Aya ya al-Ta’assi

Kutoka wikishia

Aya ya Us-wa (Ruwaza/Kigezo) (Kiarabu: آية التأسي ) Ni Aya ya 21 ya surat al-Ahzab inayomtambulisha Mtume (s.a.w.w) kuwa ni kiigizo na ruwaza njema na inawataka Waislamu wamfuate mbora huyu wa viumbe na kujiepusha na kumpinga.

Aya hii ilishuka miongoni mwa Aya za vita vya Ahzab. Kwa mujibu wa mtazamo wa baadhi ya wafasiri, kuwa kigezo na ruwaza njema Mtume sio makhsusi na maalumu kwa vita hivi tu, bali inajumuisha wakati, zama, na vitendo vyote, maneno na Sunna za Mtume (s.a.w.w). Hili ni jukumu la daima na lililo thabiti milele kwa ajili ya Waislamu wote; hata hivyo watu ambao wanaweza kustafidi na kiigizo na ruwaza njema hii ni wale ambao wana imani na rehma za Mwenyezi Mungu na Siku ya Kiyama na katu si wenye kughafilika hata kidogo na dhikri na utajo wa Mwenyezi Mungu. Baadhi ya wafasiri wamelitambua suala la kumfanya Mtume kuwa ruwaza njema kwamba ni jambo la wajibu huku wengine wakisema ni mustahabu; kama ambavyo kuna baadhi yao wametenganisha na kueleza kwamba, ni wajibu kumfanya Mtume ruwaza njema katika masuala ya dini na ni mustahabu katika mambo ya kidunia.


Andiko na tarjumi ya Aya

لَقَدْ کانَ لَکمْ فی رَسُولِ اللَّهِ أُسْوَةٌ حَسَنَةٌ لِمَنْ کانَ یرْجُوا اللَّهَ وَ الْیوْمَ الْآخِرَ وَ ذَکرَ اللَّهَ کثیراً

Hakika nyinyi mnayo ruwaza njema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa anaye mtaraji Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, na akamkumbuka Mwenyezi Mungu kwa wingi.
(Quran: 33: 21)

Utambulisho

Aya ya 21 ya Surat al-Ahzab imepewa jina la Aya ya al-Ta’assi (Aya ya ruwaza). [2] Baada ya Mwenyezi Mungu kuwalaumu wanafiki katika Aya za kabla, [3] na kabla ya kutaja baadhi ya sifa maalumu za waumini wakweli, katika Aya hii Allah anamtambulisha Mtume (s.a.w.w) kama kiongozi, kiigizo na ruwaza njema kwa ajili ya waumini na anawataka Waislamu au mukallafina (wakalifishwao na sheria za Mwenyezi Mungu) [4] au watu ambao hawakumfuata Mtume na waliamua kupingana naye, [5] wamfuate Mtume na wajiepushe na upinzani wa aina yoyote ile dhidi yake. [6] Aya hii inawatambua Waislamu wakweli kwamba, ni wale wanaomfuata Mtume na hawakupinga agizo lake lolote. [7] Katika Qur'an Aya ya 4 na 6 za Surat al-Mumtahina pia, zinamtambulisha Nabii Ibrahim (a.s) katika kujibari na kujitenga mbali na shirki na washirikina kwamba; ni ruwaza njema. [8]

Aya ya 4 ya Surat al-Mumtahina inasema:Hakika nyinyi mna mfano mzuri kwenu kwa Ibrahim na wale walio kuwa pamoja naye, walipo waambia watu wao: Hakika sisi tumejitenga nanyi na hayo mnayo yaabudu badala ya Mwenyezi Mungu.

Aya ya 6 ya surat al-Mumtahina inasema:Kwa yakini umekuwa mfano mzuri kwenu katika mwendo wao, kwa anaye mtarajia Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Na mwenye kugeuka basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujitosha, Msifiwa.

Utambuzi wa maana ya ruwaza

Us-wa (ruwaza) katika lugha ina maana ya kiongozi [10] na ina maana ya hali ambayo mtu huipata na kuiga wakati anapomfuata mtu mwingine; [11] yaani ile ile hali ya kufuata na kumfanya mtu kiigizo [12] au inatumika kwa maana ya kuwafuata wengine katika kazi na mambo mazuri. Ama katika Aya iliyotangulia ina maana ya kumfuata Mtume na kumfanya kuwa kiigizo na ruwaza; [14] ni kwa muktadha huo, ndio maana Mtume ni kiigizo na ruwaza njema na bora kabisa kwa ajili ya kumfuata na kumfanya kuwa kiigizo na kwa kumfuata yeye inawezekana kupatikana mabadiliko na mageuzi katika njia nyoofu. [15] Kuhusiana na maana na tafsiri ya Aya, kuna riwaya na hadithi nyingi zilizotajwa katika baadhi ya vitabu vya tafsiri; [16] kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, makusudio ya ruwaza njema imetambuliwa kuwa ni Sunna za Mtume (s.a.w.w). [17] Baadhi ya wafasiri wa Qur’an kimsingi wamezungumzia kauli mbili kuhusiana na maana ya Aya hii ya ruwaza njema. Maana ya kwanza ni kwamba, ruwaza njema ni Mtume mwenyewe na maana ya pili ni kwamba, Mtume sio ruwaza njema bali katika dhati yake kuna sifa ambayo kupitia kwayo ana ustahiki wa kuigwa, kufuatwa na kufanywa ruwaza njema. [18]

