Maharimu

Kutoka wikishia

Maharimu (Kiarabu: المحارم) ni watu wenye nasaba nawe (jamaa) ambao ni haramu kuwaowa. Kwa maoni ya mafaqihi, hukumu za hijabu zilizotajwa katika Qur'an, haziwalazimishi watu hawa kuvaa hijabu pale wakiwe mbele yako. Sheria kuhusiana na maharimu zimefafanuliwa vya kutosha ndani ya Qur'an. Nasaba, ndoa pamoja na kunyonya kutoka katika kifua kimoja ni moja ya sababu zinazopelekea kupatikana fungamano la kimaharimu. Suala la mafunagamano ya kimaharimu limegawika katika sehemu tatu; Maharimu kinasaba (kiukoo) "محارم نسبی", Maharimu kisababu (kupitia ndoa) "محارم سببی", Maharimu kwa kunyonya "محارم رضاعی".

Mama, nyanya (bibi), dada, binti, mjukuu, binti wa dada, binti wa kaka, shangazi na khaloo(mama mdogo) ni maharimu wa kinasaba (kiukoo) kwa mwanamme. Kwa upande mwingine, baba, babu, mwana wa kiume, kaka, mtoto wa kiume dada, mtoto wa kiume wa kaka, ami na mjomba, ni maharimu wa kinasaba (kiukoo) kwa mwanamke. Pia, mke, mama wa mke na bibi yake, binti wa mke, mke wa baba (mama wa kambo) na mke wa mwana, ni maharimu wanaotokana na sababu ya ndoa kwa mwanamme. Kwa upande wa pili; Mume, baba-mkwe (baba wa mume), babu wa mume, mwana wa kiume wa mume, mume wa mama (baba wa kambo) na mkwe (mume wa binti yako), ni maharimu kupitia sababu ya kindoa kwa mwanamke.

Kwa mujibu wa fat'wa za mafaqihi, wanawake wote wale ambao ni haramu kuwaoa kutokana na kufungamana nao kinasaba na kiujamaa, pia wanawake kama hao itakuwa ni haramu kuwaoa kupitia fungamano la umaharimu unaotokana na kunyonya. Hivyo basi ni haramu mtu kumuowa mama aliyemnyoyesha pia mama wa mama huyo, nyanya yake (bibi yake), dada yake, binti yake, mjukuu wake, pia shangazi pamoja na khaloo zake(mama wadogo). Iwapo mnyonyeshwaji atakuwa ni mtoto wa kike, basi itakuwa ni haramu kwa mtoto huyo kuolewa na; Mume wa mama mnyonyeshaji, baba yake na babu, kaka yake, ami na mjomba wake, mwana na mjukuu wake pamoja na kaka wa mume huyo. Pia ni haramu kwake kuolewa na; mtoto wa mama mnyonyeshaji, mjukuu wake, baba na babu yake, ami pamoja na mjomba wa mama huyo.

Uelewa wa dhana

Jina maharimu "محارم" ni istilahi maalumu yenye kuashiria jamaa wote ambao mtu hastahiki (haijuzu) kuoana nao. [1] Hukumu na sheria muhimu kuhusiana na Maharimu, zimetajwa na kufafanuliwa katika Aya mbili za Qur'an, nazo ni Aya ya 23 ya Surat al-Nisa na Aya ya 31 ya Surat al-nuur. Aya ya 23 ya Surat al-Nisaa, imekuja kufafanua suala la maharimu pamoja na kuharamisha kufunga ndoa baina yao. [2] Aya ya 31 ya Surat Nuur nayo imekuja kuzungumzia na kuorodhesha nasaba ya maharimu wa kike ambao mwanamme ameharamishiwa kuwaoa. [3] Katika madhehebu ya Shia kuna Hadithi kadhaa ambazo zimekuja kufafanua na kubainisha hukumu maalumu katika sheria za ndoa, ambapo baadhi ya hadithi hizo ni maalumu kuhusiana na maharimu. Kwa mfano katika vyanzo vya Hadithi kama vile; Kitabu Wasailu Al-Shia na Mustadraku Al-Wasail, kuna mlango maalumu uitwao «ابواب النکاح المحرم» "Mlango Kuhusu Kuwaowa Maharimu". Mlango huo umekusana Hadithi kuhusiana na kuwaoa au kuwaangalia na kuwakodolea macho maharimu. [4] Suala la maharimu na hukumu zake limezungumzwa na kufafanuliwa katika tofauti ya fiqhi, suala hili unaweza kulikuta kwenye mlango wa hukumu za ndoa, talaka pamoja na hukumu za maiti. [5]

