Kisasi

Kutoka wikishia

Kisasi (Kiarabu: القصاص) maana yake ni lipizo au kumlipizia mtu katika jinai za makusudi. Kisasi kinagawanyika mara mbili, kisasi ya nafsi na kisasi cha kiungo (taraf). Hukumu ya kisasi ni miongoni mwa hukumu zisizo na shaka katika dini ya Uislamu ambapo Aya za Qur'ani Tukufu, hadithi mutawatir (zilizokithiri mapokezi yake) na ijmaa zinathibitisha hilo.

Kuwa sawa katika kuwa huru na kuwa utumwani, kuwa katika dini moja, kubaleghe na akili ni katika masharti yayohitajika kwa ajili ya kuteleza kisasi. Kukiri mhalifu, ushahidi wa wanaume wawili waadilifu na kiapo (qisamah) ni katika njia za kuthibitisha kisasi kwa mtu aliyeua. Kisasi pamoja na dia, adhabu isiyo ya kimali na taazir (adhabu ambazo mtawala wa Kiislamu ndiye mwenye jukumu la kuainisha adhabu hizo) ni miongoni mwa adhabu nne kuu katika sheria ya adhabu za Kiislamu katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Kuzuia ulipizaji usio na mipaka, kudhamini uadilifu wa kimahakama na kulinda usalama wa kijami ni miongoni mwa hekiima na sababu za kutungwa na kuwekwa sheria ya kisasi. Sio wajibu kulipa kisasi mtu ambaye ana haki ya kulipizia kisasi; bali anaweza kumsaheme mhalifu na kufumbia macho haki yake kwa kuchukua kitu mbadala.

Kisasi, ni lipizo

Lipizo na kufanya kama ilivyofanyika katika jinai za makusudi inafahamika kuwa ni kisasi. [1] Kama mtu atafanya kosa la mauaji au akamjeruhi mtu, endapo atauawa au atafanyiwa majeraha kama yale yale aliyomfanyia mwenzake kwa kitendo hicho atakuwa amefanyiwa kisasi. [2] Katika vitabu vya Fiqhi mtu ambaye ametenda jinai anajulikana kwa jina la Jani (mhalifu) na aliyefanyiwa jinai anafahamika kama Majni-un alayh (mhanga). [3]

Kusamehe haki ya kisasi

Kisasi sio adhabu ya ambayo ni lazima kuitekeleza; kwa maana kwamba, mtu ambaye ni mhanga na mwenye haki ya kulipiza kisasi anaweza kusamehe na kufumbia macho haki yake hiyo au akafanya suhulu na mtu ambaye ni lazima itekelezwe kisasi kwake. [4] Kwa mujibu wa Allama Tabatabai ni kwamba, katika Aya ya kisasi, sambamba na kubainisha hukumu ya kisasi, kunashajiishwa pia suala la kusamehe na kufumbia macho haki ya kulipiza kisasi. [5]

Amir al-Muuminina (a.s) amesema katika moja ya wasia wake baada ya kupigwa upanga: Kama nikibaki hai basi mimi ni walii wa damu yangu, na kama nikifa, basi kifo ndio marejeo yangu na makazi yangu. Fauka ya hayo, alizingatia msamaha (kuhusu Ibn Muljam) kama njia ya kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu na matendo mema kwa watoto wake. Vile vile aliishauri hadhira yake kusamehe kwa sentensi "Fa'afuu" sameheni, na akatumia sehemu ya Aya 22 ya Surat Nur kama hoja yake. ((أَلَا تُحِبُّونَ أَنْ يَغْفِرَ اللهُ لَكُمْ ; Je! Nyinyi hampendi Mwenyezi Mungu akusameheni?)) [6]

Hoja za uhalali wa kisasi

Mafakihi wanalitambua suala la kisasi na kulipiza kisasi kuwa ni katika hukumu za wazi na zisizo na shaka za fiq'h ya Kiislamu ambapo kuna Aya nyingi na hadithi mutawatir (ambazo mapokezi yake yamekithiri) ambazo zinaunga mkono na kuthibitisha hilo na wameafikiana (ijmaa) katika hilo. [7] Baadhi ya hoja za Qur'ani zilizonukuliwa katika kitabu cha Jawahir al-Kalam kilichoandikwa na Muhammad Hassan Najafi ni kama ifuatavyo: [8]

