Uimamu au Uongozi

Kutoka wikishia

Uimamu (Kiarabu: الإمامة) Ni uongozi wa kidini na kidunia wa jamii ya Kiislamu na unaoshika na kuendeleza nafasi ilioachwa na Mtume (s.a.w.w) katika uongozi huo wa mambo ya kidini na kidunia. Mafundisho haya ya kushikamana na imani ya Uimamu, ni sehemu ya imani ya Kiislamu ya madhehebu ya Kishia na ni moja ya tofauti kuu za imani kati ya Waislamu wa Kishia na Sunni. Kuzingatia kwao umuhimu wa suala la Uimamu kumepelekea Waislamu hao wa madhehebu ya Shia kupewa jina la Imamiyyah.

Hakuna tofauti kati ya madhehebu mbali mbali ya Waislamu kuhusu umuhimu na ulazima wa kuwepo Imamu, ila tofauti inakuja katika aina ya Uimamu ndani ya jamii za Kiislamu. Baadhi ya wafuasi wa Asha’ira wanaamini kuwa, suala la Uimamu ni miongoni mwa ya wajibu wa kidini (kisheria), huku baadhi ya Mu’utazila wakisema kwamba; huu ni wajibu wa kiakili na ni jukumu la watu wenyewe kumchagua kiongozi wamtakao. Mashia Imamiyyah wanaamini kuwa; uongozi unafungamana na wajibu wa kiakili na ni lazima kwa Mwenye Ezi Mungu kumchagua (kumteua) kiongozi; maana yake ni kwamba ni jambo la busara kwamba Mwenye Ezi Mungu, kwa mujibu wa hekima yake, amchague kiongozi na kuto fanya hivyo haiendani na hekima na busara zake.

Kwa mtazamo wa Mashia Imamiyyah, Uimamu ni ahadi ya kiungu na Mwenye Ezi Mungu amewapa ahadi hiyo waja wake maalumu. Wao wanachukulia suala la Uimamu kama ni njia endelevu ya ukamilifu wa dini na ni fungamano endelevu la kumwongozo mwanadamu baada ya kuondoka kwa bwana Mtume (s.a.w.w).

Imamiyyah pamoja na baadhi ya madhehebu ya Kiislamu wamezingatia sifa maalumu katika cheo cha Uimamu, zikiwemo; sifa ya kuto tenda dhambi (umaasumu) na ukamilifu katika sifa zote za kibinadamu. Imamiyyah wanaamini kuwa kiongozi (Imamu) ni lazima achaguliwe kulingana na tangazo wazi kabisa kutoka kwa Mwenye zi Mungu mwenyewe, bwana Mtume au kiongozi aliye tangulia kabla yake. Wao wanaamini kuwa Imam Ali (a.s) na Maimamu wengine (a.s) wa Kishia walio fuatia baada yake, walikuwa ni maasumu na ni watu bora zaidi na wenye sifa kamilifu zaidi za kibinadamu ukilinganisha na watu wengine walioishi katika zama zao, hivyo basi wao ndio Maimamu na viongozi wa umma.

Uongozi wa kisiasa wa jamii ya Kiislamu, kutekeleza na kusimamia sharia za kimungu, kulinda na kutunza dini na mambo kama hayo, ni miongoni mwa malengo na falsafa ya Uimamu. Imamiyyah, mbali na mambo haya, Mashia Imamiyyah pia wanaamini kwaba; Maimamu ndio rejeleo pekee la kidini na kuwa ni suala hili ni miongoni mwa malengo ya Uimamu.

