Umaasumu

Kutoka wikishia

Makala hii inahusiana na isma au umaasumu (kutotenda dhambi). Kama unataka kujua kuhusiana na umaasumu wa Manabii na umaasumu wa Maimamu angalia makala ya umaasumu wa Mitume na Maimamu.


Umaasumu / isma (Kiarabu: العصمة) ni hali ya mtu kukingwa na kitendo cha kutenda dhambi na makosa. Kwa maana kwamba, isma ni hali ya kutofanya dhambi. Wataalamu wa elimu ya theolojia wa Kishia na kundi la Mu'tazilah wameitambulisha isma kuwa ni ukarimu na wema wa Mwenyezi Mungu na wanafalsafa wa Kiislamu wao wanasema ni uwezo na nguvu ya kinafsi ambayo inamfanya maasumu aepukane na dhambi na kufanya makosa.

Kuhusiana na chimbuko na chanzo cha kinga ya kutotenda dhambi na makosa, kuna mitazamo tofauti iliyoelezwa ambapo baadhi yake ni: Ukarimu na wema wa kiungu, elimu na maarifa maalumu, irada, chaguo na majimui ya mambo ya kimaumbile ya Kiungu na kibinadamu. Wanatheolojia na wanafalsafa wanaona kuwa, umaasumu unaoana na hiari na wanaami kwamba, maasumu ana uwezo wa kufanya maasi na dhambi; lakini hafanyi hivyo. Kwa msingi huo anastahiki ujira na malipo.

Kuamini kwamba, Mitume ni maasumu na hawatendi dhambi ni jambo ambalo Maulamaa wote wa Kiislamu wameafikiana katika hili. Hata hivyo kuna tofauti ya maoni na mitazamo kuhusiana na wigo wa umaasumu. Umaasumu wa Mitume kutokana na ushirikina na ukafiri, umaasumu katika kupokea na kufikisha wahyi, na umaasumu kutokana na madhambi ya kukusudia baada ya Utume ni mada ambayo kuna makubaliano na kauli moja baina ya wanachuoni.

Wanachuoni wa Shia Imamiyyah wanawachukulia Maimamu wa Shia (a.s) kuwa hawana hatia ya dhambi kubwa au ndogo na hawafanyi kosa lolote lile katika maisha yao yote. Kwa mujibu wa Allama Majlisi ni kwamba, Mashia wana ijma'a (kauli moja) kwamba malaika wote hawatendi dhambi yoyote ile iwe kubwa au ndogo.

Hata hivyo suala la umaasumu limetiliwa baadhi ya ishkali; na miongoni mwazo ni ni kwamba, baadhi wanaona kuwa, jambo hilo haliendani na maumbile na asilii ya kibinadamu ambayo ina mvuto na nguvu mbalimbali za matamanio ya kinafsi. Katika kujibu hili imeelezwa kwamba, uwepo wa mielekeo na tamaa za kimwili na matamanio ya kinafsi ni msingi tu wa kuchafuka kwa dhambi na hauhusiani na kuifanya; kwani vizingiti kama vile ujuzi na utashi vinaweza kuzuia matokeo ya tamaa hizo.


Nafasi na umuhimu

Kwa mujibu wa Sayyid Ali Husseini Milani, mmoja wa wahakiki na waandishi wa athari za kitheolojia na kiitikadi za Shia ni kwamba, suala la umaasumu ni miongoni mwa masuala muhimu ya kitheolojia na kidini ambayo kila madhehebu ya Kiislamu imeyashughulikia kwa mtazamo wake. Kuunganishwa na kuhusishwa kwa umaasumu na hoja ya maneno na vitendo vya maasumu ni jambo ambalo limeongeza umuhimu na unyeti wa mjadala huu. Kwa mtazamo wake ni kwamba, kwa kuwa Masuni wao hawaamini umaasumu wa watawala na viongozi wa Kiislamu, wanajadili suala la umaasumu chini ya mada na mijadala ya Utume tu, lakini Mashia wanalijadili suala hili chini ya mada za Utume na Uimamu, kwa sababu wenyewe wanawachukulia na kuwatambua Mitume na Maimamu wote kuwa ni maasumu na watu wenye kinga ya kutotenda dhambi. Amesema umaasumu ni katika maudhui wanazoshirikiana Waislamu; licha ya kuwa, kuna tofauti nyingi kati yao katika mifano, vigezo na maelezo yake. [1]

