Tukio la Karbala

Kutoka wikishia
Mchoro wa zamani ukionesha tukio la Karbala

Tukio la Karbala au tukio la Ashura (Kiarabu: واقعة کربلا أو واقعة عاشوراء) ni tukio la vita vya jeshi la Kufa dhidi ya Imamu Hussein (a.s) na masahaba zake huko Karbala. Tukio la Karbala lilitokea tarehe 10 Muharram mwaka wa 61 Hijiria, baada ya Imamu Hussein (a.s) kukataa kutoa kiapo cha utiifu cha kutawadhisha Yazid bin Muawiah kushika nafasi ya ukhalifa. Jambo hilo ndilo lililopelekea kuuawa shahidi Imamu na masahaba zake, kisha kutekwa kwa familia yake baada ya vita hivyo.

Tukio la Karbala linachukuliwa kuwa ni tukio la kuhuzunisha zaidi katika historia ya Uislamu. Kulingana na umuhimu wa tukio hilo, Mashia huadhimisha maombolezo makubwa zaidi kuliko mengine yote katika kumbukumbu ya kila mwaka ya tukio huilo adhimu.

Vuguvugu la tukio la Karbala lilianza baada tu ya kifo cha Muawia bin Abi Sufian kilichotokea mnamo mwezi 15 Rajabu ya mwaka wa 60 Hijiria. Huo ulikuwa ndio mwanzo wa utawala wa mtoto wa Muawia (Yazid). Kwa maana hiyo; tukio la karbala litakuwa lianzia baada ya kifo cha Muawia na kumalizika baada ya mateka wa Karbala kurudi Madina. Mtawala wa Madina alichukuwa juhuidi kubwa za kupata kiapo cha utiifu cha kumtawazisha Yazid kutoka kwa Imamu Hussein (a.s). Ili Imamu Hussein aepukane na shinikizo hilo la kiongozi wa Madina, aliamua aliondoka usiku kutoka mji wa Madina na akaelekea Makka. Katika safari hiyo, Imamu Hussein alifungamana na familia yake, idadi kadhaa ya Bani Hashimu na baadhi ya Mashia (wafuasi) wake.

Imamu Hussein (a.s) alikaa Makka kwa takriban miezi minne. Wakati huu aliokupo katika mji huo, alipokea barua za maombi -ya kumwita nakumtaka awe ni kiongozi wao- kutoka kwa watu wa Kufa. Ili kupeleleza na kuelewa na kuhakikisha ukweli kuhusiana na maaandishi yaliomo ndani barua hizo, Imamu (a.s) alimtuma Muslim bin Aqiil kwenda Kufa na Sulaiman bin Razin kwenda Basra. Kutokana na kuwepo uwezekano wa kuuawa kwa Imamu Hussein (a.s) huko Makka kupitia mkono wa mawakala wa Yazid, pamoja na kuepo wito wa maombi wa watu wa mji wa Makufi na uthibitisho kutoka kwa mjumbe wa Imamu kwamba mwaliko wa watu wa Kufa ulikuwa ni sahihi, Imamu Hussein (a.s) aliamua kuondoka mjini Makka na kuelekea Kufa mnamo tarehe 8 Dhul-Hijjah.

Kabla ya Imamu Hussein (a.s) kufika Kufa, alikuwa tayari amesha pata habari kuhusu khiana za watu wa Kufa, na baada ya kukutana na jeshi la Hur bin Yazid Riahi, Imamu aliuelekeza msafara wake Karbala, ambako alikabiliana na jeshi la Umar bin Sa'ad, jeshi ambalo lilitumwa na Ubaidullah bin Ziad dhidi ya Imamu Hussein (a.s). Majeshi mawili hayo yalipambana mwezi 10 Muharram, siku ambayo inajulikana kama ni siku ya Ashura. Baada ya Imamu Hussein (a.s) na masahaba zake kuuawa mashahidi, jeshi la Omar bin Sa'ad liilikanyaga na kuiponda miili yao kwa farasi. Wakati wa jioni ya siku ya Ashura, jeshi la Yazid lilishambulia mahema ya Imamu Hussein (a.s) na kuyachoma moto, kisha kuwachukua mateka wale walionusurika katika vita hivyo. Miongoni mwa mateka hao ni; Imam Sajjad (a.s), ambaye hakupigana katika vita hivyo kutokana na maradhi, pamoja na bibi Zainab (a.s). Askari wa Omar bin Sa'ad walivichomeka vichwa vya mashahidi kwenye ncha za mikuki na kumfikishia Obaidullah bin Ziad vichwa hivyo pamoja na mateka wa vita hivyo huko mji wa Kufa, na hatimae wakampelekea Yazidi huko huko Syria. Miili ya mashahidi wa Karbala ilizikwa usiku na watu kupitia kabila la Bani Asad baada ya jeshi la Omar Saad kuondoka katika eneo hilo la Karbala.

Nafasi na umuhimu wake

Tukio la Karbala ni moja ya matukio ya karne ya kwanza ya Hijiria ambapo Hussein bin Ali (a.s), mjukuu wa Mtume (s.a.w.w) na Imamu wa tatu wa Mashia, yeye pamoja na idadi ya masahaba zake waliuawa shahidi huko Karbala kwa amri ya Yazid bin Muawia kisha wanawake na watoto wao wakachukuliwa mateka. [1] Tukio hili linachukuliwa kuwa ni tukio la kuhuzunisha zaidi katika historia ya Uislamu [chanzo kinahitajika] na ndio tokeo msingi la msimamo dhidi ya Bani Umayya [2] Kwa mujibu wa baadhi ya watafiti, tukio hili liliwazuia Bani Umayya kupotosha dini ya Uislamu na Sunnah za bwana Mtume (s.a.w.w) [3] Shahidi Motahari anaamini ya kwamba; Miongoni mwa matukio mengi ya kihistoriani kuna matukio machache yenye riwaya za kweli, na kiwango madhubuti kinazoaminiki kama tukio la Karbala. Kwa mujibu wa imani yake, hakuna tukio hata moja katika historia - hasa katika hstoria za mbali kama vile, za karne kumi na tatu au kumi na nne zilizopita - lenye mashiko na ithibati sahihi kama tukio la Karbala. Na hata wanahistoria wa Kiislamu wenye itibari zaidi na wanaoaminika kutoka karne ya kwanza na ya pili wamesimulia kadhia za tukio hilo kupitia ithibati na bayana madhubuti, na maelezo ya nukuu zao ni yenye kuwafikiana na kukaribiana kwa kiasi kikubwa. [4] Mashia kila mwaka huomboleza tukio hili. Pia kuna kazi nyingi za sanaa na maandishi kuhusiana na tukio la Karbala.

Imamu Hussein kugoma kutoa kiapo cha utiifu kwa Yazid

Muawia katika uhai wake alifanya juhudi kubwa kwa ajili ya mwanawe, [5] jambo ambalo lilileta tija kwa Yazid daada ya kifo cha Muawiya (kilichotokea mnamo mwezi 15 Rajab mwaka wa 60 Hijiria), ambapo kwa kutokana na juhudi hizo, watu kadhaa walimuunga mkono Yazid kwa kumpa kiapo cha utiifu baada ya kifo hicho cha baba yake.[6] Bila shaka, kwa mujibu wa makubaliano ya amani kati ya Muawiah na Imam Hassan (a.s), Muawiah hakuwa na haki ya kuteua mrithi wa kushika nafasi ya ukhalifa baada yake. [7] Kutokana na ukweli huo, Yazidi baada ya kifo cha baba yake aliazimia kuchukua kiapo cha utiifu kutoka kwa wakuu wa Waislamu waliokataa wito wa Muawia wa kumpa kiapo cha utiifu mwanawe. [8] Ili kutimiza azimio lake, Yazid aliamua kumwandikia barua Walid bin Utbah (mtwala wa Madina wawakati huo), na kumtaka achukue kiapo cha utiifu kwa mabavu kutoka kwa; Hussein bin Ali, Abdullah bin Omar, Abdul Rahman bin Abi Bakar na Abdullah bin Zubeir. Yazid katika barua yake hiyo alimuamuru Walid bin 'Utba kumkata kichwa yeyote yule atakayekataa kutoa kiapo hicho miongoni mwao. Kwa mara ya pili Yazid alimwandikia Walid bin 'Utba barua nyengine na kumwamuru amwandikie barua ya orodha ya majina ya wanaomuunga mkono na wanaopingana naye, na aambatanishe kichwa cha Hussein bin Ali pamoja na majibu ya barua yake hiyo. [10] Walidi akashauriana na Marwani bin Hakam kuhusiana na matakwa hayo, [11] kisha akawamtuma Abdullahi bin Amru, Ibnu Zubair, Abdullah Ibn Omar na Abd al-Rahman Ibn Abi Bakar waende kwa Imamu Hussein (a.s). [12]

Imamu Hussein (a.s) alikwenda Daru al-Marah (ikulu) huko Madina akiwa na watu thelathini [13] wa karibu yake. [14] Walid alimjuza Imamu Hussein (a.s) kuhusiana na tukio la kifo cha Muawia, kisha akamsomea barua ya Yazid, inayomtaka Walid kuchukua kiapo cha utiifi kutoka kwa Husein bin Ali (a.s). Husein (a.s) akamwambia Walid: "Nadhani lengo lako ni kwamba; mimi nitoe kiapo hichco cha utiifu mbele ya watu." Waleed akajibu: “Bila shaka hayo ndio maoni yangu.” [15] Imam (a.s) akamjibu kwa kumwambia: “Basi nipe muda hadi kesho ili nifikirie kisha nikujulishe maoni yangu.” [16] Ilipofika wakati wa jioni wa siku iliyofuata; Mtawala wa Madina akawatuma maafisa wake wamfuate Hussein (a.s) nyumbani kwake ili wakachukue jibu lake. [17] Hussein (a.s) akaomba aengezewe muda na asubiriwe hadi asubuhi, Walidi akakubali kumpa muhula wa usiku ule hadi asubuhi.[18] Ilipofikia asubiuhi, Imamu Hussein (a.s) akaamua kuondoka Madina. [19]

