Kutekeleza ahadi

Kutoka wikishia

Kutekeleza ahadi (Kiarabu: الوفاء بالعهد) ni katika tabia njema za kimaadili, jambo ambalo limekokotezwa na kutiliwa mkazo katika Qur'ani na hadithi. Kwa mujibu wa hadithi mbalimbali za Kiislamu, kutekeleza au kutimiza ahadi ni katika asili ya dini, ishara ya yakini na kiini cha dini zote. Katika Qur'ani Tukufu, Mwenyezi Mungu ameisifu sifa hii na katika hadithi imetambulishwa kama sifa maalumu ya Maimamu wa Shia.

Wafasiri wa Qur'an wanasema kuwa, katika Qur'ani tukufu Mwenyezi Mungu amewasifu watu waaminifu na amewatambulisha kuwa miongoni mwa waumini, wakweli, wanaoswali, waliofaulu na kwamba ni watu wa peponi. Kwa mujibu wa Aya za Qur'an, kutekeleza ahadi ndiyo sababu ya kuwa pamoja na Mtume (s.a.w.w) siku ya Kiyama.

Umuhimu

Kutimiza ahadi kumetambuliwa kuwa maana yake kufanya kikamilifu kile ambacho mtu amejitolea kufanya. [1] [1] Mojawapo ya sifa muhimu zaidi za kimaadili ni kutekeleza ahadi na mkataba, na kuvunja au kukiuka ahadi kunahesabiwa kuwa mojawapo ya tabia mbaya zaidi za kimaadili. [2]

Ayatullah Makarem Shirazi anasema kuwa, jambo hili limezungumziwa kwa mapana na marefu katika Aya za Qur'an na hadithi na kukemewa kwa maneno makali kabisa na kutiliwa mkazo juu ya udharura wa kutekeleza ahadi. Aidha suala la kuvunja na kukiuka ahadi na makubaliano limekemewa mno. [3]

Katika hadithi suala la kutekeleza ahadi limetajwa kuwa ni asili na msingi wa dini na kwamba, ni ishara ya yakini. [4] Kutekeleza ahadi kumetambulishwa kuwa ni kigezo cha kumuamini Mwenyezi Mungu na siku ya malipo, [5] na kuvunja ahadi klunaelezwa kuwa kunalingana na kutokuwa na dini. [6] Inaelezwa katika hadithi iliyopokewa kutoka kwa Imamu Sajjad (a.s) ya kwamba, kutekeleza ahadi ni moja ya mambo matatu ambavyo ni kiini cha dini zote. [7] Katika Nahaj al-Balagha pia, kutekeleza ahadi kumetambuliwa kuwa moja ya wajibu muhimu zaidi za Mwenyezi Mungu. [8]

Kutekeleza ahadi; sifa ya Mwenyezi Mungu, Mitume na Maimamu

Baadhi ya wafasiri wa Qur'an wanasema kuwa, katika Qur'ani Mwenyezi Mungu amejipa sifa ya muaminifu. [9] Katika Qur'ani Tukufu Nabii Ismail ametajwa kwa sifa ya "Swadiq al-Waad" (mkweli mwenye kusadikisha ahadi). [10] Kutekeleza ahadi imetajwa kuwa moja ya sifa za Maimamu wa Kishia hususan Imamu Hussein (a.s). [11]

Wajibu wa kutekeleza ahadi; ni katika hukumu za Qur'an

Makala kuu: Aya ya wajibu wa kutekeleza ahadi

Mafakihi wakitegemea Aya isemayo: (أَوفوا بِالعُقودِ ; timizeni hadi) [12] wametoa hukumu ya kuwa wajibu kutekeleza ahadi ya mikataba yote na katika vitabu vya fikihi, wamejadili maudhui hii kwa mapana na marefu. [13] Katika kitabu cha Farhang Qur'an (Utamaduni wa Qur'an), Hashimi Rafsanjani akitegemea Aya za Qur'an [4] anasema kwamba, kutimiza ahadi ni miongoni mwa wajibu ambazo [15] Mwenyezi Mungu amezibainisha wazi katika Aya kadhaa na kutoa amri juu ya hilo. [17]

