Aya ya Shahidun

Kutoka wikishia
(Elekezwa kutoka Aya ya “Shahidun”)

Aya ya Shahidun (Kiarabu: آية الشاهد) ni Aya 17 Surat Hud, nayo ni Aya inayohusina na uthibitisho wa kuthibitisha madai ya utume wa Bwana Mtume (s.a.w.w) kupitia ushahidi wa Qur'ani, vitabu vitakatifu vilivyotangulia pamoja na waumini wenye imani ya kweli. Aya hii iliteremka ili kuimarisha imani ya Mtume (s.a.w.w) na kuthibitisha Utume wake, baada ya washirikina kumtuhumu bwana Mtume (s.a.w.w) kwa kusema uwongo.

Katika vyanzo vya Hadithi vya pande zote mbili za Shia na Sunni, wamelielezea neno shahidi lililoko katika Aya hii, kuwa linamrudia Imamu Ali (a.s). Hata hivyo, wengine wamelirejesha neno hili marejeo mengine kinyume na Imamu Ali (a.s), kama vile; Jibril, ulimi wa bwana Mtume s.a.w.w, na Qur'ani tukufu. Hakimu Hisakani katika kitabu chake Shawahid al-Tanzil amenukuu zaidi ya Hadithi 16 kuthibitisha ya kwamba; Imamu Ali (a.s) ndiye shahidi aliye kusudiwa katika Aya hiyo.

Aya ya Shahidun imetambulliwa kuwa ndio ushahidi na uthibisho wa kuthibitisha haki ya uongozi na ukhalifa wa Imamu Ali (a.s) baada ya Bwana Mtume (s.a.w.w). Hii ni kwa sababu kwa mujibu wa Aya hiyo, shahidi ni lazima awe ni nafsi ya bwana Mtume (s.a.w.w), na kwa mujibu wa Aya ya Mubahala, Imam Ali (a.s), ametambulishwa kuwa yeye ndiye nafsi ya Mtume (s.a.w.w).

Miongoni mwa vitabu vilivyotangulia, Taurati ndio kitabu pekee kilichotajwa ndani ya Aya ya Shahidun. Wafasiri wamesema ya kwamba; sababu ya suala hili; ni kule kuenea kwa mawazo ya Kiyahudi katika maeneo ambayo Quran iliteremshwa ndani yake, na ukweli wa kwamba; katika zama hizo, Wakristo walikuwa wakiishi katika sehemu za mbali kabisa na maeneo hayo, kama vile miji iliyoko katika maeneo ya Syria na Yemen.

Matini na Tafsiri ya Aya

Aya ya 17 ya Surat Hud, imepewa jina la “Shahidun”. [1] Matini na tafsiri ya Aya hii, ni kama ifuatavyo:

أَفَمَنْ كَانَ عَلَى بَيِّنَةٍ مِنْ رَبِّهِ وَيَتْلُوهُ شَاهِدٌ مِنْهُ وَمِنْ قَبْلِهِ كِتَابُ مُوسَى إِمَامًا وَرَحْمَةً أُولَئِكَ يُؤْمِنُونَ بِهِ وَمَنْ يَكْفُرْ بِهِ مِنَ الْأَحْزَابِ فَالنَّارُ مَوْعِدُهُ فَلَا تَكُ فِي مِرْيَةٍ مِنْهُ إِنَّهُ الْحَقُّ مِنْ رَبِّكَ وَلَكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يُؤْمِنُونَ

Je! Mtu mwenye hoja za wazi kutoka kwa Mola wake, na mwenye shahidi kutoka kwake, na ambaye pia kabla yake ametanguliwa na kitabu cha Musa ambacho ni mwongozo na rehema [ni msema uwongo]. Wale ambao wanatafuta ukweli watamsadiki, lakini yeyote ambaye anakataa kuamini kutoka kwenye vikundi vya wapinzani wake, (huyo yeye) atakabiliwa na adhabu ya moto. Basi usiwe na shaka juu ya hilo, kwani hiyo ndiyo haki [iliyo kujia] kutoka kwa Mola wako. Lakini wengi miongoni mwa watu si wenye kuamini.



