Wajibu wa Kumshukuru Mneemeshaji
Wajibu wa Kumshukuru Mneemeshaji (Kiarabu: وجوب شکر مُنعِم) au mfadhili ni istilahi maalumu inayotumiwa na wataalamu wa taaluma ya wanatheolojia. Nayo ni ibara yenye maana ya kwamba; kuwepo kwa hisia ya wajibu ndani ya tabia ya mwanadamu, inayomlazimisha au kumpa msukumo wa kumshukuru yule anayemneemesha mwanadamu. Wajibu huu wa kumshukuru mtoaji wa neema, umechukuliwa kama ni kanuni ya kiakili au hukumu ya kisharia ambayo imethibitishwa kupitia akili, Qur'ani na Hadithi mbali mbali. Miongoni mwa Aya zinazounga mkono suala hili, ni ni ile Aya ya 7 ya Surat Ibrahim, ambayo inatoa ufafanuzi wa kwamba; shukrani za neema huhakikisha kuendelea kwa neema hizo, huku kuifuru neema huwa ndiyo msingi na sababu ya adhabu kali ya Mwenye Ezi Mungu.
Wanazuoni wa Kiislamu wametofautiana kimaoni kuhusiana na asili ya kanuni ya wajibu wa kumshukuru Mneemeshaji. Wafuasi wa Adliyyah (ambao ni Mu‘tazila na Imamia), wanaamini kwamba; hii ni kanuni ya kiakili, ingawa pia imeungwa mkono na kuhimiliwa na Qur’ani pamoja na Riwaya. Hivyo basi hukumu za kisharia zinazounga mkono kanuni hii, ni viimarishi na viashiria tu vya kanuni hii (hukmu irshadi). Wao wanasisitiza maoni yao wakisema; Ni jambo la wazi kabisa (lisilohitaji ithibati) kwamba; ni wajibu kwa mwanadamu kumshukuru Mneemeshaji. Pia wao hutegemea hoja za sira na nyenendo za wenye akili waliotangulia (siratu Al-uqalaa). Kinyume chake, Ash‘ari, walioko katika madhehebu ya kiitikadi ya upande wa Ahlus-Sunna, wao hutegemea Aya za Qur’ani na dalili nyengine maoni yao yasemayo kwamba; Kabla ya kushuka kwa sharia za mbinguni kutumwa kwa Manabii, hakukuwa na hukumu za kiakili inayomhukumu mwanadamu na kumlazimisha kumshukru Mneemeshaji.
Wanazuoni wa Kishia huitumia kanuni hii katika nyanja mbalimbali za sayansi za Kiislamu, ikiwa ni pamoja na theolojia, usul al-fiqh, pamoja na fiqhi. Miongoni mwa maeneo inayotumika kanuni hii, pamoja na matumizi yake katika kuthibitisha wajibu wa mwanadamu kufanya uchunguzi wa masuala ya kiitikadi kabla ya kushikamana nayo. Pia kanunu hii hutumika katika kuthibitisha na umuhimu wa kuwepo kwa ijtihadi, taqlidi (kumfuata mwanazuoni katika utekelezaji wa amali), au ihtiyat (tahadhari), (kutomfuata mwanazuoni katika utekelezaji wa amali, katika hali ambayo wewe mwenyewe ni mwanazuoni mwenye daraja ya ijitihadi).
