Qassim Suleimani

Kutoka wikishia
Aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds katika Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) Qassim Suleimani

Qassim Suleimani (Kifarsi: قاسم سلیمانی) (1957-2020) aliyekuwa Kamanda wa kikosi cha Quds cha jeshi la walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) aliuawa shahidi alfajiri ya tarehe 3 Januari 2020 yeye na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu Mkuu wa kikosi cha kujitolea cha wananchi cha Hashdu al-Shaabi pamoja na wanamuqawama wengine kadhaa, katika shambulio la anga lililofanywa na jeshi la Marekani karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad.

Wakati wa vita vya Iraq dhidi ya Iran, (1980-1988) Qassim Suleimani alikuwa kamanda wa kikosi cha Tharallah batalioni ya 14 katika mji wa Kerman na alikuwa mmoja wa makamanda wa operesheni za Walfajir 8, Karbala 4 na Karbala 5. Mwaka 1998, Qassim Suleimani aliteuliwa na Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) ambacho kinaendesha shughuli zake nje ya mipaka ya Iran.

Qassim Suleimani alikuwa akiwasaidia Mujahidina wa Afghanistan katika vita dhidi ya Taliban, na baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Afghanistan, alichukua hatua kwa ajili ya kufanyika ukarabati huko. Katika vita vya siku 33 vya Lebanon na vita vya siku 22 huko Palestina, alisaidia Hizbullah na Hamas dhidi ya Israeli na kuupa mhimili wa muqawama na mapambano silaha za kisasa.

Baada ya kuibuka kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) nchini Iraq na Syria, kamanda Suleimani alipigana na magaidi hao kwa kuwepo katika maeneo hayo na kuandaa vikosi vya wananchi. Kuondoa tishio la Daesh kutoka Samarra, Najaf na Karbala ni moja ya mafanikio yake katika vita dhidi ya wanachama wa kundi hilo la kigaidi. Mbali na masuala ya kijeshi, pia alikuwa akifanya kazi katika masuala ya kiutamaduni. Kwa mujibu wa baadhi ya maofisa wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Qassim Suleimani ndiye aliyekuwa mwanzilishi wa Kamati ya Ukarabati wa Maeneo Matakatifu na alikuwa akisimamia mipango ya upanuzi wa Haram za Maimamu (a.s). Pia alikuwa na nafasi muhimu katika kurahisisha ziyara ya Arubaini ya Imamu Hussein (a.s) na kudhamini usalama wa wafanyaziara. Qassim Suleimani aliuawa shahidi alfajiri ya tarehe 3 Januari 2020 yeye na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu Mkuu wa Kikosi cha Kujitolea cha Wananchi cha Hashdu al-Shaabi pamoja na wanamuqawama wengine kadhaa, katika shambulio la anga lililofanywa na jeshi la Marekani na ndege isiyo na rubani karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad.

Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (Sepah) lililipiza kisasi cha shambulizi la kigaidi la serikali ya Marekani dhidi ya Kamanda wa kikosi cha Quds cha jeshi hilo, Luteni Jenerali Qassim Soleimani na Naibu Mkuu wa kikosi cha kujitolea cha wananchi wa Iraq Abu Mahdi al-Muhandis kwa kuvurusha makumi ya makombora dhidi ya kambi ya jeshi la Marekani ya Ainul-Assad nchini Iraq na Bunge la Iraq likapasisha mpango wa kufukuzwa wanajeshi wa Marekani nchini Iraq.

Qassim Suleimani na wenzake walisindikizwa katika miji tofauti ya Iraq na Iran, na Bashir Hussein Najafi na Sayyid Ali Khamenei waliswalia maiti zao huko Iraq na Iran. Kulingana na ripoti za baadhi ya mashirika ya habari, mazishi yake yalikuwa moja ya mazishi makubwa zaidi katika historia, na takriban watu milioni 25 walishiriki katika kusindikiza maiti yake. Alizikwa tarehe 7 Januari katika Makaburi ya Mashahidi ya Kerman.

