Wajib al-Wujud

Kutoka wikishia

Wajib al-Wujud (Kiarabu: واجب الوجود) ni uwepo ambao kuweko kwake ni wajibu na hauhitaji kitu kingine chochote katika uwepo wake. Kielelezo na mfano pekee wa Wajib al-Wujud ni Mwenyezi Mungu. Wanafalsafa wa Kiislamu wakitumia dalili na hoja kama Burhan Siddiqin na Burhan Imkan Wal-Wujub kwa ajili ya kuthibitisha uwepo wa Wajib al-Wujud.

Baadhi ya sifa maalumu za Wajib al-Wujub ni: Kutokuwa na kiini (utambulisho), kutokuwa na mpaka, kutokuwa na mchanganyiko au sehemu ya kitu, tauhidi ya dhati (asili), tauhidi ya uungu, kuwa na uhai, kuwa mjuzi wa wote, kuwa na uwezo na uumbaji.

Mgwanyo wa vilivyopo katika Wajib al-Wujud na Mumkin al-Wujud

Kwa mujibu wa mtazamo wa wanafalsafa wa Kiislamu, kila kilichopo tunapokizingatia tunakutana kwamba, hakitoki kati ya hali mbili hizi; ima kiwe uwepo wake ni Wajib al-Wujud au Mumkin al-Wujud. Iwapo kuwepo ni muhimu kwa asili ya kitu hicho, huitwa Wajib al-Wujud, na ikiwa kuwepo au kutokuwepo sio lazima kwa asili yake, inaitwa Mumkin al-Wujud (Uwepo wa Uwezekano) [1] Kwa mtazamo wa Muhammad Taqi Misbah Yazdi, mmoja wa mujtahid na wanafalsafa wa Kishia wa zama hizi, wajib al-wujud ni uwepo, ambao upo wenyewe na hauhitaji kitu kingine. Mkabala na uwepo huo kuna Mumkin al-Wujud ambao kuwepo ni wake wenyewe kwa maana kwamba, haujitegemei katika kuweko kwake yaani kuwepo kwake kunategemea uwepo mwingine. [2] Mulla Hadi Sabzevari, mwana irfan na mwanafalsafa wa Kishia wa karne ya 13 Hijiria, na Murtadha Mutahhari, mwanafalsafa wa Kishia na mwanateolojia wa karne ya 14 Hijiria Shamsia, wanasema kuwa, Wajib al-Wujud na Mumkin al-Wujud ni jambo la wazi ambalo halihitajii fasili na utoleaji maana au ufafanuzi. [3]

Hoja za kuthibitisha Wajib al-Wujud

Katika falsafa ya Kiislamu kumetumiwa dalili na hoja nyingi za kuthibitisha Wajib al-Wujud au Mwenyezi Mungu. [4] Na baadhi wanatambua kuwa, Burhan Siddiqin kuwa ni hoja na dalili imara kabisa kwa ajili ya kuthibitisha Wajib al-Wujud.; [5] hata hivyo hoja hii imebainishwa kwa sura na kwa ujengeaji hoja tofauti. [6] Ujengeaji hoja uliofanywa na Ibn Sina, Mulla Sadra, Mulla Hadi Sabzevari na Allama Tabatabai ni miongoni mwa hoja hizo. [7]

Kwa mujibu wa “Burhan Imkan wal Wujub” (hoja ya uwezekano na wajibu) kila uwepo kwa mujibu wa akili ima ni wajibu au unawezekana (Mumkin al-Wujud na Wajib al-Wjud) na haiwezekani kujaalia hilo nje ya hali hizi mbili. Haiwezekani kuvitambua kila vilivyoko duniani kwamba, uwepo wake unawezekana (Mumkin al-Wujud); kwa sababu Mumkin al-Wujud unahitajia sababu ili uweze kuwepo na sababu yake kama ni yenyewe hiyo Mumkin al-Wujud, nayo inahitajia sababu. Kama sababu zote zitakuwa ni Mumkin al-Wujud na vikawa vinahitajia sababu, hakuna wakati ulimwenguni ambapo atapatikana kiumbe. Kwa muktadha huo, kuna ulazima wa kuweko uwepo mwengine ambao hauhitajii uwepo mwingine nao ni Wajib al-Wujud (Mwenyezi Mungu). [8]

Sifa maalumu za Wajib al-Wujud

Katika vitabu vya falsafa kumebainisha sifa mbalimbali za Wajib al-Wujud. Baadhi yazo ni:

  • Kutokuwa na kiini (utambulisho): Wajib al-Wujud hauna kiini au utambulisho.
  • Hoja: Kiini au utambulisho ni kwamba, hiyo hali ya uwepo yenyewe yaani yenyewe kama yenyewe haina udharura wa uwepo wala udharura wa kutokuweko na hii maana yake ni kuwa na ulazima (kufuatana kwa lazima) na Mumkin al-Wujud). Kwa msingi huo kile ambacho kina kiini na utambulisho ni Mumkin al-Wujud na kila ambacho sio Mumkin al-Wujud, hakina kiini. Kwa muktadha huo, Wajib al-Wujud hauna kiini. [9] Murtadha Mutahhari, mwanafalsafa wa Kishia wa zama hizi anaamini kwamba, ibara ya Imamu Ali (a.s) aliyosema: لیس لذاته حدّ (dhati yake haina mpaka) inabainisha kwamba, uwepo wa Mwenyezi Mungu hauna mpaka na hivyo tunapata natija kwamba, kujaalia kiini kwa Mwenyezi Mungu ni kitu ambacho haikukabili. [10]
  • Kutokuwa na mpaka: Wajib al-Wujud hauna mpaka wowote ule.
  • Hoja: Kwa kuwa Wajib al-Wujud hauna kiini haina pia mpaka; kwani kiini kinabainisha mpaka na kuianisha daraja ya uwepo. [11] Murtadha Mutahhari amefasiri “kutokuwa na mpaka” kuwa ndio ile uwepo kuwa mutlaki. [12]
  • Kutokuwa na mchanganyiko au sehemu ya kitu: Wajib al-Wujud sio kitu kilichoundwa kutokana na vitu kadhaa na wala sio sehemu ya kitu yaani mchanganyiko na haina viambajengo vyovyote vya nje, kiakili, halisi au vinavyowezekana.
  • Hoja ya kwanza: Kwa vile Wajib al-Wujud hauna kiini, haukubali mipaka yoyote; kwa hiyo, haina jinsi au msimu. Kila kitu ambacho hakina jinsi na msimu hakina sehemu. [13]
  • Hoja ya pili: Kila chenye muundo na mchanganyiko kinahitaji vipengele vyake katika utambuzi wake na katika kuundika kwake. Ni dhahiri kwamba, kuwa mhitaji kunakinzana kabisa na kuwa Wajib al-Wujud kwa dhati yake. Kwa hiyo, kila ambacho kinajumuisha (chenye mchanganyiko) kinawezekana yaani ni Mumkin al-Wujud. Kwa hivyo Wajib al-Wujud sio mchanganyiko. [14]
  • Tauhidi ya dhati (asili): Wajib al-Wujuud ni uwepo mmoja na hauna mshirika.
  • Tauhidi ya uungu: Sababu pekee ya kukua na kukamilika viumbe, au kwa maneno mengine msimamizi na muongozaji wa ulimwengu ni Mwenyezi Mungu.
  • Hoja: Ulimwengu ni mjumuiko wa vitu vyenye uhusiano baina yao na vyenye kuhitaji; yaani baina ya vipengee na viungo vyake kuna uhusiano wa sababu na kisababishi; kwa msingi huo kukua na kukamilika kila kiumbe kuna sababu ndani yake; na sababu ile ina sababu mpaka kufikia katika Wajib al-Wujud ambaye ni sababu ya sababu zote. Kwa kuzingatia kwamba, kila sababu ya kila kitu kuna sababu yake pia, Wajib al-Wujud unapaswa kuwa sababu kuu ya kukua, kukamilika na kuongoza na kusimamia viumbe wote. [16]

Miongoni mwa sifa za Wajib al-Wujud ni kuwa hai, kuwa mjuzi, uwezo, uumbaji na kuruzuku.[17]Imesemekana kwamba kwa mujibu wa kanuni "Wajib al-Wujud kwa dhati yake, ni Wajib-ul-Wujud katika nyanja na pande zote", sifa zote za uzuri na utukufu wa Mungu zinaweza kutolewa natija. [18] Allama Hilli katika Kashf al-Murad, akifuatia Muhaqqiq Tusi katika maandishi ya kitabu cha Tajirid al-I’tiqad amefikia natija hii kwamba, sifa nyingi za kimungu zimetokana na Mwenyezi Mungu kuwa ni Wajib al-Wujub. [19]

Vyanzo

  • Ḥillī, al-Ḥasan b. Yūsuf al-. Kashf al-murād fī sharḥ tajrīd al-iʿtiqād. Edited by Ḥasan Ḥasanzāda Āmulī. Qom: Muʾassisat al-Nashr al-Islāmī, 1413 AH.
  • Ibn Sinā, Ḥusayn b. ʿAbd Allāh. Al-Shifāʾ. Qom: Nashr-i Kitābkhāna-yi Marʿashī Najafī, 1404 AH.
  • Jawādī Āmulī, ʿAbd Allāh. Tabyīn-i barāhīn-i ithbāt-i Khudā. Qom: Markaz-i Nashr-i Asrāʾ, 1378 Sh.
  • Khoeī, Mīrzā Ḥabīb Allāh l-. Minhāj al-barāʿa fī Sharḥ Nahj al-balāgha. Tehran: Maktaba al-Islāmīyya, 1400 AH.
  • Misbāḥ Yazdī, Muḥammad Taqī. Āmuzish-i ʿaqāʾid. Second edition. Tehran: Shirkat-i Chāp wa Nashr-i Bayn al-Milal (affiliated with Islamic Development Organization), 1384 Sh.
  • Muṭahharī, Murtaḍā. Majmūʿa-yi āthār. Qom: Intishārāt-i Ṣadrā, 1389 Sh.
  • Muṭahharī, Murtaḍā. Sharḥ-i manẓūma. Tehran: Ṣadrā, 1394 Sh.
  • Muṭahharī, Murtaḍā. Tawḥīd. Tehran: Ṣadrā, [n.d].
  • Rabbānī Gulpāygānī, ʿAlī. Burhān-i imkān dar andīsha-yi fīlsūfān wa mutakallimān. Published in Kalam-i islami quarterly, no. 97, 1395 Sh.
  • Subḥānī, Jaʿfar. Madkhal-i masāʾil-i jadīd-i kalāmī. Qom: Muʾassisa Imām Ṣādiq (a), 1375 Sh.
  • Ṭabāṭabāʾī, Sayyid Muḥammad Ḥusayn al-. Nihāyat al-ḥikma. Edited by Ghulamrida Fayyadi. Qom: Muʾassisah-yi Imām Khomeini, 1386 Sh.