Sunna ya Mwenye Ezi Mungu

Kutoka wikishia

Sunna ya Mwenye Ezi Mungu au Sunna za Mwenye Ezi Mungu ni istilahi ya Qur'ani inayoashiria kanuni na sheria za Mwenye Ezi Mungu katika kuendesha mchakato mzima wa uumbaji na utawala wa ulimwengu. Kwa mujibu wa wanazuoni wa Kiislamu, Sunna hizi zinatambulika kwa sifa za ukamilifu, uthabiti, na zenye kufuata na kutiririka kwenye reli yenye nidhamu madhubuti. Qur'ani ianasisitiza kwamba; Sunna hizo ni thabiti za milele, na wala haziwezi kubadilishwa wala kubadilika.

Kulingana na imani za wanazuoni wa Kiislamu, Sunna za Mwenye Ezi Mungu zinagawika katika makundi mawili muhimu, hii ni kulingana na mazingira ya ustahili wa kuwepo wa matokeo mbali mbali kuzingatia vigezo vyake: Sunna za Akhera na Sunna za Duniani. Hiyo ni kwa upande wa Mwenye Ezi Mungu mwenyewe. Pia, kwa kuzingatia athari za matendo ya mwanadamu, Sunna hizi zinagawika makundi mawili; Sunna zisizojali wa kufungika na masharti fulani, na Sunna zilizofungika katika Masharti fulani. Miongoni mwa sunna zilizotajwa katika Qur'ani ni: Sunna ya kusabiliwa na kupuruziwa kamba (istidraj), Sunna ya kuwapa waumini msaada, na Sunna ya Mwenye Ezi Mungu kubainisha na hoja kamili mbele za waja wake.

Wanazuoni wa Kiislamu pia wanasema kuwa; kudhihiri kwa Imamu Mahdi (A.S.) pamoja na masuala ya dhana ya Mahdawiyya ni miongoni mwa maakisiko wa Sunna za Mwenye Ezi Mungu. Sunnat kama vile mamlaka kuwa mikononi mwa watu wema, ushindi ya haki dhidi ya batili, na ardhi ya Mwenye Ezi Mungu kurithiwa na wanyonge, zitatimia kikamilifu wakati wa kudhihiri kwa Imamu Mahdi (a.s), jambo litakalo onesha namna ambavyo haki itakavyo shinda na utawala wa haki utakavyo enea ulimwenguni.

Kwa mujibu wa maelezo ya watafiti, welewa wa Sunna za Mwenye Ezi Mungu una athari kubwa katika kuimarisha maarifa ya kumjua Mwenye Ezi Mungu na kueneza dhana ya Tawhid katika jamii. Kwa mujibu wa imani za watafiti hawa, ufahamu wa kujua sheria zisizobadilika za ulimwenguni humu, una mchango mkubwa katika kuboresha usimamizi wa matukio ya kibinafsi na ya kijamii.

Pia, imeezwa kuwa; viongozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wamejenga msingi wa uongozi wao wa kisiasa na kijamii juu ya Sunna hizi, wakiamini kuwa kufuata Sunna hizi ni muhimu katika kufanikisha ushindi wa kijamii na kisiasa. Wao wanahusisha moja kwa moja mafanikio yao ya kisiasa na kijamii na Sunna za Mwenye Ezi Mungu katika maisha ya kila siku, wakiona kuwa hii ndiyo njia bora ya kuleta mabadiliko endelevu katika jamii ya wanadamu.

