Usalafi

Kutoka wikishia

Usalafi (Kiarabu: السلفية) au muelekeo wa kisalafi ni fikra ya kijamii na kimadhehebu ambayo ipo baina ya Waislamu wa madhehebu ya Ahlu-Sunna. Wenye fikra hii wanaamini kwamba, utatuzi wa matatizo ya Waislamu ni kufuata njia na mwenendo wa masalafi (Waislamu waliotangulia). Tapo la usalafi likitumia hadithi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) linaamini kuwa, karne tatu za awali za Uislamu ndizo karne bora kabisa za Uislamu na linaamini kwamba, kuna haja ya kurejea fikra watu walioishi katika zama hizi.

Masalafi wanaamini kuwa Qur’an na Sunna za Mtume (s.a.w.w) zina itibari pale tu zitakapofasiriwa na masahaba, tabi’ina na tabi’ina tabi’ina. Wao hawaitambui akili kama ni hoja na wanategemea Aya za Qur’an na hadithi tu katika kufahamu mafundisho ya dini.

Kwa mujibu wa ufahamu wa Usalafi kuhusiana na tawhidi (kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kuamini kwamba, Mungu ni mmoja tu) Waislamu walio wengi ni washirikina. Ibn Taymiyyah, Ibn Qayyim al-Jawziyyah, Muhammad ibn Abdul Wahhab, Muhammad al-Shawkani na Rashid Ridha ni miongoni mwa wasomi na wananadharia muhimu wa pote la usalafi. Harakati mashuhuri zaidi za Kisalafi katika zama hizi ni: Uwahabi, Ikhwan al-Muslimin na Harakati ya Deobandi (Deobandi Movement).

Makundi ya kijihadi na yenye misimamo mikali (ya kufurutu ada) kama Taliban, al-Qaeda na Daesh yameundwa na kuanzishwa kwa mujibu wa itikadi za Kisalafi na yanawatambua akthari ya Waislamu kwamba, ni makafiri na ni wajibu kupigana nao jihadi. Makundi hayo yamewauawa kwa umati Waislamu wengi wa Kisuni na Kishia.

Utambulisho

Salafa ina maana ya kutangulia. [1] Salafiyyah ni kundi linalodai kuwafuata Waislamu waliotangulia. Hata hivyo kuna tofauti za kimitazamo kuhusiana na wanaokusudiwa katika al-Salaf al-Salih (Wema Waliotangulia) ni akina nani hasa. Hata hivyo walio wengi miongoni mwao wanaamini kwamba, makusudio ya “Wema Waliotangulia” (Salaf Salih) ni shakhsia walioishi katika karne tatu za mwanzo za Uislamu (Mtume, masahaba, tabi’ina na tabi’ina tabi’ina). Hoja yao kuhusiana na hili ni “hadithi ya karne za mwanzo” ambayo Mtume amenukuliwa akisema kwamba: “Watu wangu bora kabisa (ni watu) wa karne yangu, kisha watu wanaowafuata na kisha wanaowafuata.” [2] Masalafi wanalitambua kuwa bidaa (uzushi) [3] kila ambalo linakinzana na kupingana na maneno ya masahaba wa Mtume (s.a.w.w).

Sifa za kifikra

Miongoni mwa sifa maalumu za Masalafi ni:

Kutilia mkazo nakili na kudhoofisha akili

Masalafi wanatanguliza nakili (Aya za Qur’an na hadithi) mbele ya akili. Mtazamo wa Ibn Taymiyyah, kiongozi wa Masalafi ni kwamba: Ukiacha Qur’an na Sunna (hadithi) hakuna njia nyingine ya kufahamu mafundisho ya dini kama itikadi na hukumu kupitia kwayo. Anaamini kuwa, hoja za kiakili kwa njia ya kujitegemea hazina itibari na nafasi yake ni kusadikisha tu na kukiri muhtawa wa maandiko ya dini na kuyaimarisha. [4]

Kuangalia mambo kidhahiri

Masalafi wanaangalia Aya za Qur’an kama zilivyo katika dhahiri yake na kwamba, si sahihi kufanya taawili au kufasiri Aya za Qur’ani. Kwa mfano kuhusiana na Aya ya:((الرحمن علی العرش استوی ; Arrahmani, Mwingi wa Rehema, aliye tawala juu ya Kiti cha Enzi)). [5]

