Arshi

Kutoka wikishia

Arshi (Kiarabu: العَرش) (kiti cha enzi) ni istilahi ya Kiqur'an ambayo ina maana ya kiti cha enzi ambacho kinanasibishwa na Mwenyezi Mungu. Imekuja katika baadhi ya Aya za Qur'an tukufu ya kwamba, Mwenyezi Mungu aliyetawala katika kiti cha enzi ambapo wanazuoni wa Kiislamu wametofautiana katika tafsiri ya Aya kama hizi. Baadhi ya kundi la wanazuoni wa Waislamu wa Ahlu-sunna kama Ashairah na Ahlul-Hadith wanasema kuwa, haipaswi kufanya tafakuri katika Aya hizi, bali kinachopaswa ni kuziamini tu kama zilivyo.

Kundi la wanaotazama mambo kwa dhahiri yake na al-Hashwiyyah wanaamini kwamba, arshi ndio kilekile kiti cha kimaada na kwamba, Mwenyezi Mungu ana kiti kikubwa ambacho hukaa juu yake na kuiongoza dunia. Waislamu wa madhehebu ya Shia na kundi la Mu'tazilah wao wanaamini kwamba, Aya hizi zinatoa mshabaha na hali ya ushabihishaji tu. Baadhi yao wamefasiri arshi kwa maana ya elimu ya Mwenyezi Mungu isiyo na kikomo.

Allama Muhammad Hussein Tabatabai, mwanazuoni wa Kishia na mwandishi wa kitabu cha Tafsir al-Mizan ameitaja arshi kuwa ni hatua iliyokamilika ya ulimwengu wa uwepo na mahali pa kutolea amri na maagizo ya Mwenyezi Muungu na kwamba, kukaa Mwenyezi Muungu juu ya kiti cha enzi ni kinaya ya tadibiri ya ulimwengu na elimu yake katika mambo yote.


Utambuzi wa maana matumizi ya Qur'an

Arshi katika lugha ina maana ya "kiti cha mfalme" au kitu ambacho kina kizuizi na kifuniko kwa juu. [1] Neno arshi (kiti cha enzi) limenasibishwa mara 21 na Mwenyezi Mungu katika Aya mbalimbali za Qur'an tukufu. [2] Aya ya 129 ya Surat al-Tawba inaashiria adhama ya arshi yya Mwenyezi Mungu. Aya hiyo inasema: Na Yeye ndiye Mola Mlezi wa Kiti Kikuu cha Enzi. [3]

Katika Aya kadhaa za Qur'an tukufu kumezungumziwa suala la Mwenyezi Mungu aliyetawala katika kiti cha enzi, [4] katika Aya zingine wametajwa Malaika ambao wamekizunguka kiti cha enzi na wakiwa wanamsabihi Mwenyezi Mungu. Moja ya Aya hizo inasema: Na utawaona Malaika wakizunguka pembeni mwa Kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu, wakimtakasa na kumsifu Mola wao Mlezi. Na patahukumiwa baina yao kwa haki na patasemwa: Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote! [5] au wabebaji wa arshi. [6].

Katika ya Aya 7 ya Surat Hud pia imekuja kwamba, kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu kiko juu ya maji. [7] Aya hiyo inasema: Na Yeye ndiye aliye ziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Na Kiti chake cha Enzi kilikuwa juu ya maji, ili akufanyieni mtihani ajulikane ni nani miongoni mwenu mzuri zaidi wa vitendo.

Sifa maalumu za kiti cha enzi katika hadithi

Kuna hadithi mbalimbali zilizopokewa ambazo zinazungumzia arshi (kiti cha enzi); miongoni mwanzo ni kuwa, malaika wa karibu na Mwenyezi Mungu wanakikeba kiti cha enzi na kuna mfano wa viumbe wote wa dunia katika arshi hiyo [8] au kwamba, ibara hii: «لا اله الّا اللّه، مُحَمَّدٌ رَسول‌اللّه، علیٌ امیرالمؤمنین»; Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, Muhammad (s.a.w.w) ni mjumbe wa Allah na Ali ni Amirul-Muuminina", imeandikwa juu ya arshi. [10]

Inaelezwa katika hadithi iliyopokewa kutoka kwa Mtume (s.a.w.w) ya kwamba: Katika safari ya Mi'raj wakati nilipokuwa nikiangalia arshi, nilikuwa nikiona Maasumina wote wapo upande wa kulia wa arshi. [11] Katika baadhi ya hadithi imekuja pia kwamba, arshi (kiti cha enzi) ni kubwa kuliko kiti (kursiyu). [15] Mwenyezi Mugu ameumba arshi kutokana na nuru na hakuna kiumbe ambaye anaweza kuiangalia. [16]

Mitazamo tofauti kuhusiana na arshi

Aya za Qur'an zinazohusiana na arshi (kiti cha enzi) na kursiyu (kiti) ni miongoni mwa Aya za mutashabihat (Aya ambazo kuna uwezekana kuwa na maana kadhaa) na wanazuoni wa Kiislamu wana nadharia nyingi na mitazamo tofauti. [17] Baadhi ya mitazamo hiyo ni kama ifuatavyo:

