wa kitabu hichi adhimu. Taasisi na vituo vilianzishwa kwa ajili ya kujikita mahususi katika kazi ya kueneza taaluma za Nahju al- Balagha. Wizara ya Elimu kwa upande wake, iliongeza somo maalumu katika baadhi ya fani za sayansi ya jamii. Aidha kulianzishwa rasmi Chuo Kikuu cha Nahju al- Balagha pamoja na Kituo cha Utafiti wa Nahju al- Balagha nchini Iran.[113] Hali kadhalika, baadhi ya vyuo vikuu vilianzisha fani maalumu na ya kitaalamu ya Nahju al- Balagha kwa ajili ya ngazi ya Shahada ya Uzamili na Uzamifu.[114]
Majarida mawili makuu ya kitaalamu yalitolewa chini ya anwani za Pazhouhesh-haye Nahju al-Balagha[115] na Pazhouheshname Nahj al-Balagha (Jarida la Tafiti za Nahju al- Balagha).[116] Tasnifu na makala nyingi mno ziliandikwa zikijikita katika mada za kitabu hichi muhimu.[117] Wanazuoni walisomesha Nahju al- Balagha ndani ya vyuo vya kidini. [118] Hussein Ali Montazeri anaamini kuwa Nahju al- Balagha inapaswa kuingizwa rasmi katika mitaala ya masomo ya kihawza na wazee na wasomi wanapaswa kuisomesha na kuieneza kwa nguvu zao zote.[119]
Programu za Kompyuta na Simu
Kwanza, Programu ya Daneshnameh-ye Alawi au Manhaj al-Noor inajumuisha jumla ya vitabu 110 vyenye zaidi ya juzuu 280, sherehe 33, na maelezo ya nyongeza ndani ya juzuu 163 kupitia lugha za Kifarsi na Kiarabu, pamoja na tafsiri 26 za lugha ya Kifarsi, Kiingereza, na Kifaransa, kazi iliyokamilika kupitia Kituo cha Tafiti za Kompyuta za Sayansi ya Kiislamu cha Noor.[120]
Pili, Programu ya Daneshnameh-ye Jame’i Nahju al-Balagha imekusanya idadi kadhaa ya sherehe na tafsiri katika lugha sita tofauti, uwezo wa kuyafikia maelfu ya mada anuai katika mfumo wa matawi uwezo wa kuonesha vyanzo, programu iliyozalishwa na Kituo cha Tafiti za Kompyuta cha Chuo cha Kidini cha Isfahan.[121]
Taasisi Kuu ya Nahju al- Balagha
Taasisi Kuu ya Nahju al- Balagha iliasisiwa mnamo mwaka 1974 M. ikiwa na lengo la kueneza, kukuza, na kufanya tafiti maalumu na za kitaalamu.[122] Usimamizi wa taasisi hii umefanikisha miradi muhimu ikiwemo maktaba maalumu, ukusanyaji wa nakala za kidijitali kutoka katika maandishi ya mkono ya kitabu hichi, uandalizi wa makongamano ya kisayansi, na uratibu wa kozi za mafunzo.[123]
Shaka na Majibu Yake

Baadhi ya wanazuoni wa Kisunni wamewasilisha shaka mbili kuu kuhusiana na kitabu cha Nahju al- Balagha: kwanza, haiko wazi kama maandiko haya yalikusanywa na Sayyid Radhi au yalikusanywa na kaka yake aitwaye Sayyid Murtadha; pili, kuna uwezo kuwa semi hizi si za Imamu Ali (a.s), bali zilitengenezwa kwa uongo na Sayyid Murtadha au Sayyid Radhi.[124] Ibnu Hajar al-Asqalani anaamini kuwa kitabu hichi is tasnifu ya Sayyid Murtadha, huku akiyahisabu maneno yaliyomo ndani ya kitabu hichi kuwa ni uongo na uzushi usio na mashiko yoyote.[125]
Mkabala na hayo, wanazuoni wa Kishia pamoja na wataalamu wengi wa Ahlu Sunna wanashishilia msimamo thabiti, kuwa mkusanyaji halisi wa Nahju al- Balagha ni Sayyid Radhi, na kwamba yeye aliyakusanya maandiko haya kutoka katika kauli za Imamu Ali (a.s).[126] Watafiti wamesema kuwa, shaka hiyo inayohusu utambulisho wa mkusanyaji, inadhihirisha ukosefu wa mapitio ya matini asili ya kitabu chenyewe, kwa sababu pale mwandishi anapofafanua maneno magumu ya Imamu Ali (a.s), hutumia kauli isemayo: Qala al-Radhi (Sayyid Radhi anasema), jambo linalothibitisha kuwa mkusanyaji wa kazi hii alikuwa ni Sayyid Radhi.[127] Wachambuzi wa vitabu wanasemaj kuwa, idhini rasmi ambazo wanazuoni walikuwa wakizitoa kwa ajili ya kunakili ya kupokea yalimo katika kitabu hichi, ambazo minyororo ya mapokezi yake inafika moja kwa moja kwa Sayyid Radhi, zimefikia kiwango cha thibitisho la mfululizo la mutawatir, ukweli unoondoa shaka ya aina yoyote ile dhidi yake.[128] Najashi, nguli wa elumu ya rijal aliyeishi zama moja na Sayyid Radhi, amekinasibisha kitabu hichi kwa Sayyid Radhi kwa njia sahihi kabisa.[129]