Historia Yake

Qassim Suleimani alizaliwa Machi 11, 1957 katika kijiji cha Ghanat Malek moja ya viunga vya Kaunti ya Rabor katika mji wa Kerman. [1] Akiwa na umri wa miaka 18, aliajiriwa na Idara ya Maji ya Kerman. [2] Kulingana na yeye mwenyewe, alikuwa mmoja wa waandaaji wa maandamano ya Kerman, migomo na mapigano dhidi ya vikosi vya utawala wa Kifalme wakati wa harakati za Mapinduzi ya Kiislamu. [3] Alioa wakati wa vita vya kichokozi vya Iraq dhidi ya Iran [4] na alijaliwa watoto sita. [5]

Mwaka 1398 Hijiria Shamsia aliteuliwa na Sayyid Ibrahim Raisi aliyekuwa mkuu na msimamizi wa Haram ya Imamu Ridha (a.s) wakati huo kuwa muhudumu wa haram hiyo. [6] Baada ya kuuawa shahidi aliondokea kuwa mashuhuri kwa jina la kamanda wa nyoyo na kumeandaliwa na kusambazwa nembo nyingi za matangazo katika uwanja huu. [7]

Wakati wa Vita vya Iraq na Iran

Baada ya ushindi wa Mpainduzi ya Kiislamu ya Iran, Qassim Suleimani alijiunga na Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH). Hiyo ilikuwa mwaka 1981 na akawa mmoja wa wanachama wa kitengo cha mafunzo na mwalimu wa kambi ya mafunzo ya SEPAH katika mji wa Kerman. [8] Mwaka 1982 Mohsin Rezaei, Kamanda wa wakati huo wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu alimteua Qassim Suleimani kuwa kamanda wa kikosi cha 41 cha Tharallah mjini Kerman. [9] Alikuwa mmoja wa makamanda wa operesheni za Wal-Fajr nane, Karbala nne na Karbala tano katika vita vya Iraq dhidi ya Iran [10] na alijeruhiwa mara mbili, ambapo moja kati ya matukio hayo alipata majeraha makubwa. [11]

Baada ya kumalizika kwa vita vya Iran na Iraq mnamo 1988, Suleimani kipindi fulani alikuwa kamanda wa batalioni 7 ya jeshi la Sahib al-Zaman [12] na kisha kwa mara nyingine tena akawa kamanda wa batalioni ya 41 ya Tharallah, na kabla ya kuteuliwa kama kamanda wa kikosi cha Quds, alikuwa akipigana na magenge ya magendo ya madawa ya kulevya kwenye mipaka ya Iran na Afghanistan. [13]

Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la SEPAH

Makala Asili: Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH)

Mwaka 1998, Qassim Suleimani aliteuliwa na Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran kuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH). [14] Kikosi cha Quds ni tawi la Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kinachoendesha shughuli zake nje ya mipaka ya Iran ambapo mwaka 1369 Hijiria Shamsia kiliunganishwa katika muundo wa SEPAH. Kamanda wa kwanza wa kikosi hiki alikuwa Ahmad Vahidi na baada yake Qassim Suleimani akachukua jukumu la ukamanda wa kikosi hicho. Baada ya kuuawa shahidi Qassim Suleimani, Ismail Qaani alichukua jukumu la ukamanda wa kikosi hiki. [15]

Mapambano Dhidi ya Taliban na Al-Qaeda Nchini Afghanistan

Uteuzi wa Qassim Suleimani kama kamanda wa kikosi cha Quds ulienda sambamba na kupamba moto harakati za kundi la Taliban nchini Afghanistan. [16] Qassim Suleimani alikuwa akishirikiana na Mujahidina wa Afghanistan, akiwemo Ahmad Shah Massoud, [17] na kwa mujibu wa baadhi ya nukuu za Mujahidina, walipigana mara kwa mara dhidi ya Taliban na Al-Qaeda nchini Afghanistan. [18] Kumesambazwa video ya uwepo wake katika Bonde la Panjshir na mkutano wake na Ahmad Shah Massoud wakati wa vita vya Mujahidina wa Afghanistan na Taliban. [19]