Utambulisho na Nafa Yake
Kumshukuru Mneemeshaja ni hisia na jukumu la kiakili na kisharia, linalomwajibisha mwanadamu kumshuku yule aliye mneemesha.[1] Elimu hasa inayohusiana na nadharia hii, ni sayansi ya kikalamu (theolojia ya Kiislamu), ingawa wanazuoni wa fiqhi pia nao huchukua na kuitumia kama ni nyenzo maalumu ya kuainisha baadhi ya hukumu za kisheria.[2]
Wafasiri wa Qur’ani wametaja Aya kadhaa kama ni ushahidi wa kuwepo kwa kanuni hii. Miongoni mwa Aya hizo ni pamoja na; Aya ya 11 hadi 15 za Surat Az-Zukhruf,[3] Aya ya 107 ya Surat Al-A‘raf,[4] Aya ya 109 ya Surat Al-An‘am,[5] Aya ya 164 ya Surat Al-Baqarah,[6] pamoja na Aya ya 7 ya Surat Ibrahim.[7] Aya hizi ndizo zinazonabainisha kuwepo kwa wajibu wa mwanadamu katika kuthamini na kushukuru neema za Mwenye Ezi Mungu. Pia kuna masimulizi kadhaa ya Riwaya zinathibitisha uzito wa shukrani juu ya neema za Mwenye Ezi Mungu. Kwa mfano, katika moja ya Hadithi mashuhuri imesimuliwa kutoka kwa Imam Ali (a.s) akisema kwamba: "Hata kama Mwenyezi Mungu hangetoa onyo lolote lile kuhusiana na adhabu ya dhambi, bado kwa ajili ya kushukuru neema zake, ingekuwa ni wajibu kujiepusha na kutenda dhambi."[8]
Pia kanuni hii ya ulazima wa kumshukuru Mneemeshaji, imepewa sisitizo ndani ya mashairi ya washairi mbali mbali. Mathalan, Maulana Jalaluddin Rumi (aliyeaga dunia mwaka mwaka 672 Hijria) ameandika katika moja ya shairi yake akisema:
- Shukrani kwa Mneemeshaji ni amri ya hekima toka kwa Rabana, la si hivyo, lango la ghadhabu ya milele litafunguka bila huruma.[9]
Saadi Shirazi (aliaga dunia mwaka 691 Hijria) naye anaakisi kanuni kupitia shairi lake lisemalo:
- Sipinde wala sikiuke kumshukuru Mneemeshaji Ama sivyo, siku ya malipo ni maskini mhamani.[10]
Msingi wa Akili au wa Kisharia?
Mojawapo ya hitilafu baina ya madhehebu za kiitikadi za Uadiliah na Ash’ariyya, miongoni mwa Waislamu, juu ya msingi wa kumshukukuru Mneemeshaja , ni kwamba je, msingi huu ni wa kimantiki au wa kisheria?[11] Kwa mtazamo wa Adliyya, yaani Mu'tazila[12] na Imamiyya,[13] ni kwamba; kanuni hii imejengeka juu ya misingi na hoja za kiakili, na zile amri na makatazo ya kisharia kuhusiana na kanuni hii, ni sharia au elekezi (amru au hukmu irshadi) tu.[14] Sheikh Ansari (aliyefariki 1281 Hijria), faqih na msomi wa Kishia wa fani ya usul al-fiqhi, anaamini kwamba; mzizi hasa wa suala hili unatokana na tafauti katika welewa wa dhana ya ya husnu na qubhu (asili ya uzuri na ubaya wa mambo mbali mbali) baina ya Adliyya na Ash’ariyya; kumaanisha kwamba iwapo mtu ataitambua akili kuwa ndio chanzo cha kutambua husnu na qubhu (wema na ubaya), huyo atakubaliana na kuwepo kwa ulazima wa kiakili juu ya kumshukuru Mneemeshaji. Lakini iwapo, ataamini wamba, husnu na qubhu ni sifa mbili zitokazo na vipimo vya kisheria tu (kama ilivyo kwa upande wa Ash’ariyya), huyo yeye ataamini kuwa wajibu wa kumshukuru Mneemeshaja unatokana na maamrisho ya kisharia.[15]