Hukumu

Mara tu baada kuthibiti ukaribu wa kinasaba, papo hapo huharamika kuoana baina yao, na hujuzu kila mmoja kumuangalia mwenzake na kudhihirisha mapambo yao na baadhi ya sehemu za mwili wao ambazo si haramu kuziangali, kama vile nywele na mikono. [6] Kwa mujibu wa mtazamo wa mafaqihi, ukiachana na mke na mume, ni haramu kwa waliobaki miongoni mwa Maharimu kuangaliana tupu zao, na kuangalia viungo vyingine ni halali kwa sharti ya kwamba muangalio huo usiwe ni mwangalio wa kimatamanio na kujiburudisha. [7] Pia, si wajibu kwa wanawake kufunika miili yao isipokuwa sehemu maalumu za miili yao. [8]

Sababu zinazopelekea umaharimu

Kuna sababu maalumu zinazopelekea kupatikana kwa fungamano la nasabu ya umaharimu, ambapo hupelekea kuzaliwa kwa hukumu maalumu za umaharimu baina ya pande mbili. [9] Kuna mambo 11 yaliyotajwa katika vitabu vya fiqhi yanayosababisha na kupelekea kupatikana kwa fungamano la umaharamu, na hatimae kuharamika kwa ndoa baina ya wenye mafungamano ya kiumaharimu. Sababu kuu katika suala hili zimegawika katika kategoria tatu; Umaharimu wa nasaba ya kiukoo, Umaharimu wa nasaba ya kindoa na Umaharimu wa nasaba ya kunyonya. [11]

  • Umaharimu kupitia Nasaba: Nasaba ni uhusiano na fungamano la kiukoo na kijamaa linalopatikana baada ya wanadamu kufungamana na kuzaana kwa njia ya ndoa au isiyo ya ndoa. [Maelezo] Kwa maana hiyo maharimu wa kinasaba ni watu wanaozaliwa wakiwa na nasaba ya umaharimu baina yao na wale watu wa ukoo wao. [12]
  • Umaharimu kupitia njia ya kunyonya: Kunyonyesha ni moja wapo ya mambo yanayojenga fungamano la kiumaharimu. Hivyo basi iwapo mtoto atanyonyeshwa na mwanamke ambaye si mama yake mzazi, tendo hilo litasababisha kujengeka kwa aina ya fungamano la kiumaharimu baina ya mtoto na mama huyo pamoja na jamaa na watu wanaohusiana na mama huyo.[13] Bila shaka, kuna masharti maalumu katika kutengemaa kwa fungamano na umaharimu kupitia njia ya unyonyeshaji, miongoni mwa masharti hayo ni kwamba; Mwanamke anayenyonyesha awe amepata mimba kwa njia ya halali, yaani awe ameolewa kisheria, mnyonyeshwaji awe amenyonya mara kadhaa na kwa mfululizo (yaani sio awe leo kanyonya kisha akakata, kisha akaja kunyonya tena siku ya tatu au ya nne yake), awe amenyonya kwa mama mmoja sio kwa mama tofauti, awe hakukla chakula chengine isipokuwa maziwa ya mama huyo tu na mnyonyaji (mtoto) awe chini ya miaka miwili kwa hisabu ya mwezi wa mwandamo. [14]
  • Umaharimu kupitia ndoa: Umaharimu kupitia ndoa hutimia kusoma au kukariri mkataba wa ndoa. Mkataba huu wa ndoa pamoja na kujenga umaharimu baina ya mume na mke, pia hujenga fungamano la umaharimu la kuwafanya baadhi ya jamaa wa mume kuwa ni maharimu wa baadhi ya jamaa wa mke, ambao huitwa "محارم سبَبَی" maharimu kupitia sababu ya ndoa. [15]

Aina za Maharimu

Kulingana na sababu zinazopelekea umaharimu, umaharimu umeweza kugawika katika kategoria tatu, nazo ni:

Maharimu wa Nasaba

Kwa mujibu wa maoni ya mafaqihi, wakitegemea Aya ya 23 ya Surat al-Nisaa, [16] kuna makundi saba ya wanawake ambao ni maharimu wa makundi saba za wanaume: [17]

