Hajar al-Aswad

Kutoka wikishia
Makala hii inahusiana na Hajar al-Aswad (Jiwe Jeusi). Ili kufahamu kuhusiana na rukn hajar al-Aswad (moja ya engo za Kaaba) na kugusa na kubusu angalia katika Rukn Hajar al-Aswad na kugusa hajar.
Eneo la Hajar al-As'wad katika Kaaba

Hajar al-Aswad ni jiwe jeusi ambalo linapatikana katika moja ya kuta za al-Ka'aba tukufu (Nyumba ya Mwenyezi Mungu huko Makka). Jiwe hili ambalo liko katika pembe moja upande wa Mashariki mwa nguzo ya Al-Yamani. Kwa mujibu wa hadithi kutoka kwa Imamu Muhammad Baqir(a.s) ni kuwa, Hajar al-Aswad ni moja kati ya mawe matatu ya peponi ambayo yapo katika mgongo wa ardhi. Mtume (s.a.w.w) ameusia kugusa na kubusu Hajar al-Aswad na mafaqihi (wanazuoni wa elimu ya fiqhi) wa kiislamu wanaamini kuwa, ni mustahabu kubusu jiwe hili. Kufanya tawafu (kuzunguka) Kaaba huanzia na kumalizikia mkabala na Hajar al-Aswad. Katika kila tawafu ya wajibu na sunna imesisitizwa na kutakiwa kugusa Hajar al-Aswad kwa mkono wa kulia na kulibusu, na kama haikuwezekana kufanya hivyo basi kuashiria kwa mkono na kuhuisha mfungamano na ahadi nalo. Kwa mujibu wa baadhi ya wanazuoni wa kishia, katika mzozo wa Muhammad ibn Hanafia na Imamu Sajjad (a.s) kuhusiana na kuwa Imamu, Imamu Sajjad (a.s) alilifanya Hajar al-Aswad kuwa hakimu na jiwe hilo likatoa ushahidi kwa Uimamu wa Imamu Sajjad (a.s). Katika kipindi chote cha historia, jiwe hili tukufu lilishambuliwa mara kadhaa na kulijitokeza watu wengi waliokuwa na nia ya kuliharibu au kuliiba ambapo baadhi ya wakati walifanikiwa.

Utambulisho na nafasi ya Hajar al-As'wad

Imamu Ja’afar Swadiq (a.s) amesema: {Mwenyezi Mungu ameumba Hajar al-Aswad na kisha kuchukua ahadi kutoka kwa waja. Halafu akaliambia jiwe hilo: Weka na hifadhi ahadi hii ndani yako. Waumini kwa kugusa Hajar al-Aswad huonyesha kufungamana kwao na ahadi yao}. [1]

Hajar al-Aswad ni jiwe jeusi ambalo limewekwa katika ukuta wa al-Kaaba (Nyumba ya Mwenyezi Mungu huko Makka). Jiwe hili ambalo liko katika pembe moja upande wa Mashariki [2] mwa nguzo ya Al-Yamani [3]. Jiwe hili lina thamani kubwa mno ya kiroho kwa Waislamu. [4] Upande wa Mashariki mwa al-Ka'aba kutokana na kuwa na Hajar al-Aswad hapo, ni mashuhuri pia kwa ruknu au nguzo ya hajar al-aswad. [5] Urefu wake kutoka katika usawa wa ardhi ya Masjdul-Haram ni mita moja na nusu. Jiwe hilo limefunikwa na chuma cha fedha safi kabisa ni sehemu ya mabaki ya maeneo ya awali ya kufanyia ibada katika mgongo wa ardhi. Mabaki ya jiwe hili hii leo ni vipande vidogo vinane ambapo kikubwa miongoni mwao kina usawa wa tende moja. [6] Kwa mujibu wa hadithi kutoka kwa Imamu Muhammad Baqir(a.s) ni kuwa, kuna mawe matatu kutoka peponi ambayo yapo katika mgongo wa ardhi na moja kati ya mawe hayo ni Hajar al-Aswad. [7]