- Pia soma: Husnu wa Qubhu
Hoja za Waodai Kuwa ni Kanuni ya Kiakili
Wanazuoni wa elimu ya kalamu wameeleza kuwa msingi wa kiakili wa ulazima wa kumshukuru Mwenye Kuneemesha unatokana na dhati ya jambo lenyewe lilivyo, ambapo akili inahukumu kuwa; shukrani kwa Mneemeshaji ni wajibu usio na shaka ndani yake.[16]
Al-Karajaki (aliyefariki 449 Hijria), ambaye mwanatheolojia mashuhuri wa Kishia, anaeleza kuwa; ulazima wa kumshukuru Mneemeshaji , ni kanuni iliyokubaliwa kwa makubaliano ya wenye akili timamu, bila mzozo wowote wa kimawazo kuhusu ukweli wake.[17] Kuna hoja mbalimbali za kimantiki zilizowasilishwa ili kuimarisha dhana hii. Mathalani, Allamah Hilli (aliyefariki 726 Hijria), mwanazuoni mashuhuri wa elimu ya kalamu na mwanafiqhi wa Kishia, anajenga hoja zake akisema kwamba; ikiwa kumshukuru Mneemeshaja si wajibu wa kiakili, basi hata utafutaji wa maarifa kwa ajili ya kumtambua Yeye hautakuwa na ulazima wowote ule ndani yake. Kutokuwepo kwa wajibu wa kutafuta maarifa hayo kunapelekea kubatilika kwa utumwaji wa mitume manabii kwa wanadamu, jambo ambalo ni lenye kukinzana na misingi ya mafundisho ya kiakili na ya kiwahyi. Kwa hivyo, kumshukuru Mneemeshaji ni wajibu wa kiakili unaojengeka juu ya misingi imara ya mantiki na falsafa.[18]
Hoja za Waodai Kuwa ni Kanuni ya Kisharia
Kwa mujibu wa madhehebu ya Ash’ariyya, kinyume na mtazamo wa Adliyya, ulazima wa kumshukuru Mneemeshaji hautokani na hukumu za kiakili bali unatokana na sharia. Ili kuimarisha mtazamo wao, wao wanaleta hoja zifuatazo:
- Kwanza, Aya ya 15 ya Surat al-Israa na Aya ya 165 ya Suratu an-Nisaa zinaashiria kuwa, kabla ya bi‘tha ya manabii (kutumwa kwa mitume) na kuwekwa au kushushwa kwa sharia, mwanadamu hawezi kustahili adhabu. Kwa mujibu wa mtazamo wa Ash’ariyya, hili linathibitisha kuwa akili kama akili, haina uwezo wa kuhukumu ulazima wa shukrani za kumshukuru Mwenye Ezi Mungu.[19]
Hata hivyo, wapinzani wa hoja hii wanajibu kwamba; Aya hizo zinahusiana na adhabu ya kidunia, na si ya Akhera. Aidha wapainzani hawa wanaendelea wakisema kwamba; sababu halisi ya kuadhibiwa kwa mja fulani, ni uasi wa mtu dhidi ya Mola wake unaoambatana na ufahamu wa asili ya ubaya autendao, bila ya kujali namna yeye alivyouewa uasi huo. Hivyo basi ikiwa mtu, kwa kutumia akili, anatambua asili ya ulazima wa kumshukuru Mwenye Ezi Mungu kisha akalikaidi suala hilo, huyo atakuwa ni mwenye kustahili adhabu.[20]
- Pili, Ash’ariyya wanadai kwamba dhana ya ulazima wa kumshukru Mneemeshaji, haiwezi kueleweka bila kuwepo kwa amri ya Mwenye Ezi Mungu, kwani kabla ya amri hiyo, hakutakuwa na maana ya kuwepo kwa ulazima huo. Kwa mtazamo wao, thawabu ni matokeo ya utiifu wa amri za Mungu, na adhabu hutokana na uasi dhidi ya amri hizo, hivyo basi dhana hizi hupata maana kamili baada ya kuwekwa kwa makatazo na amri za Mwenyezi Mungu.[21] Wapinzani wa hoja hii wanapinga mtazamo huo kwa kusema kuwa; kinachozungumziwa hapa ni wajib wa kiakili, yaani, ulazima unaotokana na mantiki na dhana ya haki na ya msingi, na si wajib wa kisheria, ambao unatokana na utekelezaji wa sharia za Mwenye Ezi Mungu.[22]
