Msikiti Mkuu wa Basra

Kutoka wikishia

Msikiti wa Jamia wa Basra (Msikiti Mkuu wa Basra) ndio msikiti mkongwe zaidi uliojengwa nchini Iraq, ulioko katika mji wa Basra. Msikiti huu pia unajulikana kama "Masjid Khut’wah Imam Ali (AS)" (Nyayo za Imam Ali) kutokana na kuwepo kwa Imamu wa kwanza wa Shia ndani yake. Baada ya kumalizika kwa vita vya Jamal, Imam Ali (a.s.) alikwenda katika msikiti huo na kutoa khutba kwa watu. Katika kipindi cha miaka yote hii, Msikiti Mkuu wa Basra umeboreshwa na kukarabatiwa.

Hakuna kilichosalia katika msikiti wa zamani isipokuwa mnara, na msikiti mpya wenye usanifu wa kisasa umejengwa karibu nao ukiwa na usanifu majengo wa kisasa. Tangu mwanzo kabisa, Msikiti wa Basra ulikuwa mahali pa duru za elimu na uwepo wa shule za fikra. Watu wengi wa Iraq huenda mahali hapa kwa miguu kwenye hafla za kidini.

Utambulisho jumla na umuhimu wake

Msikiti wa Jamia wa Basra ni mojawapo ya sehemu maarufu za ibada katika Uislamu [1] na ni msikiti mkuu wa kwanza kujengwa Iraq na msikiti wa tatu katika Uislamu. [2] Kile ambacho kumeufanya Msikiti Mkuu wa Basra kuwa na umuhimu katiika kipindi chote cha historia, ni utendaji tofauti wa kisiasa, kimahakama, kimafunzo, kimalezi na kijamii. [3] Chuo Kikuu cha Basra kinatajwa kuwa shule ya kwanza ya fiqhi, hadithi, usuli na falsafa, ambayo ilikuwa mahali pa majadiliano na mijadala ya kinahau, kifasihi, kiteolojia na kidini kati ya shakhsia za kisayansi katika zama tofauti. [4] Kutokana na mapana ya msikiti huu katika uandaaji wa darsa za masomo na kuwepo kwa shule za kifikra, Basra ilipewa jina la "Hazina ya Uislamu". [5]

Inaelezwa kwamba Msikiti wa Basra ulikuwa kituo na kambi ya Mashia, na harakati zote za Mashia dhidi ya Bani Umayya zilianzia kwenye msikiti huu, na wakaufanya kuwa kituo cha kupigania na kudai haki za Ahlul-Bayt (a.s). Kutubu na kutangaza Abul Hassan al-Ash’ari kutoka katika kundi la Mu’atazilah [7] na mjadala wa Hisham Ibn al-Hakam na Amr bin Ubayd, mwanateolojia wa Kisunni [8] ni miongoni mwa matukio mengine yaliyotokea katika msikiti huu.

Kwa mujibu wa baadhi ya mafaqihi wa Kishia, itikafu inasihi tu katika Masjid al-Haram, Masjid al-Nabi, Msikiti wa Jamia wa Kufa na Msikiti wa Jamia wa Basra na hakuna tatizo kufanya itikafu katika misikiti mingine, kwa nia ya rajaa (kutarajia kukubaliwa). [9] Kwa mujibu wa Sheikh Swaduq ni kuwa, sababu ya kujuzu kufanya itikafu katika misikiti hii minne ni hii kwamba, katika misikiti hiyo minne ni awe ameswalisha humo Sala ya Ijumaa Imamu muadilifu, na Ali (a.s.) aliswalisha Swala ya Ijumaa katika Msikiti wa Basra. [10]

