Dua ya kumi na nne ya Sahifa Sajjadiyya
Nakala ya Sahifa al-Sajjadiyah, katika hati ya Naskh ya Abdullah Yazdi, iliyoandikwa katika Sha'ban 1102 AH. | |
Mtoaji / Mwandishi | Imamu Sajjad (a.s) |
---|---|
Lugha | Kiarabu |
Msimulizi / Mpokezi | Mutawakkil ibn Harun |
Mada | Kuwaombea himaya waliodhulumiwa, pamoja na kuomba nusura ya Mwenye Ezi Mungu dhidi ya watawala dhalimu. |
Chanzo | Sahifa Sajjadiyah |
Tafsiri kwa Lugha ya | Kifarsi |
Dua ya Kumi na Nne ya Sahifa Sajjadiyya (Kiarabu: الدعاء الرابع عشر من الصحيفة السجادية) ni miongoni mwa dua zilizorithiriwa kutoka kwa Imamu Sajjad (a.s), ambayo ndani yake Imamu anatafuta nusura ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kupata ukombozi na ulinzi dhidi ya uonevu wa watawala dhalimu. Ndani ya dua hii, Imamu Sajjad (a.s) amegusia utambuzi wa Mwenye Ezi Mungu juu ya hatima za wahanga wa dhuluma za watawala madhalimu katika zama mbali mbali, na anamuomba Mungu mbele ya hadhara Yake, ili amwezeshe kuzishinda hisia za chuki na ghadhabu zinazoweza kumvaa dhidi ya mahasimu wake. Kadhalika, Imamu Sajjad (a.s) anaiomba kupata hadhi daraja ya ridhaa (umaridhawa) na kuwa na taslimu (kujisalimisha kikamilifu) mbele ya Mwenye Ezi Mungu.
Aidha, dua hii ya kumi na nne imechambuliwa na kufafanuliwa katika tafsiri mbali mbali zilizochambua maandiko ya Sahifa Sajjadiyya. Miongoni mwa tafsiri zilizoandikwa kwa lugha ya Kiajemi ni pamoja na; Diyare Asheghan cha Hussein Ansarian na Shuhud wa Shenakht cha Hassan Mamduhi Kermanshahi. Pia kuna waandishi waliotoa uchambuzi na ufafanuzi wa dua hii kwa lugha ya Kiarabu, moja ya vikitabu mashuhuri katika uwanja huu, ni Riyadhu al-Salikina, kilichoandikwa na Sayyid Ali Khan Madani.
Mada ya Dua ya Kumi na Nne
Muhimili mkuu wa dua ya kumi na nne ya kitabu cha Sahifa Sajjadiyya umejikunjua katika kuwaombea himaya waliodhulumiwa, pamoja na kuomba nusura ya Mwenye Ezi Mungu dhidi ya watawala dhalimu.[1] Kwa mujibu wa maelezo ya Muhammad Jawad Haji Aliakbari, Mwenyekiti wa Baraza la Urasimishaji wa Sera za Maimamu wa Sala za Ijumaa nchini Iran, ni kwamba; Kiongozi wa Mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu, Ayatollah Khamenei, alitoa agizo rasmi la usomaji wa dua hii mahususi kwa ajili ya kuomba ushindi kwa wapiganaji wa Harakati za Ukinzani dhidi ya Israel. Maagizo hayo yalijiri wakati wa uvamizi wa Israeli nchini Lebanoni mwaka 2024.[2] Kufuatia agizo hilo, imeripotiwa kuwa; dua hii ilianza kusomwa kijumuiya katika misikiti mbali mbali nchini Iran.