Uelewa wa Dhana ya Sunna za Mwenye Ezi Mungu

Sunna za Mwenye Ezi Mungu zimeelezwa kwa maana ya desturi na mfumo msingi unaotawala kwenye utendaji wa matendo ya Mwenye Ezi Mungu, Sunna ambazo ndiyo msingi katika utawala na uendeshaji wa ulimwengu. [1] Mwanafalsafa mashuhuri na mfasiri wa Kishia, Abdullah Jawadi Amuli, anafafanua na kuzielezea Sunna za Mwenye Ezi Mungu kama ni mfumo wa sheria za uumbaji na mpangilio wa Kiungu, unaoweza kufahamika kwa njia za welewa wa kifalsafa na kupitia matokeo ya kila siku. [2]

Kulingana na mtazamo wa watafiti mbali mbali, dhana ya Sunna za Mwenye Ezi Mungu katika mwangaza wa maana zilizomo ndani ya Qur’an, dhana hii inahusishwa na maneno maalumu ndani ya Qur’ani kama vile; “Amr” (amri), “Irada” (matakwa), “Qawl” (kauli), “Hukm” (hukumu), “Ja’al” (jaala), “Kataba” (kuandika), “Fardha” (kuwajibisha), “Qadha” (kaamuzi), na “Qadar” (kipimo). [3] Watafiti hawa wanasema kwamba; Sunna za Mwenye Ezi Mungu zina upeo mkubwa kwa namna mbili: kwanza, kwa utofauti wa mbinu na mipango ya Mwenye Ezi Mungu, na pili, kwa uenevu wa uwepo wake ulioenea mwote. Katika mtindo huu, hakuna kiumbe chochote kile kinachoweza kuwa nje ya miale ya Sunna za Mwenye Ezi Mungu, ambapo katika hali yoyote ile, kiumbe hicho hakiwezi kuacha kuzungukwa na mojawapo ya Sunnat za Mwenye Ezi Mungu. [4]


Umuhimu na Nafasi ya Sunna za Mwenye Ezi Mungu

Abdullah Jawadi Amuli anaamini kwamba; Sunna za Mwenye Ezi Mungu ni tawi miongoni mwa matawi muhimu ya elimu ambayo inastahili kupewa hadhi ya elimu kamili. Akifafanua maoni yake, anasema kwamba; Sunna hizi zina athari muhimu katika nyanja mbalimbali za maisha ya mwanadamu, ikiwa ni pamoja na siasa, jamii, utamaduni, na uchumi. Hata hivyo, elimu ya kidunia, ambayo mara nyingi inazingatia mambo yanayo husiana na hapa duniani, bila kuzingatia chanzo cha uwepo duni na maisha ya baada ya kifo, mara nyingine huonekana kuchukua nafasi ya Sunna za Mwenye Ezi Mungu. Elimu hiyo kwa baadhi ya nyakati, inaweza kuwa na athari mbaya kwa mwanadamu kwa kutofautiana na misingi ya kimaumbile na kiroho, ambayo ni kinyume na Sunna za Mwenye Ezi Mungu. [5]

Sayyid Muhammad Baqir Sadr, mwanazuoni na mwanatafakuri wa Kishia, anaamini kwamba; Sunna za Mwenye Ezi Mungu zina uhusiano wa karibu mno na malengo ya Qur'ani, ambacho ni kitabu cha wokovu kinachowatoa wanadamu katika giza na kuwaelekeza kwenye nuru. Uelewa wa moja kwa moja wa Sunna hizi una athari kubwa katika kubadilisha na kuboresha matendo ya jamii na nyenendo za mtu binafsi. [6]

Wengine wanaamini kwamba; kwa vile Sunna za Mwenye Ezi Mungu zinahusiana na jinsi ya utendekaji wa matendo ya Mwenye Ezi Mungu, pamoja uhusiano Wake na viumbe vyake, hivo basi Sunna hizi zitakuwa ni zenye kutoa ushahidi wa wazi kabisa juu ya kuwepo kwa Mwenye Ezi Mungu pamoja na kuthibitisha upweke Wake. Kwa hiyo, ni wazi kwamba; kiwango cha maarifa ya mtu na jamii juu ya welewa wa Sunnah hizi, kinaathiri moja kwa moja kiwango cha welewa maarifa ya kumjua Mungu. [7] Kama ilivyoelezwa katika Qur'ani kwamba; kupuuza Sunna za Mwenye Ezi Mungu husababisha upotevu na maangamizi. [8]