Kuondoka kwa Imamu Hussein kutoka Mji wa Madina

Takribani kabla ya siku mbili ya kumalizika mwezi wa Rajab, na kwa mujibu wa riwaya nyingine, mwezi tatu Sha'ban, mwaka wa 60 Hijiria [20], Imamu Hussein (a.s) aliondoka Madina yeye pamoja na watu 84 wa familia ya Ahlul Bait, na masahaba zake kuelekea Makka. [21] Kulingana na kauli ya Ibu 'Atham; Kabla ya Imamu Hussein kuondoka Madina, kwanza alikwenda kwenye kaburi la Mtume (s.a.w.w), la bibi Fatima (a.s) na kwenye kaburi la kaka yake (Imamu Hassan (a.s)), na baada ya kuagana nao, ndipo alipoondoka mjini Madina. [22] Imamu Hussein (a.s) alifungama na wengi miongoni mwa watu wa karibu yake katika msafara wa kuondoka kwake Madina. Ukiachana Muhammad Hanafia, ambaye hakufungamana na Imamu Hussein (a.s) katika msafara huo (kutokana na ugonjwa wake), yeye alifungamana na watoto wake, ndugu zake wa kiume, ndugu zake kike pamoja na wapwa zake. [24] Mbali na familia ya Bani Hashim, pia kulikuwa na masahaba wa Imamu Hussein (a.s) ishirini na mmoja waliofungamana naye katika safari yake hiyo. [25]

Baada ya Muhammad bin Hanafia kupata taarifa kuhusu safari ya, kaka yake (Imamu Hussein) (a.s), alikwenda kwake kumuaga na Imamu Hussein (a.s) alimwandikia wasia, unaosema:


إنّی لَم اَخْرج أشِراً و لا بَطِراً و لا مُفْسِداً و لا ظالِماً وَ إنّما خَرجْتُ لِطلبِ الإصلاح فی اُمّةِ جَدّی اُریدُ أنْ آمُرَ بالمَعْروفِ و أنْهی عن المُنکَرِ و أسیرَ بِسیرةِ جدّی و سیرةِ أبی علی بن أبی طالب



Kwa hakika, sikusimama (dhidi ya Yazid) kwa nia uovu, au kutokujuwa shukura, na wala si kwa nia ya ufisadi au nia ya dhulumu, bali nimesimama kwa ajili kutafuta mageuzi ya kuurekebisha umma wa babu yangu. Maimamo wangu ni kwa ajili ya kuamrisha mema na kukataza mabaya, ni kwa ajili ya kuurudisha umma kwenye nyenendo na msingi wa babu yangu na baba yangu Ali bin Abi Talib (a.s). [26]


Ramani ya njia ya msafara wa Imam Hussein (a.s) kutoka Madina kwenda Makka na kutoka Makka hadi Karbala

Imamu Husein (a.s) aliondoka Madina pamoja na masahaba zake, na kinyume na matakwa ya jamaa zake, yeye alishika njia kuu ya kuelekea Makka. [27] Wakiwa njiani kuelekea Makka, Imamu Hussein (a.s) alikutana na Abdullah bin Muti'i, naye kamuuliza anapoelekea Imamu Hussein (a.s). Imamu (a.s) akasema: "Hihi sasa ninaelekea Makka, na nikifika huko, nitamwomba Mungu kheri juu ya safari itakayofuatia baada ya hapo. Abdullah bin Muti'i akamtahadharisha Imamu Hussein (a.s) dhidi ya watu wa Kufa na kumshauri abaki Makka. [28]

Imamu Hussein (a.s) aliwasili Makka mwezi 3 Shabani mwaka wa 60 Hijiria [29] na akakaribishwa na watu wa Makka pamoja na mahujaji. [30] Njia ya msafara wa Imamu Hussein (a.s) kutoka Madina kwenda Makka ilipitia vituo vifuatavyo: Dhu l-Hulayfa, Milal, Sayyala, 'Irqu Dhabyin, Zawhaa, Anaya, 'Araj, Lahr Jamal, Suqyaa, Abwaa, Harsha, Raabigh, Juhfa, Qadiid, Khaliis, 'Usfaan na Murru Al-Dhuhrani. [31]

Imam Hussein kuwasili Makka

Imamu Hussein (a.s) alikaa Makka kwa zaidi ya miezi minne kuanzia (mwezi 3 Shaaban hadi mwezi 8 Dhul-Hijjah). Katika kipindi alichoko katika mji huo, wakazi wa Makka walikuwa na kawaida ya wakimtembelea mara kwa mara. Inasemekana kwamba Abdullah bin Zubeir hakuwa akifurahia hali hiyo ya waku kufanya mahusiano ya karibu na Imamu Hussein (a.s). Abdu llahi bin Zubeir alikuwa na tamaa ya kupata kiapo cha utiifu kutoka wa wakaazi wa mji wa Makka, ila alielewa fika ya kwamba; uwepo wa Imamu Hussein katika mji huo, ni kizingiti kikubwa cha kufikia matakwa yake. Katu watu wa Makka hawakuwa tayari kumuacha Imamu Hussein na kumpa kiapo Abdullahi bin Zubeir, jambo ambalo lilikuwa likimsononesha mno Ibnu Zubeir. [32]

Barua za mwaliko watu wa Kufa kwa Imam Hussein (a.s)

Makala Asili: Barua za watu wa Kufa kwa Imamu Hussein (a.s)

Wakati Imamu Hussein alipokuwa Makkah, Mashia wa Iraq walielewa ya kwamba Imam Husein (a.s) hakumpa Yazid bin Muawiyah kiapo cha utiifu cha kumtawaza kama ni khalifa wa Waislamu. Kwa hiyo, walikusanyika kwenye nyumba ya Suleiman bin Suradi Khuzai na kumwandikia barua Imamu na kumtaka aende mji wa Kufa. [33] Siku mbili baada ya kutuma barua hiyo, wakatuma tena barua 150 nyengine kwa Imamu Hussein (a.s), kila barua moja kati yake ilikiwa na sahihi ya mtu mmoja hadi wanne. [34] Husein bin Ali (a.s) alikaa kimya bila kujibu barua hizo, hadi mmiminiko wa barua kutoka kwa watu hao wa mji wa Kufa ukafurutu ada, baada ya kufikia hali hiyo, Imamu Hussein (a.s) akawaandikia barua yenye ujumbe ufuatao:

...Mimi ninamtuma ndugu yangu ambaye ni binamu yangu naye ni mtu ninayemwamini kati ya watu wa nyumbani kwangu (familia yangu). Nimemwambia anijulishe kuhusiana hali halisi ilivyo, harakati zenu pamoja na itikadi zenu. Ikiwa ataniandikia kwamba; uhakika wa hali zenu unaendana sawa na maandishi ya barua zenu, basi bila shaka Mungu akipenda nitakuja mjini kwenu...-Eleweni ya kwamba- Imamu ni mtu atendaye kulingana na kitabu cha Mwenyezi Mungu tu, anayetekeleza uadilifu, anayeamini dini ya haki, na anayejitolea kwa ajili Mungu.

Muslim bin Aqiil kutumwa Mji wa Kufa

Imamu Husein (a.s) alimpa barua Muslim bin Aqiil, binamu yake, aende Iraq akachunguze hali ilivyo katika mji huo kisha amjulishe hali halisis ilivyo.” [36] Baada ya kufika katika mji wa Kufa, Muslim ima alikaa katika nyumba ya Mukhtar bin Abi 'Ubaid Thaqafiy, [37] au nyumba ya Muslim bin Ausajah. [38] Mashia wakawa wanakwenda kukutana naye katika mahala alipofikia, naye akawa anawasomea ujumbe ulioko katika barua hiyo. [39] Katika hali hiyo, Muslim awaka anachukua kiapo cha utiifu kwa ajili ya Imamu Husein (a.s) kutoka kwa watu mbali mbali. [40] Katika mji huo wa Kufa, Muslim bin 'Aqiil aliweza kupata kiasi cha viapo 12,000 [41] au 18,000. [42] Ila kwa mujibu wa nukuu nyengine, Muslim aliweza kukusanya zaidi ya watu 30,000 [43] na kuchukua viapo vya utiifu kwa ajili ya Imamu Hussein (a.s) kutoka kwao. Muslim alimwandikia barua Imamu Hussein na kuthibitisha kuwepo idadi kubwa ya watu walitoa ahadi ya utiifu na akamtaka Imamu Hussein aende katika mji huo wa Kufa. [44]

Yazid, aliposikia habari za kiapo cha utiifu cha watu wa Kufa kupitia Muslim na pia muala nyororo alioupata kutoka kwa Numan bin Bashir (mtawala wa Kufa wakati huo), aliamua kumteua Ubaidullah bin Ziad, ambaye alikuwa ni mtawala wa Basra wakati huo, ili aje kutawala watu wa mji wa Kufa. [45] Baada ya Ibnu Ziad kuingia mjini Kufa, alianza kuwasaka waliotoa kiapo cha utiifu kwa Imamu Hussein (a.s), na kuwatisha wakuu wa makabila wa mji huo. [46] Ripoti za historia zinaeleza juu ya hofu ya watu kutokana na propaganda za Ubaidullah, khofu ambayo iliwafnya watawanyike kwa haraka mno na kuachana na Muslim bin 'Aqiil, hadi ikafikia hali ya Muslim kuachwa peke yake akiwa hana maha pa kulala. [47] Hali hiyo ya iliendelea hatimaye baada ya mzozo fulani, alijisalimisha kupitia barua ya amani ya Muhammad bin Ash'ath [48] na kupelekwa ikulu. Ila Ibnu Ziad akaidharau na kuitupilia mbali barua ya amani ya Ibnu Ash'ath, kisha akaamuru wafuasi wake kumkata kichwa Muslim bin 'Aqiil. [49]

Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti za kihistoria, Muslim, ambaye alikuwa na wasiwasi kuhusu Imamu Husein (a.s), alimuusia Omar bin Sa'ad, ambaye anatokana na kabila la Quraishi, kumtuma mtu kwa Imam na kumkataza Imamu Hussein asiende katika mji huo wa Kufa. [50] Omar bin Sa'ad naye akamtuma kuufikisha ujumbe wa Muslim kwa Imamu Hussein katika kituo cha makazi kilichokuwa kikijulikana kwa jina la Zubaala. [51]

Safari ya Imamu Hussein (a.s) kuelekea mji wa Kufa

Imamu Husein (a.s) aliondoka Makka kwenda Kufa mnamo siku ya nane ya Dhul-Hijjah [52] siku ambayo Muslim alisimama kwa ajili ya Hussein (a.s) mjini humo akiwa pamoja na watu 82, [53] ambao 60 kati yao walikuwa ni Mashia watoka mji huo Kufa. [54]

Kwa mujibu wa maelezo ya Sheikh Mufid, Imamu Hussein (a.s) alisimamisha hijja yake bila ya kuikamilisha ili aondoke haraka mjini Makka. Hivyo basi aliamua kuibadili nia yake kutoka hijja na kwenda ibada ya Umra ya mufrad kisha akavua ihram. [55] Hata hivyo kutokana na ushahidi wa kihistoria na simulizi kadhaa, kuna baadhi ya watafiti waliosema kwamba; Tokea mwanzo Imamu Husein alikusudia kufanya ibada ya umra, na baada ya kumaliza ibada yake hiyo, aliondoka mjini Makka. [56]