Wanaichukulia Aya hiyo kidhahiri kama ilivyo na wanasema kwamba, bila shaka Mwenyezi Mungu ana kiti cha enzi ambacho anakaa juu yake. Kadhalika kuhusiana na Aya ya “Yadullah” wanasema kuwa, Mwenyezi Mungu ana mkono hasa kwa maana ya mkono. [6]

Utakfiri (ukufurushaji)

Miongoni mwa makundi ya Kiislamu ambayo yamekuwa yakikufurishwa na masalafi ni Falasifah, Batiniyah, Ismailiyah, Shia Ithnaashariyah, Qadriyah na Ashairah. [7]

Baadhi ya vitu ambavyo kwa mujibu wa Ibn Taymiyyah vinapelekea ukafiri ni: Kufanya tawasuli, kujifananisha na makafiri, kupinga hadithi mutawatir na kupinga Ij’maa. [8] Baadhi ya makundi mapya ya kisalafi ambayo ni mashuhuri zaidi kwa usalafi-utakfiri, yamepanua zaidi wigo wa maana na misdaqi ya kufru na kupitia kukufurisha watu wanajuzisha operesheni za kijihadi. [9]

Historia

Huko nyuma As’hab al-Hadith walikuwa na mielekeo ya usalafi hata kama hawakuwa wakifahamika kwa jina hili, lakini istilahi ya usalafi ilikuwa imeenea baina yao. [10] Ahmad bin Hambal (aliaga dunia 241), kiongozi wao sambamba na kufuata sunna za Mtume alikuwa akiwalingania watu kuwafuata masahaba wa Mtume (11] au waongofu miongoni mwa masahaba na tabi’ina. [12]

Usalafi katika wafuasi wa Ibn Hambal katika karne zilizofuata kuna wakati uligeuka na kuwa makele makubwa katika jamii. Kwa mfano katika karne ya 4 Hijria Abu Bakr Barbahari, mtoa waadhi wa Kihambali alilikusanya kundi la Mahambali lililokuwa na misimamo ya kufurutu ada katika mji wa Baghdad, Iraq na kuanza kuchukua hatua kama kupingana na kumbukumbu ya Ashura ya Imam Hussein (a.s) na hivyo akawa ameliweka mkabala na Ushia na vilevile kupingana na masuala kama namna ya kuamini sifa za Mwenyezi Mungu akawa ameliweka mkabala na Ahlu-Sunna. [13]

Jina la Usalafi (Salafiyah) lilianza kutumika katika karne ya 8 Hijria kwa makundi yaliyokuwa na muelekeo na usalafi ambapo Ibn Taymiyyah (aliyeaga dunia 728 Hijria) msomi na mwanazuoni wa Kihanbali huko Damascus, aliandika vitabu vingi na hivyo akawa ameeneza fikra na mitazamo ya kisalafi. [14[ Ahmad Paktachi anasema, Ibn Taymiyyah aliandika Minhaj al-Sunna kama jibu kwa Mashia na vitabu vingine kama al-Risalah al-Hamawiyyah akitoa majibu kwa Ashairah na aliandika pia vitabu akitoa majibu kwa makundi ya Kisufi na wafuasi wa Ibn Arabi. Kuamrisha mema na kukataza maovu, kufungua mlango wa jihadi na kupinga taqlid, sambamba na kuwa na mahudhurio amilifu katika uga wa kisiasa na kijamii, ni miongoni mwa mafundisho yake ambayo alikuwa akiyatilia mkazo. [15]

Baada ya Ibn Taymiyyah, Ibn Qayyim al-Jawziyah (aliaga dunia 751 Hijria) anahesabiwa kuwa muenezaji mkuu wa fikra za Ibn Taymiyyah. Baada yake, Ibn Rajab Hambali (aliyeaga dunia795 Hijria) aliendeleza njia hiyo. [16] Miongoni mwa Maulamaa wa Kihambali wa vizazi vya baadaye, muelekeo wa Kisalafi lilikuwa jambo lililokuwa limeenea kwani watu kama Othman bin Qaid (aliaga dunia 1097 Hijria) huko Najd na Muhammad bin Ahmad Saffarini huko Sham walikuwa masalafi. [17]

