Suratu al-Ikhlas

Kutoka wikishia

Surat Ikhlas au Surat Tawhid au Qul-huwallahu Ahad ni sura ya 112 katika mpangilio wa msahafu na ipo katika Juzuu ya 30. Sura hii imeshuka Makka. Sura hii imeitwa Ikhlas au Tawhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu) kutokana na kuwa, ndani yake inazungumzia suala la kuweko Mungu mmoja tu na inamuachilia huru mwanadamu kunako shirki na kumshirikisha Mwenyezi Mungu. Muhtawa na mambo yaliyoko ndani ya sura hii ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kutokuwa kwake mhitaji wa mwingine. Kuna fadhila nyingi zimenukuliwa kuhusiana na sura hii. Miongoni mwazo ni: Sura ya Ikhlas (Qul-huwallahu Ahad) ina hukumu ya theluthi moja ya Qur’ani na mwenye kuisoma mara tatu ni sawa na amehitimisha Qur’ani. Imesisitizwa na kukokotezwa mno katika hadithi juu ya kuisoma sura hii katika Swala za kila siku. Imekuja katika hadithi ya kwamba, Bwana Mtume (saww) anamfananisha Imamu Ali (as) na Sura ya Ikhlas na anasema, kama ambavyo kusoma Surat Ikhlas mara tatu ni mithili ya kusoma Qur’ani yote, basi kumpenda Amirul-Muuminina , kwa ulimi, moyo katika vitendo ni kupenda Uislamu wote. Sura hii ni katika sura nne ambazo zinaanza na Qul yaani “sema” na hivyo zinajulikana kwa jina la “Qul Nne”

Utambulisho

  • Kuitwa kwa majina hayo

Sura hii ni mashuhuri jina la Surat Ikhlas au Tawhidi[1] Ama kuhusiana na sababu ya kuitwa kwa jina hilo ni kwamba, inatoa wasifu wa kwamba, Mwenyezi Mungu ni mmoja na wa pekee, hakuzaa, wala hakuzaliwa na hana mshirika. Na ndio maana ikapewa jina la Tawhidi (kumpwekesha Mwenyezi Mungu)[2] Na imeitwa jina la Ikhlas kutokana na maudhui na yaliyomo ndani ya sura hii kwa hakika yanamuokoa, kumuachilia huru na kumuweka mbali mwanadamu na shirki na kumshirikisha Mwenyezi Mungu, na kwa msingi huo, anaokoka na moto wa jahanamu.[3] Vilevile katika hadithi na vyanzo vyake vya kale, sura hii imeitwa Qul-huwallah Ahad” kwa mnasaba wa Aya hiyo ambayo ni ya kwanza katika sura hii. [4] Kwa hakika kumetajea na kubainisha majina mengine mengi ya sura hii. Miongoni mwayo ni: Swamad, Nejat, maarifat, asas, tajrid, tafrid, baraat na muqashqishah. [5]

  • Mahali na Mpangilio wa Kushuka

Sheikh Tabarsi anaitambua sura hii kuwa ni miongoni mwa sura za Makki yaani zilizoshuka Makka na anaandika kwamba, na vilevile inasemekana sura hii ni Madani yaani imeshuka Madina. [6] Suyuti mmoja wa Maulamaa na wanazuoni wa Ahlu Sunna pia anaamini kuwa, Surat Ikhlas imeshuka mara mbili: Mara moja imeshuka Makka na mara ya pili Madina; [7] hata hivyo Allama Tabatabai anaandika: Kwa mujibu wa tukio lililotajwa kuhusiana na sababu ya kushuka kwake, inaonekana kwamba, kuwa kwake ni Makki yaani iliyoshuka Makka kuko wazi na bayana zaidi. [8] Kimpangilio wa kushuka, Surat Ikhlasi ni ya 22 kushushiwa Bwana Mtume (saww). Katika mpangilio wa sasa wa msahafu, sura hii ni ya 112 [9] na ipo katika Juzuu Amma (juzuu ya 30).

  • Idadi ya Aya Zake na Sifa Nyingine Maalumu

Surat Ikhlas ina Aya 4, maneno 15 na herufi 47. Sura hii ni katika sura zinazotambulika kama Mufassalaat (zenye Aya fupi). Sura hii na sura nyingine tatu za Kafirun, An-nas na Falaq zote zinaanza na neno Qul (sema) na hivyo zimeondokea pia kufahamika kwa jina la Qul Nne. [10] Surat Ikhals ni miongoni mwa sura zinazotambulika kama jami’i al-nuzuuli yaani sura ambazo Aya zake zote zimeshuka kwa mara moja. [11].