Katika mwezi wa mwisho ambao Imamu Hussein (a.s) alikaa huko Makka, ambapo ilikuwa ikishakiwa ya kwamba; kuna uwezekano wa Imamu Hussein (a.s) kusafiri na kulekea mji Kufa, baadhi ya watu, akiwemo Abdullah bin Abbas, walikwenda kwake ili kumzuia asisafiri kuelekea Kufa, ila juhuidi zao hazikufanikiwa. [57]

Baada ya Imamu Hussein (a.s) na masahaba zake kuondoka mji wa Makka, Yahya bin Said, kamanda wa walinzi wa 'Amru bin Said bin 'Aas - ambaye pia aliku ni gavana wa Makka - pamoja na kundi la masahaba zake, walimfungia njia Hussein (a.s), Lakini Imamu Hussein hakuwajali na akaendelea na safari yake. [58]

Vituo vya mapumziko vya msafara kutoka Makka hadi Kufa

Vituo vya kupumzikia vya msafara wa Imamu Hussein (a.s) kutoka Makka kuelekea Kufa ni kama ifuatavyo:

  1. Bustan Banu Amir.
  2. Tan'im (Mahala ambapo Imamu Hussein (a.s) aliuteke msafara uliokuwa ukiongozwa na Buhairu bin Risani al-Himyari, wakala wa Yazid huko Yemen ambaye alikuwa akimpelekea ngawira kutoka mji wa Safaya kwenda Syria).
  3. Sifah: Mahala ambapo Imamu (a.s) alikutana mshairi maarufu Farazdaq.
  4. Dhatu 'Irqi: Mahala ambapo Imam (a.s) alikutana na Bishru bin al-Ghalib na 'Aunu bin 'Abdullahi bin Ja'far.
  5. Wadi Aqiq.
  6. Ghamra.
  7. Ummu Khirman.
  8. Salah.
  9. Afi'iyyah
  10. Ma'adin al-Fuzan.
  11. 'Umqu.
  12. Sulailiyya.
  13. Mughaitha Ma'awan.
  14. Nuqra.
  15. Haajir: Mahala ambapo Imamu (a.s) alimtuma Qais bin Mushir kwenda mji wa Kufa.
  16. Sumaira.
  17. Tuaz.
  18. Ajfar: Mahala alipokutana Imamu Hussein (a.s) na na 'Abdullah bin al-Muti'i al-'Adawi na kumnasihi Imamu (a.s) arejee na asiendelea na safari yake.
  19. Khuzaimiya.
  20. Zarud (Zuhayr bin al-Qain kuungana na msafara wa Imamu (a.s) na Imamu Hussein kukutana na watoto wa Muslim na kupokea habari za kuuawa shahidi Muslim na Hani.
  21. Al-Tha'alabiyyah.
  22. Batani.
  23. Shuquuq.
  24. Zubala: Alipopokea habari za kifo cha kishahidi cha Qais na kundi la watu kujiunga na msafara wa Imam (a.s) akiwemo Nafi'i bin Hilal.
  25. Batnu al-'Aqaba: Mahapa ambapo Imamu (a.s) alikutana na 'Amru bin Luzan na ushauri wake kwa Imam (a.s) wa kumtaka kurejea.
  26. 'Amiyyah
  27. Waqisa.
  28. Sharaf.
  29. Birka Abu al-Misk.
  30. Jabal Dhu Husam: Imamu Hussein (a.s) kukutana na jeshi la Hurru bin Yazid al-Riyahi.
  31. Baidha: Mahala alipotoa Imamu (a.s) hotuba maarufu kwa masahaba zake pamoja na Hurru.
  32. Musaijad.
  33. Hamam.
  34. Mughaitha
  35. Ummu Qar'wan.
  36. 'Udhaibu al-Hijanaati (njia ya Kufa ilikuwa ni kutoka Udhaibu hadi Qadisiyyah na al-Hira, lakini Imamu (a.s) alibadilisha njia yake na hatiame akasimama Karbala.
  37. Qasr Bani Muqatil: Mahala Imamu (a.s) alipokutana na Ubaidu Allah bin Hurru al-Ju'ufi na kukataa kwake kumsaidia Imamu (a.s)
  38. Qatqatana.
  39. Karbala, Wadi Al-Taff: Imamu Hussein (a.s) aliingia Karbala mwezi 2 Muharram mwaka wa 61 Hijiria. [59]

Akiwa njiani Imam Hussein (a.s), alijaribu kuwavutia au kuwafunua watu akili ili waondoke kutoka katika giza la dhulma na wafungamane naye katika kupigania haki; Miongoni mwa juhudi zake katika kuuanika ukweli na kuutandaza hadharani; ni pale alipokuwa Dhatu 'Irqi, ambapo Bishr bin Ghalib Al-Asadi alimfikia Imamu na kumpa habari juuu ya hali ya machafuko ilioko mjini Kufa na Imamu akamuunga mkono na kuthibitisha maneno yake.Bishr bin Ghalib Al-Asadi akamuuliza Imamu Hussein (a.s) kuhusu Aya isemayo: ((یوْمَ نَدْعُو کُلَّ أُنَاس بِإِمَامِهِم)) ; "Siku tutakapowaita watu wote kupitia Maimamu wao". [60] Imamu Hussein (a.s) akasema: "Kuna makundi mawili ya maimamu; kundi linalowalingania watu kwenye uwongofu na kundi linalowalingania kwenye upotovu." Hivyo basi yeyote yule atakayemfuata imamu wa uongofu atakwenda peponi, na atakayemfuata imamu wa upotofu ataingia motoni. [61] Bishr bin Ghalib hakufuatana na Imam Hussein (a.s) katika mapambano yake dhidi ya dhulma. Inasemekana ya kwamba; baada ya kumalizika kwa tukio la Karbala, yeye alikuwa alikuwa akienda kulia kwenye kaburi la Imamu Hussein (a.s) akidhihirisha majuto yake kwa kutomsaidia Imamu Hussein (a.s). [62]

Katika eneo la Tha'albiyya, mtu mmoja aitwaye Abu Hirrah Al-Azdi alikuja kwa Imamu Hussein (a.s) na kumuuliza makusudio ya safari yake hiyo, na Imamu Hussein (a.s) akamjibu kwa kusema:

Bani Umayya wamechukua mali yangu, nikavuta subra, wakanitukana pia nikavuta subra, ila nilivyowaona wamedhamiria kumwaga damu yangu nikaamua kukimbia. Ewe Abu Hirrah! Elewa ya kwamba mimi nitauawa na kundi la waasi na Mwenyezi Mungu atawavisha kabisa vazi la unyonge (atawadhalilisha) na atawachagulia mtawala atakaye wadhalilisha na kuwatawala kwa upanga mkali. [63]

Kutumwa kwa Qais bin Mus'har kwenda mji wa Kufa

Imamu Hussein (a.s) alipofika eneo la Batnu al-Rummah, aliandika barua kwa watu wa Kufa na kuwajulisha juu ya safari yake kuelekea mji wao. [64] Aliikabidhi barua hiyo kwa Qais bin Mus'har Al-Saidawiy. Hata hivyo, wakati Qais aliposimamishwa na maafisa wa Ubaidullah bin Ziad huko Qadisiyyah, ilimbidi aichane barua hiyo ili wasigundue yaliyomo ndani yake. Wakati Qais alipoletwa mbele ya Ibnu Ziyad, alitakiwa kufichua majina ya watu ambao Imamu Hussein (a.s) alikuwa amewaandikia barua hiyo au apande mimbari na kumtukana Imamu Hussein (a.s) na familia yake. Ibnu Ziad alimlazimisha Qais kufnaya alivyomwamrisha la si hivyo, ataamuru akatwe kichwa. Qais bin Mus'har Al-Saidawiy alichagua wazo la kupanda mimbari, ila badala ya kumtukana Imamu Hussein na familia yake, akaanza kumsifu Imamu Husein (a.s) kwa kusema: "Kwa hakika si mwengine bali ni Hussein bin Ali (a.s) ambaye ni mbora wa viumbe wa Mwenyezi Mungu, ambaye yuko njiani kuuelekea mji wenu, hivyo basi muungeni mkono na mumpe himaya zenu". Baada ya kufanya hivyo, Ibnu Ziad akaamuru atupwe kutaka juu ya ya paa la kasri la Dar al-Imara. [65]

Kutumwa kwa Abdullahi bin Yaqtar kwenda mji wa Kufa

Imesimuliwa ya kwamba; kabla ya Imamu Hussein (a.s) kupata habari kuhusu kifo cha kishahidi cha Muslim, alimtuma Abdullah ibn Yaqtar, kaka yake (Ibnu Yaqta) wa kunyonya [66], kwa Muslim. Hata hivyo, alitekwa na Huswein bin Tamimi na kupelekwa kwa Ubaidullahi bin Ziad. Ubaidullahi aliamuru Abdullah ibn Yaqtar apelekwe juu ya kasri ya Dar al-Amara ili amlaani Imamu Hussein (a.s) na baba yake (Ali bin Abitalib) mbele ya watu wa Kufa! Ibnu Yaqtar alipokwenda juu ya kasri, aliwahutubia watu na kusema: "Enyi watu! Mimi ni mjumbe wa Hussein (a.s), ambaye ni mjukuu wa Mtume (s.a.w.w) na ni mtoto wa bint yake (Fatima); basi fanyeni hima kumsaidia, na simameni dhidi ya mwana wa Marjana." [67] Ubaidullah alipoona hivyo, aliamuru atupwe chini kutoka juu ya kasri, na hatima yake ikawa ni kuuawa kishahidi. [68] Habari za kuuawa kishahidi kwa Abdullahi ibn Yaqtar, pamoja na habari za kuuawa kishahidi kwa Muslim na Hani, zilimfikia Imamu Hussein (a.s) akiwa kwenye makazi ya eneo la Zubaleh. [69]

Barua ya Imamu Hussein kwa Gavana wa Basra

Makala Asili: Barua ya Imam Hussein kwa watu wa Basra

Imam Hussein (a.s) aliwaandikia barua wazee (wakuu wa makabila) wa Basra na akaituma barua hiyo kupitia Salim bin Razien kwa viongozi wa makabila matano ya Basra (yaani: 'Aaliyah, Bakru bin Wael, Tamim, Abdu al-Qais, na Azdi). [70] Salim aliwasilisha nakala ya barua ya Imamu kwa kila mmoja wa viongozi wa Basra ambao ni; Malik bin Musmi'i Bakri, Ahnaf bin Qais, Mundhir bin Jaaruud, Mas'uud bin Amru, Qais bin Haitham, na Amru bin Ubaidullah bin Ma'amar. [71]