Nafasi na Umuhimu wa Uimamu

Suala la Uimamu ni moja ya masuala muhimu na lenye tofauti katika jamii ya Kiislamu, ambalo pia limezua mijadala kadhaa miongoni mwa madhehebu ya Kiislamu. [1] Imamiyyah wanachukulia Uimamu kama ni mwendelezo wa unabii wa bwana Mtume Muhammad (s.a.w.w), na ndio sababu inayo hakikisha kuwa Uislamu unaendelea kuwepo na kubaki hai ulimwenguni humu, na kwamba nyadhifa za Imamu ni sawa na nyadhifa za bwana Mtume (s.a.w.w). [2] Imani katika Uimamu, kwa mtazamo wa Imamiyyah, ni sehemu ya msingi ya dini (Usuli al-Ddiin), na kwa sababu hiyo, suala hili linachukuliwa kuwa ni suala la kiitikadi. [3] Hata hivyo, baadhi ya Asha’ira, Mu’tazila, [4] na madhehebu mengine ya Sunni, wameclihukulia suala hili kuwa ni suala linalo fungamana na matawi ya dini au kwa lugha nyengine ni suala la kifiqhi. [5]

Muhammad Hussein Kashif al-Ghita katika kitabu Aslu al-Shi’a wa Usuulihaa ameichukulia imani katika Uimamu kuwa ni moja ya misingi inayotofautisha Shia na madhehebu mengine ya Kiislamu. [6] Kwa sababu hiyo, wafuasi wanao shikamana ni imami ya Uimamu wa Maimamu kumi na mbiili wanajulikana kama ni Imamiyyah, [7] na yeyote asiyekubaliana na hilo, kiautomatiki huwa yuko nje ya Uishia. [8]

Allama Hilli katika utangulizi wa kitabu Minhaju al-Karamah fi Ma’rifati al-Imamah analichukulia suala la Uimamu kuwa ni moja ya masuala muhimu zaidi, na ni miongoni mwa nguzo za imani ambayo kwa kuielewa na kukubaliana nayo, mtu huweza kupata maisha ya milele Peponi na kuepuka ghadhabu za Mwenyezi Mungu. [9]

Kulayni katika kitabu cha Al-Kafi amenukuu Hadithi kutoka kwa Imamu Ridha (a.s) akielezea umuhimu wa Uimamu. [10] Katika Hadithi hiyo, Uimamu unaelezewa kuwa na sifa kadhaa kama vile; Uimamu ni cheo cha manabii, Uimamu ni urithi wa mawasii (washika na nafasi za Mitume), Uimamu ni uongozi wa kiungu, Uimamu ni urithi wa Mtume, Uimamu ni kushika hatamu za uongozi wa Waislamu, Uiamamu ni kuirekebisha dunia na kuleta heshima kwa waumini, Uimamu ni mizizi wa Uislamu na tawi lake lenye kuunawirisha Uilamu huo. [11]

Uimamu ni Ahadi ya Mungu

Makala Asili: Aya ya Ibtilaa Ibrahim

Kulingana na Aya ya 124 ya Surat al-Baqarah ni kwamba; baada ya Nabii Ibrahim kufikia cheo cha Uimamu, pia aliamua kuomba cheo hicho kwa ajili ya kizazi chake, lakini Mwenye Ezi Mungu akamjibu:

لاینالُ عَهدی الظّالِمینَ
Katu ahadi yangu hawataipata wale wenye kudhulumu. [12]

Wafasiri wengi wamesema kuwa maana ya "ahadi" katika Aya hii ni Uimamu. [13] Kwa hiyo, Imamiyyah wanaamini kuwa Uimamu ni cheo ambacho Mwenye Ezi Mungu huwapa waja wake maalumu aliowachagua. [14]

Uimamu ni Msingi wa Kukamilika kwa Dini

Makala Asili: Aya ya al-Ikmal na Aya ya al-Tabligh

Mashia Imamiyyah wakitegemea Aya ya Ikmal na Aya ya Tabligh na pia Riwaya za Maimamu (a.s) ambazo zimesimuliwa katika kutota kutoa tafsiri na ufafanuzi wa Aya hizi, wameuzingatia Uimamu [15] kuwa ndio sababu ianyo pelekea kukamilika kwa dini hii. [16] Kwa mujibu wao, Aya ya Ikmalu al-Din, ilioshuka siku ya tukio la Ghadir, baada ya Mtume (s.aw.w) kumchagua Imam Ali (a.s), na kumtangaza kama ndiye Imamu na mrithi wake, ni kielelezo kinacho ashiria kukamilika kwa dini tendo hilo la bwana Mtume (s.a.w.w). [17]

