Dhambi

Kutoka wikishia

Dhambi (Kiarabu: الذنب) maana yake ni kuasi amri ya Mwenyezi Mungu au kwa maneno mengine ni kufanya jambo ambalo Mwenyezi Mungu amelikataza au kuacha kufanya jambo ambalo imetolewa amri ya kulifanya. Madhambi yanagawanyika katika sehemu mbili. Madhambi makubwa na madhambi madogo. Dhambi kubwa ni zile ambazo katika Qur'an na hadithi kuwa kwake ni dhambi kubwa limebainishwa wazi au anayetenda dhambi hizo ameahidiwa adhabu; kama vile kuua nafsi, kuzini, kula mali ya yatima na kula riba.

Kwa mujibu wa mafundisho ya dini ya Uislamu, baadhi ya dhambi zina athari maalumu kama kupelekea kukosa neema, kupoteza heshima na kufa haraka. Kwa mujibu wa Aya za Qur'an Tukufu baadhi ya matendo mema, hupelekea kufutiwa dhambi. Kitendo hiki kinajulikana kwa jina la takfir yaani kufutiwa dhambi. Kwa mujibu wa baadhi ya hadithi, Mwenyezi Mungu huwafutia dhambi waja wake kupitia mambo kama maradhi na umasikini. Aidha katika Qur'an Tukufu imekuja kuwa, kama mtenda dhambi atatubia, basi Mwenyezi Mungu humfutia dhambi zake.

Waislamu wa Madhehebu ya Shia wanaamini kuwa, Mitume na Maasumina 14 hawatendi dhambi.


Maana ya neno

Dhambi maana yake ni kuasi amri za Mwenyezi Mungu au kwa maneno mengine ni kufanya jambo ambalo Mwenyezi Mungu amelikataza au kuacha kufanya jambo ambalo imetolewa amri ya kulifanya. Neno hili visawe vyake katika lugha ya Kiarabu ni maasiya, Ithmu, Dhanmbu, Sayyiah na Khatiyah.


Mgawanyo wa dhambi

Kwa mujibu wa ukubwa na udogo wake

Katika baadhi ya vitabu vya akhlaq (maadili), dhambi zimegawanywa katika sehemu mbili. Madhambi makubwa na madhambi madogo. Chimbuko la ugawaji huu ni Qur'an Tukufu na hadithi. Kwa mfano imekuja katika Aya ya 31 ya Surat al-Nisaa kwamba: Mkiyaepuka makubwa mnayokatazwa, tutakufutieni makosa yenu madogo, na tutakuingizeni mahali patukufu. Sayyied Muhammad Hussein Tabatabai anasema: Makusudio ya "makosa" katika Aya iliyotangua ni madhambi madogo; hii ni kwa sababu, imekuja mkabala na madhambi makubwa. Aya hii inabainisha nukta hii kwamba, madhambi yamegawanyika katika sehemu mbili yaani kubwa na ndogo.

Imekuja katika kitabu cha Ur'wat al-Uthqaa kwamba, madhambi makubwa ni ambayo ukubwa na udogo wake umeelezwa bayana au mwenye kufanya dhambi hizo ameahidiwa adhabu au katika Qur'ani na hadithi moja madhambi yametambulika kama ni dhambi kubwa zaidi.

Kuua nafsi, kuzini, kumtuhumu mwanamke mwenye kujiheshimu, kula mali ya yatima, kula riba, kuacha swala, kuiba na kukata tamaa na rehma za Mwenyezi Mungu, ni miongoni mwa madhambi makubwa ambayo yametajwa katika hadithi mbalimbali.

Mgawanyo wa dhambi kwa mujibu wa athari zake

Katika baadhi ya hadithi, dhambi zimegawanywa kwa mujibu wa athari na matokeo yake. Kwa mfano katika kitabu cha Maani al-Akhbar imenukuliwa hadithi kutoka kwa Imam Sajjad (a.s) kwamba, dhambi zimegawanywa katika makundi kadhaa ambapo baadhi yake ni kama ifuatavyo:

Athari za dhambi kimaada na kiroho

Kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa kutoka kwa Imam Swadiq (a.s) ni kuwa: Pindi mtu anapofanya dhambi, hujitokeza doa jeusi katika moyo wake. Endapo atatubia, doa hilo hufutika; lakini kama ataendelea kutenda dhambi, doa lile jeusi mduara wake hupanuka na kuwa mkubwa mpaka likafunika sehemu yote ile na hivyo yote kuwa nyeusi. Wakati sehemu ile nyeupe inapobadilika na kuwa nyeusi yote, mwenye moyo ule katu hawezi kuona ukweli, haki na uhakika. Katika hadithi moja Imam Ali (a.s) akitumia hoja ya Aya isemayo: "Na misiba inayo kusibuni ni kwa sababu ya vitendo vya mikono yenu" anaona kuwa, madhambi ni sababu ya belua na balaa ambayo humpata mwanadamu katika maisha; hata kupata mchubuko au kudondoka chini.

Vifuta madhambi

Katika kitabu cha Mizan al-Hikmah kuna sehemu yenye anuani isemayo: Mukaffiraat Dhunub (Vifuta Madhambi) ambapo ndani yake zimebainishwa sababu na mambo yanayofuta dhambi kwa mujibu wa hadithi. Kwa mujibu wa kitabu hicho, umasikini, maradhi, bashasha, kumsaidia madhulumu, kusujudu sana na kumswalia Mtume (s.a.w.w) ni miongoni mwa mambo yanayofuta dhambi.