Yaliyomo ndani ya barua hiyo yalikuwa ni wito wa kufuata Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunnah za Mtume Muhammad (s.a.w.w), kwani Sunnah ilikuwa imeachwa na uzushi umechukua nafasi yake. Imamu aliahidi kuwaongoza kwenye njia iliyonyooka ikiwa watasikiliza maneno yake na kufuata maamrisho yake. [72]

Hata hivyo, wazee wote wa Basra waliopokea nakala ya barua hiyo waliificha isipokuwa Mundhir bin Jaaruud, ambaye alishuku kwamba; yawezekana barua hizo ni ujanja ulitokana na Ubaidullah bin Ziyad. [73] Kwa hiyo, katika usiku wa kabla ya kuondoka kwa Ibn Ziyad kwenda Kufa, Mundhir aliripoti jambo hilo kwake. [74] Ibn Ziad naye akamtaka mjumbe wa Hussein (a.s) awasilishwe kwake kisha akamkata kichwa. [75]

Kubadilisha njia na kuelekea Karbala

Imam Hussein (a.s) baada ya kufika Adhaibu al-Hajanat, alilazimika kubadili njia yake na kuelekea Karbala. [76]

Makabiliano na jeshi la Hurru bin Yazid Al-Riyahi

Ibn Ziad alipopata habari kuhusu harakati za Imamu Hussein kuelekea Kufa, alimtuma mkuu wake wa jeshi, ambaye ni Huswein bin Tamimi, pamoja na wanajeshi elfu nne waelekee Qadisiyyah na wafuatilia maeneo yaliopo kati ya Qadisiyyah na Khaffani, na baina ya Qutqutaaniyyah hadi la'ala'a. Aliwataka wanajeshi hao wachunguze mapito ya watu katika maeneo hayo kisha wamfikishie habari za wanaopita maeneo hayo. [77] Harru bin Yazid Riyahi na askari wake elfu moja pia walikuwa sehemu ya jeshi hili, lililotumwa chini ya uongozi wa Husein bin Tamim ili kuzuia harakati za msafara wa Imam Hussein (a.s).[78]

Abu Makhnaf, amenukuu habari kutoka kwa watu wawili wa kabila la Bani Asad walikuwa pamoja na Imamu Hussein (a.s) katika safari hii, ya kwamba; wakati msafara ule ulipoondoka kwenye makazi yake ya eneo la Sharaf, ulikutana na askari wa adui wakati wa nusu mchana wa siku hiyo. Katika hali hiyo, Imamu Hussein aliamua kuutiririsha msafara wake na kuelekea upande wa Dhul-Husam. [79]

Adhuhuri, Harru bin Yazid na askari wake walikabiliana na Imamu Hussein (a.s) na masahaba zake. Imamu Hussein akawaamuru watu wake wawape maji askari wa Harru pamoja na farasi wao. Ilipoingia wakati wa sala ya adhuhuri, Imamu Hussein (a.s) alimuamuru muadhini wake -ambaye ni Hajaj bin Masruq Ja’afiy- asome adhana, ulipofika wakati wa kusali, Imamu Hussein (a.s) baada ya kumtakasa na kumhimidi Mwenyezi Mungu, aliwahutubia watu na kusema: "Enyi watu! nimesimama hapa mbele yenu, ili mupate kuwa udhuru baina yenu na Mola wenu, mimi sikuja kwenu, ila baada ya kupokea barua zenu, na kujiwa na wajumbe watokao kwenu walionitaka nije kwenu wakidai kuwa hawana imamu (kiongozi), huenenda Mola akakuongozeni kupitia mimi, hivyo basi; ikiwa bado mmesimama juu ya viapo na hadi zenu, basi mimi nitakuja mjini kwenu, ila kama kuja kwangu kutakuwa ni madhara kwenu, basi niambieni ili nirudi". Baada ya hayo Hurru pamoja na jeshi lake wakawa wamekaa kimya bila ya kusema jambo. Katika hali hiyo Imamu Hussein (a.s) akaamuru ikimiwe sala, Imamu akasalisha sala ya adhuhuri na Hurru pamoja na jeshi lake wakamfuata na kusali nyuma yake. [80]

Baada ya kusali sala ya Alasiri, Imamu Hussein (a.s) aliwageukia watu na kusema, "Enyi watu! Mtamkhofu Mwenyezi Mungu na kutambua ya kwamba haki yabidi iwafikie wanaostahiki, mtakuwa mmejitengenezea njia ya kumridhisha Mwenyezi Mungu. Sisi ni Ahlulbait, ndio tunaostahiki zaidi kushika nafasi ya uongozi wa jamii kuliko na wale wanaodai uongozi kwa hadaa na uongo, amabo matendo yao katika kukuongozeni hayaendani na misingi adilifu, na kazi yao ni kukufanyieni dhulma tu. Kama hamtuhisabu kuwa sisi ndio wenye haki hii na hamtaki kututii, na kama barua zenu hazilingani na maneno na rai zenu, basi mimi hivi sasa nitaamua kurudi nilikotoka." Harru ibn Yazid akajibu, "Mimi sina habari yoyote ili kuhusiana na barua ulizozitaja, na wala sisi hatukuwa miongoni mwa waandishi wa barua hizo, sisi tumeamrishwa kukupeleka kwa Ubaidullah ibn Ziad mara tu tunapokutana nawe." [81]

Hussein (a.s) akawambia masahaba zake wageuze njia tayari kwa kurudi walikota, lakini Harru na jeshi lake wakamzuia. Hurru akasema: "Ni lazima nikupeleke kwa Ubaidullahi bin Ziad!" Hussein (a.s) akamjibu kwa kusema: "Naapa kwa Mungu, sitafungamana nawe kwenda kwa Ubadullahi." Hur akasema: Sijaagizwa kupigana nanyi; ila nimaagizwa nisikubanduke hadi nikupeleke mji wa Kufa, kwa hiyo kama unakataa kuja, basi ni bora ukashika njia ambayo haitakupeleka Kufa wala Madina; ili nipate kisingizio cha kumwandikia barua Ubaidullahi. Na kama utapenda kumwandikia barua Yazid basi mwandikie, huenda labda hii italeta amani na mwafaka mwema, na kwa maoni yangu hii ni bora kuliko mimi kujichafua mbele yako kupitia vita na migogoro." [82]

Msafara wa Imamu Hussein (a.s) ulisogea kutoka upande wa kushoto wa barabara za "Udhaibu" na "Qadisiyyah" na kufuata njia nyengine, Hurru naye akawa pamoja naye katika msafara huo. [83]

Kuwasili kwa mjumbe wa Ubaidullahi

Hussein (a.s), akiwa kwenye makazi ya “Baidhah” [84], baada ya kusali sala ya asubuhi, aliondoka yeye pamoja na masahaba zake na wakafika “Nainawa” karibu adhuhuri. Wakiwa katika eneo hilo Hurru alipokea barua kutoka kwa mjumbe wa Ubaidullahi isemayo: “Atakapokufikia mjumbe wangu na ukaipokea barua yangu, basi mdhibiti na uwe mkakamavu na mkali dhidi ya Hussein bin Ali (a.s), na wala usimuache ateremke mahala popote pale isipokuwa katika jangwa lisilo na mahala pa kujihami na wala maji. Nimemuamuru mjumbe wangu asitengane nawe mpaka alete khabari ya kwamba amri yangu imetimia, wa salaam.” [86]

Hurru alimsomea Imamu (a.s) barua ya Ibn Ziad na Hussein bin Ali (a.s) akamwambia: “Acha tutue Nainawi au Ghaadhiriyyah.” [87] Hurru akamwambia: “Haiwezekani, kwa sababu Ubaidullah, amembakisha aliyeileta barua hii awe ni mpelelezi dhidi yangu!" Zuhair bin Qain alipendekeza wapigane dhidi ya Hurru na jeshi lake, kwa sababu kazi itakuwa ni ngumu zaidi iwapo jeshi la hurru litaungana na askari wengine wa Ubaidullah. Imam akajibu, “Mimi katu sitakuwa ni mwanzilishi wa vita". Kisha wakaendelea na msafara wao hadi Karbala, walipofika Karbala, Hurru na wafuasi wake wakasimama mbele ya msafara wao na kumzuia Imamu na masahaba wake kuendelea na safari yao. [89]

Imam akiwa Karbala

Kuwasili kwa Imam Hussein (a.s) huko Karbala

Vyanzo vingi katika ripoti zake, vimeitaja siku ya pili ya Muharram ya mwaka wa 61 Hijiria kuwa ndio siku ambayo Imam Hussein (a.s) na masahaba zake waliingia Karbala. [90] Dainuri ambaye ni mwanahistoria wa karne ya tatu Hijiria, ameutaja mwezi mosi wa Muharram, kuwa ndio siku ambayo Imamu na masahaba zake walifika Karbala. [91] Kwa mujibu wa ripoti za katika kitabu chake "Maqtalu al-Hussein", ni kwamba; wakati Hurru alipomwambia Hussein bin Ali (a.s): “Tueni hapa, kwani hapa ndio karibu na mto Furati iko,” Imamu Hussein (a.s) alimuuliza: “Mahala hapa panaitwaje? Akamwambia: "Panaitwa Karbala". Imamu (a.s) akasema: Hapa ndipo mahala pa Karbu (mateso) na Balaa. Baba yangu alipokuwa anaelekea Siffin alipita hapa nami nikiwa pamoja naye. Akasimama na kuuliza jina lake. Wtu waliokuwa pamoja naye wakamwambia jina lake, naye akasema: Hapa ndipo mahali vitakapofikia vipando vyao, na ndio mahala patakapomwagwa damu zao". Waliokuwa pamoja naye wakamuuliza ni makusudio yake. Akasema: “Hapa ndipo mahala utakapofikia msafara kutoka katika familia ya Muhammad (s.a.w.w).”[92] Kisha Imamu Hussein (a.s) akasema: “Hapa ndipo mahali pa vipando vyetu na mahema yetu, na hapa ndipo mahali ambapo watu wetu watauawa na ni mahali patakapomwagika damu yetu.” [93] Kisha akaamrisha wapakue mizigo yao.

