Sayyid Said Akhtar Rizvi

Kutoka wikishia
Sayyid Said Akhtar Rizvi

Sayyid Said Akhtar Rizvi (Kiarabu: السيد سعيد أختر الرضوي) (1927-2002 A.D) aliyekuwa mashuri kwa jina la Allamah Sayyid Akhtar Rizvi na aliyekuwa na lakabu (jina mashuhuri) la raisi wa muballighiin ni miongoni mwa wabunifu na waasisi wa taasisi ya Bilal Muslim Mission na Madrasa ya Ahlul-Baiti (a.s) katika nchi ya Tanzania. Pia alikuwa ni mwanachama wa baraza kuu la Majmaa Jahaani ya Ahlul-Baiti (Jumuiya ya Kimataifa ya Ahlul-Bayt) na mnamo mwaka 1993 A.D alianzisha tawi lingine la taasisi hii katika nchi ya Tanzania.

Allamah Rizvi pamoja na kuwa na harakati mbali mbali katika kuwaunganisha na kuileta pamoja jamii ya Khoja Ithna asharia wa Tanzania, pia alijishughulisha na harakati mbali mbali katika nyanja za kielimu na kitamaduni, na kuna athari nyingi sana alizo ziacha kama vile kutunga na kutarjumi pia kufasiri vitabu viingi kwa lugha ya Kiingereza, Kiarabu na Kiurdu, na ameweza kutarjumi juzuu kadhaa za Tafsiri makini na (yenye thamani )ya Al-Miizaan kitabu ambacho ni Tungo na uandishi wa Allama Twabatwabai, na pia ametarumi kitabu muhimu Al-Ghadiir kilicho tungwa na kuandikwa na Allamah Al-amini na hiki ni miongoni mwa vitabu vilivyo tarjumiwa na Sayyid Akhtar.

Marhum Allamah Akhtar Rizvi katika uwanja huu wa tablighi aliweza kuwaongoa na kuwaingiza takriban watu wapatao elfu khamsini kwenye madhehebu ya Kishia na pia kuasisi na kujenga misikiti, madrasa, maktaba, na Hawzah (vyuo vya kidini) kadhaa za kielimu na bila kusahau dispensari nk…

Historia ya Maisha Yake

Allamah Sayyid Akhtari Rizvi alizaliwa mnamo tarehe 5 Januari mwaka 1927 A.D katika kijiji cha Ashri katika viunga vya Siiwaan, wilaya ya Bahaar nchini India katika familia ya wanazuwoni, na alipata malezi yake katika nyumba ya baba yake katika kijiji cha Goopalpor katika viunga vya Siiwaan mahala ambapo ilikuwa ni sehemu ya malezi na mafunzo ya wanazuwoni wengi wakubwa. Sayyid Akhtar anatokana na masayyid wa ukoo wa Rizvi ambao nasaba yao inapitia kwa mtoto wa sayyid Mussa Mubarqai (a.s) na kukomea kwa Imamu Mussa Ridha (a.s) Baba yake Allamah Rizvi Ayatullah Al-haj Sayyidi Abul-hasan Rizvi alikuwa ni miongoni mwa wanazuwoni na matabibu maarufu katika zama zake. Allamah Rizvi alipata masomo yake ya mwanzo na ya msingi (primary) katika kijiji cha Goopaalpor, kisha katika umri wa miaka nane akifuatana na baba yake akahamia mji wa Pante na kujiunga na madrasa ya Abbasiyah kisha baada ya hapo akajiunga na madrasa ya kielimu ya Suleimaniyyah na kujishughulisha na usomaji wa masomo ya kidini katika madrasa hiyo sambamba na kujishughulisha na masomo hayo pia alikuwa akiedelea na mafunzo ya lugha ya Kiingereza na Kifarsi (Kiajemi) pia akijishughulisha na masomo ya hesabu.

