Hussein Badreddin al-Houthi

Kutoka wikishia
Hussein Houth

Hussein Badreddin al-Houthi (Kiarabu: حسين بدر الدين الحوثي) (1960-2004) ni muasisisi na kiongozi wa kwanza wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen. Alikuwa mfuasi wa madhehebu ya Shia Zaidiyyah na akiwa ameathirika na fikra na mitazamo ya Imamu Khomeini, aliliweka suala la uadui dhidi ya Marekani na Israel katika nara zake na alibainisha kadhia ya Palestina kuwa ni katika masuala yanayopewa kipaumbele na yeye na harakati yake. Hussein Badreddin al-Houthi alianza harakati zake za kisiasa kwa mapambano dhidi ya upenyaji na ushawishi wa fikra potofu kama Uwahabi. Alikuwa mbunifu wa nara na kaulimbiu mashuhuri ya Wahouthi kwa jina la Sarkha. Hussein Badreddin al-Houthi kutokana na uadui wake na Marekani, aliuawa shahidi na serikali ya Yemen chini ya uongozi wa Ali Abdalluh Saleh.

Nafasi Yake

Hussein Badreddin al-Houthi alizaliwa 1960 katika eneo la Marran katika mkoa wa Saada nchini Yemen. [1] Alikuwa mwanasiasa, kamanda wa kijeshi na muasisi wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen na kiongozi wa kwanza wa harakati hiyo. [2] Madhehebui yake na familia yake yalikuwa Shia Zaidiyyah Jaroudi. [3] Marafiki na walimu wake walikuwa wakimsifu kutokana na kuwa na akili pana, upeo mkubwa wa maarifa, elimu na kujisomea sana. [4] Aidha aliondokea kusifika kwa sifa zingine kama za ushujaa, muono wa mbali na upana wa kifua [5] (kuvumilia mitazamo ya wengine). Nasaba yake inafika kwa Imamu Hassan (a.s). [6] Inaelezwa kuwa, baba yake yaani Badreddin al-Houthi alikuwa mmoja wa Marajii watajika wa madhehebu ya Shia Zaidiyya. [7]

Kumbukumbu na maombolezo ya mauaji ya Hussein Badreddin Houthi huko Sana'a (2023 AD)

Hussein al-Houthi amechukuliwa kuwa mwenye muelekeo wa imani na itikadi za Shia Ith'naasharia ambapo alikuwa akiamini umaasumu wa Maimamu na uwepo wa Imamu Mahdi Muahidiwa. [8] Wengine pia wamesema kwamba alibadilisha madhehebu yake na kujiunga na mashehebu ya Shia Ith'naasharia. [9]

Kwa mujibu wa baadhi ya watafiti ni kuwa, harakati mbalimbali za makundi kama vile ya Uwahabi, Ikhwanul Muslimin, Ujamaa, Nasiriyah, na kutokea kwa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kulikuwa na taathira katika kuundika fikra za Hussein al-Houthi. [10] Harakati za kivyama na mashauriano na wasomi na wanazuoni wa na wa mataifa mengine ni mambo mengine yaliyochangia kuundika wa mfumo wa kifikra wa Houssein al-Houthi. [11] Hotuba zake zilizokuwa na anuani ya Malazim zimekusanywa na zinatumiwa na wanachama wa Harakati ya Ansarullah kama hati ya kiitikadi ya harakati hiyo. [12]

Hussein al-Houthi alijifunza masomo ya dini kutoka kwa babake. [13] Baada ya kuhitimu katika fani ya fasihi, alienda Sudan kwa ajili ya kukamilisha masomo yake. [14] Ameandiika vitabu kadhaa na maarufu zaidi ni Al-Sarkha Fi Wajh Al-Mustakbirin.