Mifano ya Utumiaji wa Kanuni Hii Katika Taaluma za Dini
Katika taaluma mbalimbali za dini, dhana ya wajibu wa kumshukuru Mneemeshaji imekuwa mhimili wa hoja za kiakili, inayotumika katika fani tofauti za kidini. Miongoni mwa maeneo mnamotumika dhana hii ni kama ifuatavyo:
Ulazima wa Uchunguzi wa Kina Katika Itikadi
Katika jitihada za kuthibitisha wajibu wa kuchunguza uwepo wa Mungu sambamba na masuala mengine ya kiimani, wataalamu wa theolojia wamejenga hoja zao juu ya kanuni mbili kuu, wakitumia kanuni hizo kama ndiyo misingi ya mantiki na kiakili. Nazo ni; kanuni ya wujub daf‘i dharar muhtamal (wajibu wa kujihadhari na madhara yanayoweza kutokea)[23] na wujub shukr al-mun‘im (wajibu wa kumshukuru Mneemeshaji).[24] Mchakato wa hoja zao unafuata mpangilio ufuatao:
- Kumshukuru Mwenye Kuneemesha ni wajibu wa kiakili.
- Shukrani haziwezi kuwa timilifu bila kumtambua Mwenye Kuneemesha na wala haiwezekani kushukuru kikamilifu asiyefahamika.
- Utambuzi wa Kumtambua Mwenye Kuneemesha unapatikana kupitia uchunguzi na uhakiki wa kina.
- Kwa hivyo, kuchunguza Juu ya Uwepo Mwenye Kuneemesha ni wajibu wa kiakili na wa lazima kwa kila mtu mwenye busara.[25]
Misingi ya Kitheolojia ya Fani ya Usul al-Fiqh
Baadhi ya wataalamu wa fani ya usul al-fiqhi (misingi ya ufahamu wa sharia za fiqhi), wamesema kwamba; wajibu wa kumshukuru Mneemeshaji, ni moja ya misingi ya kitheolojia ya sayansi ya usul al-fiqhi. Wao wanasema kwamba; Allama Hilli aliihisabu kanuni hii kama ni moja ya misingi ya kitheolojia ya usul al-fiqhi na akafungua mlango maalumu katika kujadili juu ya kanunu hiyo.[26]Sheikh Bahai ambaye ni mwanazuoni mwengine wa fani ya usul al-fiqhi, ambaye aliitaja na kuichunguza kanuni hii, kisha kuitambua kama ni moja ya misingi ya kitheolojia ya fani ya usul al-fiqhi.[27]
Msingi wa Tatu: Ijtihad, Ihtiyat, na Taqlid
Moja kati ya marejeo makuu yanayorejelewa katika kuthibitisha kanuni hii (wajibu wa kumshukuru Mneemeshaji), yanapatikana katika mjadala mitatu, ambayo ni; ulazima wa kufanya ijtihad (juhudi za kutambua hukumu za kisheria), ulazima wa ihtiyat (kutofuata mjitahidi kwa aliyefikia cheo cha ijitihadi), pamoja na ulazima wa taqlid (kumfuata mwanasheria mwenye sifa katika matendo ya kidini). [28] Kwa mujibu wa kanuni hii (wajibu wa kumshukuru Mneemeshaji), akili inaamini kuwa; ni wajibu wa mwanadamu kumshukuru Mneemeshaji. Na haiwezekani kwa mtu fulani kutimiza shukrani hizo bila ya kuwa na ufahamu wa sheria za Mneemeshaji. Hivyo basi, ni lazima kwa wanadamu kushikamana na mambo yafuatayo:
- Kufanya ijtihad: Kujifunza kuchambua na kutoa hukumu za kidini kwa kujitegemea mwenyewe (na kuwa tegemeo la wengine).