Kulingana na jeshi la Afghanistan, uwepo wa Suleimani nchini Afghanistan ulikuwa na mafanikio, kwa sababu alikuwa na shakhsia ya kiutu wa kirafiki ambayo ingeweza kuufanya upande mwingine kuwa na imani naye na alikuwa na uwezo mkubwa wa kuweka msingi wa usitishaji vita na ushirikiano kati ya vikosi. [20]

Mapambano na Israel Huko Lebanon na Palestina

Qassim Suleiman akiwa na Ahmad Shah Masoud

Wakati wa uvamizi wa Israeli dhidi ya Lebanon katika vita vya siku 33, Qassim Suleimani alikuwepo katika viunga vya kusini mwa Beirut na katika chumba cha kuongozea operesheni za Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon. [21]

Kulingana na mmoja wa viongozi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS), Qassim Suleimani alikuwa na uhusiano wa kina na Hamas na alikuwa akiunga mkono muqawama na mapambano ya wananchi wa Palestina. [22] Kwa msingi huo, aliweza kuwapa Hamas silaha za hali ya juu [23] na njia za chini kwa chini zilizochimbwa kwa ajili ya kukabiliana na Israel, ilikuwa mojawapo ya mipango ya kioperesheni ya Emad Mughniyeh na Qassim Suleimani. [24]

Vita Dhidi ya Daesh Nchini Iraq

Sayyied Hassan Nasrullah akiwa na Qassim Suleiman na Imad Mughuni

Qassim Suleimani alikuwa mmoja wa makamanda wa vita dhidi ya kundi la kigaidi la Daesh nchini Iraq [25] na Syria. [26] Daesh lilikuwa kundi la Takfiri lililoibuka baada ya kuanguka kwa Saddam nchini Iraq. [27] Mnamo 2014, mji wa Mosul ulitekwa na Daesh na Baghdad, mji mkuu wa Iraq, pia ulikaribua kuporomoka na kuangukia mikononi mwa magaidi hao. Qassim Suleimani alikutana na Sayyid Ali Sistani, Marjaa Taqlidi nchini Iraq, na baada ya hapo Ayatullah Sistani akatoa fat’wa ya jihad dhidi ya Daesh (ISIS). [28]

Kwa kuandaa na kukusanya sehemu ya vikosi vya Hashd al-Shaabi, akawa na nafasi na mchango muhimu katika kuwafukuza wanachama wa kundi la kigaidi la Daesh kutoka Iraq, kiasi kwamba, Haider al-Abadi, Waziri Mkuu wa Iraq wakati huo, alimtaja Qassim Suleimani kama mmoja wa waitifaki na washirika wakuu wa Iraq katika vita dhidi ya ISIS. [29] [30] Kamanada Suleimani alitoa ushauri kwa Kikosi cha Kujitolea cha Wananchi cha Hashdu al-Shaabi, jeshi la Iraqi na vikosi vya Serikali yenye mamlaka ya kujitawala ya Kurdistan ya Iraq katika operesheni nyingi dhidi ya Daesh; ikiwa ni pamoja na kukomboa mji wa Amerli katika jimbo la Salah al-Din la Iraq, [31] kuudhibiti mji wa Tikrit na kuuondoa mikononi mwa magaidi, [32] kuzuia kupenya kwa ISIS katika mji wa Erbil kaskazini mwa Iraq, [33] na pia mapambano dhidi ya Daesh huko Samarra. [34]

Mapambano Dhidi ya Makundi ya Kukufurisha Nchini Syria

Ili kupambana na makundi ya kukufurisha likiwemo la Daesh nchini Syria, kamanda Suleimani alileta uratibu katika vikosi vya ulinzi vya Kitaifa vya Syria. [35] Mnamo 2011, vikosi vilivyo chini ya amri yake vilivyojulikana kama walinzi wa Haram, ikiwa ni pamoja na Jeshi la Fatemiyun na Jeshi la Zainbiyun, lilikwenda Syria. 36] [37] Ukombozi wa Bukamal [38], ukombozi wa mji wa kihistoria wa Tadmor kusini mashariki mwa Homs [39] na kukombolewa kwa mji wa Al-Qusayr ni miongoni mwa mafanikio yake katika vita vya Syria. 40]

