Risalat al-Huquq

Kutoka wikishia

Risalat al-Huquq (Risala ya Haki) ni hadithi kutoka kwa Imam Zainul Abidin (as) ambayo inaelezea haki 50 zilizoko katika mabega ya mwanadamu (ambazo anapaswa kuzifanya); kama vile haki ya Mwenyezi Mungu, viongozi, viungo vya mwili, ndugu na matendo kama Swala, Saumu, Hija, kuchinja na kutoa sadaka. Chanzo cha kale kabisa cha hadithi hii ni Tuhaf al-Uqul kitabu ambacho kimeandikwa na Ibn Shu'ba Harrani (aliaga dunia 381 H) na vitabu vitatu vya Shekhe Saduq (aliaga dunia 381H) ambavyo ni al-Khisal, Man La Yahdhuruh al-Faqih (vitabu hivi viwili ni miongoni mwa Kutub al-Ar'ba yaani vitabu vinne vya hadithi vya Mashia vyenye itibari) na al-Amali. Watalaamu na wahakiki wa masuala ya hadithi wanasema kuwa, hadithi hii (ya Risalat al-Huquq) ina itibari kutokana na kutimiza masharti kama ya vigezo vya wapokezi na vyanzo vyake. Hati na risala hii ya haki ya Imam Zainul-Abidin (as) imetarjumiwa kwa lugha ya Kifarsi kwa tarjumi nyingi na kwa lugha nyingine kama Kiingereza, Kifaransa, Kiurdu, Kihindi na kadhalika na kuchapishwa na kusambazwa, kama ambavyo kuna vitabu vimeandikwa kutoa ufafanuzi wa risala hii muhimu kuhusiana na haki mbalimbali.

Utambulisho Jumla

Risala ya Haki (Risalat al-Huquq) ni hadithi kutoka kwa Imam Zainul Abidin (as) ambayo inabainisha na kulezea haki zilizoko katika mabega ya mwanadamu (ambazo anapaswa kuzifanya); kama vile haki ya Mwenyezi Mungu, viongozi, viungo vya mwili, ndugu na kadhalika. [1] Kwa mujibu wa kitabu cha al-Khisal, Imam Zainul Abidin (as) alimuandikia hadithi hii mmoja wa masahaba zake katika sura ya barua. Katika nakili hii ya Shekhe Saduq ni kwamba, imekuja mwanzoni mwa hadithi: "Hii ni barua ya Ali ibn Hussein kwa mmoja wa masahaba zake."[2]

Itibari ya Hadithi na Vyanzo Vyake

Wataalamu na wahakiki wa elimu ya hadithi kwa kuzingatia mlolongo wa mapokezi (sanadi) ya Risalat al-Huqu na kwamba, imekuja na kupokewa katika vitabu vyenye kuaminika, wanaitambua hadithi hii kuwa ina itibari na ya kuaminika mno. [3] Hadithi hii imenukuliwa na Abu Hamza Thumali kutoka kwa Imam Zainul Abidin (as) ambapo wataalamu wa elimu ya hadithi wa Kishia wanamtaja kama ni "mmoja wa Mashia wateule" na mtu wa kuaminika.[4] Vyanzo vikongwe zaidi pia vya hadithi ambavyo ndani yake riwaya zimenukuliwa kwa ukamilifu ni: Tuhaf al-Uqul, kilichondikwa na Ibn Shu'ba Harrani, [5] (aliaga dunia 381 H), al-Khisal, [6] Man La Yahdhuruh al-Faqih [7] na al-Amali,[8] ambavyo vyote vitatu vimeandikwa na Shekhe Swaduq (aliyeaga dunia 381 H). Shekhe Mirza ibn Hussein ibn Muhammad Nouri Tabarsi, mashuhuri kwa lakabu ya Muhaddith Nouri amesema katika kitabu chake chha Mustadrak al-Wasail kwamba, Sayyid ibn Tawus (589-664) naye ameileta hadithi hiyo katika kitabu chake cha Fallah al-Wasail na kusema kwamba, amenukuu hadithi hiyo kutoka katika kitabu cha Rasail al-Aimah kilichoandikwa na Muhammad bin Ya'buq Kulayni mashuhuri kwa lakabu ya Thiqatul-Islam.[9] Hata hivyo maneno haya hayapo katika nakala iliyochapishwa ya kitabu cha Fallah al-Wasail; lakini wasahihishaji wa Mustadrak wanasema kuwa, yanapatika katika nakala ya lithografia (iliyoandikwa na kuchora na jiwe).[10] Nukta nyingine ni kuwa, kitabu cha Rasail al-Aimah cha Kulayni hakipo tena.[11]

Tofauti ya Vyanzo

Katika vyanzo vya hadithi matini ya hadithi ya Risalat al-Huquq imekuliwa ikiwa na utofauti. Miongoni mwa vyanzo hivyo ni vitabu viwili vya Tuhaf al-Uqul na al-Khisal ambavyo ndani yake hadithi hii imekuja kwa sura pana zaidi na ina utangulizi ambao unabainisha dondoo ya maudhui. [12] Utangulizi huu haupo katika kitabu cha Man la yahdhuruuh al-faqih na al-Amali. [13] Kadhalika katika kitabu cha al-Amali, hadithi hii inaanza na maudhui ya haki ya mtu kwake yeye mwenyewe [14] kinyume na vitabu vingine vitatu ambavyo vyenyewe vinaianza hadithi hii kwa haki ya Mwenyezi Mungu. [15]