- Kuchukua ihtiyat: Tahadhari maalumu kwa aliyefikia daraja ya ijitihadi ila bado hajaruhusu watu kumfuata, ambaye hufanya matendo yake kwa uangalifu mkubwa ili kuhakikisha sheria za Mwenye Ezi Mungu zinatekelezwa.
- Kufanya taqlid: Kumfuata mwanasheria mwenye sifa na ujuzi wa kutosha.[28]
Rejea
- ↑ Hashimi Shahroudi, Farhange Fiqh, 1382 S, juz. 6, uk. 447; Sanu, Mu'ujam Mustalahat Usul al-Fiqh, 1427 AH, uk. 250.
- ↑ Hashimi Shahroudi, Farhange Fiqh, 1382 S, juz. 6, uk. 447
- ↑ Hakim Jeshmi, Al-Tahdhib Fi al-Tafsir, 1440 AH, juz. 9, uk. 6287.
- ↑ Tabarsi, Majma'u al-Bayan, 1408 AH, juz. 4, uk. 701.
- ↑ Abul-Fatuh Razi, Rawdh al-Jinan, 1371, juz. 7, uk. 410.
- ↑ Fakhr al-Razi, Al-Tafsir al-Kabir, 1420 AH, juz. 4, uk. 173.
- ↑ Tabataba'i, Al-Mizan, 1352 S, juz. 12, uk. 23.
- ↑ Nahj al-Balagha, Hekima ya 290.
- ↑ Rumi, Muthnawa Maanawi, 1376 S, juz. 1, uk. 448.
- ↑ Saadi, Kuliyaat Saadi, 1320 S, uk. 208
- ↑ Shahrestani, Al-Milalu wa al-Nihal, 1415 AH, juz. 1, uku. 55-56; Othman, Al-Qamous al-Mubiin, 1423 AH, uk. 192.
- ↑ Tizama: Qadhi Abdul-Jabbar, Al-Mughni, Beta, juz. 15, uk. 27.
- ↑ Tizama: Al-Ka'ashif al-Ghittaa, Asl al-Shi’a wa Usuliha, 1413 AH, uk. 76; Subhani Tabrizi, Al-Insaf, 1381, juz. 3, 37.
- ↑ Al-Talqani, Al-Sheikhiya, Nash-atuha wa Tatawuriha wa Masdar Dirasatiha, 1420 AH, uk. 299.
- ↑ Sheikh Ansari, Matarih al-Indhar, 1404 AH, uk. 231.
- ↑ Tizama: Karajaki, Kanzul al-Fua'd, 1410 AH, juz. 1, uk. 221; Sheikh Tusi, Al-Tabiyan, Dar Ihya Al-Turath Al-Arabi, Juz. 7, uk. 340; Allama Hilli, Hassan ibn Yusuf, Mabadiu al-Usull, 1404 AH, uk. 93.
- ↑ Tizama: Karajaki, Kanzul al-Fua'd, 1410 AH, juz. 1, uk. 221.
- ↑ Allamah Hilli, Tahdhib al-Usul, 1380 S, uk. 54.
- ↑ Fakhr Razi, Al-Mahsul Fi Ilm Usul Fiqh, 1420 AH, juz. 1, uk. 67.
- ↑ Kashif al-Ghita, Ghayat al-Mamul, Beta, uk. 199.
- ↑ Al-Ghazal, Al-Mustasfi, 1413 AH, uk. 49.
- ↑ Mudhaffar, Dalail al-Sidqi, 1422 AH, juz. 2, uk. 159.
- ↑ Tizama: Ibn Maytham, Qawaid al-Maram, 1406 AH, uk. 28–29.
- ↑ Hashimi Shahroudi, Farhange Fiqh, 1382 S, juz. 6, uk. 447.
- ↑ Ibn Nawbakht, Al-Yaqout, 1413 AH, uk. 27; Sheikh Tusi, Tamhid al-Usul, 1362 S, uk. 206; Ibn Maytham, Qawaid Al-Maram, 1406 AH, uk. 29; Fadhil Miqdad, Al-Itimad, 1412 AH, uk. 48.