Ibnu Abi al-Hadid akielezea jambo hili anasema kuwa, kutilia shaka juu ya kunasibishwa kwa maudhui za Nahju al- Balagha na Imamu Ali (a.s) ni matokeo ya kufuata matamanio ya nafsi pamoja na ushabiki na taasubi pofu.[130] Hoja thabiti aliyobainisha ukweli huu inajengeka juu ya msingi usemao kuwa, sehemu fulani ya Nahju al- Balagha ni sehemu ya semi za Imamu Ali (a.s), kwa sababu usahihi wake umethibitika kupitia mapokezi ya mfululizo ya mutawatir, na kila mtu mwenye akili anahukumu kuwa matini yote iko katika mtiririko wenye mtindo mmoja unaolingana na unaoshikamana kisawasawa.[131] Ibnu Taymiyyah naye pia alikuwa akiichukulia Nahju al- Balagha kuwa ni maneno na semi za Imamu Ali (a.s), hii ni kwa mujibu wa yale aliyoyanakili mwanafunzi wake aitwaye Salahuddin al-Safadi.[132] Kadhalika, Allamah Bahr al-Ulum amebainisha ukweli huo akisema kuwa, ile kauli inayodai kuwa kitabu hichi kimetengenezwa kwa njia ya uongo ni miongoni mwa tuhuma kubwa katika uwanja vya historia.[133]
Ukusanyaji wa Kale
Katika harakati za kupinga madai ya uzushi, Sayyid Hibatuddin al-Shahrastani anaamini kuwa Sayyid Radhi si mwandishi wa kwanza kabisa kukusanya hotuba na semi za Imamu Ali (a.s), bali kulikuwa na watu wengi kabla yake waliokuwa wakihifadhi hotuba na maneno ya Imamu huyu muadhamu (a.s).[134] Yaaqubi ambaye ni mtaalamu wa fani ya historia, amebainisha wazi katika kitabu chake cha historia, uwepo wa hotuba mia nne zilizorithiwa kutoka kwa Imamu Ali (a.s).[135] Hali kadhalika, Al-Mas'udi ambaye ni mwandishi wa kitabu cha Muruj al-Dhahabi anaeleza kuwa, kulikuwa na watu kadhaa waliohifadhi zaidi ya hotuba 480 zilizotolewa na Imamu Ali (a.s).[136] Ibnu Shu'uba al-Harrani mwandishi wa kitabu Tuhafu al-Uquul, naye pia anaamini kuwa, kama hotuba za Imamu Ali (a.s) zinazohusu tauhidi pekee zingekusanywa pamoja, basi ukubwa wa maandiko hayo ungekuwa sawa na ukubwa wa kitabu cha Tuhafu al-Uquli.[137]
Zaid bin Wahb ndiye mtu wa kwanza kabisa kuandika hotuba za Imamu Ali (a.s) na kuzifuma katika mfumo wa kitabu, naye alikuwa ni mmoja wa wafuasi wa Imamu Ali (a.s). Kitabu chake hicho kile kilichokuwa kikiitwa Kitabu al-Khutabi kilichoendelea kuwepo hadi karne ya tano Hijria.[138] Vitabu kama vile Khutabu Amirul-Mu’minina kilichotungwa na Mas'ada bin Sadaqa, Khutabu Ali kilichoandikwa na Ibrahim bin Hakam al-Fazari, Khutabu Amirul-Muuminina kilichotungwa na Abdul Azim al-Hassani, pamoja na kitabu cha Khutabu Aliyyin wa Kutubihi ila Ummaalihi kilichoandikwa na Ali bin Muhammad al-Madaini, vyote vinasomeka kama miongoni mwa maandiko ya mwanzo kabisa kabla ya zama za Sayyid Radhi.[139]
Nakala za Mkono na Chapa

Kitabu cha Nahju al- Balagha ni miongoni mwa vitabu ambavyo kabla ya teknolojia ya uchapishaji, tayari kulikuwa na mamia ya nakala ya kitabu hicho zilizonakiliwa kwa njia ya maandishi ya mkono.[141] Ripoti mbalimbali zinabainisha kuwa katika maktaba za nchini Iran pekee, kulikuwa na jumla ya nakala 300 za maandishi ya mkono zilizotambuliwa rasmi.[142] Sayyid Abdul Aziz Tabatabai Yazdi ametaja na kuchambua sifa za nakala 160 za kale za Nahju al- Balagha kuanzia karne ya tano hadi ya kumi Hijria.[143]
Maandiko yafuatayo yanatambuliwa kama miongoni mwa nakala muhimu zaidi za maandishi ya mkono za Nahju al- Balagha.
Kwanza, Nakala iliyoandikwa mnamo mwaka 469 Hijria kupitia kalamu ya Hussein bin Hassan Mu'addib, nakala inayohifadhiwa ndani ya Maktaba ya Ayatullah Mar'ashi Najafi.
Pili, Nakala iliyoandikwa mnamo mwaka 485 Hijria kupitia mkono wa Adnan bin Ibrahim inayopatikana ndani ya Maktaba ya Sayyid Muhammad Ali Rawdhati kule Isfahan.
Tatu, Nakala iliyoandikwa mnamo mwaka 494 Hijria kupitia kalamu ya Fadhlullah bin Tahir Husseini ambayo chapa ya picha ilichapishwa na Maktaba ya Msikiti Mkuu wa Tehran mnamo mwaka 1402 Hijria.
