Teolojia ya Kiislamu

Kutoka wikishia

Makala hii inahusiana na Teolojia ya Kiislamu. Ili kujua kuhusiana na Elimu ya Teolojia kwa mujibu wa madhehebu ya Shia Imamiyyah angalia makala ya Teolojia ya Shia Imamiyyah.

Teolojia ya Kiislamu ni tawi la elimu za Kiislamu ambayo hujadili kuhusiana na misingi ya kiitikadi ya Kiislamu na kuitetea kwa hoja. Pia teolojia ya Kiislamu ina jukumu la kujibu maswali yanayozushwa kuhusu sababu za hukumu za Sharia, mkusanyiko wa mafundisho ya dini na vitendo vya Mwenyezi Mungu katika kutunga sheria. Ili kuthibitisha masuala yake na kuwakinaisha hadhira na mlengwa, mwanateolojia hutumia mbinu mbalimbali kama vile hoja, kutoa mifano na mjadala. Sayansi hii pia imetajwa pia kwa majina kama vile misingi ya dini, elimu ya misingi ya itikadi na fiqh Akbar (Fikihi Kubwa).

Kuhusu historia ya chimbuko la elimu hii imeelezwa kuwa, kulikuwa na mijadala ya kiteolojia tangu mwanzo wa Uislamu, na suala lake la kwanza lilikuwa ni jabr (kulazimishwa) na ikhtiyar (kuachiwa hiari). Majadiliano kama vile sifa za Mwenyezi Mungu, hasa tauhidi na uadilifu wa Mwenyezi Mungu, ubaya na uzuri wa matendo, qadhaa na kadari, Utume, Ufufuo na Uimamu ni miongoni mwa mada na mijadala muhimu katika sayansi au elimu ya teolojia.

Tofauti juu ya masuala ya kiteolojia ndiyo iliyokuwa chimbuko la kuibuka kwa madhehebu mengi ya kiteolojia katika Uislamu. Madhehebu muhimu zaidi zilizotajwa kwa Shia ni Imamiyyah, Zaydiyyah, Ismailiyyah na Kaisaniyyah, na madhehebu za kiteolojia za Sunni zimeorodheshwa kuwa ni Murjiah, Ahl al-Hadith, Ashairah, Maturidiyyah na Wahhabiyyah. Sheikh Mufid (aliyefariki 413 H), Khwaja Nasir al-Din Tusi (aliyefariki 672 Hijiria) na Allamah Hali (aliyefariki 726 Hijiria) ni miongoni mwa wanateolojia mashuhuri wa Imamiyyah. Qadhi Abdul Jabbar Mu'tazili, Abul Hasan Ash'ari, Abu Hamid Ghazali na Fakhr Razi wanahesabiwa kuwa wanateolojia maarufu wa Kisunni.

Vitabu vya Tas’hih al-I’tiqad, Tajrid al-I’tiqad na Kashf al-Murad, ni miongoni mwa vitabu muhimu vya kiteolojia vya Waislamu wa madhehebu ya Shia. Sharh al-Usul al-Khamsah, Sharh al-Maqasid na Sharh al-Mawaqif ni miongoni mwa athari za kiteolojia za Ahlu-Sunna.

Teolojia mpya ni elimu ambayo ina mtazamo tofauti kuhusiana na kuwa moja au kutofautiana kwake na teolojia (ya zamani). Baadhi ya maudhui na mijadala ya teolojia mpya ni: Kutoa maana, chimbuko, lugha ya dini, hitajio la mwanadamu kwa dini, akili na dini, akili na imani, elimu na dini, tajiriba (uzoefu) na dini na wingi wa mielekeo.

Maana na Majina

Teolojia ni mojawapo ya elimu za Kiislamu zinazojadili imani za Kiislamu [1] kwa namna ambayo wahusika wanatoa ufafanuzi, kuzitolea hoja na kuzitetea. [2] Bila shaka, fasili na utoaji maana mwingine wa elimu hii umetolewa ambapo kila mmoja wao anabainisha sifa maalumu ya elimu hii; [3] kama vile, teolojia ni taaluma ya kinadharia inayoweza kutumika kuthibitisha imani za kidini kwa hoja, [4] au ni elimu inayojadili asili, sifa na matendo ya Mwenyezi Mungu. [5]

