Allahumma Kun Li-Waliyyik (Dua)

Kutoka wikishia
Dua ya Allahumma Kun Li-Waliyyik

Dua ya Allahumma Kun Li-Waliyyik (Kiarabu: دعاء اَللّهُمَّ کُنْ لِوَلیّك ) au dua ya kumuombea na kumtakia afya njema na uzima Imamu Mahdi (a.t.f.s) ni dua ambayo husomwa kumuombea uzima na afya Imamu Mahdi (a.t.f.s), Imam wa 12 wa Waislamu wa madhehebu ya Shia. Dua hii inaanza na: “Allahumma Kun Li-Waliyyik” Ewe Mola kuwa kwa Walii Wako, na imenukuliwa katika kitabu cha Tahdhib al-Ahkam kutoka kwa Imam Baqir (a.s) na Imam Swadiq (a.s).

Katika dua hii, kumetumika maneno na ibara mbali mbali kwa ajili ya kuomuombea uzima na kumtakia afya njema Imamu Mahdi (a.t.f.s). Dua hii imetajwa kuwa miongoni mwa amali za kufanya siku ya Laylatul-Qadr (Mfunguo 23 Ramadhani); lakini inaweza kusomwa wakati wowote. Sanadi na mapokezi ya dua hii ni mursal (hadithi ambayo hakujatajwa jina la mpokezi katika sanadi na mapokezi ya hadithi); hata hivyo imesemekana kwamba, kutokana na ukweli kwamba dua hii imenukuliwa katika vyanzo vya kutegemewa vya hadithi na vitabu vya dua, inaweza kuhukumiwa juu ya usahihi na kuwa kwake na itibari.

Katika vyanzo vingi katika dua hii imetajwa ibara ya fulani bin fulani badala ya jina la Imamu Mahdi (atfs). Ni kutokana na sababu hiyo ndio maana, baadhi wamejaalia kwamba, dua hii ni kwa ajili ya kila Imamu katika zama zake za Uimamu na si mahususi tu kwa ajili ya Imamu Mahdi (a.t.f.s). Kuna kitabu kilichoandikwa na Sheikh Mohsen Qara'ati kiitwacho: “Sherh duaa salamati Imame zaman” ambacho kinatoa ufafanuzi wa dua hii.

Andiko la dua

Dua ya “Allahumma Kun Li-Waliyyik” imenukuliwa kwa ibara tofauti tofauti. Matini na andiko la dua hii kama ilivyonukuliwea katika kitabu cha Misbah al-Mujtahid cha Sheikh Tusi ni:

اللَّهُمَ کُنْ لِوَلِیکَ فُلَانِ بْنِ فُلَانٍ فِی هَذِهِ السَّاعَةِ وَ فِی کُلِّ سَاعَةٍ وَلِیاً وَ حَافِظاً وَ قَائِداً وَ نَاصِراً وَ دَلِیلًا وَ عَیناً حَتَّی تُسْکِنَهُ أَرْضَکَ طَوْعاً وَ تُمَتِّعَهُ فِیهَا طَوِیلً
Ewe Mwenyezi Mungu! Kuwa kwa Walii Wako (ambaye ni) Fulani bin Fulani, katikamuda huu (saa hii) na kila muda (saa zote), Walii, Mlinzi na Muhifadhi wake, Kiongozi, Mwenye kumnusuru, muongozaji (dira) na Jicho (lake...). Mpaka utakapo mdhihirisha juu ya ardhi yako na mjaalie aishi kwa muda mrefu (katika ardhi hii).[1] Dua hii imenukuliwa ikiwa na baadhi ya nyongeza katika kitabu cha Iqbal al-A’mal. [2]

.

