Kusoma Qur’an juzuu kwa juzuu

Kutoka wikishia

Kusoma Qur’ani juzuu kwa juzuu kikawaida hufanyika kwa sura ya mjumuiko. Kusoma Qur’ani juzuu kwa juzuu katika mwezi mtukufu wa Ramadhani, vikao vya kuhitimisha Qur’ani na vilevile katika shughuli ya khitma, kurehemu na kuwakumbuka waliotangulia mbele ya haki ni ada iliyozoeleka. Kazi ya kuigawa Qur’ani katika juzuu 30 ilifanyika mwanzoni mwa karne ya kwanza au karne ya pili Hijria.

Ada ya kusoma Qur’ani juzuu kwa juzuu

Katika vikao vya kusoma Qur’ani juzuu kwa juzuu, qarii (msomaji wa Qur’ani) husoma juzuu kadhaa na hadhirina wengine hutegea sikio, wengine husoma kwa kumfuatisha au na wao husoma kwa sauti ya chini na ya kunong’ona. [1] Mtindo huu umeenea sana hasa katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani au katika vikao vya kuhitimisha Qur’ani majumbani. Vilevile katika shughuli za kurehemu na kuwakumbuka waliofariki dunia (mashuhuri kama kusoma hitima), juzuu thelathini hugawiwa watu mbalimbali ili kila mmoja asome juzuu moja au sehemu yake, na kwa utaratibu huo Qur’ani huhitimishwa. [3] Usomaji wa Qur’ani wa namna hii yaani wa juzuu kwa juzuu katika zama hizi unafanyika pia kwa njia ya mawasiliano ya intaneti. [4]

Kuhitimisha Qur’ani

Moja ya mbinu na mtindo wa kuhitimisha Qur’ani ulioenea ni kusoma Qur’ani juzuu kwa juzuu. Katika baadhi ya vikao vinavyofanyika majumbani au misikitini, kila mtu husoma juzuu moja au kadhaa. Kadhalika kwa kusoma juzuu moja kila siku ya mwezi mtukufu wa Ramadhani, mpaka inapofikia mwishoni mwa mwezi mtukufu wa Ramadhani mtu anakuwa amefanikiwa kuhitimisha Qur’ani yote. [6] Mtindo huu unajuliakana kusini mwa Iran kwa jina la mkabala au usomaji wa mkabala. [7] Shughuli ya kusoma Qur’ani juzuu kwa juzuu hufanyika katika mwezi mtukufu wa Ramadhani katika mataifa mbalimbali ya dunia. Hafla kama hizi zinazofanyika katika maeneo ya kidini kama Haram ya Imam Ridha (as) na Haram ya Bibi Fatma Maasuma (as) nchini Iran hurushwa hewani na Shirika la Radio na Utangazji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. [8]

Kuigawa Qur’ani katika juzuu

Kuigawa Qur’ani katika juzuu thelathini kulifanyika katika karne ya kwanza au ya pili Hijria lengo likiwa ni kusahilisha na kurahisisha katika kusoma, kuhifadhi na kubeba Qur;ani tukufu. [9] Kazi ya kuigawa Qur’ani katika juzuu thelathini inanasibishwa na Hajjaj bin Yusuf al-Thaqafi [10] na Ma’mun Abbasi. Hata hivyo Zarkashi, mmoja wa wafasiri wa Qur’ani tukufu wa karne ya 8 Hijria alikuwa akilitambua suala la kuenea ugawaji wa Qur’ani katika juzuu thelathini kwamba, lilianzia mashuleni. [12] Katika baadhi ya mataifa ya Kiislamu huchapishwa juzuu za Qur’ani kwa sura ya kujitegemea na kusambazwa.