Tilawat al-Qur’an

Kutoka wikishia

Tilawat al-Qur’an au Qiraat al-Qur’an (Kiarabu: تلاوة القرآن، أو قراءة القرآن) ni kusoma Qur’an kwa kuangalizia juu ya msahafu ambapo Mwenyezi Mungu amemsisitizia Mtume (s.a.w.w) na Waislamu wengine kusoma Qur’an. Katika hadithi pia kusoma Qur’an kunaelezwa kuwa kuna thawabu nyingi sana.

Kusoma Qur’an kuna adabu na hukumu zake. Kwa mujibu wa fat’wa za mafakihi ni haramu kwa mwenye janaba au hedhi kusoma Sura za Azaim au aya ambayo ina sijida na itakaposomwa moja kati ya Aya zenye sijida basi ni wajibu kusujudu. Mafakihi wanajadili kuhusiana na Ghina’ (kuimba) katika usomaji wa Qur’an na wana mitazamo tofauti. Baadhi wanasema sio haramu. Kadhalika kuwa na udhu, kuelekera kibla, kutia uturi na kutadabari na kutafakari ni katika mambo yaliyotajwa kuwa ni mustahabu wakati wa kusoma Qur’an. Kusoma Qur’an katika baadhi ya maeneo na katika baadhi ya nyakati kama mwezi wa Ramadhani na huko Makka kumesisitizwa na kutiliwa mkazo zaidi.

Uhakika na utulivu wa moyo, kuwa mbali na wahaka (hofu), kuwa na ufahamu na muono wa mbali, kuimarisha nguvu ya kuhifadhi, kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu, kuongeza imani n.k ni miongoni athari zilizobainishwa zinazopatikana kwa kusoma Qur’an.

Maana na Nafasi ya Tilawa

Kitabu cha juzuu nne kinachotumika katika kufundishia Qur'an shule za msingi nchini Iran

Tilawat al-Qur’an au Qiraat al-Qur’an ni kusoma Qur’an kwa kuangalizia juu ya msahafu. [1] Kwa mujibu wa Abdul Baqi katika kitabu cha Al-Mu’jam al-Mufahras, neno “tilawat” limetumika mara moja tu katika Qur’an, lakini maneno yanayotokana nalo yametumika zaidi ya mara 50 katika Qur’an. [2] Kumetajwa athari zinazopatikana za kusoma Qur’an ambapo miongoni mwazo ni kupata utulivu wa moyo, kuwa mbali na wahaka (hofu na wasiwasi), kuwa na ufahamu na muono wa mbali, kuimarisha nguvu ya kuhifadhi, kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu na kuongeza imani. [3] Kadhalika imekuja katika hadithi: Kusoma Qur’an kwa kuangalia katika msahafu huwa sababu ya kupunguziwa madhambi ya wazazi hata kama ni makafiri. [4]

Katika baadhi ya nchi za Kiislamu, vikao na mikutano rasmi huanza kwa kisomo cha Qur'an. Kabla ya adhana, sauti ya kisomo cha Qur'an hurushwa hewani kupitia vipaza sauti vya misikiti. Pia, hufanyika vikao na darsa za usomaji Qur’an majumbani. [5] Kwa mujibu wa mkuu wa Shirika la Dar al-Qur'an la Iran mwaka wa 1399 Hijiria Shamsia, kulikuwa na vikao 10,000 vya usomaji wa Qur'an majumbani nchini Iran ambavyo vilikuwa amilifu. [16] Kadhalika Wizara ya Elimu na Malezi ya Iran imeweka somo la ufundishaji Qur’an katika ngazi mbalimbali vya masomo mashuleni [7] na kumeanzisha vituo vingi nchini Iran kwa ajili ya kufundishia usomaji wa Qu’ran. [8]

