Khana al-Amin

Kutoka wikishia

Khana al-Amin (Kiarabu: خان الأمين) ambayo maana yake ni mwaminifu amefanya khiyana. Hii ni itikadi ya baadhi ya Maulamaa wa Ahlu-Sunna wanayoinasibisha kwa Waislamu wa madhehebu ya Shia. Kwa mujibu wa madai yao ni kwamba, Waislamu wa Kishia wanaamini kwamba, malaika wa wahyi Jibril (a.s) alisaliti na kufanya khiyana ambapo badala ya kumpelekea Wahyi Imamu Ali (a.s) akampelekea Mtume Muhammad (s.a.w.w). Na ni kutokana na sababu hiyo ndio maana Mashia mwishoni mwa Sala zao wanakariri neno Khana al-Amin (amefanya khiayana Amin wa Wahyi).

Hii ni katika hali ambayo kwa mujibu wa imani na itikadi ya Mashia ni kuwa, wao siyo tu kwamba, hawamtambui Imamu Ali kuwa ni Mtume bali wanaamini kuwa, Malaika Jibril ni Maasumu na hakosei. Kadhalika Mashia mwishoni mwa Sala wanatoa takbira tatu (Allah Akbar) na sio kweli kwamba, wanasema Khana al-Amin mwishoni mwa Sala. Huu ni katika uzushi na tuhuma zisizo na msingi dhidi ya Mashia.

Kwa mujibu wa Maulamaa wa Kishia madai haya ni tuhuma na uzushi dhidi ya Mashia na lengo lake ni kutaka kuyafananisha madhehebu ya Kishia na dini ya Uyahudi; kwani, kuna kundi miongoni mwa Mayahudi ambalo linaamini kwamba, malaika Jibril alipewa jukumu na Mwenyezi Mungu la kumfikishia Utume mtu fulani miongoni mwa kaumu ya Mayahudi lakiini yeye akamfikishia mtu mwingine.

Kunasibishwa kwa Itikadi ya "Khana al-Amin" na Mashia

Khana al-Amin ambayo maana yake mwaminifu (malaika Jibril) amefanya khiyana ni itikadi ya baadhi ya Maulamaa wa Ahlu-Sunna [1] na Mawahabi [2] ambayo wanainasibisha kwa Waislamu wa madhehebu ya Shia; hata hivyo baadhi yao wameinasibisha itikadi hii kwa kundi la maghulati wa Kishia. [3] Kwa mujibu wa madai yao ni kuwa, Waislamu wa Kishia wanaamini kwamba, Malaika wa Wahyi Jibri (a.s) alisaliti na kufanya khiyana ambapo badala ya kumpelekea Wahyi Imamu Ali (a.s) akampelekea Muhammad (s.a.w.w). [4]

Kwa mujibu wa Abdallah bin Jibrayn (aliaga dunia 1430 Hijiria) Mufti wa Mawahabi amenukuliwa katika maelezo yake akisema, baadhi ya Mashia kabla ya kutoa salamu ya Sala (salamu ya kukamilisha Sala) hupiga mikono yao katika mapaja yao na kukariri maneno haya: "Khana al-Amin". [5] Hata hivyo ukweli halisi wa mambo ni kuwa, Mashia hawasemi maneno hayo katika Sala; bali wanachokifanya baada ya salamu ya Sala ni kunyanyua mikono yao na kupiga takbira kila wanaponyanyua mikono yao hiyo na hufanya hiivyo mara tatu; [6] hii ni kutokana na kuwa, kwa mujibu wa fat'wa za mafakihi wa Kishia, ni mustahabu kutamka takbira mara tatu baada ya kutoa salamu ya kukamilisha Sala. [7]

Kutegemea Shairi la Ibn Hammad

Baadhi ya Maulamaa wa Ahlu-Sunna wanatumia beti za mashairi zinazonasibishwa kwa Ali bin Hammad Basri, mshairi wa Kishia wa karne ya 4 Hijiria kama hoja ya kuthibitisha madai yao kwamba, kundi miongoni mwa Mashia wanaamini kwamba, Jibril alifanya khiyana. Beti hizo za mashairi zinasema:

ضَلَّ الأمینُ و صَدَّها عَنْ حَیدر - تَاللّهِ ما کانَ الأمینُ أمینا


Amin (Jibril) amepotea na kalizuia hilo kwa Haidar - Wallahi! Jibril al-Amin hakuwa mwaminifu.[9]


Kadhi Nurullah Shushtari na Abu Ali Hairi, ambao ni miongoni mwa Maulamaa wa Kishia wanasema: Neno “Amin” katika shairi hilo ni kinaya ya Abu Ubaydah Jarrah ambaye Masuni wanamtambua kama amin (mwaminifu) wa umma na ambaye alifanya juhudi za kuhakikisha Abu Bakr bin Abi Quhaf anatwaa Ukhalifa na kuupokonya kutoka kwa Imamu Ali (a.s). [10] Katika hadithi iliyonukuliwa katika Sahihi Bukhari, moja ya vitabu sita vya hadithi (Sihah Sittah) vyenye itibari kwa Waislamu wa Kisuni, Abu Ubaydah Jarrah anatambuliswhwa kuwa ni amin (mwaminifu) wa umma wa Kiislamu. [11]