Imepokewa kwamba; baada ya wao kutua Karbala, Imamu Hussein (a.s) aliwakusanya watoto wake, ndugu zake na familia yake na akawatazama na kulia. Kisha akasema: “Ewe Mola, hakika sisi ni familia ya Mtume wako Muhammad (s.a.w.w) ambao tumetolewa kutoka kwenye makazi yetu na mji wetu, hali tukiwa katika mfazaiko kuchanganyikiwa na kutangatanga, huku tukiwa tumeliacha kaburi la babu yetu [Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) nyuma yetu), kutokana na kushambuliwa na kuhujumiwa na Bani Umayya. Ewe Mola tuchukulie haki yetu kutoka kwao na utusaidie dhidi ya madhalimu. Kisha akawageukia masahaba zake na kusema:

اَلنَّاسُ عَبِیدُ الدُّنْیا وَالدِّینُ لَعْقٌ عَلَی أَلْسِنَتِهِمْ یحُوطُونَهُ مَا دَرَّتْ مَعَایشُهُمْ فَإِذَا مُحِّصُوا بِالْبَلَاءِ قَلَّ الدَّیانُونَ



"Watu ni watumwa wa dunia, na dini ipo kwenye ncha ya ndimi zao tu, wanajishikiza nayo kwa kiasi cha mahitajio ya rizki zao tu, na wanapojaribiwa na kutahiniwa kupitia balaa fulani, basi ni wachache tu ndio watakaobakia katika dini." Rejea kitabu Maqtalu Al-Hussein cha Kharazmi, juz 1, uk 337.

Baada ya hapo, Imamu alinunua ardhi ya Karbala, yeye ukubwa wa maili nne kwa maili nne, kutoka kwa wakazi wa huko kwa thamani ya dirham elfu sitini na akaweka nao sharti ya kwamba; wawaongoze watu kwenye kaburi lake na wawahudumie kwa muda wa siku tatu watakaokuja kulizuru kabiri lake . [94]

Har bin Yazid Riahi alimwandikia barua Ubaidullahi bin Ziad na kumfahamisha kuhusu kutua kwa Husein (a.s) katika ardhi hiyo. [95] Kufuatia barua hiyo, Ubaidullahi alimwandikia barua Imamu Hussein (a.s) isemayo:

"Ewe Hussein, nimepata habari kuhusu kutua kwako katika ardhi ya Karbala; Amirul-Muuminina - Yazid bin Muawia - ameniamrisha nisipwese wala nisilishibishe tumbo langu mpaka nikukutanishe na Mwenyezi Mungu Mjuzi na Mpole, (yaani nikutoe roho), au nikulazimishe uyakubali yangu mimi na uukubali utawala na serikali ya Yazid bin Muawiya, wassalaam."[96]

Imepokewa kutoka katika vyanzo kadhaa ya kwamba; baada ya kuisoma barua hii, Hussein (a.s) aliitupa kando na kusema: “Hawataokolewa watu wanaotanguliza kuridhika kwao wenyewe kabla ya kuridhika kwa Muumba wao". Mjumbe wa Ibnu Ziad akamuuliza Imamu Hussein (a.s): Ewe Aba Abdillahi, hutajibu barua hii? Imamu Hussein (a.s) akasema: “Jibu labarua yake ni adhabu chungu ya Mwenye Ezi Mungu, ambayo hivi karibuni itampata". Yule mjumbe akarudi kwa Ibnu Ziad na akamwambia yale aliyoyasema Imamu Hussein (a.s). Ubeidullahi akaamuru jeshi liandaliwe kwa ajili ya vita dhidi ya Hussein (a.s). [97]

Kuingia kwa Omar bin Sa'ad ndani ya Karbala

Siku ya mwezi tatu Muharram Umar bin Sa'ad aliingia Karbala akiwa pamoja ja jeshi la watu elfu nne watoka mji wa Kufa. [98] Kuhusiana na msukumo na ushawishi uliomfanya Omar bin Sa'ad aende Karbala, imeelezwa ya kwamba; Ubadullahi bin Ziad almpa cheo ja ujemedari wa kuongoza jeshi la watu wa Kufa lenye idadi ya watu elfu nne, na kumtaka aende kwenye vitongoji vya Rai na Dastabiy na apambane na Wadailami (Wairani watokao mji wa Dailam ulioko Kaskazini mwa Iran) wanaishi ndani ya viutongoji hivyo. Pia Ubaidullahi alikuwa tayari kashamwandikia Omar bin Sa'ad waraka wa kumtawalisha na kumpa uongozi wa mji wa Rai (ulioko Iran). Omar bin Sa'ad pamoja na wafuasi wake wakaweka kambi yao katika kitongoji kijulikanacho kwa jin lana 'Hammam A'ayun' kiliopo nje ya mji wa Kufa. Omara bin Sa'ad alikuwa akijitayarisha kwa ajili ya kwenda Rai, ila baada ya Imamu Hussein (a.s) kuelekea mji wa Kufa, Ibnu Ziad akamwamrisha Omar bin Sa'ad aende kupambana na Imamu Hussein (a.s), na baada ya kumaliza mapambano hayo aelekee mjini Rai. Ibnu Zian hakufurahia kwenda kupambana na Imamu Hussein (a.s), kwa hiyo alimwomba Ubaidullahi amruhusu aende Rai badala yeye kupambana na Imamu Hussein (a.s). Ubaidullahi alikataa maombi ya Omar bin Sa'ad, na akamshurutisha kama atakataa kupigana na Hussein (a.s), basi ajiuzulu nafasi ya uongozi wa mji wa Rai. [99] Au katiba ya baba yake na baba yake, na uthabiti wake, kwa shida, ambayo iko katika eneo hili, ambalo. ina nguvu sana. Baada ya omar bin Sa'ad kuona sistizo la nguvu kutoka kwa Ubaidullahi bin Ziad, akaamua kukubali kwenda Karbala. 100 Hivyo akaondoka kuelekea Karbala yeye pamoja na jeshi lake, na kesho yake ambayo Imamu Hussein alfika Kitongoji cha Nainawa, Omar bin Sa'ad akwa tayari ameshafika Karbala. [101]

Mazungumzo kati ya Imamu Hussein (a.s) na Omar bin Sa'ad

Baada ya Omar bin Sa'ad kutuama vizuri katika ardhi ya Karbala, alitaka kumtumia Imamu Hussein (a.s) mjumbe, ili amuulize ni kwa nini amrkuja katika ardhi hiyo na anataka nini? Aliipendekeza kazi hii ifanye na Uzra bin Qais Ahmasi pamoja na wazee wengine ambao walikuwa wameandika barua za mwaliko wa kumwita Imamu Hussein aje katika mji wao, ila wao walikataa kufanya hivyo. [102] Lakini Kathir bin Abdullah Shuaiba akakubali na akaelekea kwenye kambi ya Imamu Hussein (a.s). Abu Thumama Saaidiy hakumruhusu Kathir kwenda kwa Hussein (a.s) na silaha yake, akarudi kwa Omar bin Sa'ad bila ya natija yoyote. [103]

Baada ya kurejea kwa Kathir bin Abdullah, Omar bin Sa'ad alimwomba Qurratu bin Qais Handhaliy [104] aende kwa Imamu Hussein (a.s) naye akakubali. Katika kujibu ujumbe wa Omar Sa;ad kupitia Qurratu, Hussein (a.s) alisema: “Watu wa mji wako waliniandikia barua wakinitaka nije hapa. Sasa, kama hawanitaki, nitarudi. "Umar bin Sa'ad alifurahishwa na jibu hili". [105] Kwa hiyo alimwandikia barua Ibn Ziad na kumfahamisha kuhusu maneno ya Hussein bin Ali (a.s). [106] Ubaidullah bin Ziad, akijibu barua ya Omar Sa'ad, alimtaka achukue kiapo cha utiifu kutoka kwa Hussein (a.s) na masahaba zake cha kumtii Yazid na kumkubali kama ni khalifa. [107]

Jaribio la Ibn Ziad la kupeleka jeshi Karbala

Baada ya Imamu Hussein (a.s) kufika Karbala, Ubaidullah bin Ziad aliwakusanya watu katika msikiti wa Kufa na akagawia hongo kutoka kwa Yazid - hadi dinari elfu nne na dirham laki mbili - miongoni mwa wakuu wa makabila wa mji huo, huku akiwataka wamuunge mkono Omar bin Sa'ad katika vita vyake dhidi ya Imamu Hussein (a.s). [108]

Ubaidullah bin Ziad alimweka Amru bin Huraith kwenye ofisi ya Kufa na yeye mwenyewe akaondoka mjini humo pamoja na wafuasi wake na kupiga kambi katika kitongoji cha Nukhaila, na pia akawalazimisha watu washikanae naye kuelekea Nukhaila (a.s) [109] Ili awadhibiti watu wasije kushikamana na Imamu Hussein (a.s) Ubaidullahi aliamua kufunga daraja la Kufa na kulishikilia daraja hilo, ili ahakikikishe kuwa hakuna mtu atakayevuka katika na kuelekea kwa Hussein (a.s). [110]

Kwa amri ya Ubaidullah bin Ziad, Haswin bin Tamim na askari elfu nne chini ya uongozi wake walipewa wito waondoke Qadsiyyah na waelekee Nukhaila. [111] Muhammad bin Ash'ath bin Qais Kandi, Kathir bin Shahab na Qa'aqa'a bin Suwaid pia nao walipewa na Ibn Ziyadwito wa kuwatayarisha watu wao kwa ajili ya vita dhidi ya Hussein bin Ali (a.s). [112] Ibn Ziad pia alimtuma Suwaid bin Abdul Rahman Manqari kwenda Kufa pamoja na baadhi ya wapanda farasi na akamwamuru afanye msako mjini Kufa na amtafute na kkumtia nguvuni yeyote yule aliyepinga na kukataa kwenda vitani dhidi ya Imamu Hussein (a.s), kisha ampelekee yeye kwa ajili ya kuwahukumu. Suwaid akamkamata mmoja wa watu wa Sham (Syria) ambaye alikuja mjini Kufa kudai urithi wake, kisha akampeleka kwa Ibn Ziad. Ibn Ziad naye aliamuru auwawe kwa ajili kuwatisha watu wa Kufa. Watu walipoona ukiatili huo, wote wakaririka na kuelekea Nukhailah. [113]

Watu walipokusanyika Nukhaila, Ubaidullah alimuamuru Haswin bin Numair, Hajjar bin Abjar, Shabath bin Rib-'i na Shimru bin Dhil al-Jushan kujiunga na kambi yake ili kumsaidia Ibnu Sa'ad. [114] Shimru alikuwa ndiye mtu wa kwanza kutekeleza amri yake.[115] Baada ya Shimru akafuatia Zaid (Yazid) bin Rakaab al-Kalbi akiwa pamoja na watu elfu mbili, Haswin bin Numair Sakuni pamoja na watu elfu nne, Musabu Mari (Mozair bin Rahina Maaziniy) pamoja na watu elfu tatu, [116] Haswin bin Tamim Tahawiy akiwa na askari elfu mbili [117] na Nasru bin Harbah (Harashah) pamoja na jeshi la watu elfu mbili kutoka mji wa Kufa, wote kwa jumla wakaenda kujiunga na jeshi la Omar bin Sa'ad. [118] Kisha Ibn Ziad akamtuma mtu kwa Shabath bin Rabi'i na kumtaka aende kufungamana na Omar bin Saad. Shabbat naye akajiunga na Omar bin Sa'ad pamoja na wapanda farasi elfu moja. [119] Baada ya Shabath akafuatia Hajjar bin Abjar akiwa na jeshi la watu elfu moja. [120] Baada yake akaja Muhammad bin Ash'ath bin Qais Al- Kindiy pamoja na askari elfu moja. [121] Kisha akaja Harith bin Yazid bin Ruwaim, naye akashikamana na makundi hayo na kuelekea Karbala. [122] Kila kukicha Ubaidullah bin Ziad akawa anatuma kundi la askari wa Kufi kwenda Karbala asubuhi na jioni. Mara alikuwa akituma watu 20, 30, 50, na wakati mwingine watu wafikao100. [123] Haadi ilipofika mwezi 6 Muharram, Idadi ya jeshi la Omar bin Sa'ad ilifikia idadi ya zaidi ya watu elfu ishirini, [124] huku Ubaidullah akiwa amemfanya Omar bin Sa'ad kuwa ndiye mkuu wa jeshi zima.