Pia kuna wengine wanaoamini kwamba: Kuelewa Sunna za Mwenye Ezi ndiyo msingi wa lazima katika kutambua matukio mbali mbali yanayo jiri ndani ya maisha ya mwanadamu. Wao wanasisitiza ya kwamba, kuelewa Sunna za Mwenye Ezi Mungu, ambazo ni misingi thabiti katika utendaji Wake, ndiyo msingi imara unaomwezesha mwanadamu kuendesha mipango binafsi na jamii, ambao unampa mwanga wa kuangaza na kukadiria matukio ya baadae. Jambo ambalo lina athari ya moja kwa moja katika nyanja za malezi na silka za mwanadamu. [9]

Uongozi Uendao Sawa na Sunna za Mwenye Ezi Mungu

Sunna za Kiungu zina nafasi maalum katika mipango ya kisiasa na kijamii ya watawala wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran; ambapo baadhi ya watafiti wanadhani kwamba; mantiki ya upinzani wa Imamu Khomeini, muasisi wa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, inakwenda sambamba na Sunna za Mwenye Ezi Mungu zilizoainishwa katika Qur'ani. [10] Kwa mtazamo wao, hata maneno yake makali dhidi ya Marekani, aliyokuwa akiyatoa kabla ya kuanza kwa mapambano yake dhidi ya utawala wa kifalme wa Iran wa wakati huo, yalitokana na welewa uliochochewa na imani yake juu Sunna za Mwenye Ezi Mungu. [11]

Seyyid Ali Khamenei, kiongozi wa pili wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, anaamini kwamba; masuala kama vile kuthamini silka njema, kujenga heshima, kujenga nguvu na upinzani, uchamungu, akili safi (kutafakari), kutenda haki, kuwa uelewa makini, kuwatambua maadui, na kufanikisha maendeleo katika jamii, yote yanategemea kuenda sambamba na Snna za Kiungu. [12] Katika maelezo yake anasema kwamba; kutowalewa maadui wa Uislamu kisawasawa, ni moja ya Sunna za Kiungu zinazowahuku watu wa jamii yenye sifa hii, kwa hukumu ya kushindwa mara kwa mara katika mapambano yao. Yeye anaamini kwamba; kila wakati Waislamu walipofanikia katika nyanja za kisiasa na kijeshi, walifanya hivyo kutokana na kufuata kwao moja ya Sunna za Kiungu. Na kila pale waliposhindwa, walishindwa kutokana na Kuachana na Sunna za Kiungu. Jambo ambalo linatokana na baadhi ya matendo yao wenyewe. [13]

Abdullah Jawadi Amoli pia anaamini kwamba, miongoni mwa Sunna za Mwenye Ezi Mungu zisizobadilika ni Sunna ya kuwapindua wale waliovuka mipaka katika uasi na upinzani dhidi ya Alla. Basi kama ilivyokuwa kwa Firauna, Marekani nayo inakaribia kumalizika nguvu zake, na kila kukicha inazidi kurudi nyuma. [14]

Matukio ya Sunna za Kiungu

Watafiti wanaamini kuwa; wakati mwengine utekelezaji wa Sunna za kiungu ulioko ndani ya Qur'ani, unaonekana kuhusishwa na Mwenye Ezi Mungu mwenyewe, kama inavyo onekana kwenye Aya ya 23 ya Suratu Al-Fat’h. Pia, baadhi ya Aya inazihusisha Sunna hizi na manabii, kama ilivyo katika Aya ya 77 ya Suratu Al-Israa, ila wakati mwingine huhusishwa na watu wa kawaida, kama inavyobainika kwenye Aya ya 13 ya Suratu Al-Hijr. [15]