Kutubia dhambi

Makala asili: Toba

Katika vitabu vya Fiqih vya Waislamu wa Madhehebu ya Shia daima suala la wajibu wa kutubia dhambi limekokotezwa na kutiliwa mkazo na wajibu wa kufanya hivyo umetambuuliwa kuwa ni wa haraka. Kwa maana kwamba, mtu anapaswa kutubia dhambi haraka bila ya kuchelewesha. Sheikh Muhammad Hassan Najafi , Sayyied Yazdi anatambua kwamba, kutubia dhambi ni suala muhimu zaidi na wajibu zaidi miongoni mwa mambo ya wajibu. Kwa kufanya toba Mwenyezi Mungu humpokea mfanya dhambi kwa mujibu wa Aya ya 82 ya Surat Taha ambayo inasema: "Na hakika Mimi ni Mwingi wa Kusamehe kwa anayetubia, na akaamini, na akatenda mema, tena akaongoka" na vyovyote awavyo ntu huyu Mwenyezi Mungu humsamehe.

Umaasumu (kutotenda dhambi) ni daraja ya kujiepusha na dhambi

Makala asili: Umaasum

Katika utamaduni wa dini, Umaasumu ni daraja na cheo ambacho mwenye nacho hatendi dhambi. Mtu wa aina hii anafahamika kama Maasumu (asiyetenda dhambi). Waislamu wa Madhehebuu ya Shia wanaamini kuwa, Maasumuu hatendi dhambi kwa hiari yake. Na hii ni kutokana na kuwa, ana ufahamu kamili na wa daima juu ya ubaya wa dhambi. Shia Imamiya wanaamini kuwa, Mitume, Maimamu 12 na Bibi Fatma Zahra (a.s) wana daraja ya Umaasumu yaani katu hawatendi dhambi.

Rejea

Vyanzo

  • Swaduq, Muhammad bin Ali, Maani al-Akhbar, Mhakiki, Ali Akbar Ghaffari, Ofisi ya Intisharat Eslami, Chapa ya Kwanza, 1403 Hijria.
  • Jawad Amoli, Abdallah, Tasnim, Mhakiki: Ali Eslami, Qum, Markaz Nashr Israa, Chapa ya Pili, 1387 Hijria Shamsia.
  • Khui, Sayyyid Abul-Qassim, Swirat al-Najat, mkusanyaji na msahihishaji: Mussa Mufid al-Din Aswi Amili, Qum, Ofisi ya Uchapishaji ya al-Muntakhab, Chapa ya Kwanza, 1416 Hijria.
  • Dastighib, Sayyid Abdul-Hussein, Qum, Ofisi ya Uchapishaji ya Eslami, Chapa ya Tisa, 1375 Hijria Shamsia.
  • Qeraati, Mohsin, Gonah Shenasi, Mpangaji: Muhammad Muhammad Ishtihardi, Tehran, Kituo cha Utamaduni cha Dars-haye Qur'an, Chapa ya Kwanza, 1377 Hijria Shamsia.
  • Tabatabai, Sayyid Muhammad Hussein, al-Mizan Fi Tafsir al-Qur'an, Qum, Taasisi ya Uchapishaji ya Eslami, Chapa ya Tano, 1417 Hijria.
  • Kashif al-Ghitaa, Hassan bin Ja'afar, Anwar al-Faqahah, Najaf, Taasisi ya Kashif al-Ghitaa, Chapa ya Kwanza, 1422 Hijria.
  • Kulayni, Muhammad bin Ya’aqub, al-K’kafi, mhakiki, Ali Akbar Ghaffari na Muhammad Akhundi, Tehran, Darul-Kutub al-Islamiya, Chapa ya Nne, 1407 Hijria.
  • Sobhani, Ja'afar, Buhuth Fil Milal Wanihal; Dirasat Maudhuiyah Muqaranat Lil-Madh'hab al-Islamiyah, Qum, Kituo cha Mudiriyat Hawzat al-Ilmiyah, Chapa ya Kwanza, 1370 Hijria Shamsia.
  • Majlisi, Muhammad Baqir, Bihar al-Anwar al-Jamiyat Lidurar Akhbar al-Aimat al-At'har, Beirut, Darul Wafaa, 1403 Hijria.
  • Muhammadi Rey Shahri, Muhammad, Mizan al-Hikmah pamoja na Tarjumi ya Kifarsi, Mtarjumi: Hamid Reza Sheikhi, Qum, Darul Hadith, Chapa ya Pili, 1379 Hijria Shamsia.
  • Misbah Yazdi, Muhammad Taqi, Amozesh Aqaed, Tehran, Taasisi ya Kimataifa ya Uchapishaji na Usambazaji ya Sazeman Tablighaat Eslami, Chapa ya Pili, 1378 Hijria Shhamsia.
  • Yazdi, Sayyid Muhammad Kadhim, al-Ur'wat al-Uthqaa, Qum, Taasisi ya Uchapishaji ya Imam Ali bin Abi Twalib, Chapa ya Kwanza, 1428 Hijria.