Imamu Hussein (a.s)

Kutoka wikishia
Kaburi la Imamu Hussein (a.s)

Hussein bin Ali bin Abi Talib (a.s) (Kiarabu: (ع)الإمام الحسين بن علي بن أبي طالب ) Alizaliwa mwaka wa 4 Hijiria na kufariki mwaka wa 61 Hijiria. Hussein bin Ali bin Abi Talib (a.s) kwa upande wa madhehebu ya Kishia anatambuliwa kiumaarufu kama: Imamu Hussein (a.s). Lakabu mbili maarufu ni; Aba Abdullah na Sayyid Al-Shohadaa. HuSsein bin Ali (a.s) ni Imamu wa tatu miongoni mwa Maimamu wa Kishia. Aliuawa kishahidi katika tukio la Ashura katika ardhi ya Karbala. Yeye ni mtoto wa pili wa Imam Ali na bibi Fatimatu Al-Zahraa (a.s) na ni mjukuu wa Mtume Muhammad (s.a.w.w). Baada ya kifo cha kaka yake (Imamu Hassan (a.s)) , alishika nafasi ya Uimamu kwa takriban kipindi cha miaka kumi na moja.

Kwa mujibu wa maandiko na ripoti za kihistoria za pande zote mbili, Kishia na Kisunni, baada ya Imamu Hussein (a.s) kuzaliwa, Mtume Muhammad (s.a.w.w) alimpa mtoto huyo jina la "Hussein" na akatoa bishara ya kuuawa kwake kishahidi. Mtume wa Allah (s.a.w.w) aliwapenda sana wajukuu zake hawa wawili (Hassan na Hussein (a.s)), na akaamuru kila mtu awapende watoto wawili hao. Imamu Hussein (a.s) ni mmoja wa As-habu Al-Kisaa (Walioombewa dua ya kutoharishwa na Mtume (s.a.w.w)). Pia Imamu Hussein (a.s) ni mmoja wa walioshiriki tukio la Mubahalah ambaye ni miongoni mwa Ahlul-Bayt wa Mtume (s.a.w.w) ambao Aya ya utakaso iliteremshwa kuhusiana nao. Riwaya kadhaa za Mtume Muhammad (s.a.w.w) zimesimuliwa kuhusu fadhila za Imamu HusSein (a.s) Miongoni mwazo ni; "Hassan na Hussein ni mabwana wa vijana wa Peponi" na "Hussein ni mwanga wa mwongozo na jahazi ya wokovu."

Kuna riwaya chache tu zinazozungumzia maisha ya Imamu wa tatu wa Kishia, Ambaye ni Imamu Hussein (a.s). Imamu huyu aliishi katika miongo mitatu tofauti ya uongozi baada ya kifo cha Mtume (s.a.w.w). Miongo mitatu hiyo ni: zama za uongozi wa Imamu Ali (a.s), ambapo alisimama pega kwa bega na baba yake, pia alishiriki vita vilivyopiganwa ndani ya kipindi hicho. Aliishi ndani zama za uongozi wa kaka yake, yaani zama za Uimamu wa Imam Hassan (a.s), huku akaiwa ni mfuasi na msaidizi wake na aliwafikiana na kuadhinisha mkataba wa amani na Mu’awiah. Baada ya kifo cha kaka yake (Imamu Hassan) kishahidi, alibakia kuwa mwaminifu wa mapatano ya amani yaliyotiwa saini baina ya kaka yake na Mu’awiah. Alibaki na msimamo huo kwa muda wote wa uhai wa Mu’awiah. Aliwataka Mashia kuwa na subra pale alipoiwajibu barua zao za kumtaka yeye asimame nao katika kuuandama na kuupinga utawala wa Bani Umayya.

Kipindi cha Uimamu wa Hussein bin Ali (a.s) kiliambatana na utawala wa Mu’awiah bin Abi Sufiani. Ripoti za kihistoria zinanukuu kwa kusema; Imamu Hussein (a.s) amepinga vikali namna ya utendaji wa Mu'awiah katika baadhi ya matukio. Baada ya kuuwawa Hujru bin Adiyyu, alimwandikia barua ya kumkemea. Na katika suala la kumrithisha mwanawe (Yazid) cheo cha Ukhalifa, pia alikataa kukubali kula kiapo cha utiifu kwa Yazid. Akitoa hotuba mbele ya Mu’awiah na Waislamu wengine, alilaani vikali kitendo hicho, katika hotuba yake alimponda Mu'awiah pamoja na mwanawe, akisema kuwa Yazid ni mtu asiyefaa na wala hastakihi Ukahlifa. Akiendelea na hotuba yake alisema, haki ya Ukhalifa ni yake, na si haki ya Yazid. hotuba ya Imamu Hussein (a.s) katika mji wa Mina pia imezingatiwa kuwa ni msimamo wa kisiasa dhidi ya Bani Umayya. Hata hivyo, imeripotiwa kwamba; Mu'awiah kidhahiri, alikuwa akimwekea heshima Hussein bin Ali (a.s) kama vile alivyokuwa akiwaheshimu Makhalifa watatu (Abu Bakar, Omar na Othman).

Baada ya kifo cha Mu’awiah, Imam Hussein (a.s) hakuona kuwa ni halali kuapa kiapo cha utiifu kwa Yazid bin Mu’awiah. Hussein bin Ali (a.s) alitoka Madina kwenda Makka mwezi 28 Rajab mwaka 60 Hijiria kutokana na shinikizo la Yazid la kumlazimisha ampe kiapo cha utiifi kwa nguvu, huku akimtishia maisha yake endapo atakataa kumpa kiapo hicho. Katika muda wa miezi minne akiwa ndani ya mji wa Makka, alipokea barua nyingi kutoka kwa watu wa mji wa Kufa za kumkubali na kumtambua yeye kuwa ndiye kiongozi wao mstahiki. Baada ya kumtuma mjumbe wake (Muslim bin Aqiil) kwenda kuhakiki ukweli wa habari hizo, Muslim bin Aqeel alituma ujumbe wa kuthibitisha ukweli wa madai hayo. Imamu Hussein (a.s) kwa nia ya kuitikia wito wa watu wa Kufa, bila ya kuwa na habari za khiana za watu wa mji huo za kumgeukia mjumbe wake na kumuua, mnamo tarehe 8 Dhu al-Hijjah, aliamua kufunga safari kuelekea mji wa Kufa.

Liwali wa Kufa (Ibn Ziyad), alipopata habari kuhusu safari ya Hussein bin Ali (a.s) ya kuelekea mji wa Kufa, alituma jeshi lake kumfuata na kumzingia njiani. Baada ya askari waliongozwa na Hur bin Yazid kuziba njia yake, hakuwa na la kufanya ila ni kubadili njia na kuelekea Karbala. Siku ya Ashura, vita vilizuka kati ya Imamu Hussein na Masahaba zake na jeshi la Kufa, chini ya uongozi wa Omar bin Sa'ad. Vita hivyo vilipelekea kuuawa kishahidi Hussein bin Ali (a.s) (Imamu wa tatu wa Kishia) pamoja na Masahaba zake. Baada ya hapo, wanawake na watoto akiwemo Imamu Sajjad (a.s) ambaye alikuwa mgonjwa ndani ya siku hizo za vita, walitekwa na kupelekwa mji wa Kufa, kisha kufikishwa mji wa Sham (Syria). Mwili wa Imam Husein (a.s) pamoja na miili ya Masahaba zake, ilizikwa huko Karbala mnamo mwezi 11 au 13 ya mwezi wa Muharram. Mazishi hayo yalifanywa na baadhi ya watu kutoka kabila la Bani Asad.

Kuna mitazamo tofauti kuhusiana na safari ya Imamu Husein (a.s) ya kutoka Madina kwenda Karbala. Kundi moja linaamini kwamba; Imamu Hussein alisimama kwa ajili ya kuunda serikali, huku wengine wakiamini ya kwamba; hatua hiyo ilikuwa ni hatua ya kuokoa maisha yake tu, na si zaidi ya hilo. Kuuawa kishahidi kwa Husein bin Ali (a.s) kumekuwa na taathira kubwa kwa Waislamu na hasa Mashia katika kipindi chote cha historia. Mapambano ya Imamu Hussein (a.s) yalichochea mapambao mbali mbali yaliopata motisha wa kivita na ushujaa kutoka kwake. Mashia wakiiga kutoka kwa maimamu wao, hutilia maanani sana suala la kuadhimisha na kuomboleza siku za misiba ya Maimamu wao. Maombolezo hayo huonekana kukolea rangi zaidi katika mwezi wa Muharram na Safar. Miezi ambayo ndani yake mna siku maalumu za kuadhimisha na kuomboleza kifo cha Hussein bin Ali (a.s) pamoja na Masahaba zake. Moja kati ya amali muhimu zilizosisitizwa kwenye Hadith za Maimamu (a.s), ni kumzuru Imamu Hussein (a.s) katika miezi miwili hiyo ya Muharram na Safar. Kaburi au Raudha ya Imamu Hussein (a.s), ni moja kati ya sehemu nyeti sana zinazuriwa na wafuasi wa dhehebu la Shia.

Ukiachana na heshima ya Mashia kwa Hussein bin Ali (a.s) kama ni Imamu wa tatu miongoni mwa Maimamu wa Mashia, na sifa ya kuwa yeye ni bwana wa mashahidi, Masunni pia nao wanamheshimu sana Imamu Hussein (a.s). Heshima hizo zimejengeka kutokana na sifa njema alizomsifia Mtume (s.a.w.w), pia ni kwa sababu ya msimamo wake wa kidini na kisiasa dhidi ya Yazid.

Hazina ya urithi wa mafunzo ya Imamu Hussein (a.s) imerikodiwa kwa mfumo wa Hadithi, dua, nyaraka za barua, mashairi na hotuba mbali mbali. Yote hayo yamekusanywa katika kitabu kiitwacho; Musnad Al-Shahid. Nacho ni kitabu kilichokusanya seti nzima ya nyaraka zinazohusiana na maneno na mafunzo ya Imam Hussein (a.s). Ukiachana na kitabu hicho kilichokusanya mafunzo hayo, pia kuna urithi mwingi wa nyaraka, zinazozungumzia wasifu wake, mauaji ya Karbala na uchambuzi wa historia ya maisha yake.

Nafasi yake (a.s)

Hussein bin Ali (a.s) ni Imam wa tatu wa Mashia, mtoto wa Imamu wa kwanza wa Mashia na mjukuu wa Mtume wa Uislamu (s.a.w.w). [21] Kuna Riwaya nyingi kuhusu fadhila zake ndani ya hazina za vyanzo vya Kiislamu, na ana nafasi muhimu katika madhehebu ya Shia. Hussein bin Ali (a.s) pia anaheshimiwa sana na wafuasi wa madhehebu ya Sunni.

Hussein (a.s) katika hadithi na vyanzo vya kihistoria

Kwa mujibu wa Hadith za Shia na Sunni, Hussein bin Ali (a.s) ni mmoja ya waliokuwemo ndani ya Kisaa (ahlul-kisaa), [22] pia alikuwemo katika tukio la Mubaahalah. [23] Yeye pamoja na kaka yake, ndio maana ya tafsiri ya neno Wana wetu. katika Aya ya Mubahala. [24] Yeye pia ni miongoni mwa Ahlul-Bayt (a.s) ambao Aya ya utakaso iliteremshwa juu yao. [25]

Baada ya kifo cha kishahidi cha Imam Hassan (a.s), licha ya kuwepo watu wazima ambao ni wapevu zaidi kiumri kuliko Hussein (a.s), ila Imamu Hussein (a.s) alikuwa ndiye mtukufu zaidi miongoni mwa Bani Hashim. Kwa mujibu wa nukuu za Ya’aqubi, baada ya kifo cha kishahidi cha Hassan ibn Ali (a.s), Mu'awiah alimwambia Ibn Abbas: Kuanzia sasa wewe ndiye bwana wa watu wako. Ibn Abbas akajibu: “Katu sitaweza kufanya hivyo madhali Hussein yupo hai. [26] Pia kuna Riwaya zinazozungumzia baadhi ya mashauriano ya mambo mbali mbali ndani ya watu wa ukoo wa Bani Hashim, zinazoonesha kuheshimiwa zaidi maoni ya Hussein bin Ali kuliko ya wengine. Imepokewa kutoka kwa Amru bin Al-A'as ya kwamba; “Hussein bin Ali ndiye mpendwa zaidi miomngoni mwa wakazi wa ardhini mbele ya wakazi wa mbinguni”.

