Azar

Kutoka wikishia

Azar (Kiarabu: آزَر) ni jina lililokuja katika Qur’an Tukufu na limetajwa kuwa ni la baba au msimamizi wa Ibrahim. Kuhusiana na hili, Qur’an imetumia neno «اب» yaani baba. Wafasiri na wanazuoni wa Kishia wanaamini kwamba, kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa kutoka kwa Bwana Mtume (s.a.w.w) babu yeyote miongoni mwa mababu wa Mtume mpaka kwa Nabii Adam hapaswi kuwa mshirikina. Hivyo basi Azar ambaye alikuwa mshirikina hawezi kuwa baba wa Ibrahim na kwa msingi huo, neno «اب» yaani baba katika Aya hii lina maana nyingine isiyokuwa ya baba, kama vile amu au babu mzaa mama.

Kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa kutoka kwa Imam Swadiq (a.s) ni kuwa, Azar alikuwa mnajimu na mtabiri wa Nimrud ambaye alitabiri kwamba, atazaliwa mtoto ambaye atawaita na kuwalingania watu dini nyingine. Kutokana na utabiri huo, Nimrud alitoa amri ya kutenganishwa wanawake na wanaume na watoto wachanga wauawe. Kadhalika Azar ametambulishwa kuwa ni binamu yake Ibrahim.

Utambuzi wa shakhsia

Azar asili yake ni kijiji cha al-Kawthi huko Sawad (mji wa Kufa hii leo) [1] na ametambulishwa kuwa binamu yake Nimrud. [2] Kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa kutoka kwa Imam Swadiq (a.s) ni kuwa, Azar alikuwa mtabiri wa Nimrud [3] na alitabiri kuhusu Ibrahim (a.s) kabla ya kuzaliwa kwake ya kwamba, atazaliwa atazaliwa mtoto ambaye atawaita na kuwalingania watu dini nyingine. Kutokana na utabiri huo, Nimrud alitoa amri ya kutenganishwa wanawake na wanaume na watoto waliokuwa wakizaliwa wauawe. [4]

Azar alikuwa muabudu masanamu [5] na katika baadhi ya mashairi ya kifarsi kumeashiriwa kuabudu kwake masanamu. [6]

Ni baba au ami yake Ibrahim

Imekuja katika Aya ya 74 ya Surat al-An’am kwamba:

((وَإِذْ قَالَ إِبْرَاهِيمُ لِأَبِيهِ آزَرَ أَتَتَّخِذُ أَصْنَامًا آلِهَةً إِنِّي أَرَاكَ وَقَوْمَكَ فِي ضَلالٍ مُّبِينٍ ; Na pale Ibrahim alipo mwambia baba yake, Azar: Unayafanya masanamu kuwa ni miungu? Hakika mimi nakuona wewe na watu wako mmo katika upotofu ulio wazi)).

Baadhi ya wafasiri wa Qur’an akiwemo Fakhru Razi wamemtambua Azar kuwa ni baba wa Ibrahim kwa mujibu wa Aya hii. [8] Lakini imekuja katika Tafsir Nemooneh ya Makrim Shirazi kwamba, wafasiri wote na wanazuoni wa Kishia wanaamini kwamba, Azar hakuwa baba wa Ibrahim. [9]

Sheikh Tusi (aliyefariki dunia mwaka wa 460 AH) amemtambua Azar kuwa ni ami au babu mzaa mama wa Ibrahim (a.s) na amenukuu kutoka kwa Abu Is’haq al-Zajjaj kwamba watambuzi na wataalamu wa nasaba hawajatofautiana kuhusiana na kwamba, jina la baba yake Ibrahim lilikuwa Terah. [10] Pia ametumia kama hoja riwaya kutoka kwa Mtume ambayo kwa mujibu wake ni kwamba hakuna hata mmoja wa mababu wa Mtume mpaka Adam ambaye alikuwa mshirikina; [11] hii ni katika hali ambayo, Azar alikuwa mshirikina na kwa hivyo haiwezekani kuwa alikuwa baba wa Nabii Ibrahim (a.s). [12]

