Kuzuru Makaburi

Kutoka wikishia

Kuzuru Makaburi (Kiarabu: زيارة القبور) Kunamaanisha kutembelea makaburi na kuwepo makaburini hapo kwa ajili ya ‎kuwaheshimu na kuwaenzi waliozikwa makaburini humo. Wanazuoni wa Kiislamu wakifuata Aya za ‎Qur'ani na Hadithi, wamelihisabu suala la kutembelea makaburi -hasa ya Manabii na watu wema- kuwa ‎ni jambo la kisheria. Kuna faida kadhaa zilizo bainishwa na wanazuoni hao katika amali hiyo ya kuzuru ‎makaburi. Hata hivyo, Mawahabi wanakataza vikali amali ya kutembelea makaburi.‎

Wanazuoni wa Kiislamu -isipokuwa Mawahabi- wote kwa jumla wanakubaliana kuwa ni mustahabu (sunna) kwa ‎wanaume kutembelea makaburi. Ila wanazuoni hao wakhitilafiana kimaoni juu ya hukumu ya ‎wanawake katika kutembelea makaburi hayo. Wanazuoni wengi wa Kiimamiya wamekataa na kusema ‎kuwa; si sunna kwa wanawake kutembelea makaburi, kama ilivyo kwa upande wa wanaume. Pia, ni ‎maarufu kati ya wanazuoni wa upande wa Kisunni kuwa; ni makuruhu kwa wanawake kutenda amali ‎ya kuzuru makaburi.‎

Dhana ya Kuzuru Makaburi na Nafasi Yake

Kuzuru Makaburi kunamaanisha amali ya kutembelea makaburi na kuwepo karibu na makaburi hayo ‎kwa nia ya kujenga heshima na kuwaenzi waliomo makaburoni humo. Katika istilahi za kidini, pia dhana ‎hii inahusishwa na kutembelea makaburi ya Manabii, Maimamu, pamoja na watu wema. Jambo ‎ambalo hufungamana na ibada maalum zenye ishara na malengo kadhaa, kama vile; kujenga heshima, ‎kuomba msaada (kutawasali) na kupata baraka kutoka kwao. [1] Inasemekana kuwa; kuheshimu ‎makaburi ya marehemu waliomo ndani yake, hasa makaburi watu watukufu na wakuu wa jamii, ni ‎miongoni mwa amali zenye historia refu kabisa kwenye jamii za wanadamu, ambapo tangu zamani za ‎kale, yaonekana kuwa duniani kote watu walikuwa na kawaida ya kuwaheshimu na kuwatembelea ‎maiti wao. [2]‎ Kwa mujibu wa maelezo ya Ja’afar Subhani ni kwamba; Katika utamaduni wa Kiislamu, kutembelea ‎kaburi la Mtume (s.a.w.w), Ahlul-Bait wake (a.s), pamoja na makaburi ya waumini mbali mbali, ni moja ‎ya sehemu muhimu za utamaduni wa Kiislamu. [3]

Ziara ya makaburi, iliyofanyika Alhamisi ya mwisho ya mwaka wa Shamsi katika mava moja huko Arak (Machi 28, 2019)[4]

Dhiyauddin Maqdisi, ambaye ni mwanazuoni na ‎mwanahistoria wa upande wa madhehebu ya Hanbali (aliyefariki mwaka 663 Hijria), ameeleza akisema ‎kuwa; Kwa mujibu wa baadhi ya Riwaya, katika nyakati na maeneo yote duniani, Waislamu walikuwa ‎na kawaida ya kutembelea makaburi na kusoma Qur'ani kwa ajili ya marehemu waliomo makaburini ‎humo. Dhiyauddin Maqdisi anasema kuwa; desturi hii ni desturi yenye sifa ya makubaliano ya kipamoja ‎‎(ijmau) na hakuna aliyepinga nyenendo hizo. [5]‎ Kutembelea makaburi na kuwazuru waliomo makaburini humo katika siku za Alhamisi na Ijumaa, ni ‎miongoni mwa mila maarufu katika baadhi ya nchi za Kiislamu kama Iran. Miongoni mwa desturi na ‎amali zifanywazo na baadhi ya watu wakati wa kutembelea makaburi hayo ni; kutia Suratu ya Fatiha ‎pamoja na kusoma Qur'an, kuosha makaburi, kuwasha mishumaa, kuweka maua juu ya makaburi, ‎kugawa sadaka kwa nia ya kumfikishia thawabu marehemu aliyemo kaburini humo. [6]‎

