Taqiyyah

Kutoka wikishia

Taqiyyah (Kiarabu: التقية) ni mtu kuficha ukweli wa imani yake mbele ya wapinzani ili kujihifadhi katika sehemu za hatari anapohisi kuwa kuna hatari na madhara ya kidini na kidunia au madhara ya nafsi yake au mali yake, kwa sababu ya kutangaza itikadi (imani) yake au kujidhihirisha nayo. Ni maarufu kwa wafuasi wa madhehebu ya Shia Ithnaashariyyah, na Maimamu wao wamepata balaa na kila aina ya dhiki katika katika zama zote ambazo madhehebu yoyote au 'Umma wowote ule haujapata.

Hivyo walilazimika katika wakati mwingi wa zama zao kutumia Taqiyyah kwa kuwaficha wanao wakhalifu kwa yale ambayo yangeleta madhara katika dini na dunia, na kwa sababu hii wamejulikana sana kwa Taqiyyah kuliko wasiokuwa wao. Imeelezwa kuwa, sababu ya kuwa na muelekeo huu ni mashinikizo mbalimbali ya kisiasa, kijamii, kitamaduni, kisiasa na kadhalika, ambapo katika kipindi chote cha historia wamekuwa wakiandamwa na wapinzani wao.

Kuna aina tofauti za taqiyyah, na mafaqihi wa Kishia, wamebainisha hukmu taklifi (ni ile ambayo inabainisha moja kwa moja jukumu la mwanadamu kuhusiana na jambo au maudhui fulani; kwa mfano inamtaka mja kutekeleza ibada ya Swala au inamkataza kunywa pombe) na hukmu wadhi'i (haibainishi moja kwa moja amri au maagizo; bali kwa mfano inabainisha masharti ya kusihi amali au jambo fulani;[7] kwa mfano, hukumu hii kwamba, Swala inayoswaliwa kwa nguo yenye najisi ni batili) na masharti yake kwa mujibu wa Aya za Qur'an na Hadithi za Maimamu (a.s).

Kwa mujibu wao, pale ambapo kudhihirisha itikadi kwa wapinzani kutadhuru maisha, mali, na heshima ya mtu au watu wengine, taqiyyah ni wajibu kwa kiwango ambacho madhara yanaepukika. Taqiyyah inaweza kuwa mustahabu, makuruhu, (kuchukiza) mubaha (ruhusa) na haramu katika baadhi ya matukio na kwa mujibu wa masharti fulani.

Inasemekana kwamba mafaqihi wengi wa Kisunni pia wanaona taqiyyah kuwa inaruhusiwa pale ambapo kuna hofu ya kupoteza maisha na hata mali, kiasi cha kuzuia hasara na madhara tarajiwa. Miongoni mwa madhehebu ya Kiislamu, Zaidiyyah na Uwahabi ni yenyewe yanapinga taqiyyah.


Utambuzi wa maana

Taqiyyah ni mwanadamu kuficha ukweli wa imani yake mbele ya wapinzani ili kujihifadhi katika sehemu za hatari anapohisi kuwa kuna hatari na madhara ya kidini na kidunia. [1] Kwa maneno mengine, ni kujikinga mwenyewe au wengine kunako madhara au hasara kutoka kwa mtu mwingine kupitia kuwa pamoja na yeye katika maneno au kitendo. [2] Taqiyyah katika lugha imetokana na neno «وَقی» yenye maana ya kuhifadhi, kujizuia, kujikinga, kuficha kwa ajili ya kusalimika na maudhi. [3]

Nafasi yake

Taqiyyah ni miongoni mwa mambo ambayo yamechunguzwa katika elimu ya fiq'hi katika milango ya kifiq'h imezungumziwa katika maudhui za tohara Swala, Swaumu, Hija na kuamrisha mema na kukataza maovu. [4] Katika vitabu vinavyohusiana na kanuni za fiq'h, imetajwa kwa anuani ya kanuni na baadhi ya mafakihi wamelizungumzia katika sura ya pekee na ya kujitegea katika vitabu vyao vya fat'wa. [5]

