Nu'man bin Ajlan al-Zuraqi

Kutoka wikishia

Nu'man bin Ajlan al-Zuraqi Ansari (Kiarabu: النُعْمان بن عَجْلان الزُرَقي الأنصاري) alikuwa Gavana wa Imam Ali (a.s) huko Bahrain na Oman ambaye alimuacha Imamu na kuamua kujiunga na Mu'awiyah.

Nu'man alikuwa mmoja wa Maswahaba, wapokezi wa hadithi ya Ghadir na askari wa Imamu Ali katika vita vya Jamal na Siffin, na alimuunga mkono Imamu kwa mashairi yake. Wakati wa utawala wake huko Bahrain, kwa kutokana na kutoa Bait al-Mal (hazina ya dola) kwa Bani Zurayq, Imamu Ali alimuandikia barua na kumuonya dhidi ya kitendo chake hicho. Baada ya Nu'man kupata barua kutoka kwa Imamu na kufichuliwa upotofu wake katika kutumia vibaya Bait al-Mal aliachana na Imamu Ali na kuamua kujiunga na Mu'awiyah.

Utambulisho na Nafasi

Barua ya Imamu Ali (a.s) kwa Nu'man bin Ajlan:

Yeyote anayepuuza amana na uaminifu na akaonyesha nia ya kufanya khiyana na asiiweke safi nafsi yake na dini yake, basi amejidhuru katika dunia hii na atakachokipata baadaye kitakuwa kichungu zaidi na cha kudumu na kibaya zaidi na cha muda mrefu zaidi. Basi muogope Mwenyezi Mungu. Wewe ni kutoka kwa watu ambao wana sifa za ustahiki, tabia yako inapaswa kuwa kwa namna ambayo mimi niwe na dhana nzuri kwako, na ikiwa niliyosikia kukuhusu ni kweli, basi rudi nyuma na ubadilishe maoni yangu juu yako. Chunguza ushuru katika eneo la mamlaka yako na niandikie barua ili nitangaze msimamo wangu juu yako, In Shaa Allah. [1]

Nu'man bin Ajlan al-Zuraqi ni katika Ansari na anatokana na kabila la Bani Zurayq [2] na ni katika maswahaba wa Mtume (s.a.w.w) [3] na Imamu Ali (a.s) [4] na kipindi fulani pia aliteuliwa na Imamu Ali (a.s) kuwa gavana na mtawala wa Bahrain na Oman. [5] Daima alikuwa akiheshimiwa na Maansari. [6] Baada ya kuuawa shahidi Hamza bin Abd al-Muttalib, Nu'man alimuoa Khawla bint Qays, mke wa Hamza. [7] Wakati wa siku za kuugua Nu'man, Mtume (s.a.w.w) alimtembelea na kumuombea dua. [8] Katika kitabu cha Ansab al-Ashraf (kilichoandikwa katika karne ya tatu), Nu'man anatambulishwa kama mmoja wa watetezi wa Ahlul-Bayt (a.s) dhidi ya Mu'awiyah. [9] Pia Allama Amini amemtambulisha miongoni mwa wapokezi wa tukio la Ghadir. [10] Nu'man alikuweko katika vita vya Jamal [11] na Siffin [12] alikuwa upande wa jeshi la Imamu Ali (a.s). Menqari Katika kitabu chake cha Waq'at Siffin, amelitaja jina Nu'man kuwa ni mmoja wa mashahidi wa tukio la Hakamiat (kuhukumiwa na Qur’ani). [13] Naim bin Ajlan ambaye ni kaka wa Nu'man ni miongoni mwa mashahidi wa tukio la Karbala. [14]

Nu'man Atengana na Imamu Ali (a.s)

Baada ya vita vya Siffin, Imamu Ali (a.s) alimteua Nu'man kuwa mtawala wa Bahrain na Oman. [15] Alipokuwa mtawala wa Bahrain, Nu'man alikuwa akitoa pesa kwa Bani Zurayq kutoka katika hazina ya dola (Baitul-Mal) jambo ambalo ni kinyume cha sheria kutokana na kutostahiki waliokuwa wakipatiwa. [16] Ya'qubi, mwanahistoria wa karne ya tatu Hijria anasema, Imam Ali (a.s) alimuandikia barua Nu'man na kumuonya dhidi ya kitendo hicho. Baada ya kupokea barua ya Imam na kufichuliwa upotofu wake katika kutumia Bait al-Mal, alichukua uamuzi wa kumuacha Imam na kujiunga na Mu'awiya. [17]

Mashairi Yake ya Kumuunga Mkono Imamu Ali (a.s)

Nu'man alikuwa malenga na mshairi. [18] Nu'man ametunga mashairi ya kumuunga mkono Imamu Ali kuhusiana na tukio la Saqifa [19] na siku ya Siffin. [20]

وَصيُّ النَّبيِّ الْمُصْطَفى وَ ابْنُ عَمِّهِ
وَ قاتِلُ فُرْسانِ الضَّلالَةِ وَ الْكُفْرِ

Madhumuni ya beti hizo za mashairi: Tulimtaka Ali na alikuwa anastahiki ukhalifa, (kwa sababu) kwa kujua kwako na kutokujua, yeye ni wasii wa Mtume mteule wa Mungu na ni binamu yake, alipigana na wapanda farasi wa upotofu na ukafiri na akawaangamiza.[21]

Ibn Abi al-Hadid, katika maelezo yake ya Nahj al-Balagha, alilichukulia shairi hili la Nu'man kama jibu la shairi la Amr bin al-A’s katika tukio la Saqifa na akaongezea ubeti ufuatao:

فذاک بعون الله یدعو إلی الهدی
و ینهی عن الفحشاء و البغی و النکر
Kwa msaada wa Mungu, anaita kwenye hidaya na uongofu.
Na anakataza uchafu, uadui na ukanushaji.[22]

Rejea

Vyanzo