Vivyo hivyo kwa ajili ya kujiendeleza na masomo ya juu ya kidini mnamo mwaka 1941 A.D alihamia katika wilaya ya Otorpraadiish na kujiunga na Hawzah ya kielimu iliyo kuwa ikijulikana kwa jina la (Jaamiul-uluumi Jawaadiyah) katika mji wa Banaas. Allamah Rizvi pamoja na kuendelea na masomo ya kihauza pia aliendelea na masomo yake ya akademi.

Walimu Wake

Allamah Rizvi katika muda wote wa masomo yake alipiga goti la adabu kwa maulamaa wengi sana na aliweza kujipatia maarifa kutoka kwa maulamaa hao na baadhi yao ambao ni muhimu sana kati ya walimu na maustadhi wake ni kama wafuatao:

  • Ayatullah Sayyid Abul-Hassan Rizvi.
  • Ayatullah Sayyid Dhafar Al-Hassan Rizvi.
  • Hujjatul-islaam Sayyid Farhat Hussein.
  • Hujjatu-islaam Sheikh Mustafa Jawhar.
  • Hujjatul-islaam Sayyid Ghulaam Mustafa.
  • Hujjatul-islaam Sayyid Mukhtaar Ahmad.
  • Hujjatul-islaam Sheikh Kadhim Hussein
  • Hujjatul-islaam Sayyid Muhammd Ridha.

Marhum Said Akhrat Rizvi katika umri wa miaka 20 alichagulwa kuwa Imamu wa jamaa wa Mashia wa Lahoor (Halloor) katika nchi ya India. Pia kwa muda kadhaa alijiunga na madrasatul-waaidhiin na kujishughulisha na masomo katika madrasa hiyo na katika miaka hiyo pia aliandika vitabu na Makala kadhaa katika maudhui za kiislaam na kuvichapia katika chapa mbalimbali huko India.

Uenezaji wa Ushia Tanzania

Mwanazuwoni huyu wa kishia, mnamo mwaka 1960 A.D alihamia Tanzania kwa lengo la kueneza (kufanya tablighi) ya madhehebu ya kishia na kueneza maktab ya Ahlul-baiti (a.s) na aliishi katika mji wa Lindi na kujifunza lugha ya kiswahili. Kwa hakika yeye alikuwa na nafasi na dauru muhimu na kubwa sana katika kuiunganisha jamii ya khoja shia Ithnaa ashariyah hadi kufikia hatua kwamba pamoja na kwamba yeye hakuwa ni miongoni mwa Khoja Ithnaasharia lakini kutokana na mahusiano yake mapana na makubwa na jamii hiyo, akijulikana kuwa ni miongoni mwa watu wa jamii hiyo.

Allamah Rizvi mnamo mwaka 1962 A.D alitoa mswaada wa kuanzishwa kwa taasisi ya Bilal Muslim Mission taasisi ambayo ni miongoni mwa taasisi kubwa na muhimu ya Khoja shia Ithna ashariyah kwa lengo la kueneza Uislaam na hasa madhehebu ya Ushia baina ya Waafrika wa Tanzania, na mswaada huo aliupelekea kwenye Federation ya shia Afrika na baada ya Federation ya Afrika kukubaliana na kuwafiki muswaada huo mnamo mwaka 1967 A.D taasisi hii ikaanzishwa rasmi na baada ya mambo ya taasisi ya Bilal Muslim kukamilika kati ya mwaka 1980-1990A.D Allamah alifanya safari mbali mbali kuelekea Ulaya na Amerika ya kusini, na alikutana na baadhi ya maulamaa na kuwalingania kujitokeza kuisadia taasisi ya Bilal Muslim ya Tanzania na Kenya. Na mwishowe juhudi za mwanazuwoni huyu mkubwa hivi leo zimeufanya wigo wa harakati za Bilal Muslim Mission kuvuka bara la Afrika, na taasisi hii imekuwa na matawi katika nchi mbalimbali za Afrika pia katika nchi za Amerika, Swiden nk…

Harakati na Majukumu

Baadhi ya harakati za Allamah Rizvi ni kama zifuatazo:

  • Kuandaa muswada wa kuasisi na kuanzisha (Taasisi ya Bilal Muslim Mission) mnamo mwaka 1962A.D
  • Kiongkzi mkuu wa taasisi ya Bilal Muslim Mission
  • Kuasisi na kuanzisha (madrasa ya Ahlul-Baiti (a.s) katika mji mkuu wa Tanzania.
  • Kuasisi taasisi ya Jumuiya ya Kimataifa ya Ahlul-Bayt (Majmaa jahaani ya Ahlul-Baiti (a.s) katika mji wa London mnamo mwaka 1982 A.D.
  • Kushikilia kiti cha katibu mkuu na raisi wa Majmaa Jahaani islaami Ahlul-baiti (a.s) katika mji wa London.
  • Kuasisi na kuanzisha tawi la Majmaa jahani Ahlul-baiti nchini Tanzania.
  • Kuasisi (taasisi ya mambo ya kheri, kujitolea na misaada ya Bilal) huko India.
  • Kuwa mwanachama wa Majmaa Ahlul-Baiti (a.s)

Kisha alikuwa na mchango mkubwa katika ujenzi wa makumi ya misikiti, madrasa, maktaba, hawzah za kielimu na Dispensary na mambo mengine mengi yanye manufaa ya kijamii.

Upelekaji wa Wanafunzi wa Kiafrika Masomoni Najaf

Allamah Rizvi (Mungu amrehemu) baada ya kuweka makazi yake Afrika, aliwatuma na kuwapeleka wanafunzi wa kiafrika nchini Iraq kwenye mji wa Najaf, Lebanon na katika Hawzah ya kielimu ya Qom baada ya kukamilisha masomo yao awali ya Hawzah. Na kwa hivi sasa kuna idadi kubwa ya wanafunzi kutoka katika nchi mbali mbali za kiafrika wanao endelea na masomo yao katika Hawzah ya kielimu ya mji mtukufu wa Qom na Najaf.

Uandishi wa Hukumu na Sheria ya Mambo Binafsi kwa Mujibu wa Madhehebu ya Kishia

Allamh Rizvi alitoa maombi kwa serikali ya nchi ya Tanzania ombi ambalo liliitaka mahkama ya nchi hiyo kuwahukumu mashia wa nchi hiyo kwa mujibu wa fiqhi ya madhehebu ya Shia na haswa katika hukumu zihusianazo na mambo ya (Ndoa, Talaka na Mirathi), serikali mwanzoni ilikataa na kutupilia mbali ombi hilo, lakini kutokana na juhudi na ufuatiliaji wake mwishowe ombi hilo likakubalika. Kisha Marehemu Rizvi yeye mwenyewe akachukua jukumu la kuandika Ahkaam shaksiya kwa mujibu wa fiqhi ya madhehebu ya kishia na kuipatia serikali na hivi leo wafuasi wa Ahlul-baiti (a.s) huhukumiwa kwa mujibu wa kanuni, hukumu na sharia hii.

Utambuzi Wake wa Lugha Mbalimbali

Allamah Rizvi alikuwa ni mwenye ufahamu mzuri wa lugha mbali mbali kama vile kiurdu, Kifarisi, kiarabu, kiingereza, kishwahili, kihindi na kigujrati na mwishoni mwa umri wake alikuwa akijishughulisha na mafunzo ya lugha ya kihispania. Kwa hakika yeye akiitakidi kwamba ni lazima na ni jambo la dharura kwa mwanafuzni wa kihawza za kielimu kujifunza angalau lugha moja wapo katika ya lugha za kimataifa kwa ajili ya uenezaji na tablighi ya dini.

Safari za Kitabligh

Sayyid Said Akhtar Rizvi katika uwanja wa tabligh na uenezaji wa madhehebu ya Ahlul-baiti (a.s) kamwe hakujifunga na mipaka maalum ya kijografia. Kutokana na hili katika muda wote wa maisha yake yenye Baraka nyingi aliweza kutembelea na kusafiri kwenye nchi zaidi ya 30 za dunia kwa ajili ya kueneza Uislaam na kusambaza Maktaba ya Ahlul-baiti (a.s) na alifanya juhudi kubwa sana katika hilo.