Katika kitabu Tahdhib Al-Ahkam, dua hii imenukuliwa kutoka kwa Imam Baqir (a.s) na Imam Swadiq (a.s); [3] lakini katika vyanzo vingine, ibara ya “al-Salihina” imetajwa ingawa haijabainishwa imenukuliwa kutoka kwa Imamu gani. [4] Katika vyanzo vingi ambavyo vimenukuu dua hii, imekuja ibara ya “Fulani bin Fulani". [5] Sayyid Ibn Tawus, msomi na mtaalamu wa elimu ya hadithi wa Kishia katika karne ya sita na saba Hijria katika kitabu cha Iqbal baada ya ibara ya fulani bin fulani (Fulani mwana wa Fulani) amesema: (اللَّهُمَ کُنْ لِوَلِیکَ الْقَائِمِ بِأَمْرِکِ الْحُجَّةِ مُحَمَّدِ بْنِ الْحَسَنِ الْمَهْدِی عَلَیهِ وَ عَلَی آبَائِهِ أَفْضَلُ الصَّلَاةِ وَ السَّلَامِ). [6] Katika kitabu cha Misbah Kaf’ami pia imekuja: مُحَمَّدِ بْنِ الْحَسَنِ الْمَهْدِی) [7]). Muhammad Taqi majlisi, msomi na mtaalamu wa elimu ya hadithi wa karne ya 11 Hijiria amesema: dhahiri ya ibara ya dua ni ushahidi kwamba, inajuzu kusema jina la Imam wa Zama (a.t.f.s) badala ya fulani bin fulani; hata hivyo ni bora kama zitatumiwa moja ya lakabu za mtukufu huyo. [8] Imeelezwa katika kitabu cha Mafatihul Jinan kwamba, badala ya fulani bin fulani semeni: Al-Hujjat bin al-Hassan. [9] Baadhi ya kutokana na kuwa katika dua kumekuja ibara ya fulani bin fulani, wamejaalia juu ya uwezekano kwamba, dua hii sio mahususi kwa Imam Mahdi (a.t.f.s) bali ni ya kila Imam katika zama zake. [10]

Wakati wa kusoma dua hii

Kwa kuzingatia ibara za mwanzo za dua kwa mujibu wa hadithi, licha ya kuwa dua hii, ni maalumu kwa usiku wa tarehe 23 ya mwezi mtukufu wa Ramadhani; lakini inaweza kusomwa wakati wowote na inaweza kukaririwa katika lahadha yoyote ya maisha. [11] Ni kwa muktadha huo ndio maana imeelezwa kuwa, inastahiki kukariri dua hii kila usiku na katika Sala. [12] Kadhalika imeusiwa kwamba, dua hii isomwe baada ya Surat Fatiha na baada ya kumhimidi na kumshukuru Mwenyezi Mungu na kumsalia Mtume Muhammad (s.a.w.w). [13]

Madhumuni

Katika dua ya "Allahumma Kun Li-Waliyyik" Imam ameombewa dua ya uzima na usalama wa kiafya kwa ibara tofauti tofauti. [14] Katika dua hii ameombwa Allah kuwa msimamizi na Walii wa Imam kwa ibara sita: Walii, mlinzi, kiongozi, mnusuru, muongozaji na jicho na Mwenyezi Mungu ameombwa kuwa amfanye Imam awe chini ya hifadhi, ujongozi, nusra na ulinzi wake. [15]

Ibara ya: «فِی هَذِهِ السَّاعَةِ» “Katika saa (wakati) hii” iliyokuja katika dua hii inaashiria usiku wa Laylatul-Qadr (23 Ramadhani) na ibara ya: «وَ فِی کُلِّ سَاعَةٍ» “Na katika kila saa (kila wakati), inabainisha uzingatiaji na dua ya wakati wote na daima kwa ajili ya Imamu Mahdi (a.t.f.s). [16]