Mafunzo Msingi Yaliomo Duani Humu
Dua hii inamwelekezea Mwenye Ezi Mungu ombi la kumpa hifadhi mdhulumiwa anayekabiliwa na matendo ya kidhalimu dhidi yake, na kumwezesha kuzidhibiti na kuzishinda hisia zake za kinyongo na ghadhabu zake. Kadhalika, inatilia mkazo umuhimu wa tohara ya nafsi (self-purification) dhidi ya kasoro za kiakhlaqi (kimaadili).[3] Mafundisho ya dua ya kumi na nne, yaliyonukuliwa katika vifungu 16[4] kutoka kwa Imamu Sajjad (a.s), yameainishwa kama ifuatavyo:
- Upeo wa elimu kamilifu ya Mungu; Ukwasi wa elimu ya Mungu juu ya hatima ya wahanga wa dhuluma
- Ushahidi wa Mungu ni kamilifu na usiopingika katika uwepo wote
- Mungu ni msaidizi wa wanyonge na hasimu wa madhalimu
- Uungaji mkono wa msimamo imara dhidi ya uonevu na ukosoaji wa wanyonge wa kukubali dhuluma
- Udhaifu na uduni wa wakandamizaji
- Kuwasilisha shtaka mbele ya Mungu dhidi ya dhuluma na mdhalimu
- Umuhimu wa kudumisha adabu za kiuja (ubudiyya) katika mazingira yote
- Ombi la kupatiwa hifadhi dhidi ya kutendea wengine dhuluma
- Dua kwa ajili ya kudhibiti hisia za kinyongo na ghadhabu dhidi ya hasimu fulani
- Kuomba rehema za Mwenye Ezi Mungu kama ni fidia ya kustahimili dhulma
- Mungu kama mtoa suluhu pekee dhidi ya changamoto za waja wake
- Ombi la kuwajibishwa kwa madhalimu na kumwombea uokozi muhanga wa dhuluma
- Ombi la kutaka kuepushwa na matamanio (mielekeo hasi ya nafs) na tabia mbaya, pamoja na tabia ya kuto tosheka (kutoridhika).
- Kuridhika na maamuzi ya Mungu kwa kuwa na kuhisi za moyoni juu ya malipo ya Mungu, pamoja na kuwa na taswira ya adhabu ya maadui na madhalimu.
- Kuomba malipo (ya amali) kutoka kwa Mwenye zi Mungu peke yake.
- Kuomba na kutaraji mwitikio wa Mungu juu ya dua tuziombazo
- Kutafuta hifadhi ya uimara wa itikadi (imani)
- Mdhulumiwa yupo katika mtihani wa kudhulumiwa na dhalimu yupo katika mtihani wa dhulma dhidi ya wengine
- Ombi la kutaka kuepushwa na kukata tamaa juu ya malipizo ya Mungu dhidi ya dhalimu
- Ombi la kuomba kufikia daraja la umaridhawa na kusalimu amri mbele ya matukio mbali mbali, yawe ya kheri au shari, na kukabidhi mambo yetu kwa Mungu, na kwamba kama kheri yetu ni kupata malipo ya Akhera badala ya yale ya kiduni, basi tumtake Allah atupe uwezo wa kuwa na Subira na uvumilivu hapa duniani.[5]
Tafsiri Chambuzi za Dua ya Kumi na Nne
Kuna tafsiri nyingi chambuzi zilizochambua dua ya kumi na nne ya Sahifa Sajjadiyya miongoni mwanzo ni zile zilizoandikwa kwa lugha ya Kifarsi na wanazuoni wa Iran. Miongoni mwa kazi hizo zilizoandikwa kwa Kifarsi ni kama vile; kitabu cha uchambuzi wa Sahifa Sajjadiya, kiitwacho Diyare Asheqan, kilichoandikwa na Hussein Ansarian,[6] Shuhud wa Shenakht, kazi ya Muhammad Hassan Mamduhi Kirmanshahi,[7] na Sherh wa Tarjome Sahife Sajjadiyye, ambayo ni kazi ya Sayyid Ahmad Fahri.[8]