  • وَ لَكُمْ فِي الْقِصاصِ حَياةٌ يا أُولِي الْأَلْبابِ  ; Mtakuwa nao uhai mzuri katika kulipiza kisasi enyi wenye akili [10]
  • كُتِبَ عَلَيْكُمُ الْقِصاصُ فِي الْقَتْلى‏ الْحُرُّ بِالْحُرِّ وَ الْعَبْدُ بِالْعَبْدِ وَ الْأُنْثى‏ بِالْأُنْثى  ; Mmepewa ruhusa kulipa kisasi katika walio uwawa - muungwana kwa muungwana, na mtumwa kwa mtumwa, na mwanamke kwa mwanamke. [12]
  • وَ كَتَبْنا عَلَيْهِمْ فيها أَنَّ النَّفْسَ بِالنَّفْسِ وَ الْعَيْنَ بِالْعَيْنِ وَ الْأَنْفَ بِالْأَنْفِ وَ الْأُذُنَ بِالْأُذُنِ وَ السِّنَّ بِالسِّنِّ وَ الْجُرُوحَ قِصاصٌ فَمَنْ تَصَدَّقَ بِهِ فَهُوَ كَفَّارَةٌ لَهُ ; Na humo tuliwaandikia ya kwamba roho kwa roho, na jicho kwa jicho, na pua kwa pua, na sikio kwa sikio, na jino kwa jino, na kwa majaraha kisasi. Lakini atakaye samehe basi itakuwa ni kafara kwake. [14]
  • والْحُرُماتُ قِصاصٌ فَمَنِ اعْتَدى‏ عَلَيْكُمْ فَاعْتَدُوا عَلَيْهِ بِمِثْلِ مَا اعْتَدى‏ عَلَيْكُمْ  ; Na vitu vitakatifu vimeekewa kisasi. Anaye kushambulieni nanyi mshambulieni, kwa kadiri alivyo kushambulieni. [16]

Kisasi cha nafsi na kisasi cha kiungo

Kisasi kinagawanyika mara mbili, kisasi ya nafsi na kisasi cha kiungo (taraf):

  • Kisasi cha nafsi, ni kumuua mtu kwa kukusudia. [17]
  • Kisasi cha kiungo (taraf), ni kumdhuru na kumjeruhi mtu kwa makusudi kama vile kumkata kiungo na kadhalika. [18]

Masharti ya kutimia kisasi

Ili kisasi kitekelezwe kuna masharti ambayo yanapaswa kutimia ambayo ni:

  • Kuwa sawa katika kuwa huru na kuwa katika utumwa; [19] kwa maana kwamba, kama mtu huru atafanya jinai dhidi ya mtumwa, kisasi hakitatekelezwa dhidi yake; [20] bali atatoa dia. [21
  • Kuwa katika dini moja; kwa maana kwamba, kama Muislamu atafanya jinai dhidi ya asiyekuwa Muislamu, adhabu yake sio kisasi; [22] bali atapewa adhabu ya taazir, (adhabu ambazo mtawala wa Kiislamu ndiye mwenye jukumu la kuainisha adhabu hizo) na atalipa dia. [23]
  • Hakuna kisasi kwa baba aliyemuua mwanawe; kama baba atamuua mwanawe haitatekelezwa hukumu ya kisasi dhidi yake. Hukumu hii inahusiana pia na babu, na baba wa babu na kuendelea. [24] Katika mazingira haya adhabu yake ni kafara, dia na taazir. [25]
  • Kubaleghe na akili; mtu ambaye hajafikkia umri wa kubaleghe au kichaa (mwendawazimu) haitekelezwi hukumu ya kisasi dhidi yake. [26] Kadhalika mtu ambaye amebaleghe na mwenye akili ambaye amefanya jinai dhidi ya kichaa hukumu ya kisasi haitekelezwi dhidi yake; hata hivyo ni lazima atoe dia. [27]
  • Kumuua mtu ambaye damu yake ni halali kumwagwa; kwa maana kwamba, kama mtu atamuua mtu mwingine kwa sababu kama ya kuritadi kwake ambapo damu yake ni halali, hivyo aliyefanya mauaji hayo haitatekelezwa hukumu ya kisasi dhidi yake. [28]

Hukumu maalumu za kisasi cha kiungo

Kisasi cha kiungo mbali na masharti ya kisasi cha nafsi kina masharti mengine pia ambayo ni:

  • Kushabihiana au kuwa sawa katika uzima; kwa maana kwamba, kwa mfano kama mhalifu atakata mkono wa mtu mwingine wenye nakisi na mapungufu, hukumu ya kisasi itatekelezwa dhidi yake kama atakuwa na mkono wenye nakisi na mapungufu; kinyume na hivyo anapaswa kulipa dia. [29]
  • Kushabihiana na kuwa sawa katika viungo; kwa maana kwamba, kama mhalifu ataukata mkono wa kulia wa mwenzake, katika kutekeleza hukumu ya kisasi mkono wake wa kulia ndio unaopaswa kukatwa; isipokuwa kama hana mkono wa kulia. Katika hali hii na kwa mujibu wa mtazamo mashuhuri atakatwa mkono wake wa kushoto. [30]
  • Isipelekee madhara ya uhai; kwa maana kwamba, utekelezaji wa hukumu ya kisasi haupasi kusababisha kifo au kudhuru kiungo kingine cha mwili. Kwa mujibu wa sharti hili endapo kisasi kitakuwa na hatari ya kudhuru, hukumu haitatekelezwa na badala yake mhusika atalipa dia au arash (aina ya dia). [31]

Masharti ya kuthibitisha

Kwa mujibu wa vyanzo vya Fiqhi inawezekana kuthibitisha jinai kupitia njia tatu na kwa hivyo kutekeleza hukumu ya kisasi: Njia ya Kwanza; ni mtu mwenyewe aliyetenda jinai akiri kutenda kitendo hicho. [32] Katika hali hii lazima mhusika awe ni mwenye akili na aliyebaleghe na akiri hili kwa hiari yake na sio kwa kulazimishwa. Na njia ya Pili ni kutoa ushahidi wa hili wanaume wawili waadilifu. [33]Na pia njia ya tatu; ni kufanyike kiapo (Qisamah) dhidi ya mhalifu; kwa maana kwamba, wajitokeze watu 50 miongoni mwa mawalii wa damu na kula kiapo kwamba, mtuhumiwa ametenda jinai hiyo. [34] Kiapo hiki hufanyika pale ambapo kwa namna fulani hakuna ushahidi wa wazi na usio na shaka kwamba, mtuhumiwa ametenda jinai hiyo. [35]

Kisasi katika sheria za Iran: Sheria ya adhabu za Kiislamu

Katika sheria ya adhabu za Kiislamu katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kisasi pamoja na dia, adhabu isiyo ya kimali (kama kupigwa mijeledi) na taazir (adhabu ambazo mtawala wa Kiislamu ndiye mwenye jukumu la kuainisha adhabu hizo) ni miongoni mwa adhabu nne kuu katika sheria ya adhabu za Kiislamu katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. [36] Kwa mujibu wa kifungu cha 16 cha sheria hiii, kisasi ni adhabu kuu ya jinai ya makusudi dhidi ya nafsi, viungo na maslahi. [37] Katika kitabu cha tatu cha sheria ya adhabu za Kiislamu katika kifungo cha 289 hadi 447 kumebainishwa kwa mapana na marefu kuhusiana na sheria ya kisasi. [38]

Falsafa ya kisasi

Imeelezwa kuwa, kuzuia ulipizaji usio na mipaka, kudhamini uadilifu wa kimahakama na kulinda usalama wa kijamii ni miongoni mwa sababu za kuwa halali kisasi katika Uislamu. [39] Kwa mujibu wa baadhi sheria ya kisasi inathibitika kwa kuleta mlingano baina ya uhalifu na adhabu ya uadilifu wa kimahakama. [40] Kadhalika kuweko adhabu kama hizi kunazuia kufanya uhalifu watu wenye nia ya kutenda jinai na kwa muktadha huo, usalama wa kijamii unapatikana. [41] Faida ya tatu ni kwa kumpa haki ya kisasi mtu aliyetendewa jinai au familia yake kunaondoa kitendo cha wao kutaka kuchukua sheria mkononi na kulipiza kisasi. [42] Allama Tabatabai amesema bayana katika Tafsiri ya al-Mizan: Licha ya kuwa badala ya kisasi kuna dia na msamaha na katika kusamehe kuna huruma, kufumbia macho na kujitolea, lakini kile ambacho kinadhamini maslahi ya umma na jamii pamoja na kuthibitisha uhai wa kijamii ni kisasi na sio msamaha, dia na kitu kitu kingine ghairi ya viwili hivi. [43]

Masuala yanayofungamana