Maudhui ya Isma hujadiliwa katika mijadala na vyanzo vya kitheolojia (kiitikadi) chini ya mada ya Isma ya Mitume, Maimamu na malaika. [2] Katika baadhi ya tafsiri za Qur’an, mada hii huzungumziwa chini ya maelezo ya Aya kama vile ya Tat’hir (utakaso) na masuala yanayohusiana nayo hubainishwa. [3] Katika elimu ya Usul al-Fiq’h, Maulamaa wa elimu hii wa Ahlu-Sunna, wamekitambua kigezo cha uhalali wa ijmaa (maafikiano) kuwa ni umaasumu wa umma; kwani kwa mtazamo wao, umma wa Kiislamu ni mrithi wa Mtume na umehifadhiwa na kufanya makosa, kusahau na kusema uongo katika masuala yanayohusiana na dini. Mkabala na wao, kuna Maulamaa wa Kishia ambao wao wametambua umaasumu wa Imam kuwa ndio kigezo cha ijmaa na maafikiano; kwani kwa mtazamo wao ni kwamba, Imam ndiye mrithi na kiongozi baada ya Mtume (s.a.w.w.) na mfano wake ni maasumu na ijmaa ni hoja kutokana na kuwa ni mgunduzi wa neno na kauli ya Maasumu. [4]

Maudhui ya umaasumu imejadiliwa pia katika dini zingine kama Ukristo na Uyahudi. Wakristo wao, mbali na kumtambua Nabii Issa Masih (a.s) kuwa ni maasumu na asiyetenda dhambi, wanaamini pia kwamba, waandishi wa kitabu kitakatifu na Papa (kiongozi wa kanisa katoliki) nao pia ni maasumu na watu wasiotenda dhmabi; hata hivyo itikadi hii kwamba, papa hatendi dhambi inahusiana na kanisa katoliki pekee. [5]

Utambuzi wa maana

Wanatheolojia na wanafalsafa wa Kiislamu wametoa fasili, maana na ufafanuzi tofauti wa umaasumu kulingana na misingi yao. Baadhi ya maana hizo ni:

  • Fasili na maana iliyotolewa na wanateolojia: Wanatheolojia wa Adliyah (Imamiyah [6] na Mu’tazilah) [7] wametoa maana ya umaasumu kwa msingi wa Qaidat al-Lutf (kanuni ya ukarimu) au principle of benevolence. [8] Kwa mujibu wa msingi huo, umaasumu maana yake ni ukarimu na wema wa Kiungu ambao Mola Muumba amempatia mja wake na kupitia kwake, hafanyi jambo chafu au hatendi dhambi. [9] Allama Hilli katika kutoa maana ya umaasumu amesema: “ni ukarimu na wema uliojificha ambao ni kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya mja wake na huwa kwa namna ambayo humfanya mhusika kutokuwa na shauku wala hamu ya kuacha kutii au shauku ya kufanya maasi; licha ya kuwa uwezo wa kufanya hivyo anao.” [10]

Asha'irah wametoa fasili na maana ya umaasumu kwamba, ni kutoumbwa dhambi na Mwenyezi Mungu kwa mwanadamu ambaye ni maasumu. [11]

  • Fasili na maana iliyotolewa na wanafalsafa: Wanafalsafa wa Kiislamu. Wametoa maana ya umaasumu kwamba, ni nguvu na uwezo wa kinafsi ambayo kwa uwepo wake, mwenye umaasumu hafanyi dhambi. [12] Ayatullah Sobhani, mfasiri na mwanatheolojia wa zama hizi katika kutoa maana ya umaasumu ametofautisha baina ya dhambi, umaasumu na kutenda kosa na kwa namna fulani amekusanya pamoja fasili na maana ya Adliyah na wanafalsafa. Anasema kuwa, umaasumu (kutotenda dhambi) ni daraja ya juu kabisa ya taqwa (uchajimungu) na ameitambua kuwa ni nguvu ya ndani au uwezo na nguvu ya kinafsi ambayo inamzuia maasumu kutenda dhambi kwa sura mutlaki bali inamzuia hata kufikiria hilo. [13]