Kuuawa kishahidi kwa Hussein bin Ali(a.s)

Ujasiri wa Kutafuta uadilifu na usawa uliohitimishwa na tukio la Ashura mwaka 61 Hijiria, umemfanya Imamu Hussein (a.s) kuwa ni mashuhuri zaidi mbele ya Mashia na wasiokuwa Mashia. Hivyo basi Waislamu wote wanamtambua Hussein kupitia tukio hilo la Ashura (Karbala). Jambo ambalo pia lilipelekea kuzagaa kwa kiasi kikubwa sifa zake nyingine zilizotajwa katika vyanzo vya Hadithi mbali mbali. Na kama si tukio hilo, basi pengine yeye pia angeliwekwa gizani kama walivyowekwa Maimamu wengine (a.s). [29] Kutokana na tukio hili kuwa ndio la kwanza liliopindukia mipaka katika kuonesha dharau dhidi ya familia ya Mtume (s.a.w.w), na kausimamisha vita vya wazi dhidi yake, lilileta athari kubwa katika historia na utamaduni wa Shia. [30] Ujasiri wake ukawa ndiyo nembo ya kupinga dhuluma. Kule mapinduzi ya damu kushinda upanga, kuamrisha mema na kukataza maovu, kukawa ndio mfumo katika tamaduni za Kishia. [31]

Athari na matunda ya kifo cha kishahidi cha Imamu Hussein (a.s) yalikuwa ni makubwa mno. Kiasi kwamba baadhi ya watu walifikiri kwamba, madhehebu ya Shia yalianzishwa baada ya kifo chake cha kishahidi. [32] Katika historia yote ya Mashia, utakuta mapambano yote yaliopambanwa dhidi ya dhula, yalibuniwa kupitia wigo wa mapinduzi ya Imamu Hussein (a.s), huku kauli mbiu ya wapambanaji hao ikiwa ni kauli isemayo: Uko wapi ewe mlipiza kisasi cha mauwaji ya Hussein (یا لثارات الحسین). [33]

Miezi miwili ya Muharram na Safar ina nafasi maalum katika utamaduni wa Shia, na hasa katika siku za Tasua, Ashura, pamoja na Arubaini ya Hussein (a.s). Ibada mbalimbali hufanyika kwa ajili ya kuadhimisha tukio hili. Mashia wakifuata na kuiga nyenendo za viongozi wao, humkumbuka Hussein kila wanywapo maji, na humsalimia wakinyanyua kauli isemayo Assalamu alaika ya Hussein. [35]

Nadharia ya sunni juu ya Imamu Hussein (a.s)

Vyanzo vya kuaminika vya Kisunni vimesimulia Hadithi nyingi kuhusu hadhi na fadhila za Hussein bin Ali (a.s). [36] Ukiachana na fadhila na nafasi zake (a.s), Imamu Hussein (a.s) ameheshimiwa zaidi kutokana na msimamo wake wa kujitolea yeye na familia yaka dhidi ya dhulma. [37]

Miongoni mwa Masunni, kuna mitazamo miwili tofauti kuhusu mapinduzi ya Imamu Hussein (a.s): Wapo walioshutumu na wapo waliosifu. Miongoni mwa walioshutumu, ni Abu Bakr bin ‘Arabi, mwanachuoni wa Kisunni wa karne ya 6 wa mji wa Andalusia, ambaye alijaribu kulaani kitendo cha Hussein (a.s) na akasema kwamba; Watu walipigana na Hussein bin Ali kwa sababu ya kusikia Hadithi kutoka kwa Mtume (s.a.w.w) (kuhusu wajibu wa kupigana vita na wale wanaotaka kuleta mgawanyiko). Walipigana na Husein, kwa kuchukua hadhari ili wasije tumbukia katika fitna. [38] Ibn Taimiyyah pia anaamini kwamba; Kitendo cha Husein bin Ali (a.s) sio tu kwamba hakikuboresha hali ya kisiasa na kijamii, bali pia kilisababisha shari na fitna. [39]

Kwa upande mwingine, Ibn Khaldun, mwanahistoria wa Kisunni wa karne ya 9 kutoka mji Andalusia, alijibu mashambulizi ya maneno ya Ibn Arabi kwa kusema kuwa; Ulazima wa kuwepo Imamu mwadilifu ni moja ya sharti za vita dhidi ya kiongozi dhalimu, akithibitisha hilo, alimkiri Imamu Hussein (a.s) kuwa ndiye mwadilifu zaidi katika mapinduzi hayo. [41] Aliendelea kusema; Wakati uovo na ufasiki wa Yazid ulipo kithiri na kuwa wazi na bayana kwa kila mtu, Hussein aliona ni wajibu wake kuinuka dhidi yake, kwa sababu alijiona kuwa yeye ndiye mtu pekee mwenye sifa na uwezo wa kutekeleza kazi hiyo. Pia, mwanazuoni marufu wa Kisunni wa karne ya 13 ajulikanaye kwa jina la Shihabu Al-Diin Aalusi katika kitabu Roohu Al-Ma'ani, alitumia lugha ya wazi kumlani Ibn ‘Arabi, huku akisema kuwa kauli ya Ibu Arabi ni uwongo na tuhuma kubwa dhidi ya Hussein (a.s). [43]

Abbas Mahmoud Akkad, mwandishi na malenga wa Misri katika wa karne ya 14 Hijiria, aliye andika kitabu "Abu Al-Shohadaa Al-Hussein Ibn Ali" ameandika kwamba; wakati wa Yazid, hali ilikuwa ni mbaya mno, kiasi ya kwamba hakukuwa na njia mbadala ya kutatua hali mbaya iliopo zaidi ya kufa kishahidi tu. [44] Yeye anaamini kwamba; Harakati kama hizo za kimapinduzi ni adimu, na ni wachache ambao wameundwa na kuzaliwa kwa ajili ya kazi kama hizo. Harakati zao haziwezi kulinganishwa na wengine, kwani welewa wao katika kuyafahamu mambo, ni tofauti na wengine, pia mfumo wao wa kudai haki haulingani na wengine. [45] Taha Hussein, mwandishi wa Kisunni, anaamini kwamba; kukataa kwa Hussein kutoa kiapo cha utiifu hakukutokana na ukaidi; Kwa sababu alijua kwamba kama angekula kiapo cha utiifu kwa Yazid, angesaliti dhamiri yake na kuipinga dini yake, kwa sababu kwa maoni ya Imamu Hussein (a.s), kuweka kiapo cha utiifu kwa Yazid ilikuwa ni dhambi isiyokubalika. [46]

Umar Farroukh, akisisitiza kwamba; Ukimya mbele ya ukandamizaji hauruhusiwi kwa namna yoyote ile, yeye anaamini kwamba, sisi Waislamu leo tunamhitaji “Husseini” ainuke miongoni mwetu na atuongoze kwenye njia iliyonyooka katika kutetea ukweli na kutafuta uadilifu. [47]

Jina, ukoo, kunia na lakabu zake (a.s)

Kwa mujibu wa vyanzo vya Shia na Sunni, Mtume (s.a.w.w) ndiye aliyempa jina "Hussein". [48] Kwa ishara na dalili za Hadithi, alipewa jina hilo kwa amri ya Mungu mwenyewe. Waarabu hawakuwa na historia ya majina ya Hassan na Hussein kabla ya Uislamu, [50] ambayo ni majina mbadala ya wana wa Nabii Haruni, ambao ni Shubbar na Shabir (au Shabbir). [51]

Pia kuna Riwaya nyingine zilizotajwa kuhusiana na Imam Hussein (a.s) kupewa jina hilo. Kwa mfano kuna Riwaya isemayo; kwanza Imam Ali (a.s) alimpa mwanawe jina la “Harb” au “Ja’afar”, lakini Mtume (s.a.w.w) akamchagulia jina la Hussein. [53] Baadhi wamekanusa taarifa hizo, wakisema kuwa taarifa hizo ni uwongo. Ila hawakuorodhesha sababu wala dalili zozote zile za kuzikataa habari na taarifa hizo. [54]

Imamu Hussein (a.s) ni mtoto wa Imam Ali (a.s) na bibi Fatima (a.s) na ni mjukuu wa bwana Muhammad (s.a.w.w). Ametoka katika ukoo wa Bani Hashim na kabila la Quraish. Miongoni mwa kaka zake ni; Imamu Hassan Mujtaba (a.s), bwana Abbas (a.s) na Muhammad bin Hanafiyyah. Bibi Zainab na Umm Kulthum (a.s) ni miongoni mwa dada zake. [55]

Kunia za Hossein bin Ali ni "Abu Abdullah". [56] Abu Ali, Abu Al-Shohda (baba wa mashahidi), Abu Al-Ahrar (baba wa walio huru). Miongoni mwa kunia zake nyengine ni Abu Al-Mujahidin (baba wa wanajihadi). [57]

Hussein bin Ali (a.s) ana lakabu nyingi, baadhi yake zinaendana sawa na lakabu za kaka yake (Imam Hassan (a.s)). Lakabu maarufu kwake ni; Sayyidu Shababi Ahli Al-Junnati (Bwana wa Vijana wa Peponi). Nyengine miongoni mwazo ni: Zakiyyun, Tayyibun, Wafiyyun, Sayyidun, Mubaarakun, Naafi'un, Al-Daliilun 'Alaa Dhatillahi, Raashidun, na Taabi'un Limar-dhaatillahi. [58] Ibn Talha Al-Shafi'i, ametaja jina "Zakiyyun" na "Sayyidu Shabaabi Ahli Al-Jannati" kuwa ndio majina maarufu zaidi kuliko mengine. [59]

Katika baadhi ya Hadithi, Hussein (a.s) ametambuliwa kwa lakabu ya Shahiidun au Sayyidu Al-Shuhadaa. [60] Katika baadhi ya kumbukumbu za Riwaya, Imam Hussein ametambuliwa kwa lakabu za Tharullahi na Qatiilu Al-Abaraati. [61]

Kuna Riwaya iliyonukuliwa kutoka vyanzo vingi vya Shia na Sunni ya kwamba; Mtume (s.a.w.w) alimsifu kwa kusema: «حسین سِبطٌ مِن الاَسباط» Yaani; Hussein ni kiongozi miongozi mwa viongozi. [62] Maana ya neno سِبطٌ katika Riwaya hii, na vilevile katika baadhi ya Aya za Qur'ani, lina maana ya imamu na kiongozi mteule aliyechaguliwa na Mungu, na atokaye katika dhuria ya manabii. [63]

Wasifu na maisha yake (a.s)

Hussein bin Ali (a.s) alizaliwa Madina, na kwa mujibu wa imani ya wengi, kuzaliwa kwake kulikuwa ni katika mwaka wa nne Hijiria. [64] Hata hivyo, kuna baadhi waliosema kuwa azaliwa mwaka wa tatu Hijiria (mwandamo).

