Isma ya Bibi Fatima

Kutoka wikishia

Isma ya Bibi Fatima (a.s) (Kiarabu: (ع)عصمة السيدة فاطمة الزهراء) Ni usafi na ulinzi wa kulindwa Fatima binti ya Mtume (s.a.w.w) kutokana na dhambi na makosa. Kwa mujibu wa maelezo ya Sheikh Mufidu, ni kwamba; ismat ya Bibi Fatima (a.s) ni suala lenye makubaliano (lenye ijma’a) kati ya Waislamu wote, ila kwa mujibu wa maelezo ya Allama Majlisi, ni kwamba; suala hili ni suala lenye makubaliano (lenye ijma’a) baina ya Waislamu wa Shia. Suala la Bibi Fatima (a.s) kuwa maasumu linalazimiana na kwamba yeye ana baadhi ya sifa fulani za Manabii na Maimamu (a.s). Miongoni sifa hizo ni kama vile; kuwa ni kigezo na kwamba maneno yake na matendo yake ni hoja kwa Waislamu, la pili ni kwamba yeye ana hadhi na sifa ya kuwa kiongozi wa kidini na kuwa na uwezo wa kufasiri na kutoa kufafanua katika masuala mbali mbali ya dini. Sira ya vitendo yake pamoja na misimamo yake ni kipimo cha kutambua haki kutokana na batili. Pia yeye ni kielelezo na kigezo kamili katika nyanja mbalimbali za maisha.

Baadhi ya sababu zinazotolewa kuthibitisha usafi na utoharifu wa Bibi Zahra (a.s) ni pamoja na: Aya ya Tat-hiir, Hadithi ya Bidh-'ah, pamoja na Hadithi zinazohusiana na usafi (utohariu) wa Ahlul-Bait (a.s), kama vile Hadithi ya Thaqalaini na Safina. Hata Fakhru al-Razi, ambaye ni mmoja wa wafasiri wa Ahlu-Sunna ambaye anajulikana kama ni Imamu al-Mushakkikin (Imamu wa Kuweka Vizingiti), pia naye anaamini katika usafi (umaasumu) wa Bibi Fatima (a.s).

Umuhimu na Hadhi Yake

Kwa mujibu wa mtazmo Shia ni kwamba; Fatima binti ya bwana Mtume (s.a.w.w) ni mwenye cheo cha usafi (umaasumu) [1] na amesalimika kutokana na dhambi na aina zote za makosa. [2] Sheikh Mufidu ametaja kuwepo makubaliano ya Waislamu wote [3] na Allamah Majlisi ametaja kuwepo makubaliano ya madhehebu ya Shia kuhusiana usafi wake. [4] Watafiti wametaja sababu na hoja mbalimbali katika jitihada za kuthibitisha usafi wa Bibi Zahra (a.s.); miongoni mwazo ni kama ifuatavyo:

  • Kuwa na Baadhi ya Sifa na Hadhi Sawa na Walizo Nazo Manabii na Maimamu (a.s): Ikiwa usafi wa Fatima (a.s) utaweza thibitishwa, basi yeye naye atakuwa na baadhi ya sifa walizo nazo Manabii na Maimamu (a.s), ambazo ni kama vile; mambo aliyaridhia kutendeka (taqriri), maneno pamoja na matendo yake kuwa ni hoja juu ya wengine, kuwa ni kiongozi wa kidini, na kuwa na uwezo wa kufasiri na kufafanua masuala ya kidini. [5]
  • Kipimo cha Kutambua Haki na Batili: Kwa msingi wa usafi wa Fatima (a.s.), sira ya vitendo vyake pamoja na misimamo yake katika masuala mbalimbali kama vile kupinga unyakuzi wa ukhalifa wa Imam Ali (a.s.) na unyang'anyi wa Fadak, zitakuwa ni kipimo na msingi wa kutambua haki na batili. [6]
  • Kigezo na Rejeo: Ikiwa usafi wa Bibi Zahra (a.s) utapokelewa na kukubalika, katika hali hiyo, yeye atachukuliwa kuwa ni kielelezo kamili katika nyanja zote za maisha, kama vile; katika baadhi ya Aya za Qur'an [7] inavyobainishwa kuhusiana Manabii (a.s) kuwa ni vigezo kwa wengine. [8]

