Mnyama anayekula najisi

Kutoka wikishia

Mnyama anayekula najisi/kinyesi au Jallal ni mnyama ambaye nyama yake ni halali na amezoea kula kinyesi cha mwanadamu. Ni haramu kula nyama, kunywa maziwa na mayai ya mnyama ambaye ana mazoea ya kula najisi. Kinyesi na mkojo wa mnyama huyu ni najisi. Kuna haja ya kumfanyia istibra mnyama (ambaye nyama yake inaliwa) anayekula najisi (kumzuilia na kumshikilia kwa muda mnyama ambaye nyama yake ni halali kuliwa ambaye amezoea kula kinyesi, kwa ajili ya kuifanya nyama na maziwa yake kuwa masafi na kuondokana na najisi) na hivyo hukumu za Jallalah au mnyama anyekula najisi hazitotekelezwa kwake. Muda wa kuwafanyia istibra wanyama unatofautiana; kwa mujibu wa nadharia mashuhuri ya mafakihi, muda wa lazijma kwa ajili ya istibara (kutoharisha) ngamia ni siku 40, ng’ombe siku 20, kondoo siku 10, bata siku 5 na kuku siku 3.

Kwa wanyama ambao muda wao wa kuwashikilia (istibra) haujaainishwa katika hadithi, baadhi wanaamini kuwa, madhali sifa ya kuwa ni mnyama anayekula najisi haijamuondokea basi hukumu yake ni Jallalah licha ya kuwa baadhi wanawatambua ndege wanaofanana na kuku na bata kuwa hukumu yao ni moja katika hili.

Utambuzi wa maana

Mnyama ambaye nyama yake ni halali na amezoea kula kinyesi cha mwanadamu anaitwa mla najisi au Jallalah. [1] Kwa mtazamo wa akthari ya mafakihi ukimtoa Abu Salah Halabi, sifa hii inapatikana kwa kula tu kinyesi cha binadamu na haipatikana kwa mnyama kula najisi zingine. [2] Mafakihi wa zamani (hadi 460 Hijiria) hawakutaja muda unaohitajika ili kutambua sifa hii katika mnyama, [3] lakini vigezo mbalimbali vimeelezwa katika maneno ya wanachuoni wa baadaye kwa ajili hiyo; kula kinyesi cha mwanadamu mchana na usiku mmoja, [4] kukua kwa nyama mpya na kuimarishwa kwa mifupa kwa sababu ya kula najisi, [5] kudhihirika uharibifu na harufu mbaya katika mwili na ngozi ya mnyama, [6] na mnyama kuwa ni mla najisi kwa mujibu wa ada, [7] ni baadhi ya vigezo ambavyo vimetajwa kwa ajili ya kumuita mnyama kuwa ni mla najisi.

Mnyama ambaye nyama yake ni halali kuliwa ameitwa na hukumu za mnyama Jallalah hutekelezwa juu yake pale tu chakula chake kinapokuwa ni mavi na kinyesi cha mwanadamu. [8]

Hukumu za fikihi

Katika vitabu vya fikihi kuna hukumu maalumu zilizobainishwa kuhusiana na wanyama wanaokula najisi:

Hukumu ya kula nyama, nyama na kunywa maziwa yake

Kwa mujibu wa fat’wa za akthari ya mafakihi, ni haramu kula nyama, mnyama ambaye ana mazoea ya kula najisi; mkabala na mtazamo huo kuna baadhi ya mafakihi ambao wamesema hukumu ya hilo ni makuruhu na siyo haramu. [9] Kadhalika ni haramu kula mayai na kunywa maziwa ya mnyama ambaye amezoea kula kinyesi; kwani uhalali au uharamu wa maziwa na mayai ya wanyama unafuata uharamu na uhalali wa nyama zao. [10]

Ikiwa mnyama ambaye nyama yake ni halali kuliwa mbali na kula kinyesi cha mwanadamu akala pia chakula kingine ambacho ni tohara, hata kama chakula chake kingi yaani asilimia kubwa kitakuwa ni kinyesi, si haramu kula nyama yake bali ni makuruhu. [11]