Fikra na Mitazamo

Hussein Badreddin al-Houthi aliamini kwamba ulimwengu wa Kiislamu umekumbwa na hali ya kuzorota na njia pekee ya kuuokoa ni kurudi kwenye Qur'ani na mafundisho yake. [15]

Mtazamo Kuhusu Israel

Kuchukia ubeberu ni miongoni mwa zilizohesabiwa kuwa moja ya sifa zake maalumu. Daima aliwaonya watu wa Yemen kuhusu ushawishi na upenyaji wa Marekani katika nchi hiyo. [16] Kwa mtazamo wake, uhuru wa Palestina ulionekana kuwa kitovu cha mwamko na ustawi wa Waislamu. [17] Alisisitiza juu ya kuadhimisha na kuhuishwa Siku ya Quds na juu ya ulazima wa kuwekewa vikwazo vya bidhaa za Israel na Marekani. Sayyid Hussein hakuwa na matumaini kwa watawala wa nchi za Kiislamu kwa ajili ya ukombozi wa Palestina. [18] Aliona kuwa, maelewano na mapatano yoyote na Israeli ni kitu kisichowezekana kutokana na ukiukaji wa ahadi wa Israel. [19]

Mtazamo Wake Kuhusu Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Imamu Khomeini

Sayyid Hussein al-Houthi aliichukulia njia ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kuwa ndiyo njia pekee ya uhuru wa mataifa ya Kiislamu. [20] Alikuwa akiutambulisha mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuwa kigezo mwafaka kwa ajili ya Waislamu na alikuwa akiamini kwamba, kila ambaye atasimama dhidi ya Mapinduzi ya Kislamu, Mwenyezi Mungu atamuadhibu. [21]

Al-Houthi alikuwa akiamini kwamba, hatua ya Imamu Khomeini ya kuhusisha suna ya kujibari na washirikina iliwafanya watu watambue maana sahihi na ya Qur'an ya ibada ya Hija. [22] Aidha alikuwa akimuita muasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Ruhuullah Khomeini kwa jina la Imamu na alikuwa akitambua fikra za Imamu Khomeini kuwa ni za uokozi. [23] Alikuwa akimtambua Imamu Khomeini kama rehma ya Mwenyezi Mungu kwa mataifa ya Kiarabu na alikuwa akisema, Waarabu wamejinyima wenyewe neema hii. [24] Kadhalika alikuwa akimtambua Imamu Khomeiini kuwa ni Imamu muadilifu, mwenye taqwa (kumuogopa Mwenyezi Mungu) na mwenye kujibiwa dua (Mustajab al-Da'wah). [25]

Harakati za Kisiasa na Kijamii

Hussein al-Houthi alianza harakati zake za kisiasa kwa kupambana na ushawishi na upenyaji wa Uwahabi nchini Yemen. [26] Mnamo 1993, akiwa na lengo la kupambana na umasikini akiwakilisha jimbo la Saada [27] na kwa tiketi ya chama cha Haqq [28] aliingia katika Bunge la Wawakilishi la Yemen. [29] Alisisitiza juu ya kuweka maelewano katika mzozo kati ya chama cha General Congress na vyama viwili, Congress na Reform, na alikataa kujiunga na serikali katika kuanzisha vita. [30]

Seyyed Hussein alikataa kuhudhuria muhula uliofuata wa Baraza la Wawakilishi na akaanzisha Jumuiya ya Shabab Al-Mu'min [31], ambayo baadaye iliitwa Harakati ya Ansarullah ya Yemen. Lengo la awali la kuunda juumuiya hii lilikuwa ni kuendesha shughuli za kiutamaduni. [33] Baada ya tukio la Septemba 11 na shambulio la Marekani dhidi ya Afghanistan na Iraq na uwepo wake kijeshi katika eneo (Mashariki ya Kati) na Ghuba ya Aden, harakati za Seyed Hossein dhidi ya ubeberu na dhidi ya Marekani zilianza. [34] Alikuwa akiamini kwamba, tukio la Septemba 11 lilifanywa na vyombo vya kijasusi vya Marekani na lengo lilikuwa ni kupata kisingizio cha kushambulia nchi za Kiislamu. [35] Al-Houthi aliifanya Siku ya Palestina kuwa mwanzo wa harakati yake na kwa kutoa hotuba ya kwanza siku hii, aliwasomea tena watu maneno ya Imam Khomeini kuhusu Siku ya Kimataifa ya Quds. [36] Alifanya maandamano tofauti tofauti dhidi ya Marekani. [37] Alibuni nara na kaulimbiu mashuhuri ya Wahouthi dhidi ya Marekani na Israel inayojulikana kwa jina la Sarkha. [38]