Baadhi ya watafiti wanaamini kwamba; mfululizo wa matukio ya Sunna za Kiungu unajumuisha sababu zote za utokeaji wa matukio mbali mbali, za kimaumbile na zisizo za kimaumbile, ambapo matakwa na mapenzi ya Mwenye Ezi Mungu hutekelezwa ima njia ya moja kwa moja au kwa njia zisizo za moja kwa moja. [16]

Muhammad Taqi Mesbah Yazdi, mwanafalsafa na mfasiri wa Kishia, anaamini kwamba pale Mwenye Ezi Mungu anapo unganisha na kuzinasibisha kwake mwenyewe, zile Sunna zake zilizotekelezwa kupitia njia mbalimbali  ulimwengu humu, huwa anafanya hivyo ili kuwafahamisha wanadamu waweze kuelewa kwa undani zaidi juu ya upwekeshaji ya Mwenye Ezi Mungu (Tawhidi) katika ngazi ya vitendo. [17]


Sifa za Sunna za Kiungu


Wanazuoni wa Kiislamu, kwa wakitegemea Aya za Qur’ani, wametaja sifa kadhaa zinazohusiana na Sunna za Mwenye Ezi Mungu. Miongoni mwa sifa hizo ni:

·    Ueneji na Kiukamilifu: Kwa mujibu wa Aya ya 38 ya Suratu Al-Ahzab, Sunna za Kiungu hazina mipaka ya muda, mahali, au hali. Na zinawahusu watu wote bila ya kumbagua yoyote yule kati yao.

·    Kudumu na Kutobadilika: Kulingana na Aya ya 43 ya Suratu Fatir, Sunna za Kiungu hazibadiliki na wala nafasi yake haikaliwi na kitu chengine. Zinadumu bila mabadiliko tokea mwanzo wa uumbaji.

·    Adhabu ya Pamoja (inayohusiana na Sunna ya adhabu ya Kiungu): Kwa mujibu wa Aya ya 25 ya Suratu Al-Anfal, Sunna za kiungu haziwaathiri tu wenye makosa binafsi, bali inaathiri jamii yote inayokaa kimya na kupuuza makosa hayo.

·    Kutokuwa na Upendeleo na Kufwata na Mfumo Ulivyo: Kulingana na Aya ya 140 ya Suratu Aal-Imran, jamii yoyote inayopata welewa wa Sunna za Kiungu, inaweza kuzitumia kwa manufaa yake. Na yeyote anayezikiuka Sunaa za Mwenye Ezi Mungu, atashindwa na kurudi nyuma. Kama ilivyotokea katika Vita vya Uhud ambapo Waislamu walipata hasara kutokana na kukosa utii kwa amri za uongozi wao na kukosa uthabiti ndani dhamira zao. [18]


Kutobadilika Wala Kuhawilishwa kwa Sunna za Kiungu

Katika Aya ya 43 ya Suratu Faatir, Qur'ani inaeleza kuwa Sunna za Kiungu hazibadiliki wala hazihawilishwi. Kwa mujibu wa maoni ya Murtadha Mutahhari, mwanafikra wa Kishia, ni kwamba; kutobadilika kwa Sunna hizi kunamaanisha kwamba Sunna za Mwenye Mungu haziwezi kufutwa wala hakuna Sunna nyingine inayoweza kuchukua nafasi yake. Na Kutohawilishwa kwake, kunamaanisha kwamba; vipengele vya Sunna hizi haviwezi kubadilishwa wala kugeuzwa. [19]

Allama Tabatabai, mfasiri na mwanafalsafa wa Kishia, anaongeza kwa kusema kwamba; kubadilishwa kwa Sunna za Mwenye Ezi Mungu, kunahusisha hali ambapo rehema na neema zinachukua nafasi ya adhabu. Kuhamisha Sunna hizo kunahusisha ile hali ya adhabu kuhawilishwa kutoka kwnye jamii moja kwenda jamii nyingine. [20]