Msukumo

Kwa mujibu wa Jafar Sobhani, suala la Jibril kufanya khiyana hiyo ni itikadi ya Mayahudi; lakini maadui wa umoja wa Kiislamu walilihusisha jambo hilo na Mashia. [12] Fakhr Razi, mfasiri wa Kisunni (aliyefariki 606 Hijiria), amenukuu chini ya Aya ya 97 ya Surat Al-Baqarah kwamba: Mayahudi walikuwa na uadui na Jibril na walikuwa wakiamini kwamba, Jibril alipewa jukumu la kupeleka Utume kwa mmoja wa watu wa kaumu ya Mayahudu, lakini yeye akamkabidhi Utume mtu ambaye yuko nje ya kaumu hiyo. [13]

Ibn Abd Rabbih (aliyefariki 328 Hijiria), mwanachuoni wa madhehebu ya Kisuni, katika kitabu chake Iqd al-Farid, baada ya kutaja imani ya Mayahudi juu ya uadui wao kwa Jibril, anasema kwamba, marafidha pia wana imani hiyo; kwa mtazamo wao ni kwamba, Jibril alifanya makosa katika kufikisha Wahyi kwa Muhammad (s.a.w.w) na alipaswa kufikisha Wahyi huo kwa Ali (a.s). [14] Ibn al-Jawzi (aliyefariki 597 Hijiria), mmoja wa mafakihi wa madhehebu ya Hambali, [15] na Ibn Taymiyyah Harrani (aliyefariki 728 Hijiria), mwananadharia wa Kisalafi, [16] pia wamerudia jambo hili wakati wa kueleza hali ya mshabaha na mfanano uliopo kati ya Ushia na Uyahudi.

Kupingana na Itikadi ya Ushia

Wanachuoni wa Kishia wametambua suala la kuhusisha na Mashia imani na itikadi ya kwamba, Jibril alifanya khiyana ni tuhuma na uzushi mtupu. [17] Kwa mujibu wa wanazuoni wa Kishia ni kwamba, hakuna Shia yeyote anayeamini usaliti wa Jibril na wala hawasemi neno Khana Al-Amin. [6] Kuamini kwamba, Jibril alifanya khiyana ni imani ambayo inapingana na itikadi zingine za Mashia, ambazo ni kama ifuatavyo:

  • Umaasumu wa Malaika: Kuamini kwamba, Jibril alifanya khiayana ni jambo linalopingana na Umaasumu wake. [18] Kwani Wanazuoni na Maulamaa wa Kishia wanaamini kwamba, viumbe Malaika akiwemo Jibril ni Maasumu na hawatendi dhambi na hawaasi na kukiuka kila ambacho wanaamrishwa na Mwenyezi Mungu. [19] Kadhalika kwa mujibu wa Allama Tabatabai, mfasiri wa Qur’an wa Kishia ni kwamba, Jibril hawezi kufanya mabadiliko ya Wahyi kwa makusudi au hata kwa kusahau. [20]
  • Imamu Ali (a.s) siyo Mtume: Maulamaa wa Kishia wanaamini kwamba, Imamu Ali ni Imamu, khalifa na kiongozi wa Waislamu baada ya Mtume Muhammad (s.a.w.w), na kwa hakika yeye sio Mtume. [21] Suala la Imamu Ali kutokuwa Mtume limethibiti katika hadithi ya Manzila ambayo imetumiwa kuthibitisha Uimamu wa Imamu Ali (as), [22] na hilo limebainishwa wazi. [23]
Abdallah Jawadi Amoli, alimu na mfasiri wa Qur’an Tukufu wa Kishia anasema, hakukuwa na hakutakuweko mtu ambaye ni mkamilifu kuliko Mtume (s.a.w.w); kwani kama angekuweko, basi Muhammad asingekuwa Mtume wa mwisho. [24]

Rejea

Vyanzo

  • Ibn Taymīyya, Aḥmad b. ʿAbd al-Ḥalīm. Minhāj al-sunna al-nabawīyya fī naqd kalām al-shīʿa al-qadarīyya. Edited by Muḥammad Rashād Sālim. Riyadh: Jāmiʿat al-Imām Muḥammad b. Saʿūd al-Islāmīyya, 1406 AH/1986.
  • Ibn Jibrīn, ʿAbd Allāh b. ʿAbd al-Raḥmān. Sharḥ al-ʿaqīda al-ṭaḥāwīyya.
  • Ibn Jawzī, ʿAbd al-Raḥmān b. ʿAlī.