Kuweko Imamu Ali (a.s) katika msikiti wa Basra

Kwa mujibu wa ripoti za kihistoria, baada ya kumalizika kwa Vita vya Jamal (ngamia), Imam Ali (a.s.) aliingia katika Msikiti wa Jamia wa Basra na kutoa khutba kwa watu wa Basra akiwa amekaa juu ya mimbari. [11] Imekuja katika Dairat al-Maarif (Ensaiklopidia) ya Ushia kwamba, baada ya Imamu Ali (a.s) kutoa hotuba kali dhidi ya watu wa Basra, haikupita muda mrefu mji huo ukageuka na kuwa moja ya vituo muhimu vya Mashia. [12] Kutoka na Imamu Ali kuweko katika eneo hilo, msikiti huo umeondokea kuwa mashuhuri pia kwa jina la “Masjid Khut’wah Imam Ali (a.s) au “Masjid Imam Ali (a.s). [14] Imeelezwa katika kitabu Al-Isharat ilaa Marifat al-Ziyarat kwamba, mnara na mihrabu ya msikiti vilijengwa na Imam Ali (a.s.).[15]

Khutba ya Imamu Ali (a.s) kwa watu wa Barsa katika Msikiti wa Jamia

Enyi watu wa Basra! Enyi Mliokuwa askari wa mwanamke (Aisha), na wafuasi wa mnyama (ngamia)! amepiga kelele mkamwitika, na akajeruhiwa mkakimbia. Tabia zenu ni mbaya na ahadi zenu ni khiyana na dini yenu ni unafiki, maji yenu ya chumvi. Mwenye kuishi kati yenu yuko rehani kwa dhambi zake, mwenye kuondoka kwenu atapata amani ya rehema kutoka kwa Mola wake Mlezi. Kama nauona msikiti wenu wafanana na sehemu ya mbele ya Safina (boti), Mungu ameipeleka adhabu kutoka juu na kutoka chini yake, na waliomo humo wamezama “Wallahi mji wenu utazama, kana kwamba nauona msikiti wenu ukiwa kama sehemu ya mbele ya boti au mbuni aliyeanguka kwa kifua chake.” Hivi sasa rejeeni majumbani mwenu.

Historia ya ujenzi na ukarabati

Msikiti Mkuu wa Basra ulijengwa kwa hatua kadhaa na kufanyiwa mabadiliko ya muundo wake. [16] Msikiti huu ulijengwa kwa mara ya kwanza sambamba na kuanzishwa mji wa Basra mwaka wa 14 Hijiria wakati wa Ukhalifa wa Omar bin Khattab. Aliyeujenga alikuwa Utbah bin Ghazwan, gavana wa Basra. Awali ulijengwa kwa mianzi na mashina ya mimea. Ni kwa sababu hiyo ndio maana baadaye uliharibiwa na kuteketea kwa moto na katika zama za Muawiya, mtawala wa Basra yaani Ziyad bin Abih, aliujenga na kuuimarisha msikiti huo kwa matofali, plasta na nguzo za mawe. [17] Katika zama za utawala wa Ubaidullah bin Ziyad pia ulijengwa tena na kupanuliwa. [18] Baada ya hapo, upanuzi mkubwa zaidi wa msikiti huo ulifanyika mwaka wa 160 Hijria wakati wa utawala wa Mahdi Abbasi, na Harun Abbasi aliongeza Dar al-Amara kwenye ua wa msikiti huo. [19] Inasemekana kwamba katika kipindi hiki, karibu watu elfu ishirini walikuwa wakiswali msikitini hapo. [20]

Jengo jipya

Kwa sasa msikiti wa zamani wa Basra umeteketea [21], na mnara mmoja tu umesalia. [22] Mnamo 2000, ujenzi wa msikiti mpya ulikamilika nje ya msikiti wa zamani. Ukubwa wa jengo lake ni mita 200 na ua mkubwa. [24] Hata hivyo, inaelezwa kwamba, jengo jipya halilingani na nafasi na umuhimu wa msikiti, na mtindo wake wa usanifu hauendani na historia ya msikiti huo. [25] Kadhalika imeelezwa kwamba, Mashia wa Iraq katika minasaba mbalimbali kama kumbukizi za Siku ya Ashura, maombolezo ya kifo cha Mtume (s.a.w.w), kumbukumbu ya kuawa shahidi Imamu Ali (a.s.) na kuzaliwa kwa Imam Mahdi (a.s.) huenda kwenye msikiti huo kwa kutembea kwa miguu kutoka Basra na miji mingine. [26]