Makundi muhimu ya kisalafi

Uwahabi, Harakati ya Ikhwanul-Muslimin na Harakati ya Deobandi yanahesabiwa kuwa miongoni mwa makundi na harakati muhimu kabisa za kimadhehebu na kijamii za pote la usalafi:

Uwahabi

Makala asili: Uwahabi

Katika nusu ya pili ya karne ya 12 Hijria, Muhammad Ibn Abdul-Wahhab akiungwa mkono na kupatiwa himaya na Muhammad bin Saud huko nchini Saudi Arabia, alifanikiwa kueneza fikra za Uwahabi katika maeneo mbalimbali ya Bara Arabu. Fikra zake zilikuwa zimesimama juu ya msingi wa fikra za Ibn Taymiyyah. Abdul-Wahhab alikuwa na misimamo mikali kumshinda hata Ibn Taymiyyah. Chini ya jina la chuki dhidi ya ukengeukaji na mambo ya upotofu, Muhammad ibn Abdul-Wahhab alipunguza hadhi ya mafundisho ya dini na akahamasisha na kukusanya kundi kubwa chini ya mwavuli wa jihadi, akaanzisha serikali ya Aal Saud na kutoa pigo kubwa kwa serikali ya utawala wa Othmania. [18]

Kwa mujibu wa mafundisho ya Kiuwahabi, kuzuru makuburi na kujengea makaburi ni haramu na kwamba, kufanya tawassul ni bidaa na kwamba, kufanya hivyo ni shirk. [19] Baada ya Mawahabi kuidhibiti Saudi Arabia walibomoa na kuharibu athari nyingi zilizokuwa zimebakia tangu mwanzoni mwa Uislamu. Kubomoa makaburi ya Baqi'i mwaka 1221 Hijiria na kubomoa Haram ya Imam Hussein (a.s), kuiba dharih (eneo lililojengewa kabiri) na vitu vyake vya thamani, kuua idadi kubwa ya wafanyaziara wa Haram ya Imam Hussein (a.s) na kuwachukua mateka wanawake katika mji wa Karbala mwaka 1216 Hijria ni miongoni mwa vitendo vya kinyama vilivyofanywa na Mawahabi. [20]

Ikhwanul Muslimin

Harakati ya Ikhwanul Muslimin ni kundi la kisalafi ambalo liliasisiwa na Hassan al-Banna nchini Misri. Hassan al-Banna alikuwa akimfuata mpigania mageuzi wa kabla yake yaani Rashid Ridha ambaye kwa upande mmoja alikuwa ameathirika na mitazamo ya kifikra ya Ibn Taymiyyah na Muhammad Abduh aliyekuwa na fikra za kisalafi; [21] na kwa upande mwingine alikuwa ameathirika na Sayyied Jamal al-Ddin al-Asad Abadi aliyekuwa akipigania umoja wa Waislamu. [22]

Mwaka 1928 Hassan al-Banna alipanda mbegu ya awali ya Ikhwan al-Musmin nchini Misri akiwa na vijana sita waliokuwa wafuasi wake. Haukupita muda harakati hii ikaanzisha matawi yake katika miji mbalimbali ya Misri, Palestina, Sudan, Iraq na Syria na yeye akatambulika na wafuasi wake kwamba, kiongozi mkuu. [23]

Miongoni mwa yaliyokuwa malengo muhimu ya Ikhwan al-Muslimin ni kuasisiwa utawala wa Kiislamu, kuleta mageuzi ya kijamii na kupinga ukoloni. [24] Katika vizazi vilivyofuata ndani ya Ikhwan al-Muslimin kuliibuka vikundi vilivyojitenga ambapo kundi la vijana wenye mielekeo ya Kiislamu likipata miongozo ya fikra ya Sayyid Qutb ambaye alikuwa akilitambua suala la kuanzisha mfumo wa Kiislamu kwamba, ni jambo la dharura, liliunda makundi ya jihadi. [25]

