Hijabu

Kutoka wikishia

Hijabu ni vazi na stara ya mwanamke mbele ya mwanaume asiyekuwa maharimu wake. Mafakihi na Maulamaa wengine wa Kiislamu wanasema kuwa, hijabu ni katika mambo ya wajibu wa wazi na ni dharura katika dharura za dini ya Kiislamu kama ambavyo ni dharura miongoni mwa dharura za madhehebu na kwamba, wajibu na umuhimu wa hijabu umetiliwa mkazo na kusisitizwa katika Aya za Qur’an na hadithi zilizonukuliwa kutoka kwa Maimamu (a.s).

Mafakihi wana ijmaa (kauli moja) kuhusiana na wajibu wa hijabu kwa wanawake mbele wa wasiokuwa maharimu wao. Baadhi ya wahakiki wamebainisha faida za hukumu hii ambapo miongoni mwazo ni: Utulivu wa kinafsi, kuimarika mfungamano wa kifamilia, utulivu wa jamii, thamani na heshima kwa wanawake.

Inaelezwa kuwa, mjadala wa kielimu wa suala la hijabu nchini Iran uliibuka sambamba na kufahamu kuhusu ulimwengu wa kisasa na harakati ya kupigania katiba (Constitutional Revolution). Tukio la agizo la kuondolewa hijabu kimsingi kuliliondoa suala la hijabu kutoka katika kuwa ni kadhia ya kidini na kuwa suala la kisiasa na kiutamaduni na athari nyingi za kielimu kuhusiana na hijabu ziliandikwa katika kipindi hiki.

Baada ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kulizungumziwa suala la hijabu ya lazima na mwaka 1360 Hijiria Shamsia kukapasishwa sheria ambayo kwa mujibu wake, kutovaa hijabu kunahesabiwa kuwa ni uhalifu na kukiuka sheria. Katika kalenda ya Iran tarehe 21 Tir inayosadifiana na harakati ya wananchi wa Mash’had dhidi ya agizo la kuondoa hijabu inafahamika hapa nchini kwa anuani ya “Siku ya Usafi na Hijabu.”

Umuhimu wa hijabu katika utamaduni wa kiislamu

Hijabu na ulazima wa kuvaa na kujistiri mwanamke mbele ya mwanaume ambaye siyo maharimu wake ni miongoni mwa masuala muhimu ya Kiislamu na jambo hilo limebainishwa wazi katika Qur’an Tukufu. [1] Mafakihi wa Kishia wanasema kuwa, hijabu ni miongoni mwa masuala ya wazi na yasiyo na shaka na ya wajibu na zaidi hayo ni katika dharura miongoni mwa dharura za dini ya Uislamu. [2] Nassir Makarim Shirazi anasema, hususan katika zama za sasa watu wote ambao wana mdakhala na maingiliano na Waislamu wamefahamu ya kwamba, moja ya ratiba na mipango ya makundi yote ya Kiislamu ni hijabu ambapo hatua kwa hatua hilo limebadilika na kuwa nara na kaulimbiu na wanafungamana nalo. [3]

Katika Fiqhi kuna milango kama ya talaka [4] na ndoa ambayo mbali na kuzungumzia suala la kumuangalia asiyekuwa maharimu, kadhia ya hijabu pia inajadiliwa. [5] Katika maandiko ya fikihi na hadithi, ili kuashiria maana ya vazi, badala ya neno hijabu lilikuwa linatumika neno la sitr yaani stara [6] na kutumiwa neno la hijabu kwa ajili ya vazi la wanawake ni istilahi ambayo imekuwa ikitumika zaidi katika zama hizi. [7]

Hijabu katika lugha ina maana ya kizuizi, kitu ambacho kinatenganisha vitu viwili kwa kuweko katikati au baina ya vitu hivyo. [8]

Hukumu

Kwa mujibu wa ijmaa (kauli moja) ya mafakihi wa Kiislamu, [9] ni wajibu kwa wanawake kufunika mwili na nywele mbele ya asiyekuwa maharimu. [10] Baadhi ya mafakihi wameitambua hukumu hii kuwa ni katika dharura miongoni mwa dharura za dini na madhehebu. [11] Kuhusiana na mpaka wa uvaaji ambao ni wajibu kwa wanawake, kuna mitazamo miwili jumla; [12]