Tofauti ya Tilawa na Qiraa

Katika Qur’an maneno ya qiraa na tilawa yametumika katika kitabu hiki cha Mwenyezi Mungu. [9] Baadhi ya watambuzi wa lugha wanasema kuwa, maneno mawili ya qiraa na tilawa ni visawe (yaani yana maana moja). [10] Baadhi ya wengine wanaamini kuwa, neno tilawa ni maalumu zaidi ya qiraa; kwa maana hii kwamba, kila tilawa bila shaka ni qiraa, lakini sio kila qiraa lazima iwe tilawa. Kwa mtazamo wao ni kwamba, qiraa ambayo ni tilawa ni ile ambayo tu inaambatana na elimu na amali ya qarii. [11] Kwa mtazamo huo na kwa mujibu wa kauli ya baadhi ya waandishi ni kwamba, katika Qur’an kila ambapo makusudio ni kusoma lafudhi za Qur’an hutumiwa neno qiraa na kila mahali ambapo mbali na kusoma lafudhi za Qur’an inakusudiwa pia kuwasomea watu, kutadabari katika Aya zake au tablighi na kueneza Qur’an n.k hutumiwa neno tilawa. [12] Ghairi ya hivyo Qiraa itakuwa imeambatana na qayd (kanuni, sharti) kama ilivyokuja katika Aya ya 106 ya Surat al-Israa: ((وَقُرْآنًا فَرَقْنَاهُ لِتَقْرَأَهُ عَلَى النَّاسِ عَلَىٰ مُكْثٍ وَنَزَّلْنَاهُ تَنْزِيلًا ; Na Qur'ani tumeigawanya sehemu mbali mbali ili uwasomee watu kwa kituo, na tumeiteremsha kidogo kidogo)). [13]

Pia, kwa mujibu wa Raghib Esfahani, qiraa ina maana jumla, lakini tilawa inatumika tu kwa ajili ya kusoma vitabu vya mbinguni. [14] Hata hivyo, Ibn Mandhur amesema kwamba baadhi wanaona matumizi ya tilawa kuwa ya jumla pia. [15]

Maana ya (حق تلاوته) katika Aya ya 121 ya Surat al-Baqarah

Kwa mujibu wa Aya ya 121 ya Surat al-Baqarah Mwenyezi anatambulisha tilawa (usomaji) kuwa ina daraja ambapo daraja ya juu kabisa ni (حق تلاوته). [16]

Aya yenyewe:

((الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَتْلُونَهُ حَقَّ تِلاوَتِهِ أُوْلَئِكَ يُؤْمِنُونَ بِهِ وَمَن يَكْفُرْ بِهِ فَأُولَئِكَ هُمُ الْخَاسِرُونَ ;

Wale tulio wapa Kitabu, wakakisoma kama ipasavyo kusomwa, hao ndio kweli wanakiamini. Na wanao kikataa basi hao ndio wenye kupata hasara)).

Hata hivyo kuna mitazamo tofauti kuhusiana na makusudio ya haqq tilawa. [17] Baadhi wamesema ni kusoma kunakoambatana na unyenyekevu na kujiepusha na kubadilisha na kupotosha Aya. [18] Wengine wameeleza kuwa, Haqq tilawa (kusoma ipasavyo kusomwa) makusudio yake ni kusimama kidogo na kutakafari na kutadabari wakati wa kusoma Aya za peponi na moto na kumuomba Mwenyezi Mungu pepo na kumtaka akuepusha na shari ya moto wa jahanamu. Kundi jingine linasemna makusudio ni kusoma Qur’an kwa tartil yaani kwa kuchunga lafudhi za Qur’an na kutadabari maana zake na kufanyia kazi. [19] tartir inaashiria aina ya usomaji, au mtindo wa usomaji wa Qur’an ambao unaambatana na tadaburi na kutekeleza kanuni za tajwidi, kisimamo, kianzio na kwa kutekeleza hayo usomaji wa kweli wa Qur’an hupatikana na kutimia. [20]