Uhalali na Athari (Faida) za Kutembelea Makaburi

Wanazuoni wa Kiislamu, wakishikamana na Aya za Qur'an pamoja na Hadithi, wamehalalisha amali ya ‎kutembelea makaburi, hasa ya manabii na watu wema, na wamelishisabu jambo hili kuwa ni miongoni ‎mwa mambo kisheria. Pia wanazuoni hao wametaja faida kadhaa kuhusiana na amali ya kuzuru ‎Makaburi. [7] Miongoni mwa athari zilizotajwa kuhusiana na utembeleaji makaburi ni pamoja na; ‎kukumbuka kifo na kutosahau Akhera,[8] kupata ukuruba wa Mwenye Ezi Mungu,[9] pamoja na kuifanya ‎mioyo iwe laini na tiifu. [10] Pia yasemekana kwamba kwa kutembelea makaburi, mtu anaweza ‎kukumbuka ufupi wa maisha, na kumbukumbu hii inaweza kumfanya ashikamane na maadili mema. ‎Zaidi ya hayo, waliozikwa pia nao hupata manufaa kutoka na dua pamoja na maghufira yaombwayo na ‎wageni watembeleao makaburi hayo. [11]‎

Katika moja ya Hadithi kutoka kwa Imamu Swadiq (a.s) imesimuliwa ya kwamba, Imamu Sadiq alisema ‎kuwaambia watu akisema; “Tembeleeni makaburi ya waumini; kwani wao wanapenda kuwa karibu ‎na nanyi, kwani wao hupata khofu pale wanapokuwa mbali nanyi”. [12] Pia katika moja ya Hadithi ‎nyingine, iliyosimuliwa kutoka kwake, ni kwamba Yeye (a.s) aliwaambia watu akisema; “Watembeleeni ‎wafu wenu kwani wao hufurahia ziara zenu, na yeyote anayekwenda kwenye makaburi ya wazazi ‎wake, baada ya kuwaombea, amalizie kwa kuomba haja zake”. [13]‎

Hoja na Ithibati Juu ya Uhalali wa Kutembelea Makaburi

Wanazuoni wa Kiislamu wamehalalisha kuzuru makaburi, hasa kaburi la bwana Mtume (s.a.w.w) ‎pamoja makaburi ya waumini, na wamelihisabu kuwa ni jambo la kisheria, na wakalitolea ushahidi kwa ‎kutumia ithibati zifuatazo:‎