Zamakhshari ameitambulisha elimu ya teolojia kwamba, ni Fikihi Kubwa. [6] Feydh Kashani amesema katika kitabu cha Mafatih al-Shariah kwamba, kujifunza elimu ya teolojia ni katika utiifu mustahabu wa moyo, ambao faida yake ni kutoa majibu watu wa bidaa na uzushi. [7]

Majina na Sababu Zake

Jina maarufu la elimu hii ni Kalaam yaani "teolojia" na msomi wa elimu hii anaitwa "Motakallim yaani mwanateolojia". [8] Kuhusiana na kwamba, kwa nini elimu hii imeitwa kwa jina la teolojia, kuna sababu mbalimbali zilizobainishwa kuhusiana na hilo ambapo bora kabisa miongoni mwazo [9] ni kwamba, elimu ya teolojia inaimarisha nguvu ya mtu ya mjadala na mdahalo si kitu kingine ghairi ya mazungumzo na majadiliano. [10] Huko nyuma elimu ya teolojia ilikuwa ikitambuliwa pia kwa majina mengine kama: Elimu ya Misingi ya Dini, Elimu ya Misingi ya Itikadi, Fikihi Kubwa, Elimu ya Tawhidi na Elimu ya Dhati na Sifa. [11]

Maudhui, Malengo na Mbinu

Maudhui

Wanateolojia wana mitazamo tofauti kuhusiana na maudhui ya elimu ya teolojia. Baadhi wanaamini kwamba, elimu hii haina maudhui maalumu; [12] lakini wale ambao wanaamini kwamba, elimu ya teolojia ina maudhui kila mmoja wao amebainisha maudhui ya elimu hii. Muhimu zaidi miongoni mwa maudhui hizo ni: [13] Uwepo kama uwepo, [14] maalumati maalum (maarifa ambayo yanatumiwa kwa ajili ya kuthibitisha itikadi za kidini), [15] uwepo wa Mwenyezi Mungu, uwepo wa mumkinat (vinavyowezekana), dhati ya Mwenyezi Mungu na sifa Zake, [16] itikadi za kidini [17] na kadhalika inaelezwa kuwa, mabadiliko na ukamilikaji wa elimu ya teolojia katika kipindi chote cha historia ulipelekea maudhui zake ziwe tofauti kulingana na zama tofauti. [18]

Malengo na Faida

Wanafikra wa Kiislamu wamebainisha malengo ya elimu ya teolojia na miongoni mwayo ni:

1. Kunyambua na kutoa itikadi za Kiislamu (utambuzi wa kidini wa kiuhakiki). [19]

2. Kufafanua maana na masuala ya kiitikadi ya Kiislamu. [20]

3. Kutoa kwa mpangilio mafundisho ya kiitikadi. [21]

4. Kuthibitisha itikadi na mafundisho ya kidini. [22]

5. Kutetea itikadi za kidini mkabala wa mambo yanayoibuliwa kama utatat na ukosoaji dhidi ya itikadi hizi. [23]


Mbinu

Elimu ya teolojia hutumia mbinu mbalimbali katika hoja zake kulingana na malengo yake tofauti, utendaji, masuala na mlengwa. [24] Wamesema kuwa elimu hii inahitaji mbinu ya kutegemewa na yenye kuleta yakini ili kujua imani za kidini na kuzithibitisha; kama njia ya mlinganisho (mfano wa kimantiki); lakini kwa malengo yake mengine, ambayo ni pamoja na kutetea imani za kidini, sambamba na kuongezea mbinu zenye kuleta yakini inawezekana kutumia njia zingine; mbinu kama vile ufananisha na utoaji mifano, hotuba, mjadala na aina ya mbinu za kiakili na nakili na hata mbinu za majaribio na za kihistoria. [25]

Wakati na sababu za kutokea na kuenea kwake

Kuhusu mizizi mikuu ya elimu ya teolojia, Ibn Abi al-Hadid anaamini kwamba elimu ya teolojia na imani, ambayo ni sayansi bora zaidi, ilichukuliwa kutoka katika maneno ya Imam Ali (a.s.). [26] Muhaqqiq Arbili pia ameeleza bayana kwamba, viongozi wa shule za teolojia; Yaani, Ashairah, Mu’tazilah, Shia na Khawariji wote wanajinasibisha na Mtume (saww). [27]