Kwa mujibu wa Hassan bin Suleiman Hilli, mmoja wa wanazuoni wa Kishia wa karne ya 8 Hijiria ni kwamba: Madhumuni na makusudio ya ibara ya: «حَتَّی تُسْکِنَهُ أَرْضَکَ طَوْعاً»“Mpaka utakapo mdhihirisha juu ya Ardhi yako" ni zama na wakati wa kudhihiri Imam Mahdi (a.t.f.s) na kupata kwake nguvu; kwani katika zama za kuwa ghaiba, haki yake imeghusubiwa na hana na uwezo wa kudhihirisha haki baina ya watu. [17] Aidha anasema: Makusudio ya «تُمَتِّعَهُ فِیهَا طَوِیلًا»: “na mjaalie aishi kwa muda mrefu (katika ardhi hii)” ni raj’a (kufufuliwa kundi miongoni mwa watu na kurejea duniani katika kipindi cha kudhihiri Imamu Mahdi) na baada ya kuuawa shahidi Imam Mahdi (a.t.f.s). [18] Kwa mujibu wa Sheikh Mohsin Qara'ati, makusudio ya: «تُمَتِّعَهُ فِیهَا طَوِیلًا» Ni tumaini na matarajio ya utawala Imam Mahdi kuwa mrefu duniani. [19]

Sanadi na itibari

Dua ya Allahumma Kun Li- Waiyyik katika vyanzo vya hadithi na dua, imenukuliwa kupitia tu kwa Muhammad bin Issa bin Ubaid. [20] Kuna tofauti ya maoni juu ya uaminifu wake. [21] Najashi [22] na Sheikh Tusi [23] wamemtambua kuwa ni dhaifu. Kwa mtazamo wa Allama Hilli ni kwamba, rai yenye nguvu ni kukubali uaminifu wa Muhammad Ibn Issa. [24]

Kwa mujibu wa Allama Majlisi, sanadi na mapokezi ya dua hii ni mursal (hadithi ambayo hakujatajwa jina la mpokezi katika sanadi na mapokezi ya hadithi). [25] Hata hivyo, Sheikh Mohsen Qara'ati anasema kwamba, ushahidi kama vile kuwepo kwa dua hii katika al-Kafi [26] na Tahdhib al-Ahkam [27] na vitabu vyenye itibari kama vile. al-Mazar al-Kabir cha Ibn Mash’hadi, [28] al-Misbah cha Kaf’ami [29] na Iqbal al-A’mal cha Sayyid Ibn Tawus; [30] na kuoana madhumuni ya dua hii na akili na nakili na kwamba, sentensi zake zote na ibara za dua hii zimekuja katika dua zingine, yote haya yanaonyesha na kuwa hoja ya kuwa na itibari na kuwa sahihi dua hii. [31]

Kwa nini dua ya kumuombea afya njema Imam Mahdi (a.t.f.s)?

Kwa mujibu wa Shekhe Mohsen Qaraati, Imamu wa kumi na mbili, ni kama Maimamu wengine watoharifu, ana maisha ya kawaida na anaugua magonjwa na anapata matatizo. Kwa hiyo, dua na kutoa sadaka kwa ajili ya kumuombea afya njema ni jambo linalostahiki.[32] Amezingatia kipengele kingine cha kumuombea uzima na afya Imam Mahdi (a.t.f.s) ni kwamba, kumuombea ulinzi na hifadhi Imam kunafanyika katika fremu ya kutekeleza risala na kuvumilia jukumu (mzigo) la Uimamu – iwe wakati wa ghaiba yake au anapodhihiri. Kwa sababu kubeba mzigo huo mzito kunahitaji ulinzi na uangalizi maalumu kutoka kwa Mwenyezi Mungu. [33] Pia, katika dua zilizopokelewa kutoka kwa Maimamu (a.s), kunaonekana dua za kumuombea uzima na kumtakia afya njema Imamu wa Zama (a.t.f.s). [34]

Monografia

Kitabu cha Sharh-i duʾa-yi salamati-yi Imam-i Zaman (a.t.f.s) kilichoandikwa na Sheikh Mohsin Qara'ati

Kitabu cha Sharh-i duʾa-yi salamati-yi Imam-i Zaman, kilichoandikwa na Sheikh Mohsin Qara'ati na kupitiwa na Hassan Silmabadi, ndani yake kumejadiliwa sanadi na mapokezi ya dua hii pamoja na kutolewa ufafanuzi wake. Mwandishi baada ya utangulizi na kujadili sanadi na mapokezi, anajishughulisha na kufanya uchunguzi kuhusiana na maneno na ibara za dua hii. [35] Mwishoni mwa kitabu kunabainishwa faida za kusoma dua hii pamoja na masharti ya kukubaliwa dua. [36] Aidha mwandishi anabainisha kuwa, dua hii imekuwa mashuhuri kimakosa kwamba, ni dua ya Dua al-Faraj ilhali hii si sahihi. Kwa maana kwamba, baadhi ya watu wamekuwa wakiitaja kimakosa kuwa ni Dua al-Faraj. [37] Kitabu hiki kimechapishwa na kusambazwa katika mji wa Qom na taasisi ya Utamaduni ya Imamu Mahdi (a.t.f.s).