Ingawa neno taqiyyah halijaja ndani ya Qur'an, lakini wanazuoni wa Kiislamu wanaamini kwamba baadhi ya Aya [6] maudhui zake zinaashiria jambo hilo na ili kuthibitisha uhalali wa taqiyyah Aya hizo zimetumika kama hoja ya kuthibitisha hilo. [7] Katika vitabu vya hadithi vya Kishia, kuna hadithi nyingi zilizopokewa kutoka kwa Maimamu Maasumu (a.s) zinazozungumzia maudhui ya taqiyyah. [8]

Sheikh Kulayni mpokezi wa hadithi wa Kishia (aliyefariki 329 Hijiria) katika kitabu chake al-Kafi, ametenga sehemu maalumu yenye jina la "Bab al-Taqiyyah" (mlango wa taqiyyah) na amekusanya humo hadithi 23. [9] Hurr al-Amili pia amekusanya hadithi 146 zinazohusiana na hukumu mbalimbali za taqiyyah katika kitabu chake cha Wasail al-Shiah. [10] Pia, katika baadhi ya vyanzo vya riwaya vya Ahlu-Sunna kumenukuliwa katika sura ya mtawanyiko hadithi zinazozungumzia maudhui ya taqiyyah. [11]

Taqiyyah katika madhehebu ya Shia

Inaelezwa kwamba, taqiyyah ni katika imani za kitheolojia na kifiq'h za Kishia na ni moja ya mambo muhimu sana ambayo kupitia kwayo, Mashia wameweza kuhifadhi maktaba yao ya kifikra na kiitikadi katika kipindi chote cha historia. [12]

Kwa mujibu wa ushuhuda wa vyanzo vya kihistoria, madhehebu ya Shia yalikabiliwa na hali mbaya ya mbinyo na mashinikizo katika nyanja mbalimbali za kijamii, kiutamaduni na kisiasa katika historia ya uhai wake kiasi kwamba, kuonyesha itikadi ya Ushia mbele ya wapinzani kulikuwa kukiambatana hasara na madhara mengi ya kiroho na kimali kwao. Kwa hiyo, Maimamu wa Shia waliona taqiyyah ni muhimu ili kuokoa maisha yao na ya Mashia na wafuasi wao, na hivyo kuzuia kusambaratika na kuangamia kwa jamii ya Shia. [13]

Katika baadhi ya vyanzo vya hadithi za Shia, kuna riwaya zenye tafsiri na maana kama vile ((لا دینَ لِمَن لا تَقِیَّةَ لَه ; Hana dini ambaye hana taqiyyah)),[14]; ambayo inaeleza umuhimu wa taqiyyah miongoni mwa Maimamu Maasumu (a.s) na wafuasi wao.[15]

Kwa mujibu wa Ayatullah Makarem Shirazi, Marjaa Taqlidi wa Kishia, ni kwamba, taqiyyah si makhsusi kwa Ushia tu [16] Yeye anaamini kwamba, kila mtu au idadi ya walio wachache katika jamii katika kipindi na zama zozote zile katika historita au sehemu yoyote ile ulimwengu kama atakumbana na wapinzani na maaadui wenye taasubi (chuki), na ikawa kwamba, kama atadhihirisha imani na itikadi yake kutapatikana madhara kwake au watu walio karibu naye na hii hali ya kudhihirisha itikadi umuhimu wake ni mdogo kuliko kuhifadhi roho na mali, basi hapa anapaswa kutekeleza hukumu ya kisheria ya taqiyyah kwa kuficha itikadi yake.[17]

Katika baadhi ya hadithi ambazo zimenukuliwa kutoka kwa Maimamu wa Shia (a.s), kitendo cha taqiyyah kimeelezwa kuwa kimewahi kufanywa na baadhi ya Mitume wa Mwenyezi Mungu, kabla ya Mtume wa Uislamu (s.a.w.w), kama Shiyth (Seth), [18] Ibrahim, [19] Yusuf [20] na As'hab al-Kahf (watu wa pangoni). [21]

Shahidi wa Kwanza, mmoja wa mafakihi wa Kishia katika karne ya 8 Hijiria, alizichukulia Hadithi zilizopokewa na kunukuliwa kutoka kwa Maimamu Maasumu (a.s) kuwa zimejaa kauli za taqiyyah na akaorodhesha taqiyyah kuwa moja ya mambo muhimu ya kutofautiana hadithi. [22] Kwa muktadha huo, inaelezwa kuwa, kufahamu masuala yanayohusiana na taqiyyah katika hadithi, ni jambo lenye nafasi na umuhimu mkubwa katika kunyambua kwa umakini zaidi hukumu na masuala ya kisheria. [23]