Mtazamo mashuhuri [28] ni kwamba baada ya ushindi wa Kiislamu na kupanuka kwa wigo wa utawala wa Kiislamu, Waislamu walichanganyika na wafuasi wa dini na madhehebu nyinginezo, na hii ilisababisha kuenea kwa itikadi na maoni ya madhehebu na dini tofauti. Kwa hiyo, Waislamu wakiwa na lengo la kutetea itikadi zao za Kiislamu na kutoa majibu kwa ishkali na shubha za kiitiikadi walizokuwa wakielekezewa waliimarisha na kukuza mbinu na mijadala ya kiteolojia na kwa njia hii elimu ya teolojia ikawa imeanzishwa. [29] Kwa mujibu wa mtazamo mwingine, ili kubainisha tarehe ya chimbuko na kuibuka elimu ya teolojia, awali inapaswa kuweka wazi au kufafanua makusudio ya elimu ya teolojia. [30]

Ikiwa makusudio ya elimu ya teolojia ni kuzungumzia imani za kidini, basi tarehe ya asili yake ni sawa na tarehe ya kudhihiri Uislamu; kwa sababu mijadala hii imekuwa ikiendelea katika Qur’ani na hadithi na katika majadiliano ya Mtume (SAW) na waabudu masanamu na watu wa kitabu kuhusu Tauhidi, Utume na Ufufuo. [31]

Lakini kama makusudio ni mijadala ya kiteolojia baina ya Waislamu wenyewe na kuibuka madhehebu ya kidini na kiteolojia, tarehe ya kutokea kwake ni baada ya kufariki dunia Bwana Mtume (saww). Moja ya migogoro muhimu sana wakati huo ilikuwa ni mzozo wa suala la Uimamu, Ukhalifa, Qadha na kadari, sifa za Mwenyezi Mungu, na tukio la Hakamiyat (Hukumu ya Mwenyezi Mungu), na kufuatia hitilafu hizo, yakaja madhehebu ya Qadariyyah, Mushbibah, Khawariji na mengineyo. [32] Na ikiwa makusudio ya teolojia ni kuibuka madhehebu ya kiteolojia yenye kanuni na sheria zilizobainishwa na njia mahususi ya kiteolojia, basi tarehe ya asili yake inarudi nyuma hadi mwanzoni mwa karne ya pili ya Hijria. [33]

Sababu ya kuibuka na kuenea kwake

Kumebainishwa sababu mbalimbali za kuibuka elimu ya teolojia na kuenea kwake baina ya Waislamu na miongoni mwazo ni:

1. Mafundisho ya Qur’ani, hadithi na mahitaji ya watu: Sababu ya kwanza iliyobainishwa ya kuibuka na kujitokeza elimu ya teolojia ni mafuindisho ya Qur’ani, hadithi na hitajio la watu la kufahamu mafundisho hayo. [34] Qur’ani inatoa kipaumbele na uzingatiaji maalumu kwa mafundisho ya kiitikadi na inasema kuwa, ni laxzima kuyaamini hayo. [35] Kwa muktadha huo, wanazuoni na wasomi wa Kiislamu wealianzisha elimu ya teolojia ili kuhakikisha kwamba, watu wanafahamu mafundisho haya. [36]

2. Hitalafu na mizozo ya kisiasa: Sehemu ya mizozo ya kisiasa na kijamii, ilipelekea kustawi na kuimarika mijadala ya kiteolojia na hatua kwa hatua elimu ya teolojia ikaundika; kama mjadala kuhusiana na “Ukhalifa na Uimamu” baada ya kuaga dunia Bwana Mtume (saww), suala la “Imamu na kutenda Dhambi Kubwa” na suala la Hakamiyah (La Hukma Ila Lilahi) lililoletwa na Makhawariji, au kadhia ya “Jabr na Ikhtiyar” iliyoletwa na Bani Umayyah kwa ajili ya kuhalalisha mamlaka na madaraka yao. [37]

3. Kuchanganyika Waislamu na wasiokuwa Waislamu: Wakati Waislamu walipokuwa na maingiliano na wasiokuwa Waislamu kama Wairani, Warumi na Wamisri, kulidhihirika tofauti za kiitikadi za Waislamu na itikadi za mataifa na umma zingine na kukaanza migongano baina yao. Waislamu wakiwa na lengo la kutetea mafundisho yao ya kimsingi ya Uislamu, walikuja na suala la teolojia na wakastawisha na kuimarisha elimu hiyo; na kwa muktadha huo, elimu ya teolojia ikapanuka na kuchukua wigo mpana. [38]