  • Qur'ani: Aya ya 84 ya Surat al-Tawba inazungumzia kuzuia na kumkataka bwana Mtume (s.a.w.w) ‎asimsalie maiti yeyote yule miongoni mwa maiti wa wanafiki, na wala asisimama kando ya makaburi ‎yao kwa ajili ya kuwaombea dua. [14] Wafasiri wa Qur’ani wanasema kuwa; katazo hili ni kwa ajili ya ‎kunaonesha uhalali wa kusimama kando ya kaburi na kusoma dua, na kuihisabu amali hiyo kuwa ni ‎ibada halali; laa si hivyo! Basi Mwenye Ezi Mungu asingekataza kuwafanyia hivyo wanafiki tu, bali ‎alijumuisha makaburi ya kila mfu. [15]‎
  • Sunna za bwana Mtume (s.a.w.w): Kutembelea makaburi kulikuwa halali na ni jambo la kawaida tangu ‎mwanzoni wa Uislamu. Ibn Shabba katika kitabu chake "Tareekh al-Madina al-Munawwara" anaripoti ‎akisema kwamba; Pale bwana Mtume (s.a.w.w) alipokuwa akirudi kutoka kwenye ukombozi wa mji wa ‎Makka na kulekea Madina, alitembelea kaburi la mama yake (bibi Amina) na kusema: "Hili ni kaburi la ‎mama yangu, nilimwomba Mwenye Ezi Mungu ruhusa ya kumtembelea Nay akanirihusu kufanya ‎hivyo." [16] Pia inasemekana kuwa alitembelea makaburi ya mashahidi wa vita vya Uhud [17] pamoja ‎na makaburi ya waumini wengine yalioko ndani ya mava ya Baqi. [18]‎
  • Desturi na nyenendo za Maimamu Maasumina (a.s): Katika vyanzo vya kihistoria, kuna ripoti kadhaa ‎zinazohusiana na Maimamu kutembelea makaburi. [19] Kwa mfano, imeelezwa ya kuwa; Bibi Fatima ‎‎(a.s) alikuwa na kawaida ya kutembelea kaburi la Hamza bin Abdul-muttalib kila Ijumaa, akiswali na ‎kumlilia kaburini kwake. [20] Pia imeripotiwa na Imamu Baqir (a.s) ya kwamba; Ilikuwa ni kawaida ya ‎Imamu Hussein (a.s), kila usiku wa Ijumaa kwenda kutembelea kaburi la Imamu Hassan (a.s). [21] ‎Katika moja ya Hadithi kutoka kwa Imamu Ridha (a.s) imesimuliwa ya kwamba; Imamu Sajjad (a.s) ‎alikuwa na kawaida ya kutembelea kaburi la Imamu Ali (a.s), akasimama kando ya kaburi hilo, akilia na ‎kutoa salamu zake za kiheshima na mapenzi kwa Imamu Ali (a.s). [22] Vilevile, katika vyanzo vya ‎Hadithi za Kishia, kuna Hadithi kadhaa zinazozungumzia faida na mapendekezo ya kutembelea kaburi la ‎bwana Mtume (s.a.w.w), Maimamu wa Kishia (a.s), pamoja na makaburi ya waumini wa kawaida. [23]‎
  • Desturi na matendo ya Masahaba na Tabiina (waliofuatia baada yao): Kuna ripoti kadhaa za Masahaba ‎na Tabiina za kutembelea makaburi katika vyanzo mbali mbali vya kihistoria na Hadithi, ikionesha ‎kwamba; Masahaba na wafuasi wao, hawakulihisabu jambo hili kuwa ni miongoni mambo maovu ‎yaendayo kinyume na sheria za dini. [24]‎
  • Ijmaa (mawafikiano) ya Wanazuoni: Uhalali wa kutembelea kaburi la Mtume (s.a.w.w) na makaburi ya ‎waumini na watu wema ni jambo lenye makubaliano (ijmaa) ya wanazuoni wa Kiislamu. [25] Qadhi ‎‎‘Iyadhu (aliyefariki mnamo mwaka 544 Hijria), ambaye ni mwanazuoni na faqihi wa Madhehebu ya ‎Maliki, amesema katika kitabu chake kiitwacho "Al-Shifa bi Ta'arifi Huquq al-Mustafa" ya kwamba; ni ‎Miongoni mwa nyenendo na desturi za Waislamu zenye faida, ambazo Waislamu wote wamekubaliana ‎nazo, ni amali ya kutembelea kaburi la bwana Mtume (s.a.w.w). [26]‎
  • Desturi na nyenendo za Waislamu: Kutembelea makaburi ya waumini na kuwaombea waliozikwa ‎makaburini humo, ilikuwa ni moja ya desturi za Waislamu tangu zama za bwana Mtume (s.a.w.w). [27] ‎Abu Bakar Kashani, faqihi wa kutoka upande wa Kisunni wa karne ya sita Hijiria, kwa kutilia maanani ‎Hadithi hii ya bwana Mtume (s.a.w.w), isemayo; (‎نَهَيْتُكُمْ عَنْ زِيَارَةِ الْقُبورِ فَزُوروهَا‎ ; Nilikukatazeni ‎kutembelea makaburi, lakini sasa tembeleeni), [28] amesema kwamba; Baada ya bwana Mtume ‎‎(s.a.w.w) kuruhusu kutembelea makaburi, Waislamu walilihisabu jambao hilo kuwa ni halali, na ‎wamekuwa wakifanya hivyo tangu wakati huo hadi leo. [29]‎

Adabu za Kutembelea Makaburi

[30]