Masharti ya ruwaza

Katika Aya hii Mwenyezi Mungu anamtambulisha Mtume (s.a.w.w) kwamba, ni kiigizo na ruwaza njema kabisa kwa watu ambao wanaamini rehma za Mwenyezi Mungu na Siku ya Kiyama [19] na ambao wana matarajio na matumaini na thawabu za dunia na akhera [20] ambazo ni matunda ya amali njema; [21] watu ambao hawakughafilika na kumtaja Mwenyezi Mungu hata kwa lahadha moja bali daima walikuwa ni wenye kumtaja na kumdhukuru Mwenyezi Mungu [22] na hawakughafilika na hili katika mazingira yoyote yale iwe ni katika hali ya mazingira magumu, shida na matataizo au ni katika hali ya mazingira mazuri ya raha na kadhalika, [23] hawa ni watu ambao daima huambatanisha matumaini na suala la kumtii Mwenyezi Mungu; [24] hata hivyo baadhi wamesema makusudio ya “kukumbuka na kutaja kwa wingi” ni Swala tano; [25] kwa muktadha huo, kwa kuzingatia muendelezo wa Aya inawezekana kusema kuwa, imani juu ya Mwenyezi Mungu, ufufuo na kumtaja na kumbukuka daima Allah ni msukumo wa kumfanya Mtume (s.a.w.w) kuwa ruwaza njema. [26]

Mpaka wa kumfanya Mtume ruwaza njema

Kwa kuzingatia Aya ya ruwaza njema ni kwamba, Mtume (s.a.w.w) ni ruwaza njema na kiigizo chema katika masuala yote ya kivita na yasiyo ya kivita. Kwa maana kwamba, kumfanya ruwaza njema kunajumuisha mambo yote. [27] Ni kumfanya Mtume kiigizo na ruwaza njema katika maneno na vilevile katika matendo [28]. Kwa maneno mengine ni kuwa, Mtume ametambuliwa kuwa ni ruwaza njema katika vitendo vyote, katika hali zote na katika akhlaqi na madili yote; [29] kama anavyoamini Ayatullah Makarem Shirazi katika tafsiri ya Nemooneh ni kuwa, Mtume (s.a.w.w) ni dira na kiigizo cha Waislamu wote katika hali ya kiroho ya hali ya juu. Kusimama kidete, katika subira, kuwa macho, busara, hekima, ikhlasi, kumzingatia Mwenyezi Mungu na kutopiga magoti (kutosalimu amri) mbele ya matatizo. [30] Baadhi ya wengine wamelifanya duara la Mtume kuwa ruwaza njema kama linaishia katika subira [31] au kitendo cha Mtume katika vita na kustahamili majeraha na magumu mengi; [32] na kumfanya ruwaza njema na kumfuata katika matendo mengine licha ya kuwa ni jambo zuri [33]; lakini sio wajibu. [34]

Aya ya ruwaza njema ilishuka miongoni mwa Aya zilizoshuka kuhusiana na vita vya Ahzab. Baadhi kwa kuzingatia neno “lakum” lililo katika Aya lenye maana ya “mnayo” yaani nyinyi mnayo, wanasema kwamba, wanaozungumzishwa ni watu waliokuweko katika vita vya Ahzab ambao walimuacha Mtume katika mazingira magumu; [35] lakini baadhi ya wafasiri wengine hawatambui kwamba, wanaozungumzishwa ni watu na hadhirina wa vita vya Ahzab na wanaamini kwamba, Mtume ni ruwaza njema na bora kabisa kwa waumini wote katika nyanja zote [36] na kumfanya yeye kuwa kiigizo ni jukumu la daima na thabiti kwa Waislamu wote. [37]

Hukumu ya ruwaza (kiigizo)

Kuna hitilafu za kimitazamo baina ya Maulamaa kuhusiana na kuwa wajibu au mustahabu suala la kumfanya Mtume kuwa ruwaza na kiigizo; baadhi wamelitambua hilo kuwa ni wajibu, huku wengine wakiamini kwamba, asili katika hukumu hii ni mustahabu; isipokuwa kama kutakuwa na hoja ya kuwa kwake wajibu. Baadhi ya wengine wanaamini utenganisho katika hilo. Kwa maana kwamba, kumfuata Mtume (s.a.w.w) katika mambo ya dini ni wajibu lakini kumfanya ruwaza katika mambo ya dunia ni mustahabu. [38]

Jumbe za Aya hii

Sheikh Mohsin Qara’ati ametaja risala na jumbe za Aya hii katika kitabu cha tafsiri ya Nur; ambapo miongoni mwazo ni kwamba, kutambulisha ruwaza na kiigizo ni moja ya mbinu za kimalezi na kutambulisha ruwaza njema na kiigizo chema kunaweza kuwa sababu ya watu kupata uongofu na hivyo kuzuia kufuata viigizo bandia. [39] Kadhalika mwandishi wa tafsirti ya Qur’ ya Mihr katika kuelezea makusudio na madhumuni ya Aya hii anasema, mbali na ulazima wa kuweko ruwaza kwa wanadamu wote, kiongozi wa Uislamu ni ruwaza na kiigizo chema cha kufuatwa na watu wote. [40]