      4. Kuchanganyika na madhehebu zingine: Baada ya kupanuka kwa ardhi za Kiislamu, watu kutoka dini na madhehebu zingine walisilimu na kuingia katika Uislamu. Waliacha kanuni na misingi ambayo, Uislamu ulikuwa unaipinga; lakini kuhusu baadhi ya imani zao - ambazo maoni ya Uislamu juu yao hayakuwa wazi mwanzoni - waliwasilisha tafsiri ya Kiislamu na Qur'ani;

Kwa hiyo, kwa msaada wa mijadala ya kiteolojia, wanazuoni wa Kiislamu walijaribu kufafanua maoni ya Uislamu na kuzuia maoni hayo kuchanganyika na Uislamu. [39]

5. Harakati ya Tarjumi: Kuibuka utaalamu na mpangilio wa baadhi ya masuala ya teolojia ya Kiislamu ni mambo yaliyotokea katika zama za harakati ya tarjumi. Harakati hii ilianza katika nusu ya pili ya karne ya pili ya Hijria (150 H) na kuendelea kwa karne kadhaa. [40]

Hatua za mabadiliko na mageuzi

Hatua mbalimbali zimetajwa kuhusiana mageuzi na mabadiliko ya teolojia ya Kiislamu. Mohammad Taqi Sobhani, mmoja wa watafiti wa historia ya teolojia anaelezea hatua za mabadiliko ya sayansi hii katika hatua nne na kuandika kwamba, katika awamu hii ya upangaji jumla, pia kuna tofauti kati ya madhehebu za Kiislamu:

1- Hatua ya asili na kujitegemea.

2- Hatua ya ushindani na kuchanganyika.

3- Hatua ya kuunganisha na kubadilika.

4- Hatua ya kuhuisha na kujadidisha. [41]

Ugawaji huu ulifanyika kwa kuzingatia mabadilishano ya elimu ya teolojia na elimu za nje hususan falsafa. [42] Kulingana na Mohammad Taqi Sobhani, hatua ya kwanza inarejea nyuma katika karne tano mwanzoni mwa Uislamu na inajumuisha hatua tatu:

a) Kuibuka na kuundika.

b) Kuundika ya teolojia ya kinadharia.

c) Kuandikwa vitabu jumuishi vya teolojia. [43] 

Katika hatua ya pili (hatua ya ushindani na kuchanganyika), wanateolojia walijitokeza kwa moyo mkunjufu kuchukua mafahimu (maana) na mbinu za kifalsafa na wakafanya urekebishaji wa teolojia kwa mujibu wa mafahimu na maana hizi mpya na kwa upande mwingine walisimama wakiwa wakati kabisa na kutetea itikadi za kieteolojia mkabala wa fikra za kifalsafa. Hatua hii ilianza katika karne ya 5 hadi ya 9 Hijria. [44]

Katika hatua ya tatu (hatua ya kuunganisha na mabadiliko, teolojia ya Ahlu-Suna ilipungua sana na kwa Shia ilikuwa ni ya kifalsafa kikamilifu. [45] Hatua ya nne (hatua ya kuhuisha na kujadidisha) ilianza katika karne ya kumi na mbili. Katika hatua hii, wengine walizungumzia udharura wa kuanzisha "teolojia mpya" na juhudi zilifanywa kukuza na kupanua elimu ya teolojia na kujibu maswali mapya. Ili kutambulisha juhudi hizi, maneno na isilahi kama vile "Umu’tazilah mpya", "Uash’ari" au "muelekeo wa usalafi mpya" yametumika. Katika ulimwengu wa Ushia, pamoja na kufufua fikra ya Sadra'i (Mulla Sadra) katika elimu ya teolojia, wakati mwingine hiyo inafahamika kwa jina la falsafa ya "Sadrai Mpya", tunashuhudia uhuishaji wa shule ya kiteolojia ya baadaye, kama vile Allamah Hilli miongoni mwa mafakihi na uhuishain wa shule ya kifikra ya Kufa na Qum ambayo aghalabu inafahamika kwa jina la "shule ya tafkik” yaani kujitenga". [46]