Wanazuoni wa Kiislamu, kwa kuzingatia Sunna za bwana Mtume (s.a.w.w) na Maimamu Maasumu ‎‎(a.s), wameorodhesha adabu na matendo kadhaa yanayopendekezwa wakati wa kuzuru makaburi, ‎baadhi ya yake ni kama ifuatavyo:‎

  • Kwenda kutembelea makaburi siku ya Alhamisi, hasa wakati wa jioni. [31]‎
  • Kuweka mkono juu ya kaburi na kuelekea Kibla. [32] ‎
  • Kusoma Suratu al-Qadri mara saba. [33] ‎
  • Kusoma Ayatu al-Kursi na Sura al-Ikhlas mara tatu. [34] ‎
  • Kusoma Suratu al-Fatiha na Sura za al-Mu'awwidhatain (Qul a’udhu birabbi al-Nnasi na qul ‎audhu birabi al Falaq). [35] ‎
  • Kumwaga na kunyunyiza maji juu ya kaburi. [36]‎
  • Kuomba dua na kumwombea rehema na maghufira aliyezikwa kaburini humo. [37]‎

Hukumu ya Kutembelea Makaburi kwa Upande wa Wanawake

Hakuna khitilafu wala tofauti yoyote ile kati ya wanazuoni wa Kiislamu kuhusiana na uhalali na ‎kupendekezwa amali ya kutembelea makaburi kwa upande wa wanaume, ila kwa upande wa ‎wanawake, wanazuoni wamekhitilafiana juu ya kuwepo ruhusa na uhalali wa kisheria unaowaruhusu ‎wanawake kwenda kuzuru makaburi. Maoni ya wanazuoni wa Kiislamu kuhusiana na ruhusa hiyo ni ‎kwama ifuatavyo:‎

  • Msimamo wa madhehebu ya Shia Imamiyyah: Wanazuoni wa madhehebu ya Shia Imamiyyah ‎wamehalalisha na kupendekeza wanawake kwenda kuzuru makaburi. Sahibu Hadha'iq, ambaye ni ‎faqihi na mwanhadithi wa Kishia, amedai kuwepo kwa makubaliano ya wanazuoni kuhusiana na jambo ‎hili. [38] Hata hivyo, Muhaqqiq al-Hilli katika kitabu chake al-Mu'utabar, na Allama al-Hilli katika chake ‎‎Muntaha al-Mataalib wamesema kwamba; jambo hili ni miongoni mwa mambo yanayo chukiza ‎‎(makruhu). [39] Shahid al-Awwal katika kitabu chake Dhikra al-Shia alikubaliana na msimamo wa ‎Muhaqqiq al-Hilli akisema kuwa; Yawezekana kwamba, kule kutoa hukumu ya makruh kwa wanawake ‎kutembelea makaburi, ni kwa sababu ya jambo hili kuweza kuwa na mgongano na amri ya wanawake ‎kujisitiri, ambapo hukuhi itapelekea kuepukana na wanaume wasio maharimu. Hata hivyo, iwapo ‎hakutakuwepo na mgongano baina ya mbambo mawili hayo, basi si halali tu, bali amali hiyo ‎linapendekezwa kwa wanawake kama ilivyo kwa upande wa wanaume. [40] ‎
  • Msimamo wa Ahlu-Sunna: Kulingana na maelezo ya Taqi al-Din al-Subki katika kitabu chake Shifa-u al-‎Siqaami na kitabu «Al-Mawsu'ah al-Fiqhiyyah al-Kuwaitiyyah», ni kwamba; msimamo mashuhuri kati ‎ya wanazuoni wa Ahlu-Sunna, ni makruhu kwa wanawake kuzuru makaburi. [41] Hata hivyo Baadhi yao ‎wanao sema kwamba jambo hilii ni jambao linalopendekezwa kwa wanawake kama ilivyo kwa upande ‎wa wanaume. [42]‎
  • Msimamo wa Mawahabi: Muhammad bin Abdul Wahhab na wafuasi wake wajulikanao kwa jina la ‎Mawahabi, wameharamisha wanawake kuzuru makaburi. Uamuzi huo umeegemea kwenye Hadithi ‎isemayo: (لَعَنَ اللَّهُ زَوَّارَاتِ الْقُبُورِ‎ ; Laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu ya wanawake wanaozuru ‎makaburi). [43] Hii ndiyo Hadithi iliyotegemewa na Mawahabi kwatika kuwaharamishia wanawake ‎amali ya kuzuru makaburi. [44] Baadhi yao wamesema kuwa neno "laana" katika Hadithi linaashiria ‎kuwa ni haramu na hata wakasema kuwa; ni dhambi kubwa kwa wanawake kuzuru makaburi. [45] Hata ‎hivyo, msimamo huu umekosolewa na wanazuoni wa Kiislamu. Wengine kama vile Tirmidhi na Hakim ‎al-Nishaburi, kutoka kwa wanahadithi wa Ahlu-Sunna, wamesema kuwa; Hadithi hii ilihusiana na wakati ‎ambapo bwana Mtume (s.a.w.w) alikuwa amekataza kuzuru makaburi; ila baadae hukumu hii ilifutwa ‎wanawake nao wakaruhusiwa kuzuru makaburi. [46] Pia kuna wengine waliosema kuwa; Hadithi hii ‎inahusiana na hali ambapo kutembelea makaburi kutasababisha kutendeka kwa dhambi au jambo ‎fulani la haramu. [47] Wengine kama vile Qurtubi (aliyefariki mnamo mwaka 671 Hijria), ambaye ni ‎faqihi na mfasiri wa upande wa madhehebu ya Maliki, wamesema kuwa neno‎ زَوَّارَات‎ «Zawwaaraat» ‎lililoko katika Hadithi hiyo, wingi wa utendaji wa wa amili hiyo kwa mfumo wa kufurutu ada, na ‎linawahusu wanawake wanaotembelea makaburi mara kwa mara, kwa hiyo laana iliyo tangazwa katika ‎Hadithi hiyo, haimhusu kila mwanamke. [48] Kulingana na fatwa iliyotolewa na Dar al-Iftaa' ya Misri «‎دار الإفتاء مصر‎», ni kwamba; kutembelea makaburi ni jambo linalopendekezwa kwa watu wote, wake ‎kwa wanaume, na hukumu ya Hadithi iliyo tajwa katika mjadala huu, inahusiana na hali ambapo kuzuru ‎makaburi huko kutapelekea kuhuisha vilio, huzuni na maombolezo makaburini humo. [49]‎