Chimbuko la umaasumu

Kuhusiana na chimbuko na chanzo cha umaasumu na sababu ya kinga ya kutotenda dhambi au kufanya makosa, kuna mitazamo tofauti ambayo imebainishwa kuhusiana na hilo ambayo ni kama vile ni ukarimu wa kiungu aliyopatiwa maasumu, elimu maalumu ya maasumu kuhusiana na matokeo ya dhambi na irada na chaguo la maasumu. [14]

Ukarimu wa Kiungu

Sheikh Mufid na Sayyid Murtadha wanasema kuwa, isma (umaasumu) yaani kutotenda dhambi chimbuko lake ni ukarimu na wema wa Kiungu kwa maasumina. [15] Allama Hilli ametaja sababu nne kama chimbuko la wema huu wa Mwenyezi Mungu ambazo ni:

  1. Sifa maalumu za kinafsi au kimwili ambazo hupelekea kujitokeza nguvu ya kujiepusha kutenda dhambi.
  2. Kuwa na elimu kuhusiana na madhara ya dhambi na kufahamu ujira na malipo ya kutii.
  3. Wahyi au ilham kwa Maasumu ambayo inamfanya mtazamo wake kuhusiana na uhakika wa madhambi na kutii kuwa wa kina (msisitizo na uthibitisho wa elimu kupitia Wahyi au ilham).
  4. Kuzingatia karipio la Kiungu kuhusiana na Tark Aula (kufanya bora na kuacha bora zaidi). [16]

Elimu maalumu

Baadhi ya Maulamaa wanasema kuwa, chimbuko la umaasumu (isma) ni elimu na kuwa na uumaizi na utammbuzi maalumu kuhusiana na matokeo ya madhambi na kufahamu kuhusiana na ujira na malipo ya kutii. [17] Allama Tabatabai anaamini kwamba, kutokana na kuwa, Maasumina wana elimu waliyotunukiwa na Mwenyezi Mungu, wana irada na azma imara na madhubuti ambayo kwa kuweko irada kama hiyo, katu hawaelekei upande wa kutenda dhambi. [18] Elimu hii siyo kama elimu nyingine, siyo kitu cha kujifunza na haishindwi na matamanio na nguvu zingine. [19]

Elimu na irada

Muhammad Taqi Misbah Yazdi anasema kuwa, siri ya umaasumu (kutotenda dhambi) na maasumina iko katika viini viwili ambavyo ni kuwa na elimu kuhusiana na hakika ya mambo na ukamilifu na irada yenye nguvu katika kufikia hayo; kwani mwanadamu akiwa jahili na mjinga, hawezi kufahamu ukamilifu wa kweli na ataweka ukamilifu wa khiyali (kufikiria na kubuni akilini) nafasi ya ukamilifu wa kweli na kama hatukuwa na irada ya lazima, mwanadamu huyo hataweza kufikia katika lengo lifaalo. [20] Kwa mtazamo wake ni kwamba, Maasumu kwa kuwa kwake na elimu maalumu na irada thabiti aliyonayo, katu hawezi kufanya dhambi kwa hiari yake na ni mtiifu kwa Mwenyezi Mungu kwa hali yoyote ile. [21]

Umaasumu na hiari

Ali Rabbani Golpeygani, mhakiki na mtafiti wa theolojia wa zama hizi anasema, wasomi na wataalamu wa elimu ya theolojia na wasomi wa wafalsafa wameafikiana kwamba, umaasumu unaoana na kuendana na hiari (kufanya mambo kwa hiari) na kwamba, maasumu ana uwezo wa kufanya maasi. [22] Kwa mujibu wa akili, kama umaasumu unamlazimisha mtu ambaye ni maasumu kutii na kuacha dhambi, katika hali hii hawezi kustahiki kusifiwa na hata kuamrisha na kukataza na ujira na adhabu kwake yeye litakuwa jambo lisilo la kiakili. [23]