Mipaka ya Teolojia na Mijadala Yake Muhimu

Masuala ya teolojia hayakomei kwenye misingi ya dini au misingi ya itikadi (imani), bali mwanateolojia ana wajibu wa kujibu matatizo yoyote yanayoibuliwa dhidi ya majimui ya mafundisho na hukumu za kidini; kwa hiyo, teolojia ina wajibu wa kutetea kanuni za dini na matawi yake yote ya dini [47

Kwa mfano, jawabu la swali kuhusu falsafa ya hijabu au kwa nini Qur’ani iliteremshwa hatua kwa hatua au jawabu la matatizo yaliyojitokeza kuhusu miujiza ya Qur’ani au ufasaha wake, ni jukumu la elimu ya teolojia; ingawa kupambanua hukumu ya hijabu ni jukumu la elimu ya fiqhi na kubainisha maana na makusudio ya Aya ni jukumu la elimu ya tafsiri. [48]

Inaelezwa kuwa, jambo la kwanza la kiteolojia baina ya Waislamu lilikuwa Jabr wa ikhtiyar (kulazimishwa na kuachiwa khiari). [49] Miongoni mwa mijadala mingine katika elimu ya teolojia ni: Mjadala kuhusu sifa za Mwenyezi Mungu hususan tawhidi (kumpwekesha Mwenyezi Mungu), uadilifu wa Mwenyezi Mungu, ubaya na uzuri wa matendo, qadhaa na kadari, Utume, ufufuo, taklifu (wadhifa wa kisheria) na muujiza. [50]

Teolojia ya Imamiyyah mbali na hayo yaliyotangulia, inajadili na kuzungumzia pia kuthibitisha uwepo wa Mwenyezi Mungu, Umaasumu wa Mtume na Maimamu, Uimamu, kuthibitisha kufufuliwa mwanadamu mwili na roho, uombezi, taqiya, rajaa (kurejea/ ufufuo) na badaa (utokezo). [51]

Tofauti na Uhusiano wa Elimu ya Teolojia na Falsafa

Licha ya kuwa katika elimu zote mbili kunajadiliwa masuala ya kiakili, lakini kuna tofauti muhimu baina yao. Kuhusiana na jambo hili kumesemwa mambo mengi, lakini ibara nyepesi zaidi ambayo inawezekana kuisema ni kwamba, kama kuhusiana na Mungu na ulimwengu ambao sisi pia ni sehemu yake ni jambo ambalo linajadiliwa kwa uhuru na hakuna sharti kwamba matokeo ya majadiliano lazima yakubaliane na moja ya dini na mjadala huo unaitwa falsafa; lakini ikiwa mwanafikra amefungwa na kubanwa na sharti anailinda dini dhidi ya wapinzani na hatoki nje ya utakatifu wa dini katika hoja, mjadala na utafiti huo utakuwa ni elimu ya theolojia. [52] Baadhi ya wasomi na wanafikra wanaamini kuwa, kwa kupanuka na kuchukua wigo mpana mijadala ya kiteolojia mambo mengi ya masuala ya kifalsafa. [53]

Baadhi ya wengine wanaamini kuwa, tofauti ya kimsingi baina ya falsafa na teolojia ni katika misingi yake. Kwa maana hii kwamba, misingi ya falsafa ni ya kiakili, yaani pamoja na kuwa masuala yake ni ya kimantiki, lakini teolojia hata ikiwa ni jambo la kiakili, lakini misingi na inachukua kutoka katika wahyi, na misingi ya kiitikadi; yaani inafanya Wahyi na yanayofungamana nayo kuwa mambo yasiyo na shaka ndani yake na inafanya juhudi za kuyathibitisha.

