Haqq al-Nas

Kutoka wikishia

Haqq al-Nas (Kiarabu: حَق‌ُّالناس أو حق العباد) maana yake ni haki ya watu au haki ya waja. Haqq al-Nas inaashiria haki za watu zilizoko katika migongo na mabega ya watu wengine. Haqq al-Nas (haki za watu) ni mkabala wa Haqqullah (Haki ya Mwenyezi Mungu) ambapo katika hili ni haki za Mwenyezi Mungu ambazo ziko katika dhima na mabega ya watu ambazo wanapaswa kuzitekeleza kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Haki al-Nas haihusiana na haki za kimali tu bali inahusiana pia na roho, uhai na heshima ya watu. Haki za watu zinagawanyika katika makundi mawili kama vile haki za roho na mali za watu na kadhalika kama vile kuiba na kutoa tuhuma ya zinaa au liwati dhidi ya mtu ambazo zina pande mbili za haki za watu na haki za Mwenyezi Mungu.

Imam Sajjad (a.s) ametaja zaidi ya haki na wajibu hamsini ambazo ni wajibu wa mwanadamu katika kitabu chake cha Risala al-Huquq (Risala ya Haki). Katika hadithi hizi, inaelezwa kuwa kuweko haki za watu katika dhima ya mtu ni sababu ya kutojibiwa dua na maombi ya mhusika.

Haki za haki za watu hazisamehewi kwa kutubu na kuuawa shahidi katika njia ya Mungu, bali ni lazima zilipwe au mwenye haki aisamehe. Katika hukumu za mahakama za Kiislamu, kuna tofauti kati ya haki za watu na haki za Mwenyezi Mungu; kwa mfano, utekelezaji wa hukumu katika kesi ya haki za watu kunahitajia ombi la mmiliki wa haki; lakini haki ya Mungu haiwi chini ya matakwa ya mtu yeyote na kwamba, haki za watu zimejengeka juu ya msingi wa umakini na tahadhari; lakini haki ya Mungu inategemea urahisi na tahafifu.


Utambuzi wa maana

Katika Uislamu, haki zinagawanywa katika sehemu mbili, haki za watu na haki za Mwenyezi Mungu. [1] Maana ya haki za watu ni haki za watu ambazo ziko katika dhima na mabega ya watu wengine ambazo ni mkabala wa haki za Mwenyezi Mungu. [2] Haki za watu kwa namna fulani zinahesabiwa kuwa ni haki ya Mwenyezi Mungu; [3] lakini wakati istilahi hii inapotumiwa mkabala wa haki ya Mwenyezi Mungu makusudio yake huwa ni lile kundi la haki ambazo ziko katika mabega ya watu yaani ni lazima watu wenyewe wazitekeleze. [4]

Katika vyanzo vya hadithi na kifikihi ili kuashiria haki za watu kumetumika anuani mbalimbali kama haki za waja, [5] haki za mwanadamu, [6] haki za wanadamu, [7] na haki za Waislamu. [8]

Vielelezo

Baadhi ya mafakihi wametambua haki za watu kwamba, zimegawanyika katika aina mbili za haki: Haki za watu tu (zisizo na mchanganyiko) kama vile haki za roho na mali za watu na na haki za watu ambazo sio maalumu tu kwa watu yaani haki ambazo zina pande zote mbili yaani haki za watu na haki za Mwenyezi Mungu; kama vile kuiba, [9] haki za taazir [10] na kutoa tuhuma ya zinaa au liwati dhidi ya mtu. [11]

Haqq al-Nas haihusiani na haki za kimali tu bali zinahusiana pia na roho, uhai na heshima ya watu. [12] Kwa muktadha huo, kusengenya, [13] kutoa tuhuma, maneno ya uchochezi na kuwaudhi watu pasina ya sababu ni mingoni mwa mambo yanayohesabiwa kuwa ni katika haki za watu. [14] Katika hadithi iliyopokewa kutoka kwa Imamu Sajjad (a.s) ambayo inatambulika kama Risalat al-Huquq (Risala ya Haki) kumeorodheshwa zaidi ya haki na majukumu 50 ambayo ni wajibu wa mwanadamu kwa wengine. [15]

Umuhimu wake katika hadithi

Haki za watu zimetajwa katika hadithi kuwa moja ya mambo na sababu ambazo ni kizuizi cha dua kutakabaliwa. [16] Kwa maana kwamba, kama mtu ana haki ya mwingine aliyoipokonya kwa mfano, basi dua zake haziwezi kukubaliwa. Imam Ja'afar Swadiq (a.s) anasema kuwa, hakuna ibada bora zaidi ya kutekeleza haki ya muumini. [17] Imekuja katika hadithi ya Manahi iliyonukuliwa kutoka kwa Bwana Mtume (s.a.w.w) ya kwamba: Mtu ambaye katika shingo yake kuna haki ya mtu mwingine na ana uwezo wa kuitekeleza, lakini anasogeza mbele leo au kesho suala la kuilipa haki hiyo, basi anaandikiwa kila siku katika faili lake la dhambi ambayo ni sawa na Ash-shar. [18] Ash-shar ni jina la mtu ambaye kwa amri ya mtawala alikuwa akichukua kwa nguvu asilimia kumi ya mali za watu. [19]