Allama Tabatabai, mwanafalsafa na mfasiri wa zama hizi, sambamba na kuwasilisha ushahidi kwamba kwa Kiarabu, “اب” maana yake ni mtu ambaye anasimamia mambo ya mtu; anasema kuwa, kwa hiyo neno hili hutumika kwa: Amu, babu, baba mkwe, (baba wa mke) na hata mkuu na mzee wa kabila huitwa kwa kwa jina la “اب” yaani baba. [13] Katika Torati, kitabu kitakatifu cha Wayahudi, baba yake Nabii Ibrahimu ametajwa kuwa ni Terah. [14] Baadhi ya wanachuoni wa maadili pia wamesimulia hadithi kwa namna ya hadithi iliyogawanyika ambayo madhumuni yake ni kwamba kuna aina tatu za baba. Baba mzazi, baba ambaye anampa mtu mke (baba mkwe) na baba anayewajibika na kusimamia elimu yake (mwalimu). [15] Pia, baadhi ya wafasiri, akiwemo Allama Tabataba'i na Makarim Shirazi kutokana na, kukataa Ibrahim kumuombea msamaha "baba" yake katika Aya ya 114 ya Surah Tawba [16] na, kwa upande mwingine, kuomba msamaha kwa ajili ya "Walid" yaani mzazi wake katika Aya 41 ya Sura Ibrahim,[17] wamefikia natija hii kwamba, baba wa Ibrahim ni mtu mwingine na si Azar na «أب» yaani baba iliyokuja katika Aya tunayoizungumzia ina maana ya amu au babu mzaa mama. [18]

Ibrahim amuombea msamaha Azar

Kwa mujibu wa Aya ya 48 ya Surat Maryam [19], Nabii Ibrahim (a.s) alimuombea msamaha na maghufira Azar; [20] lakini katika Aya ya 113 ya Surat Tawba [21] Mwenyezi Mungu anawatahadharisha Waislamu kuhusiana na kuwatakia msamaha washirikina. Qur’ani ikiwa na lengo la kuondoa mgongano wa kiakili ambao unajitokeza katika hili inaeleza katika Aya inayofuata ya kwamba:

Wala haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake ila kwa sababu wa ahadi aliyo fanya naye. Lakini ilipo mbainikia kwamba yeye ni adui ya Mwenyezi Mungu, alijiepusha naye. Hakika Ibrahim alikuwa mwingi wa kuomba, mnyenyekevu, mvumilivu. [22]

Vyanzo

  • Balʾamī, Muḥammad. Tārikhnama Ṭabarī. Edited by Muḥammad Rawshan. Second edition. Tehran: Surūsh, 1378 Sh.
  • Fakhr al-Rāzī, Muḥammad b. al-ʿUmar al-. Mafātīḥ al-ghayb (al-Tafsīr al-Kabīr). Third edition. Beirut: Dār Iḥyāʾ al-Turāth al-ʿArabī, 1420 AH.
  • Khwaja ʾAbd Allāh Anṣārī. Munājātnāma. Edited by Muḥammad Ḥammaṣiyān. Kerman: Intishārāt-i Khadamāt-i Farhangī Kirmān, 1382 Sh.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī & Muḥammad Ākhūndī. Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmīyya, 1407 AH.
  • Makārim Shīrāzī, Nāṣir. Tafsīr-i nimūna. First edition. Tehran: Dār al-
  • Muṣṭafawī, Ḥasan. Al-Tahqīq fī kalimāt al-Qur'ān al-karīm. Tehran: Bungāh tarjuma wa nashr-i kitāb, 1360 Sh.
  • Qummī, ʿAlī b. Ibrāhīm al-. Tafsīr al-Qummī. Edited by Ṭayyib Mūsawī Jazāʾrī. Qom: Dār al-Kitāb, 1367 Sh.
  • Ṭabarī, Muḥammad b. Jarīr al-. Jāmiʾ al-bayān ʿan taʾwīl āyāt al-Qurʾān. First edition. Beirut: Dar al-Ma'rifa, 1412 AH.
  • Ṭabāṭabāʾī, Sayyid Muḥammad Ḥusayn al-. Al-Mīzān fī tafsīr al-Qurʾān. Fifth edition. Qom: Daftar-i Intishārāt-i Islāmī , 1417 AH.
  • Ṭurayḥī, Fakhr al-Dīn b. Muḥammad al-. Majmaʿ al-baḥrayn. Edited by Sayyid Ahmad Husayni. Tehran: al-Maktaba al-Murtaḍawīyya, 1375 Sh.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Al-Tibyān fī tafsīr al-Qurʾān. Edited by Aḥmad Qaṣīr al-ʿĀmilī. Beirut: Dār Iḥyāʾ al-Turāth al-ʿArabī, [n.d].
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Al-Amālī. Edited by Muʾassisat al-Biʿtha. Qom: Dār al-Thiqāfa li-ṭibaʿat wa al-Nashr wa al-Tawzīʿ, 1414 AH.