Lakini falsafa kwa mujibu wa fasili na maana, inachukua misingi yake kutoka katika akili. Hata hivyo hii haina maana kwamba, mwanafalsafa ni mtu asiye na imani. Kimsingi ni kuwa, tofauti kati ya falsafa na teolojia ni kuambatana na ufunuo na katika teolojia na kutofuata ufunuo katika falsafa; lakini kufungamana huku hakuna maana ya itikadi. [54]

Makundi na Kiteolojia ya Kishia

Makusudio ya makundi ya kiteolojia, ni makundi ambayo chimbuko la kuibuka na kujitokeza kwake ni nadharia na maoni mahususi ya kiitikadi na kiteolojia. [55] Tofauti ya kwanza ya kiitikadi, [56] na muhimu zaidi na mzozo mkubwa zaidi wa kidini ilikuwa ni hitilafu za Waislamu kuhusina na mrithi wa Mtume (saww). [57] Hitilafu hizi zilipelekea kutokea madhehebu mawili muhimu ya Kiislamu yaani Shia na Sunni. [58]

Makundi ya Kiteolojia ya Kishia

Makala kuu: Makundi ya Kishia

Makundi mashuhuri na muhimu zaidi ya Kishia ni: Imamiyyah, Zaydiyyah, Ismailiyyah, Kaisaniyyah. [59] Haya yanatambuliwa kama makundi mashuhuri na muhimu zaidi ya Kishia. Kuhusiana na Maghulati ambao wanaamini kwamba, Imamu Ali ni Mungu inapasa kusema kuwa, kundi hili limetambuliwa kuwa limetoka katika Uislamu. [60]

Imamiyyah

Shia Ithnaashariyyah au Mashia wa Maimamu kumi na mbili ndilo kundi kubwa zaidi miongoni mwa makundi ya Kishia. Wao wanaamini kwamba, Imamu Ali ndiye kiongozi na mrithi baada ya Mtume mara tu baada ya kuaga dunia mtukufu huyo na kisha baada yake ni watoto wake wawili Hassan na Hussein na Maimamu wengine tisa kutoka katika kizazi cha Hussein (as). [61] Inaelezwa kuwa, Ushia ulikuweko kuanzia katika zama za Bwana Mtume (saww).

Kutokana na mbinyo wa kipindi cha Bani Umayyah, Imamiyyah ilijitokeza kama kundi lililoshikamana na shule maalum ya baada ya Imam Baqir (a.s.) na Imam Sadiq (a.s.).

Maimamu hawa wawili walipata fursa ya kuanzisha mafundisho ya Shia, yakiwemo mafundisho ya teolojia ya Imamiyyah. Katika kipindi hiicho (karne ya pili ya Hijria), wanateolojia mashuhuri kama vile Hisham bin Hakam, Hisham bin Salim na Mu’min Taq walioandaliwa na kukuzwa. [62]

Imeelezwa katika kutoa wasifu wa Imamiyyah kwamba, teolojia ya Imamiyyah haikubaliani na suala la kukataa kutumia akili kunakofanywa na watu wa hadithi na Mahanbali na wala haiambatani na utumiaji akili uliochupa mipaka wa Mu'utazilah. Pia, haiafikiani na fikra mgando za Ashairah na kupuuza nafasi ya akili katika kugundua itikadi. Vyanzo vya mafundisho ya Imamiyyah ni Qur'an, Sunnah za Mtume, Ahlul-Bayt, na akili. Misingi mitano ya tauhidi, uadilifu, utume, uimamu na ufufuo inatanmbulishwa kama misingi ya kiitikadi ya Imamiyyah. [63]

. Zaydiyyah

Madhehebu ya Zaydiyyah inanasibishwa na Zayd mtoto wa Imam Sajjad (a.s). [64] Kwa mujibu wa misingi ya madhehebu haya ni kwamba, Imam Ali (a.s), Hassan (a.s) na Hussein (a.s) ndio walioteuliwa na Mtume (s.a.w.w). Ghairi ya Maimamu hawa watatu, kila ambaye anatokana na kizazi cha bibi Fatma Zahraa (a.s) na akaanzisha jihadi ya wazi na harakati na mapinduzi dhidi ya dhalimu, akawa ni alimu, msomi, mwenye kuipa mgongo dunia, shujaa na mkarimu basi ni Imam. [65] Kuhusiana na Uimamu wa Abu Bakr na Omar, Shia Zaydiyyah wana misimamo miwili: Baadhi yao wanaamini Uimamu wa wawili hawa na baadhi ya wengi hawakubaliani na Uimamu wao. Mtazamo wa leo wa Mashia Zaydiyyah wa Yemen unakaribiana na mtazamo wa kwanza.