Idadi ya Haki

Idadi ya haki ambazo zimebainishwa katika risala ya haki (Risalat al-Huquq) kwa mujibu wa Tuhaf al-Uqul ni khamsini. Imekuja katika kipande cha chini cha hadithi hii katika kitabu hiki kwamba: "Hizi ni haki 50 ambazo...". [16] Hata hivyo maneno haya hayapo katika nakili za Shekhe Swaduq kuhusiana na hadithi hii; [17] lakini Shekhe Swaduq pia alikuwa akitambua na kuamini kwamba, idadi ya haki hizo ni 50; kwa sababu katika kitabu cha al-Khisal amechagua anuani hii kwa ajili ya hadithi hii ambayo ni: "Haki 50 za Ali bin al-Hussein Kwa Masahaba Zake."[18] Baadhi ya waandishi walionukuu matini ya hadithi ya Risalat al-Huquq wametaja idadi ya haki hizo kuwa ni 51.[19] Wamesema kuwa, sababu ya jambo hilo ni kwamba, katika kitabu cha Tuhaf al-Uqul, haki ya Hija haikutajwa; lakini katika riwaya ya Swaduq imekuja.[20] Uchambuzi na tathmini iliyofanywa na mmoja wa wataalamu na wahakiki wa hadithi umezungumzia suala hili kwamba, haki ya hija ilikuwa ni katika sehemu ya hadithi ambayo ilisahaulika katika kitabu cha Tuhaf al-Uqul; pamoja na hayo yote, haki hizo ni zile zile 50 na waandishi katika kuzihesabu haki, walihesabu jambo ambalo halikuwa haki na wakalijaalia kuwa ni haki.[21]

Yaliyomo

Kuna haki 50 katika hadithi ya Risalat al-Huquq ambazo zimegawanywa katika mafungu saba: 1. Haki ya Mwenyezi Mungu 2. Haki ya viungo vya mwili; Ulimi, sikio, jicho, mkono, mguu, tumbo na utupu (uchi). 3. Haki ya matendo (amali): Sala, Hija, Saumu, sadaka na kuchinja. 4. Haki ya viongozi: Mtawala, mwalimu na mmiliki (haki ya Bwana kwa mtumwa wake). 5. Haki ya raia: Watu (haki ya watu kwa watawala), mwanafunzi, mwenza na mtumwa (haki ya mtumwa kwa Bwana wake). 6. Haki ya watu wa familia kwa mujibu wa nasaba: Mama, baba, mtoto na kaka. 7. Haki za wengine: Mtu ambaye amekuokoa kutoka katika utumwa, mtumwa ambaye wewe umemuokoa, mtenda wema, muadhini, Imamu wa Sala ya Jamaa, mtu unayeishi naye, jirani, rafiki, mshirika, mali, mdaiwa, sahiba, mwenye madai, anayekabiliwa na madai, mwenye kukushauri, mwenye kutaka ushauri kutoka kwako, mtaka nasaha, mwenye kunasihi, mkubwa, mdogo, mwenye kukuomba, mwenye kuombwa, mwenye kukufanyia ubaya, mwenye kukufurahisha, wenye dini moja na kafiri dhimmi (kafiri anayeishi katika nchi ya Kiislamu ambaye kwa mujibu wa sheria anapaswa kutoa kodi).[22]


Tarjuma Mbalimbali

Kuna tarjuuma mbalimbali za hadithi ya Risala ya Haki ya Imam Sajjad (as) kwa lugha ya Kifarsi. Katika kitabu cha Utambuzi wa kitabu cha Imam Sajjad kumetajwa takribani tarjumi 30 za hadithi hii kwa lugha ya Kifarsi. [23] Miongoni mwa tarjumi hizo ni: • Tarjumi ya Risalat al-Huquq ya Imam Sajjad; Reza Behtash. • Tarjumi ya Risalat al-Huquq ya Imam Sajjad: Sima Muuminin; Muhammad Sadiq Ghobadi • Tarjumi ya Risalat al-Huquq ya Imam Sajjad; Muhammad Javad Molaviniya. • Tarjumi ya Risalat al-Huquq ya Imam Sajjad; Ali Shiravani. [24]. Fauka ya hayo, hadithi hii imetarjumiwa pia katika baadhi ya vitabu ambavyo vimetarjumiwa na hadithi hiyo ilikuwa ndani yake kama vile tarjumi ya al-Khisal ya Shekhe Swaduq iliyofanywa na Muhammad Baqer Kameraei, Zendegani Ali bin al-Hassan, kilichoandikwa na Ja'afar Shahidi na tarjuma ya Tuhaf al-Uqul ya Ahmad Jannati. [25] Inaelezwa kuwa, yumkini aliyetarjumu kwa mara ya kwanza Risalat al-Huquq kwa lugha ya Kifarsi alikuwa Muhammad Baqir Khatunabadi (aliyeaga dunia 1127 H). [26] Kitabu cha Risalat al-Huquq kimetarjumiwa pia kwa lugha mbalimbali kama Kiingereza, Kifaransa, Kiurdu, Kihindi, Kimalayo, Kiserbia, Kiamhari na kadhalika. [27]