Sala ya Majanga

Kutoka wikishia


Swalat al-Ayat / Swala ya Majanga (Kiarabu : صلاة الآيات) ni miongoni mwa swala za wajibu wakati yanapotokea baadhi ya matukio ya kimaumbile kama vile:Kupatwa kwa jua, kupatwa kwa mwezi, tetemeko la ardhi, kila tukio lisilo la kawaida linaloogopesha na kuleta woga miongoni mwa watu wengi kama vile: Upepo mweusi au mwekundu usio wa kawaida ambao unadhihiri katika mbingu.

Swalat al-Ayat (Swala ya Majanga) ina rakaa mbili na katika kila rakaa kuna rukuu tano na sijida mbili na inawezekana kuiswali kwa sura kadhaa. Katika sura ya kwanza, katika kila rakaa inasomwa Alhamdu na sura moja kamili mara tano na katika sura ya pili, katika kila rakaa inasomwa Al-Hamdu na sura mara moja ambayo mtu ataigawa mara tano na atasoma aya moja katika kila rakaa baada ya Alhamdu.

Kama Swala ya Majanga sababu yake itakuwa sio kupatwa kwa jua au mwezi (ikawa ni kitu kingine kama tetemeko la ardhi na kadhalika) kila itakapotelezwa basi inapaswa kutekelezwa kwa nia ya adaa; lakini katika Swala ya Majanga ambayo sababu yake ni kupata jua au mwezi, inapaswa kutekelezwa wakati wa kutokea tukio lenyewe na kama haikuswaliwa wakati huo, na tukio lenyewe likawa limemalizika, basi inapaswa kutekelezwa kwa nia ya kadha.


Maana na kuitwa Kwa jina hili

Swala ya Majanga ni Swala ambayo huwa wajibu wakati yanapotokea baadhi ya matukio ya kimaumbile kama vile: Kupatwa kwa jua, kupatwa kwa mwezi tetemeko la ardhi [1] na vilevile, kila tukio lisilo la kawaida linaloogopesha na kuleta woga miongoni mwa watu wengi [2] kama vile upepo mweusi au mwekundu usio wa kawaida. [3] Ayat ni wingi wa ayah na ina maana ya alama na ishara [4] na katika hadithi matukio ya kupatwa kwa jua na mwezi yametambuliwa kama ishara na alama za Mwenyezi Mungu. [5] Katika hadithi Swala ya Majanga haijatajwa kwa anuani ya Salat al-Ayat, bali imetajwa kwa anuani ya Salat al-Kusuf; [6] lakini katika vitabu vya fiqhi maneno yote mawili yametumika. [7] Wanazuoni wanasema kuwa, sababu ya Swala hii kupewa jina la Salat al-Ayat (Swala ya Majanga), yumkini ni kutokana na kuwa, mwanadamu anapaswa kuyazingatia matukio haya na kutambua kwamba, ni ishara ya nguvu na uwezo wa Mwenyezi Mungu na kwamba, Yeye ndiye mmiliki wa msimamizi wa kila kitu. [8] Mtume (s.a.w.w) pia siku ya kifo cha mwanawe Ibrahim wakati jua lilipopatwa akiwa na lengo la kuzuia kuhusishwa tukio hilo la kifo cha mwanawe alisema kuwa, kupatwa kwa jua na mwezi ni ishara na alama mbili za Mwenyezi Mungu na akabainisha kwamba, kila linapotokea moja kati ya matukio hayo mawili mnapaswa kuswali Swala ya Majanga. [9]


Historia

Swala ya Majanga ilikuwa wajibu kwa Waislamu mwaka wa 10 Hijria. Kwa mujibu wa nyaraka za historia ni kwamba, katika mwaka huu wakati Ibrahim, mtoto wa Mtume (s.a.w.w) aliapoaga dunia, jua lilipatwa. Kundi miongoni mwa watu wakalihuisisha tukio hilo la kifo cha Ibrahim; hata hivyo Bwana Mtume (s.a.w.w) akayatambulisha matukio ya kupatwa kwa jua na kupatwa kwa mwezi kuwa ni ishara na alama za Mwenyezi Mungu na yanatokea kwa amri ya Mwenyezi Mungu na sio kwa kifo au kwa uhai wa mtu. [10] Kisha akatoa amri kwamba, kila linapotokea tukio la kupatwa kwa jua au mwezi waaswali Swala ya Majanga (Salat al-Ayat) na kisha yeye na Waislamu wakaiswali Swala hiyo. [11]