Baadhi ya fikra za kiteolojia za Zaydiyyah ni: Tawhidi kwa maana ya kukataa kumfananisha Mwenyezi Mungu, ahadi na adhabu (waad wa;-waid),kuamrisha mema na kukataza mabaya, mwenye kufanya dhambi kubwa sio muumini na wala sio kafiri bali ni fasiki. [66]

. Ismailiyyah

Ismailiyyah ni kundi miongoni mwa makundi ya Kishia ambalo baada ya Imam Swadiq (a.s) linaamini Uimamu wa mtoto wa wake mkubwa Ismail na baada ya hapo Imam Kadhim (a.s) na hawakubali Maimamu wengine wa Imamiyyah. [67] Ismailiyyah walikuwa wakiamini kwamba, Uimamu una duru na vipindi saba na kila duru huanza kwa Natiq (mtu ambaye hutambulika kama Mtume) ambaye huleta sheria mpya na kila kipindi baada yake Maimamu saba huongoza. Wanaamini kwamba, maandiko ya dini na maarifa ya Kiislamu yana dhahiri na batini. [68]

Makundi ya Kiteolojia ya Ahlu-Sunna

Makala kuu: Murji'ah, watu wa hadithi, Ashairah, Maturidiyyah, Mawahabi na Makhawariji

Murji'ah, watu wa hadithi, Ashairah, Maturidiyyah na Mawahabi ni makundi ya kiteolojia ya Ahlu-Sunna. [69] Kuhusiana na makhawariji ambao waliibuka na kujitokeza [70] baada ya tukio la Muhakkimah (مُحَکِّمة) iliyotokana na kauli yao mbiu isemayo "لا حکم الا لله" (hakuna hukumu yoyote ile halali isipokuwa ya Mwenye Ezi Mungu tu), kauli mbiu ambayo waliitumia katika kupinga suluhu baina ya Imamu Ali (a.s) na Muawiyyah. Inaelezwa kuwa, awali kundi hili lilikuwa kundi la kisiasa lakini baadaye likageuka na kuwa kundi la kiteolojia likiwa na itikadi tofauti na waislamu wengine. Itikadi muhimu ya makhawariji ni kwamba, Muislamu yeyote anayetenda dhambi kubwa ni kafiri. [71]

Katika radiamali ya itikadi za Makhawajiri kulipelekea kuibuka na kujitokeza makundi mawili ya Mur’jiah na Mu’tazilah. Mur’jiah walikuwa wakiamini kwamba, amali njema au dhambi haina taathira yoyote katika imani; lakini Muutazilah walichagua njia ya katikati na kati [72] na kusema: Mwenye kufanya dhambi kubwa sio muumini wala kafiri bali anakuwa baina ya mawili haya. [73] mu’tazilah wanaamini kwamba, haiwezekani kumuona Mwenyezi Mungu kwa macho na katika mjadala wa Jabr na ikhtiyar (kutenzwa nguvu na kuwa na hiari na irada) ni wafuasi wa hiari mutlaki. [74]

Kwa mujibu wa itikadi ya As’hab Hadithi (Watu wa Hadithi) ni kwamba, inapasa kuchukua tu dhahiri ya Qur’ani na hadithi. Wafuasi wa kundi hili walikuwa wakipinga elimu ya teolojia. Shakhsia mashuhuri zaidi wa kundi hili ni Ahmad bin hanbal. [75] Ahlul-Hadith wanaamini, inawezekana kumuona Mwenyezi Mungu [76] na katika mjadala wa Jabr na ikhtiyar (kutenzwa nguvu na kuwa na hiari na irada) wanakubaliana na nadharia ya jabr (kutenzwa nguvu). [77]

Ashairah wanaitwa watru ambao ni wafuasi wa Abul-Hassan al-Ash’ari (260-324). [78] Ashairah hawafanyii taawili sifa zilizokuja katika maandiko ya kidini kuhusiana na Mwenyezi Mungu kama «یدالله» (mkono wa Mwenyezi Mungu) na «وجه‌الله» (uso wa Mwenyezi Mungu) na wanasema kuwa, Mwenyezi Mungu ana mkono na uso lakini ni kwa namna gani, hilo ni jambo ambalo kweli halieleweki. [79] Kadhalika wao katika mjadala wa Jabr na ikhtiyar wamezungumzia suala la Nadhariat al-Kasb ambayo inajumuisha baina ya jabr na ikhtiyar. [80]