Kwa mujibu wa maoni ya wengi ni kuwa; Hussein bin Ali alizaliwa mwezi 3 Shaabani. [66] Lakini Sheikh Mufid katika kitabu cha Al- Irshaadi, alizingatia tukio la kuzaliwa kwa Imamu huyu wa tatu wa Mashia kuwa ni mwezi 5 Shaabani. [67]

Katika riwaya za kihistoria za Shia na Sunni, imeelezwa kwamba; Mtume (s.a.w.w) alilia wakati alipozaliwa Hussein (a.s) kisha akaelezea khabari ya kuuawa kwake kishahidi. [68] Kwa kuzingatia namna ya Riwaya katika Kitabu cha Kafi ilivyoelezea, Imamu Hussein (a.s) hakunyona kutoka katika kifua cha mama yake wala kutoka kwa mwanamke mwingine yeyote yule. [69]

Imepokewa kutoka kwa Umm Al-Fadhli, mke wa Abbas bin Abdi Al-Muttalib kuwa; Aliota usingizini mwake kuwa; Kipande cha mwili wa Mtume kimewekwa kwenye mapaja yake (Ummu Fazl), Mtume (s.a.w.w) akasema katika tafsiri ya ndoto yake kwamba, “Fatima atajifungua mtoto wa kiume, nawe utakuwa yaya wake”. Alipozaliwa Husein (a.s) akachukuliwa na Ummu Al-Fadhli na akawa ndiye yaya wake. [70] Baadhi ya vyanzo vimenukuuu kahabari zisemazo; Yaya wa Imamu Hussein ni mama wa Abdullahi bin Yaqtar. Lakini maandiko yanasema kwamba, Hussein (a.s) hakunyonyeshwa na hata mmoja miongoni mwao.[71]

Imeelezwa katika vyanzo vya Sunni kwamba; Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.w) aliwapenda zaidi Hassan na Hussein (a.s) kuliko wengine miongoni mwa watu wa familia yake. [72] Kiasi ya kwamba pale Hassan na Hussein walipokuwa wakienda msikitini, Mtume (s.a.w.w) alikuwa akisitisha hotuba yake, na kushuka katika mimbari yake na kuwakumbatia. [73] Imesimuliwa kutoka kwa Mtume (s.a.w.w) akisema; mapenzi yangu kwa wawili hawa yananizuia kumpenda mtu mwingine yeyote. [74]

Hussein (a.s) alikuwa ni miongoni mwa watu wa Kisaa walioshiriki katika tukio la Mubaahalah. [75] Wakati wa tukio la Mtume (s.a.w.w) kufariki, yeye alikuwa na umri wa miaka saba. Kwa hiyo, alihesabiwa ni miongoni mwa tabaka la mwisho la Masahaba wa Mtume (s.a.w.w). [76]

Hussein (a.s) katika zama za makhalifa watatu

Miaka 25 ya maisha ya Imam Husein (a.s) ilimpita wakati wa Makhalifa watatu, lakini kuna habari chache tu kuhusu maisha ya Imamu huyu wa tatu wa Mashia kuhusiana na maisha yake ya kipindi hicho. Yawezekana sabau hasa ya jambo hili ni kutokana na Ali bin Abi Talib (a.s) kujitenga na maisha ya kisiasa yeye pamoja na watoto wake katika wakati huo. [77]

Maandiko yameeleza kwamba; Mwanzoni mwa Ukhalifa wa Omar, siku moja Hussein (a.s) ambaye alikuwa na umri wa takriban miaka tisa, aliingia msikitini na alipomwona Omar akitoa hotuba kwenye mimbari ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w), alipanda juu ya mimbari na kumwambia: “Shuka kutoka kwenye mimbari ya baba yangu na ukae juu ya mimbari ya baba yako”! Omar akasema: “Baba yangu hakuwa na mimbari”. [78] Ripoti kutoka katika nyaraka za kihistoria zimeeleza kuwa, Khalifa wa pili (Omar) alikuwa akimheshimu sana Sayydna Hussein (a.s). [79]

Wakati wa zama za Ukhalifa wa Othman alipomhamisha Abu Dharr na kutokomeza kwenye ardhi ya Rabadhah, na kuwakataza watu kumuaga ua kufuatana naye. Imam Hussein (a.s), Imam Hassan (a.s) na wengine kadhaa, akiwemo baba yake, kamwe hawakuitii amri ya Khalifa. Wote kwa pamoja walikwenda kumluaga Abu. Dharr. [80]

Baadhi ya vyanzo vya Kisunni vimenukuu habari ya kuwepo kwa Hassanaini (Hassan na Hussein) katika vita vya Afriiqiyyah katika mwaka wa 26 Hijiria, [81] na vita vya Tabaristan mwaka wa 29 au 30 Hijiria. [82] Lakini ripoti kama hiyo haipatikini katika chanzo chochote kile cha Shia. Vyanzo vingi vya kihistoria vimesema kwamba; Vita vilivyotajwa hapo juu viliisha kwa upatanisho bila migogoro. [83] Ripoti ya kuwepo kwa Hassanaini katika vita hivi, ina wafuasi wake na wapinzani wake; Baadhi ya wanazuoni, kama vile Ja’afar Murtadha 'Aamiliy, wakizingatia utata wa maandishi ya Riwaya hizi, walizihesabu kuwa ni za uongo. Waliopingana na habari hizo pia wamezingatia upinzani wa Maimamu juu ya njia na mfumo uliotumiwa na Makhalifa katika vita vya kufungua miji mbali mbali. Linalounga mkono zaidi nadharia hii, ni kule Imam Ali (a.s) kutowaruhusu Hassana na Hessein kushiriki katika vita vya Siffiin. [84]

Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti za kihistoria, mwishoni mwa utawala wa Othman, wakati ambapo kulitokea kundi lililofanya ghasia na kushambulia nyumba ya Othman kwa nia ya kumuua, Imamu Hassan Mujtaba (a.s) na Imamu Hussein (a.s), licha ya kuchukizwa kwao na utendaji wa Khalifa huyu. Kupitia amri ya Imam Ali (a.s) walikwenda kuilinda nyumba ya yake. [85] Riwaya hii ina wafuasi waiungayo mkono, na pia kuna waopingana nayo. [86] Sayyid Ja'afar Murtadha, akizingatia ushahidi wa kihistoria kama vile upinzani mkali wa Imamu Ali (a.s) dhidi ya matendo ya Othman, na kuwepo kwa Riwaya zinazokinzana na Hadith hii, Kama vile Riwaya ya Othman kuukataa msaada wa Imam Hassan (a.s). Mhakiki huyu amelihesabu jambo hilo kuwa ni jambo lisiloyumkinika. Pia kwa mujibu nyenendo za Imam Ali (a.s) katika kukabiliana na viongozi waovu, kunakopelekea yeye kutokuwa na shauku ya kumtetea Othman, na wasifu wa Ali bin Abi Talib katika kuwasaidia wanyonge dhidi ya madhalimu, ni miongoni mwa dalili zilizotegemewa katika kupinga nadharia hiyo. Mhakiki huyu amemnukuu Baaqir Sharif Qurashiy katika kitabu Hayat Al- Imaam al-Hasan (a.s) akisema: “Iwapo itathibiti tukio hili kutokea, basi ni kwa sababu Imamu Ali (a.s), alitaka kuwaepusha Hasnain (a.s) na dhana ambayo ingeliweza kudhaniwa dhidi yao. Dhana ambayo ingelijenga tuhuma ya kushiriki kwao katika umwagaji damu ya Othman.” [88] Baada ya Sayyid Ja'afar Murtadha kutoridhika na Riwaya hiyo, amesema kwamba; Kule Imamu Ali (a.s) kumtuma Hassan na Hussein (a.s) kwenda kwa Othman, kulikuwa na nia ya kuwaepusha wanawe na fitna. Kwa hiyo kama Hassan na Hussein walikwenda kwa Othaman, itakuwa walikwenda kwa nia ya kuipelekea chakula na maji familia ya Othman. Akizingatia kwamba, Othman hakuwa na thamani ya kutetewa, kwa sababu hakuwa ni Khalifa muadilifu anayestahiki kubaki madarakani. [88]

Utawala wa Imamu Ali (a.s)

Hadith za Mtume zilizoandikwa kwenye kaburi la Imamu Hussein (a.s)

Kwa mujibu wa Riwaya chache zinazohusiana na utawala wa Imam Ali (a.s), baada ya watu kutoa kiapo cha utiifu kwa Amiru Al-Muuminina (a.s), Hussein (a.s) alitoa khutba. [89] Na katika vita vya Jamal, alikuwa ni kamanda aliyeongoza jeshi la kushotoni mwa vita hivyo. [90] Katika vita vya Siffiin alionekana kutoa hotuba ya kuhamasisha Jihad. [91] Na kwa mujibu wa baadhi ya vyanzo, alikuwa ni mmoja wa makamanda wa mrengo wa kulia ndani ya vita hivyo. [92] Inasemekana kwamba; Imamu Hussein alishiriki katika tukio la vita vya Siffiin la ugomvi wa maji baina ya upande wa Imamu Ali (a.s) na jeshi la watu wa Sham (Wafuasi wa Mu’awiah), na baada ya hapo Amiru Al-Mominiina Ali (a.s) akasema: "Huu ulikuwa ni ushindi wa kwanza iliofikiwa kwa baraka za Hussein". [93] Baadhi ya nukuu kuhusiana na vita vya Siffiin ni kwamba; Imamu ALi (a.s) aliwazuia Hassan na Hessein kupigana vita, na sababu hasa ilikuwa ni kukihifadhi kizazi cha Mtume (s.a.w.w). [94] Kwa mujibu wa baadhi ya vyanzo, yeye (Imamu Hussein) pia alikuwepo katika vita vya Nahrawaan. [95]

Vyanzo vingi vimesema kwamba Imamu Hussein (a.s) alikuwa pamoja na Imam Ali (a.s) [96] wakati wa kifo chake cha kishahidi, baada ya Imamu Ali kupigwa panga akiwa yupo katika sijda alipokuwa akisalisha sala ya Al-Fajihiri. Pia alishiriki kwenye hafla ya mazishi ya baba yake. [97] Ila kuna baadhi habari kutoka kitabu kiitwacho Al-Kafi na Ansaabu Al-Ashraafu zisemazo kuwa; Pale baba yake alipopigwa upanga na kujeruhiwa vibaya, Imamu Hussein (a.s) alikuwa katika mji wa Madaain akitekeleza majukumu aliyopewa na baba yake. Na habari za kujeruhiwa kwa baba yake alizipata kupitia barua ya kaka yake (Hassan) (a.s). [98]

Hussein katika zama za Imamu Hasan (a.s)

Ripoti za kihistoria zinaeleza uungwana na heshima kubwa ya Hussein bin Ali (a.s) kwa kaka yake (Imam Hassan) (a.s); Imepokewa kwamba kama Imamu Hassan (a.s) atakuwepo kwenye mkusanyiko, basi Imamu Hussein (a.s) ataonekana kukaa bila yaku kuzungumza kitu, akichunga heshima ya kaka yake. [99] Baada ya kifo cha kishahidi cha Imam Ali (a.s), kundi la Khawarij ambao walikula kiapo cha utiifu kwa Imamu Hassan (a.s), walisisitiza kupigana na watu wa Sham (wafuasi wa Mu’awiah). Na wakaenda kwa Imamu Hussein (a.s) kuapa kiapo cha utiifu kwake, akawajibu akisema: "Najikinga kwa Mwenyezi Mungu na kiapo chenu cha utiifu madhali bado Hassan yuhai". 100]