Halikadhalika, dua hii ya kumi na nne ya Sahifa Sajjadiyya imepata mchanganuo na uchambuzi mbali mbali uliofanya kwa lugha ya Kiarabu. Baadhi ya vitabu vyenye uchambuzi huo wa kina uliotolewa kwa lugha ya kiarabu kuhusiana na dua hii, ni pamoja na; Riyad al-Salikin, kitabu kilichoandikwa na Sayyid Ali Khan Madani,[9] Fi Dhilal al-Sahifa al-Sajjadiyya, kazi ya Muhammad Jawad Mughniyyah, Riyad al-'Arifina,[10] kitabu kilichoandikwa na Muhammad bin Muhammad Darabi na Afaq al-Ruh,[11] ambayo ni kazi andishi ya Sayyid Muhammad Hussein Fadlallah.[12] Isitoshe, pia msamiati msingi uliotumika ndani ya dua hii, umechunguzwa na kuorodheshwa ndani ya vitabu maalumu vya uchambuzi wa kilugha. Miongoni mwa vitabu hivyo ni; Ta'liqat 'ala al-Sahifa al-Sajjadiyya, kazi ya Faidhu Kashani[13] na Sharh al-Sahifa al-Sajjadiyya, kazi iliyofanywa na Izzu al-Din al-Jaza'iri.[14]
Matini ya Dua na Tafsiri Yake
وَ كَانَ مِنْ دُعَائِهِ عَلَيْهِ السَّلَامُ إِذَا اعْْتُدِيَ عَلَيْهِ أَوْ رَأَي مِنَ الظَّالِمِينَ مَا لَا يُحِبُّ
يَا مَنْ لَا يَخْفَى عَلَيْهِ أَنْبَاءُ الْمُتَظَلِّمِينَ
وَ يَا مَنْ لَا يَحْتَاجُ فِي قَصَصِهِمْ إِلَى شَهَادَاتِ الشَّاهِدِينَ .
وَ يَا مَنْ قَرُبَتْ نُصْرَتُهُ مِنَ الْمَظْلُومِينَ
وَ يَا مَنْ بَعُدَ عَوْنُهُ عَنِ الظَّالِمِينَ
قَدْ عَلِمْتَ ، يَا إِلَهِي ، مَا نَالَنِي مِنْ فُلَانِ بْنِ فُلَانٍ مِمَّا حَظَرْتَ وَ انْتَهَكَهُ مِنِّي مِمَّا حَجَزْتَ عَلَيْهِ ، بَطَراً فِي نِعْمَتِكَ عِنْدَهُ ، وَ اغْتِرَاراً بِنَكِيرِكَ عَلَيْهِ .
اللَّهُمَّ فَصَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ ، وَ خُذْ ظَالِمِي وَ عَدُوِّي عَنْ ظُلْمِي بِقُوَّتِكَ ، وَ افْلُلْ حَدَّهُ عَنِّي بِقُدْرَتِكَ ، وَ اجْعَلْ لَهُ شُغْلًا فِيما يَلِيهِ ، وَ عَجْزاً عَمَّا يُنَاوِيهِ
اللَّهُمَّ وَ صَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ ، وَ لَا تُسَوِّغْ لَهُ ظُلْمِي ، وَ أَحْسِنْ عَلَيْهِ عَوْنِي ، وَ اعْصِمْنِي مِنْ مِثْلِ أَفْعَالِهِ ، وَ لَا تَجْعَلْنِي فِي مِثْلِ حَالِهِ
اللَّهُمَّ صَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ وَ أَعْدِنِي عَلَيْهِ عَدْوَى حَاضِرَةً ، تَكُونُ مِنْ غَيْظِي بِهِ شِفَاءً ، وَ مِنْ حَنَقِي عَلَيْهِ وَفَاءً .
اللَّهُمَّ صَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ ، وَ عَوِّضْنِي مِنْ ظُلْمِهِ لِي عَفْوَكَ ، وَ أَبْدِلْنِي بِسُوءِ صَنِيعِهِ بِي رَحْمَتَكَ ، فَكُلُّ مَكْرُوهٍ جَلَلٌ دُونَ سَخَطِكَ ، وَ كُلُّ مَرْزِئَةٍ سَوَاءٌ مَعَ مَوْجِدَتِكَ .
اللَّهُمَّ فَكَمَا كَرَّهْتَ إِلَيَّ أَنْ أُظْلَمَ فَقِنِي مِنْ أَنْ أَظْلِمَ .