Aina za taqiyyah

Taqiyyah inagawanyika sehemu mbili kulingaana na msukumo na lengo la anayefanya taqiyyah: [24]

  • Taqiyyah ya woga: Kufanya taqiyyah (kuficha itikadi) mbele ya wapinzani katika sehemu ambayo mtu ana hofu kwamba, kuna madhara ya kiroho, kimali au kiheshima endapo atadhihirisha na kuonyesha itikadi yake halisi. [25] Taqiyyah ya woga (khofu) nayo ima ni ikrahi (ya kulazimishwa) ambapo mtu katika hali hii anatishiwa na hivyo kulazimika kutamka au kufanya kitu ambacho ni kinyume kabisa na itikadi yake kama kulazimika kukufuru, [26] au ni kitmani (kuficha itikadi) ambapo katika hali hii mtu akiwa na lengo la kuhifadhi roho na uhai wake au wa watu wanaomzunguka, hulazimika kuficha itikadi yake. [27] Taqiyyah iliyofanywa na Ammar bin Yassir mbele ya washirikina kwa ajili ya kuokoa maisha yake ni aina ya taqiyyah ya ikrahi (kulazimishwa), [28] na taqiyyah ya Muumini wa Aal Furaun mbele ya mafirauni na taqiyyah ya watu wa pangoni, ambao wakiwa na lengo la kuhifadhi na kuokoa roho zao walificha itikadi zao ni mifano ya wazi inayohesabiwa kuwa ni katika fungu la taqiyyah ya kitmani (kuficha). [29
  • Taqiyyah ya Modarati: Taqiyyah ya upole (huruma); aina hii ya taqiyyah ambayo inajulikana pia kwa jina la taqiyyah ya tahbibi (ya kuleta huba), [30] ni kuficha itikadi kwa ajili ya maslahi kama ya kulinda umoja, kuvutia upendo na urafiki na kuondoa uadui na chuki na kiujumla ni katika mambo ambayo umuhimu wake ni zaidi ya kudhihirisha mtu itikadi yake. [31] Baadhi ya mafakihi wa Kishia wakitumia hadithi kutoka kwa Maimamu Maasumu (a.s), [32] kama hoja, wametambua hatua kama kushiriki katika vikao vya Ahlu-Sunna (sio kwa ajili ya kuhifadhi roho) kama kushiriki katika Swala za jamaa pamoja nao (hususan katika msimu wa Hija), kuwatembelea wagonjwa wao, kushiriki katika shughuli zao za mazishi na mambo mengine ya kijamii kama hayo ambayo hupelekea kupatikana na kuhifadhiwa umoja, kulindwa adhama na izza (heshima) ya Waislamu, kuondoa chuki, hasama na dhana mbaya kwamba, ni mifano ya wazi ya taqiyyah ya huruma na upole au tahbibi (upendo). [33]

Kuna wengine ambao wameigawa taqiyyah katika sehemu tatu kwa mujibu wa nafasi na mazingira ya anayefanya taqiyyah. Sehemu hizo ni: Taqiyyah ya kisiasa (taqiyyah mkabala wa nguvu za kisiasa zinazotawala), taqiyyah ya kifiq'h (taqiyyah katika kubainisha hukumu) na taqiyyah ya kijamii (taqiyyah mkabala wa watu katika jamii na katika mdakhala na maingiliano nao). [34]

Hukumu

Mafakihi wa Kishia wakitumia hoja kama Qur'an na Sunna, wametaja baadhi ya hukumu zinazohusiana na taqiyyah ambazo tunazibainisha hapa:

Hukumu taklifi

Taqiyyah kwa mujibu wa hukm taklifi inagawanyika katika sehemu tano: [35]