Namna ya kuswali swala ya majanga

Swala ya Majanga ina rakaa mbili na katika kila rakaa kuna rukuu tano na sijida mbili na inawezekana kuiswali kwa sura mbili: [12]

  • Sura ya Kwanza: Katika kila rakaa inasomwa Alhamdu na sura nyingine; [13 kwa sura hii kwamba, “Alete takbira baada ya nia atasoma Al- Hamdu na sura kamili na kurukuu kisha anasimama na kusoma Al- Hamdu na sura kamili atafanya vivyo hivyo hadi mara tano na baada ya kusimama kutoka kwenye rukuu ya tano anaenda kwenye sijida mbili kisha anasimama kwa ajili ya rakaa ya pili, anafanya kama alivyofanya kati ka rakaa ya kwanza na kuleta tashahudi na kutoa salamu. [14]
  • Sura ya Pili: Katika kila rakaa inasomwa Al-Hamdu na sura mara moja; kwa sura hii kwamba, atachagua sura moja na kuigawa mara tano na baada ya nia na takbira ya kuhirimia atasoma Alhamdu na Aya moja (iwe ni Aya moja, kidogo au zaidi) kisha atarukuu na kuinuka kutoka kwenye rukuu na kusoma sehemu ya Aya iliyobakia (bila kusoma Alhamdu) na vivyo hivyo mpaka akamilishe rukuu tano na atakuwa ameshakamilisha sura kamili ambayo alisoma Aya zake mwanzo kabla ya rukuu ya tano kisha atarukuu rukuu ya tano kisha ataenda kwenye sijida na kusujudu sijida mbili na kisha ataenda katika rakaa ya pili na kusoma kama alivyosoma katika rakaa ya kwanza na baada ya kumaliza sijida mbili ataleta tashahudi na kutoa salamu.[15]

Kwa mujibu wa fatuwa za mafakihi ni kwamba, katika rakaa ya kwanza mtu anaweza kuswali sura ya kwanza na katika rakaa ya pili akaswali kwa sura ya pili kwa maana kwamba, anaweza kuchanganya baina ya sura hizo mbili za namna ya kuswali Swala ya Majanga. [16]


Mambo ya mustahabu

Baadhi ya mambo ambayo ni mustahabu katika Swala ya Majanga ni:

  • Kusoma kunuti kabla ya rukuu ya pili, ya nne, ya sita, ya nane na ya kumi. [17]
  • Matendo ambayo ni mustahabu katika Swala za kila siku, ni mustahabu pia katika Swala ya Majanga; ingawa katika Swala ya Majanga ni mustahabu badala ya adhana na ikama, mtu aseme mara tatu “as-Swalaa”. [18]
  • Kutamka takbira baada ya kila rukuu isipokuwa rukuu ya tano katika kila rakaa. [19]
  • Kuswali kwa jamaa, [20] kuswali kwa sauti [21], kurefusha Swala mpaka kuachiwa jua au mwezi [22] na kusoma sura ndefu [23] ni katika mambo mengine ya mustahabu katika Swala ya Majanga.