  1. Wajibu wa kufunika mwili isipokuwa uso (mduara wa uso), na katika mikono kuanzia kifundo cha mkono mpaka mwisho wa vidole: Akthari ya mafakihi mtazamo wao ni huu na maeneo haya mawili hayajumuishwi katika wajibu wa kujistri mwanamke hata hivyo kwa sharti kwamba, kusiwe na uwezekano wa dhambi. [13] Kwa maneno mengine ni kuwa, sio wajibu kwa mwanamke kufunika uso wake na sehemu ya kiganya cha mikono mpaka vidoleni.
  2. Wajibu kufunika mwili wote: Mafakihi kama Fadhil Miqdad [14] na Sayyid Abdul-A’la al-Sabziwari [15] wanaamini kuwa, ni wajibu kwa wanawake kufunika mwili wote hata uso na kiganjaviganja vya mikono. [16] Mar’ash Najafi anasema kuwa, mwanamke anapaswa kufunika uso na mikono kwa tahadhari ya wajibu (ihtiyati wajibu). [17] Sayyid Muhammad Kadhim Tabatabai Yazdi (mwandishi wa kitabu cha Ur’wah) mtazamo wake katika hili ni ihtiyati mustahabu. [18]

Hoja za kisheria za kuwajibishwa hijabu

Baadhi ya hoja ambazo hutumiwa na mafakihi kwa ajili ya kuthibitisha hukumu ya hijabu kuwa wajibu ni:

Qur’an

Makala asili: Aya ya Jilbab na Aya ya Hijabu

Aya za 31 katika surat al-Nur na 59 katika Surat al-Ahzab ndio Aya muhimu zaidi zinazotumiwa na mafakihi wa Kiislamu kama hoja ya kuthibitisha kuwajibishwa hijabu kwa wanawake. [19] Ayatullah Makarim Shirazi anasema, kwa akali kuna Aya 6 miongoni mwa Aya za Qur’an tukufu ambazo zinaashiria wajibu wa hijabu kwa wanawake mbele ya wasiokuwa maharimu wao. [20]

Hadithi

Inaelezwa kuwa, hadithi ambazo zinaashiria wajibu wa wanawake kuvaa hijabu mbele ya wasiokuwa maharimu wao ni mutawatir (zimepokewa kwa wingi). [21] Ayatullah Makarim Shirazi amezigawa hadithi hizo katika makundi saba ambapo baadhi yazo ni kama ifuatavyo:

  1. Hadithi ambazo zimepokewa kwa ajili ya kubainisha sehemu ya Aya ya 31 ya Surat al-Nur ambayo inasema: ((وَلَا یُبْدِینَ زِینَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا ; Wala wasionyeshe uzuri wao isipo kuwa unao dhihirika)). [23] Kwa kuzingtia hadithi hizi, makusudio ya uzuri uliodhihiri katika Ayah ii ni uso na mikono (kuanzia mwanzo wa vidole mpaka katika kifundo cha mkono na ukiacha sehemu hizo mbili, sehemu zingine zilizobakia ni wajibu kwa mwanamke kuzifunika akiwa mbele ya mwanaume ambaye si maharimu wake. [24]
  2. Hadithi zilizokuja kwa ajili ya kubainisha ya Aya ya 60 ya Surat al-Nur na ndani yake imetambuliwa kuwa inajuzu kuondoa jilbab (nguo ambayo ni kubwa zaidi kuliko mtandio (kitambaa cha kichwa) kwa wanawake waliozeeka ambayo kwao wao hakuna tena raghba na maratajio ya kuolewa. [25] Basi ni wajibu kwa wanawake wasiokuwa hao kufunika mwili na nywele zao. [26]
  3. Hadithi ambazo ndani yake imeulizwa hijabu ya makanizi, katika jibu la mipaka ya hijabu yao imebainishwa kuwa, ni huru zaidi. [27] Katika hadithi hizo kumeulizwa kuhusu hijabu ya makanizi jambo ambalo linaonyesha kuwa, asili ya maudhui yaani hijabu ni jambo ambalo uwepo wake hauna shaka. [28]
  4. Hadithi ambazo kwa mujibu wake, mabinti wanapaswa kuvaa hijabu kuanzia umri wa kubaleghe na kuendelea na wajifunike na kujistiri mbele ya wasiokuwa maharimu wao. [29] Katika hadithi hizi suala la ulazima wa kuchunga hijabu kwa wanawake na mabinti limejadiliwa na hii inaonyesha kuwa,asili ya maudhui yaani hijabu ni jambo ambalo uwepo wake hauna shaka. [30]

