Safari ya Kisheria

Kutoka wikishia

Safari ya kisheria Katika Fiqhi ya Kiislamu, inatambuliwa kuwa ni safari ambayo ndani yake msafiri lazima aswali swala zake kwa kupunguza (Swala za rakaa nne aziswali rakaa mbili) na hapaswi kufunga Swaumu. Katika Aya ya 184 ya Surat al-Baqarah hukumu ya swaumu ya msafiri imebainishwa na katika Aya ya 101 ya Surat an-Nisaa hukumu ya Swala ya msafiri imebainishwa na kuwekwa wazi. Katika vitabu vya kutoa ufafanuzi kuhusiana na mas'ala na hukumu mbalimbali, kumebainishwa masharti nane ili safari ya kisheria itimie na kusadikika kuwa ni safari ya kisheria. Miongoni mwazo ni: Masafa ya safari ya msafiri kwa uchache yawe Farsakh za kisheria nane (masafa yawe baina ya kilomita 40 mpaka 45) na masafa yake ya kwenda yasipungue farsakh ya kisheria nne. Moja ya hukumu za safari ni kwamba, mtu ambaye anasafiri kwa ajili ya kwenda kufanya jambo la haramu (safari ya maasi) anapaswa kuswali swala zake kwa kuzikamilisha na kama ni Mwezi wa Ramadhani basi anawajibika kufunga swaumu.

Maana

Safari ya kisheri ni safari ambayo ndani yake swala za rakaa nne zinaswaliwa kwa mtindo wa kupunguza na haijuzu kufunga Swaumu.[1] Kwa mujibu wa hukumu za fikihi, mtu ambaye ameondoka katika mji anaoishi, kisheria na kwa masharti maalumu anahesabiwa kuwa ni "msafiri" na hivyo ana hukumu maalumu.[2]

Masharti ya kuthibiti safari ya kisheria

Katika Fiqhi ya Kiislamu mtu anatambulika kuwa ni msafiri pale anapotimiza masharti manane:

  1. Masafa yake ya kwenda na kurudi kwa uchache yawe Farsakh za Kisheria nane (masafa yawe baina ya kilomita 40 mpaka 45) na masafa yake ya kwenda yasiwe chini ya farsakh nne.
  2. Kuanzia mwanzo wa safari awe na nia ya kukata masafa ya farsakh nane.
  3. Asibadilishe nia yake akiwa njiani.
  4. Asipitie katika Mji Wake au kukusudia kukaa mahali kwa siku kumi.
  5. Asisafiri kwa ajili ya jambo la Haramu.
  6. Asiwe miongoni mwa watu wanaoishi majangwani ambao wanatembea na kuhama hama huku na kule na kila wanapofika mahali kunapatikana maji na chakula kwa ajili yao na mifugo yao, basi hubakia hapo na baada ya muda huhamia sehemuu nyingine.
  7. Safari isiwe ni kazi yake.
  8. Afike katika Hadd Tarakhus (mahali pa ruhusa ya kisheria) yaani afike sehemu ambayo haoni tena kuta za mji wake na hasikii sauti ya Adhana.[3]

Aya za Qur'ani na Hadithi zinazohusu safari ya kisheria

Aya ya 184 ya Surat al-Baqara inahusiana na hukumu ya Saumu safarini. Imekuja katika Aya hii kwamba: "Na atakaye kuwa miongoni mwenu mgonjwa au yumo safarini basi atimize hisabu katika siku nyingine." Baadhi ya wanazuoni wa fikihi wanatumia Aya hii wakiwa na lengo la kubainisha hukumu ya kifikihi ya Saumu ya msafiri.[4] Katika Aya ya 101 ya Surat an-Nisaa pia, limezungumziwa suala la Swala safarini: Na mnaposafiri katika ardhi, sio vibaya kwenu kama mkifupisha swala, ikiwa mnaogopa kuwa wale waliokufuru watawaletea balaa. Imekuja katika baadhi ya vitabu vya fikihi ambapo Aya hii imekuwa ikitumiwa kubainisha hukumu ya kisheria ya Swala safarini.[5] Katika kitabu cha Wasa'il al-Shia katika maudhui ya Swala ya Msafiri kumenukuliwa Hadithi 248 katika mlango wa Hukumu za Swala ya Msafiri.[6] Vilevile kuna hadithi 99 katika maudhui zinazohusiana na swaumu ya msafiri.[7]