Kutangazwa Mwisho wa Daesh

Katika barua aliyoituma tarehe 21 Novemba 2017 kwa Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran, Qassim Suleimani alitangaza kumalizika kwa udhibiti wa Daesh na kutangaza kupandishwa kwa bendera ya Syria huko Bukamal moja ya miji ya Syria iliyo karibu na mpaka wa Iraq [41]. Kabla ya hapo, Soleimani alikuwa ameahidi mwaka huo huo, kwamba angetangaza mwisho wa udhibiti wa Daesh katika mgongo wa ardhi chini ya kipindi cha miezi mitatu. [42] Ifuatayo ni sehemu ya jibu la Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kwa barua ya Qassim Suleimani ya kumalizika udhibiti na mamalaka ya Daesh: " Kwa juhudi zako za kusambaratisha donda la saratani linaloangamiza la Daesh, si tu kwamba, umetoa huduma kwa mataifa ya eneo na ulimwengu kwa ujuma, bali umetoa huduma kubwa kwa jamii yote ya mwanadamu." [43]

Kamati ya Kukarabati Maeneo Matakatifu na Matembezi ya Arubaini

Kamati ya Kukarabati maeneo matakatifu ilianzishwa ikiwa inapata himaya na uungaji mkono wa moja kwa moja kutoka kwa kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH) katika kipindi cha ukamanda wa Qassim Suleimani kwa kikosi hicho na kiongozi wake alikuwa akiteuliwa na Suleimani. [44] Kadhalika kamanda Suleimani alikuwa na mchango muhimu katika kudhamini usalama kwa wafanyaziara (mazuwwar) wa matembezi ya Arubaini ya Imamu Hussein (as) na vilevile kuandaa suhula za lojistiki na vifaa vya huduma kwa wafanyaziara wa Arubaini ya Imamu Hussein (a.s), [45] na kutokana na juhudi zake visa ya Iraq kwa wafanyaziara wa Iran wa Arubaini ya Imamu Hussein (a.s) ikafutwa. [46]

Vyeo vya Kijeshi

Kutunukiwa nishani ya Zulfiqar na kiongozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa Qasim Suleimani mnamo 1397.

Mwaka 1389 Hijiria Shamsia, Sayyid Ali Khamenei, Amiri Jeshi Mkuu wa Iran alimpatia kamanda Qassim Suleimani cheo cha Meja Jenerali. [47] Mnamo Machi 10, 2019, Ayatullah Khamenei alimpa Suleimani nishani ya kijeshi ya Dhu l-Fiqar, [48] ambayo hupewa makamanda wa ngazi za juu wa kijeshi na wakuu katika vikosi vya ulinzi vya Iran ambao mipango ya tadibiri yao huwa na matokeo mazuri na muhimu ya ushindi. [49] Qassim Suleimani alikuwa kamanda wa kwanza kupokea nishani hii baada ya Mapinduzi ya Kiislamu mwaka 1979. [50] Aidha baada ya kuuawa kwake shahidi alipatiwa cheo cha Luteni Jenerali. [51]