Falsafa ya hijabu

Shahidi Murtadha Mutahhari na kundi jingine wamebainisha na kueleza hekima za ulazima wa kushikamana na hijabu kisheria. Baadhi yazo ni:

  • Utulivu wa kinafsi: Kutokuweko mipaka ya kisheria baina ya mwanaume na mwanamke na kuweko uhuru usio na mipaka katika maingiliano, huwa sababu ya maingiliano yasiyofaa ambayo huamsha na kuongeza hisia na mihemko ya kijinsia na kutaka kufanya tendo la ndoa kwa ajili ya kiu ya kiroho na hivyo kutofanikiwa kushibisha matamanio yasiyo na mwisho na ambayo kiu yake haikatiki. Kwa upande mwingine, tamaa hizi zisizo na kikomo na zisizoweza kutoshelezwa, daima hazipatikani na haziwezi kumudu aina ya hisia ya kunyimwa, na hii yenyewe husababisha matatizo ya akili na magonjwa ya akili. [31
  • Kuimarika mfungamano wa kifamilia: Kuchunga na kuzingatia wanawake suala la hijabu na kujistiri, huimarisha uhusiano na mfungamano wa kifamilia na kusababisha ukaribu wa uhusiano kati ya mume na mke katika kituo cha familia; kwa sababu kutokana na kujistiri kwa vazi la staha la hijabu, huzuiwa takwa la matamanio ya kijinsi kutoka kwa asiyekuwa mwenza na ladha na starehe za tendo la ndoa hubakia kuwa maalumu katika mazingira ya familia na hii huimarisha uhusiano kati ya mume na mke. [32]
  • Utulivu wa jamii: Kutochunga na kutoheshimiwa suala la mavazi yanayofaa na kuweko uhuru katika mahusiano ya mwanaume na mwanamke katika jamii, ladha za kijinsia zitaondoka katika mazingira ya familia na kuhamia katika anga ya jamii na hili kwa hakika hudhoofisha nguvukazi na harakati katika jamii. [33]
  • Thamani na heshima kwa mwanamke: Kwa mujibu wa Murtadha Mutahhari ni kuwa, kwa mtazamo wa dini, mwanamke kadiri atakavyokuwa mtulivu zaidi, mnyenyekevu zaidi na mwenye staha na usafi zaidi (wa kimaadili na muonekano wake) na asijiweke katika maonyesho na macho ya wanaume, thamani yake pamoja na heshima yake huongezeka. [34] Makarim Shirazi anasema kuwa, kutojistiri na kuvaa ovyo mwanamke pasi na kujistiri kwa vazi la staha la hijabu hushusha shakhsia yake na kwamba, wakati jamii inapomtaka mwanamke ambaye maungo yake hayajasitiriwa, ni jambo la kawaida siku baada ya siku kutaongerzeka matakwa ya kujipamba na kuijionyesha zaidi (atatakiwa kufanya hivyo) na katika jamii kama hii, shakhsia ya mwanamke huporomoka na kuwa kama bidhaa isiyo na thamani na thamani za kiutu husahauliwa. [35]

