Mujammi’ bin Abdallah Aidhi

Kutoka wikishia

Mujammi’ bin Abdallah Aidhi (Kiarabu: مُجَمّع بن عبد الله العائذي) ni katika masahaba wa Imamu Ali (a.s) [1] na ni katika mashahidi wa Karbala. [2] Yeye ni katika tabiina [3] na alikuwa akitokana na kabila la Madh’hij. [4] Baba yake yaani Abdallah bin Mujammi’ amehesabiwa kuwa miongoni mwa masahaba wa Mtume (s.a.w.w). [5]

Kwa mujibu wa ripoti za vyanzo vya historia, Mujammi’ alikuwa miongoni mwa watu wanne ambao baada ya kupata miongozo ya Tirimmah bin Adi [6] waliondoka katika mji wa Kufa na kwenda kuungana na Imamu Hussein (a.s) na kufikia katika eneo la Udhayb al-Hijanat katika nyumba moja iliyokuwa jirani na mji wa Kufa. Katika wakati huo, Hurr bin Yazid Riyahi alimjia Imamu Hussein na kusema, hawa hawakuwa miongoni mwa watu waliofuatana na wewe na hivyo ni lazima mimi niwatie mbaroni na kuwarejesha; hata hivyo Imam Hussein (a.s) aliwatetea na kuwataja kuwa ni katika masahaba na watu wake na akamwambia Hurr kama hatoachana nao atapigana naye vita. Hivyo Hurr akaachana nao.

Imamu aliwaambia wale watu wanne, leteni habari kuhusiana na watu wa nyuma yenu (watu wa mji wa Kufa). Mujammi’ akasema: Mabwanyenye na shakhsia kubwa wamepewa rushwa na mifuko yao imejazwa (pesa) ili waelekee upande wao. Wao wameungana pamoja dhidi yako. Watu wengine waliobakia nyoyo zao ziko upande wako; lakini kesho panga zao zitakuwa dhidi yako. Kisha Imamu Hussein akaulizia habari za Qays bin Mus’hir Saydawi aliyekwa mjumbe wake na wao wakampa habari kwamba, ameuawa shahidi. [7] Katika baadhi ya vyanzo vya historia, nukuu hii imeelezwa kuwa ni kuhusiana na Mujammi’ bin Abdallah Amiri. [8]

Kwa mujibu wa nukuu ya Abu Mikhnaf na Muhammad bin Jarir Tabari, Mujammi’ aliingia katika medani ya vita mwanzoni mwa vita akiwa pamoja na Amru bin Khalid al-Saydawi na mfanyakazi wake pamoja na Jabir bin Harith Salmani; lakini wakazingirwa na jeshi la Omar bin Sa’d. Katika hali hii, Abbas bin Ali (a.s) akawaokoa katika hali ambayo walikuwa wamejeruhiwa sana. Maadui wakawakaribia kwa mara nyingine tena na kuwaua wote katika sehemu moja. [9] imeelezwa kwamba, wakati Mujammi’ anauawa shahidi alikuwa na umri wa miaka 50. [10] Imeelezwa kwamba, Mujammi’ alikuweko pia katika vita vya Siffin. [11]

Katika Ziyarat al-Shuhadaa [12] na Ziyarat Rajabiya ya Imamu Hussein (as) [13] anatolewa salamu hii: «السَّلَامُ عَلَی مُجَمِّعِ بْنِ عَبْدِاللَّهِ الْعَائِذی» ; Amani (ya Mwenyezi Mungu) iwe juu ya Mujammi’ bin Abdallah Aidhi. Katika Ziyarat al-Shuhadaa na kwa mujibu wa nukuu ya kitabu cha al-Mazar al-Kabir cha Ibn Msh’hadi, jina lake limetajwa kuwa ni al-Aidi. [14]

Kwa mujibu wa ripoti ya Muhammad Samawi katika kitabu chake cha Ibsar al-Ain, Aidh mwana wa Mujammi’ ni miongoni mwa wale watu wane waliongana na Imamu Hussein katika eneo la Udhayb al-Hijanat na aliuawa shahidi katika tukio la Karbala akiwa kando ya baba yake. [15 [16].