Baadhi ya watafiti wanaamini kuwa; mara nyingi neno "Sunna" linapotajwa pamoja na neno "kabla /قَبل " na "waliotangulia /اوّلین " ndani ya Qur'ani, [Maelezi 1: Mifano ya maneno ni kama vile "Sunnat al-awwalin / سُنَّتُ الْأَوَّلین" yanayopatikana katika Aya ya 38 ya Suratu Al-Anfal, na "Sunnat Allah fi alladhina khalaw min qabl / سُنَّةَ اللَّهِ فِی الَّذینَ خَلَوْا مِنْ قَبْل" katika Aya ya 62 ya Surah Al-Ahzab. Maneno haya yanaonyesha kuwa Sunna na kanuni za Kiungu zilizoendeshwa kwa watu wa zamani haziwezi kubadilishwa na zitaendelea kutekelezwa kwa watu wa baadae.] huwa lina lengo ya kutoa habari ya kwamba; yale matukio yaliyozikumba jamii za zamani hayawezi kubadilishwa, na kutoa onyo juu kutokea tena kwa matukio kama hayo katika vizazi vijavyo. [21] Kwa msingi huu, Qur'ani, kupitia Aya ya 137 ya Suratu Aal-Imran, inawahimiza watu kusafiri duniani na kwa kuchunguza matokeo ya jamii zilizotangulia, waweze kugundua na kuelewa namna ya Sunna za Kiungu zinavyofanya kazi. [22]


Aina za Sunna za Kiungu

Baadhi ya wanazuoni wa Kiislamu wazimegawa Sunna za Kiungu kulingana na mazingira ya ustahili na utekelezekaji wake katika makundi mawili makuu: Sunna za akhera na Sunna za kidunia. [23] Sunna za kidunia pia nazo zimegawiwa katika makundi mawili: Sunna zisizofungamana na mashrti na Sunna zenye masharti maalum. Sunna zisizofungamana na masharti, ni zile zsizotegemea matendo ya mwanadamu, kama vile Sunna ya uongofu wa kijumla jamala, ambayo imetajwa katika Aya ya 36 ya Suratu An-Nahl na Aya ya 208 ya Suratu Ash-Shu'araa, pamoja na Sunna ya kuwajaribu watu kupitia mitihani mbali mblai, ambayo imeelezwa katika Aya ya 155 ya Suratu Al-Baqarah na Aya ya 85 ya Suratu Taa-Ha, ambazo ni Sunna zinazohusiana na wanadamu wote kwa jumla bila ubaguzi.

Sunna zenye masharti maalumu ni zile zinazo tegemea matendo maalumu ya mwanadamu, kama vile Sunna ya msaada kwa waumini, iliyotajwa katika Aya ya 47 ya Suratu Ar-Rum, na Sunna ya urithi wa uongozi, iliyotajwa katika Aya ya 54 ya Suratu Al-Maidah na Aya ya 38 ya Suratu Muhammad. [24] [Maelezo 2: Hii inamaanisha kubadilishwa kwa watu wa taifa moja na kuja watu wengine katika kufaidika na neema na baraka za Mwenyezi Mungu. Hii inatokana na kanuni za Kiungu zinazo ongoza jamii na mataifa, ambapo taifa au jamii inayotenda mema na kufuata kanuni za Mwenye Ezi Mungu hupewa neema na mamlaka ya uongozi, huku wale wanaokiuka maadili ya Muungu wakipoteza nafasi zao na neema hizo kuhamia kwa wengine.]

Watafiti wa Kiislamu, wakitafakari Aya za Qur'ani Tukufu, wamezigawa Sunna za kiungu katika makundi matatu makuu na wakatoa mifano ya Aya kwa kila kundi:

1.    Sunna ya Mwenye Ezi Mungu katika kuongoza kwenye njia sahihi, kama inavyo onekana katika Aya ya 26 ya Suratu An-Nisa.