Pia, wakirejelea Aya ya Tabligh, wanasema kwamba; Uimamu una hadhi na nafasi nyeti mno, kiasi ya kwamba kama bwabna Mtume (s.a.w.w) asingeuwasilisha na kuutangaza ipaswavyo, basi ingelikuwa ni kana kwamba yeye kamwe hakuwasilisha ujumbe wake aliyo tumwa na Mungu kuuwasilisha, jambao ambaolo lingepelekea juhudi zake kupotea kiholela. [18]

Uimamu ni Sababu ya Wendelevu wa Dini

Makala asili: Aya ya Hadi

Mashia Imamiyyah, wakitegemea Aya ya saba ya Surat al-Raad, pamoja na Hadithi chambuzi kuhusiana na Aya hiyo, [19] wanaamini kuwa Uimamu ni wendelevu wa mwongozo kwa wanadamu baada ya kuondoka kwa bwana Mtume (s.a.w.w). [20] Muhammad bin Jarir Tabari (aliyefariki mwaka 310 Hijria), miongoni mwa wafasiri wa upande wa madhehebu ya Sunni, katika kitabu chake cha tafsiri, amenukuu Hadithi kutoka kwa Ibn Abbas ya kwamba; wakati Aya ya saba ya Surat al-Raad iliteremshwa, bwana Mtume aliuweka mkono wake kwenye kifua chake na akasema: Mimi ndiye mtoaji onyo na tahadhari, kisha akaweka mkono wake begani mwa Imamu Ali (a.s) na kumwambia: Ewe Ali, wewe ni mwongozi (hadi) na baada yangu, walioongoka wataongozwa kupitia kwako wewe.[21]

Ufafanuzi wa Dhana ya Uimamu

kulingana na ufafanuzi wa Mujtahidi Lahiji, ni kwamba maana ya Uimamu inyokubaliwa na wanasomi wote wa Kiislamu,[22] ni Uongozi wa kumwongoza kila mtu katika mambo ya dini na dunia, kwa niaba na kwa urithi wa nafasi ya bwana Mtume (s.a.w.w). [23]

Pia kuna tafsiri nyengene zilizotolewa kuhusiana na maana ya Uimamu. Kwa mfano, Saif al-Din Aamadi (aliyezaliwa mwaka 575 na kufariki 622 Hijria), mmoja wa wanstheolojis wa Kisunni, yeye alitoa ufafanuzi wa Uimamu akisema: Ni kule mmoja kati ya watu kushika nafasi ya bwana Mtume (s.a.w), katika utekelezaji wa sheria na kuhakikisha ulinzi wa jamii, kwa njia ambayo kumfuata yeye huwa ni wajibu kwa umma wote. [24] Mir Sayyid Sharif Jorjani (aliye zaliwa mwaka 740 na kufariki 816 Hijiria), ambaye ni mwanazuoni wa Ash'ari, amekubaliana na ufafanuzi huo katika kitabu chake Sharh al-Mawaqif, hata Taftazani pia (aliye zaliwa mwaka 722 na kufariki 792 Hijiria) ambaye ni mwanafiqhi wa Kiash’ari katika kitabu chake Sharhu al-Maqasid ameonekena kukubaliana na tafsiri hiyo. [25] Pia wanazuoni wamesema kuwa: Uimamu ni unaibu wa kushika nafasi ya bwana Mtume kwa ajili ya kuilinda dini na kushika uongozi wa kisiasa wa jamii. [26]

Kwa mujibu wa maelezo ya Naser Makarim Shirazi ni kwamba; ufafanuzi huu unalingana tu na jukumu dhahiri la uongozi wa kiutawala, ambapo umepewa rangi ya kidini, na kule kuitwa mshika nafasi ya Mtume, na Uimamu kama huo unaweza kutimia kupitia chaguo la wanajamii wenyewe; wakati kwa upande wa Imamiyyah, cheo cha Uimamu ni suala la mamlaka ya Allah na uteuzi uko mokonoi mwa MWenye Ezi Mungu mwenyewe na sio jambo lililoko mikononi mwa watu. [27] Baadhi ya wanazuoni kama vile Qadhi Nurullah Tustari wamelifafanua suala la Uimamu kwamba: Ni cheo cha Kiungu na ni tunuko kutoka kwa Allah mwenyewe, na ni cheo chenye daraja na sifa zote kamilifu isipokuwa unabii tu.[28]