Sala ya msafiri

Makala ya asili: Kupunguza Sala

Baadhi ya hukumu za Sala ya msafiri ni kama ifuatavyo:

  • Msafiri anawajibika kuswali kwa kupunguza sala za adhuhuri, alasiri na isha; yaani badala ya kuswali rakaa nne asali rakaa mbili.[8]
  • Wakati msafiri anapofika katika Hadd Tarakhus (mahali pa ruhusa ya kisheria ambapo haoni kuta za mji wala hasikii adhana) anawajibika kuswali Swala zake za rakaa nne kwa sura ya rakaa mbili; yaani atakapokuwa mbali na mji wake kwa namna ambayo haoni tena kuta za mji na wala hawezi kusikia sauti ya adhana katika mji wake.[9]
  • Endapo wakati wa swala utawadia mtu akiwa safirini; lakini kutokana na sababu hii au ile akawa hakuswali, na kabla ya kumalizika wakati wa swala akawa amewasili katika Mji Wake, anawajibika kuswali swala zake kwa kukamilisha (haijuzu kwake kupunguza). Vilevile kama atakuwa hajaanza safari yake ukawadia wakati wa Swala, lakini akawa hakuswali na akaondoka na kwenda safarini, kama wakati wa swala utakuwa bado upo, anapaswa kuswali kwa kupunguza.[10]
  • Kama swala itakuwa ya Kadha, inapaswa kutekelezwa kama ilivyo katika asili ya mazingira yake; kwa maana kwamba, kama alipaswa kuswali kwa kupunguza lakini Swala ikampita basi wakati wa kulipa kadha anapaswa kuswali kwa kupunguza hata kama hatokuwa safarini (wakati wa kulipa kadha hiyo). Na vilevile kama jukumu lake lilikuwa ni kuswali kamili lakini hakuswali na muda wa Swala ukawa umepita, basi wakati wa kulipa kadha anapaswa kuilipa kwa sura ya kukamilisha hata kama atakuwa safarini.[11]
  • Mtu ambaye amesafiri kwa nia ya kwenda kufanya jambo la Haramu kama kuiba, anawajibika kuswali swala zake kwa kukamilisha.[12]

Swaumu ya msafiri

Baadhi ya hukumu za Swaumu ya Msafiri ni:

  • Msafiri ambaye ni wajibu kwake akiwa safarini kuswali swala za rakaa nne kwa kuzipunguza na hivyo kuswali rakaa mbili, haijuzu kwake kufunga swaumu, na msafiri ambaye anaswali kwa kukamilisha kama mtu ambaye safari ni kazi yake au safari yake ni ya maasi, anawajibika afunge akiwa safirini.[13]
  • Mtu aliyefunga kama atasafiri baada ya Adhuhuri, anawajibika kukamilisha swaumu yake. Kama atasafiri kabla ya adhuhuri atakapofika katika Hadd tarakhus, anawajibika kubatilisha swaumu yake.[14]
  • Hakuna tatizo kusafiri katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani; lakini ni Makuruhu kama safari itakuwa ni kwa ajili ya kukwepa kufunga.[15]
  • Kama msafiri atawasili baada ya adhuhuri katika Mji Wake au atafika katika sehemu ambayo amekusudia kubakia hapo siku kumi hapaswi kufunga siku hiyo.[16]
  • Kama msafiri atarejea kabla ya adhuhuri katika mji wake au atafika katika sehemu ambayo amekusudia kubakia hapo siku kumi, kama atakuwa hajafanya jambo linalotengua swaumu, anawajibika kufunga siku hiyo na kama amefanya jambo linalobatilisha swaumu, basi funga ya siku hiyo sio wajibu kwake.[17]

Mtazamo wa Ahlu-Sunnah

Kwa mujibu Sayyied Abdul-Hussein Sharafuddin (1290-1377 H) ni kwamba, wanazuoni wa kifikihi wa Ahlu-Sunnah wanaona kuwa inajuzu kufunga swaumu safarini; yaani Fatuwa yao ni kwamba, inajuzu kwa msafiri kufunga au kutofunga swaumu.[18] Kuhusiana na kuswali swala safarini wametoa hukumu hii hii pia; isipokuwa Hanafia na Ahlu-Kufa (watu wa mji wa Kufa) wao wanaamini kuwa, inalazimu kuswali kwa kupunguza.[19]