Jina la Hajar al-Aswad halijaja katika Qur’an Tukufu. Pamoja na hayo katika Surat Al-Imran imekuja kwamba, nyumba ya Mwenyezi Mungu ina ishara za wazi [8] na katika tafsiri ya Aya hii, Hajar al-Aswad imetajwa kuwa ni moja ya mifano ya wazi ya ishara za wazi za al-Ka'aba.[9] Khalifa wa pili, aliitambua Hajar al-Aswad kwamba, ni jiwe ambalo halina madhara wala manufaa kwa mwanadamu. Aliamini kuwa, kuipenda Hajar al-Aswad ni kwa sababu tu Mtume alikuwa akilipenda. Imamu Ali (as) alipingana na mtazamo huo wa Khalifa na kusema, Mwenyezi Mungu atalihuisha jiwe hili Siku ya kiyama katika hali ambayo litakuwa na ulimi mmoja na midomo miwili na kutoa ushahidi kwa wale ambao walifungamana na ahadi yao. Jiwe hili ni mithili ya mkono wa kuume wa Mwenyezi Mungu ambapo kupitia kwalo viumbe wanampa baia na kiapo cha utii. [10]. Katika ibada ya Umrat al-Qadhaa, Bwana Mtume (s.a.w.w) akiwa amepanda ngamia, alifanya tawafu [11] na kugusa Hajar al-Aswad kwa fimbo yake. [12]

Fadhila

Ali Shariati: Wakati wa kuanza ni lazima uiguse Hajar al-Aswad kwa mkono wako wa kulia. Jiwe hili ni nembo ya mkono, mkono wa kulia, mkono wa kulia wa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu amekuletea mkono wake wa kulia, nyoosha mkono wako wa kulia na mpe kiapo cha utiifu, funga naye mkataba na ahadi, batilisha ahadi na mikataba yako yote ya huko nyuma. [13].

Mtume aliusia kuguswa Hajar al-Aswad kwa mkono wa kulia na alilitambua jiwe hilo kuwa mkono wa kulia wa Mwenyezi Mungu ambao watu wanaugusa. [14] Ayatullah Jawadi Amoli (alizaliwa 1312 Hijiria Shamsia), mmoja wa Maulamaa wa Kishia anaamini kuwa, kugusa Hajar al-Aswad maana yake ni Waislamu kutoa kiapo cha dhati ya Mwenyezi Mungu. [15] Baadhi ya wanazuoni wamesema kuwa, maneno hayo ya Mtume ni kwa maana kwamba, inawezekana kufikia saada na ufanisi kupitia jiwe hili takatifu. [16] Kadhalika kuna hadithi iliyonukuliwa ambapo inaeleza kwamba, baada ya Imam Mahdi(a.t.f.s) kudhihiri ataegemea katika Hajar al-Aswad na watu watakuwa wakimpa kiapo cha utiifu. [17]

Katika kitabu cha Tafsir Nemooneh imeelezwa kuhusiana na fadhila za jiwe hili ya kwamba: Hajar al-Aswad ni kifaa na nyenzo kongwe zaidi ya ujenzi iliyotumika katika kituo cha ibada; kwani maeneo yote ya ibada yaliyoko katika mgongo wa ardhi yamekarabatiwa na kujengwa upya mara kadhaa na vifaa vyake vya ujenzi vimebadilishwa, isipokuwa jiwe hili pekee ndilo ambalo licha ya kupita maelfu ya miaka, limebakia kuwa sehemu thabiti katika eneo hilo la ibada. [18] Katika vitabu na vyanzo vya Kishia kumeusiwa na kusisitizwa kusoma baadhi ya dua kando ya Jiwe Jeusi (Hajar al-Aswad). [19] Ibada ya kutufu na kuzunguka al-Kaaba huanzia katika Hajar al-Aswad na kuishia hapo pia. [20] Katika kila tawafu ya wajibu au mustahabu imeusiwa kugusa jiwe hilo kwa mkono wa kulia na kulibusu, na kama hilo haliwezekani basi kuliashiria kwa mkono na kuhuisha nalo ahadi na mkataba. [21] Inaelezwa kuwa, Hajar al-Aswad katika kipindi chote cha historia lilikuwa likiheshimiwa mno na hakuna wakati wowote hata katika zama za ujahilia ambapo liliabudiwa na halikuwa na katika orodha ya masanamu, bali daima lilikuwa ni alama na ishara ya Tawhid(kumpwekesha Mwenyezi Mungu) na kupinga shirki. [22]

Istilam hajar (Kugusa jiwe)

Makala ya asili: Kugusa Jiwe

Istilam Hajar maana yake ni kugusa Hajar al-Aswad na kulibusu kwa nia ya kutabaruku na kupata baraka. [23] Imesisitizwa na kuusiwa katika hadithi na riwaya nyingi juu ya kugusa Hajar al-Aswad na kulibusu jiwe hili takatifu. [24] Mafaqihi wa Kishia na Kisuni wanasema kuwa, ni mustahabu kugusu na kubusu Hajar al-Aswad. [25]

Allama Sayyid Muhammad Hussein Tabatabai anasema katika Tafsir al-Mizan kwamba: Hukumu ya kugusa na kubusu Hajar al-Aswad ni ishara kwamba, hadithi na Aya zote zimeusia kuadhimisha na kutukuza alama za Mwenyezi Mungu, kuonyesa mapenzi na huba kwa Bwana Mtume (s.a.w.w) na kizazi chake na vilevile maagizo mengine mfano wa haya yalikuwa sahihi na hakuna mushkeli na tatizo na haiwezekani kuyahesabu hayo kuwa ni shirki na kumshirikisha Mwenyezi Mungu. [26]