Wajibu wa Kuwa na Imamu na Jinsi ya Kumteua

Hakuna tofauti kati ya Shia na madhehebu mengine ya Kiislamu kuhusiana umuhimu wa Uimamu. [29] Lakini khitilafu za maoni zipo katika aina ya wajibu huo na jinsi ya kumteua Imamu huyo. [30] Ila imesemwa kwamba; baadhi ya wanatheolojia wa Mu’utazila na kundi la Mkhawarij, wanaamini kuwa Uimamu si jambo la wajibu kabisa katika Uislamu. [31] Hata hivyo madhehebu mengine ambayo yanadai kuwa ni wajibu, pia nayo yanatofautiana kimitazamo kuhusu ikiwa je ni wajibu wa kiakili au ni wajibu wa sharia (kifiqhi). [32] Jubaaiyyah (wafuasi wa Abu Ali Jubaiyyah ambaye ni miongoni mwa Mu’tazila wa Basra), Ahlul-Hadith na Asha’ira wanaamini kuwa Uimamu ni wajibu wa kisheria (kifiqhi), na si wajibu wa kiakili. [33] Kwa upande mwingine, baadhi ya Mu’utazila, Maturidiyya na Zaidiyya wanaamini kuwa Uimamu ni wajibu wa kiakili, lakini wanaamini kuwa uteuzi na kumteua Imamu ni jukumu la watu. [34]

Imamiyyah wanashikilia imamu ya kuwa Uimamu ni wajibu wa kiakili, na wanadai kuwa mamlaka na uteuzi wa Imamu ni jukumu la Mwenye Ezi Mungu mwenyewe. [35] Maana ya wajibu katika mjadala huu si wajibu wa kifiki, bali ni wajibu wa kiitikadi ambao unahusiana na suala la kufaa na kutofaa kwa kiakili. Yaani, ni jambo zuri kwa Mwenyezi Mungu, na kwa mujibu wa hekima yake, amteue Imamu na kuacha jambo hilo ni jambo ovu, kwa sababu linapingana na hekima yake. [36]

Uimamu ni Lutfu (Huruma)

Pia tazama: Kanuni ya Lutf

Imamiyyah wametumia kanuni ya lutf (huruma) katika kuhalalisha wajibu Mwenyezi Mungu wa kumteua Imamu kutoka kwake yeye mwenyewe. [37] Kanuni ya lutf inamaanisha kuwa kila kitu ambacho kinasaidia na kuwapelekea watu kumtii Mwenye Ezi Mungu au kuwazuia kutenda dhambi, ni wajibu wa Mwenyezi Mungu kulifanya jambo hilo, na Mwenyezi Mungu bila shaka atalifanya kulingana na hekima zake zilivyo. [38] Kama vile kuweka wajibu wa dini na kutuma Mitume ambao huwafahamisha watu juu ya wajibu wao wa kidini. [39] Kwa mujibu wa kanuni hii, uwepo wa Imamu ni neema na ni huruma ya kiungu, kwa sababu inawafanya waja wawe karibu na utii wa Mwenye Ezi Mungu na kuwa mbali na mambo ambayo Mwenyezi Mungu amekataza. [40] Kwa hiyo, uteuzi na kumteua Imamu ni wajibu wa Mwenyezi Mungu. [41]

Sifa Makhususi za Imamu

Imamu ni yule mtu aliyekuwa na cheo cha Uimamu, [42] mtu ambaye anatakiwa kuwa na sifa zifuatazo:

Isma na Kutotenda Dhambi

Makala Asili: Umaasumu wa Maimamu

Imamiyyah na Ismailiyya wanaamini ya kwamba; Imamu ni lazima awe maasumu (asiye kosea) [43] na ili kuthibitisha hilo, wametoa hoja na mbinu za kimantiki kama vile hoja ya (Umuhali wa Tasalsul); ambayo isemayo hoja kwamba: ni muhali kwa jambo fulani kuegemea kwenye mlolongo usio na mwisho. Pia wao wametumia hoja ulazima wa kuwepo mtu wa kuhifadhi Sharia na kufasiri ibara za sharia hiyo, hoja wajibu wa kumtii Imamu, hoja ya naqdhu al-gharadh (kufeli kwa matakwa ya Mungu), hoja na kuanguka na kushuka hadhi kwa Imamu katika kesi ya kutenda dhambi. [44]

Pia wamesema kwamba; Imamu anapaswa kuwa safi na aliye tkasika kutokana na kasoro zote za kidhahiri, kama vile; magonjwa ya ngozi, kasoro zinazohusiana na ukoo, kasoro za kujihusisha na kazi za kiholela na kasoro za kujihusisha na mambo yanayo chukiza ambayo yanapelekea watu kukaa mbali naye, jambo ambalo ni kinyume na madhumuni na malengo ya Kiungu. Malengo ambayo yalikuwa ni kuwaita watu katika taa ya Mwenye Ezi Mungu na kujitenga dhambi. [45]

Ubora na Hadhi ya Imamu

Makala Asili: Ubora wa Maimamu

Kwa mtazamo wa Imamiyyah na baadhi ya wafuasi wa madhehebu ya Murjaa, Mu'tazilah, na Zaydiyyah, ni kwamba; Imamu lazima awe mtu wa juu kabisa katika elimu, dini, makarama, ujasiri (ushujaa), na sifa zote kamilifu za kiakili na kimwili, kuliko watu wengine wote wa wakati wake; [46] kwa sababu kwanza, ikiwa Imamu katika uadilifu atakuwa ni sawa na wengine, kumchagua yeye kuwa ni Imamu itakuwa haileti maana, kwa sababu kuchagua kati ya mambo mawili yaliyolingana, bila kuwepo sababu inayopelekea pendekezo hilo, huwa ni sawa na kuto chagua kitu, na jambo halikubaliki si kiakili wala kimantiki, na iwapo yeye atukuwa na daraja ya chini zaidi kuliko wengine, hiyo itakuwa ni kumpendelea mtu duni na kuachana na watu wali bora ambayo kiakili si jambo sahihi. [47] Pili ni kwamba, Aya kama vile Aya ya 35 Surat Yunus na Aya ya 9 Surat Az-Zumar, pia zinaashiria umuhimu wa kumfuata mtu bora na kumtanguliza yeye juu ya mtu duni. [48]

Chaguo la Imamu Kupitia Maandiko

Imamiyyah wanaamini kwamba; Imamu lazima atambuliwe kupitia tamko la wazi na dhahiri (linayojulikana kama "nassun jaliyyun" ambalo ni andiko au tamshi la wazi) kutoka kwa Mungu, Mtume au Imamu wa awali aliye tangulia kabla yake, [49] wao wameelekeza hoja zifuatazo katika imani hii:

  • Moja ya sifa za Imamu ni kuwa ni maasumu na umaasumu wake ni suala la kiroho ambalo haliwezi kueleweka kupitia mtu mwengine yeyote yule isipokuwa Mungu na yule ambaye amemfahamishwa na Mwenye Ezi Mungu juu ya hilo. Kwa hiyo, ni lazima ajulikane kwa watu kupitia tamko la wazi kabisa.[50]
  • Mtume (s.a.w.w) ni mtu ambaye hakuwa akiuacha umma wake bila ya Imamu hata katika uongozi wa mambo madogo madogo ya umma huo, ambapo hata alipoondoka Madina kwa siku moja au mbili, pia alikuwa akimteua mtu mwingine na kumwakilisha kushughulikia masuala ya Waislamu, inawezekanaje basi kwamba yeye apuze maswala muhimu zaidi kama naibu wa kushika nafasi yake baada yake, na awe ameondoka bila kuzingatiwa na hakumteua mtu wa kushika nafasi hiyo? Kwa hiyo, kutokana na nyenendo za maishani mwake, inaonekana wazi kuwa yeye alimtambulisha Imamu yeye mwenyewe, Imamu ambaye atakuja kushika nafsi baada yake, na bila shaka amewajulisha watu juu ya suala hilo kupitia tamko la wazi. [51]
  • Kuna Riwaya kutoka kwa Maimamu maasumu ambazo zinathibitisha umuhimu wa kumtambua Imamu kupitia “nassun” (tamko la wazi). [52]