  • Taqiyyah ya wajibu: Kwa mtazamo wa wanazuoni wa fiq'h wa Kishia ni kwamba, kama kudhihirisha itikadi mbele ya wapinzani, kutapelekea kupatikana madhara ya kinafsi, kimali na kiheshima kwa mtu mwenyewe au kwa watu wengine, na kuhusiana na kupatikana madhara haya mhusika ana elimu ya hilo au hata dhana tu, basi katika hali hii ni wajibu kwake kufanya taqiyyah kwa kiwango cha kuondoa madhara. [36] Kigezo katika taqiyyah ya wajibu ni kwamba, kupitia taqiyyah kuhifadhiwe kitu; na kukihifadhi kitu hicho na kukifanya kibakie ni wajibu na kukipoteza ni haramu. [37]
  • Taqiyyah ya mustahabu: Ni sehemu ambayo kama mtu ataacha taqiyyah, hilo halipelekei kupata madhara mara moja na wakati huo huo, lakini kuna wasiwasi kwamba, katika mustakabali kukapatikana madhara hayo au madhara hayo yatapatikana lakini hatua kwa hatua. [38] Kwa mujibu wa mafakihi wa Kishia, taqiyyah ya modaarati (upolea na kulegeza kamba) ni kielezo na mfano wa taqiyyah ambayo ni mustahabu. Sheikh Ansari (aliyeaga duunia 1281 Hijiria) yeye ametambua taqiyyah ambayo ni mustahabu kwamba, ni ile ambayo imejumuisha mambo ambayo yametajwa na kuwekwa bayana katika hadithi; kama vile kuishi na kuingiliana na Ahlu-Sunna, kuwatembelea wagonjwa wao, kuswali katika misikiti yao na kushiriki katika shughuli zao za mazishi. Kwa mujibu wa fat'wa yake, mambo mengine ambayo yapo nje ya mipaka ya hadithi haijuzu kuyafanya. [39]
  • Taqiyyah ya makuruhu: Hii ni taqiyyah ambayo kuacha kuifanya na kustahamnili madhara yake ni bora kuliko kuifanya. [40] Shahidi wa Kwanza anasema: Taqiyyah ya makuruhu ni kufanya taqiyyah katika jambo la mustahabu ambalo kulifanya kwake halina madhara ya hapo hapo wala katika mustakabali. [41]
  • Taqiyyah ya mubaha (ruhusa): Hii ni taqiyyah ambayo kuifanya na kutoifanya hakuna tofauti yoyote. [42] Kwa mujibu wa Sheikh Ansari ni kwamba, taqiyyah ambayo kupitia kwayo madhara yanaondolewa na kuepukwa kama yapo, na kutokuweko madhara kwa mtazamo wa sheria hali huwa sawa. [43]
  • Taaqiyyah ya haramu: Kufanya taqiyyah katika sehemu ambayo kuiacha kwake mtu hapati madhara (ya hapo hapo au madhara katika mustakabali.) [44]

Baadhi ya mifano ya wazi ya taqiyyah ya haramu kwa mujibu wa mafaqihi wa Kishi ni:

  1. Kufanya taqiyyah sehemu ambayo hilo linapelekea ufisadi katika dini na kuingia bidaa na uzushi katika dini. [45]
  2. Kwa mujibu wa mtazamo mashuhuri wa mafaqihi wa Kishia, [46] sehemu ambayo kunapelekea kumwagwa damu ya wengine; kama vile mtu kulazimishwa amuue muumini la sivyo atauawa yeye. Katika hali hii, haijuzu kumuua mtu kwa kisingizio cha kufanya taqiyyah na kuokoa roho na maisha yake. [47]

Hoja na nyaraka

Mafaqihi wa Kishia wakiwa na lengo la kuthibitisha kwamba, inajuzu kufanya taqiyyah wametumia hoja nne (Addilat al-Ar'baa); Qur'an, hadithi, ijma'a na akili kuthibitisha hilo. [48]

Qur'an

Aya muhimu kabisa ambayo wanazuoni wa fiq'h wanaitumia kama hoja ya kujuzisha taqiyyah ni ya 106 katika surat al-Nahl. Imekuja katika Aya hii kwamba:

Anaye mkataa Mwenyezi Mungu baada ya kuamini kwake - isipo kuwa aliye lazimishwa na hali ya kuwa moyo wake umetua juu ya Imani, lakini aliye kifungulia kifua chake kukataa - basi hao ghadhabu ya Mwenyezi Mungu ipo juu yao, na wao watapata adhabu kubwa.