اللَّهُمَّ لَا أَشْكُو إِلَى أَحَدٍ سِوَاكَ ، وَ لَا أَسْتَعِينُ بِحَاكِمٍ غَيْرِكَ ، حَاشَاكَ ، فَصَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ ، وَ صِلْ دُعَائِي بِالْإِجَابَةِ ، وَ اقْرِنْ شِكَايَتِي بِالتَّغْيِيرِ .
اللَّهُمَّ لَا تَفْتِنِّي بِالْقُنُوطِ مِنْ إِنْصَافِكَ ، وَ لَا تَفْتِنْهُ بِالْأَمْنِ مِنْ إِنْكَارِكَ ، فَيُصِرَّ عَلَى ظُلْمِي ، وَ يُحَاضِرَنِي بِحَقِّي ، وَ عَرِّفْهُ عَمَّا قَلِيلٍ مَا أَوْعَدْتَ الظَّالِمِينَ ، وَ عَرِّفْنِي مَا وَعَدْتَ مِنْ إِجَابَةِ الْمُضْطَرِّينَ .
اللَّهُمَّ صَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ ، وَ وَفِّقْنِي لِقَبُولِ مَا قَضَيْتَ لِي وَ عَلَيَّ وَ رَضِّنِي بِمَا أَخَذْتَ لِي وَ مِنِّي ، وَ اهْدِنِي لِلَّتِي هِيَ أَقْوَمُ ، وَ اسْتَعْمِلْنِي بِمَا هُوَ أَسْلَمُ
اللَّهُمَّ وَ إِنْ كَانَتِ الْخِيَرَةُ لِي عِنْدَكَ فِي تَأْخِيرِ الْأَخْذِ لِي وَ تَرْكِ الِانْتِقَامِ مِمَّنْ ظَلَمَنِي إِلَى يَوْمِ الْفَصْلِ وَ مَجْمَعِ الْخَصْمِ فَصَلِّ عَلَى مُحَمَّدٍ وَ آلِهِ ، وَ أَيِّدْنِي مِنْكَ بِنِيَّةٍ صَادِقَةٍ وَ صَبْرٍ دَائِمٍ
وَ أَعِذْنِي مِنْ سُوءِ الرَّغْبَةِ وَ هَلَعِ أَهْلِ الْحِرْصِ ، وَ صَوِّرْ فِي قَلْبِي مِثَالَ مَا ادَّخَرْتَ لِي مِنْ ثَوَابِكَ ، وَ أَعْدَدْتَ لِخَصْمِي مِنْ جَزَائِكَ وَ عِقَابِكَ ، وَ اجْعَلْ ذَلِكَ سَبَباً لِقَنَاعَتِي بِمَا قَضَيْتَ ، وَ ثِقَتِي بِمَا تَخَيَّرْتَ
آمِينَ رَبَّ الْعَالَمِينَ ، إِنَّكَ ذُو الْفَضْلِ الْعَظِيمِ ، وَ أَنْتَ عَلَى كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ
Na ifuatayo ilikuwa ni miongoni mwa dua zake (a.s), pindi anapokabiliwa na ukandamiza Fulani au anaposhuhudia jambo lisilomridhisha kutoka kwa madhalimu Fulani:
Ewe usiyefichikiwa na malalamiko ya wanaodhulumiwa.
Na Ewe usiyehitaji maelezo ya mashahidi katika kuelewa kwako matukio na visa vya ukandamizwaji wao.
Na Ewe Ambaye nusura yake iko karibu na wanaodhulumiwa.
Na Ewe Ambaye, msaada Wake uko mbali na madhalimu.
Hakika Ee Mungu wangu! umeshayajua, yale yaliopata kutoka kwa fulani bin fulani, miongoni mwa yale uliyoyakataza; na jinsi alivyonivunjia heshima kwa kufanya yale uliyomzuia asiyafanye, amefanya hivyo kwa jeuri kutokana na yale uliomneemesha, na akijidanganya kuwa yuko salama, na yumbali na hasira Zako dhidi yake.