Deobandi

Makala asili: Deobandi

Fikra za Kisalafi katika bara Hindi zilianzishwa na kuwekewa jiwe la msingi na Shah Waliullah Dehlavi (1114-1176). [26] Bwana huyu ambaye ana kitabu aliachoandika akimtetea Ibn Taymiyyah na mitazamo yake, [27] ameandika katika kitabu chake hicho kwamba, mambo kama kuzuru makaburi, kufanya tawassul, kuomba, kuweka nadhiri na kula kiapo ni katika madhihirisho ya shirk na kumshirikisha Mwenyezi Mungu. [28]

Baada ya Shah Waliullah Dehlavi, baadhi ya wanafunzi wake, kupitia kwake walianzisha Madrasa ya Deobandi na kueneza fikra zake. Shule hiyo kwa haraka sana ilinawiri na kupata ustawi na kutokana na kuchukua wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ya India na katika mataifa mengine, iligeuka na kuwa shule kubwa kabisa wa kidini nchini India. [29

Baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamuu ya Iran kundi la Deobandiyah (Deobandi) ambalo tangu kale lilikuwa likikabiliana na Ushia, lilianzisha kundi la wanamgambo lililojulikana kwa jina la Sipah-e Sahaba Pakistan lengo likiwa ni kuzuia Masuni wa Pakistan kuingia katika madhehebu ya Shia. [30]

Masalafi wa kijihadi

Kwa mujibu wa itikadi za masalafi wa zama hizi, kumeanzishwa makundi ya kijihadi ambapo baadhi yao yanajulikana kama usalafi mpya. [31] Kwa mujibu wa historia, Abdul-Wahhab alikuwa na machango mkubwa katika kuingiza mafuhumu na maana ya shirk katika fasihi ya kisalafi; hata hivyo, kivitendo masalafi wapya wameondokea kuwa mashuhuri kwa jina la masalafi matakfiri (masalafi wakufurishaji) na hilo limetokana na hatua yao ya kuwagawa watu katika makundi mawili ya wanaompwekesha na wanaomshirikisha Mwenyezi Mungu. [32]

Makundi ya kitakfiri yanawatambua Waislamu wengi kuwa ni makafiri na kwamba, ni wajibu kuwaua na wakitambua kitendo hicho kwamba, ni kufanya jihadi. [33]

Kundi la Taliban

Taliban ni kundi la kisalafi na kijihadi ambalo limechanganya madhehebu ya Deobandi na kabila la Pashto ambapo kipindi fulani huko nyuma lilifanikiwa kutawala nchini Afghanistan. [34] Aidha Agosti 2021, kundi hili lilifanikiwa tena kutwaa madarakani nchini Afghanistan. Kiini asili cha Taliban kilikuwa kikiundwa na mujahidina waliokuwa nchini Afghanistan waliokuwa wakipigana katika vita vya Afghanistan na Umoja wa Kisovieti. [35] Kiongozi wa Taliban alikuwa Mullah Muhammad Omar ambaye ndiye muasisi pia wa kundi hili. Baada ya mji wa Kabul kudhibitiwa na Taliban, Mullah Omar alipewa lakabu ya Amirul-Muuminina. Wafuasi wa kundi la Taliban walikuwa wakimtambua Mullah Omar kama Kahlifa, na wapinzani wake walitambuliwa na kundi hilo kuwa waasi dhidi ya Khalifa na damu yao ni halali kumwagwa. [36]

Taliban wanapinga mambo yote mapya. Kwa mfano awali kundi la Taliban lilipiga marufuku matumizi ya televisheni (runinga) kama ambavyo halikuwa likiruhusu mabinti kwenda shule. [37] Wanamgambo wa Taliban walikuwa wakibomoa maeneo ya kufanya ziara na turathi za kiutamaduni wakitumia nara na kaulimbiu ya kupambana na suala la kuabudu masanamu. [38]

Al-Qaeda

Baada ya Umoja wa Kisoviet kushambulia kijeshi Afghanistan, kundi lenye misimamo mikali la Waarabu, lilielekea huko likitokea katika maeneo tofauti ya dunia kwa shabaha ya kwenda kupigana jihadi. Watu hawa ambao waliondokea kuwa mashuhuri kwa jina la Waafghani Waarabu wakiongozwa na Abdullah Yusuf Azzam ambaye alikuwa na mitazamo ya jihadi ya Ikhwan al-Musmin walijipanga na kuwa na nafasi muhimu katika kuondolewa Warusi huko Afghanistan. [39]