Wafasiri wengi wa Kishia na Kisunni wamesema kuhusiana na sababu ya kushuka Aya hii kwamba, ni kuhusiana na Ammar bin Yasir. [49] Ammar alilazimika kutoa maneno ya kujitenga na kujibari na Uislamu na Mtume (s.a.w.w) akiwa chini ya mateso ya washirikina. Baadhi wakadhani kwamba, Ammar amekufuru. Wakati Mtume aliposikia kisa na tukio hilo lililompata Ammar, alisema kuwa, Ammar amejaa imani kuanzia kichwani mpaka miguuni na tawhidi imechanganyika na nyama yake. Baada ya Ammar kwenda kwa Mtume, mbora huyo wa viumbe alimliwaza na kumwambia kwamba, kama mara nyingine itatokea akawa katika mazingira magumu kama hayo basi asisite kuonyesha kuwa mbali na Uislamu na Mtume (s.a.w.w). [50] Kadhalika mafakihi wakiwa na lengo la kuthibitisha kujuzisha taqiyyah wanatumia pia Aya ya 28 ya Surat Ghafir na Aya ya 28 ya Surat al-Imran. [51]

Hadithi

Sayyid Muhammad Swadiq Rouhani na Naser Makarem Shirazi wanasema kuwa, hadithi ambazo zinatoa ishara ya kuruhusu kufanya taqiyyah zimefikia hatua ya kuwa ni mutawatir. [52] Hadithi hizi zinagawanyika katika makundi kadhaa.

  • Hadithi ambazo zinaonyesha kuwa, taqiyyah ni ngao na hifadhi ya muumini. [53
  • Hadithi zenye ibara kama “asiye na taqiyyah hana dini”. [54]
  • Hadithi ambazo ndani yake taqiyyah imetambuliwa kuwa faradhi kubwa kabisa na kitu kinachopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu na mawalii wake. [55]
  • Hadithi ambazo zinaonyesha kuwa, baadhi ya Mitume wa Mwenyezi Mungu nao pia walikuwa wakifanya taqiyyah. [56]

Sambamba na hadithi hizo, mafakihi wametumia pia hadithi kama za "la dharar" hadithi za kujibari na sabb (hadithi ambazo ndani yake zinajuzisha kuonyesha kujibari –kujitenga- na kumtusi Mtume (saww) na Maimamu watoharifu (as) kwa ajili ya taqiyyah na kulinda roho na uhai) na hadithi raf’i (kuondolewa au kufutiwa) kwa ajili ya kuthibitisha uhalali na ruhusa ya kufanya taqiyyah. [57]

Ijma'a

Muhaqqiq Karaki amesema, mafaqihi wa Kishia, wana kauli moja (ijma'a) kuhusiana na ruhusa ya kufanya taqiyyah. [58]

Akili

Utumiaji mafikihi hoja ya kiakili ni kwa namna hii ya kwamba, taqiyyah ni katika masuala ambayo ni vyema kutanguliza jambo muhimu zaidi mbele ya jambo muhimu. [59] Kutanguliza kufanya jambo muhimu zaidi na kuacha jambo muhimu, ni hatua ya lazima kwa mujibu wa akili; hii ina maana kwamba, kila mara inapotokea mukallaf ana taklifu na mambo mawili ambayo hawezi kuyafanya kwa wakati mmoja, anapaswa kutumia hukumu ya akili na hivyo kufanya jambo ambalo kwa mujibu wa akili lina umuhimu na maslahi zaidi. [60] Kuepuka madhara na kulinda roho ni katika mambo ambayo kwa mujibu wa akili yanapaswa kutangulizwa mbele ya mambo kama kudhihirisha itikadi. Kwa msingi huo, kiakili kufanya taqiyyah ni wajibu kwa ajili ya kuepuka madhara na kuokoa roho na uhai. [61]