Fadhila za Kusoma Qur’an

Qur'an imemuamrisha Mtume (s.a.w.w) na hadhira yake kuisoma Qur'an. [22] Imenukuliwa kutoka kwa Imamu Swadiq (a.s) kuhusiana na hili: Mwenye kusoma Aya katika maneno ya Mwenyezi Mungu hata kwa macho yake (bila ya kutoa sauti), basi Mwenyezi Mungu atampa thawabu ya kila herufi mema 100, atamfutia dhambi 100, na atamnyanyua juu kwa daraja 100. [23] Imekuja katika hadithi nyingine kwamba, kuna dua iliyojibiwa kwa mtu anayehitimisha Qur’an. [24] Pia, kumenukuliwa fadhila maalumu kwa kusoma baadhi ya sura na Aya. [25] Imamu Swadiq (a.s) amenukuu kutoka kwa Imamu Ali (a.s) ya kwamba amesema: Nyumba ambayo ndani yake inasomwa Qur’an baraka zake zinaongezeka na Malaika watakuwepo ndani yake na mashetani watakaa mbali. [26] Sheikh Kulayni amekusanya hadithi zinazohusiana na fadhila za kusoma Qur’an na akaziweka katika mlango maalumu. [27]

Maagizo ya kusoma Qur’an katika nyakati na sehemu maalumu

Kikao cha kusoma Qur'an katika haram ya Imamu Hussein (Ramadhan 1443 AH )[28].

Kwa mujibu wa riwaya na hadithi zilizpokewa kutoka kwa Maasumina (a.s), kusoma Qur'an katika nyakati na sehemu fulani kuna malipo maalumu. Imamu Sajjad (a.s) aliamrisha usomaji wa Qur’an mwanzo wa siku. [29] Pia, kwa mujibu wa hadithi, kusoma Aya moja ya Qur'an katika mwezi wa Ramadhani ni sawa na kuisoma Qur'an nzima katika miezi mingine. [30] Imepokewa kutoka kwa Imamu Sadiq kwamba, yeyote atakayeimaliza Qur'an Makka hatakufa isipokuwa atamuona Mtume wa Mwenyezi Mungu na mahala pake peponi. [31]

Hukumu za Fikihi za Kusoma Qur’an

Je, ni wajibu kusoma Qur’an kila siku?

Kumebainishwa mitazamo mbalimbali kuhusiana na hukumu ya kusoma Qur’an katika Sala na nje ya Sala:

  • Baadhi wakitegemnea Aya ya 20 katika Surat Muzzammil inayosema: “Basi someni kilicho chepesi katika Qur'ani” wanaona kuwa ni wajibu kusoma Qur’an. [32] Lakini kuhusiana na kuwa wajibu huo utatimia kwa kusoma kwa siku kiwango gani cha Qur’an kuna miatzanmo tofauti katika hili. [33] Baadhi wanasema kuwa, ni wajibu kusoma Aya 50 za Qur’an kila siku (ghairi ya zile mtu azisomazo katika Sala). [34] Hata hivyo, Fadhil Miqdad anasema, kwa mtazamo wa baadhi wajibu huu ni Wajib Kifai. [35]
  • Baadhi wanaona kuwa ni wajibu kusoma Qur’an katika Sala za wajibu tu. Mafakihi kama Khui, [37] Fadhil Miqdad, [38] na Allama Hilli [39] wanaamini kwamba, kwa mujibu wa Aya na hadithi kusoma Qur’an ni wajibu tu katika Sala za kila siku za wajibu. Hata hivyo Muhammad Hassan Najafi, mwandishi wa kitabu cha Jawahir AL-Kalam yeye anaamini kwamba, wajibu wa kusoma Qur’an katika Sala unachukuliwa katika Sunna na hadithi na sio katika Ayah ii. [40] Hadithi zinazohusiana na kiwango cha kusoma Qur’an zimekusanywa katika kitabu cha al-Kafi katika mlango wa: Bab fi kam yuqrau al-Qur’an Wayukhtam” (Mlango wa kiasi gani Qur’an inasomwa na kuhitimishwa). [41]

Kuwa wajibu sijida ya kisomo

Makala Asili: Azaim al-Sujud

Kwa mujibu wa wanazuoni wa fikihi wa madhehebu ya Kishia, baadhi ya Aya za Qur’an zina sijida ya wajibu ambapo kwa kusoma kwazo inapaswa kusujudu sijida ya wajibu. Aya hizo ni Aya ya 15 ya Surat as-Sajdah, Aya ya 37 katika Surat Fussilat, Aya ya 62 katika Surat al-Najm na Aya ya 19 katika Surat al-Alaq. [42] Kadhalika kwa mujibu wa Sahib al-Jawahir kuna Aya zingine 11 ambazo zina sijida ya mustahabu. [43]