Allama Muhammad Hussein Tabatabai ameandika akibainisha kuoana na kukubaliana suala la umaasumu na hiari (umaasumu na kufanya jambo ka hiari ni vitu vinavyooana) ya kwamba: Chimbuko la umaasumu (isma) ni elimu maalumu ambayo Mwenyezi Mungu amewapatia maasumina. Elimu yake msingi wake ni hiari. Kwa muktadha huo, maasumina hawafanyi dhambi kutokana na kuwa na elimu na ufahamu kuhusiana na madhara na mambo mabaya na maslahi ya matendo; kama vile mtu ambaye ana ufahamu na welewa usio na shaka kuhusiana na kwamba, sumu inaua na hivyo katu hawezi kunywa sumu. [24]

Umaasumu wa Mitume

Makala asili: Umaasumu wa Mitume

Umaasumu wa Mitume katika uga wa Wahyi ni katika misingi ya pamoja na ambayo dini zote za mbinguni zinashirikiana na zinaafikiana katika hili; [25] licha ya kuwa kuna hitilafu za kimitazamo kuhusiana na nini na daraja yake miongoni mwa wafuasi wa dini na wanafikra wa madhehebu za Kiislamu. [26]

Wanatheolojia wa Kiislamu wanaafikiana katika vitu vitatu:

  1. Umaasumu (hali ya kutotenda dhambi) Mitume katika shirk na ukafiri kabla na baada ya kutimilizwa na kupewa Utume.
  2. Umaasumu wa Mitume katika kupokea, kulinda, kuhifadhi na kufikisha Wahyi (kwa maana kwamba, hawakosei katika kutekeleza haya).
  3. Umaasumu wa Mitume kunako kutenda dhambi kwa makusudi na kwa kusahau baada ya Utume.


Ama kuhusiana na mambo matatu ambayo wanahitalifiana ni:

  1. Umaasumu wa Mitume katika kutenda dhambi kwa kusahau baada ya Utume.
  2. Umaasumu wa Mitume katika kutenda dhambi kwa makusudi na kwa kusahau kabla ya Utume.
  3. Umaasumu wa Mitume katika maisha ya kijamii na ya kwao ya kibinafsi.

Mashia Imamiyah wanaamini kuwa, Mitume wana umaasumu na kinga ya kutotenda dhambi katika mambo yote yaliyotajwa; bali si hayo tu, bali Mitume wana kinga ya kutotenda kitu chochote ambacho ni chimbuko la chuki na watu kujitenga nao. [27] Kuwafanya watu wawe na imani na Utume wa Mitume ni miongoni mwa hoja za kiakili za wajibu wa umaasumu kwa Mitume; [28] kadhalika kumetumiwa Aya za Qur’an [29] na baadhi ya hadithi [30] kama hoja katika uwanja huu. [31]

Wanaopinga kwamba, Mitume siyo maasumu na kwamba, wanatenda dhambi wamegawa Aya za Qu’ran katika makundi mawili, ambapo wametaja baadhi ya Aya ambazo zinaonyesha kupingana na umaasumu kwa Mitume wote na kundi jingine la Aya ambazo zinaonyesha kutoafikiana na umaasumu wa baadhi ya Mitume na kutumia hizo kama hoja ya upinzani wao. [32] Hata hivyo katika kuwajibu wenye itikadi hii imeelezwa kuwa, Aya hizi ni miongoni mwa Aya za mutashabihat (ambazo zinaweza kuwa na maana nyingine kwa maana kwamba, maana yake haiko wazi tofauti na Aya za muhkamat), ambazo zinapaswa kurejeshwa kwa Aya za Muhkamat, kufanyiwa taawili na tafsiri [33] na kwamba, Aya zote ambazo zinaonekana kutooana au kutoafikiana na umaasumu wa Mitume, zinapaswa kuhesabiwa kuwa zina maana ya tark aula (kufanya jambo bora na kuacha bora zaidi). [34]