Mtazamo wa Ahlu-Sunna

Imekuja katika kitabu cha al-Mausu’at al-Fiq’hiyyah al-Kuwaitiyyah (kitabu kikubwa kinachohusiana na fiq’h ya Ahlu-Sunna ambacho kina juzuu 45) ya kwamba: Kwa mujibu wa nadharia ya Maulamaa waliowengi wa Kisuni ni kuwa, wakati wa dharura; yaani katika sehemu ambayo kuna hofu ya kuuawa, kuudhiwa na kiujumla kuna hofu ya kupata madhara mengi, inajuzu kufanya taqiyyah kwa kiwango cha kuepuka na kuokoka na madhara hayo. [62]

Wakiwa na lengo la kuthibitisha uhalali na ruhusa ya kufanya taqiyyah mbali na kutumia hoja kama Aya ya 28 ya Surat al-Imran na Aya ya 106 ya Surat Nahl, wametumia pia hadithi mbalimbali. [63].

Madhehebu ya Kiislamu yanayopinga taqiyyah

Miongoni mwa madhehebu ya Ahlu-Sunna, kundi la Mawahabi ni miongoni mwa wapinzani na wakosoaji wa taqiyyah na wanawakosoa na kuwalaumu Mashia kutokana na wao kuikubali taqiyyah na kuifanyia kazi. [64] Kwa upande wa madhehebu ya Kishia pia, inaelezwa kwamba, kundi la Zaydiyyah linapinga taqiyyah. [65]

Moja ya ukosoaji unaelezwa na Ibn Taymiyyah na kisha kufuatwa katika msimamo huo na Mawahabi kuhusiana na taqiyyah ni kwamba, wanasema kufanya taqiyyah ni aina fulani ya uongo na nifaki. [66] Katika kujibu madai haya imeelezwa kwamba, maana ya taqiyyah inapingana kikamilifu na maana ya nifaki; kwani nifaki ni kuficha ukafiri na batili na kudhihirisha imani; hii ni katika hali ambayo kufanya taqiyyah ni kuficha imani na kudhihirisha ukafiri. [67]

Monografia

Kumeandika makala na vitabu vya kujitegemea (vyenye maudhi moja) kuhusiana na taqiyyah na baadhi yavyo ni:

  • Risalat fi al-Taqiyyah: Hiki ni kitabu mukhtasari kilichoandikwa na Muhaqqiq Karaki, kitabu hiki kinahusiana na hukumu ya kifiq’h ya taqiyyah iliyoandikwa katika kitabu chenye anuani ya Rasail al-Muhaqqiq Karaki. Kitabu cha Rasail al-Muhaqqiq kina juzuu tatu ambapo Risalat fi al-Taqiyyah ni juzuu ya pili. [68]
  • Risalat fi al-Taqiyyah: Mwandishi Sheikh Ansari. Kitabu hiki kinahusiana na hukumu ya kufanya taqiyyah.
  • Al-Taqiyyah: Kitabu hiki kilichoandikwa na Imam Ruhullah Khomeini kinahusiana na hukumu ya kufanya taqiyyah.
  • Taqiyyeh az didgah madhahib va ferqehaye ghair eslami: (Taqiyyah kwa mtazamo wa madhehebu na makundi yasiyo ya Kiislamu) kitabu hiki kimeandikwa na Thamir Hashim al-Amidi kwa lugha ya Kiarabu na kutarjumiwa kwa lugha ya Kifarsi na Muhammad Swadiq Arif. Ndani ya kitabu hiki, mwandishi amebainisha mitazamo ya mafakihi mashuhuri wa madhehebu nne za Kisuni kuhusiana na suala la kufanya taqiyyah.
  • Taqiyyeh Separi baroye mobareze amiqtar: (taqiyyah; kinga kwa ajili ya mapambano ya kina) mwandishi Sheikh Nassir Makarem Shirazi.

