Nafs al-Mutma'inna

Kutoka wikishia

Al-Nafs al-Mutma'inna au Nafsi iliyotulia (Kiarabu: النفس المطمئنة) inaashiria hali ya nafsi ya mwanadamu ambayo imefikia utulivu na yakini na haina muelekeo wa kutenda dhambi. Neno hili limekuja katika Aya ya 27 ya Surat al-Fajr.

Al-Nafs al-Mutmai'nna mkabala wake ni al-Nafs al-Ammara (yenye kuamrisha maovu) na Al-Nafs Al-Lawwamah, (yenye kujilaumu). Nafsi ya juu au yenye daraja la juu kabisa, ni nafsi iliyotua (al-Nafs al-Mut’mainnah) ambapo kwa kuwa na hali hiyo ya kinafsi mwanadamu anakuwa katika hali ya utulivu na yakini. Katika Nafs a-Ammara yenye kuamrisha maovu, mwanadamu huvutwa upande wa dhambi. Katika nafsi yenye kujilaumu (nafs lawwama), nafsi hii inamfanya mwanadamu ajilaumu mwenyewe kutokana na makosa na dhambi zake alizofanya.

Maulamaa wa dini tukufu ya Kiislamu wanasema kwamba, mwanadamu ana nafsi (ambayo ni yeye mwenyewe yaani mmoja) na mtu kuwa na nafsi moja haipingani na suala la uwepo wa nafs Ammara, nafs lawwama wala nafs Mutma’inna ambazo zina maana ya nafsi yenye kuamrisha maovu, nafsi yenye kujilaumu kutokana na makosa yake na nafsi yenye utulivu na yakini. Wanazuoni wa Kiislamu wanaamini kwamba, istilahi hizi (za aina za nafsi) ni hali, hatua na daraja mbali mbali ambazo zinaonyesha nafsi na kuitambulisha hali zake.

Katika baadhi ya hadithi sambamba na kubainishwa Aya ya al-Nafs al-Mutmai'nna, kumetajwa mifano na vielelezo vya nafsi hii yenye utulivu na iliyotua. Imam Ali (a.s), Imam Hussein (a.s) na mtu ambaye ana imani na Mtume (s.a.w.w) na Ahlul-Bayt wake, ni miongoni mwa vielelezo hivyo.

Utambuzi wa maana

Al-Nafs al-Mutmainna (nafsi iliyotua) ni hali ya nafsi au ada ya mtu ambayo ndani yake kutokana na kudumu katika kufuata akili katika kujitenga mbali na dhambi, kitendo hiki huwa ni uwezo na ada ya mwanadamu na katika mazingira haya hupatikana hali ya utulivu na uhakika. [1] Istilahi hii ni ya Kiqur’ani na imechukuliwa kutoka katika Aya ya 27 ya Surat al-Fajr.

Al-Nafs al-Mutmainna ni mkabala wa nafsi Ammara (nafsi yenye kuamrisha maovu) na al-Nafs Lawwamah na inahesabiwa na kutambulika kuwa, ni daraja ya juu kabisa ya nafsi. Wanazuoni wanasema kuwa, nafsi ina daraja kadhaa: Daraja ya chini zaidi ni al-Nafs al-Ammara ambayo ndani yake mwanadamu hafuati wala kutumia akili (kwa njia sahihi), bali anakuwa ni mwenye kufuata na kuiendea dhambi na ufisadi katika maamuzi na matendo yake. Yaani ni mwenye kuifuata tu nafsi yake kwa kila inachoamrisha na kutaka. Daraja ya juu kabisa.

Nafsi ya juu zaidi ya hiyo ni nafs lawwamah kwa maana ya nafsi yenye kujialaumu, ambapo katika hali hii mwanadamu ni mwenye kujilaumu kutokana mambo na matendo mabaya ambayo ameyafanya. Ama nafsi ya juu zaidi ya nafsul ammara ni nafs Mut’mainna. Katika hatua na daraja hii ya nafsi, ni kwamba kutokana na mtu kufuata maamuzi ya akili sahihi kwa muda mrefu na kwa daima, hivyo kitendo hiki huwa na athari na mazoea chanya katika nafsi yake na kuipelekea nafsi kufikia hatua na daraja ya utulivu na yakini. [2] Allama Tabatabai ameielezea al-Nafs al-Mutma’inna katika kitabu chake cha tafsir al-Mizan kwamba, ni ile ambayo inapata utulivu katika kumtaja na kumdhukuru Mwenyezi Mungu na ambayo ni yenye kumridhia Allah katika hali yoyote na inajitambua kwamba, si yenye kumiliki kheri, shari, maslahi na madhara yoyote yale na itambua kwamba, dunia ni mapito na kila fakiri na mwenye kuhitaji ni katika mitihani ya Mwenyezi Mungu; na ni kutokana na sababu hiyo ndio maana daima ipo katika mpaka wa uja na neema za dunia kwa nafsi hiyo, haziivuti katika ufisadi na uistikbari, kama ambavyo umasikini na kutokuwa nacho, nayo hayaivuti upande wa kukufuru na kuacha kushukuru. [3]