Katika suala la mkataba wa amani na Mu'awiah, Imamu Hussein (a.s) aliridhia kitendo cha kaka yake cha kutiliana saini na Mu’awiah juu ya mkataba wa amani ya mpito. Naye akawa ni msaidizi wa ndugu yake akipingana na Mashia waliokuwa wakiandamana na dhidi ya mkataba hou. [101] Imepokewa kwamba alisema: "Yeye (Imam Hassan) (a.s) ni Imamu wangu". [102] Kwa kuzingatia baadhi ya ripoti, baada ya saini ya mkataba wa amani kutimia, Imamu Hussein (a.s) alitoa kiapo cha utiifu kwa Mu'awiah, kama alivyofanya Imam Hassan (a.s) [103] na hata baada ya kifo cha kishahidi cha Imam Hassan (a.s) bado aliendelea kutimiza ahadi ya kiapo chake. [104] Kwa upande mwingine, kuna ripoti zinazoonesha kwamba; Imamu Hussein (a.s) kutokula kiapo cha utiifu kwa Mu’awiah. [105] Kwa mujibu wa baadhi ya vyanzo, yeye hakukubaliana na wazo la mkataba wa amani, na alimtahadharisha kaka yake (Imam Hassan) (a.s) juu ya ujanja na uwongo wa Mu’awiah. [106] Baadhi ya watafiti wakilinganisha ripoti hizi na orodha ya vielelezo vyengine vya dalili za kihistoria, wamegundua kuwa kuna mkinzano baina yake. [107] Kwa mfano, pale kundi la waandamanaji dhidi ya mkataba wa amani waliomtaka Hussein (a.s), aungane nao kumshambulia Mu’awiah, aliwajibu kwa kusema: “Sisi tumetia saini ya mkataba wa amani, na kamwe hatutavunja kiapo cha mkataba wetu.” [108] Ripoti nyengine inasema kwamba aliwajibu kwa kuwaambia: “Subirini maadamu Mu’awiah yuhai, ila akifa tutafanya uamuzi." [109] Hata pale Mashia walipompa mnada wa kusimama baada ya kifo cha kishahidi cha Imam Hassan (a.s), aliwajibu kwa lugha ya kutetea tendo la Imamu Mojtabi (a.s) la mkataba wa amani na Mu'awiah. Alifanya hivyo kipindi chote cha uhai wa Mu’awiah. [110] Katika mwaka wa 41 Hijiria (baada ya kufanya suluhu na Mu’awiah), Imamu Husein (a.s) alirejea kutoka Kufa kwenda Madina pamoja na kaka yake. [111]

Wake na watoto wa Imamu Hussein (a.s)

Kuna maoni tofauti kuhusu idadi ya watoto wa Imamu Husein (a.s); Vyanzo vingine vimenukuu vikisema; Yeye (a.s), alikuwa na watoto 4 wa kiume na 2 wa kike. [112] Wengine wamenukuu kuwa; Alikuwa na watoto sita wa kiume na watatu wa kike. [113]

Ikinukuliwa kutoka katika vyanzo vya karne ya sita katika kitabu Lubaabu Al-Ansaabu [126] , imenukuliwa ndani yake jina msichana aitwaye Ruqayyatun. Na kutoka katika vyanzo vya karne ya saba, kitabu Kamil Bahaai, kimetaja uwepo wa binti wa miaka minane aliyenasibishwa na Imamu Hussein (a.s), msichana ambaye alifariki huko Syria. [127] Jina la Ruqiyyatun limeakisiwa sana katika vyanzo vilivyukuja baadaye (vya miaka ya karibu). Pia kuna majina kadhaa kwenye baadhi ya vitabu vyenginine, likiwemo: Ali Asghar aliyemzaa kupitia mkewe aitwaye Shahre Baanuu, Muhammad aliyemzaa kupitia Rabaab, pamoja na Zainab. Hawa ndio waliotajwa kuwa ni watoto wa Imamu Hussein. [128] Ibn Talha Shafi'i katika kitabu maarufu; Matalib Al-Sa-uul fii Manaqibi Aali Al-Rasuuli, ametaja idadi ya watoto kumi kuwa ndio watoto wa Imam Hussein. [129]

Zama na muhula wa uimamu wake (a.s)

Kipindi cha mwanzo cha Uimamu wa Husein bin Ali (a.s) kilisadifiana na mwaka wa 10 wa utawala wa Mu’awiah. Mu’awiah alichukua madaraka ya serikali mwaka wa 41 Hijiria [130] baada ya kufanya suluhu na Imam Hassan (a.s) na kuanzisha Ukhalifa wa Bani Umayyah. Vyanzo vya Kisunni vimemtabua Mu’awiah kuwa ni mtu mjanja na mwenye miamala ya kiuvumilivu -yenye siri za chini kwa chini- na malengo ya muda mrefu. [131] Alishikamana sana na tabia dhahiri za kidini. Mara kwa mara alionekana kutumia baadhi ya misingi ya kanuni za kidini kutetea na kusimamisha Ukhalifa wake. Licha ya ukweli kwamba aliingia madarakani kwa kutumia nguvu na hila za kisiasa, ila hakuacha kutumia misingi ya dini kutetea Ukhalifa wake. [132] Mu’awiah Aliichukulia serikali yake kuwa imetokana na matakwa ya Mwenyezi Mungu na hukumu yake. [133] Pia Mu'awiah alijitambulisha kwa watu wa Sham (Syria) kuwa ni mfuasi wa Mitume aendaye sambamba naye katika nyenendo mbali mbali. Hakusita kujiita ni mja mwema wa Mwenyezi Mungu, na ni mmoja wa watetezi wa dini yake. [134] Katika vyanzo tofauti, kuna historia isemayo kwamba; Mu'awiah aliugeuza Ukhalifa kuwa ni ufalme. [135] Alionekana akisema waziwazi kwamba, uchamungu watu katika jamii haumhusu na hatilii maanani kkabisa suala la uchamungu wao. [136]

Moja ya matukio muhimu ya wakati wa utawala wa Mu'awiah, ni kuwepo kwa harakati za mrengo wa Kishia ndani ya jamii, harakati ambazo zlikuwa ndio harakati hatari zaidi dhidi ya utawala wa Mu’awiah hasa katika nchi ya Iraq. Mashia walitambulikana kwa msimamo wao maarufu dhidi ya Mu’awiah, ambapo Makhawariji pia walikuwa adui wa Mu’awiah. Mashia tofauti na Makhawarij, wao walikuwa na nguvu zaidi kinadharia na kielimu kutokana kuegemea kwao kwa Imam Ali na Ahlul-Bayt (a.s) Kwa hiyo, Mu'awiah na watendaji (maajenti) wake walishughulikia zaidi harakati za Shia ima kwa njia ya maelewano au kwa mashinikizo ya nguvu. Mojawapo ya mbinu muhimu za Mu'awiah za kukabiliana mrengo wa Kishia, ni kujenga chuki dhidi Imam Ali (a.s) miongoni mwa watu, kiasi ya kwamba suala la kumlaani na kumtukana Ali (a.s), likaendelea kuwa ni jadi tokea kipindi cha Mu'awiah hadi kipindi cha Bani Umayya. [137]

Baada ya kuimarisha misingi ya madaraka yake, Mu'awiyah alianzisha sera ya ukandamizaji na shinikizo zaid dhidi ya Mashia. Aliwaandikia mawakala wake barua ya kuwataka waondoe majina ya wapenzi wa Ali (a.s) kwenye Diwan (Idara ya Usajili wa Huduma za Jamii) na kukata posho lao kutoka Bait Al-Mal. Pia aliamuru kupuza na kuto kubali kiapo na ushahidi kutoka kutoka kwa Mashia. [138] Mu’awiah hakuacha kuwatishishia wenye kunukuu na kusambaza fadhila za Imam Ali (a.s). Hali ilikuwa ni mbaya mno, kiasi ya kwamba wapokezi na waandishi wa Riwaya wakawa wanakhofia kutaja jina Ali (a.s), na badala yake wakawa wanatumia ibara za kiistiara kama vile; “Mmoja wa Makureshi” na “mmoja wa Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu” au “Abu Zainab”, wakimaanisha Ali (a.s). [139]

Dalili na ithibati za uimamu wa maimamu (a.s)

Baada ya Imamu Hussan kuuawa shahidi mwaka wa 50 Hijiria, Imamu Hussein (a.s) alichukua nafasi ya Uimamu na kuwaongoza Mashia mwanzoni wa mwaka wa 61 Hijiria. [141] Ukiachilia mbali dalili bayana za misingi ya uongozi inayokubalika kijamii, Wanazuoni wa Kishia wamesimamisha dalili maalum za kuthibitisha Uimamu wa kila mmoja miongoni mwa Maimamu wao (a.s). Katika kuthibitisha Uimamu wa Imamu Hussein (a.s), Sheikh Mufid ametaja baadhi ya Hadithi katika kitabu Al-Irshaad, akinukuu kwa kusema; Mtume (s.a.w.w) amesema: ((ابنايَ هذانِ إمامانِ قاما أو قعدا) Maana yake; “Hawa wanangu wawili (Hassan na Hussein) ni Maimamu wawili, wakikaa au wakisimaa”. [142] Pia, Imam Ali (a.s) wakati wa kifo chake cha kishahidi alisisitiza Uimamu wa Hussein (a.s) baada ya Imam Hassan (a.s). [143] na Imamu Hassan (a.s) pia wakati wa kifo chake cha kishahidi, katika wasia wake kwa Muhammad bin Hanafiyyah, alimtambulisha Husein bin Ali (a.s) kama ni Imamu baada yake. [144] Sheikh Mufiid ameuchukulia Uimamu wa Imamu Hussein (a.s) kuwa ni Uimamu thabiti kupitia hoja na dalili za Hadith hizo ambazo pia yeye amezinukuu kitabuni mwake. Kwa maoni yake, suala la Imamu Hussein (a.s) kutotaka wafuasi wake kumuunga mkono hadi alipofariki Mu’awiah, ni kutokana na kufuata taqiyyah na kuto vunja ahadi ya mkataba wa amani baina ya Imamu Hassan na Mu’awiah. Lakini baada ya kifo cha Mu’awiah alidhihirisha na kubainisha msimamo wake kwa wale wasiokuwa na habari nao. [145]

Maandiko mbali mbali yameeleza kwamba; Kabla ya Imamu Hussein (a.s) kuondoka Madina mwaka wa 60 Hijiria, aliacha sehemu ya wasia wake kuhusiana na suala la Uimamu kwa Ummu Salama (mke wa Mtume (s.a.w.w), kama ni amana kwake. [146] Pia kabla ya kifo chake kishahid kilichotokea mwezi wa Muharram mwaka wa 61 Hijiria, aliacha wasia mwengine kwa binti yake mkubwa Fatimah, [147] ili amkabidhi Imam Sajjad (a.s).

