Ajal Mu'allaq

Kutoka wikishia

Ajal Mu'allaq (Kiarabu: الأجَل المُعَلََّق) ni kipindi kisichofahamika na chenye kubadilika cha kifo cha mwanadamu ambacho ni mkabala na Ajal Musamma (kipindi kisicho na shaka cha kifo cha mwanadamu (bila shaka kifo cha mtu fulani kitatokea katika wakati fulani). Allama Tabatabai anaamini kuwa, Ajal Mu'allaq ni kipindi cha kifo cha kila mtu kulingana na hali yake ya mwili ambapo kutokana na sababu za nje yumkini kifo chake kikatokea haraka au kwa kuchelewa.

Chini ya Aya za Qur'an kama hii: ((ثُمَّ قَضىَ أَجَلًا وَ أَجَلٌ مُّسَمًّى عِندَهُ ; kisha akakuhukumieni ajali, na muda maalumu uko kwake tu)), ambayo ni Aya ya pili ya Surat al-An'am, wafasiri wamefanya uchunguzi na utafiti kuhusu Ajal Mu'allaq na Ajal Musamma.

Kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu, mambo kama kutoa sadaka, kuunga udugu, kuishi na kuamiliana vyema na majirani, kuacha kutenda dhambi na kumzuru Imamu Hussein (a.s) ni mambo ambayo yametajwa kuwa yanapekea kucheleweshwa kifo cha mtu. Mkabala wake ni kuwa, kufanya mambo kama kuzini, kuwaudhi baba na mama, kula kiapo cha uwongo na kukata uhusiano na ndugu ni mambo ambayo yanafupisha umri wa mwanadamu.

Utambuzi wa maana

Makala asili: Ajal

Katika lugha ya Kiarabu kipindi cha kila kitu au mwisho wa kila kipindi unafahamika kwa jina la Ajal. [1] Wakati Ajal inapotumika kuhusiana na mwanadamu huwa na maana ya mwisho wa kipindi cha uhai au wakati wa kifo chake. [2] Katika Qur’an, Ajal ya aina mbili imetumika kwa ajili ya mwanadamu. Wakati mwingine imetumika kwa qaid (sharti) ya Musamma ambapo wafasiri wanasema kuwa, hiyo ni Ajal Musamma na wakati mwingine bila ya sharti ambapo katika baadhi ya maeneo kama Aya ya pili ya Surat al-An’am ambapo ndani yake kumetajwa majina ya Ajal isiyo Musamma, Qadha Ghair Mahtum [3] na Ajal Mu’allaq. [4]

Allama Tabatabai anaamini kwamba, Ajal Musamma ni kipindi ambacho bila shaka mwanadamu ataaga dunia wakati huo na ni Mwenyezi Mungu tu ndiye mwenye elimu ya hilo; mkabala wake ni Ajal Mu’allaq ambacho ni kipindi cha kuaga dunia kila mwanadamu katika hali ya kawaida ambapo inawezekana kubadilika kwa muda huo. [5] Kwa mujibu wa anavyoamini Allama Tabatabai ni kwamba, kipindi cha kuaga dunia mtu ni kwa mujibu wa hali yake ya mwili (afya ya mwili) ambapo yumkini kwa kuzingatia sababu za nje, umri wake ukapungua au kuongezeka. [5] Yaani kwa mujibu wa hali ya mtu ya mwili wake, mtu anaweza kuishi kwa mfano miaka 100, hivyo Ajal Mu'allaq yake (wakati wa kifo chake) ni miaka 100; lakini mtu huyu huyu kutokana na sababu za nje inawezekana kifo chake kikawa haraka au kikachelewa na hii ni Ajal Mussam yake. [6]

Kadhalikka angalia: Ajal Musamma

Chimbuko la Ajal Mu'allaq

Mjadala kuhusiana na Ajal Mu'allaq na Ajal Musamma umekuja chini ya Aya za Qur'an miongozi mwazo ni Aya ya pili ya Surat al-An'am [7] ambapo ndani yake kumezungumziwa uwepo wa ajal mbili kwa mwanadamu: ((هُوَ الَّذِى خَلَقَكُم مِّن طِينٍ ثُمَّ قَضىَ أَجَلًا وَ أَجَلٌ مُّسَمًّى عِندَهُ ; Yeye ndiye aliye kuumbeni kwa udongo, kisha akakuhukumieni ajali, na muda maalumu uko kwake tu)).

Kwa mujibu wa Aya hii baadhi ya wafasiri wamesema: Kuna Ajal mbili kwa mwanadamu ambapo moja kutokea kwake ni lazima na nyingine ni yenye kubadilika; [8] ya kwanza ndiye ile Ajal Musamma na ambayo imekuja kwa jina hili katika Aya na ya pili ni Ajal Mu'allaq. [9]

Hata hivyo kumezungumziwa tafsiri zingine kuhusiaana na aina mbili tajwa katika Aya iliyotangulia. [10] Kwa mfano baadhi wamesema: Makusudio ya Ajal Musamma katika Aya ni zama na kipindi cha maisha ya mwanadamu, kuanzia kipindi cha kifo hadi kuanza kwa Kiyama; na makusudio ya Ajal isio Musamma ni kipindi cha muda wa maisha ya mwanadamu duniani. [11] Kadhalika wamesema: Makusudio ya Ajal Musamma ni mwisho wa umri wa watu ambao bado wangali hai; mkabala wa Ajal nyingine ambayo mwisho wa umri wa watu ambao wamefariki dunia. [12]

Mambo yenye taathira kwa Ajal Mu'allaq

Kwa mujibu wa Aya za Qur'ani na hadithi, kufaanya baadhi ya mambo huwa sababu ya kucheleweshwa au kuharakishwa Ajal Mu'allaq. [13] Sayyid Muhammad Hussein Tabatabai akitegemea Aya za tatu na nne za Surat Nuh ameandika: Kufanya ibada kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, kuwa na taqwa na kumtii Mtume ni mambo ambayo yanachelewesha kifo. [14]

Sheikh Tusi amenukuu kutoka kwa Imam Swadiq (a.s) ya kwamba: Watu ambao wanakufa kutokana na dhambi zao ni zaidi ya watu wanaokufa kwa kifo cha kawaida, na watu ambao umri wao unakuwa mrefu kutokana na kutenda mema ni wengi zaidi ya watu ambao umri wao unaongezeka kwa njia ya kawaida. [15]

Katika hadithi kumetajwa mambo kama kutoa sadaka, kuunga udugu, kuwa na muamala mzuri na majirani, kuacha kutenda dhambi, kumzuru Imamu Hussein (a.s), kushukuru sana na kusoma Surat Tawhidi kila baada ya Sala kwamba, yanachelewesha Ajal Mu'allaq. [16] Kadhalika kufanya baadhi ya madhambi kama zinaa, kuwaudhi baba na mama, kula kiapo cha uwongo na kukata uhusiano na ndugu kunapelekea kuharakishwa Ajal Mu'allaq. [17]