Istita'a (Hija)

Kutoka wikishia

Makala hii inahusiana na uwezo wa kwenda kuhiji. Ili kufahamu kuhusiana na uwezo katika istilahi ya elimu ya thiolojia, angalia makala ya Istita'a (thiolojia).

Istita'a (Kiarabu: الاستطاعة) maana yake ni uwezo wa mtu wa kusafiri na kwenda Makka na kutekeza amali na matendo ya ibada ya Hija. Kwa mujibu wa fat'wa za mafaqihi, ibada ya Hija huwa wajibu kwa mtu pale anapokuwa na uwezo. Uwezo huu ni katika mambo manne: Uwezo wa kifedha, kiusalama, afya ya kimwili na wakati.

Uwezo wa kimali na kifedha maana yake awe na uwezo wa kulipia gharama za safari ya kwenda Makka na kuachia pesa za matumizi kwa familia yake na watu ambao wako chini ya usimamizi wake (kama mke na watoto na kadhalika). Makusudio ya uwezo wa kiusalama ni usalama wa mali wa kiroho na kiheshima katika muda wote wa safari na wa kuwa kwake Makka.

Uwezo wa kimwili ni kuwa na uwezo wa kimwili na nguvu za kutekeleza amali za Hija. Uwezo wa wakati, maana yake ni kuwa na wakati wa kutosha kwa ajili ya kusafiri kwenda Makka na kutekeleza amali za ibada ya Hija.

Miongoni mwa hukumu za kifiq'hi za istita'a ni kwamba, mtu ambaye anakopa fedha za kugharamia safari ya Hija, kimsingi huyu hahesabiki kama ni mwenye uwezo, na Hija yake hii haihesabiwi kuwa, ni Hija ya wajibu.

Maana ya kifiq'h

Istita'a kuhusiana na Hija maana yake ni mtu kuwa na uwezo wa kwenda Makka na kutekeleza amali na matendo ya ibada ya Hija. Makusudio ya uwezo sio uwezo kiakili; yaani haina maana kwamba, mtu anapaswa kwenda Hija hata kama ni kwa ugumu na taabu; bali makusudio ni uwezo wa kisheria; yaani kutimiza masharti yaliyobainishwa katika Fiqhi ya wajibu wa Hija. [1] Mtu ambaye ana uwezo wa kwenda kuhiji kiistilahi anafahamika kwa jina la Mustati'u. [2]

Ulazima wa Istita'a ili Hija iwe wajibu

Mafakihi wote wamekubaliana (Ijma'a) kwa kauli moja kwamba, ibada ya Hija huwa wajibu kwa mtu, pale anapokuwa na uwezo (istita'a). [3] Fat'wa hii inategemea Aya ya 97 ya Surat al-Imran ambayo ndani yake imebainisha wajibu wa Hija kwa sharti la kuwa na uwezo: ((وَلِلّهِ عَلَی النَّاسِ حِجُّ الْبَیتِ مَنِ اسْتَطَاعَ إِلَیهِ سَبِیلًا ; Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezae njia ya kwendea)). [4]

Masharti ya Istita'a

Kwa mujibu wa fat'wa za mafakihi uwezo (istita'a) upo katika mambo manne: Uwezo wa kifedha, kiusalama, afya ya mwili na wakati (kuwa na wakati) na masharti yake ni kama ifuatavyo:

  • Mtu awe na uwezo wa kifedha wa kulipia gharama za Hija na aweze kuiachia matumizi familia yake na watu ambao wapo chini ya usimamizi wake na wajikimu mpaka wakati atakaporejea kutoka Hija. Kadhalika awe na uwezo wa kuendesha maisha yake baada ya kurejea kutoka Hija. [5]
  • Iwe inawezekana kwake kusafiri na kwenda Makka na kusiweko na tishio [6] dhidi ya uhai wake, mali au heshima yake. [7]
  • Anayetaka kwenda Hija awe na uzima wa kiafya na kimwili kwa ajili ya safari ya Makka na uwezo wa kutekeleza amali na matendo ya ibada ya Hija. [8]
  • Awe na muda wa kutosha kwa ajili ya kwenda Makka na kutekeleza ibada ya Hija. [9]

Istita'a ya mwanamke

Kwa mujibu wa fat'wa ya mafakihi wa akthari ya madhehebu ya Ahlu-Sunna, uwezo wa mwanamke una sharti jingine nalo ni mmoja wa maharimu wake aweze kufuatana naye; lakini mafakihi wa Shia Imamiyyah wanaona kuwa, kufuatana na maharimu sio shati la mwanamke kuhesabiwa kuwa na istita'a. [10]

Hukumu

Baadhi ya hukumu za kifikihi za istita'a ni:

  • Mtu ambaye amekopa kwa wengine fedha za kugharamia safari ya Hija huko Makka, kimsingi huyu hahesabiki kama ni mwenye uwezo, na Hija yake haihesabiwi kwamba, ni Hija ya wajibu. [11]. Hata hivyo kwa mujibu wa fat'wa ya baadhi ya Marajii ni kwamba, hakuna tatizo kama mtu huyu ataweza kulipa deni lake kwa urahisi. [12]
  • Kwa mujibu wa fatwa ya baadhi ya mafakihi akiwemo Muhaqqiq Hilli na Sahib al-Jawahir ni kwamba, kama mtu ana mali ya kiwango cha istita'a ya mali, lakini kwa sasa hawezi kutumia mali hiyo, ni wajibu kwake kukopa kwa ajili ya kwenda kutekeleza ibada ya Hija. [13]
  • Kama atampatia mtu mwingine gharama za uwezo wa kifedha, mtu huyu atahesabiwa kuwa ni Mustati'u (mwenye uwezo) na ibada ya Hija ni wajibu kwake. [14]
  • Mtu ambaye hana uwezo wa kugharamia safari ya kwenda Makka, lakini amejitokeza mtu mwingine na kukubali kugharamia hilo, kama ana uhakika mtu huyo atatekeleza ahadi yake, basi anahesabiwa kuwa ni mwenye uwezo na ibada ya Hija kwake ni wajibu. [15]
  • Mtu ambaye amekuwa na uwezo (mustati'u), lakini hakwenda Hija mpaka akawa masikini, inampasa kwenda Hija kwa vyovyote vile hata kama hilo liitakuwa na taabu na ugumu kwake. Kadhalika, mtu ambaye atazeeka au akawa hana uwezo wa kimwili na akawa hana matumaini kwamba, ataweza yeye mwenyewe kwenda kutekeleza ibada ya Hija, anapasa kuajiri mtu ili akamtekelezee kwa niaba ibada ya Hija. [16]

Vyanzo

  • Ḥillī, Jaʿfar b. al-Ḥasan al-. Sharāʾiʿ al-Islām. Edited by Ṣādiq al-Shīrāzī. Tehran: Istiqlāl, 1409 AH.
  • Ḥillī, Ḥasan b. Yūsuf al-. Tadhkirat al-fuqahāʾ. Qom: Muʾassisat Āl al-Bayt li-Iḥyāʾ al-Turāth, 1414 AH.
  • Ibn Qudāma, ʿAbd al-Raḥmān b. Aḥmad. Al-Mughnī. Beirut: Dār al-Kutub al-ʿArabī, 1403 AH.
  • Ibn Saʿīd, Yaḥya b. Aḥmad. Al-Jāmiʿ li-l-Sharāʾiʿ. Qom: Muʾassisat Sayyid al-Shuhadāʾ, 1405 AH.
  • Khalkhālī, Riḍā. Muʿtamad al-ʿUrwa al-wuthqā. Qom: [n.p], 1410 AH.
  • Khomeini, Ruḥollāh. Taḥrīr al-wasīla. Najaf, [n.p], 1390 AH.
  • Kulaynī, Muḥammad b. Yaʿqūb al-. Al-Kāfī. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī. Beirut: [n.p], 1401 AH.
  • Mūsawī al-ʿĀmilī, Muḥammad b. ʿAlī al-. Madārik al-aḥkām. Qom: [n.p], 1410 AH.
  • Narāqī, Aḥmad b. Muḥammad Mahdī al-. Mustanad al-Shīʿa fī aḥkām al-sharīʿa. Qom: Muʾassisat Āl al-Bayt li-Iḥyāʾ al-Turāth, 1429 AH.
  • Nawawī, Yaḥyā b. Sharaf. al-Majmūʿ: Sharḥ al-Muhadhdhab. Beirut: Dār al-Fikr, 1421 AH.
  • Qummī, Abū l-Qāsim b. Muḥammad Ḥasan al-. Jāmiʿ al-shatāt. Edited by Murtaḍā Raḍawī. Tehran: Kiyhān, 1371 Sh.
  • Ṣadūq, Muḥammad b. ʿAlī al-. Man lā yaḥḍuruh al-faqīh. Edited by ʿAlī Akbar Ghaffārī. Qom: Daftar-i Nashr-i Islāmī, 1404 AH.
  • Ṭūsī, Muḥammad b. al-Ḥasan al-. Al-Nihāya fī mujarrad al-fiqh wa l-fatwā. Qom: Quds-i Muḥammadī, [n.d].
  • Yazdī, Sayyid Muḥammad Kāẓim al-. Al-ʿUrwa al-wuthqā. Qom: Daftar-i Nashr-i Islāmī, 1420 AH.
  • Zubaydī, Muḥammad b. Muḥammad al-. Tāj al-ʿarūs min jawāhir al-qāmūs. Edited by ʿAlī Shīrī. Beirut: Dār al-Fikr, 1414 AH.
  • Zuḥaylī, Wahba. al-Fiqh al-Islāmī wa adillatuh. Damascus: Dār al-Fikr, 1425 AH.

{End}}