Kuendelea na mkataba wa amani

Wakati wa utawala wa Mu’awiah, Imamu Hussein (a.s) aliendelea kudumisha mapatano ya amani yaliotiwa saini baiana ya Imam Hassan na Mu’awiah. [148] Akijibu barua ya kupinga maoni ya Mashia waliomtaka asimame nao kama ni kiongozi wao katika kupambana na uongozi wa Bani Umayyah, aliandika kwa kusema: "Kwa hivi sasa maoni yangu yako kinyume na maoni yenu, madhali Mu’awiah yuhai basi msifanye harakati zozote zitakazopelekea kutuhumiwa, na badala yake, bakieni mkiwa watulivu majumbali mwenu. Lakini iwapo Mu’awiah atafariki huku mimi nikiwa bado nihai, hapo basi nitakujulishe mtazamo wangu na nini mtatakiwa kufanya". [149]

Msimamo dhidi ya vitendo vya Mu'awiyah

Ingawa Imamu Hussein (a.s) hakufanya lolote dhidi ya utawala wa Mu'awiah katika kipindi chote cha uonngozi wa Mu'awiah, ila kwa mujibu wa maandiko ya mwandishi wa historia wa hivi sasa Rasul Jafarian, ni kwamba; Mahusiano kati ya Imamu Hussein (a.s) na Mu'awiah, na mazungumzo yaliyopita baina yao yanaonyesha kwamba, Imamu Hussein (a.s) hakuridhika kabisa na masharti ya Mu’awiah. [150] Barua nyingi walizoandikiana kati ya Hussein bin Ali (a.s) na Mu'awiah ni moja wapo wa ushuhuda wa hayo. Matendno ya Mu’awiah hayakuachana mbali na matendo ya Makhalifa watatu, ambao kidhahiri walikuwa wakimheshimu Hussein bin Ali (a.s) na kumtukuza, [151] pia waliwaamuru maajenti wao wasimvunjie heshima mtoto wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) na wasijaribu kumdharau. [152] Mu'awiah naye pia alisisitiza msimamo huo wakati wa wasia wake kwa mwanawe (Yazid), akimtaka amheshimu Hussein (a.s), huku akimsisitiza mwanawe kuhusu nafasi na thamani ya Hussein (a.s) ndani ya jamii. [153] Alimsisitiza mwanawe na kumsihi, iwapo atamshinda Hussein (a.s) katika kushika madaraka, basi amwache huru, kwani Hussein (a.s) ana haki kubwa kwenye jamii. [154]

Msimamo dhidi ya mauaji ya masahaba wa Imamu Ali (a.s)

Kitendo cha Mu'awiah kuwaua baadhi ya Masahaba kama vile; Hujru bin 'Adiyyu, 'Amru bin Hamaq Khuza'i na Abdullahi bin Yahya Al-Hadhrami, ni miongoni mwa mwa kesi zilizochochea ghadhabu na misimamo mikali ya Imamu Husein (a.s) dhidi ya Mu’awiah. Kuna maandiko ya kihistoria yasemaso; Imamau Hussein (a.s) alimwandikia Mu’awiah barua ya makemeo, akikosoa matendo hayo yasiyofaa, alimtahadharisha kwa kusema: "Mimi sitambui tendo bora zaidi katika amali zangu kuliko kupigana nawe jihadi." Katika mwendelezo wa barua hii, kuna ibara iliyosema: "Mimi sijaona fitma kubwa zaidi katika uma huu kuliko fitna ya uongozi wako". [156]

Pia imepokewa ya kwamba; Wakati Mu'awiah alipokutana na Imamu Hussein (a.s) katika safari ya Hija [157], alimwambia: “Je, umesikia tuliyomfanyia Hujru na wenzake zake ambao ni wafuasi wa baba yako?”. Imam akasema: "Uliwafanya nini?" Mu'awiah akajibu: "Tuliwaua, tukawafunika sanda, tukawasalia na kuwazika." Hussein bin Ali (a.s) akawajibu kwa kusema: “Ila sisi tukiwauwa wafuasi wako, basi hatutawafunika sanda, hatutawasalia na wala hatutawazika.” [158]

Kupinga utawala wa Yazid

Mnamo mwaka wa 56 Hijiria, dhidi ya masharti ya makubaliano ya amani Mu’awiah alikwenda kinyuma na mswaada wa makubaliano ya amani (kuhusu kutomteua mtu yeyote kama ni mrithi wake). Badala yake, aliwataka watu wale kiapo cha utiifu kwa mwanawe (Yazid), na wamtambue kuwa ndiye mrithi wake anayestahiki kushika nafasi ya Ukhalifa. [159] Baadhi ya watu akiwemo Imam Hussein bin Ali (a.s), walikataa kumuunga mkono Yazid. [160] Mu’awiah alikwenda Madina ili aungwe mkono na wakuu wa mji katika suala hilo, ikiwa ni miongoni mwa jitihada zake za kukamilisha malengo yake. [161] Imamu Hussein (a.s), akiwa katika mkutano uliowajumuisha Mu’awiah, Ibn Abbas na baadhi ya watumishi na wakuu wa familia ya Bani Umayyah, alilani matendo ya Mu’awiah huku akaashiria matendo maovu ya Yazid. Alijitahidi kutoa hoja na kuthibitisha nafasi yake katika suala la kushika Ukhalifa, huku akimtahadharisha Mu’awiah juu ya kumteua mwanawe (Yazid) kushika nafasi ya Ukhalifa ambayo ni haki ya Imamu Hussein (a.s) na si haki ya Yazid. [162]

Katika mkutano mwingine uliohudhuriwa na watu tofauti wakiwemo wananchi wa kawaida, Imamu Hossein (a.s) alionekana kumjibu Mu’awiah kuhusiana na sifa alizokuwa akimsifia mwanawe (Yazid). Katika jamabu zake, Imamu Hussein (a.s) alionekana kuunasibiha Ukhalifa na ukoo wake, na kudai kuwa, suala la Ukhali linahusiana na familia yake, na yeye mwenye ni mwenye haki zaidi kuliko Yazid katika suala hilo. [163]

Hotuba ya Imamu Hussein (a.s) huko Mina

Makala asili: Hotuba ya Imamu Hussein huko Mina

Katika mwaka wa 58 mwandamo, miaka miwili kabla ya kifo cha Mu'awiah, Imam Hussein (a.s) alitoa hotuba ya malalamiko huko Mina. [164] Hotuba hii ilikuja katiaka wakati wa kilele cha shinikizo la Mu'awiah dhidi ya Mashia. [165] Ndani ya hotuba yake aliashiria umuhimu wa kuamrisha mema na kukataza maovu, fadhila za Imamu Ali na nafasi ya Ahlul-Bayt (a.s). Alisisitiza umuhimu Na wajibu wa maulamaa kuamrisha mema na kukataza maovu, ulazima wa wanazuoni kusimama dhidi ya madhalimu, na pia hasara za maulamaa kuwanyamazia madhalimu.

Mwitikio wake (a.s) juu ya ukhalifa wa Yazid

Baada ya kifo cha Mu’awiah mnamo mwezi 15 Rajabu mwaka wa 60 Hijiria, Yazid aliingia madarakani [166] na akaamua kuchukua kiapo cha utiifu kwa nguvu kutoka kwa baadhi ya wenye satua (mamlaka) katika jamii, ambao hawakuridhika na maamuzi wa baba yake wa kumrithisha Ukhalifa. Miongoni mwa watu liopingana na maamuzi hayo ni Hussein bin Ali (a.s). [167] Hata hivyo Hussein (a.s) Alikataa katakata kutoa kiapo hicho. [168] Mnamo mwezi 28 Rajabu Imamu aliamua kuondoka Madina pamoja na familia yake na Masahaba zake kuelekea Makka. [169]

Alipofika Makka watu wa Makka pamoja na walikuwa wakifanya ibada ya Umra, walimpa karibisho mema Imamu Hussein (a.s). [170] Alikaa humo kwa zaidi ya miezi minne (kutoka mwezi 3 Shaabani hadi mwezi 8 Dhulhijjah). Katika kipindi hicho, watu wa mji wa Kufa wakapata habari ya kuwa Imamu wao (Hussein) (a.s) hakutoa kiapo cha utifu kwa Yazid, hivyo wakaamua kumwandikia barua na wakamwalika aende Kufa. [172] Hussein bin Ali (a.s) aliamua kumtuma Muslim bin Aqiil kwenda Kufa ili kuhakikisha madai ya watu wa Kufa na uzito wa mualiko wao unaohusu kumuunga mkono dhidi ya Yazid. Kisha Imamu Hussein, familia yake pamoja Masahaba zake wakaamua kuondoka Makka kwenda Kufa mnamo mwezi 8 Dhu Hijjah. [174]

Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti, Imamu Husein (a.s) alifahamu kuwepo kwa njama ya kumuua akiwa katika mji wa Makka, kwa hiyo ili kuhifadhi utakatifu wa Makka, akaamua kuondoka mjini humo na kwenda Iraq. [175]

Tukio la Karbala

Makala asili:Tukio la Karbala

Tukio la Karbala, ambalo lilipelekea kuuawa kishahidi Hussein bin Ali (a.s) na Masahaba zake, ndio tukio lenye nafsi muhimu zaidi ndani ya maisha yake (a.s). Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti, Imam Hussein (a.s) alikuwa anajua fika kuhusu kifo chake cha kishahidi, hata kabla ya kuondoka Makka na kuelekea Iraq. Tukio hili lilitokea baada ya yeye kukataa kutoa kiapo cha utiifu kwa Yazid. Husein (a.s) ambaye alikuwa akielekea mji Kufa yeye, familia yake pamoja na Masahaba zake kupitia mwaliko wa watu Kufa, alidhibitiwa na jeshi la upinzani chini ya uongozi wa Hurru bin Yazid Al-Riahi akiwa katika eneo liitwalo Dhuu Hasmi. Jambo amabalo lilipelekea kubadili njia. [176]

Kwa mujibu wa vyanzo vingi, walifika Karbala siku ya pili ya mwezi wa Muharram, [177] na siku iliyofwata, jeshi la watu elfu nne kutoka kwa watu wa Kufa chini ya uongozi wa Omar bin Sa’ad liliingia Karbala. [178] Kwa mujibu wa ripoti za kihistoria, kulikuwa na mazungumzo kadhaa yaliyofanyika kati ya Hussein bin Ali na Omar bin Sa'ad. [179] Ila Ibnu Ziadi hakuridhika isipokuwa ima achukue kiapo cha utiifu kutoka kwa Hussein (a.s) ajili ya Yazidi au asimamishe vita. [180]

Jioni ya mwezi tisa Muharram (Tasu'a), jeshi la Omar bin Sa'ad lilijitayarisha kwa vita, lakini Imamu Hussein (a.s) alipumzika usiku huo ili kumuomba Mwenyezi Mungu. [181] Katika usiku wa Ashura (mwezi kumi Muharram), alizungumza na Masahaba zake na kuwaruhusu kuchukua kiapo chao walichomuapia kwa ajli ya kumtii na akawaruhusu kuondoka na kuachana naye, kwani alitaka kila mmoja awe na hiari ya kubaki au kuingia vitani kwa hiari na uhuru wake kamili, bila ya kuhisi ulazima wa kubaki kwa sababu ya kiapo chao cha kumtii akiwa ni Khalifa wao. Lakini Masahaba hao walisisitiza kubaki na uaminifu wa kulinda kiapo chao juu yake. [182]

Asubuhi ya siku ya Ashura, vita vilianza na ilipofika adhuhuri, Masahaba wengi wa Hussein bin Ali (a.s) wakawa wameshauawa kishahidi. [183] Wakati wa vita, Hurru bin Yazid, mmoja wa makamanda wa jeshi la upande wa watu wa Kufa alijiunga na Imam Hussein (a.s). [184] Baada ya Masahaba kuuawa, watu wa upande wa familia ya Imamu Hussein (a.s) wakaingia vitani. Wa kwanza wao alikuwa Ali Akbar, [185] nao pia waliuawa kishahidi mmoja baada ya mwingine. Kisha Husein bin Ali (a.s) naye akaingia uwanjani na kuuwawa kishahidi jioni ya siku ya 10 ya Muharram, kupitia mkono wa Shimru bin Dhul Al-Jaushan. [186] Kwa mujibu wa baadhi ya Riwaya, Sinan bin Anas ndiye aliye mkata kichwa. [187] Siku hiyo hiyo kichwa cha Hussein bin Ali (a.s) kilitumwa kwa Ibn Ziad. [188]

Umar Sa’ad, katika utekelezaji wa amri ya Ibn Ziad, aliamuru baadhi ya farasi kurukaruka juu ya mwili wa Hussein (a.s) na kuvunjavunja mifupa yake. [189] Wanawake na watoto pamoja na Imam Sajjad (a.s), ambaye alikuwa mgonjwa siku hiyo, walichukuliwa mateka na kupelekwa mji wa Kufa, kisha wakapelekwa Sham (Syria). [190] Mwili wa Imamu Hussein (a.s) pamoja na miili ya watu wapatao 72, ambayo ni miili ya Masahaba zake [191], ilizikwa mnamo mwezi 11 au 13 Muharram. [192] Miili hiyo ilizikwa na kundi la Bani Asad. Na kwa mujibu wa baadhi ya Riwaya, kazi ya mazishi ilitendeka na kuhudhuriwa na Imamu Sajjad (a.s). [193]