Ijaza Mbalimbali Kutoka kwa Maraajiu Watukufu

Allamah Rizvi kutokana na nafasi yake, mara zote alikuwa ni mtu mwenye kutiliwa umuhimu na Maulamaa na Maraajiu wa daraja ya kwanza wa Najaful- ashraf na mji mtukufu wa Qom hadi kufika hatua ya maraji'i wengi wakubwa wa Taqliid wa ulimwengu wa kishia kumpatia Ijaza ya upokezi wa riwaya kutoka kwao, na utoaji wa hukumu pia usimamiaji wa mambo ya Hisbiyah ambayo utekelezaji wake hutegemea udhini na ruhusa ya Haakimus-shar'ii na mujtahidi alie timiza vigezo na miongoni mwa Maraaji'i walio mpatia ijazah hizo ni:

  • Ayatullah Sayyid Muhsin Hakiim.
  • Ayatullah Sayyid Abul-qaasim Khui.
  • Ayatullah Sayyid SHahabud-dini Mar'ashi Najafiy.
  • Ayatullah Sayyid Muhammad Rouhani.
  • Ayatullah Sayyid Abdul-aalaa Sabziwaari
  • Ayatullah Sayyid Muhammad ridhaa Golpaigani
  • Ayatullah Sheikh Muhammad Ali Araaki
  • Ayatullah Mirzaa Jawaad Tabriizi
  • Ayatullah Wahiid Khorasaani
  • Ayatullah Sayyid Ali Huseiniy Sistaani
  • Ayatullah Lutfullahi Swaafi Golpaogani

Athari na Vitabu Vyake (Tungo Zake)

Allamah Rizvi pamoja na harakati na shughuli nyingi za kitamblighi na kitamaduni, kamwe hakuacha kazi ya uandishi na utafiti na aliendelea kutumia kalamu yake katika kueneza maarifa ya Ahlul-baiti (a.s), kwani hata katika orodha ya kazi zake kuna Utunzi wa vitabu, tarjama na usambazaji pia uchapishaji wa makumi ya anwani za vitabu vya thamani vya kiarabu, kiingereza na Urdu. Na baadhi ya athari za mwanazuwoni huyu mkubwa wa kishia ni kama zifuatazo:

  • Uimamu, na kuna vituo mbali mbali vimekitarjumi kitabu hiki katika lugha mbalimbali na kukisambaza kwa lugha ya Urdu, Kiswahili, Boznia, Gujrati, kihindi na kiarabu.
  • Qur'an tukufu na tatizo la Akhbari na hadithi za Ahaad.
  • Mas'ala ya Badaa
  • Haja ya kuwepo Madhehebu
  • Mashia na Ushia.
  • Mashia Khoja ithnaa ashria Afrika mashariki
  • Itambue Karbala
  • Uombolezaji na bida'ah
  • Tarjama ya baadhi ya juzuu za tafsirul-miizaan cha Allamah Twabatwabai kwa lugha ya Kiingereza.

Kuaga Kwake Dunia

Mwishowe Allamah Rizvi baada ya kuishi na kukaa kwake katika nchi ya Tanzania miaka 43 mnamo tarehe 20 Juni mwaka 2002 A.D aliiaga dunia akiwa na umri wa miaka 76 katika mji wa Dar-es-Salaam mji mkuu wa nchi hii. Na mwili wa Muballighi huyu mkubwa wa Kishia baada ya usindikizaji mkubwa wa jeneza ukalazwa na kuzikwa katika makaburi ya Mashia katika mji wa Dar-es-salaam.

Kufuatia kifo cha mwana jihadi huyu asiye choka, shakhsiya mbalimbali na viongozi mbalimbali wa Kishia walitoa na kutuma salamu zao za rambi rambi kwa jamii ya Kishia wa Tanzania kufuatia kifo cha mwanazuwoni huyu na kudhihirisha masikitiko yao makubwa kufuatia msiba huu mkubwa.