2.    Sunna ya Mwenye Ezi Mungu katika kuvunja Sunna potofu, inayopatikana kwenye Aya ya 37-38 ya Suratu Al-Ahzab.

3.    Sunna ya Mwenye Ezi Mungu katika kuwaadhibu waliotangulia, kama ilivyo elezwa katika Aya ya 137 ya SuraTu Aal-Imran, Aya ya 55 ya Suratu Al-Kahf, na Aya ya 60-62 ya Suratu Al-Ahzab. [25]

Aidha, wengine wamezigawa Sunna za Kiungu katika makundi mawili: Sunna za kimaumbile (Sunnatu Takwiiniyya) na Sunna za kisheria (Sunnatu Tashri’iyya). Sunna za kisheria, ambayo zinazohusiana na mfumo wa maisha ya binadamu, pia nazo zimegawanywa katika sehemu mbili; Sunna za kibinafsi na Sunna za kijamii. [26]


Aina za Sunna za Kiungu katika Qur'ani

Kwa mujibu wa maandishi ya wafasiri na watafiti mbali mbali, ni kwamba; baadhi ya Sunna za Mwenye Ezi Mungu zimeorodheshwa ndani ya Qur'ani. Na baadhi yake ni kama zifuatazo:

Sunna ya Imlaa: Hii inahusisha kumwacha na kumsabilia dhalimu kwa muda fulani huku akiendelea kufanya maovu ili kumpa nafasi ya kutubu. Hata hivyo, mara nyingi huwa ni kumtayarisha kwa ajili ya adhabu kali kutokana na kupindkia mipaka katika dhambi zake (Rejelea: Suratu Aal Imran, Aya ya 178; Suratu Al-Qalam, Aya ya 45). [27]

Sunna ya Istidraj: Hii ni Sunna ya neema ambazo Mwenye Ezi Mungu humpa dhalimu fulani, ili aendelee kupotea zaidi, na hivyo kumsogeza hatua kwa hatua kwenye adhabu yake (Rejelea: Suratu Al-A'raf, Aya ya 182-183; Suratu At-Tawbah, Aya ya 55 na 85). [28]

Sunna ya Ushindi kwa Waumini: Waumini wanapoishi kwa kufuata imani, Mwenyezi Mungu huwaletea baraka kutoka mbinguni na msaada wake wakati wa shida (Rejelea: Suratu Al-A'raf, Aya ya 96; Suratu Al-Fath, Aya ya 4; Suratu At-Tawbah, Aya ya 25 na 40). [29]

Sunna ya Kuwatimizia Waja Hoja Kamili: Mwenye Ezi Mungu hatoangamiza watu kwa dhuluma zao bila kutoa onyo na hoja kamilifu (Rejelea: Suratu Al-An'am, Aya ya 131; Suratu Al-Isra, Aya ya 15). [30]

Sunna ya Mitihani: Wanadamu hujaribiwa kwa majaribio mbali mbali, ya neema na ya matatizo, ili kudhihirisha imani zao (Rejelea: Suratu Al-Ankabut, Aya ya 2; Suratu Al-Anbiyaa, Aya ya 35). [31]

Sunna ya Uongofu wa Kuwaongoa Waja: Mwenye Ezi Mungu hajawaacha wanadamu bila mwongozo. Ametuma mitume na viongozi wa kuwaongoza njia sahihi (Rejelea: Suratu Ta-Ha, Aya ya 133-134; Suratu Yunus, Aya ya 47; Suratu An-Nahl, Aya ya 16; Suratu Fatir, Aya ya 24). [32]

Sunna ya Adhabu: Watu na jamii dhalimu hukumbwa na maangamizi kwa sababu ya ukosefu wa shukrani kwa Mwenye Ezi Mungu (Rejelea: Suratu Al-Kahf, Aya ya 59; Suratu Al-Anbiyaa, Aya ya 11; Suratu An-Nahl, Aya ya 112). [33]