Mitazamao na athari zakae

Makala asili: Mapinduzi ya Imamu Hussein (a.s)

Kuna mitazamo tofauti kuhusu harakati za Imamu Hussein (a.s) kutoka Madina kwenda Makka, kutoka huko hadi Kufa, pamoja na vita na askari wa Omar Sa'ad huko Karbala. Kwa mujibu wa maoni ya Mohammad Esfandiari, mwanachuoni na mhakiki wa matukio ya Ashura, ni kwamba; Nadharia maarufu zaidi kuhusu lengo la Immu Hussein (a.s) katika mapinduzi yake, ni kuuawa kishahidi. Nadharia hii ina wafuasi na washabiki wengi, akiwemo Lutfullah Safi, Murtadha Mutahhari, Sayyid Muhsin Amin na Ali Shariati. [195] Mtazamo mwengine unasema kwamba; Imamu Hussein (a.s), alisimama dhidi ya Yazid kwa nia ya kusimamisha serikali. Miongoni mwa wanazuoni wa zamani wenye mtazamo huu ni Sayyid Murtadha na kwa upande wa wanazuoni wa zama za hivi karibuni, ni Salehi Najafaabaadi, ambaye amaweka wazi maoni ya mtazamo huo katika kitabu chake Shahid Jawid (Shahidi wa milele). [196] Kulingana na maoni wa Sihhati Sardiwadi ni kwamba; Watu kama Sheikh Mofid, Sheikh Tusi, Sayyid bin Taauus na Allamah Majlisi, wapo dhidi ya maoni haya. [197] Baadhi, kama Sheikh Ali Panaah Eshtihardi, wamezingatia mapinduzi na harakati hizi za Imamu wa tatu wa Mashia, kuwa sio kwa ajili ya kupigana vita na kusimamisha dola, bali ni kwa ajili ya kuokoa maisha yake. [198]

Mapinduzi ya Imamu Hussein (a.s) yalisababisha mwamko wa makundi mengi, na mara tu baada ya kuuawa kishahidi, harakati za kimapinduzi na maandamano zilianza na kuendelea kwa muda wa miaka kadhaa. Maandamano ya kwanza yalikuja kupitia ghasia za Abdullah bin 'Afif [199] dhidi ya Ibnu Ziad. Baada ya hapo zikafuatia harakati tofauti za kiupinzani, kama vile: Harakati za maandamano ya Tawwaabiin, harakati za Mukhtar, harakati za Zaid bin Ali, na harakati za Yahya bin Zaid pia ni miongoni mwazo. Pia vugvugu la harakati za Siyaahe Jaamgan zilioongozwa na Abu Muslim Khorasani dhidi ya Bani Umayyah, ambazo mwishowe zilipelekea kuporomoka kwa utawala wa Bani Ummayyah. Ghasia zote hizo zilifanyioka kupitia kauli mbiu na poropaganda za kulipiza kisasa mauwaji ya Karbala. [200]. Hata mapinduzi ya Kiisilamu ya Imam Khomeini nchini Iran, pia yalipata motisha kupitia tukio la Karbala. Imamu Khomeini alisema:"Nchi yetu isingeshinda lau si mahubiri yanayofanyika kuhusu tukio la Karbala, hotuba, maadhimisho na mikusanyiko ya maombolezo ya mauwaji ya Karbala. Kila mtu aliinuka chini ya bendera ya Imamu Husein (a.s).” [201] Katika nyanja za tamaduni za watu mbali mbali duniani, Waislamu na hata wafuasi wa dini nyingine, humchukulia Hussein bin Ali (a.s) kama ni nembo na mfano katika suala la kujitolea, kupinga dhulma, kudai uhuru, kuhami na kutetea maadili pamoja na kusimamia haki za wanadamu. [202]

Sifa zake kimwili na kiroho

Makala asili: Ahlul-Bayt (a.s), Ahlul-kisaa, Mubahala na Aya ya Tat'hir
Muonekano

Katika maandiko yanayohusu maisha ya wapokezi wa Riwaya pia maandiko ya kihistyoria, kumetajwa sifa nyingi kuhusu kufanana kwake na Mtukufu Mtume (s.a.w.w). [204] Riwaya zimeeleza kuwa; Huseein (a.s) alikuwa ni mwenye kufanana zaidi na Mtume (s.a.w.w). Kuhusu mavazi yake, imeelezwa kuwa, alikuwa akivaa kilemba cha manyoya [205] na kupaka rangi nywele pamoja na ndevu zake. [206]


Sifa alizosifiwa na Mtume (s.a.w.w)

Hadithi nyingi za Mtume (s.a.w.w) zimesimuliwa kuhusu fadhila zake (a.s), miongoni mwake ni kama ifuatavyo:

Maneno "Amani iwe juu yako, Sayyid Shabab Ahl al-Jannah" juu ya moja ya milango ya kaburi la Imamu Husein (a.s).
  1. Hassan na Hussein ni mabwana wa vijana wa Peponi”. [207]
  2. Upande wa kulia wa kiti cha enzi (Arshi ya Mungu) kumeandikwa Hussein ni nuru ya uwongofu na jahazi ya wokovu.
  3. Hussein anatokana nami nami ninatokana na Hussein. [208]
  4. Mwenye kuwapenda wawili hawa (Hasan na Hussein) amenipenda mimi, na mwenye uadui nao ana uadui nami.” [209]


Utabiri wa kifo chake

Kuna Riwaya nyingi kuhusu bishara ya kifo chake kishahidi (a.s) [210]. Moja ya Riwaya hizo ni hadithi ya Lauh, katika Hadithi hiyo Mtume (s.a.w.w) amesema kwamba; Mwenyezi Mungu alimtukuza na kumsifu Hussein kwa kifo chake cha kishahidi na akamfanya kuwa mbora wa mashahidi. [211] Allaamah Majlisi kwenye Juzu ya 44 ya kitabu chake Bihaaru Al-Anwaar, mlango wa 30, amesimulia Riwaya kuhusu jinsi Mungu alivyotoa habari za kifo cha kishahidi cha Hussein (a.s) kwa baadhi ya mitume wake, akiwemo Adam, Nuhu, Ibrahim, Zakaria na Muhammad (s.a.w.w), nao baada ya kupokea habari hiyo wakamlilia na kuhuzunika. [212] Imepokewa pia kwamba Amiru Al-Mu’minina (a.s) akiwa njiani kuelekea Siffiin, alipofika Karbala, aliashiria sehemu hiyo kwa kidole chake na kusema: "Hapa ndipo mahali patakapomwagwa damu zao”. Kulingana na nukuu za Sheikh Saduku katika kitabu Al-Amaal, “Imamu Ali (a.s) alichukua udongo wa sehemu hiyo na kunusa huku akisema: Wewe ni udongo wa ajabu, kuna watu watakaoingia Peponi bila hisabu”. [214]


Karama zake (a.s)

Katika baadhi ya Riwaya, kuna sifa nyingi bainifu za Imamu Husein zilizorodheshwa, kama vile kunywa maziwa kimiujiza kutoka kwenye kidole cha Mtume (s.a.w.w), [215] Malaika Fatras aliyesalimika na kuokoka kwa baraka za Imamu Hussein (a.s). [216] Vile vile kuna Hadithi isemayo kwamba; “Mwenyezi Mungu aliweka ponyo katika udongo wa eneo alilouwawa Hussein (a.s). Pia Allah amejaalia kutakabaliwa dua ziombwazo kaburini kwake”. [218]


Tabia zake na maadili yake (a.s)

Alikaa pamoja na masikini, alikubali mwaliko wao, alikula nao, aliwakaribisha nyumbani kwake na hakuwanyima alicho nacho nyumbani kwake. [219] Siku moja muhitaji alimwomba msaada, Imamu ambaye alikuwa anasali alifupisha sala yake na kumpa alichokuwa nacho. [220] Alikuwa akiwaacha huru watumwa na wajakazi wake kwa ajili ya tabia zao nzuri. Inasemekana kwamba; Mu’awiah alimzawadia na kumtimia Imamu Hussein Kijakazi aliyemuambatanisha na mali nyingi pamoja na nguo. Ila Imamu Hussein (a.s), akamwacha huru kwa kusoma kwake Qur'ani na kutunga shairi kuhusu dunia na mwisho wa maisha ya mwanadamu. Imamu (a.s) alimpa uhuru wake na kumpa mali zote alizoambatanishwa nazo na Muawiah wakati alipoletwa kwa Imamu Hussein (a.s). [221] Pia, siku moja, mjakazi fulani alimpa shada la maua, bila ya kusita Imamu Hussein (a.s) alimwachia huru mjakazi huyo. Watu wakasema: umemwachia huru kwa shada la maua tu? Imamu Hussein (a.s) akawasomea Aya isemayo: وَ إِذا حُیِّیتُمْ بِتَحِیَّةٍ فَحَیُّوا بِأَحْسَنَ مِنْها أَوْ رُدُّوها Maana yake ni kwamba: "Na mnapotolewa aina fulani ya salamu, basi jibuni kwa salamu iliyo bora zaidi au ijibuni kama ilivyokuja". [222] Kisha akwambia: "Mwenyezi Mungu ametufundisha adabu ya namna kama hii." [223]

Imamu Hussein (a.s) alikuwa ni mkarimu sana na alisifika kwa unyoofu wa mkono wake katika kusaidia watu. [224] Alikuwa akimheshimu sana kaka yake (Imamu Hassan (a.s)), hivyo basi alikuwa akisaidia watu kwa kiwango kisichopindukia kiwango atoacho Imamu Hassan (a.s), ili alinde heshima ya kaka yake. [226]

Maombolezo na ziara ya kaburi lake (a.s)

Makala asili: Maombolezo ya Muharram

Mashia (na hata wasiokuwa Mashia) wanamuomboleza Imam Hussein (a.s) na mashahidi wa Karbala katika mwezi wa Muharram. Mashia wana mila maalumu katika maombolezo yao. Miongoni mwa mambo muhimu na maarufu katika mila hizo ni: Kusoma tungo au mashairi ya huzuni kuhusiana na mauwaji ya Karbala, kuadhimisha msiba kwa kusoma hotuba za majonzi, kuchora picha au michoro yenye kuashiria matukio ya Karbala pamoja na kusoma andiko maarufu lijulikanalo kwa jina la Ziaratu Ashura. [227]

Maombolezo ya Imam Hussein (a.s) yalianza tangu siku za kwanza baada ya tukio la Ashura. [228] Kwa mujibu wa Riwaya, mateka wa Karbala walipokuwepo Syria, wanawake wa Bani Hashim waliomboleza kwa siku kadhaa kwa kuvaa nguo nyeusi. [229] Baada kusimama kwa baadhi ya serikali za Kishia na Mashia kupata ahueni kutokana na dhulma dhidi yao, ilipelekea maadhimisho ya tukio la Ashura kuwa ni jambo lilikubalika na kupata nguvu za kuungwa mkono kiserikali ndani ya jamii mbali mbali. [230]

Kwa mujibu wa Riwaya za kihistoria na Hadithi mbali mbali, Maimamu wa Shia walitilia maanani sana maombolezo na kulia katika maombolezo ya Hussein bin Ali (a.s), pia wakawaamuru Mashia kufanya hivyo ili kuweka hai na kudumisha kumbukumbu za Ashura. [231]

Ziara ya kuzuru Imamu Hussein (a.s)

Makala asili: Ziyara ya Imam Husein (a.s)

Kumzuru Imamu Hussein (a.s), ni jambo lililosisitizwa sana katika Hadithi za Maasumina (a.s), jambo hilo huzingatiwa kuwa ni moja miongoni mwa matendo bora apaswayo mtu kushikamana nayo. [232] Kwa mujibu wa fungu miongoni mwa mafungu ya Hadithi ni kwamba; Thawabu yake ni sawa na malipo ya Hijja na Umra. [233]

Katika vitabu vyenye ziara mbali mbali, kumekusanywa ziara tofauti zisiozofungamana na minasaba maalumu, [234] na pia kuna ziara kadhaa maalum zianazosomwa kwa nyakati na minasaba maalum. [235] Ziara zote hizo ni ziara zinazohusiana na Imamu Hussein (a.s). Miongoni mwa ziara hizo ni: Ziaratu Ashura, Ziaratu Al-Warith na Ziaratu Naahiatu Al-Muqaddasa. Hizi ndio ziara maarufu zaidi kati ya ziara mbali mbali.