Sifa Zake Maalumu

Kwa mtazamo wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran katika faili la maisha ya Suleimani, kunashuhudiwa miaka mingi ya mapambano ya dhati, yenye ikhlasi na ya kishujaa katika uwanja wa kupambana na mashetani na watenda maovu wa dunia na miaka mingi ya kutamani kufa shahidi. [52] Baadhi ya sifa zake nyingine maalumu katika nyanja mbalimbali ni: Kuwa na mapenzi maalumuu na kushikamana na Ahlul-Bayt (a.s), kuwa mtu wa uongozi wa kidini, uchamungu na kushikamana na umaanawi, kipaji cha kijeshi, roho ya ushujaa na kupambana, roho ya kutafuta kifo cha kishahidi, uaminifu, kuwa mtu wa kimataifa, umahiri katika uwanja wa diplomasia, hima na kufanya kazi kwa bidii, nidhamu na usahihi katika mambo, kuwa na misimamo ya wastani na ya kati na kati, kuwa mtu wa watu [53], kuwa na haiba ya kimataifa ya muqawama na mapambano, kuleleka katika Uislamu na njia na shule ya Imamu Khomeini [54], kunufaika na moyo wa kujitolea, kuwa na hali ya urafiki kutokuwa na woga katika njia ya Mwenyezi Mungu, na kutenda wajibu na jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu [55].

Dondoo za Maneno Yake

  • Ujasiri wa kuunda utawala wa Kiislamu ili kutoa utambulisho kwa nguzo zote za dini ulikuwa ni kielelezo maalumu cha Imamu Khomeini. Utumishi na huduma iliyotolewa na Imamu Khomeini haiwezi kulinganishwa na kazi ya mtu mwingine yeyote. [56]
  • Kipengele muhimu zaidi cha umoja ni kuwa na umoja katika masuala ya kimsingi. [57]
  • Ikiwa Mungu anampenda mtu fulani, anaijaza mioyo ya watu upendo, huba na mapenzi yake.[58]

Kuuawa Katika Uwanja wa Ndege wa Baghdad

Qassim Suleimani aliuawa shahidi alfajiri ya tarehe 3 Januari 2020 yeye na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu Mkuu wa Kikosi cha Kujitolea cha Wananchi cha Hashdu al-Shaabi pamoja na wanamuqawama wengine kadhaa, katika shambulio la anga lililofanywa na jeshi la Marekani kwa kutumia ndege isiyo na rubani karibu na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Baghdad. [59]

Saa chache baada ya shambulio hili, Wizara ya Ulinzi ya Marekani ilitoa taarifa na kutangaza kwamba shambulio hilo kwenye gari lililombeba Qassim Suleimani lilitekelezwa kwa amri ya Rais wa wakati huo wa Marekani Donald Trump. [60]

Qassim Suleimani aliwahi kulengwa mara kadhaa kabla na akanusurika kifo. Kwa mara ya kwanza ilikuwa mnamo mwaka 1360 Hijiria Shamsia wakati alipolengwa na shambulio la daktari aliyehusishwa na kundi la Munafiqin (MKO). [61] Mapema mwaka 1398, Hussein Taeb, Mkuu wa Kitengo cha Shirika la Kiintelijeshi cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH) alitangaza habari ya kukamatwa kwa watu waliopanga kumuua Qassem Suleimani katika mji wa Kerman. [62]

Radiamali

Kuuawa kwa Qassim Suleimani katika operesheni ya kigaidi kulifuatiwa na malalamiko na maandamano katika nchi tofauti za ulimwengu, na kulifanyika marasimu (hafla) za kumkumbuka katika miji tofauti ya Iran na nchi zingine za ulimwengu, na pia shakhsia wa kisiasa na kidini wa Iran na nchi zingine walionyesha radiamali zao kwa mauaji yake. Katika ujumbe wake, Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran, alimtaja Qassim Suleimani kuwa ni shakhsia wa kimataifa wa muqawama na mapambano na akatangaza siku tatu za maombolezo ya umma nchini Iran kwa mnasaba wa "kuuawa kwake shahidi". [64]

Watu wengine wa kisiasa na kidini, wakiwemo wakuu wa Mihimili Mikuu Mitatu ya dola ya Iran, Marajii Taqlidi wa Iran na Iraq walitoa risala na jumbe tofauti wakisifu ushujaa wake, ikhlasi na kujitolea kwake. [65]

