Dar es Salaam

Kutoka wikishia
Msikiti wa Mashia Katika Mji wa Dar es salaam

Dar es Salaam (Kiarabu: دارالسَّلام ) ni mji ulioko Tanzania ambako Mashia wachache wanaishi ndani yake. Mashia wa mji huu wanajumuisha wenyeji (watu wa asili) na wasio wenyeji. Mashia wasio wa asili wanaundwa na Makhoja, Mabohora na wahajiri kutoka Lebanon.

Ofisi kuu za Bilal Muslim Mission, WIPAHS na Shirikisho la Shia Khoja Afrika ni miongoni mwa mashirika na taasisi muhimu za Makhoja Shia Ithnaasharia katika mji wa Dar es Salaam.

Nafasi na Umuhimu

Dar es Salaam ndio mji mkubwa zaidi nchini Tanzania. Jiji hili lilikuwa mji mkuu wa Tanzania hadi 1996. Katika mwaka huu, mji mkuu ulihamishwa kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma. [1] Mashia wana vituo na taasisi katika mji huu. Kulingana na sensa ya 2022, mji huu ulikuwa na wakazi 5,383,728. [2]

Mashia wa Dar es Salaam wanajumuisha makundi kadhaa kama Khoja Shia Ithnaasharia, Bohora, Agakhan, wahajiri wa Kilebanon na Mashia wenyeji na asilia wa Tanzania. [3] Kulingana na Amirbahram Arabahmadi, Makhoja walianza kuishi katika mji huo kuanzia 1880 na kuendelea. [4]

Taasisi Muhimu za Mashia Khoja

Ofisi na majengo makuu ya baadhi ya taasisi za Mashia Khoja Ithnaasharia zinapatikana Dar es Salaam.

Bilal Muslim Mission

Makala asili: Bilal Muslim Mission

Bilal Muslim Mission ni katika taasisi na vikundi muhimu vya Mashia Khoja Ithnaasharia. Lengo lake kuu ni kufikisha na kueneza ujumbe wa Uislamu hususan mafundisho ya madhehebu ya Ahlul Bayt (as) baina ya Waafrika. [5]

Shirikisho la Khoja Ithnaasharia Afrika

Makala asili: Shirikisho la Khoja Ithnaasharia Afrika

Shirikisho la Shia Khoja Ithnaasharia Afrika (The African Federation of Khoja Ithna-Asheris) linaundwa na Mashia wenye asili ya India (wahindi) walioko katika eneo la Afrika Mashariki na ambalo linafanya na kuendesha shughuli zake chini ya Shirikisho la Kimataifa la Shia Khoja Ithnaasharia. Hatua na shughuli za shirikisho hili zimejikita zaidi katika masuala ya kielimu, tablighi na utoaji huduma za umma. [6]

Taasisi ya WIPAHS

Makala asili: WIPAHS

Taasisi ya WIPAHS (World Islamic Propagation and Humanitarian Services) ni katika asasi na jumuiya za kitablighi za Makhoja Shia Ithnaasharia. Taasisi hii inajitegemea na kufanya kazi zake kando na Shirikisho la Khoja Ithnaasharia Afrika na Bilal Muslim Mission na inaendesha shughuli zake katika uga wa kutoa huduma za kielimu, kiafya, kitablighi na huduma za umma. Mmoja wa waasisi na viongozi mashuhuri na waanzilishi wa taasisi hii ni Haj Saheb. [7]