Arobaini ya Imamu Hussein (a.s)

Makala asili: Arobaini ua Hussein, ziaratu al-arbain na maandamano ya arobaini

Siku ya 40 baada ya kuuawa kishahidi Imamu Hussein (a.s), iitwayo Arba'inu Al-Husseini au Siku ya Arbaini, Mashia wengi katika siku kama hiyo wanakwenda kuzuru kaburi la Imamu Hussein (a.s). Kwa mujibu wa ripoti za kihistoria, Jabir bin Abdullah Al-Ansari, ndiye mtu wa kwanza kuzuru kaburi la Imamu Hussein (a.s). [236] Katika kitabu maarufu kiitwacho Luhuuf, mateka wa Karbala pia waliwazuru mashahidi wa Karbala katika siku ya Arubaini, katika mwaka huo huo wa 61 Hijiria, ziara ambayo ilifanyika wakati wakiwa njiani wakirejea kutoka Syria kwenda Madina. [237]

Masisitizo ya Ziara ya Arbaeen yamewafanya Mashia, hususan wakazi wa Iraq, kila mwaka kuacha miji yao na kuelekea Karbala kwa mtindo wa maandamano. Nyenendo hizi, ambazo mara nyingi hufanyika kwa matembezi ya miguu, ni mojawapo ya maandamano yenye kuhudhuriwa na watu wengi zaidi duniani. Kulingana na vyanzo vya habari, mnamo 2018. Zaidi ya wanaziara milioni 18 walishiriki katika tukio hili linalofanyika kila mwaka. [238]

Dharihu (Raudha) ya Imamu Hussein

Makala asili: Raudha ya Imamu Hussein (a.s)
Hitilafu kutengeneza picha ndogo:
Bendera nyekundu juu ya Quba la Imam Hussein kama ishara ya umwagaji damu

Bendera nyekundu juu ya kuba la Imam Hussein ni alama ya hamu ya kulipiza kisasi cha umwagaji damu. [239] Eneo la kaburi la Imam Hussein (a.s) linaitwa Haa-i-ru Husseini au Raudha ya Imamu Hussein. Eneo la Haa-iru lina fadhila na kanuni maalum za kifiqhi. Moja kati ya sheria zake za kifiqhi, ni kule msafiri kuwa na uhuru wa kusali sala yake kamili, au kusali sala ya safari akiwa katika eneo hilo. [240] Kuna maoni kadhaa kuhusu eneo halisi la Raudha ya Imamu (a.s), eneo dogo kabisa lililokadiriwa katika maoni tofauti, ni kiwango cha mita 11 kutoka kwenye kaburi la Imam Hussein. Eneo ambalo ndilo linalokadiriawa kuwa na daraja na fadhila kubwa zaidi. [241]

Raudha ya Imamu Hussein (a.s)

Makala asili: Raudha ya Imamu Hussein (a.s) na Kuharibiwa kwa Raudha ya Imam Hussein (a.s)

Kwa mujibu wa ripoti zilizopo katika vitabu tofauti, jengo la kwanza la kaburi la Hussein bin Ali (a.s) lilijengwa wakati wa Mukhtar Thaghafi kupitia amri yake yeye mwenyewe. Tangu zama hizo hadi sasa, jingo hilo limekarabatiwa na kupanuliwa mara kadhaa. [242] Mara kadha haramu (raudha) ya Imamu Hussein (a.s) iliharibiwa na baadhi ya Makhalifa wa Bani Abbas, [243] na viongozi wa Kiwahabi. [244] Miongoni mwa waliofanya hivyo ni: Mutawakkil Abbasi, aliye amuru ardhi ya eneo la Raudha kuchimbuliwa kama ardhi ya kilimo na kutiwa maji kaburini mwake. [245]

Urithi wa kiroho kutoka kwa Imamu Hussein (a.s)

Musnad al-Imam al-Shaheed yenye mkusanyiko wa maneno ya Imamu Hussein (a.s.)

Kutoka katika hadithi nyingi na vyanzo vya kihistoria, kuna nukuu mbali mbali zinazosimulia urithi wa kiroho kutoka kwa Hussein bin Ali (a.s). Miongoni mwake ni: maneno yalionukuiliwa kutoka kwake, dua, barua, mashairi, khutba pamoja na wasia wake. Kazi zote hizo zimekusanywa katika kitabu kiitwacho Musnad Al-Imam Al-Shaheed kilichotungwa na Azizullahi Attaaridi. Hicho ndio Kitabu au diwani iliyokusanya maneno ya Imam Hussein (a.s).

Kuna maneno na maandiko yanayo ashiria kwamba: Hali ya kisiasa ya wakati wa utawala wa Muawiah, ilikuwa hairuhusu kukusanya Riwaya kutoka kwa Imamu Hussein (a.s). [246] Kwa hiyo, mengi yaliyosimuliwa kutoka kwake, yalikuwa ni maneno na Riwaya zilizorikodiwa katika kipindi cha safari yake ya kutoka Madina kwenda Karbala.[247] Allamah Tehrani, ni mmoja wa wanaokubaliana na maoni hayo. Allamah Tehrani anaamini ya kwamba; Shinikizo la Bani Umayyah lilisababisha mara chache sana watu kupata fursa ya kuonana na Imamu Hussein (a.s). Au pia Riwaya zilizosimuliwa kutoka kwake zilipotea kwa sababu ya woga na khofu ya wapokezi wa zama hizo. Jambo ambalo lilisababisha kupukutika kwa Riwaya hizo na kuto wafika watu wa kizazi kilicho fuata. [248] Licha ya hayo, bado kunaonekana mafunzo ya akida, hukumu za kisheria, na maadili yaliyonukuliwa kwa njia tofauti kutoka kwake (a.s). [249]

Dua: Takriban kuna idadi ya dua 20 zilizosimuliwa kutoka kwake katika kitabu cha Musnad Al-Imam Al-Shahid. Dua maarufu zaidi kati ya hizo ni dua ya 'Arafah, aliyoisomwa siku ya Arafah katika jangwa la Arafah. [250]

Mashairi yanayonasibishwa kwake: Kuna idadi kadhaa ya mashairi yamenasibishwa kwa Imamu Hussein (a.s). Muhammad Sadiq Karbasi amekusanya mashairi hayo katika juzu mbili za kitabu kiitwacho "Diiwan Al-Imami Al-Hussein" katika ukusanyaji wake, amechunguza mapokezi ya mashairi hayo pamoja na upeo wa fasihi yake. [251]

Khutba na wasia: Kuna vyanzo kadhaa vilivyo nukuu khutba za Imam Hussein (a.s). Miongi mwazo, ni khutba ya Mina, [252] khutba yake ya siku ya Ashura, [253] pamoja na wasia wake uliomwandikia ndugu yake (Muhammad Hanafiyah), ambamo katika wasia huo, alieleza madhumuni ya harakati zake za kimapinduzi. [254]

Barua: Barua 27 kutoka kwa Hussein bin Ali (a.s) zimekusanywa katika kitabu Makaatibu Al-A-i-mmah [255] Baadhi ya barua hizo, ni zile barua alizozielekeza kwa Mu’awiah, pia zile barua zilizohusiana na maudhui tofauti alizowaandikia watu mbali mbali maishani mwake.