Umaasumu wa Maimamu

Makala asili: Umaasumu wa Maimamu

Umaasumu wa Maimamu ni miongoni mwa masharti ya Uimamu katika mtazamo wa Mashia Ithaashariya na ni katika itikadi zao za kimsingi. [35] Kwa mujibu wa nukuu ya Allama Majlisi ni kuwa, Mashia Imamiyah wameafikiana kwamba, Maimamu (a.s) wana kinga na umaasumu wa kutofanya madhambi yote makubwa kwa madogo, iwe ni kwa makusudi au kwa kusahau na si wenye kufanya kosa. [36] Inaelezwa kuwa, Shia Ismailiyah nao wanatambua umaasumu kama sharti la Uimamu. [37] Mkabala na wao kuna Waislamu wa Ahlu-Sunna ambao hawalitambui suala la umaasumu na kinga ya kutotenda dhambi kama ni sharti la Uimamu [38], kwani wao wana ijma'a na kauli moja kwamba, makhalifa watatu (Abu Bakr, Omar na Othman) walikuwa Maimamu; lakini hawakuwa maasumu. [39] Mawahabi nao hawakubaliani na suala la umaasumu wa Imam na Maimamu wa Mashia na wanaamini kwamba, hiyo ni sifa makhsusi kwa Mitume tu. [40]

Kwa mujibu wa Ja'afar Sobhani ni kwamba, sababu zote za kimantiki zilizotolewa kwa ajili ya umaasumu wa Mtume, kama vile kutimia malengo ya Utume na kupata imani ya watu, pia zimejadiliwa katika suala la umaasumu wa Imam. [41]. Ili kuthibitisha umaasumu wa Maimamu (a.s), wanatheolojia wa Shia wametaja Aya na hadithi kadhaa, zikiwemo: Aya ya Ibtilaa Ibrahim, [42] Aya ya Ulul-Amr, [43] Aya ya Tat'hir, [44] na Aya ya Swadiqin, [45], Hadithi ya Thaqalayn, [46] na Hadithi ya Safina. [47].

Kwa mtazamo wa Shia, Bibi Fatima (a.s) ana hadhi ya umaasum.[55] Ili kuthibitisha umaasumu wake, Aya ya Tat'hir na Hadithi ya Bidh-'ah zimetajwa.

Umaasumu wa malaika

Kwa mujibu wa Allama Majlisi, Mashia wana ijma'a na kauli moja ya kwamba, malaika wote wana kinga ya kutotenda dhambi (maasumu) na hawafanyi dhambi yoyote ile kubwa au ndogo. Akthari ya Waislamu wa madhehebu ya Kisuni pia wanaamini hivi. [48] Kuna mitazamo mingine pia iliyobainishwa kuhusiana na kwamba, malaika ni maasumu yaani hawatendi dhambi: Baadhi wanaamini kwamba, malaika sio maasumu na hawana kinga ya kutotenda dhambi. Baadhi ya watu wameziona hoja za wafuasi na wapinzani wa umaasumu kuwa hazitoshi na wamesimama hapo katika uwanja huu. Kundi fulani pia linaowaona malaika wanaobeba wahyi na malaika wenye daraja ya juu na baadhi ya malaika wa mbinguni (mkabala na malaika wa ardhini) kuwa ni maasumu. [49]

Wanaofiki suala la umaasumu wanasema, Aya 27 ya Surat al-Anbiya [50] na Aya ya 6 ya Surat al-Tahrim [51] na hadithi nyingi [51] zinaonyesha kuwa, malaika wana isma (umaasumu). [52] Inaelezwa kuwa, kundi pekee miongoni mwa makundi ya Kiislamu linalokataa na kupinga umaasumu wa malaika ni Hashawiyah. [53]

Ayatullah Makarem Shirazi akijibu mtazamo kwamba, umaasumu kwa malaika hauna maana anasema, licha ya kuwa msukumo wa kutenda dhambi, kama vile matamanio na hasira ni vitu ambavyo havipo kwa malaika au ni dhaifu sana, lakini wana hiari ya matendo na wana nguvu ya kupinga.