Hussein al-Houthi alifanya shughuli nyingi za kijamii kwa watu wa eneo lake, ambapo miongoni mwa harakati hizo, ni pamoja na kuunda jumuiya ya hisani (masuala ya kheri) ya Marran, kuasisi shule za kidini, kuanzisha vituo vya afya na shughuli mbalimbali za ujenzi. [39]

Kukufurishwa na Kuuawa

Kaburi la Hussein Badr al-Din Houthi kabla ya kuharibiwa na Mawahabi

Harakati za al-Houthi dhidi ya Israel na Marekani zilipelekea kutolewa kwa fat’wa ya kukufurishwa na kuuawa kwake na wanazuoni waliofungamana na mfumo wa utawala wa Yemen. [40] Walidai kwamba Sayyid Hussein anadai kuwa Unabii, Umahdi na Uimamu. [41] Mnamo 2004, wafuasi 640 Hussein al-Houthi waliokuwa wakiandamana walikamatwa [42]. Kisha serikali iliyokuwa ikitawala ya Yemeni ikatangaza kitita cha dola 55,000 kwa atakayetoa taarifa zitakazopelekea kukamatwa Hussein al-Houthi. [43] Baada ya kuuawa kwa jamaa zake wa karibu wapatao 25 na serikali ya Yemen, kiasi hiki kiliongezwa hadi dola 75,000. [44] Siku sita baada ya Abdullah Saleh kurejea kutoka Marekani, vita vya serikali dhidi ya Wahouthi vilianza. [45] Kwa mujibu wa ushuhuda wa nyaraka za siri vita hivi vilifanyika kwa makubaliano baina ya Georg W. Bush Rais wa wakati huo wa Marekani na Ali Abdullah Saleh maafikiano ambayo yalifikiwa mjini Washington. [46]

Kuuawa Shahidi

Picha juu ya jalada la kitabu cha Uweys Khomeini

Mnamo 2004, (mwafaka na 1425 Hijria) Hussein al-Houthi alizingirwa kwa muda wa siku 80 na jeshi la serikali ya Yemen inayoongozwa na Ali Abdullah Saleh katika eneo la Marran. [47] Kulingana na chanzo kimoja baada ya kusimama kidete na kupambana kiume, hatimaye aliuawa shahidi. [48] Kulingana na ripoti nyingine, baada ya kujeruhiwa kichwani na miguuni na kupoteza uwezo wake wa kuona alipatiwa amani; lakini baada ya kukamatwa, aliuawa shahidi. [49] Inasemekana kwamba katika vita hivi, Wahouthi 700 na wajeshi wa jeshi la Yemen 15,000 waliuawa. [50] Baada ya kifo cha Seyed Hussein al-Houthi, kamanda wa Jeshi la Kati la Marekani alituma barua kwa Ali Abdullah Saleh akimpongeza na kumshukuru. [51]

Mnamo 2013, mwili wa Sayyid Hussein ulikabidhiwa kwa familia yake na kuzikwa huko Marran. [52] Baadae kukajengewa jengo katika kaburi lake na mwaka 2015 lilibomolewa kufuatia mashambulio ya muungano wa Saudi Arabia. [35]

Monografia

  • Uweys Khomeini; Jonbesh al-Houthi Yemeni va Didgahaye Shahid Hussein al-Houthi. Kitabu hiki kimeandikwa na Hamidreza Gharibreza. Kitabu hiki kilichapishwa na Ofisi ya Uenezaji wa Maarifa. [54]