Bani Abbas na wafuasi wao wamesema kwamba kuthibitishwa kwa Imamu kunaweza kutimia kupitia mambo kadhaa kama vile; “Nassun”, kupitia njia ya urithi au kuwa na uhusiano na Mtume (s.a.w.w). [53] Zaydiyyah wanaamini kwamba ikiwa mtu kutoka kizazi cha Sayyidah Fatima (a.s) atawalingania watu kumfuata na kushikamana naye, kisha akasimama dhidi ya dhulma kwa upanga kwa lengo la kuamrisha mema na kusimamisha sheria za Kiislamu, basi mtu huyo Uimamu wake ni sahihi. Madhehebu mengine ya Waislamu yanaamini kwamba; Imamu anatambuliwa kupitia tamko la wazi au kuteuliwa na wataalamu, wanazuoni, viongozi na wajamii wenyewe. [54]

Falsafa ya Uimamu

Kuna mitazamo mbalimbali iliyotolewa kuhusu falsafa ya Uimamu na lengo lake; Mu'tazila wanaamini kuwa lengo la Uimamu ni kutekeleza masuala ya sheria za mahaka ya kidini na kuhakikisha adhabu za mahakama hiyo zinatendeka katika jamii, na la pili ni kutekeleza amri za Mungu na mambo mengine kama hayo. [56] Maaturidiyya na Ash'ariyya, pamoja na mambo haya, wanamchukulia Imamu kama ni jemedari mkuu wa jeshi, ambapo miongoni mwa kazi zake ni; ulinzi wa mipaka, kuandaa nguvu za kijeshi, kupambana na wavuruga amani, kuwalinda wanyonge na kuwanyamazisha mizozano, kutatua migogoro na mizozo, kugawanya ngawira na mambo kama hayo ambayo hayako katika jukumu la watu wa kawaida. [57]

Mashia Imamiyyah, mbali na mambo haya, [58] tofauti na madhehebu mengine ya Kiislamu, wao pia waingiza mambo mengine katika mamlaka ya Imamu, ambapo wao waona kuwa miongoni mwa nyadhifa nyeti za Imamu ni kuifasiri dini na sheria pamoja na kushika uongozi wa kidini baada ya Mtume Muhammad (s.a.w.w). [59] Kashfu al-Ghita amesiamisha hoja nyeti katika kuthibitisha na kutetea nadharia ya kwamba; Imamu ndiye mwenye mamalaka ya kubainisha na kuifasiri. Yeye amesimamisha hoja yake kwa kusema kwamba: “Kama ilivyo ni lazima kiakili kwa mwanzilishi na mletaji wa sheria, kuwa na elimu kutoka kwa Mola wake kwa ajili ya kuzifikisha amri za Mungu wake ipaswavyo, basi pia ni muhimu kwa akili kuwepo kwa mtu anayeelezea sheria hizi, na kutokuwepo kwa mojawapo ya hizo mbili na ni lazima kuwepo kwa mfafanuzi wa sharia hizo ambaye pia mwenye elimu kutoka kwa Mola wake, na kuto kuwepo kwake husababisha ujinga wa kuto zielewa amri za Mungu. [60] Pia kuna idadi kubwa ya Aya na Hadithi fumabata (tata zisizowati), ambazo zinahitaji maelezo kutoka kwa mtu ambaye ana maarifa ya kina katika kuelewa maandiko ya Qur'ani na Sunnah. [61]