Asili na rangi

Hitilafu kutengeneza picha ndogo:
Picha ya vipande vya hajar al-as'wad

Hajar al-Aswad linatambuliwa kama ni jiwe miongoni mwa mawe ya peponi [27]. Kwa mujibu wa riwaya na hadithi mbalimbali, katika asili Hajar al-Aswad lilikuwa mmoja wa Malaika ambaye alikuwa na mfungamano mno na ahadi ya Mwenyezi Mungu kuliko malaika wengine wote, na hivyo Allah akamfanya kuwa mwaminifu na mtunza amana kwa viumbe wote. [28]

Kwa mujibu wa baadhi ya nukuu, Nabii Adam (a.s) alitumia jiwe hili la peponi kujengea al-Ka'aba. [29] Katika zama za kujengwa tena al-Ka'aba na Nabii Ibrahim (a.s), jiwe hili lilikuwa katika mlima Abu Qays na Nabii Ibrahim akalichukua na kulibandika katika Kaaba. [30].

Kwa mujibu wa hadithi mbalimbali awali jiwe hili rangi yake ilikuwa nyeupe lakini kutokana na dhambi za watu, kugusa jiwe hilo wahalifu na wanafiki, rangi yake ikabadilika na kuwa nyeusi. [31] Imeelezwa kuwa, kubadilika rangi hiyo na kuwa nyeusi sababu yake ni kuungua mara kadhaa al-Ka'aba katika duru mbalimbali. [32] Kadhalika baadhi ya hadithi zinasema, rangi ya jiwe hili ilibadilika na kuwa nyeusi kutokana na makafiri kuligusa. [33]

Muhammad Jawad Mughniyah (alizaliwa 1322 Hijria) mmoja wa wafasiri wa zama hizi wa kishia anaamini kuwa, suala la Hajar al-Aswad kuwa ni la peponi na kwamba, awali jiwe hili lilikuwa jeupe na kisha likabadilika rangi na kuwa jeusi ni maneno yanayotokana na hadithi ambayo siyo ya kutegemewa usahihi wake au ni utungaji visa ambapo sisi hatuna jukumu na kukubali hayo. [34]

Matukio ya kihistoria

Ilikuwa miaka mitano kabla ya kutimilizwa Bwana Mtume na kupewa Utume katika tukio la kukarabatiwa al-Ka'aba ambapo kila kabila miongoni mwa makabila lilitaka lenyewe ndio lipachike na kubandika Hajar al-Aswad. Hitilafu zikaongezeka na kushadidi kuhusiana na jambo hilo na hatimaye kwa pendekezo la Muhammad (s.a.w.w) jiwe hili likawekwa katika kitambaa na kila upande wa kitambaa hicho wakashikilia viongozi na wakuu wa makabila na baada ya kufika sehemu ya kuweka jiwe hilo, Mtume mwenyewe akalichukua na kulibandika sehemu yake mahususi [35] na kwa hekima na busara hiyo akawa ameepusha kuibuka mzozo mkubwa na hata pengine mapigano baina ya makabila hayo.

Kwa mujibu wa nukuu ya Ibn Hamza Tousi, msomi na mwanazuoni wa Kishia katika karne ya 6 Hijiria [36] na wengine [37] katika mzozo wa Muhammad ibn Hanafia na Imamu Sajjad (a.s) kuhusiana na Uimamu, Imamu Sajjad alimwambia na kumueleza ibn Hanafia lakini alipinga maneno ya Imamu. Hatimaye Imamu alilifanya jiwe la Hajar al-Aswad kuwa hakimu na jiwe hilo kwa idhini ya Mwenyezi Mungu likatoa ushahidi kwa Uimamu wa Imamu Sajjad (a.s).

Katika kipindi chote cha historia, jiwe hili tukufu lilishambuliwa mara kadhaa na kulijitokeza watu wengi waliokuwa na nia ya kuliharibu au kuliiba. [38] Dhul-Hija 317 Hijiria kundi la Qarmatian lilishambulia Makka. Likang’oa Hajar al-Aswad na kulipeleka katika makao yao makuu. Mwaka 339 Hijiria Qarmatian wakakubali kurejesha Hajar al-Aswad lakini kwa kupatiwa kiwango kikubwa cha fedha.[39]