Juhudi za Habib bin Madhahir za kukusanya jeshi

Kwa mujibu wa ripoti kutoka kwa Shaarani; baada ya mkusanyiko wa askari wa Omar bin Sa'ad huko Karbala, Habib bin Madhahir Asadi, alipoona uhaba wa masahaba wa Hussein (a.s), kwa idhini ya Imamu, alikwenda bila kujulikana kwa ukoo wa kabila la Bani Asad na kuwaomba waje kumsaidia Imamu Hussein (a.s). Bani Asad, wakifuatana na Habib bin Madhahir Asadi, wakaondoka usiku kuelekea kwenye kambi ya Imam Hussein (a.s), ila askari wa Omar bin Sa'ad, chini ya uongozi wa Azraq bin Harbi Saidawiy, waliwafungia njia kwenye ukingo wa mto Furati na wakazuia msaada wao. Baada ya mzozo wa hapa na pale, Bani Asad wakarudi majumbani mwao na Habib akarudi kwa Hussein peke yake. [125]

Mazungumzo ya mwisho ya Imamu Hussein (a.s) na Omar bin Sa'ad

Makala Asili: Mazungumzo kati ya Imam Hussein (a.s) na Omar bin Sa'ad

Baina ya usiku wa 4 na wa 6 wa Muharram [126], Imamu Hussein (a.s) alikutana na Omar Sa'ad mahali fulani wakiwa katikati ya majeshi mawili na wakazungumza wao kwa wao. [127] Katika mazungumzo hayo, yalitolewa mapendekezo kadha ya kukomesha vita. Mazungumzo hayo yalimshirikisha Imamu Hussein (a.s) pamoja na kaka yake (Abbas), na kwa upande wa pili, kulikuwa na Omar Sa'ad pamoja na mwanawe na mtumwa wake katika mazungumzo hayo.[128] Kwa mujibu wa maelezo ya Muhammad bin Jarir Tabari; hakuna maelezo ya kina kuhusu maudhui ya mazungumzo yao. [129] na ripoti za kihistoria zina utata pingamizi juu ya mazungumzo yaliopita katika tukio hilo. [130]

Baadhi ya watu, wakinukuu baadhi ya ripoti za kihistoria kuhusiana na mazungumzo hayo pamoja na maneno mengine ya Imamu Hussein (a.s), wamepinga kuwepo kwa aina yoyote ile ya pendekezo la Imamu Hussein (a.s) la kujisalimisha kwa Yazid au kwenda kwake.[131] Kwa upande mwingine, baadhi ya watafiti wanaamini kwamba; Barua ya Omar Sa'ad aliyomwandikia Yazid bin Muawia kufuatia mazungumzo haya inafichua madhumuni na maudhui ya mazungumzo haya. [132] Baada ya mazungumzo ya Omar bin Sa'ad na Imamu Hussein (a.s), Omar bin Sa'ad alimtumia barua Ubaidullah bin Ziad akimuelezea ya kwamba: “... Hussein bin Ali (a.s) alifanya mapatano nami, na kwamba yeye atarudi mahali alipotoka, au atakwenda katika moja ya maeneo ya Waislamu na kutosheka na haki na wajibu sawa na Waislamu wengine, au pia yuko tayari kuenda kwa Yazid na kukubaliana na lolote atakaloamrishwa na Yazid kulitekeleza, na hilo ni jambo murwa kuridhika kwenu (Yazid na vibaraka wake) na ustawi wa taifa kwa jumla.” [133] Baada ya Ubaidullah kuisoma barua hiyo alisema: “Bila shaka ndiyo barua inayostahiki kutoka kwa mtu ambaye ni kiongozi na amiru anaye wapendelea kheri watu wake!" Baada ya Ubaidullahi kuisoma barua hiyo, alikuwa karibu kukubali pendekezo hilo, ila Shimru bin Dhil al-Jaushan akawa ndio kizuizi. [134]

Mwezi 7 Muharram na kufungiwa maji

Mnamo tarehe 7 Muharram, kuliandikwa barua kutoka kwa Ubaidullah bin Ziad kwenda kwa Omar bin Sa'ad ikimtaka amfungia maji Imamu Hussein (a.s) na masahaba wake. Baada ya kupokea barua hiyo, Omar bin Sa'ad alimwagiza Amru bin Hajjaj Zubaidi kuwaongoza wapanda farasi mia tano hadi kwenye kingo za mto Furati ili kumzuia Hussein (a.s) na masahaba zake wasipate maji. [135]

Kwa mujibu wa nukuu za baadhi ya vyanzo; Baada ya wao kufungiwa njia ya kuyafikia maji hayo, na kiu zao kupindikia hali ya kawaida. Hapo ndipo Imamu Hussein (a.s) alipomtuma kaka yake (Abbas) pamoja na wapanda farasi thelathini, watembeaji kwa miguu ishirini, wakiwa na vibuyu ishirini kwenda kuchota maji. Wakiwa katika usiku wa kiza huku Nafi'i bin Hilali Al-bajali mbele na bendera yake, walianza safari yao na hatiame kufika mto wa Furati (Euphrates). Hata hivyo, Amr bin Hajjaj, ambaye alikuwa na jukumu la kuulinda mto huo, alikabiliana na masahaba wa Imamu Hussein (a.s). Katika hali hiyo miongoni mwa masahaba hao wakawa wanajaza maji, huku wengine -akiwemo Abul Fadhli na Nafi'i bin Hilali Al-bajali- wakiwa wanapambana na kuwalinda wachotaji hao maji. Hatimae juhudi zao za kijasiri ziliwaruhusu kufanikiwa na kufisha maji kwenye mahema. [136]

Siku ya Tasua

Makala Asili: Siku ya Tasua

Siku ya 'Tasua', ambayo ni siku ya mwezi 9 wa Muharram mwaka wa 61 Hijiria, Baada ya Adhuhuri, ambapo ilikuwa ni baada ya sala ya Alasiri, Shimru bin Dhil al-Jushan alimfikia Omar bin Sa'ad na akampa ujumbe wa Ibn Ziad. [137] Omar bin Sa'ad akamwambia Shimru: "Mimi mwenyewe ndiye nitakaye kuwa msimamizi wa kazi". [138]

Kwa mujibu wa moja ya riwaya; Shimru na kwa mujibu wa riwaya nyingine Abdullah bin Abi al-Mahal, mpwa wa Ummu al-Binina, alipokea barua ya dhamana kutoka kwa Ibn Ziad -ya kuwapa amani- watoto wa Ummu al-Binina. [139] Abdullah akaituma barua hiyo kwenda Karbala kupitia mtumwa wake, kisha yeye mwenyewe akafika Karbala na kuwasomea maandishi ya barua hiyo watoto wa Ummu al-Binina, lakini wao walikataa kupokea dhamana hiyo. [140] Kwa mujibu wa riwaya nyingine, Shimru ndiye aliye ipeleka barua hiyo ya dhamana Karbala na kuifikisha kwa Abbas (a.s) na ndugu zake, [141] lakini Abbas (a.s) na ndugu zake wote kawa pamoja waliikataa kupokea dhamana walioahidiwa katika barua hiyo. [142] Kwa mujibu wa maelezo ya Sheikh Mufid Shimru, alisema na kuwambia: "Enyi wapwa zangu, mmesalimika nyinyi mupo chini ya amani" Nao wakamjibu: Mwenye Ezi Mungu akulaani wewe pamoja na barua yako ya dhamana, mnatupa sisi dhamana ya amani na mnamwacha mtoto wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) bila ya amani?! [143]

Jioni ya siku ya "Tasu'a", Omar bin Sa’ad alinadi akisema: "Enyi jeshi la Mungu! Pandeni vipando vyenu minibashirie. Askari wakapanda na kuelekea kwenye kambi ya Imamu Husein (a.s). [144] Imamu alipoelewa nia chafu za maadui zake, alimwelekea ndugu yake Abbas na kumwambia: “Kama unaweza kuwashawishi kuchelewesha vita mpaka kesho itakuwa ni vyema, ili usiku wa leo tupate muda wa kumuomba na kumwabudu Mungu wetu. Mungu anaelewa ya kwamba; mimi napenda sana kusali na kusoma Qur’an.” [145] Abbas akaenda kwa askari wa maadui zao na kuwataka wampe muhula usiku ule mmoja. Ibn Sa'ad alikubali kuwapa muhula wa usiku mmoja. [146] Siku ile, mahema ya Imamu Hussein (a.s) na familia yake pamoja na mahema ya masahaba zake, yakawa wamezingirwa na maadui zao. [147]

Matukio ya usiku wa Ashura

Makala Asili: Usiku wa Ashura (Matukio)