Maudhui ya Aya

Ayatullahi Tabatabai katika tafsiri Al-Mizan anachukulia Aya ya Shahidun, kama ni msingi wenye nia ya kudumisha kuimarisha imani ya Mtume (s.a.w.w), na kufanya awe thabiti kiimani bila ya kuyumbayumba katika kushikamana na Kitabu cha wenye Ezi Mungu. Kulingana naye, Aya hii iliteremka kujibu tuhuma za washirikina ambao walimtuhumu bwana Mtume (s.a.w.w), kwa tuhuma uwongo. [2]

Katika tafsiri ya Majma' al-Bayan na Tafsiri Nemooneh, kuna aina mbili za ufafanuzi juu ya Aya hii:

  • Katika tafsiri ya kwanza, kwenye kipengele kisemacho: «أَفَمَنْ کانَ عَلی بَینَةٍ مِنْ رَبِّهِ» "Je, yule aliye na dalili za wazi kutoka kwa Mola wake" kimerudisha na kuhusishwa moja kwa moja na bwana Mtume (s.a.w.w), ambaye unabii wake ulithibitishwa kupitia njia tatu katika Aya hii;
  1. Kupitia Qur'ani, ambayo ni dalili na uthibitisho ulio wazi juu ya utume wake.
  2. Kupitia Vitabu vya mbinguni vya awali, kama vile Taurati ambavyo vimeeleza ishara na sifa zake.
  3. Wafuasi wanye roho ya kujitolea pamoja na waumini waaminifu, kama Ali bin Abi Talib (a.s), ambao ni ishara ya kweli wa mafunzo aliyokuja nayo. [3]
  • Katika baadhi ya tafsiri kipengele hichi kisemacho: «أَفَمَنْ کانَ عَلی بَینَةٍ مِنْ رَبِّهِ», "Je, yule aliye na dalili za wazi kutoka kwa Mola wake", kimerudisha na kuhusishwa na waumini wote ambao wanamwamini bwana Mtume (s.a.w.w), amabo walimwamini bwana Mtume (s.a.w.w), kwa ithibati na ushahidi wa wazi, na kupita dalili kutoka kwenye vitabu vya awali, ambavyo vimeeleza ukweli wa unabii wake, waumini ambao wako mstari wa mbele katika kuifuata Qur'ani. [4]

Imedaiwa ya kwamba; maana ya neno "bayyinah" katika Aya hii iko wazi mno, na uwazi wake sio umeweza kudhihiria mbele ya kila mmoja, bali pia umekuwa ni mwanga unaofichua kila kitu unacho andamana nacho. [5]

Ni Nani Hasa Yule Shahidi Anaye Kusudiwa Katika Aya hii?

Wafasiri na wachambuzi wana maoni tofauti kuhusiana na nani hasa Shahidi anaye kusudiwa katika Aya ya 17 ya Surat Hud. Kulingana na vitabu vingi vya Hadithi [6] na tafsiri za Kishia na Kisunni, ni kwamba; maana ya "Shahidi" anaye kusudiwa katika Aya hii ni Imamu Ali (a.s), ambaye alikuwa ndiye muamini wa kwanza aliye muamini bwana Mtume (s.a.w.w). [7] Hata Imamu Ali (a.s) yeye mwenyewe pia alijitambulisha kama ndiye mfano hai na halisi wa Shahidi aliye tajwa katika Aya hiyo. [8]

