Suratul- Fil

Kutoka wikishia

Suratul- Fil (Kiarabu: سورة الفيل), ni surah ya 105 na ni mojawapo ya sura za Makka za Qur'ani, ambayo imewekwa katika juzuu ya thelathini. Sura hii inaitwa Suratul-Fil kwa sababu inasimulia kisa cha kaumu ya watu wa tembo; kaumu ambayo iliwacha ardhi yao kwa nia ya kuiangamiza Al-Kaaba, na Mwenyezi Mungu akawapelekea ndege wa Ababil, na ndege hao wakawaangamiza kwa kuwanyeshea (kuwaangushia) mawe juu ya vichwa vyao. Kwa mujibu wa nadharia za baadhi ya Maulamaa, wamesema kwamba ikiwa mtu anataka kusoma Suratul Al-Fil katika sala za faradhi za kila siku baada ya Suratul -Fat-ha (Hamd), basi analazimika asome Suratul-Quraishi pamoja nayo Kwa sababu sura hizi mbili zinahesabiwa ni sura moja.

Kuhusiana na fadhila ya kusoma Suratul Al-Fil, imepokewa kutoka kwa Imamu Swadiq (a.s) kwamba kuisoma wakati wa sala ya faradhi kutawafanya viumbe wote walio hai washuhudie Siku ya Qiyamah kwamba alikuwa miongoni mwa walioswali. Kwa hiyo Mungu anakubali ushuhuda wao na kuwaamuru waingie Peponi.

Utambulisho

  • Jina

Kuhusiana na Suratul Fil, Sura hiyo inaelezea kisa cha kaumu ya watu wa tembo. Vile vile kwa jina jengine Sura hii inaitwa Sura Alam-Tara, kwa sababu inaanza na neno hilo.

  • Mpangilio na mahala ilipoteremshwa Sura

Suratul Fil ni mojawapo ya sura za Makka na ni surah ya 19 iliyoteremshwa kwa Mtume (s.a.w.w). Sura hii ni sura ya 105 katika mpangilio wa sasa uliomo katika misahafu [2] na imejumuishwa katika juzuu ya 30 ya Qurani.

  • Idadi ya mistari na vipengele vingine

Suratul- Fil ina aya 5, maneno 23 na herufi 97. Sura hii ni mojawapo ya sura fupi na ni mojawapo ya sura zenye kina (na aya fupi) za Quran. Suratul- Fil ni miongoni mwa Sura ambazo Aya zote 5 ziliteremshwa pamoja na kwa wakati mmoja kwa Mtume (s.a.w.w).[3]

Maudhui

Katika sura hii, Mwenyezi Mungu anaelezea kisa cha Kaumu ya watu wa tembo, walioiacha ardhi yao kwa nia ya kuiangamiza na kuiharibu Al-Kaaba, na Mungu akawaangamiza kwa kutuma ndege. Ndege ambao kwa idhini ya Mwenyezi Mungu waliangamiza kaumu ya watu wa tembo kwa kuwarushia mvua ya mawe juu ya vichwa vyao, na hatimae walitafunwa kama majani.[4]