Maturidiyyah ni kundi ambalo liliasisiwa na Abu Mansur al-Maturidi (aliaga dunia 333 Hijria). Kundi hili nalo kama lilivyo Ash’ariyah lilichagua njia baina ya Ahlu al-Hadith na Mu’tazilha. Kundi hili linaona akili ina itibari na inaitumia kwa ajili ya kugundua na kupata Misingi ya Itikadi. Madhehebu haya yanakubaliana na suala la uzuri na ubaya wa matendo, wanaona pia kuwa, irada ya mwanadamu ina nafasi katika kufanya mambo kama ambavo wanaamini kwamba, Mwenyezi Mungu anaweza kuonekana. [81]

Uwahabi ni kundi lililoanzishwa na Muhammad bin Abdul-Wahab (aliaga dunia 1206 Hijria). Mawahabi wanawatuhumu Waislamu wengine kuwa wanamshirikisha Mwenyezi Mungu katika ibada na kufanya mambo ya bidaa. [82] Kwa mujibu wa mafundisho ya Kiwahabi, kufanya tawassuli kwa mawalii wa Mwenyezi Mungu na kutaka uombezi kutoka kwao, kufunga safari na kwenda kuzuru kaburi la Mtume (saww) na Ahlul-Bayt (as), kufanya tabarruk, kuomba shifaa kutoka katika athari za Mawalii wa Mwenyezi Mungu, kujengea makaburi, kuyazuru, kujenga msikiti kando ya maakaburio na kufanya nadhiri kwa wafu ni shirki. [83]

Vitabu Muhimu vya Teolojia na Wanateolojia Mashuhuri

Vitabu vya Awail al-Maqalaat, Tas’hih al-I’tiqad, Tajrid al-I’tiqad na Kashf al-Murad ni miongoni mwa vitabu muhimu vya teolojia vya Shia Imamiyah (Shia Ithnaasharia) [84] Sheikh Mufid (336 au 338-413 Hijria), Khwaja Nasser al-Din Tusi (597-672 Hijria) na Allama Hilli (648-726 Hijria) nao ni katika wanateolojia mashuhuri wa Imamiya. [85] Baadhi ya wanateolojia muhimu na vitabu vya teolojia vya Ahlu Sunna pia kwa kuainisha madhehebu yao ya kiteolojia ni kama ifuatavyo:

Mu’tazilah: Qadhi Abdul-Jabbar. Kitabu: Sharh al-Usul al-Khamsah. [86] Ashairah: Abul-Hassan al-Ash’ari. Kitabu: Maqalaat al-Islamiyyin. [87] Qadhi Abu Bakr Baqilani. Kitabu: Tamhid al-Awail. Abu Hamid Ghazali. Kitabu: Al-Iqtisad Fil I’tiqad. Fakhruddin Razi. Kitabu: Al-Muhassal al-Ar’bain fi Usul al-Din. Saad al-Din Taftazani. Kitabu: Sharh al-Maqasid.

Maturidiyyah: Abu Mansur Maturidi. Kitabu: Al-Tawhid. Salafiyyah: Ibn Taymiyyah. Kitabu: Minhaj al-Sunah al-Nabawiiyah. [88]


Teolojia Mpya

Kuhusiana na ni nini teolojia mpya na kwamba, je ina tofauti na teolojia ya kale (teolojia ya Kiislamu) au hapana, kuna nadharia na mitazamo tofauti. Baadhi wanaamini kwamba, teolojia mpya ndio ile ile teolojia ya zamani, kwa tofauti hii kwamba, kumeibuka na kuletwa shubuha na mambo mapya katika elimu hii au kumefanyika mabadiliko katika muundo au maudhui yake; lakini kuna baadhi ambao wanaona kuwa, hizi ni elimu mbili tofauti. [90]

Katika upande mwingine imeelezwa kuwa, kile ambacho katika lugha ya Kifarsi kinaitwa kwa jina la teolojia mpya, aghalabu ndio kilekile ambacho Wamagharibi wanakiita kwa jina la falsafa ya dini. [91] Miongoni mwa mambo ambayo yanazungumziwa na kujadiliwa katika teolojia mpya aghalabu ni: Fasili na maana ya dini, chimbuko la dini, hitajio la mwanadamu kwa dini, mamlaka ya dini, lugha ya dini, akili na dini, akili na imani, elimu na dini, tajiriba ya kidini na mielekeo mingi ya kidini. [92]