Ukombozi wa Mji wa Makka

Kutoka wikishia
(Elekezwa kutoka Ukombozi wa Makka)
Picha ya jeshi la Waislamu kabla ya kukombolewa kwa Makka katika kitabu Sirat al-Nabi, ambacho kilitayarishwa katika karne ya 11 kwa amri ya Sultan Murad III, mtawala wa Ottoman, na Sayyid Suleiman Kasim Pasha.

Ukombozi wa mji wa Makka (kiarabu: فتح مكة) ni mojawapo ya vita muhimu zaidi vya bwana Mtume (s.a.w.w) ambapo mji wa Makka ulikombolewa mnamo mwaka wa 8 Hijria. Kupitia ushindi wa Makka hadi mwaka wa 10 Hijria, makabila mengi ya Bara Arab (Saudia Arabia ya sasa) yalishika Uislamu na Uislamu ukatawala na kupata nguvu katika ndani yake. Vita hivi vilijiri kama ni majibu dhidi ya uvunjaji wa mkataba wa Hudaibiya uliofanywa makabila la Kiquraishi.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) kwa busara na mkakati wake, aliukomboa mji wa Makka bila kumwaga damu, bali kwa kutumia mbinu za kushitukizia na kuwazukiwa watu wa mji huo bila ya wao wenyewe kuelewa namna ya shambulio hilo lilivyoshika nafasi. Bwana Mtume (s.a.w.w) katika ukombozi wa mji wa Makka alitangaza msamaha wa jumla jamala kwa kauli mbiu isemayo: "Leo ni siku ya huruma (msamaha)", na akawasamehe watu wote wa mji huo isipokuwa wachache tu, kama vile Ikrama bin Abu Jahli, Safwan bin Umayya, na Hind binti Utba.

Kulingana na baadhi ya ripoti, baada ya ushindi na ukombozi wa Makka, kwa pendekezo la bwana Mtume (s.a.w.w), Ali (a.s) alipanda mabegani mwa bwana Mtume (s.a.w.w), na kuvunja masanamu, yaliyo wekwa kwenye mlango wa Bani Shayba (moja ya milango ya Msikiti wa Makka). Pia, bwana Mtume (s.a.w.w), alituma vikosi kwenda maeneo ya karibu na Makka ili kuvunja nyumba za masanamu. Kupitia ushindi na ukombozi wa mji wa Makka, mikataba, makubaliano na nyadhifa zote zilifutwa, isipokuwa huduma ya kuhudumia Kaaba na ugawaji wa maji kwa mahujaji.

Umuhimu wa Ushindi wa Makka katika Historia ya Uislamu

Vita vya Ushindi wa Makka vinaelezwa kuwa mojawapo ya matukio muhimu zaidi katika historia ya Uislamu wa awali, ambapo utawala wa washirikina huko Makka ulimalizika na Uislamu ukatawala Jaziiratul-Arab. [1] Baada ya ushindi wa Makka hadi mwaka wa 10 Hijria, makabila mengi ya Bara Arab yaliingia katika Uislamu na nguvu za washirikina zikafifia barani humo. [2] Muhammad-Hussein Tabatabai na Nasir Makarim Shirazi, ambao ni miongoni mwa wafasiri wa Kishia, wamelinganisha ushindi huu na Surat Al-Nasr, na wakasema kwamba; vita hivi vilileta ushindi mkubwa mno kwa bwana Mtume (s.a.w.w), ushindi ambao ulisababisha kufutwa kwa ushirikina ndani ya Bara Arabu, na hatimae watu wakaingia katika Uislamu makundi kwa makundi. [3]

Katika vita hivi, Mtume (s.a.w.w) aliweza kuukomboa mji wa Makka bila kumwaga damu na bila kumdhuru mtu yeyote yule mjini humo. [4] Kulingana na maelezo ya Sayyid Jafar Shahidi, mwandishi wa kitabu cha Taarikh Tahlilily Islam (Tarehe Chambuzi ya Uislamu), ni kwamba; Namna ambayo Mtume (s.a.w.w) aliamiliana na watu wa Makka, ilionesha upole na huruma za Uislamu pamoja na ukarimu wa bwana Mtume (s.a.w.w) kwa wapinzani wake, hasa ukikumbuka namna ya makabila ya Waquraishi yalivyo mtesa bwana Mtume (s.a.w.w) na wafuasi wake kwa muda wa miaka ishirini, ambapo hata Waquraishi wenyewe walikuwa wakihofia kisasi kutoka kwa bwana Mtume (s.a.w.w), kutokana na matendo yao dhidi ya Waislamu. [5]