Sayyid Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon, Sayyid Abdul Malik Badr al-Din al-Houthi, kiongozi wa Ansarullah ya Yemen, na Marais wa Syria, Lebanon, na Iraq walikuwa miongoni mwa shakhsia wa kisiasa wasio wa Iran waliolaani mauaji ya Qassim Suleimani. [66] Marais wa Afghanistan [67] na Uturuki [68], pamoja na Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Russia walitoa mkono wa pole na rambirambi zao kwa taifa la Iran kutokana na kifo cha kamanda huyu wa muuqawama. [69] Agnes Calamard Ripota Maalumu wa Umoja wa Mataifa alisema, mauaji yaliyopangwa dhidi ya Qassim Suleimani na Abu Mahdi al-Mohandis yalikuwa kinyume cha sheria na yanayokinzana na sheria za kimataifa. [70] Yervand Abrahamian, mwanahistoria wa Kimarekani pia alisisitiza kwamba, Wairani walikuwa wakiichukulia Marekani kama serikali ya njama, na kuanzia sasa na kuendelea wataichukulia serikali hiyo kama ya kigaidi. [71] Mtengeneza filamu wa Marekani Michael Moore alipinga hatua ya serikali ya Marekani na akasema kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwamba, serikali ya Washington inapenda vita. [72]

Matokeo

Baadhi ya matokeo ya kuuawa shahidi Qassim Suleimani ni:

  • Kupasishwa mpango wa kuwafukuza Wamarekani kutoka Iraqi: Baada ya kuuawa shahidi Qassim Suleimani na Abu Mahdi Al-Muhandis, baadhi ya makundi ya kisiasa ya Iraq na baadhi ya watu katika nchi hiyo walitoa mwito wa kufukuzwa kwa wanajeshi wa Marekani kutoka katika ardhi ya Iraq. Januari 5 , 2020, Bunge la Iraq lilipiga kura na kupitisha mpango uliopendekezwa na wabunge wa kuhitimisha makubaliano ya kijeshi yaliyofikiwa kati ya nchi hiyo na Marekani na kuwataka wanajeshi wa Marekani waondoke nchini humo, [73] ingawa suala la kuwafukuza wanajeshi wa Marekani kutoka Iraq lilikuwa limeibuliwa mapema baada ya mashambulizi ya Marekani dhidi ya ngome za Hashd al-Shaabi, na Sayyid Kadhim Hairi Marjaa Taqlid pia alikuwa ametangaza kwamba, ni haramu kwa majeshi ya Marekani kuendelea kubakia nchini Iraq.[74]
  • Mashambulio ya makombora ya Iran dhidi ya kambi ya jeshi la anga la Marekani ya Ainul-Assad: Alfajiri ya Jumatano tarehe 8 Januari, 2020 Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (Sepah) lililipiza kisasi cha shambulizi la kigaidi la serikali ya Marekani dhidi ya kamanda wa kikosi cha Quds cha jeshi hilo, Luteni Jenerali Qassem Soleimani na naibu Mkuu wa kikosi cha kujitolea cha wananchi wa Iraq Abu Mahdi al Muhandis kwa kuvurusha makumi ya makombora dhidi ya kambi ya jeshi la Marekani katika mkoa wa al Anbar nchini Iraq. [75]
  • Kuwekwa katika kalenda: Kutangazwa tarehe 13 Dei (3 Janauri) katika kalenda ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuwa, Siku ya Kimataifa ya Muqawama (mapambano).[76]

Usindikizaji na Mazishi

Mkusanyiko wa watu kwenye mazishi ya Qassim Suleiman katika mji wa Kerman

Shughuli ya maombolezo ya kusindikiza na kuaga mwili wa Qassim Suleimani na Abu Mahdi Al-Muhandis na wenzao wengine ilifanyika Januari 4, 2020 kwa kuhudhuriwa na shakhsia wa kisiasa na kidini na umma wa Iraq katika miji ya Baghdad, Karbala na Najaf. [77] Katika mji wa Karbala Sayyid Ahmad al-Swafi mkuu na msimamizi wa haram ya Abul-Fadh al-Abbas aliongozwa Swala ya maiti hawa na huko Najaf, Sheikh Bashir Najafi aliongoza kuiswalia miili ya mashahidi hawa wapendwa. [79] Kisha miili ya mashahidi wa Kiirani na ule wa Abu Mahdi Al-Muhandis ikahamishiwa Iran ambapo tarehe 5 iliagwa na kusindikizwa katika miji ya Ahvaz na Mash'had na tarehe 6 Januari ikaagwa na kusindikizwa na mamlioni ya watu katika miji ya Tehran na Qom.