Sunna ya Marekebisho: Mwenyezi Mungu huwapangia wanadamu riziki kulingana na hali zao. [34] Mara nyingi ziada ya riziki kwa waovu, huwa ni sehemu ya mitihani au istidraj juu yao. (Rejelea: Suratu Ash-Shura, Aya ya 27). [35]

Sunna ya Msaada (Imdaad): Hii inahusu msaada wa Mungu ni kwa binadamu wote, awe muumini au si muumini, na madhumuni ya msaada huo, ni kuwafikia malengo yao. (Rejelea: Suratu Ash-Shura, Aya ya 20; Suratu Al-Isra, Aya ya 20). [36]

Sunna ya Mabadiliko: Mabadiliko ya hatima za jamii yanategemea matendo yao. Mwenyezi Mungu haondoi balaa na kuleta neema bila ya kuwepo sababu za msingi. (Rejelea: Suratu Al-Anfal, Aya ya 53; Suratu Ar-Ra’d, Aya ya 11). [27]

Sunna ya Kupamba (Tazeen): Mwenye Ezi Mungu huwapambia waja wake matendo yao, na kila jamii hujihisabu kuwa ni watenda matendo mazuri, hata kama ni wachafuzi. (Rejelea: Suratu Al-An’am, Aya ya 108). [38]

Sunna ya Mzunguko wa Wakati (Madaawala): Hii inahusisha mzunguko wa nyakati, ambapo kundi moja linaweza kufurahia baraka za kidunia huku kundi chengine likiwemo kwenye matatizo ya dunia. [39]


Baadhi ya Sunna nyingine zaidi ya hizo zilizotajwa ni:

Sunna ya Sababu na Matokeo (Asbaab na Musabbabaat): Mwenye Ezi Mungu hutenda kupitia mfumo wa sababu na matokeo katika ulimwengu humu, ambapo kila jambo lina chanzo chake. Mambo yote hutokea duniani humu kulingana mpango huo wa Mwenye Ezi Mungu.


1.    Sunna ya Kuzingira (Makr): Hii inahusu mazingiro ya Mungu katika kuwizngira baadhi ya wanadamu, ambayo ni dhidi ya mipango mibaya ya watu waovu. Katika Qur'an imeelezwa kwamba, Mwenye Ezi Mungu hutumia mazingiro yake wa Kiungu kuwashinda wale wanaopanga uovu dhidi ya waumini.

2.    Sunna ya Riziki ya Waja: Mwenye Ezi Mungu ndiye anayetoa riziki kwa waja wake, na kila mmoja hupata kulingana na hali yake na matendo yake. Riziki ya waja ipo mikononi mwa Mungu na imepangwa kwa haki kamili.

3.    Sunna kuhusu Imani, Taqwa, na Matendo Mema: Hii inahusiana na faida na baraka ambazo waumini hupata kutokana na imani yao, uchaji wao (taqwa), na matendo yao mema. Mwenye Ezi Mungu huahidi msaada na baraka kwa wale wanaoishi kwa imani na kufanya mema.

4.    Sunna ya Walioneemeshwa Wakakosa Shukurani (Mutrifin): Hii inahusu maangamizi ya jamii zilizokuwa zimezidi kwa dhambi na uovu, hasa wale walioneemeshwa kisha wakabaki na majivuno na kujihusisha na dhuluma. [40]


Kilelecha cha Sunna za Kiungu katika Zama za Uimamu wa Mahdi (A.S)

Baadhi ya watafiti wa Kiislamu wameangazia dhana ya Mahdawiyya, na kuhusisha suala hili na Sunna za Kiungu zilizotajwa katika Qur'an. Mtazamo wa Mahdawiyya ukolezekaji wa Suna nyingi za Kiungu, zikionesha namna Uimamu wa Mahdi unavyosimamia haki katika uongozi wa wanadamu kwa mwongozo wa Mwenye Ezi Mungu. Baadhi ya Sunna hizo ni:

Sunna ya Uongozi wa Watu Wema kwa Mwelekeo wa Uongozi wa Mungu: Hii inahusiana na uongozi wa watu wema, unaoratibiwa moja kwa moja na Mwenye Ezi Mungu. Aya mbalimbali zinathibitisha kuwa uongozi wa haki ni ule unaotokana na Mungu Mwenyewe (Rejelea: Suratu Al- Maidah, Aya ya 55; Suratu Al- Nisaa, Aya ya 59).


Sunna ya Mwanadamu kuwa Khalifa wa Mungu na Kubeba Majukumu Mbali mbali: Dhana ya mwanadamu kuwa khalifa wa Mungu inamuweka kiumbe huyu katika jukumu la kuongoza kwa haki na uadilifu, akiwakilisha utawala wa Mungu duniani. (Rejelea: Suratu Al- Baqara, Aya ya 30; Suratu Al- Ahzab, Aya ya 72).

Sunna ya Hatima ya Ushindi wa Haki Dhidi ya Batili: Qur'ani inaahidi ushindi wa haki dhidi ya uovu, ambapo mwisho wa safari, haki itatawala na batili itakandamizwa. (Rejelea: Suratu Al- Nisaa, Aya ya 16; Suratu Al- Anfal, Aya ya 8; Suratu Al- Tawba, Aya ya 34).

Sunna ya Utawala wa Wanyonge (Mustadhafin) Kwenye Ardhi: Mwisho wa hatima kutakuja wakati fulani ambapo wanyonge na waliodhulumiwa watawekwa kwenye nafasi za uongozi, wakirejesha haki na usawa duniani (Rejelea: Suratu Al- Qasas, Aya ya 5).

Sunna ya Kuokolewa kwa Waumini: Mwenye Ezi Mungu huwaokoa waumini kutoka katika madhila na changamoto mbalimbali, akiwaongoza kwenye njia sahihi ya haki na uadilifu (Rejelea: Suratu Al- Yunus, Aya ya 103).

Sunna ya Uongozi wa Watu Wema: Wale waliojitakasa na kutenda mema watapewa jukumu la kuongoza katika siku zijazo, wakisimamia uadilifu (Rejelea: Suratu Al- Anbiyaa, Aya ya 105; Suratu Al- Nur, Aya ya 55).

Sunna ya Ahadi ya Mungu ya Kwamba Hatima Njema ni Wachamungu: Qur'ani inathibitisha kuwa mustakabali wa dunia, ni mali ya wachamungu, ambao watasimamia dunia kwa haki (Rejelea: Suratu Al- A'raaf, Aya ya 128).

Sunna ya Ushindi wa Uislamu Juu ya Dini Zingine: Ni ahadi kutoka kwa Mwenye Ezi Mungu ya kwamba; Uislamu utashinda dini zote na kusimama kama dini ya kweli na ya pekee ulimwenguni. (Rejelea: Suratu Al- Tawba, Aya ya 33; Suratu Al- Fat'h, Aya ya 28). [41]

Baadhi ya watafiti wa Kiislamu wanaamini kuwa; Baadhi ya Sunna kama vile; Istikhlaf (Kutawalishwa), Imtihan (Mitihani), Tamhiis (Kupimwa na Kutikiswa), Imlaa (Kuzidishiwa Neema), na Istidraj (Kupuruziwa Kamba) zinahusiana kwa karibu na dhana ya Mahdawiyya, na kwamba ghaiba ya Imamu Mahdi (a.s) ni sehemu muhimu ya mitihani ya kusubiri. Katika hali ya kutokuwepo Imamu, waumini wanatakiwa kuwa na subira wakisubiri kuja kwake, na ili kufikia ushindi wa haki dhidi ya dhuluma. [42]