Vituo vya Elimu na Huduma

Vituo vya Mashia Khoja Ithnaasharia

  • umuiya (Jamati) ya Dar es Salaam: Taasisi muhimu kabisa ya Mashia Tanzania na Afrika Mashariki iliasisiwa 1973. Takribani Mashia 5,000-7000 walikuwa chini ya jumuiya hii wakati huo. [8]
  • Shule na Chuo cha mafunzo cha al-Muntazir ni moja ya vituo muhimu vya kielimu vya Makhoja Shia Ithnaasharia ambayo ipo chini ya Shirikisho la Shia Khoja Afrika na inaendeshwa na Jumuiya ya Khoja Dar es Salaam. Shule hii inatoa mafunzo ya elimu katika ngazi mbalimbali kuanzia chekechekea mpaka sekondari ya juu na ina matawi yake katika mikoa mbalimbali ya Tanzania. [9]
  • Husseini Madrasa: Hiki ni moja ya vituo vya elimu ya dini ambacho ni maalumu kwa Mashia Khoja Ithnaasharia wanaoishi Tanzania. [10]
  • Taasisi ya al-Itra Foundation: Taasisi hii pamoja na kutoa huduma mbalimbali imejikita zaidi katika uga wa kutarjumu vitabu na kuvisambaza na katika tasnia ya habari. Taasisi hii ina kituo cha Televisheni cha IBN TV kinachorusha vipindi vyake kutokea Dar es Salaam na kituo cha Radio cha Maarifa FM yenye makao yake katika mji wa Tanga. [11]
  • Kituo cha Ahlul-Bayt: Kituo hiki ni moja ya vituo vya kielimu vyenye mfungamano na Bilal Muslim Mission. Kituo hiki kina tawi pia nje ya Tanzania. [12]
  • Taasisi ya Kielimu Waliul Asr Kibaha: Hiki ni kituo cha elimu ambacho kina shule na vyuo na kinafungamana na taasisi ya WIPAHS. Taasisi hii ipo yapata kilomita 35 nje ya jiji la Dar es Salaam. [13]
  • Msikiti wa Shia Khoja Ithnaasharia: Msikiti huu upo katikati ya jiji la Dar es Salaam na mbali na kusaliwa Sala za jamaa, katika msikiti huo hufanyika pia mikusanyiko na hafla za kidini za Mashia kama Muharram, Maulidi ya Mtume na Maimamu n.k [14]

Vituo Visivyo vya Makhoja

  • Madrasa ya Imamu Ridha (a.s).
  • Taasisi ya Imamu Hussein (a.s).
  • Madrasa ya Amirul-Muuminina (as).
  • Taasisi ya Imamu Baqir (a.s).
  • Madrasa ya Sibtein (a.s).
  • Madrasa ya Ahlul-Bayt (a.s).
  • Hawza ya Imamu Swadiq (a.s).
  • Madrasa ya Fatima Zahra (a.s) yenye mfungamano na WIPAHS. [15]
  • Msikiti wa Ghadir Kigogo Post.
  • Jumuiya ya Shia Ithnaasharia Tanzania (TIC).

Maombolezo ya Muharram

Katika kumi la mwezi Muharram (Mfunguo Tano) katika mji wa Dar es Salaam hufanyika maombolezo ya kumbukumbu ya kuuawa shahidi Imamu Hussein (a.s). Katika usiku wa Ashura, Mashia hufanya matembezi kuelekea katika msikiti mkuu wa Mashia wakiwa katika hali ya maombolezo huku wakipiga vifua na kuimba kaswida za maombolezo. Mashia Wahindi na wasio Mashia hushiriki katika maombolezo haya. [16]

Shakhsia wa Kishia

Sayyid Saeed Akhtar Rizvi
  • Sayyid Saeed Akhtar Rizvi: (1927-2002) aliyekuwa mashuri kwa jina la Allamah Sayyid Akhtar Rizvi na aliyekuwa na lakabu (jina mashuhuri) la Raisi wa mubalighini ni kiongozi wa Mashia kutoka India na mubalighi wa Kishia nchini Tanzania. Yeye ni miongoni mwa wanzilishi na waasisi wa taasisi ya Bilal Muslim Mission [17] na Madrasa ya Ahlul-Baiti (a.s) katika nchi ya Tanzania. Pia alikuwa ni mwanachama wa baraza kuu la Jumuiya ya Kimataifa ya Ahl-Bayt (Majmaa Jahani ya Ahlul-Baiti) [18]. Sayyid Rizvi aliaga dunia 2002 nchini Tanzania na kuzikwa katika makaburi ya Makhoja Shia Ith’naasharia Dar es Salaam. [19]
  • Dr. Ali Dina, mmoja wa wasomi na wanazuoni mahiri wa Kikhoja na khatibu mzuri.
  • Ja’far Mehbob Somji, mmoja wa wajumbe wa Jumuiya ya Makhoja Dar es Salaam. [20]