Nne, Nakala mbalimbali zilizorithiwa tangu karne ya tano Hijria zinazohifadhiwa ndani ya Maktaba ya Hussein Ali Mahfuz, Maktaba ya Sayyid Hibatuddin al-Shahrastani, Maktaba ya Chuo Kikuu cha Sepahsalar mjini Tehran, na Kituo cha Uhuishaji wa Turathi za Kiislamu huko Qum.[144]
Publications (Chapa)
Mashirika na taasisi za uchapishaji zimekichapisha kitabu hichi mamia ya mara ndani ya nchi mbalimbali kama Iran, Misri, Lebanon, Syria, na Qatar, kikiwa kimesindikizwa na sherehe pamoja na tafsiri za lugha tofauti.[145] Chapa ya kale zaidi ya kitabu hichi ilijitokeza mnamo mwaka 1247 Hijria kule Tabriz.[146] Miongoni mwa matoleo muhimu ya chapa za Nahju al- Balagha ni hizi zifuatazo.
Kwanza, Chapa ya nchi ya Misri ya mwaka 1317 Hijria kupitia uhakiki wa Mohammad Hassan Na'il al-Marsafi ndani ya juzuu mbili.
Pili, Toleo la Beirut lililotokea ikiwa na sherehe ya Mohammad Abdu mnamo mwaka 1302 Hijria.
Tatu, Toleo la Beirut lililotokea kupitia usahihishaji wa Subhi Salih mnamo mwaka 1387 Hijria.
Four, Toleo la Tehran lililotokea ikiwa na tafsiri ya Sayyid Ali Naqi Faidhu al-Islam mnamo mwaka 1405 Hijria.
Tano, Toleo la Taasisi Kuu ya Nahju al- Balagha lililotokea mjini Tehran kupitia usahihishaji wa Azizullah Atardi mnamo mwaka 1413 Hijria.[147]
Tafiti Mahususi

Katika mada ya Nahju al- Balagha, vitabu mbalimbali vimeandikwa ikiwemo.
Kwanza, Siiri dar Nahju al-Balagha: Kitabu hichi kinakusanya makala zilizoandikwa na Murtadha Mutahhari zikijikita katika mada za teolojia, ibada, uadilifu, na ukhalifa, na kimeitafsiriwa katika lugha mbalimbali kama vile Kiarabu na Kiingereza.[148]
Pili, شناخت ویژگیهای نهج البلاغه (Kuelewa Sifa za Nahj al-Balagha): Kilichoandikwa na Muhammad Dashti kikieleza sifa za ufasaha na ukweli vya vyanzo vya kitabu hichi.[149]
Tatu, امیرالمؤمنین و نهج البلاغه (Amir al-Mu'minin na Nahj al-Balagha): Kazi iliyotungwa na Azizullah Atardi inayochambua maisha ya Sayyid Radhi na kujibu shaka zinazohusu kitabu hichi.[150]
Four, کاوشی در نهج البلاغه (Utafiti katika Nahj al-Balagha): Mfululizo wa makala za wasomi mbalimbali kama Mohammad Taqi Ja'afari na Abdullah Jawadi Amuli zilizochapishwa na Taasisi ya Nahju al- Balagha.[151]
Tano, آموزش نهج البلاغه (Mafunzo ya Nahj al-Balagha): Kitabu kilichoandikwa na Sayyid Mohammad Mehdi Jafari kikiwa kimetolewa na Wizara ya Elimu ya Iran.[152]
Rejea
- ↑ Mostafavi, «Kutambulisha Nahju al Balaghah», uk. 23.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 11.
- ↑ Mostafavi, Nahju al Balaghah wa Qur'an, uk. 32.
- ↑ Ostadi, Kitabnameh ye Nahju al Balaghah, uk. 5.
- ↑ Amin, A’yan al Shiah, Juz. 9, uk. 218.
- ↑ Rafiei, «Uasili wa Kialawi wa Nahju al Balaghah», uk. 131.
- ↑ Nuri, Mustadrak al Wasa'il, Juz. 21, uk. 204.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 559.
- ↑ Jafari, Sayyid Radhi, uk. 22.
- ↑ Amin, A’yan al Shiah, Juz. 9, uk. 218.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, Utangulizi, uk. 34.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, Utangulizi, uk. 35.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, Utangulizi, uk. 36.
- ↑ Abduh, Sharh Nahju al Balaghah, uk. 10.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 32.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 24.
- ↑ Al Husseini, Masaadir Nahji al Balaghah, Juz. 1, uk. 105.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 7, uk. 214.
- ↑ Jordac, Sauti ya Uadilifu wa Kibinadamu, uk. 282.
- ↑ Al Husseini, Masaadir Nahji al Balaghah, Juz. 1, uk. 108.
- ↑ Muhyi al Din, «Utangulizi», katika Sharh Nahji al Balaghah, uk. 2.
- ↑ Khoei, Minhaaj al Bara’ah, Juz. 21, uk. 379.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 19, uk. 184; Khoei, Minhaaj al Bara’ah, Juz. 21, uk. 379; Makarim, Payame Imame Amir al Mu'minin, Juz. 14, uk. 395.
- ↑ Jordac, Sauti ya Uadilifu wa Kibinadamu, uk. 282; «نهج البلاغه از نگاه آنتوان بارا نویسنده مسیحی» (Nahj al Balaghah kwa mtazamo wa Antoine Bara, mwandishi Mkristo), Ahlolbait.
- ↑ Jordac, Rawa’i’ Nahju al Balaghah, uk. 4.