Moja ya mambo mengine ambayo yanalazimisha ulazima wa kuwepo kwa Uimamu, ambapo pia ni moja wapo ya falsafa ya kuwepo kwa Imamu ni wajibu wa kuhifadhi sheria. [62] Kulingana na hili, uwepo wa Imamu unahakikisha kuwa dini haitobadilishwa au kuwa na upotoshaji; kwa sababu muda unavyozidi kwenda, uwepo wa maadui, uelewa mbaya wa maandiko na mambo mengine yanaweza kuwa na athari kuelewa ufahamu wa mafundisho halisi ya dini ya Mungu. Na pia, kwa kuwa kuna uwezekano wa watu kufahamu kimakosa na kuchukulia vibaya maandiko hayo, kwa hiyo ni wazi kwamba anahitajika mtu ambaye uelewa wake wa Qur'ani hauna makosa, na uwepo wake unakuwa kigezo na kipimo cha kugundua kosa la welewa wa wengine katika kuyafahamu maandiko hayo, na mtu huyo ndiye Imamu na mrithi wa bwana Mtume (s.a.w.w) ambaye ni lazima awe maasumu. [63]

Uimamu wa Imamu Ali (a.s)

Makala Asili: Uongozi wa Imamu Ali (a.s)

Kulingana na mtazamo wa Shia, Imamu Ali (a.s) ni mrithi wa moja kwa moja wa bwana Mtume (s.a.w.w) na ni Imamu baada yake. [64] Mashia wanathibitisha hili kwa kutumia Aya za Qur'ani, kama Aya ya al-Tabligh, Aya ya Wilaya, Aya ya Mawaddah, Aya ya Ulul-Amr, Aya ya al-Ikmal, Aya ya Utakaso (Ayatu Tat-hiir), na Aya ya Waaminifu (Ayatu al-Sadiqiina). [65] Allama Hilli katika kitabu chake Nahj al-Haqq wa Kashfu al-Sidqi amekusanya Aya 84 za kuthibitisha Uimamu wa Imamu Ali (a.s) na ukaimu wake baada ya bwana Mtume (s.a.w.w). [66] Mashia wanamini kwamba; kuna dalili wazi (Nassun jaliyyun) kutoka kwa bwana Mtume (s.a.w.w) juu ya Uimamu na ukaimu wa moja kwamoja wa Imamu Ali baada ya bwana Mtume (s.a.w.w), nao juu ya hilo wanategemea Hadithi zilizosadikishwa kwa njia ya tawatur (kupitia matabaka tofauti ya wapokezi), ambazo zinapatikana katika vyanzo vyao vya Hadithi na na pia katika vyanzo halali vya Ahlu al-Sunnah. Miongoni mwa Hadithi hizo ni kama vile; Hadithi ya Ghadir, Hadithi ya Manzala, na Hadithi ya Thaqalaini. [67]

Imamiyyah pia wanategemea baadhi ya hadithi za kihistoria na ushahidi kuamini kwamba Imamu Ali alikuwa mbora wa watu baada ya Mtume katika elimu, ujasiri, uadilifu na fadhila nyingine za kibinadamu, na kwa hivyo yeye pekee miongoni mwa masahaba alikuwa na haki ya kurithi uongozi wa Mtume. [68]

Uimamu wa Maimamu Wengine

Makala Asili: Uimamu wa Maimamu wa Kishia

Kwa mujibu wa maoni ya Shia Imamiyyah ni kwamba; nafasi ya uongozi wa Imamu baada ya Imam Ali (a.s.) ni haki ya Imamu Hassan (a.s), kisha Imamu Hussein (a.s), na baada yake, wanafuatia watoto tisa wa Imamu Hussein (a.s), yaani Imamu Sajjad (a.s), Imamu Baqir (a.s), Imamu Swadiq (a.s), Imamu Kadhim (a.s.), Imamu Ridha (a.s), Imamu Jawadi (a.s), Imamu Hadi (a.s), Imamu Hassan Askari (a.s), na Imamu Mahdi (a.t.f.s). [69]

Wanazuoni wa Imamiyyah katika kuthibitisha wajibu wa suala la Uimamu wametumia Hadithi ya Maimamu kumi na wawili iliyoripotiwa kutoka kwa bwana Mtume (s.a.w.w). [70] Pia wao watumia Riwaya nyengine kadhaa zilizothibitishwa kupitia njia ya “tawaatur” (zilizopokewa kupitia njia za wapokezi wa matabaka tofauti), ambazo zinathibitisha uongozi wa kila Imamu kwa njia yake maalum na pekee. [71] Pia, kulingana na imani ya Shia Imamiyyah, umaasumu na uadilifu ni masharti na ni sifa maalumu za Imamu, na kwa mujibu wa baadhi ya Riwaya, pia Maimamu wengine waliofuata baada ya Imamu Ali (a.s) walikuwa ni maasum na ni wabora kielimu, na pia walikuwa na sifa kamilifu zaidi ukulinganisha na watu wengine walioko katika zama zao. [72]