Vyanzo

  • Abū ʿAlī Miskawayh. Tajārub al-umam. Edited by Abū l-Qāsim Imāmī. Tehran: Surūsh, 1379 Sh.
  • Abū l-Faraj al-Isfahānī, ʿAlī b. al-Ḥusayn. Kitāb al-aghānī. Cairo: [n.p], 1383 AH.
  • Abū l-Faraj al-Isfahānī, ʿAlī b. al-Ḥusayn. Maqātil al-ṭālibīyyīn. Edited by Aḥmad Ṣaqar. Beirut: Dār al-Maʿrifa, [n.d].
  • Aḥmad b. Ḥanbal. Al-Musnad. Beirut: Dār al-Ṣādir, [n.d].
  • Akkād, ʿAbbās Maḥmūd al-. Abū l-shuhadāʾ al-Ḥusayn b. ʿAlī (a). Second edition. Tehran: al-Majmaʿ al-ʿĀlamī li-l-Taqrīb, 1429 AH.
  • Āl Ṭuʿma, Salmān Hādī. Karbalāʾ wa ḥaramhā-yi muṭahhar. Tehran: Mashʿar, [n.d].
  • Ālūsī, Maḥmūd b. ʿAbd Allāh al-. Rūḥ al-maʿānī fī tafsīr al-Qurʾān al-ʿAẓīm. Edited by ʿAlī ʿAbd al-Bārī ʿAṭīyya. Beirut: Dār al-Kutub al-ʿIlmīyya, 1415 AH.
  • ʿĀmilī, Jaʿfar Murtaḍā al-. Al-Ḥayāt al-sīyāsīyya li-l-Imām al-Ḥasan. Beirut: Dār al-Sīra, [n.d].
  • Balādhurī, Aḥmad b. Yaḥyā al-. Ansāb al-ashrāf. Edited by Suhayl Zakār & Rīyāḍ al-Ziriklī. Beirut: Dār al-Fikr, 1417 AH.
  • Bayhaqī, ʿAlī b. Zayd al-. Lubāb al-ansāb wa l-alqāb wa l-aʿqāb. Edited by Mahdī Rajāʾī. Qom: Maktabat Āyatollāh Marʿashī al-Najafī, 1385 Sh.
  • Bukhārī, Sahl b. ʿAbd Allāh al-. Sirr al-silsila al-ʿalawīyya. Edited by Muḥammad Ṣādiq Baḥr al-ʿUlūm. Najaf: [n.d], 1381 AH.
  • Dhahabī, Muḥammad b. Aḥmad al-. Tārīkh al-Islām wa wafayāt al-mashāhīr wa l-aʿlām. Second edition. Beirut: Dār al-Kitāb al-ʿArabī, 1409 AH.
  • Dīnawarī, Aḥmad b. Dāwūd al-. Al-Akhbār al-ṭiwāl. Edited by ʿAbd al-Munʿim ʿĀmir. Qom: Manshūrāt al-Raḍī, 1368 Sh.
  • Fakhr al-Dīn al-Rāzī, Muḥammad b. ʿUmar al-. Al-Tafsīr al-kabīr. Beirut: Dār al-Fikr, 1405 AH.
  • Ḥākim al-Nīshābūrī, Muḥammad b. ʿAbd Allāh al-. Al-Mustadrak ʿalā l-ṣaḥīḥayn. Edīted by Yūsuf ʿAbd al-Raḥmān al-Marʿashlī, Beirut: [n.p], 1406 AH.
  • Ibn ʿAbd al-Barr, Yūsuf b. ʿAbd Allāh. Al-Istīʿāb fī maʿrifat al-aṣḥāb. Edited by ʿAlī Muḥammad al-Bajāwī. Beirut: Dār al-Jail, 1412 AH.
  • Ibn Abī l-Thalj, Muḥammad b. Aḥmad. Tārīkh al-aʾimma. Edited by Maḥmūd Marʿashī. Qom: Kitābkhāna-yi Āyatollāh Marʿashī Najafī, 1406 AH.
  • Ibn Abī Shayba, ʿAbd Allāh b. Muḥammad. Al-Muṣannaf fī l-aḥādīth wa l-āthār. Edited by Saʿīd Muḥammad Laḥḥām. Beirut: [n.p], 1409 AH.
  • Ibn ʿArabī, Abū Bakr. Al-ʿAwāṣim min al-qawāṣim. Cairo: al-Maktaba al-Salafīyya, [n.d].Ibn ʿAsākir, ʿAlī b. al-Ḥasan. Tārīkh madīnat Damascus. Beirut: Dār al-Fikr, 1415 AH.
  • Ibn Aʿtham, Aḥmad. Al-Futūḥ. Beirut: Dār al-Aḍwāʾ, 1411 AH.
  • Ibn Athīr, ʿAlī b. Abī l-Karam. Al-Kāmil fī l-tārīkh. Beirut: Dār al-Ṣādir-Dār Beirut, 1965.
  • Ibn Athīr, ʿAlī b. Abī l-Karam. Usd al-ghāba fī maʿrifat al-ṣaḥāba. Beirut: Dār al-Kitāb al-ʿArabī, [n.d].
  • Ibn Bābawayh al-Qummī, Abū l-Ḥasan b. ʿAlī. Al-Imāma wa l-tabṣara min al-Ḥayra. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1363 Sh.
  • Ibn Ḥajar al-ʿAsqalānī, Muḥammad b. Aḥmad. Al-Iṣāba fī tamyīz al-ṣaḥāba. Beirut: Dār al-Kutub al-ʿIlmīyya, 1415 AH.
  • Ibn Kathīr, Ismāʿīl b. ʿUmar. Al-Bidāya wa l-nihāya. Beirut: Dār Iḥyāʾ al-Turāth al-ʿArabī, 1408 AH.
  • Ibn Khaldūn, ʿAbd al-Raḥmān b. Muḥammad. al-ʿIbar (Tārīkh Ibn Khaldūn). Beirut: Dār al-Fikr, 1401 AH.
  • Ibn Manẓūr, Muḥammad b. Mukarram. Lisān al-ʿarab. Beirut: Dār al-Ṣādir, 1414 AH.
  • Ibn Qūlawayh, Jaʿfar b. Muḥammad. Kāmil al-zīyārāt. Najaf: Dār al-Murtaḍawīyya, 1356 AH.
  • Ibn Qutayba, ʿAbd Allāh b. Muslim. Al-Imāma wa l-sīyāsa. Edited by ʿAlī Shīrī. Beirut: Dār al-Aḍwāʾ, 1410 AH.
  • Ibn Qutayba, ʿAbd Allāh b. Muslim. Al-Maʿārif. Edited by Tharwat ʿAkāsha. Cairo: al-Hiyʾa al-Miṣrīyya al-ʿĀmma li-l-Kitāb, 1960.
  • Ibn Saʿd, Muḥammad b. Manīʿ al-Baṣrī. Al-Ṭabaqāt al-kubrā. Second edition. Beirut: Dār al-Kutub al-ʿIlmīyya, 1418 AH.
  • Ibn Shahrāshūb, Muḥammad b. ʿAlī. Manāqib Āl Abī Ṭālib. Edited by Hāshim Rasūlī Maḥallātī. Qom: [n.p], [n.d].
  • Ibn Shuʿba al-Ḥarrānī, Ḥasan b. ʿAlī. Tuḥaf al-ʿuqūl. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī, 1404 AH.
  • Ibn Ṭalḥa al-Shāfiʿī, Muḥammad. Maṭālib al-suʾūl fī manāqib Āl al-rasūl. Edited by Mājid Aḥmad ʿAṭīyya, [n.p], [n.d].
  • Ibn Ṭāwūs, ʿAlī b. Mūsā. Al-Luhūf ʿalā qatlay al-ṭufūf. Qom: Uswa, 1414 AH.
  • Ibn Ṭāwūs, ʿAlī b. Mūsā. Iqbāl al-aʿmāl. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1367 Sh.
  • Ibn Tiymīyya al-Ḥarrānī. Minhāj al-sunna al-nabawīyya. Edited by Muḥammad Rashād Sālim. Riyadh: Jāmiʿat al-Imām Muḥammad b. Suʿūd al-Islāmīyya, 1406 AH.
  • Irbilī, ʿAlī b. ʿIsā al-. Kashf al-ghumma fī maʿrifat al-aʾimma. Qom, al-Radī, 1421 AH.
  • Isfandīyārī, Muḥammad. Kitābshināsī-yi tārīkhī-yi Imām Ḥusayn. Tehran: Sāzmān-i Chāp wa Nashr, 1380 Sh.
  • Ishtihārdī, ʿAlī Panāh. Haft sāla chirā ṣidā dar āward?. Qom: Intishārāt-i ʿAllāma, 1391 Sh.
  • Jaʿfarīyān, Rasūl. Ḥayāt-i fikrī wa sīyāsī-yi aʾimma. Sixth edition. Qom: Anṣārīyān, 1381 Sh.
  • Khwārizmī, Muḥammad b. Aḥmad al-. Maqtal al-Ḥusayn. Second edition. Qom: Anwār al-Hudā, 1423 AH.
  • Kilīddār, ʿAbd al-Jawād. Tārīkh-i Karbalāʾ wa ḥāʾir-i Ḥusaynī. Najaf: [n.p], 1376 Sh.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1365 Sh.
  • Majlisī, Muḥammad Bāqir al-. Biḥār al-anwār. Second edition. Tehran: Islāmīyya, 1363 Sh.
  • Maqrizī, Aḥmad b. ʿAlī. Imtāʿ al-asmāʾ bi-mā li-l-nabīyy min al-aḥwāl wa l-amwāl wa l-ḥafdat wa l-matāʿ. Beirut: Dār al-Kutub al-ʿIlmīyya, 1420 AH.
  • Minqarī, Naṣr b. Muzāhim al-. Waqʿat ṣiffīn. Sevond edition. Qom: Maktaba Āyatollāh Marʿashī al-Najafī, 1403 AH.
  • Aḥmadī Mīyānajī, ʿAlī. Makātīb al-aʾimma. Qom: Dār al-Ḥadīth, 1426 AH.
  • Motahharī, Morteza. Khadamāt-i mutaqābil-i Iran wa Islām. Tehran: Nashr-i Ṣadrā, 1380 Sh.
  • Mufīd, Muḥammad b. Muḥammad al-. Al-Irshād fī maʿrifat ḥujaj Allāh ʿalā l-ʿibād. Qom: Kungira-yi Shaykh al-Mufīd, 1413 AH.
  • Mufīd, Muḥammad b. Muḥammad al-. al-Jamal wa l-nuṣra li-sayyid al-ʿitra fī ḥarb al-Basra. Qom: Kungira-yi Shaykh al-Mufīd, 1413 AH.
  • Muḥaddithī, Jawād. Farhang-i ʿĀshūrā. Qom: Nashr-i Muʿarrif, 1380 Sh.
  • Muḥammadī Riyshahrī, Muḥammad. Dānishnāma-yi Imām Ḥusayn. Translated by Muḥammad Murādī. Qom: Dār al-Ḥadīth, 1430 AH.
  • Muqarram, ʿAbd al-Razzāq al-. Maqtal al-Ḥusayn. Beirut: Dār al-Kitāb al-Islāmīyya, [n.d].
  • Muslim b. Ḥajjāj. Ṣaḥīḥ Muslim. Beirut: Dār al-Maʿrifa, 1423 AH.
  • Nāṣirī Dāwūdī, ʿAbd al-Majīd. Inqilāb-i Karbalāʾ az dīdgāh-i ahl-i sunnat. Qom: Muʾassisa-yi Imām Khomeini, 1385 Sh.
  • Naṣr b. Muzāhim. Waqʿat al-ṣiffīn. Qom: Maktaba Āyatollāh Marʿashī al-Najafī, 1403 AH.
  • Pīshwāyī, Mahdī. Tārīkh-i qīyām wa maqtal-i jāmiʿ-i Sayyid al-Shuhadāʾ. Qom: Muʾassisa-yi Imām Khomeini, 1389 Sh.
  • Ṣadūq, Muḥammad b. ʿAlī al-. Al-Khiṣāl. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī, 1403 AH.
  • Ṣadūq, Muḥammad b. ʿAlī al-. Iʿtiqādāt. Second edition. Tehran: Islāmīyya, 1395 Sh.
  • Ṣafar ʿAlīpūr, Ḥishmat Allāh. Kitābshināsī-yi ikhtiṣāṣī-yi Imām Ḥusayn. Qom: Yaqūt, 1381 Sh.
  • Ṣāḥibī, Muḥammad Jawād. 1373 Sh. "Maqtal wa maqtal nigārān." Majalla-yi Kiyhān-i Farhangī 111.
  • Sayyid Murtaḍā, ʿAlī b. al-Ḥusayn. Tanzīh al-anbīyāʾ. Beirut: Dār al-Aḍwāʾ, 1409 AH.
  • Sibṭ b. al-Jawzī, Yūsuf. Tadhkirat al-khawāṣ. Qom: Manshūrāt al-Sharīf al-Raḍī, 1418 AH.
  • Sulaym b. al-Qays. Kitāb Sulaym b. al-Qays. Qom: Hādī, 1405 AH.
  • Suyūṭī, ʿAbd al-Raḥmān b. Abī Bakr al-. Tārīkh al-khulafāʾ. Beirut: Maktabat Nazār Muṣṭafā l-Bāzz, 1425 AH.
  • Ṭabarī, Muḥammad b. Jarīr. Dalāʾil al-imāma. Beirut: Muʾassisat al-Aʿlamī li-l-Maṭbūʿāt, 1408 AH.
  • Ṭabarī, Muḥammad b. Jarīr. Tārīkh al-umam wa l-mulūk. Second edition. Beirut: Dār al-Turāth, 1387 AH.
  • Ṭabrisī, Aḥmad b. ʿAlī. Al-Iḥtijāj ʿalā ahl al-lijāj. Mashhad: Murtaḍā, 1403 AH.
  • Ṭaqūsh, Muḥammad Suhayl. Dawlat-i umawīyān. Translated to Farsi by Ḥujjat Allāh Jūdakī. Fifth edition. Qom: Pazhūhishgāh-i Ḥawza wa Dānishgāh, 1389 Sh.
  • Tirmizī, Muḥammad b. ʿIsā al-. Sunan. Edited by ʿAbd al-Raḥmān Muḥammad ʿUthmān. Beirut: Dār al-Fikr, 1403 AH.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Al-Amālī. Qom: Dār al-Thiqāfa, 1414 AH.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Miṣbāḥ al-mutahajjid. Beirut: Muʾassisat Fiqh al-Shīʿa, 1411 AH.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Tahḍīb al-aḥkām. Edited by Mūsawī Kharsān. Beirut: [n.p], 1401 AH.
  • Yaʿqūbī, Aḥmad b. Abī Yaʿqūb. Tārīkh al-Yaʿqūbī. Beirut: Dār al-Ṣādir, [n.d].
  • Yazdī, Sayyid Muḥammad Kāẓim al-. Al-ʿUrwa al-wuthqā. Beirut: [n.p], 1404 AH.
  • Zamakhsharī, Maḥmūd al-. Al-Kashshāf. Second edition. Qom: Nashr al-Balāgha, 1415 AH.
  • Zamānī, Aḥmad. Ḥaqāʾiq-i pinhān pazhūhishī dar zindigānī-yi sīyāsī-yi Imām Ḥasan (a). third edition. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī, 1380 Sh.