Kutokuwa wazi maana ya arshi

Mtazamo wa baadhi ya makundi miongoni mwa makundi ya Ahlu-Sunna kama Ashairah na Ahlul-Hadith wanaamini kwamba, haipaswi kufanya tafakuri katika Aya hizi, bali kinachopaswa ni kuziamini tu kama zilivyo, yaani watu wajiepushe na suala la kuzitafakari. [18] Wanasema kuwa, kwa mujibu wa Qur'an, Mwenyezi Mungu yuko katika arshi; lakini kivipi, hilo ni jambo ambalo kwetu haliko wazi. [19] Kwa mfano Malik ibn Anas anasema kuhusiana na maana ya kukaa Mwenyezi Munguu katika arshi (kiti cha enzi): Maana ya kukaa iko wazi na bayana; lakini kivipi amekaa, hilo ni jambo ambalo kwetu haliwezakani kufahamika, na kuuliza kuhusiana na hilo ni bidaa na kuamini hilo ni wajibu." [20]

Arshi kuwa ni ya kimaada na kimahali

Watu wanaotazama mambo kidhahiri na al-Hashwiyyah, wamefahamu maana ya arshi kama ilivyo dhahiri yake na wakaitambua arshi kuwa ni kile kile kiti cha kimaada. Wanaamini kwamba, Mwenyezi Mungu ana arshi kubwa (kiti cha enzi) ambayo anakaa juu yake na anauongoza ulimwengu. [21] Kadhalika wanasema kuwa, arshi ina upana wa vidole vinne katika pande zake nne na chini ya Mungu kunatoka sauti kama ngurumo ya chuma. [22]

Maana ya arshi ni ufananishaji

Mu'tazilah na baadhi ya wafasiri wa Qur'an wa Kishia wanaamini kwamba, hakuna kitu cha kuonekana kinachofahamika kwa jina la arshi (kiti cha enzi), na arshi ya Mwenyezi Mungu inayozuungumziwa ni kinaya na mfananisho wa mambo mengine. [23] Hata hivyo kinaya hii ni nini? Kuna tofauti za kimitazamo kuhusiana na hili: Baadhi wanasema, kursiyu (kiti) ni kinaya ya ulimwengu wa kimaada, na arshi (kiti cha enzi) ni kinaya ya ulimwengu wa zaidi ya maada. [24] Sheikh Swaduq, amefasiri arshi kwa maana ya elimu ya Mwenyezi Mungu isiyo na kikomo. [25] Baadhi ya wengine wamesema, arshi ni kinaya ya utawala, uongozi, mamlaka na umiliki. [26]

Allama Tabatabai, mwanazuoni wa Kishia na mwandishi wa kitabu cha Tafsir al-Mizan ameitaja arshi kuwa ni hatua iliyokamilika ya ulimwengu wa uwepo na mahali pa kutolea amri na maagizo ya Mwenyezi Mungu na kwamba, kukaa Mwenyezi Mungu juu ya kiti cha enzi ni kinaya ya tadbiri ya ulimwengu na elimu yake katika mambo yote. [27]

Arshi katika dini zingine

Arshi ya Mwenyezi Mungu inazungumziwa pia katika dini zingine. Kwa mfano imekuja katika kitabu kitakatifu kwamba, usiape kwa mbingu; kwani mbingu ndio ile arshi ya Mwenyezi Mungu. [28] Aidha imetajwa kuwa ni kiti ambacho kina taa na Mwenyezi Mungu amekaa juu yake. [29] Katika sehemu nyingine ya kitabu hiki, wametajwa malaika ambao wamekaa katika kitanda (arshi) cha Mwenyezi Mungu. [30].


Vyanzo

  • Ahmadi, Jamal wa Akhariin, “Andisheh Kalami Sanayi Darbara Arsh,” dar nashreh daneshghah ba'hanr Karman, No. 22, Winter 1386 H, S.
  • Bayat Mokhtari, Mahdi, “Arsh khodah wa tafaut on ba kursy”, Majale tahqiq ulumy al-Qur'an wa hadith fi jamiat Al-Zahra, No. 2, 1390 H, S.
  • Jafari, Yaqoub, "Maarif Qur'an diidghaha dar'bareye arsh khodah" Dar mjaleh darsihaye az maktab islamy, No. 615, Murdad 1391 H.
  • Majmuat muhaqiqin, "Ayat arsh wa kursy", Dar Farahnge ulumi Qur'ani, Qom, Pazhohesh ulumi farhang islami, vabaste be daftar tablighat islami hawze ilmy Qom, Chapa aval, 1394 H.
  • Khoramshahi, Bahau al-Din, “Arsh” Dar danesh'name Qur'an wa Qur'an pezhohesh, Tehran, Nashr dostan-nahiid, chapa aval, 1377 H.
  • Dah'khoda, Ali Akbar, Lughat'name Dah'khoda, Tehran, Muasase lughat'name Dah'khoda, 1341 H.
  • Rostamy, Muhammad Zaman wa twahire aali-buweih, Sire dar israr farhangan ba ruwyekridy Qur'ani wa irafani, Qom, Pazhohesh ulumi farhang islami, 1393 H.
  • Swaduq, Muhammad bin Ali, Maani al-akhbar, Tarjumme Abdul-Ali Muhammadi Shahruvady, Tehran, Dar al-kutub al-islami, 1377 H.
  • Tabatabai, Muhammad Hussein, Al-Mizan fi Tafsiril-Qur’an, Qom, Intisharat jamiat al-madrasein, 1417 H.
  • Majlisi, Muhammad Baqer, Bihar Al-Anwar al-jamiu lidarar akhbar al-Aimat al-at'har, Beirut, Muasase al-wafaa, 1403 AH.
  • Ma'rifat, Muhammad Hadi, Tamheed fi ulumy al-Qur'ani, juzuu 3, Qom, Muasase al-nashr islamy, 1416 AH.
  • Makarim Shirazi, Nasir, Tafsir Namuneh, Tehran, Dar Al-Kutub Al-Islamiyyah, 1369 H, S.