Bibliografia (Orodha ya Seti ya Vitabu)

Baadhi ya kazi zilizoandikwa kuhusu suala la uongozi wa Imam zimeorodheshwa hapa chini:

  • Al-Ifsahu fi al-Imamah kazi iliyoandikwa na Sheikh Mufidu: Mwandishi katika kitabu hichi amejadili masuala kadhaa kama vile; ufafanuzi wa uongozi wa Imamu, umuhimu wa kumjua Imamu, uthibitisho wa Uimamu wa Imam Ali (a.s) na ubora wake mbele ya Mwenye Ezi Mungu na Mtume (s.a.w.w), kukataa madai ya uongozi wa Abu Bakar na kukataa ubora wake, kutokuwepo makubaliano ya umma juu ya uongozi wa Abu Bakar, na masuala kama hayo. [73]
  • Al-Shafi fi al-Imamah kazi iliyoandikwa na Sayyid Murtadha: Kitabu hiki kinajibu shaka na hoja za kitabu "Al-Mughni min al-Hijaaj fi al-Imamah" kilichoandikwa na Qadhi Abdul Jabbar al-Mu'tazili. [74] Kitabu hichi kilipata umaarufu miongoni mwa wanazuoni wa Shia na Sunni, ambapo kazi kadhaa zingine ziliandikwa kwa ajili ya kutoa mawazo muhtasari juu ya kitabu hichi, au pia kwa ajili ya kukosoa dhana za kitabu hichi, kama vile Talkhis al-Shafi kilichoandikwa na Sheikh Tusi. [75]
  • Minhaju al-Karamah fi Ma'rifati al-Imamah kazi iliyoandikwa na Allama Hilli: Allama Hilli katika kitabu hichi anaelezea masuala ya jumla kuhusu Uimamu, kama vile maana ya Uimamu na utafiti juu ya ulazima wa kuwepo Uimamu, na kisha anathibitisha Uimamu na ukhalifa wa moja kwa moja wa Imam Ali (a.s) na uongozi wa Maimamu wengine (a.s). [76] Inasemekana kuwa Ibnu Taymiyyah aliandika kitabu "Minhaju al-Sunnah al-Nabawiyyah" kama ni jawabu dhidi ya Allama Hilli. [77] Sayyid Ali Husseini Milani, mtafiti wa elimu ya kalamu na mwalimu katika Hawza ya Qom, aliandika maelezo na ufafanuzi juu ya kitabu hichi cha "Minhaju al-Karamah fi Ma'rifati al-Imamah" na kuyakataa moja kwa maoni ya Ibnu Taymiyyah. Kitabu hichi (cha Sayyid Ali Husseini Milani) kimechapishwa kwa jina "Sharhu Minhaju al-Karamah" katika sehemu tano. [78]
  • Imamat wa Rahbariy kazi ya Ayatullahi Murtadha Mutahhari: Ambao ni mkusanyiko unajumuisha hotuba sita za Mutahhari kuhusiana na uongozi wa Uimamu ambazo zilitolewa katika mwaka 1349 Shamsia katika Jumuiya ya Kiislamu ya Madokta. [79]
  • Al-Imamah al-Udhma 'Inda Ahlu al-Sunnah wa al-Jama'ah ambayo ni kazi iliyoandikwa na Abdullah Damijiy kutoka miongoni mwa wanazuoni wa madhehebu ya Sunni: Mwandishi katika kitabu hichi, baada ya ufafanuzi juu ya Uimamu na utafiti juu ya wajibu na umuhimu wake, anaelezea maoni ya Ahl al-Sunnah kuhusiana na suala la Uimamu. [80]

Masuala Yanayo Fungamana