Baada ya vita vya Afghanistan na kuuawa Abdullah Azzam, jukumu la uongozi wa kundi la Taliban lilichukuliwa na Osam bin Laden. Katika miaka iliyofuata, kundi hili lilitekeleza operesheni nyingi za kigaidi katika maeneo tofauti ya dunia ambapo tukio kubwa zaidi ni mashambulio ya Septemba 11, 2001 nchini Marekani. [40]

Kundi la Daesh

Makala asili: Daesh

Daesh ni kifupi cha "al-Dawla al-Islamiyah fil Iraq wa al-Sham". Hili ni kundi la kitakfiri (linalokufurisha Waislamu wengine) ambalo lilijitenga na al-Qaeda. Kundi hili lilianzishwa mwaka 2006 huko Iraq kwa jina la Jama'at al-Tawhid wal-Jihad kwa uongozi wa Abu Mus'ab al-Zarqawi. [41] Kundi hili liliondokea kuwa mashuhuri pia kwa jina la al-Qaeda ya Iraq. Baadaye kundi hili lilidhibiti na kukalia kwa mabavu baadhi ya maeneo ya Iraq na Syria na mwaka 2014 likaunda "Serikali ya Kiislamu katika Iraq na Sham" na kumtangaza Abu Bakr al-Baghdadi kuwa khalifa. [42]

Kundi la kigaidi la Daesh limetenda jinai nyingi na kuwaua watu wengi wasio na hatia. [43] Mauaji ya kikatili yaliyokuwa yakifanywa na kundi la Daesh yalimfanya hata Ayman al-Dhawahir, kiongozi wa al-Qaeda alalamikie mauaji hayo; na alikwenda mbali zaidi pale alipofikia kutangaza kwamba, Daesh haina uhusiano wowote na kundi la al-Qaeda. [44]

Mtazamo wa Usalafi kwa Ushia

Baadhi ya watafiti wanasema kuwa, kwa mtazamo wa historia, pote la usalafi lilitangaza adui yake ndani ya Ahlu-Sunna; hata hivyo masalafi wa Kiwahabi, wao tangu awali walichukua hatua zilizo dhidi ya Mashia ambapo mauaji yao katika maeneo matakatifu ya kufanya ziara (kama Karbala) katika zama za Muhammad Ibn Abdul-Wahhab ni mfano wa wazi wa hilo. Hata hivyo masalafi wasio Mawahabi kama Ikhwan al-Muslimin walikuwa na uhusiano mzuri na Mashia; na hata katika baadhi ya mambo walikuwa wakishirikiana dhidi ya Israel; hata hivyo masalafi wapya, wanawatambua Mashia kwamba, ni watu waliopotea. Wakisisitiza hatari ya Mashia, wamekuwa wakifanya njama za kuwafanya Masuni wote wawe pamoja nao katika harakati na vitendo vyao dhidi ya Mashia. [45]

Bibliografia

Kuanzia katika zama za ibn Taymiyyah hadi sasa, Maulamaa wa Kishia na Kisuni wameandika vitabu mbalimbali kukosoa usalafi. Baadhi ya vitabu hivyo ni:

  • Al-Mawahib al-Ladduniyyah fil Minah al-Muhammadiyyah, mwandishi: Ahmad Ibn Muhammad Qastallani.
  • Al-Sawaiq al-Ilahiyyah fil Radd alaa al-Wahabiyyah, mwandishi: Suleiman Ibn Abdul-Wahhhab (ndugu yake Muhammad ibn Abdul-Wahhab).
  • Manhaj al-Rashad liman arad al-Saddad, mwandishi: Sheikh Ja'afar Kashif al-Ghitaa.
  • Al-Salafiyyah Marhalat Zamaniyyah al-Mubarakah, La Madh'hab Islami, mwandishi: Muhammad Saeed Ramadhan al-Bouti.
  • Kashf al-Irtiyab fi at'bai’ Muhammad ibn Abdul-Wahhab, mwandishi: Sayyied Muhsin Amin
  • Aiin Wahabiyat, mwandishi: Sheikh Ja'afar Sohani.
  • Fitneh Wahabiyat, mwandishi: Ahmad Sayyied Zayni Dahlan.
  • Al-Tuhfat al-Madina fil Aqidat al-Salafiyah, mwandishi: Abdul-Salamaa Abdul-Karim.
  • Vahabiya, maban fikri va karnameh amali, mwandishi: Ja’afar Sobhani.
  • Qiraat fil addilat al-Salafiyah, mwandishi: Marwan Khalifaat.