Hijabu katika Iran ya sasa

Kwa mujibu wa Rasul Jafarian, nchini Iran, sambamba na harakati za kupigania katiba na kuukabili ulimwengu mpya, hijabu ikawa suala lenye changamoto; hii ni katika hali ambayo, kabla ya hapo, ilitazamwa tu kwa mtazamo wa sheria na wajibu wa Sheria. [36] Katika takriban miaka 60, hasa kuanzia 1329 hadi 1348 Hijiria Shamsia, kulikuwa na harakati pana za kielimu kuhusu hijabu nchini Iran. Kabla ya hapo, hapakuwa na kitabu cha kujitegemea cha fikihi kuhusu hijabu miongoni mwa wanazuoni wa Shia; [37] lakini katika kipindi hiki, kuliandikwa vitabu vingi zaidi vya kutetea vazi la hijabu. [38]

Reza Shah (mfalme wa wakati huo wa Iran) akiwa ameathiriwa na nchi za Magharibi na matukio yaliyotokea Uturuki, alitoa amri ya kuondoa hijabu na mwaka 1935-6 alitangaza rasmi kama ni sheria (sheria ya marufuku ya hijabu); [39] Hata hivyo kuondoa yeye na baada ya juhudi kubwa za Marajii na wanazuoni wa Iran na Iraq, sheria ya kuvua hijabu ikaondoa katika hali ya kuwa lazima. [40]

Baada ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran, suala la hijabu la lazima liliibuliwa na mjadala kuhusu kujistiri kwa vazi la hijabu wanawake wanaofanya kazi maofisini likajitokeza. [41] Mwaka 1360 Hijiria Shamsia katika kipengee cha 5 cha kifungo cha sheria nambari 180 cha kuajiri nguvukazi katika taasisi na idara za serikali na wizara kutovaa hijabu kukatambuliwa kuwa ni ukiukaji wa sheria. [42] Katika kalenda ya Iran tarehe 21 Tir inayosadifiana na kumbukumbu ya harakati ya wananchi wa Mash’had dhidi ya sheria ya uvuaji hijabu inafahamika hapa nchini kwa anuani ya “Siku ya Usafi na Hijabu”. [43]

Hijabu katika mataifa tofauti ya Kiislamu

Hijabu ina namna mbalimbali katika nchi mbalimbali za Kiislamu [44] Kwa mfano, chador nyeusi (aina ya baibui) ya kawaida hutambulika kama hijabu rasmi nchini Iran. [45] Baadhi ya wanawake nchini Iran pia huvaa chador za Kiarabu au abaya. Hata hivyo aina hii ya vazi la hijabu ni makhsusi zaidi kati ya wanawake wa Kiislamu katika maeneo ya waakazi wenye asili ya Kiarabu. [46] Katika nchi za India na Pakistani, baadhi ya wanawake wa Kiislamu wakiwa na lengo la kuchunga vazi la hijabu huvaa aina ya mavazi ya kijadi na kiasilii yanayoitwa dupatta. [47] Dupatta ni vazi refu ambalo linafika mpaka chini ya miguu na lina kitambaa cha kichwa kikubwa. Vazi hili aghalabu huvaliwa na suruali. [48] Kadhalika kuna vazi lililozoeleka baina ya waislamu nchini Indonesia mbalo linajulikana kwa jina la jilbab. [49]

Nchini Afghanistgan kuna vazi lililozoeleka baina ya wanawake wa kiislamu ambalo linajulikana kwa jina la Burqa’. Burqa’ ni kitambaa ambacho hufunika kichwa mpaka chini ya macho ambapo mbele ya macho huwa na matundu kama wavu au neti nyeusi ambayo kumsaidia kuona mwenye kuvaa. [50] Burqa’a ilizungumziwa kuwa vazi rasmi baina ya wanawake wa Kiafghani katika zama za utawala wa kundi la wanamgambo wa Taliban. [51]

Nchini Lebanon pia na katika mataifa mengine kuna baadhi ya mavazi ambayo huvaliwa na wanawake ambayo kimsingi ni stara na vazi la hijabu. [52]

Vitabu

Kitabu Rasail hijabiyeh, kilichoandikwa na Rasul Ja'afariyan

Kumeandikwa vitabu vingi kuhusiana na maudhui ya hijabu. [53] Baadhi ya vitabu vyenye maudhui hii ni:

Vyanzo

  • Makala hii imetarjumiwa kutoka حجاب Wikishia ya Kifarsi.

Gallery