Hakim Hisakani katika kitabu chake hawahid al-Tanzil ametaja zaidi ya riwaya 16 za kuthibitisha kuwa Imamu Ali (a.s) ndiye "shahidi" uliokusudiwa katika Aya hiyo; ikiwemo Riwaya kutoka kwa Anas bin Malik aliye nukuu Hadithi isemayo kwamba; ibara isemayo: «اَفَمَنْ کانَ عَلی بَینَة مِنْ رَبِّهِ», inahusiana na Mtume Muhammad (s.a.w.w), na ibara isemayo: «وَیتْلُوُهُ شاهِد مِنْهُ», inahusiana na Ali bin Abi Talib (a.s). [9] Katika maelezo yaliofuatiao katika Hadithi hii imeelezwa ya kwamba; Nafasi ya Ali (a.s) ni sawa na nafasi ya ulimi wa bwana Mtume (s.a.w.w) uliotumwa kuwaelekea na kuwapasulia ukweli watu wa mji wa Makka pale walipovunja ahadi za mikataba yao. [10] Hisakani pia amenukuu Riwaya nyingine kutoka kwa Ibnu Abbas isemayo kuwa: Shahidi aliye kusudiwa katika kipengele cha Aya hii kisemacho: «وَیتْلُوُهُ شاهِد مِنْهُ», ni Imamu Ali (a.s) peke yake. [11]

Pia kuna maoni mengini tofauti miongoni mwa wachambuzi na wafasiri mwingine wa Kiislamu, kuhusiana na mfano hai au mfano halisi wa neno Shahidi katika aya hiyo. Kwa mujibu wa maelezo ya Fadhlu bin Hassan Tabrisi katika kitabu chake Majmau al-Bayani, ni kwamba; Maoni ya Ibn Abbas na Mujahid, ambao ni miongoni mwa wafasiri wa mwanzo kabisa katika Uislamu, ni kwamba: Shahidi aliye kusudiwa katika Aya hii ni Jibril, aliye mteremshia Qur'ani bwana Mtume (s.a.w.w) kwa niaba ya Allah. Katika maoni mengine, imeelezwa ya kwamba; neno "Shahidi" linamaanisha lugha na harakati za bwana Mtume (s.a.w.w) ambazo ndio zana za kuisoma Qur'ani. Baadhi pia wamelitambua neno "bayyinah" lililoko katika ibara ya Aya hii isemayo: «اَفَمَنْ کانَ عَلی بَینَة مِنْ رَبِّهِ», kwa maana ya hoja na ushahidi wa akili, na neno "Shahidi" kwa maana ya Qur'ani. [12]

Mwanazuoni maarufu ajulikanaye kwa jina la Tabatabai, amepingana na maoni kama hayo, na kwa kurejea kwenye baadhi ya Riwaya, ametoa tafsiri iendayo kinyume na maoni ya wafasiri hawa, yeye ameifasiri ibara isemayo «وَیتْلُوُهُ شاهِد مِنْهُ», kwa maana ya Imamu Ali (a.s). [13]

Ithibati ya Kuthibitisha Uhalali wa Kushika na Nafasi ya Uongozi Ukhalifa wa Imamu Ali (a.s)

Aya hii imetumika kama ni ithibati na ushahidi wa kuthibitisha haki ya kusika nafasi ya utawala na ukhalifa kwa Imamu Ali (a.s). Kwa mujibu wa mani ya baadhi ya watafiti, neno yatluhu (وَیتْلُوُهُ) katika Aya hii linamaanisha utiifu na ufwasi, na halimaanishi kusoma. Hii ni kwa sababu kishazi "yatluhu" na "minhu" katika Aya hii vinarejelea kwenye neno afaman (أفمَن). Kwa hiyo, maana ya minhu (مِنهُ) ni ushahidi unao ashiria kuwepo kwa uhusiano wa asili na wa kiroho baina ya Shahidi (شاهِد) na Mtume (s.a.w.w) na ni kutoka kwenye nafsi yake (Mtume) (s.a.w.w). [15] Pia, kwa kuzingatia kwamba kitenzi cha yatluhu (یَتلوهُ) ambapo ni kitenzi cha zama zilizopo, ambacho ni kitendo endelevu (present continues tense), kinaashiria tende endelevu, hii inatupa hitimisho ya kwamba; utiifu na ufuasi wa Shahidi kwa Mtume wa Allah (s.a.w.w) utakuwa thabiti katika ngazi zote na nyakati zote, na mfano hai pekee wa Shahidi huyu unathibitishwa katika Hadithi na Aya nyingine, kama vile; Aya ya Mubahala, ambayo imeonesha wazi kuwa Imamu Ali (a.s) ndiye Shahidi huyo aliyetajwa katika Aya ya 17 Suratu Hud. [16]