Yaliyomo

Allama Muhammad Hussein Tabatabai anaandika katika tafsiri yake ya al-Mizan: Surat Ikhlas inatoa wasifu kwamba, Mwenyezi Mungu ni mmoja tu na wa pekee na kwamba, viumbe wote wanamhitajia Yeye katika haja zao zote na hana mshirika katika dhati, sifa na matendo. Kwa hakika hii ni tawhid halisi na kumpwekesha Mwenyezi Mungu ambayo ni mahususi kwa Qur’ani na maarifa yote (ya kimsingi, kimatawi na kimaadili) ya Kiislamu yameandaliwa kwa msingi huu. [12]

Baadhi ya maurafaa (wasomi wa elimu ya irfani) wamesfadidi na kunufaika na Aya ya: “Hakuzaa wala hakuzaliwa” na kusema kuwa, uwepo wote unafungamana na Mwenyezi Mungu na hakuna mtengano wowote kama ambavyo hakuna kiumbe yoyote ambaye anajitegemea na kilichoko ni dhihirisho la Mola wetu ambapo kwa mujibu wa Qur’ani hizi ni ishara za Mwenyezi Mungu. Imam Ali bin Abi Twalib (as) anasema akifasiri Surat Ikhlas kwamba: Mwenyezi Mungu aliyetakasika utajo wake, hakuzaa wala hakuzaliwa ili katika izza na utukufu wake asiwe na mshirika, na hana mwana wala mtoto, ili baada ya kifo chake asiwe na mrithi. [13]

Imamu Mussa al-Kadhim (as) anasema katika hadithi moja akifasiri Surat Tawhid: Hakuzaa hata awe na mrithi, na hakuzaliwa hata awe na mshirika. [14] Maudhui ya surat Ikhlas [15]

Nguzo za Tawhid na Kumpwekesha Mwenyezi Mungu Nukta ya Kwanza: Aya ya 1-2 kumpwekesha Mwenyezi Mungu katika dhati na sifa. Nukta ya Pili: Aya ya 3-4, kutokuwa na mshirika Mwenyezi Mungu katika dhati na sifa. Aya ya kwanza inaweka wazi juu ya kwamba, Mwenyezi Mungu ni mmoja na wa pekee na kwamba hakuna Mola na Muumba mwingine. Inasema: Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee. Aya ya pili inabainisha kwamba, Mwenyezi Mungu si mhitaji bali yeye ndiye mkusudiwa. Inasema: Mwenyezi Mungu Mkusudiwa Aya ya tatu inabainisha kwamba, Mwenyezi Mungu hana mtoto wala baba kama inavyosema: Hakuzaa wala hakuzaliwa. Aidha Aya ya nne na ya mwisho ya Surat Tawhid inatuwekea wazi kwamba, Allah hana mshirika katika sifa. Aya hiyo inasema: Wala hana anaye fanana naye hata mmoja.

Sababu ya Kushuka

Kuhusiana na sababu ya kushuka Surat Ikhlas, Imamu Ja’afar Swadiq (as) amenukuliwa akisema: Kundi la Mayahudi lilimuomba Bwana Mtume (saww) awatolee wasifu wa Mungu. Mtume alinyamaza kwa muda wa siku tatu na hakutoa jibu, mpaka iliposhuka Surat Ikhlas na kisha akatoa majibu ya swali lao. [16]

Imeelezwa kuwa, swali hili lilikuwa takwa na kundi miongoni mwa washirikina wa Makka [17] au takwa la Ahlul-Kitab wa Madina [18], au watu wengine. [19]