- ↑ «ماجرای مسلمانشدن یک آمریکایی به برکت نهج البلاغه» (Kisa cha kusilimu kwa Mmarekani kwa baraka ya Nahj al Balaghah), Hawzah News Agency; «اظهارات خواندنی جوان اروپایی که شیعه شد» (Kauli za kuvutia za kijana wa Ulaya aliyekuwa Shia), Estebsar; «مسلمانشدن ۸۰ سرخپوست با نهج البلاغه» (Wahindi Wekundu 80 walisilimu kupitia Nahj al Balaghah), Saheb News; «پدر و مادرم از طریق نهج البلاغه مسلمان شدند» (Wazazi wangu walisilimu kupitia Nahj al Balaghah), ISNA; «آشنایی با آموزههای متعالی نهج البلاغه زمینهساز تشرف یک جوان اهل کوزوو به تشیع بود» (Ufahamu wa mafunzo matukufu ya Nahj al Balaghah ulimvutia kijana wa Kosovo kuwa Shia), Iqna News.
- ↑ «مسلمانشدن پروفسور لگنهاوزن با مطالعه نهج البلاغه» (Profesa Muhammad Legenhausen alisilimu kwa kusoma Nahj al Balaghah), Aparat; «پروفسور محمد لگنهاوزن چگونه مسلمان و شیعه شد؟» (Profesa Muhammad Legenhausen alisilimu na kuwa Shia vipi?), YouTube.
- ↑ «بندی از شرح نهج البلاغه ابن ابیالحدید» (Sehemu kutoka Sharhu Nahj al Balaghah ya Ibn Abi al-Hadid), Maktaba na Makumbusho ya Kitaifa ya Malek.
- ↑ Makarim, Payame Imame Amir al Mu'minin, Juz. 1, uk. 39.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 11, uk. 153.
- ↑ Aqqad, Abqariyyat al Imam Ali, uk. 127.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 44.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 45.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 44.
- ↑ Jawadi Amoli, «تفسیر sora ya Juma, kipindi cha 10», Tovuti ya Esra.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 39.
- ↑ Shahidi, «Utangulizi», katika Nahju al Balaghah, uk. 14.
- ↑ Shahidi, «Utangulizi», katika Nahju al Balaghah, uk. 14.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 19.
- ↑ Ibn Maitham, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 251.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 48.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 49.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 107.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 114.
- ↑ Khoei, Minhaaj al Bara’ah, Juz. 6, uk. 70.
- ↑ Hushyar, «Sura ya Mwanadamu Mkamilifu», uk. 20.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 303.
- ↑ Mutahhari, Majmu'ah Athar, Juz. 16, uk. 360.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 306.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 19.
- ↑ Shahidi, «Utangulizi», katika Nahju al Balaghah, uk. 15.
- ↑ Beheshti, «Maadili ya Kisiasa», uk. 12.
- ↑ Shahidi, «Utangulizi», katika Nahju al Balaghah, uk. 15.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 469.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 515.
- ↑ Sayyid Radhi, Nahju al Balaghah, uk. 517.
- ↑ Ibrahim, «Utangulizi», katika Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 7.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 24-25.
- ↑ Mostafavi, «Kutambulisha Nahju al Balaghah», uk. 35-36.
- ↑ Shushtari, Bahj al-Sabbaghah, Juz. 1, uk. 20.
- ↑ Shushtari, Bahj al-Sabbaghah, Juz. 1, uk. 20-22.
- ↑ Mehrizi, Ufahamu wa Matini, uk. 159.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 22.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 25.
- ↑ Mahmoudi, Nahj al-Sa'adah, Juz. 1, uk. 5.
- ↑ Kashif al-Ghita, Mustadrak Nahj al-Balagha, uk. 193.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 26.
- ↑ Nimah, Masadir Nahj al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Dashti, Asnad wa Madarik-e Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Dashti, Asnad wa Madarik-e Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Ostadi, Kitabnameh-ye Nahju al-Balagha, uk. 8.
- ↑ Al Husseini, Masaadiru Nahji al-Balagha, Juz. 1, uk. 6.
- ↑ Dinparvar, «Nahju al-Balagha», uk. 60.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 77.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 78.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 77.
- ↑ Subhani, «Kupitia Nahju al Balaghah», uk. 45.
- ↑ Faidh al-Islam, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 10.
- ↑ Ayati, Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Jafari, Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Dashti, Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Fooladvand, Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Ansarian, Nahju al-Balagha, uk. 5.
- ↑ Irna, «Habari za Pakistan», uk. 2.
- ↑ «صفارزاده نهج البلاغه را به سه زبان ترجمه کرد», Tovuti ya Hawzah.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 78.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 78-79.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 78.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 73.
- ↑ Boroujerdi, «Sherehe za Nahju al Balaghah», uk. 119.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 73.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 500.
- ↑ Boroujerdi, «Sherehe za Nahju al Balaghah», uk. 124.
- ↑ Ibn Maitham, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 400.
- ↑ Khoei, Minhaaj al Bara’ah, Juz. 1, uk. 300.
- ↑ Rawandi, Minhaaju al-Bara’ah, Juz. 1, uk. 250.
- ↑ Kaidari, Hada'iqu al-Haqa'iqi, Juz. 1, uk. 300.
- ↑ Jafari, Tafsiri ya Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 500.
- ↑ Faidh al-Islam, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 450.
- ↑ Lahiji, Sharh Nahji al-Balagheh, uk. 300.