- ↑ Dhamir, Daneshname Usuliyan Shia, uk. 323.
- ↑ Dhamir, Daneshname Usuliyan Shia, uk. 323.
- ↑ Hakim, Mustamsik al-Urwat al-Wuthqa, 1374 S, juz. 1, uk. 6; Muwahidi Najafi, al-Burhan al-Sadid Fi al-Ijtihad wa al-Taqlid, 1387 S, uk. 36-34; Saifi Mazandarani, Dalil Tahrir Al-Wasilah, 1436 AH, uk. 3; Sanad, Sanad al-Urwat al-Wuthqa (Ijtihad na Taqlid), 1394 S, juz. 1, uk. 23-24.
Vyanzo
- Al-Taliqani, Muhammad Hassan, Al-Sheikhiyyah Nash'atuha wa Tatawwuriha wa Masadir Dirasatuha, Beirut, Al-Amal Lil-Mathbu'at, 1420 H.
- Al-Kashif al-Ghitha', Muhammad Hussein bin Ali, Asl al-Shi'ah wa Usuluha, Beirut, Al-A'lami Lil-Mathbu'at, 1413 H.
- Ibnu Nubakht, Ibrahim bin Nubakht, Al-Yaqout Fi Ilm al-Kalam, Qom, Maktabah Ayatullah al-Udhma al-Mar'ashi al-Najafi (r.a), 1413 H.
- Abul Futuh Razi, Hussein bin Ali, Rawdh al-Jinan wa Ruh al-Jinan Fi Tafsir al-Qur'an, Mashhad, Astan Quds Radhawi, Bunyad Pazuheshhaye Islami, 1371 S.
- Ibnu Fahd Hilli, Ahmad bin Muhammad, 'Uddat al-Da'i, Qom, Dar al-Kitab al-Islami, 1407 H.
- Ibnu Maytham, Maytham bin Ali, Qawa'id al-Maram Fi Ilm al-Kalam, Qom, Maktabah Ayatullah al-Udhma al-Mar'ashi al-Najafi (r.a), 1406 H.
- Ashtihardi, Ali Panah, Madarik al-Urwah, Tehran, Munadhamat al-Auqaf wa al-Shu'un al-Khairiyyah, Dar al-Uswat Lil-Tiba'ah wa al-Nashr, 1417 H.
- Hakim Jashami, Muhsin bin Muhammad, Al-Tahdzib fi al-Tafsir, Kairo, Dar al-Kitab al-Mishri, 1440 H.
- Hakim, Sayyid Muhsin, Mustamsak al-Urwah al-Wutsqa, Qom, Dar al-Tafsir, 1374 HS.
- Sanu, Quthb Musthafa, Mu'jam Musthalahat Ushul al-Fiqh, Damaskus, Dar al-Fikr, 1427 H.
- Subhani Tabrizi, Ja'far, Al-Insaf fi Masa'il Dama Fiha al-Khilaf, Qom, Mu'assasah al-Imam al-Shadiq (as), 1381 HS.
- Saa'di, Mushlih al-Din, Kulliyat Sa'di, Tahqiq Muhammad Ali Furughi, Tehran, Chapkhaneh Barukhaim, 1320 HS.
- Sand, Muhammad, Sand al-Urwah al-Wutsqa (Al-Ijtihad wa al-Taqlid), Beirut, Dar al-Kaukhab, 1394 HS.
- Sayyid Radhi, Muhammad bin Husain, Nahj al-Balaghah, Tahqiq Shubhi Shalih, Qom, Hijrah, 1414 H.
- Saifi Mazandarani, Ali Akbar, Dalil Tahrir al-Wasilah (Al-Ijtihad wa al-Taqlid), Qom, Mu'assasah Tanzhim wa Nasyr Atsar al-Imam al-Khomeini (Quds Sarrahu), 1436 H.