Maana ya Swamad

Maana ya Swamad ni mkusudiwa na mkubwa ambaye wote wanamrejea yeye katika hawaiji na mahitaji yao na ni wenye kumhitajia yeye na kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni Muumba wa ulimwengu matokeo yake ni kuwa, kila kisichokuwa yeye kinamhitajia katika dhati yake na asili ya uwepo wake na katika sifa zake na matendo yake. Alif na laam zilizoko katika neno al-Swamad ni jambo linaloweka wazi kuhusu mkusudiwa mwenye kuhodhi hilo na hali hii ya kuwa mkusudiwa ni mutlaki haina sharti na hivyo kuwa na matokeo matatu ya moja kwa moja ambayo: Mosi, hakuzaa. Kinyume kabisa na madai ya manaswara kwamba, Masihi ni mwana wa Mungu. Pili, hakuzaliwa, kwa maana kwamba, hana baba wala mama. Tatu, wala hana anayefanana naye hata mmoja si katika dhati wala katika matendo. Kuzaa na kuzaliwa maana yake ni kuwa na hitajio, kuwa na mafungamano na kuwa na mtu anayefanana na wewe. [20]

Daraja ya Imamu Ali (as) na Surat Ikhlas

Imekuja katika hadithi ya kwamba, Bwana Mtume (saww) anamfananisha Imamu Ali (as) na Sura ya Ikhlas. Anasema katika hadithi hiyo: Mfano wa Ali bin Abi Twalib baina ya watu ni mithili ya Ql-huwallahu Ahad” katika Qur’ani. Kama ambavyo kila mwenye kusoma Surat Ikhlas mara tatu anahesabiwa sawa amesoma Qur’ani yote, basi kila ambaye atampenda Ali bin Abi Twalib Ali (as), kwa ulimi, moyo na katika vitendo, atakuwa ameupenda Uislamu wote. Kisha mwisho anasema: Ninaapa kwa yule ambaye ameniteua kwa ajili ya risala (Utume), kama watu wa ardhini watampenda Ali kama watu wa mbinguni, Mwenyezi Mungu hatomuingiza mtu miongoni mwao katika moto wa jahanamu. [21] Kuhusiana na hili, kuna beti za mashairi ambazo zinanasibishwa na Buali Sina ambazo zinabainisha wasifu wa Imamu Ali na mshabaha wake na Surat Ikhals. [22]

Sulaiman ibn Khawajah Killan Ibrahim ibn Baba Khawajah al-Balkhi al-Qunduzi msomi na mwanazuoni wa Kisuni amenukuu hadithi iliyotangulia katika kitabu chake cha Yanabi al-Mawaddah. [23] Kadhalika katika vitabu na vyanzo vingine vya hadithi vya Waislamu wa Kisuni kuna hadithi yenye madhumuni kama hii ambayo inatambulisha daraja ya Amirul-Muuminina Ali (as) kwamba, ni mithili ya Surat Ikhlas. [24]

Fadhila na Sifa Maalumu

Imenukuliwa kutoka kwa Bwana Mtume (saww) na Imamu Muhammada Baqir (as) kwamba, Surat Ikhlas ni sawa na theluthi moja ya Qur’ani. [25]. Imenukuliwa pia kutoka kwa Imam Ridha (as) kwamba, kila ambaye atasoma Surat Tawhid (Qul-huwallah) na akawa na imani nayo atakuwa ametambua tawhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu). [26] Imenukuliwa pia kutoka kwa Mtume ya kwamba: Someni sana sura hii kwani sura hii ni nuru ya Qur’ani. [27. Kadhalika imenukuliwa kutoka kwa Imamu Ali (as) kwamba, kila mwenye kusoma Surat Ikhlas na Qadar mchana au usiku wake mara 100, baada ya kifo chake, Mwenyezi Mungu atatia nuru kaburi lake na atakuwa pamoja na hiyo mpaka peponi. [28] Kwa upande wake Imamu Ja’afar Swadiq (as) anasema: Kila ambaye itampita siku na katika Swala zake tano akawa hakusoma Surat Tawhidi, huambiwa wewe si katika wanaoswali. [29]

Katika vynazo na vitabu vya hadithi kumenukuliwa sifa maalumu zinazopatikana kwa kusoma sura hii. Miongoni mwazo ni: Kupoa maumivu ya jicho [30], kumlinda mtu akiwa safarini (kama atasoma mara 11) [31], vilele msomaji wa sura hii hulindwa na malaika 50 akiwa usingizini [32], kusoma sura hii kunandoa umasikini na kutokuwa na kitu [33], kunapelekea kusamehewa madhambi (kama itasomwa mara 200 usiku, siku ya Ijumaa na katika Swala mbili ikisomwa mara katika rakaa mbili), kadhalika katika kujibiwa dua (kama itasomwa katika rakaa ya kwanza baada ya Alhamdu. [35]