Nafasi yake katika fikihi na sheria

Katika vyanzo vya Fiqhi haki za watu zinazungumziwa katika sehemu ya hukumu za mahakama. [20] Katika kanuni za kisheria za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia suala hili limezingatiwa na kupewa umuhimu. [21] Kwa mfano dia, kisasi na baadhi ya makosa ya taaziri (makosa ambayo mtawala wa Kiislamu ndiye mwenye jukumu la kuainisha adhabu hizo) kama kuvunjia heshima yametambuliwa kuwa ni kosa katika mlango wa kuwa ni haki za watu. [22]

Tofauti yake na haki ya Mwenyezi Mungu

Baina ya haki za watu na haki ya Mwenyezi Mungu kuna tofauti kadhaa zilizotajwa ambapo baadhi yazo ni kama zifuatazo:

  • Kuthibiti haki za watu mbele ya hakimu ni rahisi zaidi kuliko kuthibiti haki ya Mwenyezi Mungu. Kwa sababu haki ya Mwenyezi Mungu haithibiti kwa shahidi mwanamume mmoja na mashahidi wawili wanawake, au shahidi mmoja mwanamume na kiapo, au kwa ushahidi wa wanawake peke yao. Lakini baadhi ya haki za watu zinaweza kuthibitishwa kwa ushahidi huu. [23]
  • Utekelezaji wa hukumu katika Haqq al-Nas kunanahitaji ombi na takwa la mwenye haki. Lakini haki ya Mwenyezi Mungu haitegemei matakwa na mashtaka ya mtu yeyote yule. [24] Katika kipengee cha 159 cha kanuni ya taazirat ya Iran, kumfuatilia na kumuadhibu mhalifu katika haki za watu, kunategenea matakwa na maombi ya mwenye haki au kaimu wake wa kisheria. [25] Kama hajawasilisha maombi na mashtaka ya kudai haki yake, ufuatiliaji huo na kumuadhibu mhalifu ni mambo ambayo hayafanyiki.
  • Katika Haqq al-Nas tofauti na Haqqullah, hakimu hawezi kumzuia mhalifu kukiri na kuungama. [26]
  • Baadhi ya mifano ya Haqq al-Nas inaweza kusamehewa au kuhamishwa lakini katika Haqqullah msamaha wa mtu ambaye uhalifu ulitendwa dhidi yake hilo halipelekei kufutika na kuondoka kwa haki husika. [27]
  • Haki za watu haziondoki hata kwa toba, lakini baadhi ya haki za Mwenyezi Mungu huondoka kupitia njia ya kutubia. [28]
  • Haki ya watu imejengeka juu ya msingi wa umakini na tahadhari, lakini haki ya Mwenyezi Mungu inategemea urahisi na tahafifu. [29] Inasemekana kwamba, baadhi ya mafaqihi wanatambua kwamba, tofauti kati ya haki ya Mungu na haki ya watu katika hukumu za mahakama chimbuko lake ni hili. [30]
  • Haki ya watu haisamehewi kwa mtu kuuawa shahidi katika njia ya Mwenyezi Mungu; lakini haki ya Mwenyezi Mungu inasamehewa kwa mtu kuuawa shahidi katika njia ya Mwenyezi Mungu. [31] Ni kwa muktadha huo ndio maana imeelezwa kuwa, katika usiku wa Ashura Imam Hussein aliwaambia masahaba zake kwamba, watu ambao wana haki za watu katika shingo zao waondoke na katika jeshi lake. [32]

Kufidia

Katika suala la haki za watu mbali na kutubia mhusika anapaswa kufidia haki za watu au mwenye haki asamehe. [33] Kwa mujibu wa baadhi ya mafakihi, jambo hili linajumuisha pia haki za mtu zilizoporwa kabla ya kubaleghe kwake. [34]

Kwa mujibu wa hadithi iliyopokewa kutoka kwa Bwana Mtume (s.a.w.w) ni kwamba, siku ya Kiyama mtu ambaye alichukua, kupora au kudhulumu haki za watu na hivyo ana haki za watu katika mabega yake, zitachukuliwa kutoka katika amali zake njema na kupatiwa mwenye haki na endapo amali njema zitakuwa zimekwisha, basi zitachukuliwa kutoka katika dhambi za mwenye haki na kuwekwa katika fungu la aliyedhulumu haki; na kisha ataingizwa motoni. [35] Kwa mujibu wa hadithi nyingine iliyopokewa kutoka kwa Imam Swadiq (a.s) katika kitabu cha Li'ali al-Akhbar ni kwamba: Hali mbaya kabisa ya mwanadamu siku ya Kiyama ni pale wanaostahiki Zaka na Khumsi watakaposimama mbele yake na Mwenyezi Mungu kuwapa mbadala wa mambo mema ya mtu huyu. [36] Huyu ni mtu ambaye alipokuwa hapa duniani alikuwa na uwezo wa kutoa Zaka na Khumsi lakini hakutoa na kuwapatia wanaostahiki.

Vitabu

Baadhi ya vitabu vilivyoandikkwa kuhusiana na maudhui hii ni:

  • Negahi be haqq Naas: Mwandishi Mahmoud Akbari. Utangulizi wa kitabu hiki umeandikwa na Ayatullah Makarim Shirazi. Baadhi ya milango ya kitabu hiki ni: Umuhimu wa haki za watu, haki za watu na vipato vya haramu, haki za watu na masuala ya kifedha na kisheria, n.k. [37]
  • Haqq al-Nas: Mwandishi Abbas Rahimi. Kitabu hiki kimeandikwa kwa lugha ya Kifarsi. Kitabu hiki kina milango sita ambapo heshima ya Waislamu na haki za watu siku ya Kiyama ni miongoni mwa maudhui za milango hiyo. [38]