Sababu ya Uvamizi Huo wa Kijeshi

Makala Asili: Sulhu al-Hudaibiyah
Muhuri wa ukumbusho wa kukombolewa kwa mji wa Makka

Uvunjaji wa mkataba wa Hudaibiya uliofanywa na makabila ya Waquraishi ndiyo sababu kuu ilimfanya bwana Mtume (s.a.w.w) kuelekeza jeshi lake mjini Makka, na hatimae kuukomboa mji huo. [6] Mnamo mwaka wa sita Hijria, Waislamu na washirikina wakiwa katika eneo la Hudaibiya, walitilana mkataba wa amani utakaudumu kwa muda wa miaka kumi bila kushambuliana. [7] Hapo awali kabila la Bani Khuza’a lilikuwa liliungana na Waislamu, na kabila la Bani Bakar lilkaungana na Waquraishi. [8] Katika vita vilivyotokea mnamo mwaka wa nane Hijiria kati ya makabila haya mawili, Waquraish wakisaidia upande wa kabila la Bani Bakrwalifanikiwa kuwaua baadhi ya watu wa kabila la Bani Khuza’a. [9] Hiyo ikawa ndiyo sababu ya Waquraishi kuvunja mkataba wa amani wa Hudaibiya baada ya kipindi kisicho zidi miaka miwili. [10] Ingawa baada ya hapo Abu Sufyan alikwenda Madina kuomba msamaha, ila ombi lake hilo halikukubaliwa. [11] Muda mchache baada ya hapo, bwana Mtume (s.a.w.w) aliongoza jeshi la watu elfu kumi kuelekea mjini Makka. [12]

Ushindi wa Waislamu Bila Kumwaga Damu

Mchoro wenye kumuonesha Bilal Habashi akitoa adhana ndani ya mji wa Makka katika kitabu cha Sira ya Mtume.

Kwa mujibu wa maelezo ya wanahistoria, ni kwamba; Mtume (s.a.w.w) aliweza kuukomboa mji wa Makka bila kumwaga damu, bali aliweza kufanikisha kazi hiyo kwa kutumia busara na mikakati yake ya hekima. [13] Kwa amri ya bwana Mtume (s.a.w.w), monamo tarehe 10 Ramadhani mwaka wa 8 Hijria, jeshi la Waislamu liliondoka mjini Madina, [14] likizingatia kanuni ya kuwashitukizia maadui zao bila wao hajafikiria na kupata nafasi yakujihami. [15] Hata kwa wanajeshi wa Kiislamu pia halikujua kituo kikusudiwacho na msafara wa jeshi hilo. [16] Hadi jeshi lilipofika Marru al-Dhahraan (ambalo kwa sasa ni Bonde la Fatima, ambalo ni kilomita 24 kutoka Makka), [17] bado wakaazi wa Makka na wapelelezi wao hawakuwa na habari kuhusu harakati za jeshi la Kiislamu. [18] Ila baada ya Abu Sufyan kufahamu juu ya uwepo wa jeshi la Kiislamu karibu na jiji la Makka, bwana Mtume (s.a.w.w) alimtaka Abbas bin Abdul Muttalib, alimpeleka Abu Sufyan kwenye bondeni ili aweze kuona ukubwa wa jeshi Waislamu, [19] na hivyo aondoe kabisa mawazo ya upinzani wa kupambana na Waislamu hao. Alifanya hivyo ili Makka iweze kukombolewa bila vita. [20] Hatimae Abu Sufyan akaja mbele ya bwana Mtume (s.a.w.w) na akasilimu. [21]