Mwanzoni mwa usiku wa Ashura, Imamu Hussein (a.s) aliwakusanya masahaba zake na baada ya kumhimidi Mwenyezi Mungu akawaambia: “Nadhani hii ndiyo siku ya mwisho ya sisi kuwa na muhula kutoka kwa watu hawa. Fahamuni kwamba nilikupeni ruhusa ya kuondoka na kwenda majumbani mwenu. Hivyo basi kila mtu yupo huru kuondoka bila y akhofu yoyote, nendeni kwa amani nami nimeridhika kukurudishieni viapo vyenu vya utiifu wenu juu yangu. Sasa kwa vile giza la usiku limekufunikeni, basi lichukue giza hilo kama ndio kipando chenu na nendeni zenuni.” Katika wakati huo, kwanza familia ya Imamu na kisha masahaba wa Imamu wote -kupitia ibara za hamasa- walitangaza uaminifu wao katika kushikanmana na Imamu Hussein (a.s), wao walisisitiza juu ya kutoa muhanga maisha yao kwa ajili ya kumtetea Imamu Hussein (a.s). Ibara zao za hamasa zimerikodiwa katika vyanzo kadhaa vya kihistoria. [148]

Maneno ya Imamu Hussein kuhusiana na wafuasi wake usiku wa kuamkia Ashura

أَمَّا بَعْدُ فَإِنِّي لَا أَعْلَمُ أَصْحَاباً أَوْفَى وَ لَا خَيْراً مِنْ أَصْحَابِي وَ لَا أَهْلَ بَيْتٍ أَبَرَّ وَ لَا أَوْصَلَ مِنْ أَهْلِ بَيْتِي فَجَزَاكُمُ اللَّهُ عَنِّي خَيْرا



"Tafsiri yake ni kwamba; Kwa hakika mimi sijawaona wafuasi bora wenye kujua fadhila kama wafuasi wangu mimi, na wala sijaona familia njema zaidi na yenye huruma zaidi kuliko familia yangu mimi, basi Mola akulipeni jaza njema kwa kheri zenu juu yangu." Rejea kitabu cha Sheikh Mofid, Al-Irshad, chapa ya mwaka 1399 Shamsia, Juzuu 2, uk 91

Wasiwasi wa Bibi Zainab (a.s)

Baada ya Imamu Hussein kutangaza hadharani wasifu juu ya uaminifu wa masahaba, alirudi kambini na akaingia kwenye hema la bibi Zainab (a.s). Nafi'f Ibnu Hilal alikiwa amekaa nje ya hema akimsubiri Hussein (a.s) akamsikia bibi Zainab (a.s) akimwambia Imamu Hussein (a.s); “Je, umewajaribu masahaba zako? Nina wasiwasi wasije wakatupa kisogo na kukusalimisha kwa madui wakati vita vitakapo wadia." Hussein (a.s) akajibu kwa kusema: “Naapa kwa Mwenye Ezi Mungu, nimewajaribu wafuasi hawa na nimewakuta ni watu ambao vifua vyao wamevigeuza kuwa ndio ngao, kwa namna ambayo wanayatazama mauti katika pembe ya macho yao, na wanayapenda mauti wakiwa katika njia yangu kama vile mtoto mchanga anyonyae anavyopenda anavyokuwa na shauku ya kukikumbatia kifua cha mama yake." Pale Nafi'i alipohisi kwamba Ahlul-Bait wa Imamu Hussein (a.s) walikuwa na wasiwasi juu ya uaminifu na uimara wa masahaba wao, alikwenda kwa Habib bin Madhahir na baada ya kushauriana naye, akaamua kushikiamana na masahaba wengine ili kumhakikishia Husein (a.s) na Ahlul-Bait wake ya kwamba; wataendelea kuwalinda hadi tone la mwisho la damu yao litakapodondoka chini na kumaliza uhai wao. [149]

Habibu bin Madhahir alitoa wito kwa masahaba wa Hussein (a.s) kukusanyika pamoja. Kisha akawaambia Bani Hashim: Rudini kwenye mahema yanu; Kisha akawageukia masahaba wenzake na kuwasimulia aliyoyasikia kutoka kwa Nafi'i. Wote kwa pamoja wakasema: "Tunaapa kwa Mungu aliyetubariki na kutujaalia kuwa katika nafasi hii, lau tusingesubiri amri ya Hussein a.s), tungewashambulia kwa haraka ili kuyatakasa maisha yetu na kuyaangaza macho yetu (kwa nuru ya Mola wetu)." Habibu bin Madhahir, pamoja na masahaba wenzake, wakasogea hatua baada ya hatua hadi kwenye hema la Ahlul-Bait (a.s) wakiwa na panga zilizochomolewa kutoka katika ala zake, na wote kwa sauti moja na wakasema: “Enyi watoharifu wa kizazi cha Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w! Hizi ndizo panga za wanaume na vijana wako shujaa, ambazo hazitarudi alani mpaka zikate shingo za wenye dhamira mbaya juu yenu. Na hii ni mikuki ya wana wenu, iliowapa ya kwamba haitaingia ila kwenye vifua vya wale waliokuiteni kisha wakakufanyieni khiana.” [150]

Matukio ya Siku ya Ashura

Makala Asili: Siku ya Ashura (matukio)

Baada ya kusali sala ya asubuhi, Imamu Hussein (a.s) alipanga safu za vikosi vyake (wapanda farasi 32 na askari 40 wa miguu) tayari kwa mapambano. [152] Hussein (a.s) alipanda farasi kwa dhamira ya kuwakamilishia hoja maadui zake, yeye pamoja na kundi la masahaba kadhaa walikwenda mbele ya jeshi la madui na kwa ajili ya kuweka bayana juu ya haki na dhamira yake katika msimamo wake. Baada ya Imamu Hussein (a.s) kuwahutubia maadui zake, Zuheir bin Qain akaanza kuzungumza na maadui zao na kuwabainishia wasifu na hadhi ya Imamu Hussein (a.s). [154]

Moja ya matukio ya asubuhi ya Ashura ni kujiuzulu kwa Harru bin Yazid Riahi na kuachana na jeshi la Omar bin Sa'ad kisha kujiunga na kambi ya Imamu Hussein (a.s). [155]

Mwanzoni mwa vita, mashambulizi yalifanywa kwa njia ya vikundi. Yaani kila upande ulitoa kundi la jeshi fulani ili waingie mapambanoni. Kwa mujibu wa baadhi ya simulizi za kihistoria, hadi masahaba 50 wa Imam waliuawa kishahidi katika shambulio la kwanza. Baada ya hapo, masahaba wa Imamu waliamua kwenda kupigana mmoja mmoja au wawili wawili. Masahaba hao hawakumruhusu yeyote yule kutoka katika jeshi la maadui kumkaribia Imamu Hussein (a.s). [156] Baada ya kuuawa shahidi masahaba wa Imam Hussein (a.s.) asubuhi na alasiri ya Ashura, ambao si miongoni mwa watu wa kabila la bani Hasim, hapo masahaba wa kabila la Bani Hashimi wa Hussein (a.s) walijitokeza kwa ajili ya kuingia vitani. Mtu wa kwanza kutoka kwa Bani Hashim ambaye alimuomba Hussein (a.s) ruhusa ya kingia uwanjani, na hatimae kuuawa kishahidi, alikuwa ni Ali Akbar. [157] Baada yake, watu wengine wa familia ya Imamu nao waliingia uwanjani mmoja baada ya mwingine na mwishowe wakauawa kishahidi. Abul Fadhli al-Abbas (a.s), mshika bendera wa jeshi na mlinzi wa mahema, pia aliuawa kishahidi kupitia mapambano yaliojiri baina yake na walinzi wa mto Furati (Eufrates). [158]

Baada ya kifo cha kishahidi cha masahaba kutoka ukoo wa Bani Hashim, Imamu Hussein (a.s.) aliingia vitani, lakini kwa muda fulani hakuna hata mtu mmoja kutoka upande wa jeshi la watu Kufa aliyejitokeza kukabiliana naye. Alipokua vitani, licha ya upweke wa Hussein (a.s) na majeraha mazito aliopata kichwani na mwilini mwake, ila bado Hussein (a.s) alionekana kuuzungusha upanga wake bila woga dhidi ya maadui zake. [159]

Kuuawa Shahidi kwa Imam Hussein

Askari wa miguu chini ya uongozi wa Shimru bin Dhil al-Jushan walimzunguka Hussein (a.s); Lakini bado hakukutokea aliyejitokeza na kumsogelea Imamu Hussein (a.s) huku Shimru akiwahimiza kumshambuli na kumwingia mwilini. [160] Baada Shimru kuona hali hiyo, aliwaamuru wapiga mishale kumpopoa Imamu (a.s) kwa mishale. Kwa sababu ya wingi wa mishale, mwili wa Imamu Hussein (a.s) ukuwa umejaa mishale kila mahala. [Maelezo 1] [161] Katika hali hiyo, Hussein bin Ali (a.s) alirudi nyuma na maadui zake wakawa wakapanga mstari mbele yake. [162] Majeraha na uchovu vilimfanya Husein (a.s) kuwa dhaifu sana ikambidi kusimama na kupumzika kidogo. Akiwa katika hali hiyo, kulitoka jiwe kutoka upande wa maadui zake na kusibu paji la lake la uso, damu zikaanza kutiririka kutoka usoni mwake. Mara tu Imamu (a.s) alipotaka kujifuta damu usoni mwake kupitia pindo la kanzu yake (au kwa kipande cha kitambaa) [163], mara mshale wenye ncha tatu na wenye sumu ukarushwa na kutua juu ya moyo wake. [164] Hapo hapo Malik bin Nusair akampiga kwa upanga Hussein (a.s) kichwani kwake, pigo zito mno, kiasi ya kamba ya kofia ya Imamu ilichanika kupitia pigo hilo. [165] Seyyed Ibn Tawus [166] ameeleza kwa kwamba; kuanguka kwa Imamu Hussein (a.s) kutoka juu ya farasi wake hadi ardhini, kulifuatia baada ya mvua ya mishale kutoka na shambulio la idadi kubwa ya askari kwa amri ya Shimru kumhujumu Imamu Hussein (a.s) katika tukio hilo. Shambuli kubwa dhidi yake, liliufanya mwili wake uwe dhaifu mno, kiasi ya kwamba akawa hata nguvu ya kusimama pia hana, na akawa anatapatapa huku akijizoa na kuanguka chini tena. [167]

[168] Pia mmoja wa askari anayeitwaye Zar'atu bin Shariik Al-Tamimi alimpiga pigo zito Imamu Hussein (a.s) katika bega lake la upande wa kushoto. Sinan bin Anas Nakhai naye akamchoma Imamu Hussein (a.s) katika koo yake. Kisha Saleh bin Wahb Ja'afi (kwa mujibu wa kauli nyengine ni Sinan bin Anas) akaja na kumpiga Hussein bin Ali (a.s) ubavuni kwa mkuki, kulikopelekea kuanguka kutoka kwenye mgongo wa farasi na kuangukia paja la kuliani kwake.[169] Shimru bin Dhi al-Jawshan pamoja na kundi la askari wa Omar Sa'ad, akiwemo Sinan bin Anas na Khuli bin Yazid Asbahiy, walimsogelea Hussein (a.s). Shimru aliwahimiza kummaliza Hudsein (a.s) haraka iwezekanavyo [170] lakini hakuna aliyekubali miongoni mwao. Alivyoona hivyo alimuamuru Kholi kukikata kichwa cha Imamu Hussein (a.s). Kholi alipoingia kwenye dunia hiyo ya mauaji, mikono na mwili wake ulitetemeka na akashindwa kutekeleza alicho amrishwa. Shimru [171] au kwa mujibu kauli nyingine Sinan bin Anas [172] alishuka kutoka kwenye farasi na kukikata kichwa cha Imamu Hussein (a.s) na kumkabidhi Khuli. [173] Allameh Tehrani katika kitabu chake 'Lamaatu al-Hussein [174] anaamini ya kwamba; Nayyir Tabrizi katika shairi lake maarufu amefafanu vyema hali ya viumbe mbalimbali katika ulimwengu -kila mmoja kulingana na uwezo wake na kipaji chake- walivyomlilia Imamu Hussein (a.s) wakati wa tukio la Karbala.