Vyanzo

  • Aḥmad b. Ḥanbal. Musnad al-Imām Aḥmad b. Ḥanbal. Beirut: Dār Ṣādir, [n.d].
  • Azraqī, Muḥammad b. ʿAbd Allāh. Akhbār Makka wa mā jāʾa fīhā min al-āthār. Narration of Isḥāq b. Aḥmad Khuzāʿī. volume 1. Göttingen: 1275 AH.
  • ʿAyyāshī, Muḥammad b. Masʿūd al-. Tafsīr al-ʿAyyāshī. Edited by Rasūlī Maḥallātī. Qom: 1380-1381 AH.
  • Fāsī al-Makkī, Muḥammad b. Aḥmad. Shifāʾ al-gharām bi akhbār al-balad al-ḥarām. Beirut: Dār al-Kitāb al-ʿArabī, [n.d].
  • Ḥusayn ʿAbd Allāh Bāslāmih. Tārīkh al-kaʿba al-muʿazzama, ʿimāratuhā wa kiswatuhā wa sidānatuhā. Edited by Yaḥyā Ḥamza Wazna. Cairo: 1420 AH-2000.
  • Hughes, Thomas Patrick. A Dictionary of Islam. p. 154. W. H. Allen & Co, 1885.
  • Ibn Hishām, ʿAbd al-Malik. Al-Sīrat al-Nabī. Edited by Muḥammad Muḥyi al-Dīn ʿAbd al-Ḥamīd. Cairo: 1963.
  • Ibn Zahīra, Muḥammad Jārullāh. Al-Jāmiʿ al-laṭīf fī faḍl-i Makka wa ahluhā wa bināʾ al-Bayt al-Sharīf. Edited by ʿAlī ʿUmar. Cairo: 1423 AH.
  • Jazīrī, ʿAbd al-Raḥmān. Al-Fiqh ʿalā al-madhāhib al-arbaʿa. Istanbul: 1404 AH-1984.
  • Kurdī, Muḥammad Ṭāhir. Al-Tārīkh al-qawīm li Makka wa bayt Allāh al-karīm. Beirut: 1420 AH.
  • Kurdī, ʿUbaydullāh Muḥammad Amīn. Makka wa Madīna: taṣwīrī az tuwsiʿa wa nawsāzī. Translated to Farsi by Ḥusayn Ṣābirī. [n.p]: Muʾassisat Tahqīqāt wa Nashr Maʿārif Ahl -al-Bayt (a), [n.d].
  • Kharbutali, ʿAlī Ḥasanī. Tārīkh al-kaʿba. Beirut: 1411 AH.
  • Murwārīd, ʿAlī Aṣghar. Qawāmīs al-Ḥajj. Tehran: Markaz al-Buhūth al-Ḥajj wa al-ʿUmra, 1406 AH.
  • Maṭar, Fūziya Ḥusayn. Tārīkh ʿimārat al-ḥaram al-Makkī al-sharīf ilā nihāyat al-ʿaṣr al-ʿAbbāsī al-awwal. Jeddah: 1402 AH-1982.
  • Mughnīya, Muḥammad Jawād al-. Al-Fiqh ʿalā madhāhib al-khamsa: al-Jaʿfarī, al-Ḥanafī, al-Mālikī, al-Shāfiʿī, al-Ḥanbalī. Beirut: 1404 AH.
  • Muqaddas Ardibīlī, Aḥmad b. Muḥammad. Majmaʿ al-fāʾida wa al-burhān fī sharḥ irshād al-adhhān. Edited by Mujtabā Irāqī, ʿAlīpanāh Ishtihārdī and Ḥusayn Yazdī Iṣfahānī. volume 7. Qom: 1409 AH.
  • Rāwandī, Saʿīd b. Hibat Allāh al-. Al-Kharāʾij wa l-jarāʾiḥ. Qom: 1409 AH.
  • Shahīd al-Thānī, Zayn al-Dīn b. ʿAlī. Al-Rawḍa al-bahiyya fī sharḥ al-lumʿat al-Dimashqiyya. Edited by Muḥammad Kalāntar. Najaf: 1398 AH.
  • Ṣadūq, Muḥammad b. ʿAlī al-. Man lā yaḥḍuruh al-faqīh. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī. Qom: 1404 AH.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. [n.p]. [n.d].
  • Majlisī, Muḥammad Bāqir al-. Biḥār al-anwār. [n.p]. [n.d].
  • Dihkhudā, ʿAlī Akbar. Lughatnāma. [n.p]. [n.d].
  • Ibn Athīr, ʿAlī b. Muḥammad. Al-Kāmil fī l-tārīkh. [n.p]. [n.d].
  • Ḥurr al-ʿĀmilī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Wasāʾil al-Shīʿa. [n.p]. [n.d].
  • Ṭabarī, Muḥammad b. Jarīr al-. Tārīkh al-Ṭabarī. [n.p]. [n.d].