Haramu kwa Mwenye Janaba na Hedhi Kusoma Sura za Azaim

Kwa mujibu wa mtazamo wa mafakihi wa Kishia, ni haramu kwa mtu mwenye janaba [44] na mwenye hedhi [45] kusoma sura. Hata hivyo mafakihi wamnaetofautiana kuhusiana na kuwa je ni haramu kusoma Aya tu zenye sijida au ni haramu kusoma Sura kamili yenye Aya hii. [46] Allama Hilli anasema, ni haramu kwa mwenye janaba na hedhi kusoma hata herufi moja ya sura ya sura hizi. [47]

Wajibu wa Kuheshimiwa Qur’an

Kwa mtazamo wa mafakihi ni kuwa, ni wajibu kuheshimiwa Qur’an na ni haramu kuivunjia heshima. Mambo kama: Kusoma kwa nama ambayo hakuendani na hadhi na heshima yake au kusoma kunakoambatana na musiki ni miongoni mwa mifano na vielelezo vinavyotajwa kuwa ni kuvunjia heshima Qur’an Tukufu. [48] Kadhalika imekatazwa katika maandiko ya kidini kuhusu kusoma Qur’an katika maeneo kama bafuni na chooni. [49]

Hukumu ya Kughani na Kuimba Katika Tilawa

Mafakihi wa Kishia wametofautiana kuhusiana na kusoma Qur’an kwa kuimba (ghina). [50] Inaelezwa kuwa, akthari yao wanatambua suala la ghina' na kuimba kiujumla kuwa ni haramu na hukumu hiyo haiondolewi katika kusoma Qur’an kwa hali hii. Mtazamo huu umenasibishwa na mafakihi kama Ibn Idris, Fakhr al-Muhaqqin, Ahmad bin Muhammad Ardabili, Sayyid Jawad Amili, Mulla Ahmad Naraqo na Sheikh Ansari. [51] Kadhalika kujuzisha kusoma Qur’an kwa ghina na kuimba kumenasibishwa na mafakihi kama Kulayni, Sheikh Tusi, Sayyid Abdul A’la Sabzivari, Mullah Ahmad Naraqi katika Mustanad al-Shiah na Muhammad Hadi Tehran ambao kimsimngi hawatambui kuwa ghina’ (kuimba) kiujumla kuwa ni haramu bali wanasema kuwa, itakuwa haramu pale hilo litakapoambatana na haramu. [52]

Adabu za Kusoma Qur’an

Kwa mujibu wa Aya za Qur'an na hadithi za Maasumina (a.s), kusoma Qur'an kuna adabu zake maalumu. Kutia udhu, kuelekea Kibla, kufikiri na kutadabari juu ya aya za Mwenyezi Mungu, [55] kunyamaza na kusikiliza aya zinazosomwa na msomaji (Qarii) wa Qur'ani, [56] kuanza na kuomba kinga kwa Mwenyezi Mungu ( Audhubillah), [57] kusema baadhi ya dhikri wakati wa kusoma baadhi ya Aya za Qur’an na kusoma dua ya kuanza na kuhitimisha Qur’an ni miongoni mwa mambo ya mustahabu ya kusoma Qur’an. [58] Pia, ikhlasi, kujiweka mbali na ria na kujionyesha, unyenyekevu [59] na kufuata yaliyomo katika Aya zinazosomwa [60] ni miongoni mwa adabu zilizoamrishwa na kukokotezwa katika hadithi. [61]

Kwa mujibu wa amri na maagizo ya Mtume (s.a.w.w), Qur'an inapasa kusomwa kwa masikitiko na huzuni ili kuwa na taathira kubwa katika moyo na nafsi ya mwanadamu. [62] Vile vile imeamrishwa kuwa lahani inayotumika katika kusoma Qur'an inapaswa kuwa ya Kiarabu na lahani isiyo ya Kiarabu, haipaswi kutumika kusomea Qur’an. [63]

