Kudhihirisha Sauti

Kutoka wikishia

Al-Jahr (Kiarabu: الجهر) ni kudhihirisha sauti au kusali kwa sauti na kwa mujibu wa kauli mashuhuri ni wajibu kwa mwanaume kusoma kwa sauti alhamdu na sura katika Sala ya Asubuhi na rakaa mbili za mwanzo za Sala ya Magharibi na Isha. Maudhui ya Jahr (kudhihirisha sauti) hujadiliwa katika milango ya Sala, Hija na dia na ina hukumu zake maalumu. Kundi miongoni mwa mafakihi linasema kuwa, kigezo cha kudhihirisha sauti ni kudhihiri kiini cha sauti na kuainisha hilo liko mikononi mwa ada na mazoea ya watu. Aidha mafakihi wanasema kuwa, ni mustahabu kudhihirisha sauti katika ibada kama za Sala ya Ayaat, Sala ya Ijumaa, Sala za Idi Mbili, Sala ya kuomba mvua, kusoma kunuti na kusoma talbiya kwa wanaume. Kwa mujibu wa nadharia mashuhuria ya mafakihi, ni makuruhu (haipendezi) kwa maamuma kudhihirisha sauti katika kusoma dhikri zingine za Sala. Hata hivyo ni wajibu kusoma kimya kimya na bila kunyanyua sauti (ikhfat) tasbihi nne (Tasbihat al-Araba’).

Mtu ambaye amemdhuru mwenzake na kumfanya kiini cha sauti yake kutoweza kutoa na kudhihirisha sauti anapaswa kumlia dia kamili.

Maana na nafasi

Jahr (kudhihirisha sauti) ni kinyume cha Ikhfaat (kutodhihirisha) na maana yake ni kutoa sauti na kusoma kwa sauti ya juu na ya kusikika. [1] Kundi miongoni mwa mafakihi linasema kuwa, kigezo cha kudhihirisha sauti ni kudhihiri kiini cha sauti [2] na kuainisha hilo liko mikononi mwa ada na mazoea ya watu. [3] Mafakihi wanasema kuwa, kuchunga suala la kudhihirisha sauti hakupaswi kupelekea kutoa sauti kwa namna isiyo ya kawaida na ambayo haijazoeleka na kuwa katika hali ya kupayuka. [4] Maudhui ya Jahr (kudhihirisha sauti) hujadiliwa katika milango ya Sala, Hija na dia. [5] Istilahi ya Jahr imetumika katika elimu ya tajwidi na ina maana ya kubana pumzi na kuiachia mara moja wakati wa kutamka baadhi ya herufi. [6] Herufi 18 kati ya herufi 28 za lugha ya Kiarabu zina sifa hii na ni mashuhuri kwa jina la “al-Huruf al-Majhurah” (mkabala wa al-Huruf al-Mahmusah ambazo ni herufi zingine zilizobakia). [7]

Hukumu za Jahr

Mafakihi wa Kishia wamebainisha kuhusiana na hukumu za Jahr (kudhihirisha sauti) ambapo wamesema, kuna mahali ni wajibu, mustahabu, inajuzu na makuruhu (inachukiza) kufanya hivyo. Hukumu hizo ni kama ifuatavyo:

Sehemu ambazo ni wajibu kudhihirisha sauti

Kauli mashuhuri ni wajibu kwa mwanaume kusoma kwa sauti alhamdu na sura katika Sala ya Asubuhi na rakaa mbili za mwanzo za Sala ya Magharibi na Isha. [8] Inaeelezwa kuwa, ni wajibu kudhihirisha sauti wakati wa kusoma Bismillah katika Sala za Alfajiri, Magharibi, Isha, Sala ya Ijumaa na ni mustahabu kudhihirisha sauti wakati wa kusoma Bismillah katika Sala ambazo haipaswi kudhihirisha sauti (ikhfaat) na kuna ijmaa na kauli moja katika hili. [9] Kwa mujibu wa rai ya mafakihi ni kuwa, endapo mtu anayesali atasoma kimya kimya mahali ambapo ni wajibu kudhihirisha sauti au kinyume chake yaani akasoma kwa sauti sehemu ambayo ni wajibu kusoma kimya kimya, Sala yake itabatilika lakini kama hilo litafanyika kwa kusahau basi Sala yake itakuwa sahihi. [10]

Ikitokea mtu ambaye amemdhuru mwenzake na kufanya kiini cha sauti yake kutoweza kutoa na kudhihirisha sauti ni wajibu kwake kumlipa dia kamili. [11]

Sehemu ambazo ni mustahabu kudhihirisha sauti

Katika baadhi ya sehemu kwa mujibu wa wanazuoni wa fikihi (seheria za Kiislamu) ni mustahabu kudhihirisha sauti.

  1. Sala ya Majanga. [12]
  2. Sala ya Ijumaa. [13]
  3. Al-Hamdu na Sura katika Sala ya Adhuhuri katika siku ya Ijumaa kwa wanaume. [14]
  4. Sala Mbili za Idi (Eidul-Fitr na Eidul Adh’ha). [15]
  5. Sala ya kuomba mvua. [16]
  6. Sala za mustahabu za usiku. [17]
  7. Kusoma kunuti kwa mujibu wa kauli mashuhuri. [18]
  8. Kusoma Bismillahi katika maeneo ambayo ni wajibu kutodhihirisha sauti (ikhfaat) hata kama anayesali atachagua kusoma Alhamdu badala ya tasbihi nne (katika rakaa ya tatu na ya nne katika Sala). [19]
  9. Takbira za Sala ya maiti kwa Imamu wa jamaa. [20]
  10. Takbirat al-Ihram (takriba ya kuhirimia) kwa Imamu wa Jamaa, [21]
  11. Talbiya kwa wanaume. [22]

Aidha inajuzu kusoma kwa kudhihirisha sauti katika hali zifuatazo na mwenye kusali anaweza kusoma kwa sauti:

Makuruhu kudhihirisha sauti

Ni mashuhuri baina ya mafakihi ya kwamba, ni makuruhu (inachukiza) kwa Maamuma [26] kusoma kwa sauti nyuradi na dhikri za Sala isipokuwa Alhamdu, Sura na tasbihi nne (Tasbihat al-Ar’ba’a) ni wajibu kusoma tasbihat al-Ar’ba’a bila ya kudhihirisha sauti. [27]