- ↑ Makarim, Payame Imam Amir al-Mu'minin, Juz. 1, uk. 400.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 28.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 28.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 28.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 28.
- ↑ Kashif al-Ghita, Mustadraku Nahji al-Balagha, J.1, uk.16.
- ↑ Mousavi, Tamamu Nahji al-Balagha, Juz. 1, uk. 500.
- ↑ Mahmoudi, Nahj al-Sa'adah, Juz. 1, uk. 500.
- ↑ Tember-haye Iran, uk. 19.
- ↑ Dinparvar, «Nahju al-Balagha», uk. 61.
- ↑ Ripoti ya Kitabu, Nahju al-Balagha, uk. 98.
- ↑ Mutahhari, Majmu'ah Athar, Juz. 16, uk. 347.
- ↑ Dinparvar, «Nahju al-Balagha», uk. 61-62.
- ↑ «مروری بر شناسنامه رشته علوم و معارف نهج البلاغه در کشور» (Muhtasari wa taaluma ya Sayansi na Maarifa ya Nahj al Balaghah nchini), Jumuiya ya Kisayansi ya Nahj al Balaghah.
- ↑ «پژوهشهای نهج البلاغه» (Jarida la Tafiti za Nahj al Balaghah), Pazhouhesh-haye Nahj-al-Balagha.
- ↑ «سایت پژوهشنامه نهج البلاغه» (Tovuti ya Jarida la Utafiti la Nahj al Balaghah), Chuo Kikuu cha Bu-Ali Sina.
- ↑ Dinparvar, «Nahju al-Balagha», uk. 62.
- ↑ Mutahhari, Adl-e Ilahi, uk. 212; Montazeri, Darsa za Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 63.
- ↑ Montazeri, Darsa za Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 63.
- ↑ Noor, «Manhaj al Noor», uk. 164.
- ↑ Sajjadi, «Programu za Isfahan», uk. 226.
- ↑ Zamani, «Bonyad-e Nahju al-Balagha», uk. 34.
- ↑ Rabiei, «Bonyad-e Nahju al-Balagha», uk. 439.
- ↑ Ibn Khallikan, Wafayat al-A'yan, Juz. 3, uk. 313; Yafei, Mira'at al-Jinan, Juz. 3, uk. 43.
- ↑ Ibn Hajar, Lisan al-Mizan, Juz. 4, uk. 223.
- ↑ Davani, «Mwandishi wa Nahju al Balaghah», uk. 117.
- ↑ Atardi, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 1, uk. 14.
- ↑ Shahrestani, «Ma huwa Nahju al Balaghah», uk. 13.
- ↑ Najashi, Rijal al-Najashi, uk. 398.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 10, uk. 127.
- ↑ Ibn Abi al Hadid, Sharh Nahju al Balaghah, Juz. 10, uk. 128.
- ↑ Safadi, Al-Wafi bil-Wafayat, Juz. 2, uk. 277.
- ↑ Bahr al-Ulum, Al-Fawa'id al-Rijaliyah, Juz. 3, uk. 118.
- ↑ Shahrestani, «Ma huwa Nahju al Balaghah», uk. 21.
- ↑ Yaqubi, «Mwenendo wa Watu», uk. 15.
- ↑ Masudi, Muruju al-Dhahabi, Juz. 2, uk. 419.
- ↑ Harrani, Tuhafu al_Uquli, uk. 61.
- ↑ Mostafavi, «Kutambulisha Nahju al Balaghah», uk. 33.
- ↑ Mostafavi, «Kutambulisha Nahju al Balaghah», uk. 33-35.
- ↑ «نهجالبلاغه ایلخانان» (Nahjul Balaghah ya Enzi ya Ilkhanid), Maktaba na Makumbusho ya Kitaifa ya Malek.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 83.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 83.
- ↑ Tabatabaei, «Nakala za Kale za Nahju al Balaghah», uk. 5.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 84-85.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 80.
- ↑ Tabatabaei, «Katika Uwanja wa Nahju al Balaghah», uk. 24.
- ↑ Hafezyan, «Nahju al Balaghah», uk. 80.
- ↑ Mutahhari, «Kupitia Nahju al Balaghah», uk. 17-18.
- ↑ Dashti, «Kutambua Sifa za Nahju al Balaghah», uk. 5.
- ↑ Atardi, Amirul-Mu'minin na Nahju al Balaghah, uk. 5.
- ↑ Wataalamu, «Utafiti katika Nahju al Balaghah», uk. 5.
- ↑ Jafari, «Mafunzo ya Nahju al Balaghah», uk. 5.
Vyanzo
- Abduh, Muhammad. Sharhu Nahji al- Balagha. Cairo: Matba'at al-Instiqamah, b.t.
- Al-Husayni al-Khatib, Sayyid Abd al-Zahra. Masadiru Nahji al- Balagha wa Asaniduhu. Beirut: Dar al-Zahra, 1409 H.
- Amin, Muhsin. A‘yanu al-Shi‘ah. Beirut: Dar al-Ta‘aruf li al-Matbu‘at, 1406 H.
- Aqqad, Abbas Mahmud. Abqariyyatu al-Imamu Ali. Beirut: Al-Maktabah al-Asriyah, 1431 H.
- Atardi, Azizullah. Amir al-Mu’minin wa Nahju al- Balagha. Tehran: Atarod, 2000 M.
- Atardi, Azizullah. "Muqaddimah". Katika Sharhu Nahji al- Balagha ya mwanazuoni wa karne ya nane. Qum: Atarod, 1996 M.
