Harakati ya Khorasani

Kutoka wikishia

Harakati ya Khorasani (Kiarabu: خروج الخُراسانيّ) ni katika alama na ishara za kudhihiri Imam Mahdi (a.t.f.s) ambapo imekuja katika hadithi mbalimbali ya kwamba, mtu kutoka katika watu wa Khorasan atajitokeza na kuanzisha harakati sambamba na kuibuka harakati ya Sufiyani na harakati ya Yamani. Baadhi ya wahakiki wamemtambua Bwana huyu kwa jina la mtu mwenye bendera za rangi nyeusi ambapo jeshi lake likiongozwa na kamanda Shuaib bin Swaleh litaishinda harakati ya Sufiyani.

Hata hivyo kuna mitazamo tofauti baina ya wahakiki na watafiti wa imani ya Mahdawiat (kuamini kwamba, mwisho wa zama atakuja mkombozi ambaye atakuja kuijaza dunia uadilifu na usawa baada ya kujaa dhulma na uonevu) kuhusiana na bendera zenye rangi nyeusi. Baadhi wanaamini kuwa, makusudio ya bendera zenye rangi nyeusi ni bendera ya Abu Muslim Khorasani ambaye alianzisha harakati dhidi ya utawala wa Bani Umayya na baadhi yao wanaamini kwamba, bendera hizi zinaashiria harakati ambayo itaibuka na kutokea kabla ya kudhihiri Imam Mahdi (a.t.f.s).

Sayyid Khorasani

Katika hadithi kumetajwa harakati ya mtu anayejulikana kama Khorasani kwamba, ni katika ishara na alama za kudhihiri Imam Mahdi (a.t.f.s). [1] Neno Khorasani lililokuja katika hadithi linahusiana na Khorasan mashariki mwa ardhi (mashariki mwa ardhi za Kiiislamu) na mtu ambaye ataanzisha harakati akiwa pamoja na watu wa Khorasan. [2]

Katika hadithi tajwa hakujabainishwa sifa maalumu za Khorasani kama vile kuwa kwake ni Sayyid (anayetokana na kizazi cha Mtume). [3] Pamoja na hayo Ali Kurani anasema katika kitabu chake cha Asr al-Dhuhur, katika vyanzo vya Ahlu-Sunna [4] na vilevile katika vyanzo vya baadaye vya Mashia, Khorasani ametambuliwa kuwa anatokana na kizazi cha Imamu Hassan (a.s) au Imamu Hussein (a.s) na ametajwa kama Khorasani Hashemi [5]. Kwa muktadha huo, Khorasani anatajwa na kujulikana pia kama Sayyid Khorasani. [6] Kadhalika katika vyanzo hivi kumetajwa sifa zake nyingine kama vile katika shavu lake la kulia na katika mkono wake wa kulia kuna kiwaa (alama ya doa). [7]

Je, Harakari ya Khorasani ni Alama ya Kudhihiri Imam Mahdi (a.s)?

Harakati ya Khorasani sambamba na ngurumo au sauti kali kutoka mbinguni, kuuawa nafsi takasifu (nafs Zakiya), kujitokeza Sufiyani na Khasf al-Bayda' (kumezwa eneo la Bayda') ni mambo ambayo yametajwa kuwa ni katika alama za kudhihiri Imam Mahdi mtarajiwa (a.t.f.s). [8] Kwa mujibu wa hadithi ambayo inanasibishwa na Imamu Swadiq (a.s) ni kwamba: Khorasani, Safiyani na Yamani wataanzisha harakati kwa wakati mmoja, wote watatu wataanzisha harakati katika mwaka mmoja, mwezi mmoja na katika siku moja. [9] Aidha imekuja katika hadithi mbalimbali ya kwamba, Harakati ya Khorasani itaanzia mashariki (sehemu ya mashariki mwa ardhi za Kiislamu) na itaelekea upande wa Iraq. [10] Katika Insaiklopidia ya Imam Mahdi (a.t.f.s), hadithi hii imetiliwa shaka kuhusiana na sanadi na mlolongo wake wa mapokezi. [11]

Bendera Nyeusi na Sayyid Khorasani

Makala Asili: Bendera nyeusi

Gwaride la bendera nyeusi linaashiria harakati ya kikundi chenye kubeba bendera za rangi nyeusi katika eneo la mashariki mwa ardhi za Kiislamu ambapo katika baadhi ya hadithi tukio hilii linatajwa kuwa moja ya Alama za kudhihiri Imamu Mahdi (a.t.f.s). Kwa mujibu wa baadhi ya hadithi, bendera hizi ni za kijana anyetokana na Bani Hashim huko Khorasan ambaye wakati wa kutoka na kuanzisha harakati yake Shuaib bin Swaleh ataambatana naye. [13] Baadhi ya wahakiki wa Kishia wanaamini kuwa, makusudio ya bendera nyeusi ni harakati ya Abu Muslim Khorasani ambaye alianzisha uasi na mapambano dhidi ya utawala wa Bani Umayya na kupelekea kushika hatamu utawala wa Bani Abbas. [14] Baadhi ya wahakiki wengine wao wanaamini kwamba, bendera hizi zinaashiria harakati ambayo itaibuka na kutokea kabla ya kudhihiri Imam Mahdi (a.t.f.s). [15]

Ali Kurani, mwandishi wa Kitabu cha Asr al-Dhuhur amemtambua Sayyid Khorasani kuwa ndiye mmiliki wa bendera nyeusi ambaye kamanda wa jeshi lake ni Shuaib ibn Swaleh ambapo kutatokea vita baina ya jeshi lake na Sufiyani na atamshinda Sufiyani. [16] Atatoa baia na kiapo cha utiifu kwa Imam Mahdi (a.t.f.s). [17]

Hata hivyo maneno haya yamekosolewa kwani kitabu cha Asr al-Dhuhur kikiwa na lengo la kuthibitisha haya, kimechukua hadithi kutoka katika kitabu cha al-Fitan kilichoandikwa na Ibn Hammad ambapo ndani yake hakuna jina la Khorasani. Kadhalika kitabu cha al-Fitan hakina itibari kwa Mashia; kwa sababu akthari ya hadithi zake hazijanukuliwa kutoka kwa Maasumu.

Masuala Yanayo Fungamana