  • Mama na bibi wa ubande wa baba na upande wa mama. [18]
  • Binti na mjukuu na watakaozaliwa kutoka kwao. [19]
  • Dada [20]
  • Mabinti wa kaka na watoto wake wa kiume, wajukuu na watakaozaliwa na watoto wa kaka kadri watakavyoendelea. [21]
  • Binti ya dada, watoto wake wa kiume, wajukuu pamoja na watakaozaliwa na watoto na wajukuu hao. [22]
  • Shangazi ni pamoja na mashangazi wa baba na mashangazi wa mama. [23]
  • Khaloo pamoja na makhaloo wa baba na makhaloo wa mama. [24]
  • Baba na babu, mwana wa kiume pamoja na mwana wa mwana wa kiume, kaka, mtoto wa dada, mtoto wa kaka, ami na ami wa baba na mama, mjomba na mjomba wa baba na mama ni Maharimu wa wanawake. [25]

Maharimu kupitia njia ya kunyonya

Makala asili:Umaharimu wa kuchangia ziwa

Hadithi maarufu iliyotegemewa na mafaqihi, ni ile Hadithi ya Mtume (s.a.w.w) isemayo kwamba; “chochote kilichoharamika kutokana na nasaba, pia nacho ni haramu kutokana na fungamano la kiujamaa litokanalo na kunyonya”. [26] Kwa mujibu wa maelezo ya Hadithi hii, wanazuoni wametoa fat'wa ya kwamba; Wanawake wote ambao ni haramu kuwaoa kutokana na fungamano la nasaba, pia huwa ni haramu kuwaoa kupitia fungamano la kiujamaa (umaharimu) litokanalo na njia ya kunyonya. [27] Katika suala la maharimu kupitia njia ya kunyonya, ikiwa mtoto atakuwa ni wa kiume, basi yeye atakuwa na fungamano la kiumaharimu na mwanamke aliyemnyonyesha, pamoja na mama wa mama huyo, nyanya (bibi), dada, binti, mjukuu, shangazi pamoja na khaloo(mama mdodo). [28] Ikiwa mtoto mchanga aliyenyonyeshwa ni mwanamke, basi yeye huyo atakuwa na fungamano la umaharimu na mume wa mwanamke aliyemnyonyesha , pamoja na baba yake, kaka yake, ami yake, mjomba wake, mtoto wake wa kiume pamoja na wajukuu zake. Pia kwa upande mwingine, yeye atakuwa na fungamano la umaharimu na kaka wa mwanamke aliyemnyonyesha, mtoto, mjukuu, baba na babu, ami pia na mjomba wa mama huyo. [29]

Maharimu Kisababu (Kupitia ndoa)

Wanawake ambao ni maharimu kwa upande wa wanaume kupitia ndoa ni pamoja na: mke, mama wa mke na bibi yake, binti wa mke, mke wa baba yako mzazi (mama wa kambo) na mke wa mwanao.[30]

Kwa upande wa muolewa (mke), yeye huwa na fungamano la umaharimu na; Mumewe, baba mkwe, babu wa mume, mtoto wa mumewe, mume wa mama yake (baba wa kambo) pamoja na mkwe. [31] Pia, hairuhusiwi kwa mwanamme kumuoa shemeji yake ilihali dada yake bado yuko katika ndoa yake, ila iwapo dada ataachwa au atafariki, basi hapo yeye ataweza kuolewa na shemeji yake huyo. [32] Hata hivyo, ni lazima kwake kuchunga sheria za hijabu mbele ya mume wa dada yake. [33]

Masuali yanayofungamana

Vyanzo

  • Bani Hashim Khomaini, Sayyid Muhammad Hassan, Risalah Taudhih al-Masāil Marāji' Muthabeqe ba Fatawa Sizdah Nafar az Marāji' Mu'azzame Taqlid, Qom: Darftare Intisyarate Islami Jameeh Mudarrisin Hauzah Ilmiah Qom, 1385 HS.
  • Farahidi, Khalil Ahmad, Al-'Ain, Diedit oleh: Mahdi Makhzumi dan Ibrahim Samirrai, Qom: Nashr Hijrat, 1410 H.
  • Imam Khumaini. Tahrir al-Wasilah. Qom: Muassasah Mathbu'at Dar al-Ilm, tanpa tahun.
  • Khurramshahi, Bahauddin, Danesynameh Qur'an va Quran Pazuhi, Teheran: Intisyarat Dustan, 1377 HS.
  • Mufid, Muhammad bin Muhammad, Al-Muqni'ah, Qom: Kongres Internasional yang ke-1000 Sheikh Mufid, 1413 H.
  • Najafi, Muhammad Hassan, Jawāhir al-Kalām fi Sharh Sharāyi' al-Islam, Beirut: Dar Ihya at-Turats al-Arabi, 1404 H.