Kuwa najisi mkojo, kinyesi, jasho na mabaki ya maji au chakula

Kwa mujibu wa mafakihi, mkojo na kinyesi cha wanyama wanaokula najisi ni najisi. [12] Hata hivyo, mafakihi wametofautiana kuhusiana na kuwa najisi au tohara jasho la ngamia. Kwa muktadha huo, endapo jasho la ngamia anayekula najisi litagusana na kitu, baadhi ya mafaqihi wameona kuwa ni wajibu kutoharisha. [13] Lakini wengi miongoni mwa mafaqihi wanalichukulia jasho la ngamia anayekula kinyesi kuwa ni safi na tohara. [14] Baadhi ya watafiti licha ya kuwa wanaona jasho la ngamia anayekula najisi ni safi na tohara, lakini wanaamini kwamba mwenye kusali anapaswa kuliondoa mwilini mwake. [15] Baadhi ya waandishi wameunganisha jasho la wanyama wengine ambao wamezoea kula najisi katika kuwa najisi na kuwa tohara, na jasho la ngamia aliyezoea kula najisi na kuziyttambua hukumu zake kuwa ni moja. [16].

Baadhi ya mafaqihi wameichukulia sur (maji yaliyobakia au chakula) ya mnyama aliyezoea kula najisi kuwa ni najisi. [17] Kwahiyo, ni kama ilivyo kwa najisi nyingine ni haramu kula na kunywa sur (chakula au maji yaliyobakia). Mkabala na wao kuna baadhi hawajahukumu kama mabaki ya maji au chakula kilicholiwa na mnyama anayekula najisi kuwa ni najisi bali wameona kuwa ni makuruhu. [19]

Kupanda Ngamia anayekula najisi katika ibada ya Hija na Umra

Imetambuliwa kuwa kupanda ngamia katika msimu wa Hija na Umra ambaye amezoea kula najisi ni makuruhu. [20]

Istibra

Iwapo mnyama anayekula najisi atazuiliwa kula najisi kwa muda fulani na kulishwa majani safi tu, hukumu zote za mnyama najisi zitaondolewa kwake. Katika fiqhi, kitendo hiki kinaitwa Istibra. [21] Hata hivyo, baadhi ya mafakihi hawajatambua kama ni lazima majani anayolisha pia yawe masafi kwa ajili ya kumuondolea mnyama huyo sifa ya mla najisi. [22]

Muda wa istibra

Kwa mujibu wa mtazamo wa akthari ya mafakihi ni kuwa, muda wa lazima kwa ajili ya istibra (kutoharisha) ngamia ni siku 40, ng’ombe siku 20, kondoo siku 10, bata siku 5 na kuku siku 3. [23] Kipindi hiki kimetajwa katika hadithi maarufu na mafakihi wanaona kuwa ni lazima kukizingatia. [24] Katika hadithi ambazo sio mashuhuri, muda wa istibara wa bata umetajwa kuwa ni siku tatu, [25] sita [26] na siku saba. [27] Kwa kondoo muda wake umetajwa kuwa ni siku saba [28] na siku 14, [29] na kwa ajili ya ng’ombe siku 30. Hata hivyo katika hadithi zote imeelezwa kwamba muda wa istibra kwa ngamia ni siku 40 na kuku ni siku tatu tu. [31]

Muda unaohitajika kwa ajili ya istibra kwa baadhi ya wanyama kama vile jogoo, bata mzinga, bata bukini, kware na mbuzi haujatajwa katika hadithi. Baadhi ya mafaqihi wamewachukulia ndege wanaofanana na kuku na bata kuwa sawa katika hukumu yao. [32] Hata hivyo, baadhi ya wengine wanaamini kwamba wanyama wote ambao muda maalumu haujatajwa katika hadithi, wataendelea kutambuliwa kwa sifa hiyo ya kula najisi madhali katika ada na mazoea ya watu hawajatambuliwa kwa sifa nyingine. [33]