Rezai Isfahani, mtafiti wa masuala ya Qur'an akitegemea kama hoja baadhi ya Aya za Qur'an [18] ameandika, mwanadamu ana jukumu na masuuliiya mbele ya ahadi na mambo aliyojifunga nayo na endapo atakiuka hayo basi ataitwa na kuulizwa juu ya hilo. [19]

Athari za uaminifu katika Qur'an

Watafiti wa masuala ya Qur'an na kwa mujibu wa Aya za Qur’an tukufu wametaja athari za kutekeleza ahadi ambapo baadhi yazo ni kuwa jirani na Mtume (s.a.w.w) siku ya Kiyama, [20] kupata dhama ya kuingia peponi, [21] kupata ujira mkubwa, [22] kuwa sababu ya kufaulu, kupata nusura, izza na heshima. [23]

Kutekeleza ahadi ni kanuni jumuishi ya dunia

Ayatullah Makarim Shirazi ameandika, kwa mujibu wa hadithi, kutekeleza ahadi ni kanuni na sheria jumuishi na ya ulimwengu wote ambapo inawahusu Waislamu na makafiri pia. [24] Ayatullah Makarim Shirazi anaamini kuwa, ulazima wa kufungamana na ahadi, makubaliano na mkataba ni jambo lililoko katika fitra na maumbile ya mwanadamu na ni kutokana na sababu hiyo ndio maana kaumu na mataifa yote, yawe yana itikadi na imani ya dini au yasiwe nayo, lakini yanalihesabu jambo hilo kuwa ni la lazima. [25] Akitegemea Aya ya 177 Surat al-Baqarah [26] (Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi. Bali wema ni wa anaye muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii, na anawapa mali, kwa kupenda kwake, jamaa na mayatima na masikini na wasafiri, na waombao, na katika ugombozi, na akawa anashika Sala, na akatoa Zaka, na wanao timiza ahadi yao wanapo ahidi, na wanao vumilia katika shida na dhara na wakati wa vita; hao ndio walio sadikisha, na hao ndio wajilindao), anabainisha kwamba, mafuhumu na maana ya kutimiza au kutekeleza ahadi katika Qur’ani hakujawekewa sharti lolote bali hilo linajumuisha ahadi zote za Mwenyezi Mungu na ahadi na makubaliano ya watu baina yao, iwe ni Waislamu au makafiri na madhali wanafungamana na ahadi zao Waislamu nao wanapaswa kuheshimu na kufungamana na ahadi zao na kutokiuka makubaliano waliofikia au ahadi waliotoa. [27]

Imekuja katika barua ya Imamu Ali (a.s) kwa Malik Ashtar kwamba: Watu wote wa dunia kutokana na hitilafu za kifikra na mielekeo waliyonayo wanakubaliana kuhusiana na suala la kutekeleza ahadi; hata washirikina katika zama za ujahilia walikuwa wakichunga na kuheshimu hilo. Katika barua hii, Malik Ashtar ametakiwa kufungamana na ahadi zake na makafiri. [28]

Sifa maalumu za uaminifu

Kwa mujibu wa Allama Tabatabai, katika Qur’ani waaminifu wametambulishwa kwa sifa maalumu; miongoni mwazo ni: Wamo katika orodha ya wenye akili na wenye fikra, waunganishaji wa mafungano ya Kimwenyezi Mungu, ni wenye kumuogopa Mwenyezi Mungu, wana subira na ni wenye kusali (kutekeleza ibada ya Sala) ambapo wanapambana na mambo mabaya na machafu kupitia mambo mema. [29] Rezaei Isfahani, mtafiti wa masuala ya Qur’ani ameandika: Katikka Aya miongoni mwa Aya za Qur’ani waaminifu wametajwa kwa sifa kama wahisani, [30] na watu wenye imani. [31] [32]