Upinzani wa Ibn Taimiyyah na Mawahabi Dhidi ya Amali ya Kuzuru Makaburi

Ibn Taymiyyah na Mawahabi, kwa kutumia Hadithi ya Shaddu al-Rihal ‎(شَدُّ الرِحال), wameharamisha ‎safari ya kusafiri kwa ajili ya kuzuru makaburi, hata kama litakuwa ni kaburi la bwana Mtume (s.a.w.w), ‎na wakalihisabu jambo hilo kuwa ni la bid'a na la kishirikina. [50] Kwa mujibu wa mtazamo wao, ‎kulingana na Hadithi hii, ni halali tu kusafiri kwa ajili ya kutembelea misikiti mitatu mitakatifu, nayo ni; ‎Masjid al-Haram, Masjid al-Aqsa, na Masjid al-Nabawi. [51]‎

Wanazuoni wa Kiislamu wamekosoa vikali msimamo huu. Wanazuoni wengi wa Ahlu-Sunna kama vile ‎Nawawi,[52] Ibn Hajar al-Asqalani,[53] Ghazali,[54] Mulla Ali Qari Hanafi,[55] Shamsu al-Din al-Dhahabi,[56] Jassas,[57] Ibn ‎Abidina faqihi wa Kihanafi,[58] Zaraqani faqihi wa Kimaliki,[59] Ibn Qudamah faqihi wa Kihanbali[60] na wengi ‎wengineo, wanaamini kuwa; Hadithi ya Shaddu al-Rihal iliyo rejelewa na Ibn Taymiyyah kwa ajili ya ‎kupinga amali ya kuzuru makaburi, hasa kaburi la bwana Mtume (s.a.w.w), haikuja kwa ajili ya kuzuia ‎na kuharamisha ziara hizo,[61] bali ni kwa ajili ya inabainisha ubora wa misikiti hiyo mitatu mitukufu. ‎

Masuala Yanayo Husiana

Rejea

Vyanzo