Vyanzo

  • Qur'an Tukufu
  • Ali Kashif al-Ghitha, Muhammad Hussein. Asl al-Syi'ah wa Ushuluhā, Qom: cet. Ala Ali Ja'far, 1415.
  • Alusi, Muhammad bin Abdullah. Ruh al-Ma'āni, Beirut: Dar Ihya al-Tsurats al-Arabi, tanpa tahun.
  • Ibnu Abil Hadid, Sharah Nahj al-Balāghah, Qom: cet. Muhammad Abul Fadhl Ibrahim, 1404.
  • Ibnu Jauzi, Al-Muntadzam fi Tarikh al-Muluk wa al-Umam, Beirut: cet. Muhammad Abdul Qadir Atha wa Musthafa, Abdul Qadir Atha, 1412/1992.
  • Asqalani, Ibnu Hajar. Fath al-Bari, Sharah Sahih al-Bukhari, Beirut: Dar al-Ma'rifah, tanpa tahun.
  • Ibnu Hazm, al-Mahalla, Beirut: cet. Ahmad Muhammad Shajir, Dar al-Jalil, tanpa tahun.
  • Ibnu Hambal, Musnad al-Imam Ahmad bin Hanbal, Kairo: 1313, cet. ofset, Beirut, tanpa tahun.
  • Ibnu Khallakan, Ibnu Manzhur, Muhammad Abu Zuhrah ,-Imām al-Shādiq, Hayatuhu wa 'Asruhu, Ārāuhu wa Fiqhuh, Qahirah, 1993.
  • Ibnu Mandzur, Muhammad bin Mukarram, Lisān al-Arab, juz. 15, Beirut: Dar al-Fikr, Dar Shadir, tanpa tahun.
  • Amin, Muhsin. Naqdh al-Washi'ah atau Shiah baina al-Haqāiq wa al-Auhām, Beirut: 1403/1983.
  • Amini, Abdul Hussein, Al-Ghadir fi Kitāb wa al-Sunah wa al-Adab, juz. 1, Beirut: 1387/1967.
  • Anshari, Murtadha bin Muhammad Amin, Al-Taqiyyah, Qom: cet. Fars Hasun, 1412.
  • Bahrani, Yusuf bin Ahmad, Al-Hadāiq al-Nāshirah fi Ahkām Itrah al-Thāhirah, Qom: 1363-1367.
  • Bukhari Ju'fi, Muhammad bin Ismail, Sahih Bukhari, Istanbul: 1981/1401.
  • Tsa'labi, Ahmad bin Muhammad Qashash al-Anbiyā al-Musamma 'Arāisy al-Majālis. Beirut: al-Maktabah al-Tsaqafah, tanpa tahun.
  • Jashshash, Ahmad bin Ali, Kitāb Ahkām al-Qurān. Istanbul: 1335-1338. Cet. Ofset, Beirut: 1406/1986.
  • Jauhari, Ismail bin Hamad, Al-Sehah: Taj al-Lughah wa Sehah al-Arabiyyah. Beirut: Riset: Athar, Ahmad Abdul Ghafur, Dar al-Ilm lil Malayin, tanpa tahun.
  • Hurr Amili, Tafshil Wasāil al-Shiah ila Tahshil al-Shari'ah. Qom:1409-1412.
  • Halabi, Ali bin Ibrahim, Al-Sirah al-Halabiyyah. Beirut: 1320, cet. ofset, tanpa tahun.
  • Khomeini, Ruhullah."Al-Rasāil, Qom: 1385.
  • Khomeini, Ruhullah, Al-Makasib al-Muharramah, Qom: 1374 SH.
  • Subhani, Ja'far, Al-Inshāf fi Masāil dāma fihā al-Khilaf, Qom: 1381 SH.
  • Shubbar, Abdullah, Ushul Ashliyah wa al-Qawāid al-Shar'iyyah, Qom: 1404.
  • Sharafuddin, Abdul Husain.Ajwibah Masāil Jarullah, Qom:cet. Abdul Zahra Yasari, 1416/1995.
  • Shamsul Aimmah Sarakhsi, Muhammad bin Ahmad, Kitāb al-Mabsuth, Beirut: 1406/1986.
  • Shahrestani, Muhammad bin Abdul Karim, al-Milāl wa al-Nihal, Beirut: cet. Muhammad Sayid Kilani, 1406/1986.
  • Al-Shan'ani, Abu Bakar 'Abd al-Razzaq bin Hamam (211), al-Mushnnaf, Riset: Habib Rahman al-A'dhami. Beirut: al-Maktab al-Islami, cet. 2, 1403 H.