Kusoma Surat Ikhlas

Imekokotezwa na kutiliwa mkazo mno kusoma Surat Ikhlas katika Swala za wajibu. Inaelezwa kuwa, ni makuruhu kusoma sura moja katika rakaa mbili za Swala isipokuwa kama sura hiyo itakuwa ni Ikhlas (Qul-huwallahu).[36] Kinyume na sura nyingine za Qur’ani ambapo mwenye kuswali anaweza kuiacha sura anayoisoma kabla ya kufika nusu na kuamua kusoma sura nyingine, kuhusiana na Surat Ikhlas na Surat Kafirun anayeswali akianza kusoma moja kati ya sura hizi mbili anawajibika kuikamilisha.[37]

Ni mustahabu kusoma Surat Ikhlas katika Swala nyingi za mustahabu kama Swala ya Amirul-Muuminina (as), kusoma mara 50 katika kila rakaa miongoni mwa rakaa nne, kusoma mara 50 katika rakaa ya kwanza ya Swala ya Bibi Fatma (as) [38], katika rakaa ya kwanza ya Swala ya usiku, [39], katika rakaa moja ya witri, [40], sunna ya alfajiri, katika rakaa ya kwanza ya sunna ya adhuhuri na magharibi, Swala ya ihramu na Swala ya tawafu [41] na vilevile wakati wa kuzuru makaburi [42] na kusimama katika viwanja vya Arafa. [43]. Kadhalika imeusiwa kwamba, wakati mtu anapopita makaburini asome Surat Ikhlas mara 11 na atoe zawadi ya thawabu zake kwa maiti waliozikwa hapo. [44.

Rejea

  • القرآن الكريم.
  • الألوسي، محمود بن عبد الله، روح المعاني في تفسير القرآن العظيم والسبع المثاني، بيروت - لبنان، دار إحياء التراث العربي، ط 1، 1421 هـ.
  • البحراني، هاشم بن سليمان، البرهان في تفسير القرآن، بيروت - لبنان، دار إحياء التراث العربي، ط 1، 1429 هـ.
  • الحر العاملي، محمد بن الحسن، وسائل الشيعة، بيروت-لبنان، مؤسسة آل البيتKigezo:هم، ط 2، 1424 هـ‏.
  • الخرمشاهي، بهاء الدين، موسوعة القرآن والدراسات القرآنية، إيران - طهران، مؤسسة الأصدقاء، 1377 ش.
  • الرازي، محمد بن عمر، التفسير الكبير، بيروت - لبنان، دار الكتب العلمية، ط 4. 1434 هـ.
  • الزمخشري، محمود بن عمر، الكشّاف، بيروت - لبنان، دار صادر، ط 1، 1431 هـ.
  • الطباطبائي، محمد حسين، الميزان في تفسير القرآن، قم - إيران، دار المجتبى، ط 1، 1430 هـ.
  • الطبرسي، الفضل بن الحسن، تفسير جوامع الجامع، قم-ايران، مؤسسة النشر الإسلامي التابعة لجماعة المدرّسين، ط 2، 1430 هـ.
  • الطبرسي، الفضل بن الحسن، مجمع البيان، بيروت - لبنان، مؤسسة الميرة، ط 1، 1430 هـ.
  • الطبرسي، الفضل بن الحسن، مجمع البيان، قم -إيران، دار الأسوة، ط 1، 1426 هـ.
  • الطوسي، محمد بن الحسن، التبيان في تفسير القرآن، قم - إيران، مؤسسة النشر الإسلامي، ط 1، 1431 هـ.
  • الموسوي، عباس بن علي، الواضح في التفسير، بيروت - لبنان، مركز الغدير، ط 1، 1433 هـ.
  • معرفة، محمد هادي، التمهيد في علوم القرآن، قم-إيران، ذوي القربى، ط 1، 1428 هـ.
  • مكارم الشيرازي، ناصر، الأمثل في تفسير كتاب الله المنزل، بيروت - لبنان، مؤسسة الأميرة، ط 2، 1430 هـ.
  1. الخرمشاهي، موسوعة القرآن والبحوث، ج 2، ص 1270-1271.
  2. الرازي، التفسير الكبير، ج 32، ص 161.
  3. الرازي، التفسير الكبير، ج 32، ص 127؛ الطبرسي، مجمع البيان، ج 10، ص 703.