Katika kitabu chake cha Risaleh Sayr wasuluk, Allama Bahr al-Ulum ameitaja Nafsi iliyotua (al-Nafs al-Mutma’inna) kwamba, ni hatua ya kuingia katika hijra na kuhama kukubwa ambapo ni hijra na kuhama kutoka katika uwepo wake na kukataa (kuacha na kujikomboa) na kusafiri kuelekea katika ulimwengu wa uwepo mutlaki na uzingatiaji kikamilifu. Na ameitambua Aya ya “Ewe nafsi iliyo tulia!” kwamba, mhutubiwa na mlengwa ni nafsi ambayo imemaliza jihadi kubwa na imeingia katika hatua ya ulimwengu wa ushindi ambao ni makao ya utulivu na nafsi yake imejisalimisha kwa haki. Ama sehemu ya Aya inayosema: “Rejea kwa Mola wako Mlezi”, ni hijra na kuhama kutoka katika uwepo wake na kuelekea katika uwepo wa haki ambayo ni Mwenyezi Mungu na baada ya kugura na kuhajiri huku, nafsi hii huwa ni yenye kuridhia kuhusiana na maamuzi na kadari ya kisheria na ya kimaumbile ya Mwenyezi Mungu na hakuna tukio la kinyume na hakuna maasi yoyote ambayo yatafanywa nayo. [4]


Kutokuweko mgongano

Maulamaa wa dini tukufu ya Kiislamu wanasema kwamba, mwanadamu ana nafsi moja (ambayo ni yeye mwenyewe yaani mmoja) na mtu kuwa na nafsi moja haipingani na suala la uwepo wa nafs Ammara, nafs lawwama wala nafs Mutma’inna ambazo zina maana ya nafsi yenye kuamrisha maovu, nafsi yenye kujilaumu kutokana na makosa yake na nafsi yenye utulivu na yakini. Wanazuoni wa Kiislamu wanaamini kwamba, istilahi hizi (za aina za nafsi) ni hali, hatua na daraja mbali mbali ambazo zinaonyesha nafsi na kuitambulisha hali zake; [6] kwa maana kwamba, wakati nafsi inapofanya matendo maovu na mabaya, tunaiita kuwa ni nafsi Ammara (yenye kuamrisha maovu), na inapotokea kwamba, imefanya kosa na kisha ikajilaumu, basi hiyo tunaiita kuwa ni nafs lawwamah (nafsi yenye kujilaumu). [7]

Vielelezo katika hadithi vya al-Nafs al-Mutma’inna

Katika hadithi kuna mifano na vielelezo vilivyobainishwa kuhusiana na “al-Nafs al-Mutma’inna” ambayo imekuja katika Aya ya 27 ya Surat al-Fajr Sheikh Kulayini amenukuu hadithi katika kitabu chake cha al-Kafi ambayo inaitambua nafsi iliyotua kuwa ni nafsi ambayo ina imani na Mtume na watu wa nyumbani kwake (Ahlul-Bayt). [8] Kwa mujibu wa hadithi iliyokuja katika kitabu cha Shawahid al-Tanzil, Imam Ali (a.s), [9] na kwa mujibu wa hadithi nyingine kutoka katika kitabu cha tafsir Qumi, Imam Hussein (as) ni kielelezo cha hilo. [10] Kwa mujibu wa Hussein Ali Muntaziri, dalili na hoja ya tafsiri hii ni kwamba, Imam Hussein (as) kwa kusimamam kwake kidete katika njia ya Mwenyezi Mungu ameonyesha kuwa, ana nafsi iliyotua na anastahiki maneno hayo ya Mwenyezi Mungu. [11]

Al-Nafs al-Mutma’inna katika akhlaq

Baadhi ya wasomi wanaamini kuwa, utulivu wa mwanadamu katika hatua ya al-Nafs al-Mut’mainna unahusiana na masuala ya kiakhlaq (kimaadili0). Sayyid Muhammad Hussein Tabatabai analitambua suala la utulivu wa nafsi kwamba, unatokana na hilo katika tafsiri yake ya Aya ya 28 ya Surat al-Raad ambayo inamhesabu Mwenyezi Mungu kuwa ni mmiliki wa kila kitu; na natija na matokeo yake ni kwamba, kupata neema za Mwenyezi Mungu hakumfanyi azidi ujeuri na kuasi kama ambavyo kutokuwa na kitu hakumfanyi akufuru na kuacha kushukuru. [12]

Vyanzo

  • Ḥaskānī, ʿUbayd Allāh b. ʿAbd Allāh al-.Shawāhid al-tanzīl li-qawāʿid al-tafḍīl. 1st Edition. Edited by Muḥammad Bāqir Maḥmūdī. Tehran: Majmaʿ Iḥyāʾ Farhang-i Islāmi affiliated to Wizārat-i Farhang wa Irshād-i Islāmī, 1411 AH.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī & Muḥammad Ākhūndī. 4th Edition. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1407 AH.
  • Majlisī, Muḥammad Bāqir al-. Biḥār al-anwār al-jāmiʿa li-durar akhbār al-aʾimmat al-aṭhār. 3rd edition. Beirut: Dār Iḥyāʾ al-Turāth al-ʿArabī, 1403 AH.
  • Misbāḥ Yazdī, Muḥammad Taqī. Āʾyīn-i parwāz. Edited by Javād Muhaddithī. 9th Edition. Qom: Intishārāt-i Muʾassisa-yi Āmūzishī wa Pazhūhishī-yi Imām Khomeiniī, 1399 Sh.
  • Misbāḥ Yazdī, Muḥammad Taqī. Akhlāq wa ʿirfān Islāmī. Maʿrifat Journal. No 127, 1387 Sh.
  • Muṭahharī, Murtaḍā. Majmūʿa-yi āthār. Tehran: Intishārāt-i Ṣadrā, 1389 Sh.
  • Qummī, ʿAlī b. Ibrāhīm al-. Tafsīr al-Qummī. Edited by Ṭayyib Mūsawī Jazāʾrī. 4th Edition. Qom: Dār al-Kitāb, 1404 AH.
  • Ṭabāṭabāʾī, Sayyid Muḥammad Ḥusayn al-. Al-Mīzān fī tafsīr al-Qurʾān. 5th Edition. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī, 1417 AH.