Kulingana na baadhi ya ripoti, Waislamu walifanikiwa kuukomboa mji wa Makka mnamo tarehe 20 Ramadhani wakitumia kauli mbiu isemayo: "Nahnu ʿIbadu Allahi Haqqan Haqqa / Sisi kweli ni watumishi wa Mungu." [23] Hata hivyo, wanahistoria wana mawazo tofauti kuhusiana na siku halisi ya kuingia kwa Waislamu mjini Makka, ambapo wanahistoria wengine wametaja tarehe tofauti, ila zote zinahusiana na kipindi hicho hicho cha mwezi wa Ramadhani. [24] Bwana Mtume (s.a.w.w) aliwahakikishia usalama wale wote waliokuwa ndani ya Msikiti wa Makka, waliokuwa ndani ya nyumba ya Abu Sufyan, pamoja na wale waliobaki majumbani mwao wakisubiri hatima zao. [25] Katika siku ya ushindi wa Makka, hakukuwa na Mwislamu yeyote yule aliyeuawa isipokuwa watu wawili waliopotea njia, ambao ni Kurzu bin Jabir [26] na Khunais bin Khalid al-Ash'ari [27] (au Khalid al-Ash'ari), [28] ambao walipitia njia nyingine na hatimae kuuawa na washirikina njiani. [29]

Msamaha Mkuu

Baada ya kuingia Makka, bwana Mtume (s.a.w.w) alitangaza msamaha mkuu kwa wakazi wa mji huo, [30] kisha akawataka viongozi wa jeshi lake kuepuka vita na umwagaji damu, na kukabiliana tu na wale waliokusudia vita mingoni mwa wakazi hao. [31] Sa'ad bin 'Ubada, aliyekuwa amebeba bendera ya jeshi la Waislamu, alinadi akisema: «الْيَوْمُ يَوْمُ الْمَلْحَمَة ; Leo ni siku ya kisasi», jambo ambalo lililowatia khofu wakaazi wa Makka. [32] Kauli hiyo ya Sa'ad ilimkasirisha sana bwana Mtume (s.a.w.w), [33] naye akakabiliana nayo kwa kauli mbiu isemayo: «الْيَوْمَ يَوْمُ الْمَرْحَمَة ; Leo ni siku ya kuhurumiana». [34] Kisha akaichukua bendera ilioko mokononi mwake na kukabidhisha ima mikononi mwa Imam Ali (a.s) [35] au kwa mwana wa Sa'ad. [36] Bwana Mtume (s.a.w.w) hakuwachukwa watu wa Makka na kuwageuza watumwa, bali aliwaachia huru na kuwaita «طُلَقاء ; Tulaqaa» (walioachiliwa huru). [37] Hiyo ndiyo sababu hasa ya Abu Sufyan pamoja na watu Makka kuitwa Tulaqa, kwa maana ya watu waioachiwa huru. [38] Baadhi ya watafiti wanasema kwamba; neno "Tulaqaa" lilikuwa na maana ya aibu kwa sababu ya kule wakaazi wa Makka kulazimishwa kumkubali Mtume (s.a.w.w) kwa shingo upande. [39] Kufuatia ukombozi wa mji wa Makka, Mtume (s.a.w.w) alifuta mikataba, makubaliano, na nyadhifa zote zilizokuwa zikishikiliwa na watu mbali mbali, isipokuwa huduma ya Kaaba na ugawaji wa maji kwa mahujaji (« سِقایَةُالحاجّ ; siqayatu al-hajj) peke yake. [40]

Walioachwa Nje ya Msamaha Mkuu

Bwana Mtume (s.a.w.) aliwavua baadhi ya watu na kuwaweka nje ya msamaha mkuu, na akaamuru wauawe hata kama wangekuwa wamejificha chini ya pazia la Kaaba. [41] Idadi ya watu hawa haijatajwa kwa uwazi katika vyanzo vya kihistoria, badala yake kumetajwa orodha tofauti kuhusiana na idadi yao. Ila idadi kubwa zaidi iliyo tajwa kuhusiana na watu hao, ilikuwa ni jumla ya watu ishirini. [42] Majina ya baadhi ya watu hawa, kama ilivyoorodheshwa na Sayyid Jafar Murtadha Amili katika kitabu chake Al-Sahih Min Sirati Al-Nabi Al-A’adham, ni kama ifuatavyo: [43]

