It’am Ghadir

Kutoka wikishia

It’am Ghadir (kulisha chakula katika Sikukuu ya Ghadir) ni moja ada na mazoea ya Waislamu wa madhehebu ya Shia ambapo imesisitizwa kulisha chakula katika kumbukumbu na maadhimisho ya Siku ya Ghadir. Kwa mujibu wa hadithi iliyosimuliwa na Imamu Ali bin Mussa al-Ridha (a.s.), malipo na thawabu za kulisha chakula siku ya Ghadir ni sawa na malipo ya kuwalisha Mitume na Sidiqin wote, na Mashia wanaombwa kushiriki katika ada ya kulisha chakula siku Ghadir kadri wawezavyo.

Ada ya kulisha chakula siku ya maadhimisho ya Sikukuu ya Ghadir hufanywa katika nchi tofauti kama vile Iran, Afghanistan, Pakistani na Uturuki kwa mila, ada na mbinu tofauti. Nchini Iran, watu hugawa vyakula majumbani, misikitini na katika Husseiniya mbalimbali na kuwapatia watu. Katika maadhimisho ya kilomita 10 ya Ghadir, ambayo yalifanyika Tehran Iran mwaka 2023, kuliandaliwa Maukib 1300 vya washiriki ambapo vilitoa huduma ya vyakula na vinywaji.

Ada ya Mashia

Maandalizi ya kulisha watu 20,000 siku ya Eid Ghadir (Haram Abdul Azim, Julai 8, 2023)

Kulisha Ghadir au kuwapa wengine chakula siku ya Eid Ghadir inachukuliwa kuwa ni miongoni mwa ada za Mashia katika Siku ya Ghadir. [2] Kulisha Ghadir kunachukuliwa kuwa ni miongoni mwa mila ambazo Mashia huzifanya kuiadhimisha Siku ya Ghadir na pia kujadidisha baia na kiapo chao cha utii kwa Imam Ali (a.s). [3] Katika riwaya iliyosimuliwa kutoka kwa Imam Sadiq (a.s), siku ya Ghadir imeitwa kwa jina la Siku ya kulisha chakula. [4]

Kulisha Ghadir kumevutia hisia za Mashia wa nchi mbalimbali; huko Afghanistan, masharifu (watu wa kizazi cha Mtume) hutoa chakula na nadhiri kwa majirani na jamaa zao. [5] Katika mikoa tofauti ya Pakistani, kama vile Lahore, Karachi, Quetta na Peshawar, wakati wa kusherehekea sikukuu ya Ghadir, meza na vitanga vya chakula hutandikwa. [6] Maalawi wa Uturuki katika baadhi ya miji ya nchi hiyo hugawa chakula katika Sikukuu ya Ghadir, kinaitwacho Harissa. [7]

Nchini Iran sunna na ada hii hufanywa na watu kwa kugawa vyakula majumbani, katika misikiti na Husseiniya. [8] Katika maadhimisho ya kilomita 10 ya Ghadir, ambayo yalifanyika Tehran Iran mwaka 2023, kuliandaliwa zaidi ya Maukib 1300 vya washiriki vilitoa huduma ya chakula na vinywaji kwa mamilioni ya watu. [9] Mjini Mashhad, vitengo mbalimbali vinavyohusiana na Haram ya Imamu Ridha (Astan Quds Radhawi) pia mwaka 2021 kwa ushiriki wa harambee ya wananchi kuligawiwa vyakula kwa mamilioni ya wananchi katika maeneo mbalimbali ya Iran. [10]

Maagizo na sira ya Maimamu ya kulisha Ghadir

Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti, Maimamu waliwahimiza Mashia kulisha siku ya Ghadir; kama ilivyo katika hadithi, ambapo kulisha siku ya Ghadir kumekokotezwa na kutiliwa himizo kando ya kumfuturisha aliyefunga swaumu, kutoa idi (zawadi ya sikukuu) na kuunga udugu. [11] Katika riwaya ya Imam Ridha (a.s), Mashia wanaombwa kushiriki katika kulisha siku ya Ghadir kadiri wawezavyo. [12]

Thawabu za kulisha siku ya Ghadir

Imekuja katika hadithi iliyonukuliwa kutoka kwa Imamu Ridha (a.s) kwamba, thawabu za kumlisha muumini siku ya Ghadir ni sawa na thawabu za kuwalisha Manabii na sidiqin wote; [14] kadhalika imenukuliwa na Imamu Ridha (a.s) kutoka katika hotuba ya Imamu Ali (a.s) kwamba: Kila mtu ambaye siku ya Ghadir atamlisha Muumini kama vile amelisha makundi ya kumi ya watu. Imamu Ali (a.s) alitoa maana ya kundi la watu kuwa ni kila kundi ni sawa na Manabii, mawalii na mashahidi laki moja. Imamu Ali alisema pia kuwa, anayetoa chakula na kulisha watu siku ya Ghadir hilo ni dhamana na bima ya Mwenyezi Mungu kwake kunako ukafiri na ufakiri. [15]

Imesisitizwa na kukokotezwa katika hadithi juu ya kuwalisha wahitaji, [16] waumini, [17] ndugu katika dini, [18] na vilevile kuwafuturisha waliofunga Swaumu [19] katika siku ya Ghadir. Ni mustahabu kufunga Swaumu siku ya Ghadir [20] na jambo hili ni mashuhuri baina ya Waislamu wa madhehebu ya Shia. [21]