Tarehe 6 Januari 2020, Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Jamuhuri ya Kiislamuu ya Iran, aliuswalia mwili wa Qassim Suleimani na wenzake, akiwemo Abu Mahdi Al-Muhandis, mjini Tehran. Katika shughuli ya kuuaga na kuusindikiza mwili wa Qassim Suleimani mjini Tehran, Ismail Haniya, Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) alihutubia hadhirina sambamba na kuzungumzia juhudi za Qassim Suleimani za ukombozi wa Palestina alimtaja kamanda Suleimani kuwa ni: "Shahidi wa Quds". [81] Tovuti ya habari ya Kirussia ya Russiya Al-Yaum ilitaja shughuli ya usindikizaji na uagaji mwili wake kuwa, kubwa zaidi katika historia baada ya shughuli ya kuuaga mwili wa Imamu Khomeini. [82] Kulingana na msemaji wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, takriban watu milioni 25 walishiriki katika kusindikiza kwa maombolezo mwili wa shahidi Suleimani. [83]

Wasia

Kwa mujibu wa wasia uliosomwa tarehe 13 Februaria 2020 katika kumbukumbu ya Arubaini ya Qassim Suleimani mjini Tehran na Ismail Qaani, kamanda wa Kikosi cha Quds, [85] shahidi huyo alizingatia na kutaja suala la kumfuata Sayyid Ali Khamenei na kumuunga Waliyul-Faqih (Fakihi Mtawala), kuwazingatia watoto wa mashahidi na kuheshimu vikosi vya jeshi la Iran. Katika sehemu nyingine ya wasia wake huo alitaja umuhimu wa Jamhuri ya Kiislamu na kuitaja kuwa ni Haram na akaonya kwamba iwapo adui ataharibu Haram hii, basi hakuna Haram itakayobakia. [86] Shughuli ya kumbukumbuu ya Arubainii ya Qassim Suleimani ilifanyika katika miji tofauti ya Iran na katika baadhi ya nchi zingine duniani. [87]

Monografia

Kuna athari nyingi zilizochapishwa na kusambazwa kuhusiana na shahidi Qassim Suleimani ambapo baadhi yazo ni:

  • Az Chizi NemitarsidanMaandishi ya italiki (Sikuwa Nikiogopa Kitu); hiki ni kitabu kinachozungumzia maisha ya Qassim Suleimani ambacho amekiandika mwenyewe. [100]
  • Hajj Qassim: Utafiti katika kumbukumbu za Haj Qassim Suleimani." Katika kitabu hiki kuna baadhi ya kumbukumbu na hotuba za Haj Qassim Suleimani katika kipindi cha vita vya Iran na Iraq. [101]
  • Sarbazan Sardar (askari wa Jenerali): Mwandishi wa kitabu hiki ni Murtadha Keramati.
  • Suluk Dar Maktab Soleimani: (Mwenendo/suluki katika fikra za Suleimani), kimeandiikwa na Muhammad Javad Rudgar. Kitabu hiki kinabainisha misingi na mtindo wa irfani ya kijami ya Qassim Suleimani. [104]
  • Aql Sorkh: Mjumuiko wa makala teule za wasomi wa elimu ya kiutu na kijami katika mlango wa shakhsia na mtazamo wa kilimwengu wa Haj Qassim. [105
  • Suleimani Azizi: (Mpendwa Suleimani), kitabu hiki ni ripoti ya maisha na andiko la wasia wa Haj Qassim. [106]
  • Shakhes-haye Maktab Soleimani: (Vigezo vya fikra na njia ya Suleimani); Kitabu hiki kinabainisha sifa maalumu za kiitikadi na kiutamaduni za shakhsia ya shahidi Suleimani. [107]