Ewe Mola wangu, mshushie rehma Zako Muhammad na Aali zake, na umdhibiti kwa nguvu Zako mkandamizaji wangu na hasimu wangu (huyu ili) asiweze kunidhulumu, na uyapunguze makali yake dhidi yangu kwa kudura Yako, na umshughulishe na yale yanayomwelekea (yanayomdhuru) yeye mwenyewe, na umtie ajizi ya kutoweza kufafikia yale anayonikusudia.
Ewe Mola wangu, na umshushie rehema na amani Muhammad na Aali zake. Na usimruhusu (dhalimu huyu) wala kumrahisishia udhalimu wake dhidi yangu, na unipe nusura kamili dhidi yake. Unihifadhi dhidi ya hisia za kuiga nyenendo zake, na usinijaalie kuwa na hali (au sifa) kama yake.
Ewe Mungu, mpe mshushie rehema zako Muhammad na Aali zake, na unisaidie dhidi ya [adui] huyu kwa kumpatiliza mara moja; kitendo kitakachokuwa ni tiba kwa hasira yangu dhidi yake, na kitakachotosheleza (kukidhi kiwango cha) chuki yangu dhidi yake.
Ewe Mola, zishushie swala na salamu Muhammad na Aali zake, na unifidie kwa msamaha Wako dhidi ya uonevu wake kwangu, na ubadilishe ubaya wa kitendo chake dhidi yangu kwa huruma Yako. Hakika, kila tukio hasi ni duni mbele ya ghadhabu Yako, na kila janga ni hafifu mbele ya fadhila Yako.
Ewe Mungu, kama vile ulivyonifanya nichukie kudhulumiwa, basi vilevile nilinde nisiwe ni mwenye kuwadhulum wengine.
Ewe Mola wangu, mimi simlalamikii yeyote yule isipokuwa Wewe, wala sitafuti msaada wa mwamuzi (hakimu) yeyote yule ghairi Yako, Hasha wa Kalla (katu siwezi kuwa maamuzi kama hayo) ! Basi, mrehemu Muhammad na Aali zake, na uiunganishe dua yangu hii na kabuli (yako), na liweke shitaka langu hili sambamba na maboresho (mabadiliko).
Ewe Mungu, usinitahini kwa mtihani wa kukata tamaa ya insafu Yako, na wala usimtahi yeye (adui yangu) kwa mtihani wa kujiona yuko salama na yumbali na adhabu yako. Kwani hilo litamfanya yeye aendelee kunidhulumu na kunizuilia haki zangu. Na umuonjeshe hivi karibuni kile ulichowaahidi madhalimu, na unionyeshe kile ulichowaahidi katika kuwajibu walio na dhiki.
Ewe Mola wangu, mshushie swala na salamu Muhammad na Aali zake. Na unipe taufiki (uniwezeshe) ya kukubali yale uliyokadiria kwa ajili yangu na dhidi yangu, na nijaalie niwe na ridhaa (nitosheke) kwa yale uliyonitunukia na uliyonipokonya. Na nielekeze kwenye mwenendo ulio adilifu zaidi, na uniajiri (nitumikishe) kwenye shughuli zenye amani zaidi.
Ewe Mola wangu, na iwapo kheri yangu mbele Yako ipo katika kuakhirisha kunichukulia haki yangu na kuacha kisasi kwa aliyenidhulumu hadi Siku ya Upambanuzi na makusanyiko ya mahasimu (Siku ya Kiama), basi mswalie Muhammad na Aali zake, na unithibitishe kwa kunipa nia safi na subira ya kudumu kutoka Kwako.
Na unihifadhi dhidi ya shauku ovu na jazba ya watu wenye uchu wa kupidukia mipaka. Na unichoree moyoni mwangu taswira ya kile ulichonihifadhia katika thawabu Zako, na kile ulichomuandalia hasimu wangu katika jazaa na adhabu Yako. Na jaalia (taswira au mchoro huo) uwe ni chimbuko la qanaa yangu kwa yale uliyokadiria, na (uwe ni msingi wa) uthabiti wa imani juu ya yale uliyonichagulia.
Amina (iwe hivyo), Ewe Mola wa walimwengu wote. Bila shaka Wewe ni mwenye wema wa kupindukia (adhimu), Nawe ni Mweza wa kila kitu.