Wakati wa swala ya majanga na kadha yake

Wakati wa Swala ya Majanga ya kupatwa kwa jua na kupatwa kwa mwezi ni kuanzia wakati kunapoanza kupatwa kwa jua au mwezi mpaka kudhihiri kwake [24] au mpaka mwisho wa kudhihiri kwake. [25] Muhammad Hassan Najafi au Swahib al-Jawahir kama anavyojulikana ni kwamba, kwa mujibu wa tahadhari ya wajibu (ihtiyat wajib) haipaswi kuichelewesha Swala hii kwa kiwango ambacho mwezi au jua likaanza kuachiwa. Endapo Swala ya Majanga ya kupatwa kwa jua au mwezi haitaswaliwa kwa wakati wake ni wajibu kulipa kadha. [27] Swala ya Majanga inayohusiana na tetemeko la ardhi na mambo mengine (isipokuwa kupatwa kwa mwezi na jua), hazina kadha [28] bali kila wakati itakaposwaliwa, basi inapaswa kuswaliwa kwa nia ya adaa. [29]


Josho la kupatwa kwa jua

Allama Hilli anasema kuwa, baadhi ya mafuqahaa wa Kishia kama Sayyid Murtadha, Salari Deylami na Abu Salah Halabi wametoa fatuwa inayosema kuwa: Kama mtu hakuweza kuswali Swala ya Majanga ya kupatwa kwa jua au mwezi katika wakati wake (wakati tukio hilo lilipotokea), ni wajibu kwake mbali na kulipa kadha ya Swala hiyo aoge pia. Allama Hilli kwa upande wake na kundi jingine la wanazuoni kama Sheikh Mufid, Ibn Barraj na Ibn Idris Hilli, wao wanasema ni mustahabu kuoga na sio wajibu. Hata hivyo kuwa wajibu au kuwa mustahabu kuoga huko kunahusiana na pale, mwezi au jua unapopatatwa kikamilifu na mtu akawa hajaswali Swala hiyo kwa wakati wake kwa makusudi. [30] Katika hadithi ghusl (josho) hii imetajwa kwa jina la josho la kupatwa kwa jua.


Kutanguliza swala za kila siku katika ufinyu wa wakati

Kuswali Swala ya Majanga inayohusiana na kupatwa kwa mwezi au jua ni wajibu wa haraka (wa papo hapo), lakini kama Swala ya Majanga itakuwa wajibu katika wakati wa Swala za kila siku, awali ni wajibu kuswali Swala ambayo wakati wake ni finyu na isiposwaliwa muda wake utapita. Endapo wakati ni finyu kwa Swala zote mbili, basi hapa inapaswa kutangulizwa Swala ya wajibu ya kila siku kwa Swala ya Mjanga. [33]


Hukumu nyingine

  • Kila rukuu miongoni mwa rukuu za Swala ya Majanga ni nguzo na kama itaongezwa au kupunguzwa kwa makusudi au kwa kusahau, Swala itabatilika. [34]
  • Swala ya Majanga ni wajibu tu kwa watu ambao matukio hayo ya kimaumbile yametokea katika eneo lao. [35
  • Kwa mujibu wa nadharia za baadhi ya wanazuoni wa fiq'h ni kwamba, mwanamke mwenye hedhi au damu ya nifasi Swala ya Majanga imemuondokea; [36] ingawa wamesema kuwa, kwa mujibu wa ihtiyat wajib (tahadhari ya wajibu) anapaswa kuilipa kadha baada ya kutoharika. (37]
  • Swala ya Majanga ya kupatwa kwa mwezi au jua huwa wajibu pale matukio hayo mawili yanapoweza kuonekana kwa jicho la kawaida (sio chombo kama teleskopu). Ikiwa tukio hilo ni dogo mno kiasi cha kuwezekana kuonekana tu kwa kutumia chombo na ikawa ni la kupita kwa haraka, Swala ya Majanga haitokuwa wajibu. [38]
  • Matetemeko madogo ya ardhi yanayotokea baada ya tetemeko kuu na la asili la ardhi kama yatakuwa yanajitegemea, yatapelekea Swala ya Majanga kuwa wajibu. [39] Na vilevile mtetemeo hafifu wa ardhi kama utahisika. [40]
  • Endapo Swala kadhaa zitakuwa wajibu kutokana na matukio mbalimbali na tofauti, kwa mujibu wa tahadhari ya wajibu ni lazima kuianisha katika nia ya kwamba Swala ya Majanga anayoswali ni kwa ajili ya tukio lipi. [41]