Suala la Usafi au isma ya bibi Fatima (a.s.) limejadiliwa katika vitabu mbali mbali vya tafsiri na chini ya baadhi ya Aya za Qur'ani, na kutoka hapo likaingia kwenye uwanja wa mijadala ya kielimu ikiwemo “elmu al-kalam” ambayo ni elimu ya itikadi na elimu ya misingi ya fiqhi (usuli al-fiqhi). [9] Inasemekana kuwa asili ya suala la isma ya Bibi Fatima linaanzia wakati wa bwana Mtume (s.a.w.w), hata baadhi ya maneno yake na pia baadhi ya aya za Qur'an kama vile Aya ya Mubahala na Aya ya Tat-hir zinaonesha uwepo wa suala hili. [10] Ripoti za mwanzo kabisa za kihistoria kuhusiana na isma ya bibi Fatima (a.s) zinarejea katika kipindi cha baada ya kufariki kwa bwana Mtume (s.a.w.w) na katika suala la unyang'anyi wa Fadak, ambapo Imamu Ali (a.s) [11] alitumia Aya ya Tat-hir kaama ni hoja katika kuthibitisha isma ya Bibi Zahra (a.s). [12]

Tegemeo la Aya ya Tathir Juu ya kuthibitisha Isma ya Bibi Fatima

Makala kuu: Aya ya Tat-hir

Wanazuoni wa Kishia wamekuwa wakitegemea Aya ya Tat-hir ili kuthibitisha Isma ya Fatima (s.a). [13] Kulingana na Hadithi zilizosimuliwa kutoka kwa Waislamu wa pande zote mbili; Shia [14] na Ahlu Sunna, [15] ni kwamba; Aya hii iliteremshwa kwa heshima ya As-habu al-Kisaa. Kwa hivyo, maana ya Ahlu Bayt katika Aya hii, ni watu watano ambao ni; (Mtume (s.a.w), Imam Ali (a.s), Bibi Fatima (s.a), pamoja na Hassan na Hussein (a.s). [16] Kulingana na baadhi ya Hadithi, bwana Mtume (s.a.w.w) katika kila sala ya asubuhi na kulingana na Hadithi nyingine, katika kila sala alikuwa akifika kwenye nyumba ya Fatima (s.a) na kutoa salamu na akisema: Enyi Ahlu Bait, sala sala! Na akimalza hayo alikuwa akisoma Aya ya Tat-hir. [17] Fakhr Razi amesema kuwa Hadithi inayohusiana na kuteremshwa kwa Aya ya Tat-hir. Pia Fakhr Razi kawatambulisha Ahlu Bait kuwa ni As-habu Kisaa, kusema kwamba suala hili limekubalika na kupata muwafaka (ijma’a) wa wanazuoni wa Hadithi pamoja na Tafsir. [18] Aya hii ianzungumzia matakwa na mapenzi ya Mungu ya kutaka kuondoa uchafu kutoka kwa Ahlu Bait (a.s), na kule kuondoa uchafu kutoka kwa Ahlu Bayt (a.s), kuna maana ya kuwafanya wa kuwa ni Maasumina (watohaarifu). [19]

Katika moja ya Hadithi kutoka kwa bwamba, Mtume (s.a.w.w) imesimuliwa akisema kuwa; Maasum (wasio na dhambi), ndiwo walioteremkiwa na Aya ya Tat-hir nao ni: mimi, Ali, Fatima, Hassan na Hussein (a.s). [20] Imam Ali (a.s) naye katika tukio la upokonyaji wa Fadak, alitumia Aya ya Tat-hir kama ni hoja katika kuthibitisha isma ya Bibi Fatima (s.a) na utakaso wake kutokana aina zote za dhambi. [21] Pia imeelezwa kwamba; Aya ya Mubahala nayo inathibitisha isma ya Fatima (s.a). [22]

Kuthibitisha Isma ya Bibi Fatima Kupitia Hadithi ya Bidh’a

Makala kuu: Hadithi ya Bidh’a

Hadithi ya Bidh’a ni moja ya hoja zitumikazo kama ni ithibati ya kuthibitisha isma ya Bibi Fatima (s.a). [23] Katika Hadithi hii, ambayo Allama Majlisi ameihesabu kuwa ni mutawatir (iliosimuliwa na watu wengi kutoka matabaka kadhaa ya wapokezi wa Hadithi), [24] imeelezwa yta kwamba; kumuudhi na kumkasirisha bibi Fatima (a.s), ni sawa na kumkasirisha na kumuudhi bwana Mtume (s.a.w.w), na kuridhika kwake, ndio kuridhika kwa bwana Mtume (s.a.w.w). Kwa msingi huu, kama Bibi Fatima (s.a) angelifanya dhambi, kisha akakatazwa na kukemewa na mtu fulani, naye akawa ni mwenye kukasirika kutokana na makemeo hayo! Basi kukasirika kwake kusinge mkasirisha Mtume (s.a.w.w). [25] Kwa kuwa Mungu huridhika tu na matendo mema na haridhishwi na dhambi wala uasi wa kuasiwa amri zake, basi kama Bibi Fatima (s.a) angefanya dhambi, bila shaka angekuwa ameridhika na kitu ambacho Mungu haridhiki nacho. [26] Baadhi ya wanazuoni wameifahamu Hadithi hii kwa maana ya kuthibitisha isma ya Bibi Fatima (s.a) kutokana na dhambi, na wengine kama Ayatullah Wahid Khurasani wameifahamu Hadithi hii kwa maana ya kuthibitisha isma kamili na tandavu (izuiayo kutokufanya dhambi pamoja na aina zote za mitelezo na kukosea). [27]