Rejea
- ↑ Mamduhi, Shuhud wa Shenakhte, 1388 S, juz. 2, uk. 34.
- ↑ «Ayaat Fat-hi wa Duaye Nasri; Tawsiye Rahbar Inqilab Baraye Piruzy Jabhat Muqawamat», Tovuti ya Daftar Hifdh wa Nashr A'thar Hadhrat Ayatullah al-Udhma Khamenei.
- ↑ Mamduhi, Shuhud wa Shenakhte, 1388 S, juz. 2, uk. 34.
- ↑ Tarjume wa Sherh Duaye Chahradahom Sahife Sajadiye, Tovuti Erfan.
- ↑ Ansarian, Diyar Asheqan, 1993, juz. 5, uk. 223-290; Mamduhi, Shuhud wa Shanakhte, 1382 S, juz. 2, uk. 34-53.
- ↑ Ansarian, Diyar Ashiqan, 1372 S, juz. 5, uk. 21-74.
- ↑ Mamduhi, Kitab Shuhud wa Shanakhte, 1388 S, juz. 1, uk. 451-464.
- ↑ Fihri, Sherh wa Tafsir Sahifa Sajjadiyah, 1388 S, juz. 1, uk. 499-515.
- ↑ Madani Shirazi, Riyadh al-Salikin, 1435 AH, juz. 2, uk. 401-423.
- ↑ Mughniyah, Fi Dhilal al-Sahifa, 1428 AH, uk. 153-159.
- ↑ Darabi, Riyadh al-Arifin, 1379 AH, uk. 133-136.
- ↑ Fadhlullah, Afaq al-Ruh, 1420 AH, juz. 1, uk. 261-273.
- ↑ Faidh Kashani, Taaliqat Ala al-Sahaifa al-Sajadiyeh, 1407 AH, uk. 34.
- ↑ Jazairi, Sherh al-Sahifa al-Sajjadiyah, 1402, uk. 94-95.
Vyanzo
- «Ayaat Fat-hi wa Duaye Nasri; Tawsiye Rahbar Inqilab Baraye Piruzy Jabhat Muqawamat», Tovuti ya Daftar Hifdh wa Nashr A'thar Hadhrat Ayatullah al-Udhma Khamenei, Darji Matalib: 29 Aban 1403 S, Bozdad: 6 Adhar 1403 S.
- Ansarian, Hussein, Diyar Asheqan, Tafsir Jamii Sahifa Sajjadiyah, Tehran, Payam Azadi, 1374.
- Khalji, Muhammad Taqi, Asrar al-Khamushan, Qom, Parto Khorshid, 1383 S.
- Darabi, Muhammad bin Muhammad, Riyadh al-Arifin Fi Sherh Sahifa Sajjadiyah, Muhaqiq Hussein Dargahi, Tehran, Nashr Us-wah, 1379.
- Fadhlullah, Sayyid Muhammad Hussein, A'faq al-Ruh, Beirut, Dar al-Malik, 1420 AH.
- Fahri, Sayyid Ahmad, Sherh wa Tarjume Sahifa Sajjadiyeh, Tehran, Us-wah, 1388 S.
- Faidh Kashani, Muhammad bin Murtaza, Taaliqat Ala Sahifa Sajjadiyah, Tehran, Muasase al-Bahth wa al-Tahqiqat al-Thaqafiyah, 1407 AH.
- Mughniyeh, Muhammad Jawad, Fi Dhilal al-Sahifa al-Sajjadiyyah, Qom, Dar al-Kitab al-Islami, 1428 AH.
- Madani Shirazi, Sayyid Ali Khan, Riyadh al-Salikiin Fi Sherh Sahifa Sayyid al-Sajidin, Qom, Muasase al-Nashr al-Islami, 1435 AH.
- Mamduhi Kermanshahi, Hassan, Shuhud wa Shenakhte: Tarjume wa Sherh Sahifa al-Sajjadiyyah, Ba Muqadime Ayatullah Jawadi Amuli, Qom, Bostan Kitab, 1385 S.