Mbinu ya Mtume ya Kusoma Qur’an

Imepokewa kutoka kwa Imamu Baqir (a.s) kwamba Mtume (s.a.w.w) alikuwa na sauti nzuri sana katika kusoma Qur'ani, [64] alikuwa akisoma Qur'ani kwa utulivu na taratibu, kiasi kwamba, Ummu Salamah amenukuliwa akisema: Mtume (s.a.w.w) alikuwa akisoma Qur’an kwa uwazi na alikuwa akisoma herufi kwa herufi na Aya kwa Aya kiasi kwamba, ilikuwa ikiwezekana kuhesabu herufi za Aya. [65] Imam Ali (a.s) alitambulisha njia ya kisomo cha Mtume (s.a.w.w) bila ya kukariri sambamba na kuvuta herufi na tartili. [66]

Kusoma Qur’an Katika Msahafu ni Bora au Kusoma Kimoyomoyo?

Kwa mujibu wa baadhi ya riwaya, kusoma Qur'ani kwa kuangalia juu ya Mushaf kuna faida zaidi kuliko kuzisoma Aya kwa moyo na kwa kuhifadhi; Imamu Sadiq (a.s) alisema kuwa sababu ya kauli hii ni kwamba macho yananufaika kwa kutazama maandishi ya Qur'an. [67] Mfasiri wa Kisunni Zarkashi, kwa kuzikosoa na kuzipitia hadithi husika, anaamini kwamba vigezo katika suala hili ni kutadabari na manufaa zaidi ya mtu na mahudhurio yake ya moyo wakati anaposomaAnasoma; kwa hiyo, ikiwa mtu ananufaika zaidi wakati wa kuhifadhi, kusoma kwake kwa hifdhi na kwa moyo kuna fadhila zaidi, ghairi ya hivyo kusoma kwa kuangalia juu ya msahafu ni bora zaidi. [68]

Mbinu za usomaji wa Qur’an

Maulamaa na wanazuoni wa elimu ya Qur’an wamebainisha katika vitabu vyao mbinu an aina mbalimbali za usomaji wa Qur’an. Ugawaji huu umezingatia zaidi kasi, utulivu na mwendo wa taratibu wakati wa kusoma aya za Qur’an:

  1. Tahdir: Aina hii ya usomaji ni kusoma kwa haraka Qur’an na kuhafifisha kanuni zake kwa mfano kusoma kwa ufupi mada (sehemu za kuvutwa) na kusoma kwa sakna sehemu ambazo zina harakah (fat’h, dhamma au kasra) kwa namna ambayo hali hiyo hamtoi Qarii katika mpaka wa tartil. [69] Wakati Qarii (msomaji) anapotaka kuhitimisha Qur’an katika kipindi cha muda mfupi na kusoma Aya nyingi za Qur’an hutumia aina hii ya usomaji. [70]
  2. Tadwir: Kusoma Aya za Qur’an kwa utulivu na taratibu kiasi kwamba, kunaaambata ana kutafakari na kutadabari maana za Aya zake na kuchunga kanuni zote za tajwidi. [71] Aina hii ya usomaji kwa upande wa kasi ipo baina ya usomaji wa Tahqiq na Tahdir. Aina hii ya usomaji ni mashuhuri baina ya watu wa kawaida kwa jina la “Tartil”. [72] Allami anasema katika kitabu chake cha “Pezhoheshi dar ilme tajweed”, aina hii ya usomaji ilikuwa ikitumiwa na viongozi wa usomaji. [73]
  3. Tahqiq: Kuipa haki kila herufi, kutekeleza mada (sehemu za kuvuta na kurefusha), sambamba na kufanya uhakiki, kuzipa harakah (dhamma, kasra na fat’ha) haki yake, ghunnah na kadhakika. Usomaji huu kwa upande wa kasi ni usomaji wa taratibu zaidi wa usomaji Qur’an. Baada ya kupita zama usomaji huo umeondokea kuwa mashuhuri kwa jina la Usomaji wa katika vikao. [74] usomaji huu unafahamika pia kwa jina la tilawat Taghnimi. [75]