- Ayati, Abd al-Muhammad. Nahju al- Balagha. Tehran: Daftar-e Nashr-e Farhang-e Islami, 1999 M.
- Bahr al-Ulum, Muhammad Mahdi ibn Murtadha. Al-Fawa’id al-Rijaliyyah. Tehran: Maktabat al-Sadiq, 1984 M.
- Beheshti, Ahmad; Sadriyeh, Payam. «اخلاق سیاسی در نامههای نهج البلاغه» (Maadili ya kisiasa katika barua za Nahju al- Balagha). Pazhouhesh-haye Nahju al- Balagha, Na. 30 (2010 M), uk. 12–35.
- Boroujerdi, Mustafa; Sadra'i Khoei, Ali. «شرحهای نهج البلاغه» (Sherehe za Nahju al- Balagha). Katika Daneshnameh-ye Imamu Ali (a), Juz. 12. Tehran: Mu'assasah-ye Farhangi wa Andisheh-ye Islami, 2001 M.
- Dashti, Muhammad. Asnad wa Madarik-e Nahju al- Balagha. Qum: Mu'assasah-ye Farhangi wa Tahqiqati-ye Amir al-Mu'minin (a), 1999 M.
- Dashti, Muhammad. Ruwat wa Muhaddithan-e Nahju al- Balagha. Qum: Mu'assasah-ye Farhangi wa Tahqiqati-ye Amir al-Mu'minin (a), 1999 M.
- Dashti, Muhammad. Shenakht wa Vizhegihaye Nahju al- Balagha. Qum: Mu'assasah-ye Farhangi wa Tahqiqati-ye Amir al-Mu'minin (a), 2013 M.
- Davani, Ali. «سید رضی گردآورنده نهج البلاغه» (Sayyid Radhi, mkusanyaji wa Nahju al- Balagha). Katika Maqalat darbareh-ye Nahju al- Balagha wa Gardavarandeh-ye An. Tehran: Bonyad-e Nahju al- Balagha, 1994 M.
- Dinparvar, Sayyid Jamal al-Din. «نهج البلاغه؛ سندی ماندگار» (Nahju al- Balagha; hati ya kudumu). Pazhouhesh-haye Nahju al- Balagha, Na. 2–3 (2001 M), uk. 60–75.
- Faidh al-Islam, Sayyid Ali Naqi. Tarjumah wa Sharh-e Nahju al- Balagha. Tehran: Mu'assasah-ye Chap wa Nashr, 2000 M.
- Hafezyan Baboli, Abulfazl. «نهج البلاغه» (Nahju al- Balagha). Katika Daneshnameh-ye Imamu Ali (a), Juz. 12. Tehran: Mu'assasah-ye Farhangi wa Andisheh-ye Islami, 2001 M.
- Harrani, Ibn Shu'bah. Tuhaf al-'Uqul 'an Al al-Rasul. Qum: Daftar-e Intisharat-e Islami, 1404 H.
- Hushyar, Yaser; Tajalil, Jalil. «بررسی تطبیقی سیمای انسان کامل در خطبه متقین نهج البلاغه و آثار عزیزالدین نسفی» (Tathmini linganishi ya sura ya mwanadamu mkamilifu katika Hotuba ya Muttaqin ya Nahju al- Balagha na athari za Aziz al-Din Nasafi). Pazhouhesh-haye Nahju al- Balagha, Na. 46 (2015 M), uk. 20–35.
- Ibn Hajar al-Asqalani, Ahmad ibn Ali. Lisan al-Mizan. Beirut: Mu'assasat al-A'lami li al-Matbu'at, 1390 H.
- Ibn Khallikan, Ahmad ibn Muhammad. Wafayat al-A'yan wa Anba' Abna' al-Zaman. Beirut: Dar Sadir, 1900 M.
- Kaidari, Qutb al-Din. Hada'iq al-Haqa'iq fi Sharh Nahju al- Balagha. Qum: Bonyad-e Nahju al- Balagha, 1416 H.
- Kashif al-Ghita, Hadi. Mustadrak Nahju al-Balagha. Beirut: Maktabat al-Andalus, b.t.
- Lahiji, Mirza Muhammad Baqir. Sharh Nahju al- Balagha. Tehran: Markaz-e Pazhouhesh-e Miras-e Maktub, 2000 M.
- Mahmoudi, Muhammad Baqir. Nahju al-Sa'adah fi Mustadrak Nahju al- Balagha. Tehran: Wizarat-e Farhang wa Irshad-e Islami, 1418 H.
- Mas'udi, Ali ibn al-Husayn. Muruj al-Dhahab. Qum: Dar al-Hijrah, 1409 H.
- Mehrizi, Mehdi. Shenakht-e Mutun-e Hadith wa Nahju al- Balagha. Qum: Markaz-e Jahani-ye Ulum-e Islami, 1998 M.
- Moayedi, AbulHassan. «راهنمای پژوهشهای نهج البلاغه» (Mwongozo wa tafiti za Nahju al- Balagha). Motale'at-e Tafsir, Na. 1 (2010 M), uk. 1–15.
- Montazeri, Husayn Ali. Dars-haye Nahju al- Balagha. Tehran: Daftar-e Nashr-e Sara'i, 2004 M.
- Mortazavi, Sayyid Jalil. Pazhouheshi dar Nahju al- Balagha. Tehran: Dar al-Irfan, 2021 M.