- Shahrastani, Muhammad bin Abdul Karim, Al-Milal wa al-Nihal, Beirut, Dar al-Ma'rifah, 1415 H.
- Sheikh Anshari, Murtadha bin Muhammad Amin, Matharih al-Anzhar, Qom, Mu'assasah Al al-Bait (alaihim al-salam) li-Ihya al-Turats, 1404 H.
- Sheikh Bahai, Muhammad bin Husain, Zubdah al-Ushul ma'a Hawasy al-Musannif 'Alaiha, Qom, Dar al-Basyir, 1383 HS.
- Sheikh Tusi, Muhammad bin Hassan, Al-Tibyan Fi Tafsir al-Qur'an, Beirut, Dar Ihya al-Turats al-Arabi, tanpa tahun.
- Sheikh Tusi, Muhammad bin Hassan, Tamhid al-Ushul Fi Ilm al-Kalam, Tehran, Intisharat Daneshgah Tehran, 1362 HS.
- Dhamiri, Muhammad Ridha, Danishnameh Ushuliyan Shia, Qom, Bustan Kitab, 1387 HS.
- Tabataba'i, Sayyid Muhammad Hussein, Al-Mizan fi Tafsir al-Qur'an, Beirut, Al-A'lami fi al-Mat-bu'at, 1352 HS.
- Tabarsi, Fadhl bin Hassan, Majma'u al-Bayan Fi Tafsir al-Qur'an, Beirut, Dar al-Ma'rifah, 1408 H.
- Utsman, Mahmud Hamid, Al-Qamus al-Mubin fi Ishtilahat al-Ushuliyyin, Riyadh, Dar al-Zahim, 1423 H.
- Allamah Hilli, Hasan bin Yusuf, Mabadi al-Wushul ila Ilm al-Ushul, Qom, Mathba'ah al-Ilmiyyah, 1404 H.
- Ghazali, Muhammad bin Muhammad, Al-Mustashfa fi Ilm al-Ushul, Beirut, Dar al-Kutub al-Ilmiyyah, 1413 H.
- Fadhil Miqdad, Miqdad bin Abdullah, Al-I'timad fi Sharh Wajib al-I'tiqad, Mashhad, Astana al-Radhawiyyah al-Muqaddasah, Majma'u al-Buhuth al-Islamiyyah, 1412 H.
- Fakhruddin Razi, Muhammad bin Umar, Al-Tafsir al-Kabir, Beirut, Dar Ihya al-Turath al-Arabi, 1420 H.
- Qadhi Abdul-Jabbar, Abdul-Jabbar bin Ahmad, Al-Mughni Fi Abuwab al-Tauhid wa al-Adl, Tahqiq Qasim Mahmud Muhammad.
- Kashif al-Ghitha', Ja'far bin Khidhr, Ghayat al-Ma'mul.
- Karajaki, Muhammad bin Ali, Kanzu al-Fawaid, Qom, Dar al-Dhakhair, 1410 H.
- Mazandarani, Muhammad Salih, Sharh Usul al-Kafi, Beirut, Dar Ihya al-Turath al-Arabi, 1429 H.
- Mudhaffar, Muhammad Hassan, Dalail al-Sidq Li Nahj al-Haq, Qom, Mu'assasat Ahlul-Bait (a.s) li-Ihya al-Turath, 1422 H.
- Muwahhidi Najafi, Muhammad Baqir, Al-Burhan al-Sadid Fi al-Ijtihad wa al-Taqlid, Qom, Dar al-Tafsir, 1387 S.
- Mawlawi, Muhammad bin Muhammad, Mathnawi Maa'nawi, Tahqiq Abdul Karim Saush, Tehran, Intisharat Ilmi Farhangi, 1376 S.
- Hashimi Shahrudi, Mahmud, Farhang Fiqh Muthabiq Mazhab Ahlul-Bait (a.s), Qom, Mu'assasat Dairat al-Ma'arif Fiqh Islami bar Madhhab Ahlul-Bait (a.s), 1382 S.