Matukio baada ya kifo cha kishahidi cha Imamu (a.s)

Baada ya Imamu Hussein kuanguka kutoka kwenye farasi wake, Dul-Janahi (Farasi wa Imamu Hussein) alikwenda pembeni yake na akawa anuzunguka mwili wa Imamu Hussein aliyekuwa amepoteza fahamu, huku akimnusa na kumbusu. Kisha akajipaka kwenye paji la uso wake damu ya mwili wa Imamu Hussein (a.s), alionekana kuikita miguu yake chini na kuinamisha kichwa chake, kisha akaelekea kwenye mahema. [178] Imam Baqir (a.s) katika moja ya riwaya anasema: "Farasi huyo wakati alipokuwa anarudi mahemani alikuwa akisema:الظليمة ، الظليمة ، من اُمّة قتلتْ ابن بنت نبيّها ; "Dhulma ilioje! Dhulma ilioje! kutoka katika kaumu hii, ambapo wao wameamua kumuuwa mtoto wa binti ya Mtume Wao (s.a.w.w)". [179] Dhul -Janahi Alipofika kwenye mahemani, alikuwa akilia na kupiga kichwa chake chini. Familia ya Imamu Hussein walipomwona Farasi wa Imamu Hussein katika hali hiyo, walitoka nje ya mahema yao na kumkusanyikia na kumpapasa kichwani, uso na miguuni mwake. Kulthum akaweka mikono yake miwili juu ya kichwa chake na kusema: "Waa Muhammadaah Waa Jaddaah Waa Nabiyyaah.." "Mtume wee! Babu yetu wee! Ee Nabii wetu wee!" [180] Ibara hii ni miongoni mwa ibara zinazosomwa katika mikusanyiko wa maadhimisho ya maombolezo ya kifo cha Imamu Hussein (a.s). [181]

Kupora mahemani

Baada ya kifo cha kishahidi cha Hussein bin Ali (a.s), askari wa upande wa maadui walishambulia mahema na kupora vilivyokuwemo ndani yake. Kila mmoja wao katika jambo hilo alikuwa akishindana na wengine.” [183] Shimru naye akiwa na kundi la askari aliingia mahemani kwa nia ya kumuua Imamu Sajjad (a.s), lakini bibi Zainab (a.s) akawazuia. Kwa mujibu wa riwaya nyingine; baadhi ya askari wa Omar bin Sa'ad walipinga jambo hilo. [184] Omar bin Sa'ad aliwaamuru wanawake watoharifu wa Bani Hashim kukusanyika kwenye hema moja na akawapa baadhi ya askari kuwalinda. [185]

Farasi kuuponda mwili wa Imamu (a.s)

Kwa amri ya Omar bin Sa'ad na kwa mujibu wa amri ya Ibnu Ziad, watu kumi wa kujitolea kutoka katika askari wa Kufa waliupiga teke mwili wa Imamu Hussein (a.s) na kuuponda kwa kwata za farasi wao na kuivunja mifupa ya kifua na mgongo wake. [186] Watu kumi waliojitolea kufanya kazi hiyo ni:

Kupeleka vichwa vya mashahidi huko Kufa

Siku hiyo hiyo ya mauwaji, Omar bin Sa'ad alikituma kichwa Imamu Hussein (a.s) kupitia Kholi bin Yazid Asbahi na Hamid bin Muslim Azdiy ili wakifikishe kwa Ubaidullah bin Ziad. Vile vile aliamuru vichwa vya mashahidi wa Karbala viondolewe kwenye miili yao, ambavyo vilikuwa ni vichwa vya mashahidi 72, ambavyo alivikabidhi kwa Shimru bin Dhi al-Jawshan, Qais bin Ash'ath, Amru bin Hajjaj na Uzratu bin Qais, ili wavifikisha mjini Kufa. [190]

Kutekwa kwa Familia ya Imamu (a.s)

Makala Asili: Mateka wa Karbala

Imamu Sajjad (a.s), ambaye alikuwa ni mgonjwa, pamoja na bibi Zainab (a.s) pamoja na wengine waliosalimika roho zao vitani, walikamatwa mateka na kupelekwa mjini Kufa kwa Ibn Ziad, kisha kufikishwa kwenye kasri ya Yazid huko Syria. [191]


Maziko ya Mashahidi

Kupitia amri ya Omar bin Sa'ad, miili ya askari wa Kufa ilizikwa bila pingamizi; Lakini mwili wa Hussein (a.s) pamoja na miili ya masahaba zake ilibakia ardhini bila kuzikwa. [192] Tarehe 11 Muharram [193] au tarehe 13 Muharram [194] zimetajwa kuwa ndio siku za kuzikwa mashahidi wa Karbala. Kwa mujibu wa baadhi ya kauli; baada ya Omar bin Sa'ad na wafuasi wake kuondoka Karbala, kundi la watu wa kabila la Bani Asad -waliokuwa wakiishi karibu na Karbala- waliingia kwenye eneo la Karbala, na ulipofika usiku ambapo walihisi kuwa wapo salama na hawaonekani na maadui, walimsalia sala ya maiti Imamu Hussein (a.s) pamoja na masahaba zake, kisha wakawazika. [195] Kwa mujibu wa riwaya fulani, mwili wa Imamu Hussein (a.s) alizikwa kupitia msaada wa Imamu Sajjad (a.s). [196]

Masuala yanayofungamana

Vyanzo

  • Qurʾān.
  • Abū l-Faraj al-Iṣfahānī, ʿAlī b. al-Ḥusayn. Maqātil al-ṭālibīyyīn. Edited by Aḥmad Ṣaqar. Beirut: Dār al-Maʿrifa, n.d.
  • Balādhurī, Aḥmad b. Yaḥyā al-. Ansāb al-ashrāf (vol. 5). Edited by Iḥsān ʿAbbās. Beirut: Jamīʿat al-Mutasharriqīn al-Amānīyya, 1979.
  • Balādhurī, Aḥmad b. Yaḥyā al-. Ansāb al-ashrāf (vol. 3 & vol. 1). Edited by Muḥammad Bāqir Maḥmūdī. Beirut: Dār al-Taʿāruf, 1977.
  • Dīnawarī, Aḥmad b. Dāwūd al-. Akhbār al-ṭiwāl. Edited by ʿAbd al-Munʿim ʿĀmir. Qom: Manshūrāt Raḍī, 1368 Sh.
  • Dīnawarī, Ibn Qutayba al-. Al-Imāma wa l-sīyāsa. Edited by ʿAlī Shīrī. Beirut: Dār al-Aḍwāʾ, 1990.
  • Ibn Aʿtham. Al-Futūḥ. Edited by ʿAlī Shīrī. Beirut: Dār al-Aḍwāʾ, 1991.
  • Ibn Athīr, ʿAlī b. Abī l-Karam. Al-Kāmil fī l-tārīkh. Beirut: Dār Ṣādir, 1965.
  • Ibn Kathīr, Ismāʿīl b. ʿUmar. Al-Bidāya wa l-nihāya. Beirut: Dār al-Fikr, 1986.
  • Ibn Miskawayh, Abū ʿAlī. Tajārub al-umam. Edited by Abū l-Qāsim Imāmī. Tehran: Surūsh, 1379 Sh.
  • Ibn Shahr Ashūb. Manāqib Āl Abī Ṭālib. Qom: ʿAllāma, 1379 AH.
  • Irbilī, ʿAlī b. ʿIsā. Kashf al-ghumma. Tabriz: Maktabat Banī Hāshimī, 1381 AH.
  • Khwārizmī, Muwaffaq b. Aḥmad al-. Maqtal al-Ḥusayn. Edited by Muḥammad al-Samāwī. Qom: Maktabat al-Mufīd, n.d.
  • Kulaynī, Muḥmmad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, n.d.
  • Masʿūdī, ʿAlī b. al-Ḥusayn al-. Murūj al-dhahab wa maʿādin al-jawhar. Edited by Asʿad Dāghir. Qom: Dār al-Hijra, 1409 AH.
  • Mufīd, Muḥammad b. Muḥammad b. Nuʿmān al-. Al-Irshād. Qom: Kungiri-yi Shaykh al-Mufīd, 1413 AH.
  • Mūsawī al-Muqarram, ʿAbd al-Razzāq al-. Maqtal al-Ḥusayn. Beirut: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, n.d.
  • Nūrī, Mīrza Ḥusayn al-. Mustadrak al-wasāʾil wa mustanbaṭ al-masāʾil. Beirut: Muʾassisat Āl al-Bayt, 1408 AH.
  • Sayyid b. Ṭāwūs, ʿAlī b. Mūsā al-. Al-Luhūf. Tehran: Jahān, 1348 Sh.
  • Shaykh al-Ṣadūq, Muḥammad b. ʿAlī al-. Al-Amālī. Qom: Qism al-Dirāsāt al-Islāmīyya –Muʾssisat al-Biʿtha- 1417 AH.
  • Ṭabarī, Muḥammad b. Jarīr al-. Tārīkh al-umam wa l-mulūk. Edited by Muḥammad Abū l-Faḍl Ibrāhīm. Beirut: Dār al-Turāth, 1967.
  • Ṭabrisī, Faḍl b. al-Ḥasan al-. Iʿlām al-warā b-aʿlām al-hudā. Tehran: Islāmīyya, 1390 AH.
  • Ṭurayḥī, Fakhr al-Dīn al-. Majmaʿ al-Baḥrayn. 3rd edition. Tehran: Murtaḍawī, 1375 Sh.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Al-Istibṣār fī-mā akhtulif min al-akhbār. Beirut: Dār al-Taʿāruf, 1401 AH.