Nenda kwa yaliyomo

Shahrbanu

Kutoka wikishia

Shahrbanu (Kiarabu: شهر بانو) ni mama wa Imamu Sajjad (a.s). Wanahistoria na wapokezi wa hadithi wanasimulia kwamba, Shahrbanu ni binti wa Yazgerd III, mfalme wa mwisho wa ukoo wa Sasanian. Shahrbanu aliolewa na Imamu Hussein (a.s) baada ya Uislamu kuingia Iran na akafanikiwa kumzalia mumewe huyo mtoto aliyejulikana kwa jina la Sajjad. Hata hivyo kuna tofauti za kimitazamo kuhusiana na jina, nasaba, tarehe aliyoaga dunia, wakati wa kuingia kuingia kwake Madina na namna alivyoolewa na Imamu Hussein (a.s). Kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa katka kitabu cha Dalail al-Imamah (kilichoandikwa katika karne ya tatu Hijria) ni kwamba, Shahrbanu alichukuliwa mateka wakati wa kukombolewa ardhi mbalimbali za Waislamu katika zama za Omar bin al-Khattab na kupelekwa Madina na akaolewa na Imamu Hussein (a.s) baada ya kuachiliwa huru.

Ripoti mbalimbali za historia zinaonyesha kuwa, Shahrbanu aliaga dunia wakati wa kuzaliwa kwa Imamu Sajjad (a.s). Pamoja na hayo imeelezwa kuwa, yeye ni miongoni mwa waliokuweko katika tukio la Karbala, na baada ya kuuawa shahidi Imamu Hussein alisafiri na kuelekea katika mji wa Rey nchi Iran, akiwa huko alitoweka katika mmoja wa milima eneo hilo. Na ni kutokana na sababu hiyo ambapo eneo moja la mlima lililoko kusini mwa mlima Rey linanasibishwa naye. Eneo ambalo watu huenda kufanya ziara na kufanya ibada mbali mbali ndani yake. Kisa cha safari yake kutoka Karbala hadi mji wa Rey kinahisabiwa kuwa ni miongoni mwa mambo ya upotoshaji wa tukio la Ashura. Kadhalika baadhi ya wahakiki wamepinga eneo hilo linalonasibishwa naye na watu kwenda kufanya ziara mahali hapo.

Nasaba

Shahrbanu ni mama wa Imam Ali bin Hussein Zainul-Abidin (a.s). Sheikh Muhammad Hadi Yusuf Gharawi (aliyezaliwa 1327 Hijria Shamsia) ambaye ni mwanahistoria [1] anasema, mama wa Imam Sajjad (a.s) ni binti wa mfalme Yazgerd III, lakini kuna hitilafu za kimitazamo kuhusiana na jina lake. [2] Aidha kwa mujibu wa Ibn Shahrashub (aliyeaga dunia 588 Hijria) ni kwamba, mama wa Imam Sajjad (a.s) ni Shahrbanu binti wa Yazgerd III, lakini pamoja na hayo majina yake yaliyotajwa kwamba ni ya kwake ni Shah-i Zanan, Jahan, Sulafa, Khawla, Barra, Maryam na Fatma. [3] Katika vyanzo mbalimbali yametajwa majina kama Salama, [4] Shahrnaz, [5] Harar na Ghazzalah [6] kuwa ni majina yake pia. Kadhalika majina ya baba yake yametajwa kuwa ni Sobhan [7] na Noshjan [8]. Katika nukuu moja, mama wa Imam Sajjad (a.s) ametambulishwa kuwa ni kanizi (binti asiyekuwa Mwislamu aliyechukuliwa mateka katika vita baina ya Waislamu na makafiri) kutoka Kabul, Afghanistan. [9]

Jarullah Zamakhshari (aliyeaga dunia 538 Hijria) alimu na msomi wa Kisuni anasema: Imam Sajjad (a.s) alikuwa akiitwa kwa jina la Ibn al-Khayratein (mwana wa mtu mwenye kheri mbili) kutokana na kuwa, mama yake alikuwa akitokana na nasaba ya Yazgerd. [10]

Kuingia Madina na Kuolewa na Imamu Hussein (a.s)

Kuhusiana na kuingia Shahrbanu katika mji wa Madina na kuolewa na Imamu Hussein (a.s) kuna mitazamo kadhaa:

  • Katika zama za utawala wa Imamu Ali (a.s): Kwa mujibu wa hadithi zilizonukuliwa katika vitabu vya al-Irshad, [11] I’lam al-Wara, [12] Rawdhat al-Waidhin, [13] Tajul Mawaalid [14 na Kash al-Ghummah [15] ni kuwa, wafanyakazi wa Imamu Ali (a.s) huko mashariki (mashariki mwa ardhi za Kiislamu) walimtumia mabinti wawili wa Yazgerd. Imamu Ali (a.s) akamchukua binti mmoja na kumpatia Hussein (a.s) na mwingine akampatia Muhammad bin Abu Bakar.
  • Katika utawala wa Omar ibn al-Khattab: [16] Kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa katika kitabu cha Dalail al-Imamah (kilichoandikwa katika karne ya tatu Hijria) Shahrbanu alikuwa kanizi. Omar bin al-Khattab alitaka kumuuza binti huyo wa Yazeged; lakini Imamu Ali (a.s) akitegemea inayoelezea juu ya kutendewa wema watu wanaotoka katika kaumu zenye heshima alipinga hilo. Kisha akamtumia binti huyo kama hisa yake na kumuachilia huru katika njia ya Mwenyezi Mungu. Baada yake Bani Hashim na watu wengine wakafanya hivyo pia. Kwa msingi huyo wakampa binti huyo hiari ya kumchagua mtu awe mume wake, naye akamchagua Imamu Hussein (a.s) na hivyo akaolewa naye. [17] Kwa mujibu wa riwaya iliyosimuliwa katika Al-Kafi, Omar ibn al-Khattab alitaka kumchukua kwa ajili yake mwenyewe, lakini Imamu Ali (a.s) aliizuia.[18] Bila shaka, Murtaza Mutahari (aliyefariki mwaka 1358 Hijiria), mwanachuoni wa Kishia, hakuichukulia riwaya ya Al-Kafi kuwa ni sahihi; Kwa sababu wasimulizi wake wawili si wa kutegemewa kulingana na wanazuoni wa hadithi.[19]
  • Katika zama za ukhalifa wa Othman bin Affan: Kwa mujibu wa hadithi iliyonukuliwa katika kitabu cha Uyun Akhbar al-Ridha ni kuwa, tukio hili lilitokea katika zama za ukhalifa wa Othman bin Affan na kwamba, alimpatia Imamu Hussein (a.s) binti huyo. [20] Muhammad Hadi Yusuf Gharawi (aliyezaliwa 1327) ameikubali nukuu hii katika kitabu cha al-Mausu’ah al-Tarikh al-Islami. [21].

Shaka

Shahidi Murtadha Mutahhari anasema katika kitabu cha Khadamat Mutaqabila Islam wa Iran kwamba: Kuoana na Imamu Hussein (a.s) binti aliyejulikana kwa jina la Shahrbanu kwa mujibu wa nyaraka ni jambo linalotia shaka na baadhi ya wahakiki wametilia shaka jambo hili na kukitambua kama kisa cha kutunga.[22] Sayyid Ja’far Sahidi (aliaga dunia 1386 Hijria Shamsia) ametaja katika kitabu chake cha Zendegani Ali ibn Hussein na kutaja ushuhuda wa shaka hii kuhusiana na kutofahamiwa Shahrbanu na watu wa Bani Hashim katika karne ya pili.

Kufa Kwake

Baadhi ya wanahistoria wanasema kuwa, mama wa Imamu Sajjad (a.s) aliaga dunia wakati anajifungua mtoto wake huyu. [25] Imeandikwa katika kitabu cha Tabaqat al-Kubra (kilichoandikwa katika karne ya 3 Hijria) ya kwamba, baada ya kuuliwa shahidi Imamu Hussein (a.s), Shahrbanu aliolewa na Zubaid aliyekuwa mfanyakazi wa Imamu Hussein na kufanikiwa kuzaa mtoto aliyejulikana kwa jina la Abdallah. [26] Imenukuliwa pia ya kwamba, baada ya tukio la Karbala Shahrbanu alikwenda Iran na kutoweka katika mlima mmoja jirani na mji wa Rey. [27] Hata hivyo Sheikh Mirza Nuri (aliyeaga dunia mnamo mwaka 1320 Hijria) mmoja wa wapokezi wa Hadithi wa Kishia analitaja jambo hili kwamba, ni katika upotoshaji wa tukio la Ashura. [28] Hii leo katika eneo la mlimani jirani na Rey kuna haram ya Bibi Shahrbanu ambayo inanasibishwa na mama huyu wa Imamu Sajjad. [29] Hata hivyo, kunasibishwa eneo hili na kutajwa kuwa ni haram ya Bibi Shahrbanu ni jambo ambalo limepingwa na kukakatiwa na baadhi ya waandishi. [30] Kwa hiyo linalofahamika vyema hapa ni kuwa tunaweza kufupisha masuala kadhaa kuhusiana na Shahrbanu:

  1. Kuna hitilafu kubwa kuhusiana na jina la Shahrbanu
  2. Kuna hitilafu kuhusiana na jina la baba yake.
  3. Kuna tofauti miongoni mwa wanahistoria kuhusiananna historia ya familia yake.
  4. Kwa hakika Yazgerd aliipekea mbali familia yake na medani ya vita ili iwe katika amani na hivyo hili linaondoa uwezekano wa wana familia yake kuchukuliwa mateka.
  5. Jina la Shahrbanu limezungumziwa katika karne ya tatu Hijria.
  6. Yazgerd aliuawa mwaka wa 30 Hijria katika zama za utawala wa Othman bin Affan jambo ambalo linaongeza uwezekano wa kuwa mbali nadhari ya kuchukuliwa mateka binti zake katika zama za Khalifa wa Pili.

Rejea

Vyanzo