Hadithi ya Bidh’a imepokewa na inapatikana katika vyanzo kadhaa vya Ahlu Sunna kama vile; Sahihi Bukhari [28] na Sahihi Muslim. [29] [30] Katika hadithi zingine, imeelezwa kwamba; kuridhika na kutoridhika kwa Fatima ni sawa na kuridhika na kutoridhika kwa Mwenye Ezi Mungu. [31]

Kuthibitisha Isma ya Bibi Fatima Kupitia Hadithi za Thaqalaini na Safina

Hadithi kadhaa zinazo thibitisha Isma za Ahlu Bait (a.s) kama vile; Hadithi ya Thaqalaini na Hadithi ya Safina zote huhisabiwa kuwa ni miongoni mwa hoja za kuthibitisha isma ya Fatima (s.a), [32] uthibitikaji wa hoja hii, kunategemea hoja ya kuwa bibi Fatima (s.a) ni miongoni mwa Ahlu Bait (a.s). [33] Kwa mujibu wa maelezo ya Allama Majlisi, Hadithi zinazosisitiza juu ya ulazima wa kushikamana na Ahlu Bait (a.s), kama Hadithi ya Thaqalaini na Hadithi ya Safina, pia nazo ni zenye kuthibitisha isma ya bibi Fatima (s.a), hii ni kwa sababu ya kwamba; Walengwa wa kushikamana nao katika amri iliyo tolewa na Mwenye Ezi Mungu, inahusiana na kushikamana na watu wenye sifa ya umaasum. Mtu anayefanya dhambi, sio tu kwamba si lazima kushikamana naye wala kumfuata, bali pia ni wajibu wetu kumzuia na kumkemea kwa mujibu wa kanuni ya kuamrisha mema na kukataza maovu. [34]

Katika moja ya Hadithi imeelezwa kwamba; Kila usiku wa Miraj, bwana Mtume (s.a.w.w), aliona nuru ya Fatima na Maimamu wa Shia na akamuuliza Mwenye Ezi Mungu, "Hawa ni kina nani?" Akajibiwa kwa sauti isemayo: "Hawa ni Ali, Fatima, Hassan, Hussein, na watoto wa Hussein ambao ni watoharfu na ni Maasumina”. [35]

Mtazamo wa Ahlu Sunna kuhusu Isma ya Bibi Fatima (a.s)

Baadhi ya wanazuoni wa upande wa Ahlu Sunna kama vile; Shihabuddin Alusi (aliyefariki mwaka 1270 Hijiria), ambaye ni mfasiri wa Qur’ani, amemchukulia Bibi Mariam kuwa ni msafi aliye takaswa kutokana na dhambi na uchafu, na kisha akamhisabu bibi Fatima (s.a) kuwa ni mbora zaidi kuliko bibi Mariam (s.a) usemi wake huo umetegemea Aya ya Qur’ani isemayo: وَإِذْ قَالَتِ الْمَلَائِكَةُ يَا مَرْيَمُ إِنَّ اللهَ اصْطَفَاكِ وَطَهَّرَكِ وَاصْطَفَاكِ عَلَىٰ نِسَاءِ الْعَالَمِينَ؛ ; Na (kumbuka) pale Malaika waliposema: Ewe Mariam, hakika Mwenye Ezi Mungu amekuchagua na kukutakasa na amekuchagua juu ya wanawake wa walimwengu wote [3:42]. [36] 37 Kwa mujibu wa maoni ya Hassan Hassanzadeh Amuli (aliyefariki mwaka 1400 Hijiria), ambaye ni mwanazuoni wa Shia, ni kwamba Fakhr Razi, ambaye ni mfasiri wa Ahlu Sunna wa karne ya sita Hijria, licha ya kuwa ni bigwa wa kuweka vizingiti na kujenga shaka katika kila kitu, sifa ambayo imempelekea kujulikana kama ni "Imamu wa Kujenga Shaka (Imamu al-Mushakkikina)", ila katu hakuwa na shaka yoyote ile kuhusiana na isma ya Bibi Fatima (s.a). [38]

Rejea

Vyanzo