Vyanzo

  • Abu Zuhrah, Muhammad, Tarikh al-Madzahib al-Islamiyah, Beirut, Dar al-Fikr al-Arabi.
  • Ali Zadeh Musawi, Sayyied Mahdi, Salafigari va Wahhabiyat, Penerbit Awaye Munji, 1393 HS.
  • Alipoor Gorji, Mahmud dan Syadi Sha'bani Kiha. Salafigari az Ma'na ta Bardasyhaye na Duruste Mabani, Di Jurnal Siyasat Pazohi, Musim Panas. 1397 HS.
  • Al-Mash'abi, Abdul Majid bin Salim, Manhaj Ibni Taimiyah fi Mas'alalati al-Takfir, Riyadh, Maktab Adhwa’ al-Salaf, 1418 H.
  • Asahesh Thalab Tusi, Muhamamd Kazhim. "Albanna Hassan" dalam Daniesh Name Jahane Islam, Juz.4, Teheran, Bunyad Dairatu al-Ma’arif Islami. 1377 HS.
  • Farmaniyan, Mahdi, Jeryan Shenasi Fikri-Farhanggi Salafigari Mu'ashir, Qom, Fazuheshgah Ulume Islami Imam Shadiq as. Cet. Kedua. 1396 HS.
  • Farmaniyan, Mahdi, Salafiyeh va Taqrib, Di Majalah Haft Aseman, No. 47, 1389 HS.
  • Farmaniyan, Mahdi, Tarikhe Tafakkure Salafigari, Qom, Penerbitan dar al-I’lam li Madrasah Ahlulbait as. 1394 HS.
  • Firuzabadi, Sayid Hasan. Takfirihaye Daisy ra Behtar beshnasim. Teheran. Daneshgah Ali Milli. 1393 HS.
  • Ibnu Badran Dimasyqi, Abdul Qadir bin Ahmad, Al-Madhal ila Madzhab al-Imam Ahmad bin Hanbal. Riset: Abdullah bin Abdul Muhsin Turki. Beirut. Muassasah al-Risalah. Cet. Kedua. 1401 H/1981.
  • Ibnu Manzhur, Muhammad bin Mukrim, Lisan al-Arab. Beirut, Dar Shadir, Cet. Ketiga, 1414 H.
  • ISIS mengumumkan kekhalifahannya, buletin News, 9 Tir 1393(30 Juni 2014)
  • Karami Charmeh, Kamran, Salafigari va Khawar Miyane Arabi, Teheran, Kantor berita Fars, 1393 HS.
  • Karimi Haji Khadimi, Maziyar, Tabar Shenasi Jeryane Takfiri; Barresi Mauridi unbissye Thaliban dar Afganistan, Di Majalah Muthala’at Bidari Islami. Musim Semi dan Musim Panas. 1395 HS.
  • Mughniyah, Muhammad Jawad, Hadzihi Hiya al-Wahhabiyah. Teheran, Munadzmah al-I’lam al-Islami.
  • Nahlehhaye Fikri Thaliban; Az Deobandiyeh ta Wahhabiyat, Kantor berita Rassa, 15 Mehr 1395 (6 oktober 2016)
  • Paketchi, Ahmad dan Husein Husyanggi, Bunyadgarai va Salafiyeh, Penerbit Universitas Imam Shadiq as. 1393 HS.
  • Poorhasan, Nashir dan Abdul Majid Saifi, Taqabul Neosalafiha ba Syiayan va payomadhae an bar Ittihade Jahane Islam. Syiah Shenasi. No. 52. Musim Dingin. 1394HS.
  • Ridhwani, Ali Asghar. Wahhabiyane Takfiri, Teheran. Penerbit Mas’ar. 1390 HS.
  • Yusufi Ashkawari, Ikhwanul Muslimin, Di Dairatu al-Ma’arif Bozorg Islami, juz. 7, Teheran. Markaz Dairatu al-Ma’arif Bozorg Islami. 1377 HS