Wanaume

  • Ikrimatu bin Abi Jahl: Aliye kimbia Makka kabla ya Waislamu kuingia mji huo; ila mkewe, ambaye alikuwa tayari ameshakuwa Mwislamu, alikwenda kwa bwana Mtume (s.a.w.w) na kumwombea msamaha mumewe kupitia heshima yake. [44]
  • Safwan bin Umayya: Aliye kimbia kutoka mji Makka; lakini baada ya Umair bin Wahb kumwombea msamaha, alirudi kwa bwana Mtume (s.a.w.w). Alipofika alimwomba bwana Mtume (s.a.w.w) muhula wa miezi miwili ili aweze kusilimu, na bwana Mtume (s.a.w.w) akakubali kumpa muhula huo. Hatimae baada ya kumaliza kipidi cha muhula huo Safwan bin Umayya alisilimu kwa hiari yake mwenyewe. [45]
  • Abdullah bin Abi Sarh: Othman bin Affan, ambaye alikuwa kaka wa kambo wa Abdullah, ndiye aliye mwombea msamaha Abdullah bin Abi Sarh kwa bwana Mtume (s.a.w.w). [46]
  • Abdullah bin Khatal: Aliuawa baada ya yeye kusilimu kwake, hii ni baada ya kuritadi, [47] na kumuua moja kati ya Waislamu, jambao ambali lilipelekea ya kuvamiwa na Waislamu na kuuliwa akiwa karibu na Kaaba. [48]
  • Muqis bin Sabaata: Yeye alikuja kumuua mmoja wa Waislamu kisha akaritadi, jambao ambalo lilipelekewa Naimah bin Abdullah al-Kinani kukabiliana naye, na hatimae kuumua. [49]
  • Wahshi bin Harb: Aliyekuwa muuaji wa Hamza bin Abdul-Muttalib, ami yake bwana Mtume. Yeye baada ya muda fulani, alikuja kwa bwana Mtume (s.a.w.w) na kusilimu. [50]

Wanawake

  • Hind bint Utba: Mama wa Muawiya, ambaye alipokuwa katika vita vya Uhud, alifanya ukatili wa kuchana tumbo la Hamza bin Abdul-Muttalib na kula ini lake. Yeye kwa wakati huu aliamua kujifunika uso wake na kusilamu yeye pamoja na wanawake wengine baada ya kuapa kiapo cha utiifu kwa kwa bwana Mtume (s.a.w.w). [51]
  • Sara, mjakazi wa Amru bin Hisham: Yeye kabla ya hapo alikuwa ni mpelelezi wa washirikina dhidi Waislamu. [52] Yeye alikuwa ni miongoni mwa waliouawa siku ya ukombozi wa mji wa Makka. [53]
  • Qariba na Fartana, wajakazi wawili wa Abdullah bin Khatal: Hawa wao walikuwa ni waimbaji waliokuwa wakimchafua bwa Mtume (s.a.w.w) kupitia nyimbo zao. [54] Qariba aliuawa, lakini Fartana alisilimu na akaendelea kulishi hadi enzi za ukhalifa wa Othman. [55]

Kuvunjwa kwa Masanamu

Makala Asili: Tukio la Kuvunja kwa Masanu
Mchoro wenye kuakisi Tukio la Uvunjaji wa Masanamu katika Kitabu cha Sira ya Mtume.

Ripoti kadhaa rimeripoti zikisema kwamba; Baada ya ushindi na ukombozi wa mji wa Makka, bwana Mtume (s.a.w.w) aliamua kuvunja miungu (masanamu) iliyopo juu ya paa la Kaaba. [56] Kwa pendekezo la bwana Mtume (s.a.w.w), Ali (a.s) alipanda juu ya mabega ya Mtume (s.a.w.w) na kuiporomosha chini miungu hiyo. [57] Kulingana na baadhi ya Hadithi ni kwamba; baada ya Imam Ali (a.s) kuporomosha sanamu la Hubal -sanamu kubwa na muhimu zaidi katika Msikiti wa Makka- kutoka juu ya Kaaba, walizika sanamu hilo kwenye mlango wa Bani Shayba (moja ya milango ya Msikiti wa Makka). [58] Baada ya ukombozi wa Makka, bwana Mtume (s.a.w.w) alituma vikosi vidogo viende sehemu mbalimbali za Makka, ili kubomoa nyumba za ibada ya masanamu. [59] Ilipofika mchana wa siku ya ukombozi wa Makka, Bilal Habashi, kwa amri ya bwana Mtume (s.a.w.w), alipanda juu ya Kaaba na kutoa adhana, jambo ambalo liliwasikitisha sana makafiri wa Makka. [60]

Rejea

Vyanzo