  • Muhammad bin Makki, Shahid Awwal, Al-Bayān, Qom: cet. Muhamad Hasun, 1412.
  • Muhammad bin Makki, Shahid Awwal, Al-Qawāid wa al-Fawāid: Fi al-Fiqh wa al-Ushul wa al-Arabiyyah.Najaf: cet. Abdul Hadi Hamin, 1399/1979, Qom: cet. ofset, tanpa tahun.
  • Thabathabai, Muhammad Husain. Al-Mizan fi Tafsir al-Quran. Beirut: 1390-1394/1971-1974.
  • Thabarsi, Fadhl bin Hassan, Majma' al-Bayan fi Tafsir al-Quran. Diteliti dan komentari oleh Hasyim Rasuli dan Fadhlullah Yazdi Thabathabai. Tehran: Nasir Khosru, 1372 SH.
  • Thabari, Muhammad bin Jarir.Tārikh al-Thabari: Tarikh al-Umam wa al-Muluk. Beirut: cet. Muhammad Abul Fadhl Ibrahim, 1382-1387/1962-1967.
  • Thusi, Muhammad bin Hassan, al-Tibyān fi Tafsir al-Qurān. Beirut: cet. Ahmad Habib Qashir, Amili, tanpa tahun.
  • Thusi, Muhammad bin Hassan, Al-Fehrest. Qom; cet. Jawad Qayumi, 1417.
  • Ghazali, Muhammad bin Muhammad.Ihyā' Ulumuddin, Beirut: Dar Nadwah al-Jadid, tanpa tahun.
  • Fadhil Miqdad, Miqdad bin Abdullah. Al-Lawāmi' al-Ilahiyyah fi Mabāhits al-Kalāmiyah. Qom: cet. Muhammad Ali Qadhi Thabathabai, 1380.
  • Fakhr al-Razi, Muhammad bin Umar. Al-Tafsir al-Kabir atau Mafatih al-Ghaib, Beirut: 1421/200.
  • Firuz Abadi, Muhammad bin Ya'qub. Al-Qāmus al-Muhith, Beirut:1407/1987.
  • Qashimi, Muhammad Jamaluddin, Tafsir al-Qasimi, al-Musama Mahasin al-Ta'wil, Beirut: cet. Muhammad Fuad Abdul Baqi, 1398/1978.
  • Qurthubi, Muhammad bin Ahmad, Al-Jāmi' li Ahkām al-Qurān, Beirut: 1405/1985.
  • Kulaini, Muhammad bin Ya'qub. Al-Kāfi, Beirut: cet. Ali Akbar Ghaffari, 1401.
  • Majlisi, Muhammad Baqir. Bihār al-Anwār, Beirut: 1983/1403.
  • Muhaqqiq Karaki, Ali bin Husain.Rasāil al-Muhaqqiq al-Karaki. Qom: cet. Muhammad Hasun, jld. 2, Risalah fi al-Taqiyyah, 1409.
  • Muraghi, Ahmad Musthafa, Tafsir al-Maraghi, Beirut: 1365.
  • Muzhaffar, Muhammad Ridha, Aqāid al-Imamiyyah, Qom: tanpa tahun.
  • Mufid, Muhammad bin Muhammad. Awāil al-Maqālat fi al-Madzahib wa al-Mukhtarat, Qom: cet. Abasqali, Tabriz: 1371, cet. ofset, Qom, tanpa tahun.
  • Mufid, Muhammad bin Ya'qub, Tashih I'tiqād al-Imāmiyah, Beirut: cet. Husain Dargahi, 1414/1993.
  • Musawi, Bujunurdi, Hassan, Al-Qawāid al-Fiqhiyah, Qom: cet. Mahdi Mehrizi dan *Muhammad Husain Daraiti, 1377.
  • Najasyi, Ahmad bin Ali, Fehrest Asmā Mushannafai al-Shiah al-Mushtahrab bi Rijāl al-Najāshi, Qom: cet. Musa Shabiri Zanjani, 1407.
  • Nasfa, Abdullah bin Ahmad, Tafsir al-Qurān al-Jalil, al-Musama bi Madarik al-Tanzil wa Haqāiq al-Ta'wil, Beirut: Dar al-Kitab al-Arabi, tanpa tahun.
  • Naishaburi, Ali bin Ahmad Wakhidi, Asbāb al-Nuzul al-Ayāt, Kairo: 1388/1968.