- Mostafavi, Sayyid Javad. «معرفی نهج البلاغه» (Utambulisho wa Nahju al- Balagha). Meshkat, Na. 1 (1982 M), uk. 23–35.
- Mostafavi, Sayyid Javad. Rabiteh-ye Nahju al- Balagha wa Qur'an. Tehran: Bonyad-e Nahju al-Balagha, 2007 M.
- Musawi, Sayyid Sadiq. Tamam Nahju al-Balagha. Beirut: Mu'assasat al-A'lami li al-Matbu'at, 1426 H.
- Mutahhari, Murtadha. Adl-e Ilahi. Tehran: Sadra, 1997 M.
- Mutahhari, Murtadha. Fi Rihab Nahju al- Balagha. Beirut: Dar al-Islamiyyah, 1413 H.
- Mutahhari, Murtadha. Glimpses of the Nahju al- Balagha. Tehran: Ahl al-Bayt (a) World Assembly, 2013 M.
- Mutahhari, Murtadha. Majmu'ah Athar. Tehran: Sadra, 1993 M.
- Mutahhari, Murtadha. Sayri dar Nahju al- Balagha. Tehran: Sadra, 2000 M.
- Najashi, Ahmad ibn Ali. Rijal al-Najashi. Qum: Daftar-e Intisharat-e Islami, 1365 Sh.
- Ni'imah, Abdullah. Masadir Nahju al- Balagha. Najaf: Maktabat al-Rawdah al-Haydariyyah, 1392 H.
- Noor. «منهاج النور (دانشنامه علوی)» (Manhaj al-Noor [Daneshnameh-ye Alawi]). Pazhouhesh wa Howzah, Na. 15 (2003 M), uk. 164–170.
- Nuri, Mirza Husayn. Mustadrak al-Wasa'il wa Mustanbat al-Masa'il. Beirut: Mu'assasat Al al-Bayt li-Ihya' al-Turath, 1408 H.
- Qifti, Ali ibn Yusuf. Inbah al-Ruwat 'ala Anbah al-Nuhat. Beirut: Al-Maktabah al-Asriyyah, 1424 H.
- Rabiei, Manijeh. «بنیاد نهج البلاغه» (Bonyad-e Nahju al- Balagha). Katika Daneshnameh-ye Jahan-e Islam, Juz. 4. Tehran: Bonyad-e Da'irat al-Ma'arif-e Bozorg-e Islami, 1998 M.
- Rafiei, Behrouz. «اصالت علوی نهج البلاغه» (Asili ya Kialawi ya Nahju al- Balagha). Roshanshenasi-ye Olum-e Ensani, Na. 26 (2001 M), uk. 131–150.
- Rah-avard-e Noor. «سی دی دانشنامه نهج البلاغه» (CD ya Daneshnameh-ye Nahju al- Balagha). Rah-avard-e Noor, Na. 13 (2000 M), uk. 164–170.
- Rawandi, Qutb al-Din. Minhaj al-Bara'ah fi Sharh Nahju al- Balagha. Qum: Maktabat Ayatullah Mar'ashi Najafi, 1406 H.
- Safadi, Salah al-Din. Al-Wafi bi al-Wafayat. Beirut: Dar Ihya' al-Turath al-Arabi, 1420 H.
- Sajjadi, Sayyid Ahmad. «معرفی سی دی نهج البلاغه حوزه علمیه اصفهان» (Utambulisho wa CD ya Nahju al- Balagha ya Hawzah ya Isfahan). Pazhouhesh wa Howzah, Na. 3 (2000 M), uk. 226–235.
- Sayyid Radhi, Muhammad ibn Husayn. Nahju al- Balagha. Tafsiri ya Abd al-Muhammad Ayati. Tehran: Daftar-e Nashr-e Farhang-e Islami, 1999 M.
- Sayyid Radhi, Muhammad ibn Husayn. Nahju al- Balagha. Tafsiri ya Husayn Ansarian. Tehran: Payam-e Azadi, 2009 M.
- Sayyid Radhi, Muhammad ibn Husayn. Nahju al- Balagha. Tafsiri ya Muhammad Dashti. Qum: Mashhur, 2000 M.
- Sayyid Radhi, Muhammad ibn Husayn. Nahju al- Balagha. Tafsiri ya Muhammad Mahdi Fuladvand. Tehran: Saeb, 2001 M.
- Sayyid Radhi, Muhammad ibn Husayn. Nahju al- Balagha. Tafsiri ya Muhammad Taqi Ja'fari. Mashhad: Bonyad-e Pazhouheshhaye Islami, 2001 M.
- Sayyid Radhi, Muhammad ibn Husayn. Nahju al- Balagha. Qum: Hijrat, 1414 H.
- Shahidi, Sayyid Ja'far. «مقدمه» (Utangulizi). Katika Nahju al- Balagha. Tehran: Sherkat-e Entesharat-e Elmi wa Farhangi, 1999 M.
- Shahristani, Sayyid Hibat al-Din. Ma Huwa Nahju al- Balagha. Beirut: Dar al-Thaqafah, 1961 M.
- Shushtari, Muhammad Taqi. Bahj al-Sabbaghah fi Sharh Nahju al- Balagha. Tehran: Amirkabir, 1997 M.
- Taasisi ya Tebyan. Tembr-haye Iran. Qum: Mu'assasah-ye Farhangi wa Ettela'rasani-ye Tebyan, 2008 M.