Sababu ya Kurejelea Taurati

Katika Aya hii, Taurati ndio ushahidi pekee uliotajwa kutoka vitabu vilivyo pita. Wafasiri wanaamini kuwamba sababu hasa juu ya hili, inatokana na kule kuenea kwa mawazo ya Wayahudi katika maeneo ambayo Qur'ani ilishuka ndani yake, na kwamba; kwa upande wa Wakristo waliishi katika maeneo ya mbali kabisa kwa wakati huo, kama vile maeneo ya mji wa Sham (Syria) na Yemen. [17] Sababu nyingine ni kwamba sifa za Mtume (s.a.w) zimeelezewa kwa kina zaidi katika Taurati kuliko kwatika Injili. [18]

Vyanzo

  • Ḥaskānī, ʿUbayd Allāh b. ʿAbd Allāh al-. Shawāhid al-tanzīl li-qawāʿid al-tafḍīl. Tehran: Muʾassisa Ṭab' wa Nashr-i Wizārat-i Irshād, 1411 AH.
  • Hilālī, Sulaym b. Qays. Kitāb Sulaym b. Qays al-Hilālī. Qom: Al-Ḥadī, 1405 AH.
  • Ḥillī, al-Ḥasan b. Yūsuf al-. Nahj al-ḥaq. Qom: Muʾassisa Dār al-Hijra, 1407 AH.
  • Ḥuwayzī, ʿAbd ʿAlī b. al-Jumʿa al-. Tafsīr nūr al-thaqalayn. Qom: Muʾassisa Ismā'ilīyān, 1415 AH.
  • Ibn ʿUqda al-Kūfī, Aḥmad b. Muḥammad. Faḍaʾīl Amīr al-Muʾminīn. Qom: Dalīl-i Mā, 1424 AH.
  • Ibn Ḥayyūn al-Tamīmīyy, al-Nuʿmān b. Muḥammad. Daʿāim al-Islām wa dhikr al-ḥalāl wa l-ḥarām fī al-qaḍāyā wa al-aḥkām. 2nd edition. Qom: Muʾassisat Āl al-Bayt, 1385 AH.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmiyya, 1407 AH.
  • Makārim Shīrāzī, Nāṣir. Tafsīr-i nimūna. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmiyya, 1371 Sh.
  • Manṣūrī, Sayyid Muḥammad and Ṣādiqī, Zahrā. Wujūh-i mukhtalif-i adabī dar ʿibārāt-i āghāzīn-i āya-yi 17 Sūra-yi Hūd wa bāztab-i ān dar tafsīr-i ʿibārāt-i shāhid minh, Different literary aspects in the opening phrase of Qur'an 11:17 and its reflection in the interpretation of the phrase "a witness of his own (family). The Journal of Research in Quranic Sciences and Hadith. No 26, 1405 AH.
  • Suyūṭī, ʿAbd al-Raḥmān b. Abī Bakr al-. Al-Durr al-manthūr fī tafsīr bi l-maʾthūr. Qom: Kitābkhāna Āyat Allāh al-Marʿashī Najafī, 1404 AH.
  • Ṭabāṭabāʾī, Mūhammad Ḥusayn al-. Al-Mīzān fī tafsīr al-Qurʾān. Beirut: Muʾassisat al-Aʿlamī li-l-Maṭbūʿāt, 1390 AH.
  • Ṭabrisī, Faḍl b. al-Ḥasan al-. Majmaʿ al-bayān fī tafsīr al-Qurʾān. Tehran: Nāṣir Khusraw, 1372 Sh.