Chanzo na dalili za kuteremshwa Sura hii

Kuhusiana na sababu za uteremshwaji wa Suratul Fil, imenukuliwa kutoka kwa Imamu Sajjad (a.s) kwamba, yeye amesimulia kuhusu adhama ya uteremshwaji wa Sura Al-Fil: Abu Talib alimuuliza Mtume (s.a.w.w): Je, umetumwa kuwaongoza na kuwahubiria watu wote, au unawahubiria watu wako tu? Mtukufu Mtume (s.a.w.w) akajibu: “Hapana, mimi nimetumwa kwa watu wote, weupe na weusi, Waarabu na wasiokuwa Waarabu; ninawaita wale wote walio juu ya milima na bahari kwenye ibada hii, ninawaalika wote wa Uajemi na Rumi. "Maneno hayo ya Mtume Mtukufu (s.a.w.w) yalisikika katika masikio ya watu wa Quraishi na kuwaletea mshangao mkubwa. Watu wa Quraish wakamwambia Abu Talib: Je, husikii anachosema mtoto wa ndugu yako? -(Abu Talib alikuwa mtoto wa Ami yake Mtume (s.a.w.w)- Naapa kwa Mwenyezi Mungu, ikiwa watu wa Uajemi na Rumi watasikia maneno haya, watatutoa katika ardhi yetu na watayatenganisha mawe ya Al-Kaaba kipande baada ya kipande. (wakimaanisha wataharibu Kaaba). Hapa ndipo Mwenyezi Mungu alipoteremsha Suratul- Fil kuhusu maneno yao kwamba watu wa Uajemi na Rumi wanaiharibu Al-Kaaba.[6]

Usomaji wa Surah Fil katika sala

Kwa mujibu wa baadhi ya nadharia za Maulamaa, wamesema kwamba; kama mtu anataka kusoma Suratul- Al-Fil katika sala za faradhi za kila siku baada ya Suratul-Hamd, basi asome Sura hii pamoja na Suratul- Quraish. Kwa sababu surah hizi mbili zinajulikana na kujumuishwa kama ni sura moja.[7]

Sifa na fadhila za Suratul-Fil

:Makala asili: Fadhila za Surah

Miongoni mwa fadhila za kusoma Suratul Fil, imepokewa kutoka kwa Imamu Swadiq (a.s) kwamba kuisoma sura hii wakati wa sala ya faradhi kutawafanya viumbe wote wa dunia washuhudie Siku ya Qiyaamah kwamba yeye alikuwa miongoni mwa walioswali, na mwitaji ataita Siku ya Kiyama na kusema hakika mulimshuhudia mja wangu akiswali. Na nilikubali ushuhuda wenu juu yake, basi muingizeni Peponi naye ni miongoni mwa wanao pendwa na Mwenyezi Mungu na vitendo vyake.[8] Katika baadhi ya hadithi, kuna sifa na fadhila zimetajwa kwa ajili ya kusoma Suratul Fil, ikiwa ni pamoja na kuondoa uovu wa adui [9] kutodhalilishwa na kutoathiriwa na kashfa au fitna zozote zile .[10]

Vyanzo

  • Fattāl al-Niyshābūrī, Muḥammad b. Aḥmad. Rawḍat al-wāʿiẓīn wa baṣīrat al-muttaʿiẓīn. Qom: Intishārāt-i Raḍī, 1375 Sh.
  • Ḥurr al-ʿĀmilī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Wasāʾil al-Shīʿa. Qom: Āl al-Bayt, 1414 AH.
  • Khurramshāhī, Bahāʾ al-Dīn. Dānishnāma-yi Qurʾān wa Qurʾān pazhūhī. Tehran: Dūstan-Nahīd, 1377 Sh.
  • Maʿrifat, Muḥammad Hadī. Āmūzish-i ʿulūm-i Qurʾān. Tehran: Sāzmān-i Tablīghāt-i Islāmī, 1371 Sh.
  • Ṣadūq, Muḥammad b. ʿAlī al-. Thawāb al-aʿmāl wa ʿiqāb al-aʿmāl. Edited by Ṣādiq Ḥasanzāda. Tehran: Armaghān-i Ṭūbā, 1382 Sh.
  • Ṭabāṭabāʾī, Muḥammad Ḥusayn. Al-Mīzān fī tafsīr al-Qurʾān. Translated to Farsi by Mūsawī Hamidānī. Fifth edition. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī, 1374 Sh.
  • Ṭabrisī, Faḍl b. al-Ḥasan al-. Majmaʿ al-bayān. Translated to Farsi by Bīstūnī. Mashhad: Āstān-i Quds-i Raḍawī, 1390 Sh.
  • Tawḍīḥ al-masāʾil-i marājiʿ. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī, 1392 Sh.