Vyanzo

  • Ḥillī, Ḥasan b. Sulaymān al-. Mukhtaṣr al-baṣāʾir. Edited by Mushtāq Muẓaffar. 1th edition. Qom: Daftar-i Nashr-i-i Islāmī, 1421 AH.
  • Ḥillī, al-Ḥasan b. Yūsuf al-. Rijāl al-ʿallāma al-Ḥillī. Edited by Sayyid Muḥammad Ṣādiq Baḥr al-ʿUlūm. 2th edition. Najaf: Dār al-Dhakhāʾir, 1411 AH.
  • Ibn al-Mashhadī, Muḥammad. Al-Mazār al-kabīr. Edited by Jawād Qayyūmī Iṣfahānī. 1th edition. Qom: Daftar-i Nashr-i-i Islāmī, 1419 AH.
  • Ibn Ṭāwūs, ʿAlī b. Mūsā. Iqbāl al-aʿmāl. 2th edition. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1409 AH.
  • Kafʿamī, Ibrāhīm b. ʿAlī al-. Al-Balad al-amīn wa l-dirʿ al-ḥaṣīn. Beirut: Muʾassisah-yi al-Aʿlamī, 1418 AH.
  • Kafʿamī, Ibrāhīm b. ʿAlī al-. Al-Miṣbāḥ fī al-adʿiya wa al-ṣalawāt wa al-ziyārāt. Qom: Dār al-Raḍī, 1405 AH.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī & Muḥammad Ākhūndī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1407 AH.
  • Majlisī, Muḥammad Bāqir al-. Malādh al-akhyār fi fahm tahdhib al-akhbār. Edited by Mahdī Rajāʾī. Qom: Kitābkhāna-yi Marʿashī Najafī, 1406-1407 AH.
  • Majlisī, Muḥammad Bāqir al-. Mirʾāt al-ʿuqūl fī sharḥ akhbar Āl al-Rasūl. Edited by Sayyid Hashim Rasūlī Maḥallātī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmiyya, 1404 AH.
  • Majlisī, Muḥammad Taqī. Rawḍat al-muttaqīn fī sharḥ man lā yaḥḍuruh al-faqīh. 2nd edition. Qom: Muʾassisa-yi Farhangī Islamī Kūshanpūr, 1406 AH.
  • Najāshī, Aḥmad b. ʿAlī al-. Rijāl al-Najāshī. Qom: Jāmiʿat al-Mudarrisīn, 1365 Sh.
  • Qarāʾatī, Muḥsin. Sharḥ-i duʿāyi salāmatī-yi Imam-i Zaman(a). Qom: Bunyād-i Farhangī-yi Haḍrat-i Mahdī-yi Mawʿūd(a), 1393 sh.
  • Qummī, Shaykh ʿAbbās. Mafātīḥ al-jinān. Qom: Majmaʿ Iḥyāʾ al-Thiqāfat al-Islāmiya, [n.d].
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥaasn al-. Al-Rijāl al-Ṭūsī. Edited by Jawād Qayyūmī Iṣfahānī. 3th edition. Qom: Daftar-i Nashr-i-i Islāmī, 1373 sh.
  • Ṭūsī, Muḥamamd b. al-Ḥasan al-. Miṣbāḥ al-mutahajjid wa silāḥ al-mutaʿabbid. Beirut: Muʾassisat Fiqh al-Shīʿa, 1411 AH.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Tahdhīb al-aḥkām. Edited by Sayyid Ḥasan al-Khirsān. 4th edition. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1407 AH.