Ishkali na majibu

Kuna waliohoji na kutilia ishkali na alama ya swali miongonii mwa wanaokana na kupinga umaasumu ambapo baadhi ya hizo ishkali ni:

  • Umaasumu hauendani na maumbile ya kibinadamu

Ahmad Amin, mwandishi wa zama hizi wa Kimisri anasema kuwa, umaasumu (kutotenda dhambi) ni suala ambalo halioani na kwenda sambamba na maumbile ya mwanadamu; kwani kimsingi mwanadamuu ana nguvu mbalimbali za kimatamanio na za kinafsi. Mwanadamu kama ambavyo ana hali ya kuelekea upande wa mambo mazuri, kadhalika ana hali ya kuelekea upande wa mambo mabaya. Kama hali hizo zitaondolewa kwa mwanadamu, itakuwa kama vile amepokonywa hali yake ya ubinadamu. Kwa msingi huo, hakuna mtu ambaye amesalimika na maasi hata Mitume (a.s). [54]

Ayatollah Jawad Amoli katika kujibu ishkali hii sambamba na kuashiria johari na kiini cha mwandamu ambacho ni nafsi yake anasema kuwa, johari ya mwanadamu imeumbnwa kwa namna ambayo ina uwezo wa kukwea kuelea katika kilele cha umaasumu na hali ya kutotenda dhambi; kwani nafsi ya mwanadamu katika hali yake ya kupanda juu, inapata uwezo wa kuwa na kinga ya kusahau, mghafala na ujahili. Kwa mtazamo wake ni kwamba, kama nafsi ya mtu itafika katika hatua ya akili asili na daraja inayojulikana kama upeo wa hali ya juu na sahihi, katika hali hii itakuwa ni yenye kudiriki haki na hakika tu, na itasalimika na hali yoyote ile ya shaka, kusitasita, kusahau na mghafala. Kwa msingi huo, mtu kama huyu atavuka katika ulimwengu wa maada, dhana na kufikiria (kuweka taswira) na kufika katika chemchemi ya uhakika. Katika hali hii anapata uwezekano wa kuwa na hali ya umaasumu. [55]

  • Chimbuko la fikra ya umaasumu

Kwa mtazamo wa baadhi ya watu, fikra ya umaasumu haikuweko katika vyanzo vya awali vya Kiislamu na kwamba, hii ni bidaa na uzushi ambao umeingizwa katika mafundisho ya Uislamu na Ahlul-Kitab, Iran ya kale, usufi au mafundisho ya Kizartoshti. [56]

Imeelezwa katika kujibu hili kwamba, kuwa na itikadi ya umaasumu wa Mitume ni jambo ambalo lilikuwa limeenea mwanzoni mwa Uislamu baina ya Waislamu na lina mizizi katika mafundisho ya Qur'an na Mtume wa Uislamu. [57] Ahlul-Kitabu hawawezi kuwa chimbuko la umaasumu; kwa sababu Torati imewanasibisha Mitume na madhambi mabaya kabisa. [58] Katika hali ambayo usufi haukuwa umeibuka na kujitokeza, fikra ya umaasumu ilikuwa imeenea baina ya Mashia. Kwa msingi huo, usufi nao hauwezi kuwa ndio chimbuko na chanzo cha fikra ya umaasumu. [59] hata tukijaalia kwamba, kuna mashirikiano ya mafundisho ya umaasumu baina ya Uislamu na uzartoshti, hiyo haina maana ya kuathiriana baina ya dini hizi; bali hilo ni kwa sababu Johari na kini cha dini zote za Mwenyezi Mungu kinashhirikiana na kina hali ya kuafikiana na kuoana katika misingi yake. [60]

Bibliografia

Kumeandikwa vitabu mbalimbali kuhusiana na isma (umaasumu); na miongoni mwavyo ni:


Kitabu "kutotenda dhambi kutoka kwa mtazamo wa sunni na shia", na Sayyied Ali Hosseini Milani
  • Al-Tanbiyah al-Maalum; al-Burhan alaa tanzih al-Masum al al-Sahw wal-Nisyan, mwandishi: Sheikh Hurr al-Amili
  • Ismat az manzar Fariqayn (Shia na Ahlu-Sunna), mwandishi: Sayyid Ali Husseini Milani.
  • Ismat az didgah Shieh va Ahle Tasanun, mwandishi: Fatime Mohaqqeq.
  • Manshae Esmat az Gonah va Khata; nazariha va didgaha, mwandishi: Abdul-Hussein Kafi.
  • Esmat zarurat va aasar, mwandishi: Sayyid Mussa Hashimi Tonekaboni.
  • Pezhuheshi dar Esmat Maasuuman (a.s), waandishi: Ahmad Hussein Sharifi na Hassan Yusufiyan.