- Tabataba'i, Sayyid Abd al-Aziz. «بازماندههای نسخههای خطی نهج البلاغه تا پایان قرن هشتم هجری» (Nakala zilizosalia za maandishi ya mkono ya Nahju al- Balagha hadi mwisho wa karne ya nane Hijria). Turathuna, Na. 5 (1406 H), uk. 5–25.
- Tabataba'i, Sayyid Abd al-Aziz. «بازماندههای نسخههای خطی نهج البلاغه» (Nakala zilizosalia za maandishi ya mkono za Nahju al- Balagha). Turathuna, Na. 7–8 (1406 H), uk. 15–35.
- Tabataba'i, Sayyid Abd al-Aziz. «در قلمرو نهج البلاغه» (Katika viuga vya Nahju al- Balagha): Turathuna, Na. 29 (1412 H), uk. 24–50.
- Wataalamu. Pazhouheshi dar Nahju al- Balagha. Tehran: Bonyad-e Nahju al- Balagha, 2022 M.
- Yafei, Abdullah ibn As'ad. Mira'at al-Jinan wa Ibrat al-Yaqzan. Beirut: Dar al-Kutub al-Ilmiyyah, 1417 H.
- Yaqubi, Ahmad ibn Ishaq. Mushakalat al-Nas li-Zamanihim. Beirut: Dar al-Kitab al-Jadid, 1980 M.
- Zamani, Karim. «آشنایی با نهادهای علمی و فرهنگی بنیاد نهج البلاغه» (Utambulisho wa taasisi za kielimu na kiutamaduni za Bonyad-e Nahju al- Balagha). Keyhan-e Farhangi, Na. 31 (1986 M), uk. 34–45.
- «بندی از شرح نهج البلاغه ابن ابیالحدید» (Sehemu kutoka Sharhu Nahju al- Balagha ya Ibn Abi al-Hadid). Maktaba na Makumbusho ya Kitaifa ya Malek. Tarehe ya kuchapishwa: 10 Aprili 2021. Tarehe ya kutembelewa: 2 Agosti 2026.
- «پژوهشهای نهج البلاغه» (Jarida la Tafiti za Nahju al- Balagha). Pazhouhesh-haye Nahju al-Balagha. Tarehe ya kuchapishwa: 10 Aprili 2026. Tarehe ya kutembelewa: 2 Agosti 2026.
- «نهج البلاغه از نگاه آنتوان بارا نویسنده مسیحی» (Nahju al- Balagha kwa mtazamo wa Antoine Bara, mwandishi Mkristo). Ahlolbait. Tarehe ya kuchapishwa: 10 Desemba 2017. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.
- «اظهارات خواندنی جوان اروپایی که شیعه شد» (Kauli za kuvutia za kijana wa Ulaya aliyekuwa Shia). Estebsar. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.
- «صفارزاده نهج البلاغه را به سه زبان ترجمه کرد» (Saffarzadeh alitafsiri Nahju al- Balagha katika lugha tatu). Hawzah. Tarehe ya kuchapishwa: 27 Agosti 2008. Tarehe ya kutembelewa: 8 Julai 2024.
- «تفسیر سوره جمعه جلسه ۱۰» (Tafsiri ya Sura al-Jumu'ah, kipindi cha 10). Tovuti Rasmi ya Ayatullah Jawadi Amuli. Tarehe ya kuchapishwa: 16 Aprili 2018. Tarehe ya kutembelewa: 8 Agosti 2024.
- «سایت پژوهشنامه نهج البلاغه» (Tovuti ya Jarida la Utafiti la Nahju al- Balagha). Chuo Kikuu cha Bu-Ali Sina. Tarehe ya kutembelewa: 8 Agosti 2024.
- «مروری بر شناسنامه رشته علوم و معارف نهج البلاغه در کشور» (Muhtasari wa taaluma ya Sayansi na Maarifa ya Nahju al- Balagha nchini). Jumuiya ya Kisayansi ya Nahju al- Balagha. Tarehe ya kutembelewa: 8 Agosti 2024.
- «مسلمانشدن ۸۰ سرخپوست با نهج البلاغه» (Wahindi Wekundu 80 walisilimu kupitia Nahju al- Balagha). Saheb News. Tarehe ya kuchapishwa: 8 Septemba 2014. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.
- «مسلمانشدن پروفسور لگنهاوزن با مطالعه نهج البلاغه» (Profesa Muhammad Legenhausen alisilimu kwa kusoma Nahju al- Balagha). Aparat. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.
- «ماجرای مسلمانشدن یک آمریکایی به برکت نهج البلاغه» (Kisa cha kusilimu kwa Mmarekani kwa baraka ya Nahju al- Balagha). Hawzah News Agency. Tarehe ya kuchapishwa: 8 Aprili 2012. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.
- «آشنایی WITH مشاهیر و نخبگان فرهنگی پاکستان» (Utambulisho wa watu mashuhuri na wasomi wa utamaduni wa Pakistan). IRNA. Tarehe ya kuchapishwa: 10 Februari 2010. Tarehe ya kutembelewa: 24 Septemba 2024.
- «پدر و مادرم از طریق نهج البلاغه مسلمان شدند» (Wazazi wangu walisilimu kupitia Nahju al- Balagha). ISNA. Tarehe ya kuchapishwa: 20 Oktoba 2014. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.
- «پروفسور محمد لگنهاوزن چگونه مسلمان و شیعه شد؟» (Profesa Muhammad Legenhausen alisilimu na kuwa Shia vipi?). YouTube. Tarehe ya kutembelewa: 15 Agosti 2024.