Rejea

  1. Insaiklopidia ya Taasisi ya Sheria ya Kiislamu, Farhang Fiqh, 1392, juzuu ya 4, uk.469.
  2. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, juzuu ya 1, uk.683.
  3. Bani Hashemi Khomeini, Maelezo ya Maelezo ya Marejeleo, 1381, Juzuu ya 1, ukurasa wa 683-707.
  4. Kwa mfano, tazama Allameh Hali, Mantehi al-Muttalib, 1412 AH, juzuu ya 9, uk.315; Fazel Kazemi, Masalak Al-Afham hadi Ayat Al-Ahkam, 1365, juzuu ya 1, ukurasa wa 332-332.
  5. Kwa mfano, tazama Mousavi Sabzevari, Mahzb al-Ahkam, 1413 AH, juz.9, uk.309; Sobhani, Al-Ansaf Fi Masala Dam Fiha Al-Khalaf, 1381/1423 AH, Juzuu 1, uk 325.
  6. Har Ameli, zana za Shia, 1409 AH, juzuu ya 8, ukurasa wa 451-539.
  7. Har Ameli, zana za Kishia, 1409 AH, juzuu ya 10, ukurasa wa 173-209.
  8. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masail, 1381, juzuu ya 1, uk.683.
  9. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, juzuu ya 1, uk.707.
  10. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il ya Rejea, 1381, Juzuu ya 1, uk.733.
  11. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il ya Rejea, 1381, Juzuu ya 1, uk.733.
  12. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, Juzuu ya 1, uk.695.
  13. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, Juzuu ya 1, uk.951.
  14. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, Juzuu ya 1, uk.953.
  15. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, Juzuu ya 1, uk.951.
  16. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Masa'il, 1381, Juzuu ya 1, uk.953.
  17. Bani Hashemi Khomeini, Ufafanuzi wa Marejeo, 1381, Juzuu ya 1, uk.994.
  18. Sharaf al-Din, Ensaiklopidia ya Imam Sharaf al-Din, 1431 AH, juzuu ya 4, uk.56.
  19. Sharaf al-Din, Ensaiklopidia ya Imam Sharaf al-Din, 1431 AH, juzuu ya 4, uk.51.

Vyanzo

  • Quran
  • Bani Hashimi Khomeini, Sayyied Mohammad Hassan, Tawdhwih al-masa'l, Qom, Ofisi ya Machapisho ya Kiislamu ya Seminari ya Qom, 1381 Shamsia.
  • Huru a'mili, Muhammad ibn Hassan, wasailu-shia , Uhakiki na marekebisho kikundi cha Utafiti cha Taasisi ya Ahlulbayt, Qom, Taasisi ya ahlulbayt, Toleo la Kwanza, 1409 Qamaria.
  • Sub'hani, Ja'far, Al-inswaf fi masa'il daa'ma fiha al-khilaf, Qom, Taasisi ya Imam Sadiq (a.s), 1381 shamsia/1431 Qamaria.
  • Sharafu-deen, Sayyied Abdul-Hussein, Mawsuat Al-imam Sharafu-deen, Beirut, Darul-Muarikh al-arabi, 1431 Qamaria.
  • Allameh Hily, Hassan ibn Yusuf, Muntaha lil-matulab fi tahqiq al-madh'hab, Mashhad, Majmau al-buhuth al-islamiyah, toleo la kwanza, 1412 Qamaria.
  • Fadhil Jawad Kadhimi, Jawad, Masaa'lik al-ifhami al-ayat al-ahkam, msahihishaji Mohammad Baqir Shareef-zadeh, Tehran, Mortazawi,1365 Shamsia.
  • Taasisi ya maarifa ya kiislam, Farhange ba madh'hab ahlulbayt(a.s), Toleo la Kwanza, 1392 Shamsia.
  • Musawi Sabzewari, Sayyied Abdul-Ali, Mahzab al-ahkam fi bayaan al-halal wa al-haram, Qom, Aprili, 1413 Qamaria.